MICHIRIZI YA DAMU -12
“Mleteni lakini nitamfanyia baada ya saa tano,” alisema Dk. Watson.
“Haina shida.”
Hawakutaka kubaki nyumbani hapo, haraka sana akachukuliwa na kupelekwa katika hospitali hiyo. Muda wote huo Fareed alikuwa na hofu moyoni mwake, alihisi kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wake.
Alikuwa na mzigo mkubwa wa madawa ya kulevya tumboni mwake, wakati mwingine alihisi kwamba kete zile zingeweza kupasuka na madawa hayo kusambaa mwilini mwake na kumuua.
Hakutaka kuona hilo likitokea, alilia kimyakimya, kwake, Belleck alionekana kuwa mwanaume katili aliyeithamini fedha yake kuliko hata uhai wa watu wengine. Huyo hakuwa mwanaume aliyestahili kuwa hai, alitakiwa kuuawa kwani kwa kutumia fedha zake alipata nafasi ya kuwafanyia watu wengine matendo mabaya ya kikatili.
“Mungu nisaidie! Nikitoka katika hili, nitakukabidhi maisha yangu!” alisema Fareed huku gari likiwa safarini kuelekea hospitalini huko.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika hospitalini hapo ambapo moja kwa moja akachukuliwa na kupelekwa katika chumba maalumu kwa ajili ya mapumziko. Hapo alipokuwa, muda wote mwili wake ulikuwa ukimtetemeka, aliogopa, mbele yake alikiona kifo kitu ambacho hakutaka kukiona kikitokea mpaka pale atakapokamilisha ndoto zake.
“Mbona unakuwa na hofu sana?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Hapana! Sina hofu!”
“Usiogope. Ni suala la kuchukua mzigo wetu na wewe tutakuruhusu kuondoka,” alisema mwanaume huyo, japokuwa alijitahidi kumuondoa hofu Fareed lakini hakuonekana kuwa na amani hata kidogo.
Baada ya dakika kadhaa, daktari huyo akafika mahali hapo, akamwangalia fareed, uso wake ulikuwa na maswali mengi juu ya jinsi aliyokuwa nayo mtu aliyeletwa hospitalini kwake siku hiyo.
“Huyu ni mwanamke au mwanaume?” aliuliza Dk. Watson.
“Mwanaume!”
“Hapana! Mbona kama mwanamke?”
“Ni mwanaume tata!”
“Hapo sawa. Tena kwa sababu ana tabia chafu hivyo, nitamfanyia upasuaji bila ganzi,” alisema daktari huyo.
Baada ya dakika kadhaa, akamwambia Fareed aingie katika chumba kingine kabisa. Akasimama na kuelekea katika chumba hicho ambacho kwa kukiangalia tu wala usingejiuliza maswali mengi juu ya kazi iliyokuwa ikifanyika ndani ya chumba hicho.
Kulikuwa na vifaa vingi vya kufanyia upasuaji, kilitisha na kila wakati Fareed alipokuwa akikiangalia mapigo yake ya moyo yalidunda kwa nguvu, aliogopa mno na kuuona mwisho wake ukiwa umekaribia.
“Usiwe na hofu, chukua maji kwanza unywe,” alisema daktari huyo huku akimpa maji ambayo aliyawekea dawa ya usingizi. Fareed hakujua, akayapokea maji hayo na kunywa harakaharaka, baada ya dakika mbili tu, macho yake yakawa mazito na hapohapo kulala kwenye kiti alichokuwepo. Akanyanyuliwa na kulazwa kwenye kitanda cha kufanyia upasuaji tayari kwa kufanya kazi hiyo.
****
“Mchungaji! Mimi ni mkosaji! Nimekuja kutubu dhambi zangu! Nimekuwa nikimtumikia shetani kwa kipindi kirefu katika maisha yangu. Nimemtenda Mungu wangu dhambi! Nimekuja kutubu mchungaji,” alisikika mtu mmoja akimwambia padri aliyekuwa kwenye chumba kidogo cha kuungama dhambi.
“Umefanya nini mtoto wa Mungu?” aliuliza padri huyo.
“Nimezini kwa kipindi chote cha maisha yangu, nimekuwa na tamaa ya fedha, nimekuwa nikimtumikia shetani kwa kila aina ya uchafu. Nimechoka, ninataka kuokoka mchungaji, sitaki kumtumikia tena shetani,” alisikika mtu huyo akizungumza na padri huyo ambaye muda wote alikuwa akionyesha ishara ya msalaba.
