Kifo siku ya harusi yangu

Kifo siku ya harusi yangu

SEHEMU YA 24



Furaha imerejea tena katika maisha ya Genesis, kumrejesha tena Farida halikuwa jambo jepesi. Ni ushindi mkubwa katika maisha yake. Mama yake ameshaamua kwa moyo mmoja kumwacha Genesis arudiane na mpenzi wake akidai kwamba kama mzazi ameamua kuheshimu hisia za mwanaye!

Bianca anaonekana hana furaha kabisa, anajaribu kumpigia mama yake simu na kupanga namna ya kuwasambaratisha tena; Wazo lake linakuwa ni kumuua Farida lakini mama yake anampinga na kumwambia kwamba amwachie mwenyewe atajua cha kufanya.

Upande wa pili tunamwona Farida akiwa na Genesis katika Ufukwe wa Coco, Masaki jijini Dar es Salaam. Farida anaonekana kuwa na jambo zito alilotaka kumwambia mpenzi wake. Baada ya kumzungusha sana, akamwambia kwamba amepata chuo. Genesis anashtuka mno.
Halikuwa jambo rahisi kuaminika kiasi kile. Ghafla Farida akamrukia, wakakumbatiana kwa furaha.

KWA sekunde ishirini walibaki wamekumbatiana kwa furaha huku Farida akishindwa kuzuia machozi yake. Macho yalikuwa chapachapa! Kwake yalikuwa mafanikio makubwa na kama ni kizingiti walikuwa wanaruka cha mwisho!

Aliwafahamu vizuri sana wazazi wa Genesis ambao walipenda elimu kuliko kitu chochote. Kupata nafasi ya chuo, ilikuwa sawa na kumaliza kabisa shahada yake ya kwanza. Aliuamini sana uwezo wake hivyo suala la kusoma lisingekuwa tatizo kwake.

Baadaye waliachiana lakini wakasimama kwa mtindo wa kuangaliana. Genesis akiwa hana la kusema, furaha iliyokuwa ndani ya moyo wake, haikuwa rahisi kuitoa nje kwa maneno.

Hata kama maneno yalikuwepo lakini hakuelewa ni yapi hasa yangeweza kujitosheleza kumwambia mpenzi wake na akaelewa kwamba amempongeza!

Genesis alitulia kama maji yaliyoganda kwenye jokofu akimwangalia Farida ambaye alionekana kuwehuka na furaha aliyokuwa nayo!

“Hongera mama, hongera sana!” Hatimaye Genesis akasema.
“Nashukuru sana baba, ahsante sana mpenzi wangu!”
“Siamini Farida wangu, sasa unakwenda kukata ngebe zote. Hakuna atakayeleta tena kipingamizi. Ni kipi sasa kama tayari umeshapata chuo?”

“Nakwambia nina furaha sana, hebu twende hivi...” Farida akasema akimshika mkono mpenzi wake na kumwongoza kutembea ufukweni.
Nyuso zao zilikuwa zimepambwa na tabasamu pana, walikuwa kama wamezaliwa kwenye ulimwengu mpya wa peke yao.

Ndoto ya muda mrefu ilikuwa imetimia.
“Umepata chuo gani mpenzi wangu?” Genesis akamwuliza.
“Chuo Kikuu Huria cha Arab.”
“Kipo nchi gani?”
“Saudi Arabia.”

“Hongera sana, huko mama lazima muda wote uvae juba na hijabu, najua hutaweza kunisaliti!” Genesis akasema akicheka.

“Hata bila hivyo mpenzi wangu, najua wajibu wangu kwako kwa hiyo hakuna anayenichunga zaidi ya mimi mwenyewe. Niamini mpenzi wangu, mimi sihitaji ulinzi, najilinda mwenyewe!” Farida akasema kwa sauti iliyojaa utulivu.

“Nakutania mpenzi wangu, mimi na wewe tena!”
“Usijali mpenzi wangu, najua hata wewe huwezi kwenda kinyume na mimi!”

“Ni kweli mama, nilisaliti mara moja tu na nilikueleza ukweli lakini hili kamwe haliwezi kutokea tena, nipo makini sana kwa sasa Farida wangu. Siwezi kumruhusu mwanamke mwingine yeyote aujue mwili wangu zaidi yako!”
“Nimefurahi kusikia hivyo.”
“Kozi gani umepata?”
“Sociology!”

“Kozi nzuri sana, utaratibu ukoje lakini? Wamekupa ofa ya nini na nini?”
“Kila kitu mpenzi wangu, ninachotakiwa kufanya ni kuandaa utaratibu wa kupata tiketi tu basi! Nikifika huko kila kitu ni juu yao kuanzia hosteli, malazi, steshenari na mahitaji mengine yote muhimu.”

“Safi sana, hiyo ni bahati ya kipekee.”
“Lakini mpenzi wangu, kuna kitu kinanichanganya kidogo.”
“Nini?”

“Natakiwa kuripoti chuoni baada ya miezi mitatu kutoka sasa!”
“Sasa hapo unapaswa kuchanganyikiwa au kufurahia?”
“Tiketi je?”

“Sasa hilo ndiyo la kukuchanganya? Niachie mimi, nitajua cha kufanya. Kwanza inabidi tusafiri kwenda Zanzibar, tukafanye ‘shopping’ kwanza kabla ya safari yako.”
“Nitafurahi sana mpenzi wangu.”

“Anza kufurahi sasa.”
Siku yao ilikuwa nzuri hakika, Genesis alijiona mwenye bahati sana kuona ndoto zake za kumuoa mwanamke ambaye moyo wake umemthibitisha zikianza kunukia kukamilika. Ilikuwa siku yao ya furaha kupita kiasi.

Jioni Genesis alimrudisha Farida nyumbani kwao Kwa Aziz-Ally. Aliposhuka, aliwasha gari na kugeuza kurudi zake chuoni. Baada ya kuegesha gari lake, akachukua simu na kumpigia baba yake Profesa Mshana.

“Baba huwezi kuamini, ndoto zangu zinakaribia kuwa kweli!” Genesis alianza kusema baada ya baba yake kupokea simu.
“Genesis kwani leo tumesalimia mwanangu?”

“Samahani baba, shikamoo...” akasalimia Genesis.
“Mar-haba mwanangu. Haya sasa niambie hilo ulilotaka kuniambia.”
“Farida amepata chuo baba.”
“Safi sana. Amepata wapi, kozi gani na lini ataanza masomo?” Profesa Mshana akauliza akionekana kufurahishwa sana na taarifa hiyo.

“Amepata Arab Open University, Riyadh, Saudi Arabia, atasoma Sociology!”
“Safi sana, imekuwa vizuri mwanangu maana utaoa mwanamke msomi ambaye hatakuwa mzigo kwako. Unajua Genesis, kama nilivyokuambia mwanzo, ili uwe na familia bora, lazima uwe na mwanamke bora pia. Ninaposema mwanamke bora namaanisha pamoja na elimu.

Kama mwanamke hana elimu ya kutosha, hawezi kuwa bora.
“Ni imani hiyo ndiyo ilinifanya mimi nikamuoa mama yako ambaye ni bora na tukawazaa watoto wetu bora, wenye akili na wasomi. Kwa hiyo nimefurahi sana kusikia habari hizo!”

“Ahsante sana baba, naomba fikisha taarifa hizi hadi kwa mama, simpatii picha jinsi atakavyofurahi!”
“Sawa Genesis, masomo mema.”
“Nawe jioni njema baba.”

“Nashukuru.”
Wakakata simu zao.
***
Ikiwa ni miezi minne tu kabla ya Genesis kumaliza masomo yake Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Farida alibakiza miezi miwili kabla ya kuripoti Saudi Arabia katika Chuo Kikuu cha Arab.

Farida na Genesis walikuwa visiwani Zanzibar kwa ajili ya manunuzi ya mavazi na mahitaji mengine muhimu. Mpaka wakati huo kila kitu kilikuwa tayari, kilichobaki ilikuwa ni kuchukua tiketi ya ndege tu tayari kwa safari ya Saudi Arabia.

Walikaa Zanzibar kwa wiki nzima wakila raha za kila aina. Walifikia katika hoteli nzuri, wakifanya kila kitu isipokuwa ngono! Pamoja na kwamba Genesis alikuwa ameshawahi kufanya mapenzi mara moja na Bianca tangu kuzaliwa kwake, hakutaka kufanya hivyo na Farida.

Alitamani sana kuoa mwanamke ambaye angekuwa mwali kabisa, asiyeguswa na mwanaume yeyote. Kwake ilikuwa fahari kubwa sana kuoa mwanamke aliye bikra. Usiku wa mwisho kabla ya kurejea Dar es Salaam, walijikuta wakitumia muda mwingi sana kunyonyana ndimi, hali iliyoamsha hisia zao za mapenzi.

Mwili wa Genesis ukawaka kama moto wa kifuu. Alijikuta akitamani sana kufanya mapenzi na Farida kwa mara ya kwanza. Msimamo wake aliokuwa nao awali, alijikuta akitaka kuusaliti mwenyewe.

Wakiwa katika zoezi hilo, Farida akitoa mihemo ya ushawishi, Genesis alitaka kuanza kumwingilia Farida.
“Hapana, hapana Genesis, si makubaliano yetu!” Farida alisema akimtoa Genesis pembeni yake.
“Najua mpenzi lakini ukumbuke kwamba hata mimi nina hisia.”
“Sawa lakini si wakati wake Genesis, umesahau makubaliano yetu mara hii?”

“Farida mara moja tu, naomba utibu moyo wangu. Sina hali mpenzi wangu, jaribu kuwa na moyo wa huruma.”

“Sitaweza kuruhusu jambo hili litokee Genesis, nitakuwa nimeidhulumu nafsi yangu lakini pia nitakuwa nimemkosea mama yangu na hata Mungu pia.”

“Kwani hunipendi Farida?”
“Nakupenda mpenzi wangu lakini hatuna ndoa, ni mapema sana kwetu kufanya hivi!”
“Nakuuliza swali na ninaomba unijibu kwa uhakika na usahihi.”
“Uliza.”

“Ni kweli bado unayo bikra yako?”
“Ndiyo mpenzi wangu, ahadi yangu haiwezi kubadilika, hii ni zawadi yako baada ya ndoa. Vumilia mpenzi wangu, najua ni ngumu lakini vumilia!” Farida akasema kwa sauti ya taratibu sana.
“Nakupenda sana Farida, naomba unisamehe kwa hili lililotaka kutokea.”

“Usijali, nimeshakusamehe. Nakupenda pia mpenzi wangu!”
Wakakumbatiana tena, wakavuta shuka na kulala. Penzi lao lilikuwa la dhati.
***
Taratibu zote za safari zikafanyika, kila kitu kilikamilika na hatimaye siku ya safari ikafika. Genesis ndiye aliyempeleka Farida mpaka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akiwa na mizigo yake.

Robo saa kabla ya ndege kuruka, Genesis alikuwa anaagana na mpenzi wake Farida, akiwa na majonzi mazito. Alikuwa anakwenda kuanza kipindi kigumu sana cha kuishi mbali na mpenzi wake.
“Farida naumia sana moyoni lakini nenda kasome mama, zingatia kilichokupeleka Saudi Arabia na ujue kwamba Tanzania umemuacha mwanaume anayekupenda sana.”

“Nakuhakikishia hilo mpenzi wangu, hata wewe pia napenda iwe hivyo kwako. Nakupenda sana Genesis, nakwenda kuishi maisha mapya kabisa ya kuwa mbali na wewe. Najua nitaumia sana, lakini nitazoea. Nakupenda sana!” Akasema Farida na kumbusu Genesis katikati ya midomo yake.

Genesis akashuhudia Farida akiondoka na kuingia sehemu maalumu ya abiria wanaosafiri, hakutaka kuondoka mapema uwanjani, alisubiri mpaka ndege iliporuka angani. Bila kujali kama Farida alikuwa anamuona au laa, alipunga hewani akiamini mpenzi wake alikuwa akiona mkono wake.

Ndege ilipoishilia kabisa, akarudi zake kwenye gari na kwenda zake chuoni.
***
Ndege ya Shirika la Ndege ya Emirates iliacha anga na kukanyaga ardhi ya Saudi Arabia katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa King Khalid, jijini Riyadh saa 12:45 za jioni. Abiria walianza kushuka mmoja baada ya mwingine na kupita moja kwa moja hadi kwenye sehemu ya kusubiria mizigo.

Farida alitembea kwa kujiamini, kama vile aliwahi kufika Saudi Arabia lakini ukweli ni kwamba kila kitu kilikuwa kigeni kwake.

Ilikuwa mara ya kwanza kusafiri kwenda nje ya nchi lakini pia ilikuwa mara ya kwanza kupanda ndege! Alikwenda hadi sehemu ya kusubiri mizigo, akaangalia mizigo iliyokuwa ikipita mbele yake, hadi alipoona begi lake na kulichukua! Baada ya hapo akatembea kwa kujiamini akielekea sehemu ya ukaguzi kabla ya kutoka nje.

Aliweka begi lake sehemu ya ukaguzi, akiwa mwenye furaha sana.
Akiwa amesimama, ghafla akashangaa wanaume sita wakiwa wamemzunguka, mikononi mwao wakiwa na bastola. Farida akatoa macho yake kwa mshangao.
“Nini kimetokea?” Farida akauliza kwa mshangao akiangalia begi lake lililokuwa wazi.

“Tulia hivyo hivyo, maelezo mengine utayapata polisi, funga begi lako na ulibebe, kisha tuongozane!” Mmoja wa watu hao alisema.
Farida alipowaangalia vizuri, hakupata tabu kugundua kwamba alikuwa mikononi mwa polisi lakini hakujua sababu ya kukamatwa baada ya mzigo wake kukaguliwa.

Akabaki anatetemeka.
“Chukua begi lako twende!” Mwingine akasema kwa ukali.

FARIDA alikuwa katika taharuki kubwa, ni kweli aliweza kugundua kwamba waliokuwa mbele yake walikuwa ni maaskari, lakini hakujua kosa lake lilikuwa ni nini hadi aamriwe kubeba begi lake na kuongoza kituoni.
“Binti unatuchelewesha, beba begi lako twende!” Askari mmoja akamuamrisha.

“Kwani nina kosa gani?”
“Hujui kosa lako?”
“Ndiyo maana nauliza.”
“Labda tukuulize swali moja jepesi!”
“Ndiyo!”
“Hili begi hapa chini unalitambua?”
“Ndiyo!”
“Ni la nani?”
“Langu.”

“Kweli?”
“Ndiyo ni langu, huoni hata jina limeandikwa Farida Mubaraka, ndiye mimi. Ni langu!”
“Sasa kama ni lako, unatakiwa kulibeba ili tuongozane hadi kituoni, mambo mengine yote utayajua huko huko!”
“Lakini nina haki ya kujua kosa langu!” Farida akasema akitetemeka.

“Paaaa!” Kibao kikali kilitua shavuni mwa Farida.
“Mbona mnanipiga bila sababu?” Farida akauliza, macho yake yakianza kulengwalengwa na machozi.
“Hebu fungua begi lako!” Askari mmoja aliamrisha na Farida akatii kwa kuanza kulifungua.
“Fungua hiyo zipu ya pembeni!” Akasema tena na Farida akatii.

Kitu alichokutana nacho, kilimshtua sana Farida. Alishindwa kuelewa kilifikaje kwenye begi lake, maana hakukijua na wala hakutoka nacho Dar es Salaam.
“Haya beba twende!” Akaamrishwa.

Farida akafungwa pingu na kuongozana na maaskari hao hadi nje, ambapo waliingia kwenye gari lao na safari ya kwenda Makao Makuu ya Polisi, Kitengo cha Upelelezi, jijini Riyadh ikaanza.
***
Ilikuwa ndiyo wiki ya kwanza ya mitihani ya mwisho kabla ya kumaliza chuo, Genesis alikuwa mwenye mawazo sana jioni hiyo. Mpaka muda huo, alikuwa hajapata simu kutoka kwa Farida ambaye walikubaliana atakapofika tu, amjulishe. Moyo wa Genesis haukuwa na amani kabisa. Alichohitaji yeye ni Farida wake kumweleza kama alikuwa amefika salama.

Jambo hilo lilimnyima raha kabisa, akaamua kuingia bwenini mapema sana. Akiwa amejilaza mawazo tele kichwani mwake yakizunguka, rafiki yake Greyson akatokea.

“Mzee vipi mbona unalalalala una hamu ya kudisko nini?”
“Hapana kaka, acha nipumzishe kichwa kidogo!”
“Lakini tupo kwenye mitihani ya mwisho kabisa kaka, kufanya vizuri kwenye test za wiki na assignment hakuwezi kukusaidia, kama utachemka huku mwishoni!”
“Najua Greyson, lakini acha nipumzike, kichwa changu kimejaa sana kaka!”

“Nini tena? Isije kuwa umeshaanza kummisi Farida wakati ni jana tu ameondoka!”
“Pamoja na hilo pia.”
“Lakini hutakiwi kuwaza sana, twende zetu!”
“Wapi?”
“Tukasome!”
“Kaka ng’ombe hawezi kunenepa siku ya mnada, leo sijisikii kusoma kabisa.”

“Sasa?”
“Nini?”
“Umeshakula?”
“Bado.”
“Twende basi tukale, tena leo nina hamu sana na mbuzi choma, twende Udasa Bar, wana nyama ya mbuzi nzuri sana pale!”
“Poa.”

Genesis akajiinua kitandani na kuchukua shati kisha akavaa. Wakatoka na Greyson taratibu wakifuata barabara kuelekea Baa ya Udasa ilipokuwa. Walipofika waliweka oda na kuagiza vinywaji. Sehemu waliyokuwa wamekaa, kulikuwa na runinga mbele yao.

Wakiwa wanaangalia runinga huku wakiendelea na mazungumzo yao, chini ya kioo cha runinga yakapita maneno yaliyosomeka BREAKING NEWS, baadaye maneno mengine yakafuata yaliyoandikwa kwa Lugha ya Kiingereza yakisomeka kwa Kiswahili; ‘Riyadh, Saudi Arabia.

Raia wa Tanzania Farida Mubaraka, amekamatwa na maaskari jijini hapa akiwa na dawa za kulevya aina ya heroin. Msichana huyo mwenye umri wa miaka 22, alisema amekuja nchini hapa kwa ajili ya kujiunga na Chuo Kikuu Huria cha Arab. Tutawaletea taarifa zaidi hapo baadaye.’
“Nini?” Genesis alisema kwa sauti akitoa macho.
“Vipi Genesis?” Greyson akamwuliza.
“Ile habari inamuhusu Farida!”
“Farida mpenzi wako?”
“Ndiyo!”
“Si jana tu ameondoka kwenda Saudi Arabia?”
“Ndiyo!”

