Jamani hii habari inanipa raha! naona muisome tena hapa nimeikoleza, naona tuna waandishi wa habari wchache sana kama huyu..
Msafara wa JK wapigwa mawe
2008-10-16 13:47:02
Na Thobias Mwanakatwe, Chunya
Ziara ya Rais Jakaya Kikwete mkoani Mbeya imeingia dosari baada ya wananchi wa kijiji cha Kanga wilayani Chunya kupiga mawe magari sita yaliyokuwa katika msafara wake yakiwa yamewabeba mawaziri, waandishi wa habari na viongozi waandamizi wa serikali na kusababisha baadhi yao kujeruhiwa.
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea katika kijiji hicho majira ya saa 7:30 usiku wakati msafara wa Rais ukiwa njiani kuelekea Mbeya mjini ukitokea mji wa Mwakwajuni wilayani Chunya ambako Rais Kikwete alikuwa ziarani.
Miongoni mwa magari yaliyopigwa mawe ni la Waziri wa Miundombinu, Dk. Shukuru Kawabwa, ambalo jiwe lilipiga upande wake na kugonga `wepa`. Hata hivyo, halikuvunja kioo wala kumjeruhi Waziri huyo.
Magari mengine yaliyopigwa mawe ni la Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mwatumu Mahiza, gari la Mbunge wa kuteuliwa na Rais, Thomas Mwang`onda lenye namba za usajili T 894 AAY na gari namba STK 2429 lililokuwa limewabeba waandishi wa habari, ambalo limevunjwa vioo vya mlango na waandishi wawili kujeruhiwa.
Magari mengine yaliyopigwa mawe na wananchi hao ni STK 3240 na STJ 3958 linalotumiwa na Afisa Elimu Mkoa wa Mbeya, katika msafara huo lilikuwa limewachukua maafisa wa serikali kutoka Ikulu.
Kutokana na tukio hilo, waandishi wawili wa magazeti ya serikali pamoja na kijana mmoja, Chipukizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wote walijeruhiwa na walipewa huduma ya kwanza na madaktari ambao wapo katika msafara wa Rais mara baada ya magari kuwasili katika Ikulu Ndogo ya mjini Mbeya majira ya saa 3.00 usiku.
Baadhi ya viongozi waliozungumza na gazeti hili katika Ikulu Ndogo, walisema kuwa wananchi waliofanya tukio hilo walikuwa wamejipanga pembeni mwa barabara na baada ya magari manne ya mwanzo kupita, ndipo mawe yalianza kuvurumishwa.
Baada ya magari hayo manne kupita, magari yaliyokuwa nyuma yalianza kuvurumishiwa mvua ya mawe na wananchi hao.
Habari zaidi ambazo gazeti ilizipata zinaeleza kuwa hatua ya wananchi hao kufanya uhalifu huo ilitokana na hasira ya kushindwa kumwona Rais Kikwete baada ya kumsubiri kwa muda mrefu ili apite katika kijiji hicho na ili wamweleze kero zao.
Kutokana na muda kuwa umekwenda na giza kutanda, Rais Kikwete hakuweza kusimama katika kijiji hicho, hali iliamsha hasira za watu hao ambao waliamua kukusanya mawe na kuanza kushambulia magari yaliyokuwa kwenye msafara.
Hata hivyo, gari la Rais Kikwete, mke wake pamoja na walinzi wake hayakuhusika katika kadhia hiyo ya aina yake inayoashiria kuporomoka kwa maadili kwa kiwango cha juu kwa wananchi kiasi cha kutokuheshimu hata msafara wa kiongozi mkuu wa nchi.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, John Mwakipesile, akizungumza na waandishi wa habari saa 3:30 usiku Ikulu Ndogo mjini hapa, alisema waliofanya kitendo hicho ni walevi na kwamba serikali itahakikisha inachukua hatua kali dhidi yao.
Alisema kutokana na tukio hilo, ratiba ya Rais Kikwete katika ziara yake mkoani humo itabadilika na msafara wake hautatembea tena usiku.
Kuanzia sasa hivi ratiba ya msafara wa Rais kutembelea sehemu mbalimbali za mkoa itabadilishwa kwa kuanza mapema asubuhi na kurejea mapema ili kuepuka tukio kama la leo (jana) lisijirudie, alisema.
Mwakipesile alisema tayari kikosi cha Polisi cha Kutuliza Ghasia (FFU), kimepelekwa katika kijiji cha Kanga kusaka wahusika wa tukio hilo la aibu kuwahi kutoka katika Jamhuri ya Tanzania.
Tukio hili linatokea siku tano tu baada ya msafara wa Rais Kikwete kusimamishwa mara tatu na wakazi wa mkoa huo, Oktoba 10, mwaka huu siku alipoanza ziara ya siku 10.
Katika matukio hayo yaliyoanzia Mbeya Mjini eneo la soko la Mwanjelwa, wananchi walisimama barabarani kuzuia msafara wake ili kumweleza kilio chao juu ya mafisadi kutokuadhibiwa na hali ya maisha kuzidi kuwa duni miongoni mwao.
Pia walitaka kupewa sababu za kutokuwekwa matuta barabarani hali ambayo imesababisha watoto wao wengi kugongwa na magari; wananchi hao kadhalika walitaka kujua kwa nini hawana huduma ya maji safi.
SWALI: Je wananchi hawa wangekuwa na silaha za moto,JK angepona kweli naona, hivi? siyo kweli tunaongozwa na Rais ambaye watanzania wengi wameshamuua mawazoni mwao? wamekosa tu uwezo au chansi?
waberoya