“Mungu atakusamehe dhambi zako. Amesema kwamba hata kama dhambi zako zinakuwa nyekundu kama damu, atazisafisha na kuwa nyeupe kama theluji,” alisema padri huyo.
****
“What is wrong with her?” (nini kimemtokea?)
“Asthma.” (pumu)
“Where is her inhler?” (kifaa chake cha kuwekea dawa ya pumu kipo wapi?) alisikika mwanamke mmoja akiuliza.
“Here it is but there is nothing in it!” (hiki hapa lakini ndani hakuna kitu) alisikika msichana mmoja akijibu.
“What?” (nini?)
Kila mmoja ndani ya nyumba alichanganyikiwa, mtoto Kyle alikuwa amebanwa na pumu ambayo ilikuwa ikimsumbua kila siku. Mama yake na mfanyakazi wa ndani walichanganyikiwa, walijaribu kuangalia dawa ya kumpa iliyokuwa kwenye kifaa kidogo kinachojulikana kama inhler ambacho alitakiwa kuivuta kwa mdomo dawa hiyo lakini kitu cha kushangaza kabisa, kifaa hicho hakikuwa na dawa yoyote ile.
Waliuona mwisho wa Kyle, alikuwa akilalamika, alikipandisha kifua chake juu kama mtu aliyetaka kukata roho, alipumua juu juu kwa tabu sana kiasi kwamba kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba binti yao angekufa usiku huo.
Mama yake hakutaka kuchelewa, haraka sana akachukua simu yake na kumpigia mume wake, Dk. Watson ambaye alikuwa ni daktari kwa lengo la kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea kwa mtoto wao, Kyle.
“Unasemaje?” alisikika daktari huyo akiuliza kutoka upande wa pili wa simu.
“Kyle anakufa! Njoo na dawa haraka sana.”
“Dawa zake zipo wapi?”
“Zimekwisha…” alijibu mwanamke huyo na kukata simu.
Kyle hakuwa kwenye hali nzuri hata mara moja, kadiri dakika zilivyozidi kwenda mbele ndivyo hali yake ilivyozidi kuwa mbaya kiasi kwamba kila mmoja ndani ya nyumba hiyo alijua kwamba siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya mwisho kwa msichana huyo kuishi duniani.
Upande wa pili Dk. Watson ambaye alitakiwa kumpasua Fareed na kutoa kete za madawa ya kulevya alichanganyikiwa kupita kawaida. Alimuandaa mwanaume huyo kitandani, alimnywesha maji yaliyokuwa na dawa ya usingizi na alipotaka kumfanyia upasuaji akapokea simu hiyo kutoka kwa mkewe, simu ambayo ilimtisha kupita kawaida.
Hakutaka kubaki hospitalini hapo, mtoto wake, Kyle alikuwa kila kitu katika maisha yake, alimpenda kuliko kitu chochote kile, kuipuuzia simu ile na kuendelea kufanya mambo yake kwake lilionekana kuwa jambo la kijinga ambalo hakuwahi kulifanya katika maisha yake yote, alichoamua ni kuwaambia vijana waliomleta Fareed kwamba asingeweza kumpasua kwani kulikuwa na simu muhimu aliyokuwa amepigiwa.
“Ila si mara moja tu dokta?” aliuliza kijana mmoja.
“Hapana! Hii kazi inahitaji umakini sana kwani unaweza kumpasua ilimradi tu ukazipasua kete hizo na kupata hasara,” alisema daktari huyo, akawaaga na kuwaambia kwamba angerudi baada ya kumnunulia mtoto wake dawa iliyokuwa ikihitajika.
“Kwa hiyo huyu tumfanyaje?”
“Mwacheni humohumo nitakuja!”
“Sawa.”
Vijana wale hawakuwa na neno lolote lile, walichokijua ni kwamba Fareed alikuwa salama ndani ya chumba kile, wakabaki mahali hapo huku wakipiga stori kwani hawakutakiwa kuondoka mahali hapo mpaka daktari huyo atakaporudi na kufanya kile alichotakiwa kufanya.
Muda ukazidi kwenda mbele, dakika zilikatika lakini Dk. Watson hakuwa amerudi hospitalini hapo kitu kilichowafanya kuwa na wasiwasi kwamba inawezekana daktari huyo aliwakimbia.
Wakampigia simu, akawaambia kwamba angekuja kwani hali ambayo alimkuta nayo mtoto wake haikuwa nzuri, ilikuwa ni lazima akae naye kidogo na kurudi hospitalini hapo kuendelea na kazi.