“Mungu wangu! Unataka kusema kwamba anajihusisha na dawa za kulevya?”
“Kaka kwani hujaona?”
“Yaani sijajua kama huyu mwanamke ana tabia ya kijinga kiasi hiki, halafu anafanya mambo yake kwa siri.”
“Lakini wamesema taarifa kamili itafuata baadaye, kwanini tusisubiri kwanza?”
“Sawa.”

Waliendelea kusubiri, muda wote huku macho yao yakiwa kwenye runinga, kiasi cha dakika ishirini baadaye, Kituo cha ITV walichokuwa wakiangalia, kiliunganisha matangazo yake na Shirika la Utangazaji la CNN, kisha habari na picha zikaonekana!

Genesis alichanganyikiwa, hakuamini kama aliyekuwa akionekana kwenye runinga alikuwa mpenzi wake Farida, lakini ukweli uliendelea kubaki kuwa huo. Aliyeonekana akiwa chini ya ulinzi wa polisi, katika Uwanja wa Ndege wa King Khalid alikuwa ni Farida.
“Si nilikwambia?” Akasema Genesis akiinuka.
“Vipi?”

“Twende hapatufai tena hapa.”
Wote wakainuka na kuanza kutokauelekea bwenini, wakiwa njiani, Genesis akampigia mama yake simu na kumpa taarifa ya tukio zima la Farida.

“Unasemaje?” Mama yake akauliza kwa mshtuko mkubwa.
“Weka ITV mama ujionee mwenyewe.”
“Hebu ngoja niweke!” Akasema mama yake Genesis na kukata simu.

Robo saa baadaye akampigia Genesis. Alikuwa akizungumza kwa sauti ya chini sana, akionesha kusikitishwa na kitendo cha Farida.

“Lakini mwanangu tulikuambia ni vema ukamchunguza kwanza huyo mtu wako kabla ya kuamua chochote, sasa umeona madhara yake. Ungekuja kuoa mwanamke teja!” Akasema mama Genesis.

“Mama sikujua kama Farida ana mambo ya hatari kiasi hicho.”
“Sasa itakuwaje?”
“Itakuwaje vipi tena mama, siwezi kuendelea na teja mimi!”
“Pole sana mwanangu, kwa hiyo unadhani nini cha kufanya?”

“Lazima nizungumze na Bianca tena. Sijui nitaongea nini anielewe maana nilishampa maneno yote mabaya. Lakini mama kuna jambo naomba unisaidie mama yangu!”
“Nini baba, sema kama nitaweza nitafanya hivyo!”
“Naomba unisaidie kumbembeleza Bianca, mimi hawezi kunielewa tena!”
“Unasemaje?”

“Unisaidie kumshawishi Bianca akubali kuwa na mimi, siwezi kuhangaika na teja tena!”
“Huo ndiyo uamuzi wa kiume mwanangu, safi sana. Naahidi kukusaidia!”

“Kweli mama?”
“Nitakusaidia mwanangu!”
Genesis alikata simu akiwa na furaha ya ajabu. Hakuona tena thamani ya Farida, sasa alimtaka Bianca kwa nguvu zote.

Je, nini kitatokea? Ni kweli Farida anajihusisha na biashara ya dawa za kulevya?
 
SEHEMU YA 25


Wakiwa hapo, wakiangalia runinga habari ya dharura inaonesha, ni habari ya kushtua sana, kwani msichana wa Kitanzania anaonekana akikamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa King Khalid, mjini Riyadh, Saudi Arabia kwa kosa la kuingia na dawa za kulevya. Msichana huyo ni Farida Mbaraka.

Genesis anachanganyikiwa na kuamua kumpigia simu mama yake, Genesis anamwambia kila kitu na kumlaumu sana Farida lakini mwisho wa yote, anamuomba mama yake amsaidie kuzungumza upya na Bianca!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

MUDA wa kutafakari jambo kwa makini kwa Genesis haukuwepo kwa wakati huo. Alichokuwa akijua ni kwamba Farida alikuwa mwanamke hatari ambaye anahusika na dawa za kulevya. Alishidwa kuelewa ni lini alianza kujihusisha na biashara hiyo haramu.

Alianza kumchukia kuliko kawaida, mapenzi yake yote yakayeyuka. Hakuwa mwanamke sahihi tena kwake.

Alichopanga kichwani mwake ni kuzungumza na Bianca ili afunge naye ndoa haraka sana mara baada ya kumaliza masomo. Hilo tu, ndilo lililoutawala ubongo wake.
Farida kwake alikuwa msaliti na mwanamke hatari ambaye angeweza kumsababishia matatizo makubwa.

“Kesho lazima niende nyumbani, hata kama nina mitihani, nitakwenda usiku. Lazima nikazungumze vizuri na wazazi wangu!” Aliwaza Genesis muda mfupi baada ya kukata simu aliyokuwa akizungumza na mama yake.

“Haikuwa riziki yangu, si mwanamke ninayemtaka, kwa tabia zake hizo, atafute mateja wenzake,” akajisemea Genesis akiwa na maumivu makali moyoni.

Alianza kumchukia Farida lakini kwa kiasi kikubwa ni kama alikuwa akilazimisha hali hiyo, maana moyoni mwake bado alihisi kuwepo kwa chembechembe za mapenzi mazito juu ya Farida. Hakutaka kufanya kitu chochote tena usiku huo, akaamua kwenda kulala.

***
Siku iliisha vibaya sana kwa Genesis, alipata shida sana akiwa katika chumba cha mtihani, kwani muda mwingi alikuwa akifikiria jinsi alivyopoteza muda wake kumhangaikia mwanamke ambaye kumbe alikuwa na tabia mbaya! Alijuta kupoteza muda wake lakini kubwa ambalo alikuwa akigoma kukiri, ni kwamba alikuwa anampoteza mwanamke ambaye alimpenda sana.

Alijikaza kufanya mitihani vyema, jioni akaingia kwenye gari lake na safari ya kwenda Masaki ikaanza. Alipofika nyumbani kwao, akaona magari yote nje, la baba yake na mama yake, hiyo ilikuwa alama tosha kwamba, wazazi wote walikuwa wamesharejea nyumbani usiku huo.

Akaegesha na kushuka kisha akaanza kupiga hatua za taratibu kuelekea kwenye mlango mkubwa wa kuingia ndani. Alipoingia sebeleni akawaona wazazi wote kwa pamoja wakiwa wamekaa pale sebuleni wakiangalia runinga.

Kuanzia pale mlangoni, akapiga magoti na kuanza kutambaa hadi kwa baba yake ambapo alianguka miguuni mwake na kuanza kulia kwa uchungu.

“Baba nisamehe, naomba msamaha wako baba...” akasema Genesis kwa sauti iliyojaa majonzi huku akilia.
“Amka mwanangu, keti tafadhali!”
“Nisamehe kwanza baba, najuta kutokuwasikiliza. Sikujua kama Farida ni hatari kiasi kile.”

“Sawa, keti pale.”
“Lakini Genesis tulikuambia lazima upate muda wa kutosha kumchunguza Farida lakini ukatuona sisi ni wapumbavu, sasa ona aibu ambayo unatupa!” Mama yake akadakia.

“Ndiyo maana nipo hapa mama, nipo hapa kwa ajili ya kuwataka radhi wazazi wangu. Nimekuwa mpumbavu kuliko kawaida lakini ninyi ni wazazi wangu. Kukosea kwangu hakuniondoi thamani yangu ya awali.

“Naomba mnisamehe wazazi wangu, nimejifunza. Unajua mama wakati mwingine ni vizuri kupitia makosa, maana sasa nimejua mlichokuwa mnakizungumza awali!” Genesis alisema maneno hayo kwa uchungu mkubwa.

“Sisi hatukuwa na tatizo na yule binti, hasa baada ya kuwa amepata chuo, shida yetu ilikuwa, ni lini mmechunguzana vya kutosha? Unajua familia yao vizuri? Sasa kwa papara zako, ndiyo maana haya mambo yametokea!” Profesa Mshana akasema akimwangalia Genesis usoni.

“Naombeni mnisamehe tafadhali!”
“Ok! Hebu kaa hapo kwenye kiti!” Profesa Mshana akasema tena.
“Mmenisamehe?”

“Ndiyo mwanangu, sisi ni wazazi wako. Hatuwezi kuwa na kinyongo na wewe. Mtoto akinyea mkono haukatwi baba, unasafishwa na mkono huo huo unaendelea kulia chakula na mambo mengine. Tumeshakusamehe lakini tunaamini umejifunza au hujajifunza?” Mama yake akasema.

“Nimejifunza mama...nawashukuru sana kwa msamaha wenu, nimeshinda sina amani kabisa leo.”
“Tuliza kichwa chako. Malizia mitihani yako vizuri, ondoa mawazo kichwani mwako!”

“Sawa baba!”
Baada ya hapo walikaa mezani kwa ajili ya chakula cha jioni, hapo ndipo Genesis alipomkumbusha mama yake kuhusu suala la kuzungumza na Bianca.
“Hivi mama umeshazungumza na Bianca?”
“Ndiyo!”

“Amesemaje?”
“Kwa kweli mwenzio amekuwa mgumu kidogo.”
“Mgumu?”
“Ndiyo, anasema huna msimamo!”
“Lakini mama umeshindwa kunisaidia kumshawishi kwa namna yoyote ile?!”

“Nimejaribu sana lakini mwisho amesema anataka kuzungumza na wewe mwenyewe.”
“Kweli?” Genesis akasema kwa mshtuko.
“Ndiyo, kesho mtafute.”
“Sawa mama.”

Walipomaliza kula, Genesis hakuwa na muda wa kusubiri zaidi, akaamua kuagana na wazazi wake ili arudi chuoni. Profesa Mshana akaamua kumtoa hadi nje. Genesis akiwa anataka kuingia ndani ya gari, baba yake akamsimamisha.
“Mwanangu lazima uwe makini sana na wanawake, inahitajika akili sana katika kufanya uchaguzi wa mke.

Asitokee mtu wa kukubadilisha akili yako, mke sahihi kwako ni Bianca. Zingatia hilo baba, wewe ndiye mrithi wangu ninayekutegemea, usiniangushe bwana!” Akasema Profesa Mshana.

“Nimekuelewa vizuri sana baba, ahsante!”
“Safari njema, usiku mwema!”
“Nanyi pia!” Genesis akasema akifungua mlango wa gari.
“Genesis...” Profesa Mshana akaita akigonga dirisha.
“Ndiyo baba!”

“Chukua hizi!” Profesa Mshana akasema akimkabidhi Genesis kiasi cha shilingi laki moja.
“Baba!”
“Vipi?”
“Sijaishiwa bado mzee wangu!”

“Weka mafuta, wewe ndiye dume wangu bwana. Nenda usijali, nimekupatia kwa sababu umenifurahisha kutambua kosa lako na kuwaangukia wazazi wako. Hiyo ndiyo adabu mwanangu, najua hata nikiondoka duniani kesho, utaishi na watu vizuri sana. Umenifurahisa sana mwanangu!”

“Ahsante baba!”
Genesis akawasha gari na kuliondoa taratibu, baba yake akiwa amesimama akimsindikiza kwa macho, Genesis hakujali, akili yake ilikuwa kwa Bianca. Hakuwa tayari kulala bila kuonana naye, alitaka azungumze naye usiku huo huo.

Alipondooka tu maeneo ya nyumbani kwao, akatafuta jina la Bianca kwenye simu yake kisha akaruhusu simu itoke, muda mfupi baadaye Bianca alipokea.
“Habari yako Bianca?”
“Poa.”

“Unaendeleaje?”
“Na nini?”
“Namaanisha hali yako!”
“Sema kilichokufanya unyanyue simu unipigie!”

“Bianca punguza hasira tafadhali, nahitaji kuzungumza na wewe. Najua nimekukosea lakini nipe nafasi japo kidogo tu niongee na wewe mama. Najua utanielewa, tafadhali naomba unikubalie!”
“Genesis!”

“Naam!”
“Naomba unisikilize kwa makini sana, tena uweke masikio yako wazi maneno yangu yaweze kupenya vizuri kwenye ngoma za masikio yako!”
“Nakusikia mama.”

“Moyo wangu siyo wa majaribio, siyo wa kuumizwa na kuachwa kila siku. Nimekupenda na kukupa kila aina ya mapenzi lakini unaniona mjinga na kumfuata huyo teja wako Farida. Leo hii unajifanya unataka kuzungumza na mimi kwa sababu Farida amekamatwa, akiachiwa umrudie tena siyo?” Bianca alisema kwa dharau na hasira sana.

“Siyo hivyo mpenzi wangu, mambo yote haya sikuyajua kabla, naona Mungu ameamua kunionesha ili nirudi tena kwako. Tafadhali nipe nafasi nikutane na wewe usiku huu. Lazima nizungumze na wewe!” Akasema Genesis lakini hakujibiwa.

“Halooo! Haloo! Haloo Bianca...” Genesis aliita lakini hakuitikiwa, muda mfupi baadaye akagundua kwamba alikuwa akizungumza kwenye simu iliyokatwa!

“ANANIKATIA simu mimi? Bianca amefikia hatua ya kunikatia simu, haiwezekani!” Akajisemea Genesis akiongeza mwendo wa gari.

Alikuwa akiendesha gari kwa kasi ya ajabu, ilikuwa lazima usiku huo akutane na Bianca na kuzungumza naye. Isingekuwa rahisi kulala bila kukutana naye. Farida alikuwa mbaya sana katika maisha yake, alimchukia kuliko kitu chochote.

“Chanzo cha haya yote ni yule teja, kama siyo yeye ningekuwa nipo na Bianca wangu. Kama ningewasikiliza wazazi wangu tangu mwanzoni, haya mambo yasingetokea kabisa. Farida ni hatari sana, hafai!” Akazidi kuwaza Genesis.

Akapata wazo lingine, aliamua kumtumia Greyson azungumze na Bianca ili akubali kukutana naye usiku huo. Mara moja akachukua simu yake na kumpigia Greyson. Simu iliita muda mfupi sana kabla ya Greyson kupokea.
“Vipi kaka?”
“Poa, uko wapi?”
“Natokea nyumbani nakuja chuo!”
“Nipe mpya?”

“Sina mpya mshikaji lakini kama unavyojua tena nataka kuzungumza na Bianca, Farida ameshakuwa siyo tena!”
“Sasa si umpigie?”
“Huwezi kuamini, majibu aliyonipa hayafai!”
“Kivipi?”
“Kifupi hataki kukutana na mimi!”
“Sasa?”

“Ndiyo maana nimekupigia kaka, naomba unisaidie kumtafuta, mimi nipo njiani nakuja. Hadi nikifika hapo uwe umeshamuweka sawa!”
“Poa.”

“Kaka jitahidi, Jumamosi nitakupeleka Bagamoyo kwa bili yangu, tena uje na shemeji kabisa!”
“Sawa, itakuwa poa kama na Bianca naye atakuwa na sisi huko.”

“Wewe ndiye wa kumaliza ndugu yangu, nakutegemea, fanya mambo.”
“Poa, nitajitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu!”
“Haya kaka.”

Genesis akakanyaga mafuta sawasawa, aliendesha kwa kasi kama alikuwa kwenye mashindano ya magari. Alitakiwa kuwahi chuoni haraka ili aweze kukutana na Bianca. Farida hakuwa na thamani tena.
***
“Enhee imekuwaje?”
“Mwenzangu...amenipigia!”
“Ikawaje sasa?”
“Anataka kukutana na mimi!”
“Umemjibu nini?”
“Nimemkatia simu!”

“Ha! Ha! Ha! Umemkatia simu?”
“Ndiyo nimemkatia simu, halafu nimezima kabisa, ni sasa hivi ndiyo nimewasha ili nikupigie!”
“Safi kabisa mwanangu, lazima umsumbue kidogo ili aone umuhimu wako, naye sijui kwa nini mwanangu anang’ang’ania mateja wakati mwanamke mzuri upo kwa ajili yake!”

“Yaani mama acha tu, nimeamini penye miti hapana wajenzi mama!”
Haya yalikuwa mazungumzo kati ya mama Genesis na Bianca usiku huo, muda mfupi baada ya Genesis kuondoka nyumbani kwao akielekea chuoni. Ni mama Genesis ndiye aliyemuagiza Bianca amsumbue kidogo Genesis ili aone umuhimu wake, jambo ambalo Bianca alilifanya.

Hakutaka kumkubalia haraka, wakati akijibizana naye vibaya kwenye simu, ndani ya moyo wake alikuwa akiugulia ndani ya mapenzi mazito na kama Genesis angebadilisha mawazo basi angeteseka sana. Hiyo ilikuwa siri yake na mama yake.

“Sasa usimtese sana, kama akikupigia tena kubali kukutana naye!” Hatimaye mama Genesis akasema.
“Lakini uwe makini na masharti yako yaendelee kuwa yale yale. Unatakiwa kuwa na msimamo na aelewe thamani yako kama mwanamke!”

“Nimekuelewa vizuri sana mama.”
“Ahsante sana binti yangu, nafurahi kwa jinsi unavyoelewa mambo haraka.”
“Usiku mwema mama.”

“Nawe pia, mtihani mwema.”
“Tena kesho ndiyo tunamalizia.”
“Vizuri sana, mmalize salama, mkaribie kijijini!”
Wakacheka wote na kukata simu.
***
Genesis alishuka kwenye gari lake baada ya kuegesha kisha akaanza kutembea kwa mwendo wa kasi kwenda bwenini kwake. Tofauti na matarajio yake, hakumkuta Greyson. Hapo ndipo alipoamua kupigia simu.
“Uko wapi Greyson!”
“Nipo hapa Hill Park!”
“Umempigia?”

“Ndiyo!”
“Amesemaje?”
“Leo hana muda wa kukutana na wewe!”
“Greyson rafiki yangu, kwa hiyo umeshindwa kabisa kuzungumza naye. Umeshindwa kabisa?”
“Njoo hapa Hill Park tuzungumze vizuri.”
“Sawa kaka, nakuja.”

Genesis akatoka nje, kisha akaanza kutembea taratibu kwa miguu akielekea kwenye daraja dogo lililopo chini ya jengo la Utawala, akapandisha kilima kidogo hadi Utawala, hapo akakata kulia akifuata Barabara ya Changanyikeni. Mbele kidogo ya Kituo cha Polisi cha Chuo Kikuu, akakata kushoto akiacha Benki ya NBC kulia kwake, hapo akaingia Hill Park Bar.