Lilipofika saa moja, Fareed akashtuka kutoka katika usingizi aliokuwa nao. Kitu cha kwanza kabisa baada ya kuyafumbua macho yake ni kuangalia mahali alipokuwa.
Aligundua kwamba palikuwa ni hospitalini, hakukumbuka ni kwa namna gani alifika mahali hapo lakini baada ya kukaa na kukumbuka kwa sekunde kadhaa, akakumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Akakurupuka kutoka kitandani pale, ile haikuwa sehemu salama, alijua fika kwamba kama asingeondoka ndani ya chumba hicho ilikuwa ni lazima kupasuliwa tumbo lake na kutolewa kete za madawa ya kulevya zilizokuwa tumboni mwake.
Hakutaka kuona hilo likitokea, ilikuwa ni lazima kuondoka hospitalini hapo, akateremka kutoka kitandani, akaufuata mlango lakini hata kabla hajaufungua, akawasikia watu wakiwa wanaongea kwa nje.
“Mmh!” alijikuta akiguna.
Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, akarudi kitandani pale na kutulia, kichwa chake kilimuuma, alitamani hata kupitia katika mlango mwingine lakini kitu kibaya kwake ni kwamba hakukuwa na mlango wowote zaidi ya ule waliokuwa wakiutumia.
Minong’ono ile ya watu bado iliendelea kusikika kutoka nje ya chumba kile, aliogopa, kwa jinsi alivyoona, ilikuwa ni lazima watu hao waingie ndani kumwangalia kwani hakujua daktari alikuwa mahali gani.
Alichokifanya ni kuusogelea mlango na kisha kuufunga kwa ndani, hakutaka mtu yeyoite aingie ndani ya chumba kile na kumkamata, alijua kwamba angekufa, ila hakuwa tayari kuona akifa siku hiyo.
“Ni lazima nifanye kitu!” alisema lakini hata kabla hajafanya kitu hicho, akasikia kitasa cha mlango kikianza kutekenywa kwa ajili ya kufunguliwa lakini haukufunguka kitu kilichowafanya kuanza kuugonga kwa lengo la kuuvunja.
****
Belleck alikuwa ametulia, masikio yake yalikuwa kwenye simu yake, alitaka kufahamu kile kilichokuwa kikiendelea nchini Ufaransa, alitaka kujua kama tayari Fareed alifanyiwa upasuaji na kutolewa kwa kete za madawa ya kulevya au kitu hicho hakikuwa kimefanyika.
Alisubiri sana, tangu Fareed afikishwe ndani ya hospitali, aliambiwa kwamba angepigiwa simu na kupewa kila kitu kilichokuwa kimeendelea lakini mpaka saa moja na nusu bado hakuwa ametaarifiwa kitu chochote kile.
Alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilitokea, hakutaka kuvumilia, hapohapo akachukua simu yake na kupiga upande wa pili, simu ilipopokelewa, akaambiwa kila kitu kilichokuwa kimetokea.
“Kwa hiyo Dk. Wtason hayupo?” aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Ndiyo mkuu!”
“Atatuchelesha, ingieni ndani na mmuue kisha zitoeni hizo kete, hakuna haja ya kuendelea kumsubiri muda wote,” alisema Belleck na kukata simu.
Ilikuwa ni amri, vijana hao hawakutaka kuendelea kumsubiri daktari huyo, walitaka kufanya kile walichokuwa wameambiwa. Fareed alikuwa ndani ya chumba kile, haikuwa kazi kubwa kuingia na kumuua kisha kulipasua tumbo lake na kuzitoa kete alizokuwa amezimeza.
Wakaufuata mlango kwa lengo la kuufungua, haukufunguka, ulionekana kufungwa kwa ndani. Kwa kuwa hiyo haikuwa hospitali kubwa sana, hakukuwa na wagonjwa wengi wala madaktari hivyo kuanza kuupiga mlango huo kwa lengo la kuuvunja na kuingia, tayari walipewa agizo kwamba mtu huyo auawe hivyo hawakuwa na msalie mtume.
****
“What are you doing?” (mnafanya nini?) lilisikika swali kutoka kwa mwanamke aliyekuwa nyuma ya watu hao waliokuwa wakijaribu kuuvunja mlango ule wa humba alichokuwemo Fareed.
Vijana wa Belleck wakageuka nyuma na kumwangalia mtu aliyewauliza swali hilo. Alikuwa nesi wa hospitali hiyo, kibonge, aliyevalia gauni refu jeupe huku kichwani akiwa na kikofia kidogo cha kilichoonesha kwamba alikuwa muuguzi.
Bastola zilikuwa mikononi mwao, kitendo cha mwanamke huyo kuziona bastola hizo, hakutaka kubaki mahali hapo, akaanza kukimbia huku akiwaita polisi kwani alijua kwamba watu hao hawakuwa watu wazuri hata mara moja.
Ilikuwa ni hatari kwao, walijua kwamba hospitalini hapo kulikuwa na polisi, walijua fika kwamba walimiliki bastola zile kimagendo, wakaogopa na kuhisi kwamba kungekuwa na jambo baya, walichokifanya ni kukimbia mahali hapo kwenda kujificha kwani kama wangekutwa na polisi waliokuwa wakiitwa, maisha yao yangekuwa hatarini.
Fareed alikuwa ndani ya chumba kile, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, alitamani hata kama kungekuwa na mlango wa kuingia darini, aingie na kujificha huko lakini alipoangalia, hakukuwa na malngo huo.
Bado kitasa kiliendelea kutekenywa, mule ndani alikuwa akiogopa mno, alikosa amani na muda wowote ule alikiona kifo chake kikiwa mbele yake. Wakati akijifikiria ni kitu gani alitakiwa kufanya ndipo akasikia sauti ya mwanamke yule ikiwauliza wanaume hao, badala ya kujibu swali waliloulizwa, wakaanza kukimbia huku mwanamke huyo akiwaita polisi.
Ghafla, ukimya ukatawala mahali hapo, akaona nafuu moyoni mwake, hakutaka kubaki ndani, aliamini kwamba hakukuwa na mtu yeyote nje ya chumba hicho hivyo alichokifanya ni kuchukua mkoba wake uliokuwa na nyaraka zake za kusafiria na kuufungua mlango,akachungulia nje ya chumba kile, kweli hakukuwa na mtu hivyo kuanza kutoka.
Alifanikiwa, hakukuwa na hatari yoyote ile, hakutaka kusubiri, alijua kabisa kwamba kuendelea kusubiri mahali hapo ingekuwa hatari kwa maisha yake hivyo akaondoka kwa kupitia mlango mwingine, kwani kama asingefanya hivyo ilikuwa ni lazima kuuawa mahali hapo.
Akaondoka mpaka nje ya hospitali ile. Akaanza kutembea kuelekea sehemu iliyokuwa na magari mengi yaliyokuwa yamepaki. Alikuwa akijifichaficha kwani mahali hapo hakukuonekana kuwa na amani kwa maisha yake.
Akafika sehemu moja iliyokuwa na kiukuta na kutulia hapo. Macho yake alikuwa ameyaelekezea kule kulipokuwa na mlango wa kutokea katika jengo la hospitali hiyo, akawaona wale wanaume wawili wakiwa sehemu wamesimama, alijua dhahiri kwamba walikuwa wakimsubiri yeye.
Hakutoka mahali hapo, aliendelea kusimama na baada ya dakika kadhaa akamuona Dk. Watson akiteremka kutoka katika gari lililoingia sekunde chache, alipowaona wale vijana, akawafuata, akazungumza nao kwa sekunde kumi, ghafla wote wakaanza kukimbia kuelekea ndani.
Alijua fika kwamba walimpa taarifa kuhusu yeye, hakutaka kusubiri mahali hapo, haraka sana akachomoka pale alipokuwa na kuelekea nje ya hospitali hiyo ambapo baada ya kufika huko, akachukua teksi na kuondoka mahali hapo.
***
Dk. Watson na vijana wale wakafika mpaka ndani ya chumba kile, walishtuka, hakukuwa na mtu yeyote yule, Fareed ambaye walimuacha humo hakuwepo.
Walichanganyikiwa, hawakuamini kile walichokuwa wamekikuta. Wakaanza kumtafuta kila kona ndani ya hospitali hiyo lakini mtu huyo hakuonekana. Hawakujua ni kitu gani walitakiwa kufanya, hawakujua mahali alipokuwa ameelekea, hawakujua ni jinsi gani wangemwambia bosi wao, Belleck ambaye alikuwa akisubiri taarifa ya kifo cha Fareed kwa hamu kubwa.
“Yupo wapi?” aliuliza Dk. Watson.
“Hatujui! Ila tulimuacha humu ndani!”
“Sasa yupo wapi?”
“Hatujui!”
Itaendelea kesho