“Umekaa wapi?” Genesis akamwuliza Greyson kwenye simu alipokuwa akiingia kwenye baa hiyo.

“Nimeshakuona, njoo hapa pembeni ya kaunta.”
“Ok! Ah...nimekuona...unakunywa pombe na kesho tuna mtihani? Halafu ah...huyo si Bianca?” Genesis akasema baada ya kumuona Greyson akiwa amekaa na Bianca huku akinywa pombe.

“Acha maneno mengi, njoo kamanda wangu!”
Genesis akakazana hadi kwenye ile meza, alipofika hapo, akakutanisha macho yake na Bianca aliyekuwa amekaa kimya kwenye kiti. Genesis akapiga magoti chini mbele ya Bianca. Tayari macho yake yalishaanza kulengwalengwa na machozi.

“Nisamehe Bianca wangu, dunia imenifunindisha mama, siwezi kubadilika tena, naomba msamaha wako!” Genesis alisema kwa sauti iliyojaa majonzi sana.
“Kaa tafadhali.”

“Umenisamehe?”
“Keti kwanza.”
“Nitaketi utakapokuwa umenisamehe.”
“Genesis...” Bianca akaita.
“Nakusikia.”

“Ni kweli unataka kurudiana na mimi?”
“Kweli mpenzi.”
“Ni kweli umeamua kuachana moja kwa moja na Farida?”
“Kweli mpenzi.”

“Nini kitathibitisha maneno yako?”
“Bianca huwezi kuamini, lakini ndiyo ukweli, NATAKA KUFUNGA NDOA NA WEWE SASA. NAAMINI NDOA NDIYO ITAKUWA KUFULI YA MAPENZI YETU. TUKIMALIZA TU CHUO, NATAKA NIKUOE!”

“Kweli?” Bianca akauliza akionekana kushtuka sana.
“Huo ndiyo ukweli wangu mpenzi, naomba unikubalie!”
“Nimekubali mpenzi.”

Bianca akasimama na kukumbatiana na Genesis. Ilikuwa furaha kubwa sana kwa Genesis lakini kwa Bianca ilikuwa mara mia zaidi ya Genesis. Kilichofuata hapo ilikuwa kula na kunywa mpaka usiku sana.

Je, nini kitatokea? Ndoa itafungwa? Nini kitampata Farida huko Saudi Arabia baada ya kukamatwa na madawa ya kulevya?
 
SEHEMU YA 26


Penzi la Genesis na Farida linayeyuka baada ya Genesis kuona habari kwenye runinga, ikimuonesha Farida akikatamatwa na dawa za kulevya aina ya Heroin katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa King Khalid, jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Ni hapo ndipo alipobadilisha mawazo ya kuamua tena kurudi kwa wazazi wake, akawaangukia na kuwaeleza kwamba amebadilisha mawazo.

Jambo hilo liliwafurahisha wazazi wake. Alichokifanya Genesis ni kuwasiliana na Bianca ili akubali kurudiana naye, lakini cha kushangaza, Bianca akamkatia simu na kuizima kabisa.

Hapo Genesis akaamua kumtumia rafiki yake Greyson, ajaribu kumtafuta Bianca na kuzungumza naye, jambo ambalo Greyson alilifanya na baadaye Genesis alipojaribu kumtafuta, alimjibu kwamba aende Hill Park alipokuwa amekaa, ndipo waweze kuzungumza zaidi.

Kitu cha kushangaza, Genesis alipokwenda pale akamkuta Greyson akiwa na Bianca, jambo hilo likamfurahisha sana. Mazungumzo yakafanyika na mwisho kwa pamoja wakakumbatiana kwa furaha baada ya kusameheana na kufungua ukurasa mpya.
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

“TIMIZA ahadi yako Genesis, tafadhali sana, sitaki uniumize tena, nimeamua kukupa moyo wangu kwa mara nyingine tena, lakini ili nikuamini kwamba huna nia mbaya, inabidi utimize ahadi yako mapema sana,” akasema Bianca akimwangalia Genesis machoni.

“Itakuwa hivyo mpenzi wangu!”
“Kweli baba?”
“Niamini!”

“Nakuamini mpenzi wangu, nakupenda sana Genesis na sitakuwa tayari kukupoteza tena!”Hata mimi pia mpenzi nakuahidi, namchukia sana Farida, mwanamke aliyejifanya ana mapenzi na kujidai mwema kumbe nyuma yake kuna madudu yasiyotamanika!”

“Achana na teja bwana!”
“Mara mbili?”
Wote wakakauka kwa kucheka. Walikuwa na furaha sana, kwanza ya kurudisha mapenzi yao, lakini pili walikuwa wanakwenda kufanya mtihani wa mwisho wa kumaliza masomo yao. Kwao ilikuwa ushindi mkubwa kwa kuwa waliua ndege wawili kwa jiwe moja!

***
Bustani ilikuwa imependeza sana, taa za rangi zilizokuwa zimening’inizwa juu ya miti, zilizidisha mandhari ya bustani hiyo kuwa ya kuvutia zaidi. Ilikuwa tafrija fupi ya kuwapongeza Genesis na Bianca kwa kumaliza masomo yao Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Zilikuwa familia mbili katika bustani hiyo ya kupendeza iliyokuwa ndani ya jumba la kifahari ya Profesa Mshana, Masaki, jijini Dar es Salaam. Dk. Rwegoshora na mkewe walikuwa wamependeza sana, pembeni yao alikuwa amekaa binti yao Bianca. Profesa Mshana alikuwa na mke wake, pamoja na watoto wake wawili; Genesis na Dk. Bernadetha, wote wakiwa na furaha sana.

Kwao ilikuwa zaidi ya sherehe ya kuwapongeza vijana wao kwa kuhitimu na kutunikiwa shahada zao, ilikuwa ni sherehe pia ya kubariki uhusiano wao na kuwashinikiza wafunge ndoa haraka iwezekano.

“Kwanza tunawapongeza sana vijana wetu, kwa hatua hii nzuri mliyofikia. Hakika mnahitaji pongezi. Lakini jambo kubwa zaidi ambalo tunataka kulisikia kutoka kwenu ni kila mmoja kurudisha moyo kwa mwenzake!” Akasema Profesa Mshana akiwaangalia Bianca na Genesis kwa zamu.

“Bianca, je unanihakikishia kwamba, unampenda Genesis kwa dhati ya moyo wako na upo tayari kufunga naye ndoa?” Profesa Mshana akamwuliza Bianca akimwangalia usoni.

“Ndiyo baba, nampenda na nipo tayari kufunga naye ndoa.”
“Vizuri sana...” akasema Profesa Mshana akiwaangalia wazee wenzake.
“Genesis...” akaita Dk. Rwegoshora.
“Naam baba!”

“Je, unanihakikishia kwamba unampenda Bianca kwa dhati na ungependa awe mke wako katika ndoa takatifu?”
“Ndiyo baba, nampenda na ninahitaji kufunga naye ndoa.”
“Ni kweli hutarudi nyuma kumkumbuka Farida?”

“Farida baba? Haiwezekani, yule mwanamke namfananisha na shetani, hawezi kurudi tena katika maisha yangu.
Kwanza naamini muda huu atakuwa ameshanyongwa. Acha afe, simtaki tena!” Akajibu Genesis kwa hasira sana.
“Nimefurahi kusikia hivyo mwanangu, je, wote mpo tayari kuoana?”
“Tupo tayari!” Wote wakajibu kwa pamoja.

“Basi kama yote hayo ni sawa na mmekiri mbele yetu sisi wazazi wenu tunashukuru,” alisema Dk. Rwegoshora.
Kisha akawaamuru watu wote waliuohudhuria hafla hiyo wasimame na kunyanyua glasi zao juu kisha akawataka wazigonganishe kama ishara ya kuwaombea Genesis na Bianca maisha mema na kudumu katika penzi lao.

Watu wote wakasimama, wakanyanyua glasi zao, kisha kwa pamoja wakazigonganisha.
“Chears!!!”

Lilikuwa tukio la furaha sana, kila mmoja alikuwa anatabasamu, maana vijana wao walikuwa wanakwenda kufanya kile walichopenda kitokee kwa muda mrefu sana. Vichwani mwao kulikuwa na ndoa tu; ilikuwa lazima wahakikishe wanafunga ndoa mapema sana.

***
Mipango yote ilikuwa tayari, hakuna aliyepinga harusi ya Genesis na Bianca. Muda mfupi sana baada ya kumaliza masomo yao walipanda madhabahuni kufunga ndoa. Kanisa lilikuwa limejaa watu wengi sana kuhushudia ndoa hiyo.

Kanisa la Mt. Peter lilifurika watu, wakiwa na nyuso zinazowakilisha kilichokuwa ndani ya mioyo yao. Ni wazi kwamba walikuwa na furaha isiyo na kifani. Tayari Genesis na Bianca walikuwa mbele ya Padri Mathayo Mnaa, akiwafungusha ndoa takatifu.

“Ndugu Genesis Greyson Mshana, umekubali kumuoa Bi Bianca Rwegoshora ili awe mke wako katika dhiki na faraja, njaa na shibe, katika furaha na shida, umtunze, akutunze mpaka kifo kiwatenganishe? Kama ndiyo...jibu ndiyo Mungu nisaidie!” Akasema Padri Mathayo Mnaa akiwamwangalia Genesis aliyekuwa amependeza sana na suti ya rangi nyeusi.

“Ndiyo, Mungu nisaidie!” Genesis akajibu kwa utulivu.
Vigelegele, shangwe na makofi vikalipuka ukumbini humo wakishangilia jibu la Genesis. Baada ya hapo, Padri akamgeukia Bianca na kumwuliza: “Bi Bianca Rwegoshora, umekubali kuolewa na Bwana Genesis Greyson Mshana awe mume wako katika dhiki na faraja, njaa na shibe, katika furaha na shida, umtunze, akutunze mpaka kifo kiwatenganishe? Kama ndiyo...jibu ndiyo Mungu nisaidie!”

“Ndiyo Mungu nisaidie!” Bianca naye akajibu na kusababisha shangwe kanisani.
“Mmejibu vema...kwa kuwa mmejibu kwa vinywa vyenu wenyewe, kwa ridhaa na dhamira ya dhati kutoka ndani ya mioyo yenu mbele ya mashahidi hawa wa Parokia hii. Kwa mamlaka niliyopewa na Kanisa pamoja na maagizo ya Mungu, nawafungisha ndoa hii takatifu, mwende mkawe mwili mmoja katika Kristu Yesu...katika Jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu...Amen....” Padri Mnaa akasema.

“Amen!” Kanisa zima likaitikia.
“Enendeni sasa mkaishi pamoja, mkatunzane kwa dhati na mzae na kuijaza nchi!”
Hivyo ndivyo ndoa yao ilivyofungwa, maharusi wakavalishana pete kisha wakaweka sahihi zao kwenye vyeti vya ndoa na baada ya hapo, wakarudi kwenye viti vyao kuketi. Ibada ikaendelea mpaka mwisho, safari ya kwenda ukumbini ikaanza.

***
Mamia ya watu walikuwa wamefurika ndani ya Ukumbi wa Pundamilia ulio ndani ya hoteli ya maarufu ya Atrium, karibu kila mtu maarufu nchini Tanzania alikuwa ndani ya ukumbi huu. Kuanzia Rais, Mawaziri, Makatibu Wakuu, wanamichezo, wasanii na wafanyabiashara wakubwa wa Kiasia na Afrika.

Hakika ilionekana siku ya furaha, watu wakiwa wameketi kwenye meza zao wakiendelea kunywa vinywaji taratibu. Wanaume wakiwa wamevalia suti nyeusi na wanawake magauni ya rangi nyeupe na zambarau, hakika walipendeza.

Kila Genesis alipozungusha macho yake huku na kule ndani ya ukumbi alionekana kutoamini kilichokuwa kinatendeka, hatimaye baada ya safari ndefu ya kupanda na kushuka milima, alikuwa amemuoa Bianca Rwegoshora, mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wazazi na ndugu wa pande zote mbili walionekana kufurahia kila kitu kilichokuwa kikitokea ukumbini, kwao hakika ulikuwa ushindi, walikuwa wamefanikisha kutokea kwa jambo ambalo kwa muda mrefu walilihangaikia sana, kuhakikisha kwamba Genesis anamuoa Bianca badala ya Farida Mbaraka, kisa tu alikuwa ni mtoto aliyetokea familia duni, wazazi wake wakiwa hawana elimu hata ya darasa la saba. Hicho ndicho kilikuwa kikwazo, hakuna aliyeuangalia uzuri wake, wala ukarimu wa moyo wake, alihukumiwa sababu ya umasikini wake, hakika iliuma.

Pamoja na yote hayo, Genesis alishindwa kabisa kuzuia hisia zake, bado alimkumbuka sana Farida. Pamoja na kwamba alishamtoa moyoni na kuamua kufunga ndoa na Bianca lakini ndani ya nafsi yake bado aliendelea kumkumbuka.

Alishangazwa na hali ile iliyomwingia ghafla na kwa kasi sana moyoni mwake, alishaachana kabisa na Farida akiamini alikuwa ni mtumiaji na muuzaji wa dawa za kulevya, lakini muda huu ambao tayari ameshafunga ndoa, anashangaa mwanamke huyo anamuingia moyoni mwake kwa kasi ya ajabu sana.


ZILIKUWA hisia kali kuliko kawaida, hisia ambazo zilimjia kwa kasi na kuanza kumfikiria upya Farida. Alishangaa mapenzi yake yakirudi kama zamani na kutamani sana Farida ndiye angekuwa amekaa kushoto kwake pale ukumbini katika ndoa yake ile, awe ndiye mkewe.

Hilo halikuwezekana kwani tayari alikuwa ameshachelewa. Jambo hilo lilisababisha furaha yake ipotee, uso wake usawajike na kupoteza nuru. Tabasamu likajificha na kwa mtu yeyote ambaye alimfahamu vizuri Genesis, basi ilikuwa rahisi sana kufahamu kwamba hakuwa katika hali yake ya kawaida. Bianca aliweza kugundua hilo na kuamua kumuuliza.

“Genesis!” Ilikuwa ni sauti ya Bianca akimuita.
Genesis akageuza kichwa chake na kumwangalia.
Ilikuwa lazima atumie akili nyingi sana katika kumfanya asigundue kwamba alikuwa na mawazo. Akausogeza mdomo wake karibu na wake na kumbusu. Kitendo kile kiliwafurahisha sana wapiga picha ambao walijua cha kufanya!

“Pyaaaaa... Pyaaaaaa... Kwachaaa...” zilikuwa ni kamera zikifyatua huku mwanga wa flash ukizidisha umaridadi wao.
“Yes sweetie!” (Ndiyo mpenzi) Genesis akaitika baada ya kutoa mdomo wake kwenye lipsi za Bianca.

“What is going on your mind?”(Nini kinaendelea mawazoni mwako?) Bianca alimuuliza Genesis.
“Why?”(Kwa nini?)
“You seem to be contemplating too hard!”(Unaonekana kufikiria sana.)

“No! I am just thinking about our future, where we have come from, where we are and where we are going!”(Hapana! Nafikiria tu kuhusu maisha yetu ya baadaye, tulikotoka, tulipo na tunakokwenda!) Genesis akajaribu kudanganya huku ndani ya moyo wake kukiwa na kitu tofauti kabisa na alichokitamka kinywani mwake.

“Isn’t Farida on your mind?”(Farida hayupo kichwani mwako?)
“Me? No way! That drug dealer? Probably she is dead by now!” (Mimi? Huyo muuza dawa ya kulevya? Labda amekwishakufa) Aliongea Genesis akichukua kitambaa na kujifuta machoni.

Alichokitamka kilikuwa tofauti kabisa na ukweli uliokuwa moyoni mwake. Alikuwa akimpenda sana Farida, tena kwa kasi kuliko kawaida lakini haikuwa rahisi kukubali ukweli huo. Kila jina lake lilipotajwa, huzuni iliingia moyoni mwake na machozi kumlengalenga!

Hakuwahi kukutana na msichana mwenye sifa kama zake, hakika alimpenda sana. Alikuwa na sifa zote, kuanzia uzuri wa sura, maumbile, tabia na mwenendo wake. Hivyo ndivyo alivyohitaji kutoka kwa mwanamke wa kuishi naye maisha.

“Then why are you so sad? Are you not happy that we are finally married?”(Sasa kwa nini una huzuni siku ya harusi yetu? Haufurahii kwamba hatimaye tumeoana?) Hatimaye Bianca akamuuliza Genesis.

“I am so happy and excited, though I can’t stop myself thinking of Farida!”(Nina furaha sana ingawa siwezi kujizuia kumfikiria Farida!) Genesis akasema akiwa na dhamira ya kutua mzigo mzito uliokuwa moyoni mwake.

“But a few minutes ago you said she is not on your mind!”(Lakini dakika chache zilizopita ulisema hayupo akilini mwako!)
“Let me just be brutally honest with you! I can’t stop thinking of Farida!”(Acha tu niwe muaminifu kupita kiasi, siwezi kuacha kumfikiria Farida) Genesis aliongea maneno hayo akimwagalia Bianca usoni ambaye aliinamisha kichwa chake chini kuonesha maelezo yale yalimuumiza lakini kwa Genesis ilikuwa ni bora aumie akiwa amemwambia ukweli.

Haikuwa rahisi kumsahau Farida, kila siku alimsumbua akili na mawazo yake, mpaka wakati huo alikuwa hajaamini kabisa kwamba alikuwa ni mfanyabiashara wa dawa za kulevya, aliyekamatwa na dawa hizo nchini Saudi Arabia siku ya kwanza tu, baada ya kuingia nchini humo kwa ajili ya kujiunga na Chuo Kikuu Huria cha Arab.

Kwa nchi za Kiarabu, hukumu pekee kwa mtu aliyekamatwa akijaribu kuingiza dawa za kulevya ilikuwa ni kupigwa risasi mbele ya kadamnasi hadi kufa; ndiyo hukumu iliyokuwa ikimkabili Farida nchini humo.

“Lakini aliondoka kwa lengo la kwenda kujiunga na Chuo Kikuu Huria cha Arab, naye akitamani awe angalau na digrii na familia yangu iweze kumkubali. Alifanya kila kilichowezekana ili wazazi wangu wampende. Hivi ni kweli Farida alikuwa akifanya biashara ya dawa za kulevya?” Alijiuliza Genesis bila kupata majibu.

Ingawa Bianca alikuwa pembeni yake, tena siku ya harusi yao! Bado kichwani mwake alikuwemo Farida. Fikra za kwamba angekuwa amekwishapigwa risasi mpaka wakati huo zilimsumbua sana kiasi cha kumfanya asifurahie kitu chochote kilichokuwa kikiendelea ukumbini ingawa karibu kila mtu alishangilia wao kufunga ndoa. Kitu pekee kilichokuwa kichwani mwake ilikuwa ni kuondoka ukumbini na kwenda chumbani kupumzika.

Kuna kitu kilianza kumwambia kwamba alitakiwa kuchunguza zaidi, alikataa kabisa kuamini kwamba Farida alikuwa akifanya biashara ya dawa za kulevya. Kila alipojaribu kumfikiria vizuri Farida kichwani mwake, alishindwa kupata majibu ya moja kwa moja.

Yalikuwa mawazo ya ajabu sana, ambayo kuna wakati alikuwa akishangaa ni kwa nini hayakuja mapema kabla hajapanda madhabahuni na kufunga ndoa na Bianca. Alianza kuamini huenda kama angepata muda wa kufuatilia na kuchunguza zaidi, angegundua kitu kingine zaidi nyuma ya tukio lile. Kwa wakati huo hakuwa na la kufanya zaidi ya kujilaumu.

Akiwa katika mawazo hayo, ghafla simu yake ikaingiza ujumbe mfupi wa maneno, akajua ni kutoka kwa baadhi ya rafiki zake waliompongeza kwa kufunga ndoa lakini alipofungua ujumbe huo ilikuwa tofauti kabisa! Alikutana na maneno; SIRI KUBWA.

Akaanza kuendelea kusoma, ambapo alikutana na anwani ya barua pepe ya Bianca, pia kukiwa na maneno ya siri. Chini yake kulikuwa na maandishi yaliyosomeka: “Tumekuletea hii ili uingie kwenye sanduku la barua pepe la mkeo upate kumwelewa vizuri na unyama aliomfanyia Farida!”

Genesis akashtuka sana, moyo wake ukaruka mapigo kadhaa, jasho likaanza kumtoka, huku akihisi presha yake kuanza kushuka kwa kasi. Hakuwa na hamu tena ya kukaa ukumbini. Alitaka kwenda chumbani kwa ajili ya kuangalia kwenye anwani ya barua pepe hiyo ili kuona ukweli uliojificha! Muda huo huo akamgeukia Bianca.
“Sijisikii vizuri!”

“Nini tena?”
“Nataka kwenda kupumzika, ni vizuri tukaondoka.”
“Genesis, tuondoke mapema kiasi hiki? Kabla wazazi hawajaondoka?”

“Naumwa!” Alisingizia huku akigeuza kichwa na kuongea na Kelvin, mpambe wake.
“Vipi tena?” Kelvin aliuliza.
“Aisee mwambie MC atangaze kuwa tunaondoka kwenda chumbani kupumzika.”

“Eti shemeji?” Kelvin alimuuliza Bianca.
“Kama yeye ameamua mimi sina kizuizi.”

Bila kipingamizi, Kelvin alifanya kama alivyoombwa. MC akatangaza juu ya kuondoka kwao na watu wote wakasimama huku wakishangilia.

Walitembea kwa madaha lakini Genesis alikuwa akijilazimisha, ndani ya moyo wake alikuwa na mzigo mzito wa mawazo. Alitaka kujua siri iliyojificha katika anwani ya barua pepe ya mkewe.

Je, nini kitatokea? Kuna siri gani na ni nani amemtumia?
 
SEHEMU YA 27


Baadaye Genesis hakuona sababu ya kuendelea kuficha, akaamua kuwa mkweli kwamba hawezi kuacha kumfikiria Farida. Bianca akashtuka sana lakini Genesis akamhakikishia kwamba, hawezi kumfikiria mtu anayejihusisha na dawa za kulevya.

Wakiwa katika majibizano hayo, simu ya Genesis ikaingiza ujumbe mfupi wa maneno, akachukua na kufungua, ndipo alipokutana na maneno ya kushtua sana. Katika ujumbe ule maneno yalisomeka: “Siri kubwa”

halafu mbele yake kukiwa na maneno “Tumekuletea hii, ili uingie kwenye sanduku la barua pepe la mkeo, ili upate kumwelewa vizuri na unyama aliomfanyia Farida!”

Genesis akashtuka sana, hakuwa tayari kuendelea kukaa pale ukumbini akiwa na mzigo wa mawazo, akamuomba mpambe wake Kelvin amwambie MC atangaze kwamba wanakwenda kupumzika. Hilo likafanyika haraka sana na watu wote wakasimama na wao kutoka nje wakishangiliwa!
Pamoja na kushangiliwa huko, ndani ya moyo wa Genesis hakukuwa na furaha kabisa.
Je, nini kitatokea? Kuna siri gani? SONGA NAYO...

SHANGWE na vigelegele kutoka kwa wageni waalikwa vilikuwa furaha kwa Bianca lakini kwa Genesis, ilikuwa sawa na makelele masikioni mwake. Ndani ya moyo wake alikuwa na donge zito lililomsumbua na kumtesa!

Alitaka kujua ni nini alikuwa ameambiwa aangalie kwenye anuwani ya barua pepe ya Bianca. Mapigo ya moyo wake yakawa yanabadilika na kupiga kwa kasi sana, baada ya mwendo kidogo wakawa wamefika nje ya ukumbi huo mkubwa na wa kisasa kabisa jijini Dar es Salaam.
Nje waliingia kwenye lifti na kupanda hadi ghorofa ya tatu kulipokuwa na chumba chao. Kelvin na mke wake Martina walikuwa pamoja nao mpaka ndani ambako bila kuchelewa waliwaaga na kuondoka.

Kitu cha kwanza Genesis alichofanya ilikuwa ni kwenda kwenye kompyuta yenye mtandao wa ‘intaneti’, haraka akaiwasha na kuingia kwenye tovuti ya g-mail akaandika bianca10@gmail.com, kisha kwenye neno la siri akaandika neno hadohado, hayo ndiyo yalikuwa maneno ya siri ya anuani ya barua pepe ya Bianca. Aliyafanya yote hayo Bianca akiwa amejilaza kitandani, bila kumsogelea.

Akabonyeza sehemu iliyoandikwa ‘sign in’, muda mfupi tu baadaye sanduku la barua pepe la Bianca likafunguka, iliyokuwa juu kabisa iliandikwa “The truth about innocent Farida Mbaraka”

Maneno yaliyomaanisha ukweli kuhusu Farida Mbaraka asiye na hatia. Moyo wa Genesis ukapiga kwa kasi, jasho likimtoka huku akisubiri ifunguke, sekunde chache baadaye kila kitu kilikuwa wazi, akaanza kusoma huku akibubujikwa na machozi, mara kadhaa aligeuza shingo yake kumwangalia Bianca aliyekuwa amejilaza kitandani, hasira zikazidi kumpanda zaidi na zaidi, akamwonea Farida huruma kiasi cha kutamani kuua, hakustahili unyama aliotendewa kwa sababu yake. Kwa kitendo kile, hakumchukia Bianca peke yake bali pia hata familia yake.

Hatimaye akafikia uamuzi wa kufanya alichoona kinafaa, kama Farida alikuwa ameshapigwa risasi sababu ya dawa za kulevya ambazo hazimiliki, basi waliofanya mpango huo ilikuwa lazima wafe. Moyo wa Genesis ulishachafuka, alikuwa na hasira kuliko kawaida.

Mara moja akanyanyuka alipokuwa ameketi na kutembea mpaka kwenye meza iliyokuwa pembeni, juu yake kulikuwa na sinia lenye chakula, pia vikiwepo visu na uma. Akachukua kisu kimoja kikali.

“Hiki kinatosha!” Akawaza akikichukua kisha kuanza kutembea taratibu hadi kitandani alipolala Bianca akiwa hajui kilichoendelea.

Genesis akahesabu moja mpaka tatu kisha akaushusha mkono wake kwa kasi kifuani mwa Bianca upande wa moyo, damu nyingi zikaruka na kulowanisha nguo zake, mara moja akakichomoa tena na kukizamisha mara ya pili kisha kuchukua mto na kumgandamiza nao Bianca mdomoni ili kelele zake zisitoke nje, dakika tano baadaye alitulia, tayari alishakufa.

“Mungu wangu nimefanya nini? Kwa nini nimeua? Si ningemwacha tu na kutafuta mwanamke mwingine?” Aliwaza Genesis lakini haikuwa na maana kwa wakati huo.

Alikuwa ameshachelewa, kwani Bianca tayari alikuwa marehemu. Damu nyingi ilikuwa ikibubujika kutoka kifuani kwa Bianca na kulowanisha mashuka huku nyingine ikitiririka hadi sakafuni. Mikono na suti ya Genesis ililowa vibaya.
Bianca alikuwa ndani ya shela, akihangaika kitandani wakati roho ikijaribu kuutoka mwili.

Ubongo wake ukafanya kazi kwa kasi kuliko kawaida, Genesis alikiona kitanzi mbele yake. Ilikuwa lazima anyongwe kutokana na kosa la mauaji yale. Uamuzi mmoja ukaingia kichwani mwake, ilikuwa lazima ajiue ili kuukwepa mkono wa serikali. Alitumia kwa muda akitafakari jinsi ya kujitoa uhai wake. Akaamua kujirusha kutoka ghorofa ya tatu hadi chini, akiamini angekufa!

Hicho ndicho alichokifanya! Alitaka kuukimbia uso wa dunia, akitamani siku moja kukutana na Bianca pamoja na Farida mbele ya haki, aliyeamini lazima atapigwa risasi na kufariki, huko ndipo wangezungumza na kujadili kilichotokea duniani.

Ilikuwa kitendo cha sekunde moja tu, Genesis akapanda juu ya dirisha na kujirusha chini, akiamini hadi akifika chini kabisa, angekuwa ameshafariki dunia. Huo ungekuwa mwisho wake wa mateso ya moyo duniani. Kwake ilikuwa bora kufa kuliko kuendelea kubaki hai, akafumba macho yake ili asione kitakachotokea.

***
“Puuuu!” Ulikuwa mlio wa Genesis baada ya kuanguka chini.
Kwa bahati nzuri Genesis alianguka upande wa nyuma wa hoteli hiyo kwa hiyo hakukuwa na mtu yeyote aliyemuona. Tofauti na matarajio yake, aliangukia
miguu na hakupata maumivu kama alivyotegemea kukatisha uhai wake. Kwa dakika tano nzima alibaki amekaa pale chini kama ameduwaa. Kishindo chake hakikusikika kutokana na sauti ya muziki kutoka ukumbuni kuwa kubwa.

“Hapanifai hapa!” Aliwaza akifikiria kitu cha kufanya.
Kitendo cha kuendelea kubaki eneo lile, ilikuwa ni sawa na kujiacha mdomoni mwa simba, kwani muda wowote kama ingejulikana kwamba amemuua Bianca basi angekamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria ambapo hukumu yake lazima ingekuwa ni kunyongwa!

Akaangaza macho yake huku na huko na kujiridhisha kwamba hakuonekana na mtu yeyote. Akasimama na kujipanguza vumbi kisha akaanza kupiga hatua za taratibu kuelekea kwenye geti la nyuma la kutokea nje.

Kwa bahati nzuri geti lilikuwa wazi na hapakuwa na mlinzi, mara moja akatoka hadi nje, ambapo alizunguka hadi barabarani na kusimamisha teksi. Gari liliposimama alikuwa ameshaingia ndani na kumwelekeza dereva nyumbani kwao.

Gari liliondolewa kwa kasi kama alivyoagiza. Alipofika aliingia moja kwa moja hadi ndani. Mlinzi getini akashangazwa sana na hali aliyokuwa nayo Genesis, tayari taa nyekundu ilishawaka kichwani mwake, kama asingekuwa makini yule mlinzi angewasiliana na wazazi wake kumwuliza kilichotokea.
“Vipi Genesis mbona upo katika hali hii?”
“Hali gani?”

“Kwanza ulipaswa kuwa ukumbini.”
“Lakini Juma hiyo siyo kazi yako!”
“Samahani!”
“Hebu naomba simu yako!”
“Ya nini?”

“Nina shida nayo!”
Juma akatoa na kumkabidhi Genesis ambaye aliichukua na kuingia nayo ndani. Aliichukua ile simu kwa lengo la kukatisha mawasiliano kati yake na wazazi wake, hakuwa na lengo lingine zaidi ya hilo.

Mara moja akavua ile suti kisha akavaa suruali ya jinzi na tisheti nyeusi, akachukua fedha za kutosha, kisha akaingia chumbani kwa wazazi wake na kuvunja droo na kuchukua fedha.
“Hapa nipo sawa!”

Alihakikisha amechukua kila kitu, ikiwemo hati yake ya kusafiria, hakuwa na begi kubwa, alibeba begi dogo sana aliloweka suruali mbili na tisheti mbili tu.
“Hapa nipo sawa!” Akajisemea akitoka nje lakini akilini akiwa hajui anapokwenda.

HAKUTAKIWA kupoteza hata sekunde tano, kufanya hivyo kungemaanisha angeingia mikononi mwa polisi, mara moja na tuhuma za mauaji dhidi yake zingemkabili. Genesis anatoka akiwa hana amani kabisa moyoni mwake.

Matumaini yake yote yametoweka, ndoto zake zimefifia, siku ya ndoa yake ambayo kimsingi ilitakiwa kuwa ya furaha imegeuka kuwa ya majonzi na msiba. Alikuwa na majeraha makubwa sana moyoni mwake, akiwa haamini kama safari yake ya kielimu ingeishia vibaya kiasi kile.

Akapiga hatua ya kwanza, ya pili, tatu akiwa bado hajajua uelekeo wake. Akasimama ghafla na kuwaza. Sekunde tano baadaye akagundua kwamba kitendo kile kilikuwa cha hatari, hakutakiwa kusimama.

“Natakiwa kuondoka, lakini sijajua kwamba natakiwa kwenda wapi! Anyway ngoja niangalie gari kwanza!” Akawaza huku akianza kupiga hatua za taratibu kwenda kwenye sehemu yalipoegeshwa magari.

Akayaangalia yote, gari lake aina ya Toyota Rav 4 lisingeweza kutembea mwendo mrefu, lakini VX ya baba yake ingeweza kumtorosha kwa uhakika. Akarudi ndani na kwenda moja kwa moja chumbani kwa wazazi wake, akachukua funguo na kutoka.

Alipofungua mlango, aliondoa gari kwa kasi mpaka getini aliposimamishwa na mlinzi.
“Juma unafanya nini?” Genesis akamwuliza mlinzi akionekana kukasirika.
“Unakwenda wapi?”

“Hiyo siyo kazi yako!”
“Inaweza kuwa kazi yangu, kwa sababu umetoka na gari la mzee, siku zote bosi hataki gari hili liguswe na mtu yeyote zaidi yake!”
“Juma!” Genesis akaita.
“Naam!”
“Hebu sogea hapa!”
Juma akasogea taratibu ili aweze kumsikiliza, lilikuwa kosa kubwa sana, Genesis alitoa mkono wake na kumpiga kibao kikubwa usoni.

“Pumbavu kabisa, fungua geti nyama wewe!” Genesis akasema kwa hasira.
Hakutaka kupotezewa muda, laiti kama Juma angejua kilichokuwa kikimsumbua Genesis, angemruhusu aondoke haraka eneo lile ili aweze kukwepa mkono wa dola, lakini hilo hakulijua. lilikuwa ni siri ya Genesis mwenyewe!
“Nafungua, lakini naomba basi simu yangu!”
“Simu?”
“Ndiyo!”

“Si nilikuambia nina shida nayo?”
“Sawa!”
Juma akafungua mlango na Genesis akaliondoa kwa kasi sana. Macho yake yalipotua kwenye saa iliyokuwa kwenye gari, akagundua kwamba ilikuwa imeshafika saa 6:21 za usiku. Genesis akaendesha gari kwa kasi kama limeibiwa!

Mpaka alipofika kwenye mataa ya Ubungo bado Genesis alikuwa hajajua anapotaka kwenda, ingawa taa ya kuongoza magari iliwaka nyekundu, yeye hakusimama, aliangalia huku na huko aliporidhika kwamba magari yalikuwa yamesimama alipita moja kwa moja!
“Acha niende Nairobi, huko nitajua cha kufanya!” Akawaza akikanyaga mafuta sawasawa.

Kikubwa kilichokuwa mbele yake ilikuwa ni kukimbia mkono wa dola. Aliendesha gari kwa kasi kuliko kawaida. Hata alipokutana na vizuizi njiani na kusimamishwa na askari hakufanya hivyo.

Saa 12:15 za asubuhi alikuwa akipita kwenye keep- left cha Moshi Mjini, eneo ya YMCA akiachana na njia inayokwenda katikati ya mji na ile inayoelekea katika Hospitali ya KCMC na kunyoosha moja kwa moja akiifuata barabara ya Arusha.

Njia nzima alihakikisha anasikiliza Radio One akiamini kwamba kama kungekuwa na habari yoyote ya dharura, kituo hicho kingekuwa cha kwanza kurusha matangazo hayo kupitia mpango wao wa ‘Radio One Breaking News.’

Dakika arobaini baadaye alikuwa anaingia Arusha Mjini, akiwa amechoka sana. Alipofika Mianzini, aliingia ndani kidogo na kuegesha gari lake kisha akatulia akitafakari kitu cha kufanya. Akiwa katikati ya mawazo, akasikia taarifa iliyomshtua sana katika redio yake iliyokuwa ndani ya gari.

“Binti wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Bianca Rwegoshora amekutwa amekufa ndani ya chumba cha Hoteli ya Atrium, Afrikasana jijini Dar es Salaam, ikiwa ni muda mfupi baada ya kufunga ndoa na mtoto wa Profesa Mshana aitwaye Genesis.

“Maiti ya Bianca imeonekana kupigwa kisu tumboni. Hata hivyo bwana harusi Genesis Mshana, hajulikani alipo, mpaka sasa. Polisi bado wanaendelea na uchunguzi.”

Genesis akashtuka sana. Ni wazi kwamba kila kitu kilikuwa kimeshaharibika na alikuwa anatafutwa popote alipo. Alivuta pumzi ndefu sana kisha akazishusha taratibu kabisa, akijaribu kufikiria cha kufanya.
“Hapa lazima niwe makini, naamini hata baba ameshagundua kwamba mimi ndiye muuaji na hata gari lake atajua nimeamua kuliiba! Nitafanya nini sasa?” Aliwaza bila kupata majibu.

Baadaye akagundua kwamba hatakiwi kutumia muda mwingi kufikiria, kwani kufanya hivyo ingekuwa rahisi kukamatwa. Akashuka haraka na kuchukua begi lake na akatembea kwa miguu akiliangalia lile gari!

Alishaamua kulitelekeza, gari lile halikuwa na maana yoyote tena kwake, wakati alikuwa akisakwa kila kona. Akachepuka kidogo hadi barabarani alipoingia kwenye taxi moja iliyokuwa imeegeshwa.

“Unajua kuendesha gari vizuri kaka?”
“Salamu kwanza ndugu yangu, mimi ni mzima!” Dereva akasema akitabasamu.
“Salamu kwangu haina maana kubwa sana kama kuwahi ninapokwenda, hebu nijibu unaweza kuendesha gari vizuri?”
“Inawezekana sijajua vizuri maana yako, hebu fafanua kidogo.”
“Unaweza kukimbiza?”
“Kazi ndogo kwangu, unaenda wapi?”

“Nataka kwenda Namanga!”
“Poa braza!” Akajibu Yule dereva akitabasamu.
Safari ya Namanga ilikuwa lazima alipwe fedha nyingi, kwa muda ule wa asubuhi, hakika angekuwa ameanza siku yake vizuri sana.
“Endesha gari!” Akaamrisha Genesis.

Gari likaondolewa hadi kwenye mataa ya Mianzini, likasimama kwa muda, taa ziliporuhusu dereva akanyoosha kuifuata Barabara ya Nairobi, akiendesha kwa kasi kama alivyoagizwa.

Mbele kidogo kwenye makutano ya barabara ya kwenda Dodoma, ikiwa inatazamana na Klabu maarufu ya Triple A, akanyosha kuifuata barabara hiyo ya Nairobi, kasi ikiwa ni ile ile. Mshale ulikuwa umesimama kwenye kilometa 120 kwa saa.

Mwendo wa dakika tano tu, wakiwa ndiyo kwanza wameanza kupanda kilima cha Banda la Maziwa, Genesis akashuhudia maaskari wanne wakiwa na silaha wametanda barabarani, wakilipiga mkono gari lao lisimame. Moyo wake ukalipuka kwa nguvu puu!
“Usisimame!” Genesis akamwambia dereva.
“Kivipi wakati unaona wametanda barabarani?” Dereva akauliza akianza kupunguza mwendo.

“IKIWEZEKANA WAGONGE!”
“Unasemaje?” Dereva akauliza akiwa ametoa macho.
Je, nini kitatokea? Genesis atakamatwa?

MALIZIA UTAM WAPENDWA LEO NAWAPENDELEA ONE LOVE TO ALL MA FANS

Ukweli aliokutana nao Genesis kwenye anwani pepe ya mkewe Bianca siku ya harusi yao, ndiyo ulimchanganya kichwa chake na kusababisha aamue kumuua Bianca kwa kumchoma kisu kisha kuruka kutoka ghorofa ya tatu katika hoteli waliyokuwa wamepangiwa kwa lengo la kujiua bila mafanikio.

Baada ya kuanguka chini akiwa mzima, akapata wazo lingine, akaamua kwenda nyumbani kwao na kuchukua gari la baba yake, kisha kutoroka nalo kuelekea Nairobi kupitia Arusha. Alipofika Arusha, akasikia habari kupitia redio iliyokuwa kwenye gari kuwa Bianca alikuwa amekufa na yeye alikuwa akisakwa.

Akaamua kulitelekeza gari eneo la Mianzini, Arusha kisha akakodi teksi iliyompeleka hadi Namanga, ambapo hapo akatumia usafiri wa kuungaunga hadi alipoingia jijini Riyadh, Saudi Arabia, alipokuta gumzo la binti wa Kitanzania Farida Mbaraka, kuingiza dawa za kulevya na kutakiwa kunyongwa mchana huo.

Haraka akachukua taxi na kumwambia dereva amuwahishe katika eneo la mauaji. Ilibaki nusu saa tu na hakuwa na uhakika kama angefanikiwa kufika kabla mpenzi wake hajapigwa risasi na kupoteza maisha yake.

Alifanikiwa kufika eneo la tukio zikiwa zimebaki sekunde chache tu kabla ya Farida kupigwa risasi hadi kufa, sauti ya mtu akihesabu kutokea kumi kushuka chini ilisikika kutoka katika spika zilizokuwa kila kona la uwanja ule.

Genesis akaanza kukimbia akipangua umati wa watu akielekea eneo ambalo Farida alikuwa amefungwa kwenye mti, uso wake ukiwa umefunikwa kwa kitambaa cheusi. Akiwa anakaribia kabisa kufika eneo la tukio, sauti ya mtu aliyekuwa akihesabu ikiwa imefikia ‘mbili’ alipiga kelele akisema kwamba anao ukweli, kwahiyo wasimuue kwanza Farida.

Hakuwa na uhakika kama sauti yake ilisikika na ilibaki kusikika neno ‘One’ (moja) ndipo risasi zianze kuingia mwilini mwa Farida. Genesis alikuwa anatetemeka kwa hofu, akiwa na hamu ya kumuokoa Farida ambaye hakuwa na hatia.

“ACHENI kwanza…” sauti kutoka kwa mmoja wa maaskari waliokuwa wamesimama pembeni ya Farida ilisikika.

Genesis akafurahi sana, huo ulikuwa mwanzo mzuri wa kuelekea kwenye mafanikio ya kumuokoa mpenzi wake. Hakutaka kabisa Farida afe akiwa hana hatia yoyote.

“Mleteni hapa,” sauti ile ile ikaamrisha tena.
Genesis akapita hadi karibu kabisa na Farida, ambaye midomo yake ilionekana ikicheza na kuchanua tabasamu, alionekana kupata matumaini baada ya kusikia sauti ya Genesis.

Wakati Genesis akitembea taratibu akiwa chini ya ulinzi wa askari uwanjani pale, kitambaa cheusi kilichokuwa kimefungwa usoni mwa Farida kilionekana kuanza kulowanishwa na machozi ya uchungu yaliyoanza kutiririka machoni mwake.

“Ni nani wewe?” Yule askari akauliza kwa lugha ya kiingereza.
“Naitwa Genesis.”
“Genesis?”
“Ndiyo.”

“Unatokea wapi?”
“Dar es Salaam, Tanzania!”
“Tanzania?”
“Ndiyo!”

“Na wewe unahusika na hizo dawa za Farida?”
“Hapana Mkuu.”
“Sasa kwanini uko hapa halafu unazuia serikali isifanye kazi yake?”

“Sina nia ya kuizuia serikali kufanya kazi yake, najua kwamba dawa za kulevya ni haramu na hatari kwa taifa lolote lile duniani, ni halali pia kwa hukumu iliyotolewa kwa Farida maana alikamatwa na hizo dawa.

“Hata hivyo, hakuna mtu ambaye haamini kuwa Farida alikamatwa na dawa za kulevya, lakini upo ukweli mwingine ambao hakuna anayeufahamu zaidi yangu. Farida hahusiki kabisa na hizo dawa!” Genesis alisema kwa uchungu sana.

“Hivi wewe una akili kweli? Dawa zimekutwa kwenye begi lake mwenyewe, halafu unasema kwamba hahusiki unamaanisha nini? Unacheza na serikali?”

“Hapana Mkuu, ngoja niwaeleze vizuri…huyo binti mrembo aliyefungwa kamba hapo mtini alikuwa mpenzi wangu, mapenzi yetu yalianzia tangu tukiwa shuleni, tulipendana sana lakini kulikuwa na kikwazo kutoka kwa wazazi wangu ambao hawakutaka mimi nimuoe badala yake kuna binti mwingine walitaka nimuoe…

“Huyo binti anaitwa Bianca, ambaye ni mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Dk. Rwegoshora. Familia hizi mbili kwa kushirikiana kwa pamoja, walifanya kila hila ili mimi nikatae kumuoa Farida lakini mimi niliendelea kuwa na msimamo wangu.

“Kuna wakati walikuwa wanataka kufaulu kutuachanisha, lakini baadaye nikajikuta nashindwa kuwa na uhusiano na Bianca na kurudiana na Farida wangu,” alisema Genesis akiwa anamwaga machozi.

Uwanja mzima ulikuwa kimya ukimsikiliza kwa makini sana, stori yake ilivuta hisia za watu wengi ambao mwanzoni walikuwa na imani kwamba Farida alihusika na mauaji hayo, sasa walianza kubadilishwa fikra hizo na maelezo ya Genesis.

“Nilihangaika sana kumtafutia chuo, maana wazazi wangu walisema ili niweze kumuoa, lazima awe amesoma angalau awe na shahada ya kwanza, katika kuhangaika kutuma maombi katika vyuo mbalimbali, Farida akajibiwa maombi yake na Chuo Kikuu Huria cha Riyadh.

“Ndipo tulipofanya jitihada zote za mipango ya safari ya kuja hapa. Mimi ndiye niliyesafiri naye kutokea Dar es Salaam mpaka Zanzibar kwa ajili ya kufanya manunuzi ya mahitaji ya kuja nayo chuoni.

“Siku ya safari nikamsindikiza hadi uwanjani alipopanda ndege na kuja huku, jioni ya siku hiyo, nikamuona Farida kwenye runinga akiwa amekamatwa Uwanja wa Ndege wa Riyadh, akihusishwa na dawa za kulevya, nikafadhaika sana.

“Nikajua Farida si mwanamke sahihi tena kwangu, kama nilivyokuwa nikifikiria, nikaamua kuachana naye. Nikawaeleza wazazi wangu hali halisi na wote kwa pamoja wakanishauri nirudiane na Bianca. Taratibu za ndoa zikafanyika mara moja kisha nikafunga ndoa na Bianca.

“Siku ya harusi yetu, tukiwa ukumbini, simu yangu ikaingiza ujumbe mfupi wa maneno ambao ulinichanganya sana kichwa changu, nilipewa anwani pepe ya mke wangu Bianca pamoja na maneno ya siri ya kuingilia, nikijulishwa kwamba niende nikaangilie mchezo mchafu aliofanyiwa Farida.

“Mkuu sikuamini nilichokiona, Farida hakuhusika kabisa na dawa za kulevya zilizokutwa katika begi lake, bali kuna mchezo mchafu ulifanywa na wazazi wangu wakishirikiana na wazazi wa Bianca ili kumpoteza halafu mimi nimuoe Bianca,” akasema Genesis kwa uchungu sana, macho yake yakizidi kuzingirwa na machozi.

“Una uhakika na unachokiongea?”
“Ndiyo Mkuu!”
“Ilikuwaje?”

“Ni habari ndefu, lakini nitawasimulia, sitaki kuona Farida akifa bila kosa kwa sababu ya penzi langu. Ni afadhali kama angekuwa anahusika kweli na hizo dawa, lakini si kweli, ni unyanyasaji tu!” Alisema Genesis akiangalia chini, huku akishindwa kabisa kuthibiti machozi yaliyokuwa yakimtiririka mashavuni mwake.

***
Ilikuwa saa 2:00 usiku, watu wawili wakionekana kuwa na jambo muhimu sana la kujadiliana ndani ya hoteli ya kifahari. Wamekaa kwenye kona ambayo haikuwa na watu wengine zaidi yao.

Ilivyoonekana hawakutaka kabisa usumbufu. Hawa ni Bi. Rwegoshora na Bi. Mshana, wazazi wa Genesis na Bianca.
“Nimepata wazo,” akasema mama Genesis akimwangalia mama yake Bianca.
“Wazo gani?”
“Lazima tutengeneze mchongo ili yule mtoto afe!”

“Afe?”
“Ndiyo, anatakiwa kufa.”
“Mh! Mwenzangu mimi sijawahi kuua na kiukweli naogopa sana, kwani hakuna njia nyingine?”

“Hata kama ikiwepo, lakini kumuua ndiyo utakuwa mwisho wa kidomodomo chake. Mtoto anavyomng’ang’ania mwanangu, sijui amempa nini? Yaani nachanganyikiwa kabisa, lakini lazima tumkomeshe.”

“Mh! Sijui kwanini roho yangu inakataa kuua kiasi hicho, nina wasiwasi mwingi moyoni, nadhani tutafute njia nyingine.”
“Kwani wewe hutaki binti yako aolewe na kijana wangu?”
“Nataka!”

“Sasa nisikilize mimi, tutamfanyia mpango wa chuo Saudi Arabia, halafu tutamwekea dawa za kulevya kwenye begi lake, mchezo umeisha!”
“Itakuwaje sasa?”

“Ni kazi rahisi sana, wapo watu nitakaocheza nao, ambao watafanya zoezi zima kwa usiri mkubwa, wakati anaingia kwenye chumba cha ukaguzi uwanja wa ndege, begi lake likipitishwa, ndiyo litawekwa dawa za kulevya, akishuka Riyadh, ndiyo anakutana na kimbembe,si unajua sheria za nchi za Kiarabu? Adhabu yake itakuwa ni kifo tu, wakimkamata na kidhibiti… siyo kitu kigumu kama unavyofikiria!”

“Kweli?”
“Niachie mimi!”
Mama Bianca akatabasamu na kukubaliana na mama Genesis katika kukamilisha mchezo huo. Lengo likiwa moja tu, Farida auawe Uarabuni ili iwe nafasi kwa Bianca kuolewa na Genesis.

Je, walitumia mbinu gani? Nini kitampata Farida na Genesis?
 
SEHEMU YA 28


Aliyekuwa akihesabu akaamuru askari waache kwanza kumuua ili kusikia hoja za Genesis kama zilikuwa na uzito. Ni hapo Genesis alipoanza kusimulia jinsi mpango wa mauaji ulivyosukwa na mama yake pamoja na mama wa Bianca.

Uamuzi wa kikao cha mama Genesis na mama Bianca ukawa ni Farida atengenezewe mchongo ili akamatwe na dawa za kulevya katika nchi za Kiarabu wakiwa na uhakika kwamba adhabu pekee kwa nchi hizo ingekuwa ni kifo tu!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

MOYO wa mama Genesis ulikuwa umeshachafuka kabisa, hakutaka kusikia jina la Farida, alimchukia kupita kiasi, kitu pekee ambacho kilizunguka katika ubongo wake ni kusikia kuwa Farida amekufa, aliamini kwa kufanya hivyo, usumbufu kwa mwanaye ungeisha na angekuwa na maamuzi ya kufunga ndoa na Bianca.

Mama Genesis alitakiwa kutengeneza timu sahihi ambayo ingekuwa na msaada kwake kwa kumuingiza Farida kwenye mtego ambao asingeweza kutoka.
Wazo lake likawa ni kutafuta kwanza hao watu kisha kukutana nao na kupanga namna ya kummaliza Farida.

“Hawezi kumng’ang’ania mwanangu kiasi hiki, lazima nimmalize, hana ujanja, nitamuonesha kwamba mimi ni msomi, ni rahisi sana,” akawaza mama Genesis asubuhi hiyo akiwa ofisini kwake.
“Afadhali, nimeshapata wazo...” akajisemea kwa sauti ya chini mama Genesis.

Muda huo huo akachukua simu yake ya mkononi kisha akatafuta jina la mama Bianca na kumpigia. Simu haikuita kwa muda mrefu sana, ikapokelewa.
“Vipi mwenzangu?” Sauti ya mama Bianca ilisikika kwenye spika ya simu ya mama Genesis.

“Salama, lete mpya!”
“Ninalo basi mwenzangu, nilipoona tu jina lako kwenye kioo cha simu yangu, nikajua lazima kuna jipya, haya niambie!”
“Ni kweli lipo jipya!”
“Enheee...”
“Leo usiku, tukutane pale kwenye sehemu yetu, nitakuwa na hao jamaa ambao watatusaidia.”

“Sawa, lakini umeshazungumza nao?”
“Nimewaambia kwamba kuna dili tu, kwahiyo wakifika watakutana nalo, mwenzangu, nani anayekuwa na maswali mengi mbele ya fedha?”
“Ni kweli kabisa, basi hiyo usiku!”
“Haya.”

Pamoja na kwamba mama Bianca aliishi muda mrefu nje ya nchi, safari hii akiwa ametokea Uswis, kwa muda mfupi sana aliokuwa katika uhusiano wa karibu na mama Genesis amejikuta ameanza kuwa mswahili wa kiwango cha mwisho! Jambo hilo hakulijua, lakini ukweli wenyewe ulikuwa hivyo.

Siku ya mama Genesis haikuwa ngumu tena, hapo alianza kupiga kazi kwa nguvu, uso wake ukiwa unang’aa huku tabasamu pana likiwa limechanua usoni mwake. Kila aliyekutana naye, hakupata shida kugundua kwamba alikuwa na furaha, lakini siri ya furaha yake alikuwa nayo mwenyewe, alikuwa na furaha ya mipango ya mauaji!
***

Mama Genesis ndiye alikuwa mwenyekiti wa kikao hicho haramu kilichopanga mauaji! Kwa bahati mbaya, hakuna aliyekuwa akijua nia ya kikao hicho zaidi ya mama Bianca ambaye alikuwa kimya akimtazama na mama Genesis.

Macho ya mama Genesis yakahama kutoka kwa mama Bianca na kuanza kuwatembelea wajumbe wengine mmoja baada ya mwingine pale mezani. Alianza na Festo, akayarudisha macho yake kwa Dulla kisha akamalizia na Patrick.

“Kwanza kabisa napenda kuwatoa hofu juu ya kikao hiki!” Akaanza kusema mama Genesis.

“Kifupi ni kikao kizuri, chenye lengo la kutengeneza fedha!”
“Bila shaka hamfahamiani, labda nianze kwa kuwatambulisha,” akasema tena mama Genesis akihamishia macho yake kwa mama Bianca.
“Mrs. Rwegoshora, kutana na Patrick Mkonyi, yeye anafanya kazi airport Kitengo cha Ukaguzi wa Mizigo inayoingia na kutoka uwanjani!” Akasema mama Genesis.

“Nimefurahi sana kukufahamu!” Akasema mama Bianca.
“Nami pia nimefurahi sana kukutana nawe!” Akasema Patrick akiachia tabasamu usoni.

Mama Genesis akatengeneza cheko la ushindi, kisha akacheka kidogo halafu akayarudisha macho yake tena kwa mama Bianca, akasema: “Huyu hapa ni Dulla, anaishi Kinondoni, naomba nimtambulishe kwako kama mzee wa kazi, nikisema hivyo najua unakuwa unaelewa namaanisha nini!”

Wote wakacheka isipokuwa Dulla ambaye alikuwa akiangalia chini kama anayeona aibu.
“Ahsante sana, nimefurahi kukufahamu Dulla!” Mama Bianca akasema akiendelea kucheka.

“Nami pia,” Dulla akajibu akionekana kujilazimisha kucheka ili awe sawa na wenzake.
“...na yule ni Festo, yeye ni mkali wa IT, kwenye fani hiyo hakuna kinachomshinda!”

“Pia nimefurahi kukutana nawe Festo!” Akasema mama Bianca.
“Karibu sana Mrs. Rwegoshora,” akasema Festo.
“Nashukuru!”
“Dulla, Festo na Patrick...” mama Genesis akawaita, wote wakahamishia macho kwake.

“Huyu anaitwa Mrs. Rwegoshora, bila shaka jina lake si geni sana, kifupi ndiye mke wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali!”
Wote wakawa wakapigwa na butwaa, hawakutarajia kukutana na mtu mzito kama yeye ghafla, tena kwenye kikao cha siri kama kile, kwao yalikuwa ni maajabu makubwa.

“Kuna kazi tunataka mtusaidie, inatakiwa ifanywe katika mazingira ya siri kubwa lakini malipo yake yatakuwa mazuri!” Akasema mama Genesis akiwatazama wote kwa zamu.

“Tayari tuna wazo, naweza kusema tunajua pa kuanzia, lakini tumewaita ili ninyi mtoe mawazo yenu ni jinsi gani kila mmoja atakavyofanya kazi kwa nafasi yake kulingana na jinsi tulivyokubaliana!”

“Ni dili gani?” Dulla alikuwa wa kwanza kuuliza.
“Taratibu Dulla, lazima tutawaambia tu.”
“Sawa!”

Mama Bianca akawaeleza kila kitu, kuanzia jinsi Genesis alivyokutana na Farida na jinsi ambavyo hawapendi aolewe naye, kisha wakawaambia vile wanavyotaka wao.

Wote walionekana kuelewa, lakini bado walishindwa kuelewa ni kwa namna gani kazi hiyo ingefanyika.

“Najua mna mawazo mengi juu ya namna kazi hii itakavyofanyika, lakini msiwe na wasiwasi, ni rahisi sana. Huyo binti anahangaika kutafuta vyuo duniani kote, sisi tutampanga na atatuma maombi kwenye nchi moja ya Kiarabu, akishamaliza zoezi hilo, kitakachofanyika sasa ni wewe Festo kutengeneza anwani pepe na kufanya mawasiliano naye akiamini kwamba anawasiliana na watu wa chuo alichoomba, kisha unamwita chuoni, kazi itamalizikia uwanja wa ndege kwa Patrick, ambapo hapo tayari Dulla atakuwa ameshaweka mkono wake!” Akasema mama Genesis na kuwaangalia wote kwa zamu.


“NAONA kama tunaongea sana, sioni sababu ya kuvuta maneno, kabla ya kuichambua dili yenyewe vizuri, hebu tuambie mnatulipa kiasi gani? Hilo ndilo la msingi kwanza!” Akasema Dulla uso wake ukionekana kuwa na uchu sana wa fedha.

“Una wasiwasi na fedha Dulla?” Mama Genesis akauliza.
“Siyo suala la wasiwasi hapa, nataka kujua tunazungumza dili la kiasi gani!”
“Milioni tisa!” Akasema mama Genesis kwa kujiamini.

“Kila mmoja au?” Patrick akadakia.
“Kwa wote, hapo namaanisha kila mmoja atapata tatu!”
“Hapana...” Festo akasema.
“...ni fedha ndogo sana ukilinganisha na kazi yenyewe!” Akaongeza kusema.

“Kwahiyo mnahitaji kiasi gani?”
“Sijajua kwa wenzangu, lakini mimi bila milioni saba, najitoa katika hiyo kazi!”
“Hapo sawa, saba inaweza kuwa poa,” akasema Dulla.

“Sikia, fedha siyo tatizo kikubwa ni kazi kukamilika. Potelea mbali, tutawapa milioni ishirini, nyie wenyewe mtajua namna ya kugawana.”
“Lini hiyo fedha?” Festo akauliza.

“Kesho tutawapatia milioni kumi kwanza, kazi ikiisha tutawamalizia.”
“Sawa, sasa twende kwenye kazi yenyewe, inafanyikaje?” Dulla akauliza.

“Ni rahisi sana, ni kama nilivyosema awali, kwa sasa fahamu kwamba, Dulla utatakiwa kupata dawa za kulevya aina ya heroin, halafu unampasia Patrick ambaye atakuwa nazo hadi siku ya safari. Hata hivyo, si lazima kununua mapema, kwa kuwa mtakuwa mnawasiliana, wenyewe mtajua jinsi ya kufanya kazi.

“Festo angalia ni nchi gani na chuo gani tunaweza kufanya mipango, halafu sisi tutahakikisha Farida ametuma maombi kwenye hicho chuo!”
“Sawa...kwa haraka napendekeza Saudi Arabia, chuo wacha niendelee kuangalia kwenye mtandao, leo jioni nitakuambia ni wapi!”

“Basi vizuri, naona kikao chetu kiishie hapa, kila mtu afanye kazi yake kwa nafasi yake vizuri,” akasema mama Genesis.
“Bila shaka!” Patrick akajibu haraka haraka.

Kikao kikafungwa. Mwisho wa kikao ukawa mwanzo wa kuendelea na vinywaji, walivyokunywa hadi wakaridhika na kutawanyika kila mmoja akiwaza namna ya kukamilisha kazi hiyo.

***
Ilikuwa lazima mama Genesis atumie akili nyingi sana, hakutakiwa kufanya mchezo katika kazi ngumu kama ile tena iliyohusisha mauaji. Isingekuwa rahisi kwake kuzungumza moja kwa moja na Farida juu ya mpango wa chuo, hivyo akaamua kumtumia mwanaye Genesis ili iwe rahisi zaidi kwake.

Kabla ya kufanya jambo hilo, kwanza alianza kwa kumpigia simu Festo ili kujua amechagua chuo nchini Saudi Arabia. Akatoka sebuleni alipokuwa amekaa na kwenda zake hadi chumbani kwake, huko ndipo alipochukua simu yake na kumpigia Festo.

“Nipe taarifa Festo!”
“Najua unaulizia juu ya chuo, siyo mama?”
“Ni kweli!”
“Tena nilikuwa nakupigia muda si mrefu. Nimechagua Chuo Kikuu Huria cha Riyadh!”

“Ok! Sawa acha mimi nianze kazi yangu usiku huu.”
“Hata mimi tayari nimeshaanza majukumu yangu, hadi kesho nitakuwa na jibu la maana.”
“Sawa, usiku mwema.”

“Nawe pia.”
Muda huo huo mama Genesis akatoka sebuleni kisha akamwita Genesis karibu yake. Sauti yake pekee ilitosha kuonesha kwamba alikuwa na jambo zuri la kuzungumza na mwanaye. Alimwita kwa sauti ya upendo sana.

“Naam mama...” akaitika Genesis.
“Njoo mwanangu, kuna jambo nahitaji kuzungumza na wewe!” Mama Genesis akasema na mwanaye bila kupoteza muda akasimama na kumfuata. Macho yake yakaonesha unyenyekevu mkubwa, akitaka kusikia mama yake alikuwa na jambo gani la kumwambia.

“Mwanangu mwenzio amefikia wapi kuhusu chuo?”
“Farida?”
“Ndiyo!”
“Bado anahangaika, nimekuwa nikimsaidia kutuma maombi katika vyuo mbalimbali!”

“Lakini mimi nina wazo!”
“Lipi mama?”
“Nilipokuwa ofisini, nilipata muda wa kutembelea mitandao ya vyuo mbalimbali, kuna baadhi nimeona hawana masharti magumu sana, kwanini msijaribu kutuma na hivyo?”

“Ni vyuo gani mama?”
“Vipo vingi, nimeodhoresha kwenye karatasi lipo chumbani, asubuhi nitakupa anuwani pepe zao ili mjaribu kutuma na huko.”
“Ahsante sana mama, utakuwa umetusaidia sana, kweli sasa naona upendo wako kwa mkweo!”

“Usijali yule ni mwanangu kama ulivyo wewe, kwa hiyo ni jukumu langu kuhakikisha anakuwa na maisha mazuri kama jinsi tunavyohangaika kwa ajili yako.”
“Ahsante sana mama.”

Genesis alifurahi sana, kwanza mama yake kuonekana kumkubali mpenzi wake, wakati mwanzoni alikuwa hamtaki lakini kubwa zaidi kuonesha jitihada za kumsaidia ili aweze kujiunga na masomo. Kwake ilikuwa faraja kubwa sana, lakini hakujua ndani ya msaada ule wa mama yake kulikuwa na kitu gani. Hatari iliyokuwepo hakuitambua hakika.

***
Kitu cha kwanza kufanya baada ya kuamka asubuhi hiyo, ilikuwa ni kumuomba mama yake anuwani pepe za vyuo alivyoona kwenye mtandao. Ilikuwa kazi nyepesi sana kwa mama Genesis ambaye aliingia ndani mara moja na kutoka na katarasi yenye orodha ya vyuo na anuwani pepe zake kumi!

Alifanya hivyo kwa nia ya kumchanganya ili asifikirie chochote kuhusu kuhusika na lolote litakalotokea baadaye, katika vyuo vile kumi, ni kimoja tu ndicho kilichokuwa kinahusika; Chuo Kikuu Huria cha Riyadh!

Asubuhi hiyo hiyo, Genesis akawasha gari hadi Kwa-Aziz Ali alipomchukua Farida na kwenda mjini walikoshinda kutwa nzima wakisambaza maombi katika vyuo kumi alivyopewa na mama yake, hata hivyo siri ya kwamba mama yake ndiye aliyempa orodha ya vyuo hivyo, iliendelea kubaki moyoni mwake.

“Naamini kati ya hivi, lazima utaitwa katika chuo kimojawapo,” akasema Genesis akitabasamu.
“Bila shaka mpenzi!” Farida akaitikia akimwangalia Genesis usoni.

Wote wakaachia matabasamu usoni mwao, laiti wangejua kilichokuwa nyuma ya maombi yale lazima wangelia sana, lakini walikuwa kwenye giza nene, tena katikati ya msitu wenye wanyama hatari! Walikuwa wakifanya mchezo hatari wa kujichimbia kaburi wenyewe bila kujua!

Je, nini kitatokea? Nini kilifuata baada ya hapo?
 
SEHEMU YA 29


Festo ameshaanza kazi na tayari amemtumia mama Genesis jina la chuo na anwani ya barua pepe aliyotakiwa Farida kutuma, kisha akampa na orodha ya vyuo vingine tisa ili kukamilisha idadi ya vyuo kumi kwa ajili ya kumchanganya Farida!

Genesis na Farida wameshasambaza maombi katika vyuo mbalimbali na kilichokuwa kikisubiriwa kwa hamu ni majibu tu! Hakuna aliyekuwa akijua kilichokuwa nyuma ya pazia. Laiti wangejua!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

“AHSANTE sana Genesis wangu, hapo unaonesha ni kiasi gani unavyonipenda na ulivyo na uchungu na maisha yangu, najua unatamani sana kuona na mimi angalau nakuwa na shahada yangu kama wewe!” Alisema Farida akiwa ameyatuliza macho yake usoni mwa Genesis.

“Usijali mpenzi wangu, nipo kwa ajili yako. Napenda ndoa yetu ifanyike na ndiyo maana nimeamua kufanya haya yote kwa ajili yako. Mwamini Mungu mpenzi, lazima utapata chuo!”

“Nashukuru kwa kunipa moyo mpenzi wangu, ndiyo maana najivunia sana kuwa na wewe, naamini ndoa yetu itakuwa yenye nguvu na imara ambayo kwamwe haitatetereka!”
“Bila shaka mpenzi wangu, hilo ndilo linalozunguka kichwani mwangu pia.”

Zoezi la kutuma maombi lilipokamilika, walitoka na kwenda zao ufukweni kwa ajili ya kupunga upepo na kufurahia mapenzi yao. Kwa hakika siku yao ilikuwa nzuri sana, kila mmoja alipendezwa na uwepo wa mwenzake katika uhusiano wao.

Huko walikula na kunywa hadi jioni kabisa Genesis alipomrudisha Farida nyumbani kwao, Mtoni Kwaazizi Ally. Wakiwa mita chache kabla ya kufikia nyumba yao, Farida alikuwa mzito sana kushuka kwenye gari akitaka kuendelea kubaki na mpenzi wake.

“Sweetie umefika, shuka acha mimi niwahi hii foleni.”
“Sijui kwa nini hisia zangu zinakuwa kali kiasi hiki kwako, nashindwa kuelewa sijui umeniwekea nini mpenzi, nakupenda mpaka nachanganyikiwa.”

“Usijali!”
“Kwa hiyo unaondoka?”
“Ndiyo... wewe shuka, nenda ukawasalimie wazazi, tutaonana kesho!”
“Jamani, kwa hiyo hutanipigia hata simu?”
“Labda mtu mwingine si wewe mpenzi wangu, unadhani ni rahisi kiasi hicho kulala bila kusikia sauti yako?”
“Najua siyo rahisi mpenzi lakini nilichokuwa nafanya ni kukukumbusha.”

“Poa mpenzi baadaye.”
“Haya urudi salama.”
“Ok!”
Genesis akainama kidogo, kisha Farida akasogeza kinywa chake jirani kabisa na cha Genesis, hapo wakaanza kubadilishana mate. Dakika tano baadaye waliachiana wakiwa hoi, huku Genesis akionekana kuelemewa na mapenzi mazito.

Macho ya Genesis yalionesha wazi kwamba hisia zake zimebadilika, alikuwa na mhemko mkali na alichokuwa akikihitaji ilikuwa ni penzi la Farida.
“Hapana Genesis...” Farida akasema baada ya kuelewa Genesis alichokuwa akikitaka.
“Tafadhali mpenzi, mara moja tu!”
“Umesahau ahadi yetu?”
“Nakumbuka lakini nimezidiwa.”

“Hapana, hatuwezi kufanya hivyo. Kwanza nitakuwa najisaliti mwenyewe, nasaliti penzi letu, halafu nitakuwa nimemkosea mama yangu, tafadhali vumilia mpenzi wangu. Kama tumeweza kukaa siku zote hizo bila kufanya mapenzi na ukaweza kuvumilia, naamini hata leo utaweza kufanya hivyo.”

Genesis hakujibu kitu zaidi ya kutingisha kichwa kuashiria kwamba alikuwa amekubaliana na mawazo ya Farida ambayo yalimvunja nguvu.
“Umeshinda Farida,” hatimaye Genesis akasema huku akijitahidi kulazimisha tabasamu.

“Ok! Poa.”
“Haya mwaya uende salama!”
“Ahsante.”
Walishindwa kuelewa ni kwa nini walitumia muda mrefu kuagana. Haikuwa kawaida yao, siku hiyo walikuwa na mvuto mkubwa sana wa kimahaba kuliko siku nyingine yoyote iliyotangulia. Farida akashuka garini kwa shingo upande, Genesis akamsindikiza kwa macho mpaka alipoishia, akawasha gari lake na kuondoka.

***
Jioni hiyo mama Bianca alionekana kuwa na furaha sana, alikatiza sebuleni akitokea nje na kumuona binti yake Bianca akiwa mwenye huzuni sana, hakupenda mwanaye awe katika hali hiyo.
“Bianca...” akaita mama Genesis.
“Mama!”

“Kwa nini upo hivyo?”
“Usijali mama, nipo sawa.”
“Nakujua vizuri sana binti yangu, ni mimi ndiye niliyekuzaa, nakufahamu tangu utotoni mwako, ukiwa haupo sawa najua, ndiyo maana nimeona tofauti uliyonayo leo!”
“Ni kweli mama sipo sawa.”

“Bila shaka ni kuhusu Genesis!”
“Unadhani ni nani mwingine anayeweza kunichanganya kichwa changu kama si yeye?”
“Basi nakuomba utulie, maana jibu limeshapatikana, njoo chumbani kwangu!” Mama Bianca akasema huku akipiga hatua kuelekea chumbani kwake na Bianca akimfuata kwa nyuma.

Ilikuwa vigumu sana kwa Bianca kuingia chumbani kwa wazazi wake, siku hiyo ilikuwa maajabu kwake, alijua kwa vyovyote vile kulikuwa na jambo la muhimu sana alilotaka kuambiwa na mama yake, akaongoza nyuma ya mama yake mpaka chumbani.
“Kazi imeshaisha!”
“Kivipi mama?”

“Upo mpango mzuri sana wa kumpoteza Farida, atakufa siku si nyingi na huo utakuwa mwisho wake na Genesis na mwanzo mpya wa mapenzi yenu ambayo lazima mwisho wake utakuwa ni ndoa.”
“Kivipi?” Bianca akauliza akitoa macho.

“Nitakusimulia,” mama Bianca akasema na kuanza kumsimulia kila kitu hatua kwa hatua.
Bianca alishtuka sana, hakutegemea kama mama yake na mama Genesis walikuwa wamepanga mpango wenye nguvu kiasi kile.
“Nakupenda sana mama, nimefurahi sana kusikia hivyo!”
“Usiogope mwanangu, ila kuna jambo moja!”
“Nini tena?”

“Utakuwa ukitumiwa waraka pepe kwenye anwani yako, ambayo itakuwa na maelezo yote jinsi kazi inavyoendelea hatua kwa hatua.”
“Sawa mama.”
Furaha ya Bianca ambayo ilikuwa imepotea ikarejea kwa nguvu ajabu. Tayari alishajihesabu kuwa ni mshindi.
***

Watu waliokuwa wamefurika katika uwanja wa mauaji walibadilisha fikra zao ghafla, maelezo ya Genesis yaliwatia simanzi. Mwanzoni walikuwa wanamchukia sana Farida na walitaka auawe, lakini sasa wakawa wanamwonea huruma kwa kuepuka kifo ambacho hakikumhusu!
Farida aliyekuwa amefungwa kamba pale mtini na kitambaa cheusi usoni alikuwa akilia muda wote Genesis alipokuwa akisimulia. Ni machozi ya Farida ndiyo yaliyomuumiza Genesis na kushindwa kuendelea kusimulia tena.

Macho yake yalikuwa yamefunikwa na machozi, makamasi yakichuruzika puani mwake. Alihema kwa shida, akionekana kuwa na mapenzi mazito kwa Farida wake.

“Genesis endelea tafadhali, baada ya hapo ilikuwaje? Lazima tupate maelezo yako vizuri, najua unaumia lakini lazima ujikaze ili tuweze kukusaidia...” mkuu wa kikosi akasema lakini Genesis alionekana kukosa nguvu za kuendelea kusimulia.

HAKUWEZA kuzuia hisia zake za huzuni, moyo wake ulikuwa kama umepondeka, akiwa hana amani kabisa, kilichozidisha maumuvu yake ilikuwa ni machozi ya Farida ambaye alikuwa kama yupo kwenye ndoto!

Hakuwahi kufikiria kama kulikuwa na ukweli nyuma ya lile tukio, mpaka anafikishwa kwenye uwanja wa mauaji, alikuwa hajui ni kitu gani kilitokea na wala hakuwahi kuwafikiria mama Genesis na mama Bianca ndiyo waliohusika na tukio lile.

Genesis alikuwa mkombozi wake, hakutegemea kama alikuwa anakwenda kupishana na kifo ambacho tayari kilikuwa mbele yake. Akazidi kulia na kumfanya Genesis kushindwa kuongea chochote!

“Tafadhali Genesis, jikaze...tumekupa hii nafasi kwa heshima, ni vyema kama utaitumia vizuri ili tuweze kuona ukweli,” akasema Mkuu wa Kikosi akimwangalia Genesis usoni.
“Inauma Mkuu!” Genesis akasema.
“Najua!”

“Inauma sana!”
“Ni kweli Genesis, lakini inakupasa ueleze kilichotokea.”
“Farida anataka kuuawa bila kosa, hana alichofanya zaidi ya watu wenye roho mbaya kutaka kumuangamiza.”

“Sawa, lakini bado hajafa na mpaka sasa, zoezi limeahirishwa ili kupisha maelezo yako, tafadhali zungumza Genesis.”
“Sawa Mkuu, baada ya hapo, nakumbuka asubuhi hiyo mama aliniita nikiwa natoka kwenda kwenye mizunguko yangu...na kweli haikuwa mizunguko hasa, bali nilikuwa nina ahadi ya kukutana na Farida!” Akaanza kusimulia tena Genesis.

“Enheee...” Mkuu wa Kikosi akaitikia.
“Nilitii agizo la mama, nikabadilisha uelekeo na kumfuata, nikapokelewa na tabasamu la mama, utadhani alikuwa mwema...” akaendelea kusema Genesis akiangalia juu, akionekana kuzidi kuvuta kumbukumbu zake vizuri.

***
Tabasamu la mama yake lilikuwa taswira ya jambo jema alilotaka kumweleza, Genesis akamfuata hadi kwenye sofa kubwa alilokuwa amekaa mama yake. Naye akakaa hapo. Tabasamu la mama Genesis likazidi kuchanua, kwa kiasi kikubwa ni kama lilimchanganya Genesis.

Haikuwa kawaida ya mama yake kutabasamu bila sababu. Alichokifanya Genesis ilikuwa ni kurudisha tabasamu kwa mama yake kisha akaanza kuzungumza.
“Inaonekana kuna jambo muhimu na zuri unataka kuniambia,” akasema Genesis akimwangalia mama yake usoni.

“Kwanza umependeza sana!”
“Ahsante mama.”
“Unakwenda kwenye mkutano nini? Mbona hivyo...hapo ni umemaliza tu chuo, sasa ukianza kazi ofisini itakuwaje?” Akasema mama Genesis akionekana kuwa na dalili zote za kufanya mzaha.

“Mama ni hilo tu!” Genesis akasema akiona haya.
“Hapana siyo hilo mwanangu, kwanza vipi mizunguko yako ya leo?”
“Nitakuwa mjini mpaka jioni kabisa, nitakutana na marafiki zangu niliomaliza nao St. Thomas!”
“Sawa lakini leo jioni nilitaka kuwapa ofa ya chakula cha usiku wewe na dada yako!”

“Saa ngapi?”
“Saa 2.00 usiku!”
“Bila baba?”
“Nilitaka kutoka na wanangu tu, lakini kama umependekeza, basi iwe hivyo!”
“Sawa mama, wapi?”

“Johannesburg Hotel, Sinza Mori.”
“Ahsante kwa ofa yako mama, lakini nitakuja moja kwa moja hapo, muda huo nadhani ndiyo nitakuwa namalizana na jamaa zangu!”
“Sawa!”
Genesis akasimama na kuanza kupiga hatua za taratibu kuelekea nje, kabla hajafika kwenye mlango mkubwa wa kutokea nje, sauti ya mama yake ikimuita tena. Akasimama na kugeuka.

“Njoo mara moja!”
“Sawa mama!”
Sekunde chache, Genesis alikuwa amesimama mbele ya mama yake, akionekana kuwa makini sana kusikiliza wito wa mama yake ambaye alikuwa na jambo la kumwambia.
“Nilitaka kusahau, vipi kuhusu mwali wangu?”
“Farida?!”

“Kwani nina wali wangapi mwanangu zaidi ya Farida?”
“Mzima!”
“Sijamaanisha hivyo, ni kuhusu chuo!”
“Aaaah! Tumeshatuma maombi mama, ndiyo tunasubiria majibu!”
“Mwombee mwenzako Mungu afanye miujiza apate chuo,” akasema mama Genesis kwa sauti ya unyenyekevu iliyojaa mapenzi, lakini ndani yake kulikuwa na unafiki mtupu!

“Sawa mama, nafanya hivyo kila siku kabla ya kulala.”
“Vizuri sana, ilikuwa ni hivyo tu, kama ni kweli unafanya hivyo, vizuri sana.”
Genesis akaondoka zake. Siku nzima, alishinda na Farida kila wakati wakifungua anwani pepe yake na kuangalia kama walikuwa wametumiwa majibu. Jioni alimrudisha nyumbani kwao Mtoni Kwaaziz-Ali, kisha kilichofuata ilikuwa ni kwenda kwenye mualiko wa mama yake.

Akitokea Barabara ya Kawawa, kwenye mataa ya Magomeni Mapipa, alisimama kwenye foleni mpaka taa zilizoelekeza Barabara ya Morogoro kuelekea Ubungo zilipowaka, ndipo alipokata kushoto na kunyoosha moja kwa moja hadi Shekilango, alipokata kulia akiifuata barabara hiyo inayoelekea Sinza.

Alipofika Mori kwenye kituo cha daladala, alikata kulia akiifuata barabara inayoelekea Johannesburg Hotel. Mbele kidogo, akaifuata barabara hiyo ya vumbi, aliegesha gari lake nje ya jengo refu la ghorofa la hoteli hiyo. Akashuka na kumpigia mama yake, tayari walikuwa wameshafika, hivyo akamuagizia mahali walipokuwa wamekaa.
“Shikamoo mama, shikamoo baba!” Genesis akawasalimia kwa wakati mmoja wazazi wake ambao nao wakaitikia.

“Karibu!” Dada yake akasema.
“Ahsante, vipi nimechelewa sana?”
“Hapana, tena ndiyo tumeagiza vyakula, wote tunakula aina moja!”
“Ni nini?”
“Makange!”

Wote wakacheka, katika familia hiyo, hakuna chakula walichokuwa wakipenda kama makange. Waliendelea na mazungumzo na muda mfupi baadaye chakula kilifika mezani, wakaanza kula kwa furaha.
“Najua Genesis utakuwa umeshangaa kwa mwaliko huu wa ghafla, lakini ukweli ni kwamba, mtoko huu ni kwa ajili yako mwanangu.

Sina kitu kikubwa sana cha kuzungumza, ila nataka kukupa pongezi kutokana na uvumilivu wako katika kipindi chote cha misukosuko kati yako na Bianca na Farida, lakini hatimaye umeonesha msimamo wako thabiti kwa Farida.

“Kama tulivyokuambia awali, sisi kama wazazi wako hatuna kipingamizi na uamuzi wako. Tunakutoa wasiwasi kabisa, kwamba sasa tumebadilika na tupo pamoja na wewe, Farida chaguo lako ndiyo chaguo letu pia,” alisema mama Genesis kwa sauti iliyojaa utulivu mkubwa.

Sauti hiyo ndiyo iliyomfanya Genesis ashindwe kuzuia hisia zake, hivyo kuyaacha machozi yaanze kumiminika mashavuni mwake. Zilikuwa hisia za mapenzi ya dhati kwa Farida wake, lakini alifurahishwa sana na maneno ya mama yake, kumbe ndani yake kulikuwa na kitu kingine kabisa!

Kitu ambacho pengine kingemfanya alie maisha yake, ndani ya kauli ya mama yake kulikuwa na mkakati wa kifo! Mkakati ambao Genesis hakuujua!

Je, nini kitatokea? Maelezo ya Genesis yatawaridhisha maasakari wale?
 
Huyu mleta story hashauriki ukiimaliza hii story utaniambia mkuu wangu ilivyoisha story zake ni ndefu episode moja anashusha maepisode mengi sana mtu unapata uvivu wa kusoma
Karibu sana!
 
Huyu mleta story hashauriki ukiimaliza hii story utaniambia mkuu wangu ilivyoisha story zake ni ndefu episode moja anashusha maepisode mengi sana mtu unapata uvivu wa kusoma
Pole mamaa
Nmeishia episode ya 19 tu, nmechoka hatare nkaanza kuhisi usingizi!!
 
Pole mamaa
Nmeishia episode ya 19 tu, nmechoka hatare nkaanza kuhisi usingizi!!
Kanungila Karim kwa hali hii msahau tu Shunie
Hutampata ng'o labda ubadilike mkubwa
[emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23] Mm hizi za leo alivyoanza sijaanza hata moja yaani nguvu zimeniisha na ndio nimeshatoka kwenye huu uzi kwakweli
 
[emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23] Mm hizi za leo alivyoanza sijaanza hata moja yaani nguvu zimeniisha na ndio nimeshatoka kwenye huu uzi kwakweli
Pole sana!
Inachosha sana kunapokuwepo na mfululizo wa episode zaidi ya tano kwa siku. Kuna wakati hata ladha ya riwaya kupotea!

Jitahidi upatapo mda uwe unaptia ptia mamaa!!
 
Huo mda ukipata ukirudi unakuta episode 20 yaani mm ukitaka nisisome story nikute story imewekwa na imeisha siwezi au hivi mtu anapost episode nyingi siwezi napenda sana story kwa hapo nashindwa mm

Halafu mtu tunamuelewesha usifanye hivyo anaona sifa mwenyewe acha asome mwenyewe
Pole sana!
Inachosha sana kunapokuwepo na mfululizo wa episode zaidi ya tano kwa siku. Kuna wakati hata ladha ya riwaya kupotea!

Jitahidi upatapo mda uwe unaptia ptia mamaa!!
 
Msamehe bure tu Shunie
Huo mda ukipata ukirudi unakuta episode 20 yaani mm ukitaka nisisome story nikute story imewekwa na imeisha siwezi au hivi mtu anapost episode nyingi siwezi napenda sana story kwa hapo nashindwa mm

Halafu mtu tunamuelewesha usifanye hivyo anaona sifa mwenyewe acha asome mwenyewe
 
SEHEMU YA 30


Katika maelezo yake, Genesis alieleza jinsi mama yake alivyomwalika katika mtoko wa chakula cha usiku, wakiwa huko alimwambia kwamba alikuwa na maneno ya kumwambia. Katika hali ya kushangaza sana, mama yake akasisitiza kwamba hana matatizo tena na Farida na kwamba ni mwanamke mwema ambaye familia nzima imemkubali tofauti na ilivyokuwa mwanzoni.

Maneno hayo yakamfariji sana Genesis, faraja ambayo baadaye iligeuka mzigo wa huzuni kisha akaanza kumwaga machozi.Ilikuwa vigumu sana kuzuia hisia zake.
Je, nini kitatokea? Farida atapishana na risasi hadi kifo chake? SONGA NAYO…

WAKATI Genesis akilia machozi ya furaha, ndani ya ubongo wa mama yake kulikuwa na kitu tofauti kabisa, hakuwa anamaanisha alichokuwa akikitamka, ilikuwa ni kinyume chake. Kauli ile haikuwa ya kawaida kutoka kinywani mwa mama yake, lakini siku za karibuni ilikuwa kama wimbo mzuri na mpya masikioni mwake!

“Nyamaza baba, najua ni vigumu kuamini maneno ya mama yako, lakini unatakiwa kufahamu kwamba hakuna marefu yasiyo na ncha. Sisi kwa pamoja tumeamua kuwa upande wako, usiwe na wasiwasi kabisa juu ya hilo!” Profesa Mshana akasema.

“Najua baba, lakini sijui kwanini moyo wangu unazidiwa na furaha kiasi hiki!”
“Hilo linalotokea, si kwa hiyari yako baba, ni hisia za ndani, lakini tafadhali jikaze.”
“Nashindwa baba…sijui niseme neno gani kudhihirisha furaha yangu, lakini napenda kuwaambia kwamba nimefurahishwa sana na uamuzi wenu.”

“Sawa baba, tulia tuendelee kupata chakula!”
Kazi ya kumnyamazisha Genesis haikuwa ndogo, iliwachukua takribani dakika tano nzima hadi alipotulia kabisa na kuendelea kupata chakula.

“Halafu Genny, vipi kuhusu chuo?” Profesa Mshana akauliza, akimwita jina lake kwa kifupi.
“Chuo?”
“Ndiyo!”
“Ndiyo jambo ambalo linatuumiza kichwa zaidi mimi na Farida, lakini juhudi zetu si haba baba, siamini kama tutafeli safari hii!”

“Vizuri sana, nimefurahi sana kusikia hivyo, jitahidini hasa wewe kama mwanaume, lazima uoneshe ni kweli unaweza kuwa baba bora kwake, hilo unaweza kulionesha kwa kuanza kuchukua majukumu makubwa kama hayo mapema!”
“Najua baba, ni kweli najitahidi sana na mama amekuwa karibu na mimi kuhakikisha kwamba nafanikisha hili.”

“Vyema mwanangu, lazima nione kazi ya shahada yako kichwani na si shahada ya kwenye karatasi!”
“Ha! Ha! Ha! Ha!” Wote wakacheka.
Mazungumzo mengine yakaendelea hadi usiku kabisa walipoamua kurejea nyumbani kwao Masaki. Kutokea Johannesburg Hotel, Sinza Mori hadi nyumbani kuliwachukua robo saa tu, hasa kutokanana usiku huo kutokuwa na foleni ya magari barabarani.

“Ahsante sana mama, nimefurahia sana mtoko wako!” Akasema Genesis akiingia katika mlango mkubwa wa nyumba yao, baada ya kuegesha gari nje.

“Nashukuru mwanangu kama umefurahia, lengo langu hasa lilikuwa ni kukufurahisha, kama imekuwa hivyo ni vizuri sana.”
“Usiku mwema mama!”
“Nawe pia mwanangu!”

“Dad usiku mwema!”
“Lala salama pia mwanangu!”
“Dada, ulale salama, kesho!”
“Poa Genesis!”
Aliwatakia usiku mwema mmoja baada ya mwingine, akionekana mwenye furaha kuliko kawaida. Kwa Genesis kuishi na Farida pekee kulitosha kabisa kumfanya ajisikie amani kuliko kawaida ndani ya moyo wake.

Akaingia chumbani mwake, alipowasha taa kisha akavua nguo zote na kusogea jirani na kioo kilichokuwa kwenye meza yake ya kujipambia, akajiangalia machoni kwa udadisi mkubwa kama anayeangalia kitu fulani kikubwa.

Akanyoosha mkono wake kifuani kisha akaanza kujipiga-piga kwa nguvu huku maneno kinywani mwake yakimtoka: “Mungu anipe nini tena Genesis mimi?”

Akatoka kwenye kioo na kuchukua taulo lake, akajifunga kiunoni na kuingia katika bafu lililokuwa chumbani mwake. Huko alifungua koki inayotoa maji ya moto, kisha akachanganya na ya baridi kidogo, akayaruhusu yapite juu ya ngozi ya mwili wake.

Dakika tano zilimtosha kabisa kuoga na kurudi chumbani alipovaa nguo za kulalia na kujitupa kitandani akiwa na simu yake. Hapo hapo akamtafuta Farida hewani. Kwa bahati nzuri alikuwa anapatikana, wakaanza kuzungumza.

“Unaweza kukisia nipo wapi?” Genesis akamwuliza Farida kwa sauti ya taratibu sana.

“Zaidi ya nyumbani mpenzi wangu?”
“Ni kweli nipo nyumbani, sehemu gani?” Genesis akauliza akicheka.
“Chumbani kwako.”
“Kweli kwenye nini?”
“Kitanda!”
“Umepatia kabisa, nafanya nini sasa hivi?”
“Unaongea na mimi!”
“Ha! Ha! Ha!” Wote wakacheka kwenye simu.

Maneno ya Genesis yalikuwa yamejaa mahaba mazito, akijisikia huru sana kuzungumza na mwanamke wa maisha yake, mwanamke ambaye alikuwa ndani ya moyo wake, ambaye aliridhika kuwa naye kwa kila hali.

“Mpenzi wangu napenda kukuambia kwamba mama amebadilika sana juu ya huu uhusiano wetu siku hizi!” Genesis akasema.
“Kweli mpenzi, hata mimi pia namuona.”

“Na siyo mama tu, hata baba na dada, yaani niseme familia nzima ipo upande wetu, sasa hivi nina amani sana na haya mapenzi yetu. Huwezi kuamini leo mama ametupeleka hotelini kula, halafu kikubwa amesema kwamba anafurahishwa na uhusiano wetu.”
“Kweli?” Farida akauliza ilhali akionekana kujua jibu atakalopewa na Genesis.
“Kweli mpenzi wangu.”
“Basi tumshukuru Mungu kwa hili, najua nikipata chuo ndiyo nitakubalika zaidi.”

“Bila shaka mpenzi wangu, nadhani kikubwa ni kuendelea kumwomba Mungu na atatusaidia, sidhani kama sisi tuna dhambi kiasi hicho!”
“Genesis bwana, hata kama tuna dhambi, Mungu hawezi kukataa kujibu maombi yetu kwa sababu ya dhambi zetu kama tutajitakasa kwake.”
“Nimefurahi sana kusikia hivyo!”
“Mpenzi wangu usiku mwema, tambua kwamba nakupenda sana!”
“Hata mimi nakupenda pia mpenzi wangu!”

Wakakata simu zao. Genesis akajitahidi kuvuta usingizi, lakini ilimchukua muda mrefu kuupata, hata alipoweza kupitiwa na usingizi, njozi zote zilikuwa ni juu ya maisha yake mapya na mpenzi wake Farida.
***
“Uko wapi Genesis?” Ilikuwa ni sauti ya Farida kwenye simu mchana huo akizungumza na Genesis.

“Nyumbani, vipi kuna nini?”
“Nina habari njema.”
“Zipi tena?”

“Huwezi kuamini nimepata chuo!”
“Nini?”
“Nimeitwa chuoni mpenzi wangu!”
“Tafadhali sana, njoo moja kwa moja nyumbani sasa hivi, chukua teksi mimi nitalipa. Nataka hizi taarifa uzifikishe kwa mdomo wako kwa mama yako!”
“Nusu saa ijayo nitakuwa hapo mpenzi!”
Genesis hakuwa tayari kuona mpenzi wake anahukumiwa kifo kwa kosa ambalo si la kweli. Alichokifanya ilikuwa ni kwenda hadi Saudi Arabia kisha akaeleza kila kitu kwa uwazi na ukweli kabisa. Alikuwa akizungumza kwa kujiamini maana ushahidi wote ulikuwa katika anuwani pepe ya marehemu mke wake Bianca.

Akaeleza mipango yote ilivyofanyika chini ya timu iliyoongozwa na mama yake, mama Bianca, Patrick, Dulla na Festo hadi kufanikisha Farida kuingia kweye mtego ambao umesababisha afungwe kwenye mti akiwa na kitambaa usoni akisubiri risasi zianze kupenya mwilini mwake.

Ulikuwa mchezo wa hatari, ambapo Farida aliona waraka pepe wa wito wa kwenda kujiunga katika Chuo Kikuu Huria cha Riyadh, nchini Saudi Arabia. Akafurahi sana na kumjulisha mpenzi wake Genesis ambaye alimwambia kwamba, taarifa hizo aende akazifikishe kwa mdomo wake mwenyewe kwa mama yake mzazi, nyumbani kwao Masaki.

Jambo hilo Farida alilifanya, huku familia nzima ikionekana kufurahia, lakini kumbe nyuma yake kulikuwa na kitu tofauti. Siku ya safari ilipofika, Genesis alimfikisha hadi uwanja wa ndege na kuagana naye, hapo ndipo alipokwenda kukutana na matatizo nchini Saudi Arabia.

Maelezo ya Genesis yakapewa kipaumbele, ikaamriwa Farida afunguliwe kamba na kitambaa usoni ili wapelekwe Makao Makuu ya Polisi kwa mahojiano zaidi.

Pamoja na yote hayo, Genesis aliamini kabisa kesi ya mauaji ya Bianca ilikuwa mbele yake na ilikuwa lazima ahukumiwe kifo, ila hakuwa tayari kuona Farida anakufa kwa kosa ambalo hakufanya, moyoni aliumia sana.

UMATI wote ulipiga kelele ukishinikiza Farida aachiwe huru kwa kuwa hakuwa na kosa. Watu wote walikuwa upande wake, walibadilishwa na maelezo ya Genesis ambayo yalionekana kuwa na maana na nguvu kubwa.
“Aachiwe huru!” Sauti zilisikika.

“Hana hatia...” sauti nyingine zilipiga kelele.
“Mwacheni!”
Viwanja vyote vililipuka kwa kelele ajabu, tofauti na mwanzoni ambapo walikuwa wanashinikiza zoezi la kumuua lifanyike haraka. Kelele hizo, zilimfanya Mkuu wa Kikosi kusogea kwenye kipaza sauti na kutuliza wananchi.

“Wote tumemsikiliza kwa makini sana Genesis, sisi kama chombo cha dola, kwa sasa tumeahirisha zoezi la kumuua Farida, lakini bado tuna mengi ya kuzungumza nao nje ya viwanja hivi.

“Nawaombeni muwe watulivu na wavumilivu, tunakwenda nao ofisini na yatakayozungumzwa huko ikiwa ni pamoja na uamuzi tutakaoufikia kwa pamoja, tutawatangazia kupitia vyombo vya habari. Tunahitaji sana utulivu wenu tafadhalini sana,” akasema Mkuu wa Kikosi kwa sauti kubwa.
“Hapanaaa...hana hatia...mwacheni...” kelele hizi ziliendelea kusikika.
Baada ya kuona kwamba pamoja na maelezo hayo, vurugu zinaendelea, maaskari waliamua kutumia nguvu ya ziada, wakarusha mabomu ya machozi na watu kuanza kusambaratika!
Wakaingia zao kwenye gari na safari ya kwenda Makao Makuu ya Polisi ikaanza, raia wakibaki wanajifuta machozi.
***
“Unaweza kutueleza japo kwa ufupi ulivyokutana na Farida?” Insp. Farook aliyekuwa akizungumza na Genesis katika chumba cha mahojiano alimwuliza.
“Ndiyo Mkuu.”
“Endelea...”
“Nilikutana naye shuleni, wakati nikiwa nasoma kidato cha pili. Kifupi tulisoma naye shule moja na huko ndipo mapenzi yetu yalipoibuka!”

“Kuhusu huyo marehemu Bianca?”
“Naye pia tulisoma wote, lakini wazazi wake ni rafiki na wazazi wangu. Unajua Bianca awali alikuwa akiishi Uswis na wazazi wake, kwa hiyo walirudi Tanzania baada ya kuishi huko kwa muda mrefu.

“Kwa sasa baba yake ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali nchini Tanzania. Wazazi wa pande zote mbili walitamani sana mimi niishi naye, ndiyo maana wakafanya yote hayo!”
“Kwanini ulimuua Bianca?”

“Niliudhika baada ya kugundua ukweli, sikuwa na zawadi nyingine ya kumpa zaidi ya kumuua, hata hivyo najua nilifanya makosa na sasa najutia!”
“Unatambua kwamba, utakabiliana na kesi ya mauaji ambayo mwisho wake inaweza kuwa kifo?”

“Najua...nipo tayari na wala sijutii juu ya hilo, maana ni kweli nilimuua. Kikubwa kwangu sikutaka kabisa Farida afe kwa kosa ambalo hakulifanya, ndiyo maana nipo hapa!” Akasema Genesis kwa kujiamini.
“Sawa Genesis, nashukuru sana kwa ushirikiano wako, bado kuna mengi ya kuzungumza na wewe, kwa hiyo utaendelea kuwa hapa!”
“Hakuna tatizo katika hilo.”

Mpelelezi akatoka na kwenda ofisini kwa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai aitwaye Abdullazizi Mubarak ambapo huko alipeleka ripoti nzima, hiyo ni baada ya kuzungumza na Genesis pamoja na Farida.
Alipofika ofisini kwake aliweka faili lenye ripoti nzima mezani kisha akaketi kwenye kiti na kumsikiliza kwa makini mkuu wake wa kazi.

“Kila kitu kimo humu,” alisema Insp. Farook.
“Lakini kwa haraka, kabla sijaanza kupitia ripoti yako, unaweza kuniambia umegundua nini?”
“Maelezo yao yana ukweli Mkuu, ni kweli kabisa Farida hahusiki kabisa na hii kesi.”

“Umefikiria kufanya nini?”
“Kikubwa nilichoona Mkuu, ni kuwasiliana na wenzetu wa Tanzania ili tuwapelekee watu wao!”
“Sawa, acha nipitie kidogo halafu nitakujulisha hatua inayofuata.”
“Sawa Mkuu.”
Insp. Farook akapiga saluti mbele ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai na kuondoka zake. Ofisini alibaki peke yake na kuanza kusoma ripoti nzima taratibu. Moyo wake uliumia sana baada ya kuona mchezo ule mchafu ambao ulilenga kumuua Farida.

Alitamani sana kesi ile iendeshwe nchini mwake lakini jambo hilo halikuwezekana kulingana na kanuni walizojiwekea. Kwanza Farida hakuhusika kabisa na kesi ile, lakini pia Genesis alikuwa na kesi ya kujibu kuhusu mauaji ya Bianca.

Hapakuwa na kitu kingine chochote cha kufanya zaidi ya kufanyika haraka mawasiliano nchini Tanzania na kuwajulisha juu ya kilichoendelea.

Makubaliano yakawa ni yale yale, kwamba Genesis na Farida warudishwe Tanzania kwa ajili ya kuendeshwa kwa kesi zao.
***
Gari lililojaa maaskari liliingia kwa kasi ya ajabu katika geti la kuingilia Chuo Kikuu cha Global Engineering. Walinzi wa getini walishangazwa sana na hali hiyo.

“Kuna usalama kweli?” Askari mmoja wa getini akamwuliza mwenzake.
“Mh! Sijui.”
Safari ya gari lile iliishia nje ya Jengo la Utawala kulipokuwa na ofisi za chuo hicho. Maaskari wakashuka kwa kasi na kuzunguka eneo hilo, kisha watatu waliokuwa na silaha mikononi mwai tayari kwa lolote, wakaanza kupiga hatua za haraka kwenda ofisini kwa mama Genesis.

Walibisha hodi mara moja, tayari walikuwa ndani. Mikononi mwao wakiwa na silaha na zote walizielekeza kwake.

“Uko chini ya ulinzi, hutakiwi kufanya kitu chochote mama zaidi ya kusimama na kutoka nje, ukaingie kwenye gari!” Alisema mmoja wa askari wale kwa sauti iliyomaanisha.
“Kuna nini?”
“Utajua Oystebay!”
“Oyterbay tena?” Akauliza mama Genesis woga wake ukionekana dhahiri.

“Ndiyo Oysterbay Polisi!”
Hakuweza kujua kilichotokea, mwili mzima ulikuwa unatetemeka kwa hofu, bila hiyari yake akasimama na kutoka akiwafuata maaskari wale. Alifungwa pingu kisha akatolewa akipita na pingu mbele ya Sekretari wake ambaye mpaka muda huo hakujua kilichokuwa kikiendelea.

“Lakini nataka kujua nimefanya nini?” Mama Genesis akauliza tena, kichwani mwake kukiwa na giza tupu.
“Nimeshakuambia utajua Polisi, ingia kwenye gari!” Askari huyo akamuamrisha kwa hasira.

Mama Genesis akaingizwa nyuma ya gari aina ya Land Rover 110, akakaa chini, akiwa amezungukwa na maaskari kila upande waliokuwa na silaha mkononi. Mpaka wakati huo hakujua kilichokuwa kikiendelea, lakini ubongoni mwake kuliwaka taa nyekundu!
Harufu kali ya jela ikaanza kunukia. Hakika hakuipenda kabisa harufu hiyo, lakini iliendelea kunukia zaidi.

Je, nini kitatokea? Mama Genesis atasalimika katika mikono ya dola? Vipi kuhusu mama Bianca, Patrick, Festo na Dulla?
 
SEHEMU YA 31




Maelezo yake yakapewa kipaumbele, ikaamriwa Farida afunguliwe kamba na kitambaa usoni ili wapelekwe makao makuu ya polisi kwa mahojiano zaidi. Baada ya Genesis kuhojiwa na Insp. Farook, ripoti ikapelekwa ofisini kwa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai, Abdullazizi Mubarak ambaye aliamuru Genesis na Farida warudishwe Tanzania.
Upande wa pili, gari lililojaa maaskari linaingia Chuo Kikuu cha Global Engineering kwa kasi sana. Linasimama mbele ya jengo la utawala, wakashuka na kwenda moja kwa moja ofisini kwa mama Genesis kisha wakamkamata.

Hawakumweleza sababu za kumkamata ingawa aliomba sana. Wakamchukua tayari kwa safari ya kwenda katika Kituo cha Polisi Oysterbay, akiwa hajui chochote, lakini akihisi hatari kubwa mbele yake.
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

GARI la Polisi aina ya Landrover 110 liliingia kwa kasi katika Kituo cha Polisi Oysterbay kama lilivyotoka muda mfupi uliopita. Maaskari wote wakashuka haraka kisha wakamuamrisha mama Genesis naye ashuke haraka.

Aliposhuka wakamuongoza moja kwa moja hadi kaunta alipopitishwa mkuku na kupandishwa ngazi hadi ghorofa ya kwanza katika Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai(OCID) Wilaya ya Kinondoni, Yussuf Wambura.

Maaskari wawili waliingia na kupiga saluti mbele ya meza ya Wambura, ambaye alizipokea haraka na kuachana nao, akahamishia macho yake kwa mama Genesis ambaye alikuwa akitetemeka kwa woga.

“Huyu hapa afande!” Mmoja wa maaskari wale akasema.
“Ndiye huyu?”
“Ndiyo Mkuu!”
“Naomba mtupishe,” akasema Wambura akiwa ameukunja uso wake.
“Hivi kabla sijakufunga, unaweza kuniambia ni kwanini umefanya mchezo mchafu wa kipumbavu kiasi hiki?” Wambura akauliza akiwa ametoa macho yake kwa hasira.

“Mpaka sasa hivi sijajua kinachoendelea, kwani kuna nini?” Mama Genesis akauliza.
“Sura yako inaonesha una ukarimu sana, msomi na mwenye kujitambua, lakini kumbe umejivika ngozi ya mwanakondoo wakati wewe ni simba mla watu!”

“Maneno yako yamejaa mafumbo mkuu, naweza kujua kilichosababisha niwe hapa?” Mama Genesis akajikaza kidogo na kujitahidi kuuliza.
“Mwanao yuko wapi?”
“Nani?”
“Genesis!”
“Genesis?!” Mama Genesis akauliza kwa mshangao, macho yake yakianza kulengwalengwa na machozi.

“Ndiyo...aliyefanya sherehe ya harusi pale Atrium Hotel.”
“Afande mbona hiyo kesi ipo hapa?”
“Kesi ya nini?”
“Baada ya mke wake kukutwa amekufa, Genesis hakuonekana, mpaka sasa tumechanganyikiwa na taarifa zipo hapa!”
“Najua zipo hapa.”

“Mbona sikuelewi afande, kama taarifa unazo, kwanini unaniuliza tena?”
“Sikiliza, usijifanye mjanja, unasumbua jeshi la polisi kumbe ukweli unao wewe. Hata kifo cha Bianca umesababisha wewe na genge lako. Unadhani serikali imelala wewe ufanye ujinga wako isijue?

“Dola ina mkono mrefu mama, tunaweza kukukamata hata kama ulifanyia mambo yako gizani. Sasa nataka kukuambia jambo moja, Genesis yupo hai!”
“Mwanangu yupo hai?”
“Ndiyo yupo hai...na ni yeye ndiye aliyevumbua upumbavu wote ulioufanya!”
“Kwanini mnanificha kwa muda wote huo lakini?”
“Unataka kujua ukweli?”

“Ndiyo afande.”
“Subiri.”
Wambura akachukua mkonga wa simu iliyokuwa mezani kisha akabonyeza namba fulani na baadaye akaanza kuzungumza na mtu wa upande wa pili. Baada ya hapo akarudisha chombo sehemu yake kisha akayatuliza macho yake kwa mama Genesis ambaye hakuwa anajua chochote kinachoendelea.

Dakika moja baadaye, mlango uligongwa na kufunguliwa kwa wakati mmoja. Wakaingia maaskari wawili ambao walipiga saluti mbele ya mkuu wao kisha wakamsogeza mtu waliyeingia naye mbele ya Wambura. Mpaka muda huo, mama Genesis alikuwa hajakutanisha uso wake na mtu huyo.

“Hebu geuka nyuma uniambie kama unamfahamu huyo mtu hapo nyuma yako!” Akasema Wambura akimwangalia mama Genesis.
Mama Genesis akageuza uso wake nyuma, sura aliyokutana nayo, hakutegemea hata kidogo, akahisi kuzimia. Alikuwa ni Dulla amesimama akimwangalia kwa jicho la huzuni sana. Moyo wake ukapiga kwa nguvu puu!
“Vipi unamfahamu?” Wambura akamwuliza.

Lilikuwa swali gumu sana kwa mama Genesis, alibaki kimya kwa muda mrefu bila kujibu kitu. Mpaka hapo, tayari alikuwa ana majibu! Alishajua kwamba, kila alichokifanya kilikuwa kimeshajulikana.
“Nakuuliza unamfahamu?” Wambura akauliza tena.
Mama Genesis hakuwa na jibu.
***

Mipango ya safari ikafanyika haraka, siku tatu baadaye Genesis na Farida walikuwa angani wakirejeshwa nchini Tanzania kwa ajili ya kwenda kukabiliana na kesi zao. Waliongozana na maaskari wawili, mmoja wa kike aliyekuwa kwa ajili ya Farida na mwingine wa kiume ambaye alimlinda Genesis.

Muda wote kwenye ndege Farida alikuwa akilia, machozi yake yalikuwa na sababu kuu mbili, kwanza alikuwa haamini kama kweli amefanikiwa kutoka katika kifo ambacho kilikuwa mbele yake. Sababu nyingine ambayo kwake ilikuwa kubwa zaidi ni Genesis, aliamini kuwa hakuwa na mahali pa kutokea katika kesi itakayomkabili.

Kilichogonga kichwani mwake ni kuwa, lazima Genesis auawe au afungwe kifungo cha maisha kwa kosa la mauaji ambalo alilikiri. Machozi yake yakawa mwiba mchongoma kwa Genesis aliyekuwa ameketi jirani yake.
“Farida kwanini unalia?” Genesis akamwuliza.
“Nakupenda Genesis!”

“Najua, hata mimi nakupenda pia.”
“Kuhusu wewe hata usiposema, mambo uliyoyafanya kwa ajili yangu ni makubwa sana! Yanatosha kuongea.”
“Sasa kama yote hayo unayajua, kwa nini unalia?”
“Mpenzi wangu, huoni hatari iliyopo mbele yako?”
“Hatari? Hatari gani?”

“Hiyo kesi ya mauaji ya Bianca!”
“Usijali mpenzi wangu, Mungu mwenyewe ndiye atakayetenda, anajua wakati nilipokuwa nafanya kitendo hicho, moyoni mwangu nilikuwa na dhamira gani. Kama anajua, atanipigania. Hata hivyo sijutii kabisa, moyo wangu una amani.

“Ninafurahi kuona kwamba naelekea kufanikiwa kukutoa kwenye kifo, ambacho hukuwa na hatia nacho. Ni afadhali mimi ambaye hata kama nitahukumiwa kifo, ni kweli niliua, nitakuacha huru na moyo wangu utaendelea kuwa na amani siku zote!”
Genesis aliongea maneno mazito sana ambayo yalizidi kumchoma Farida moyoni mwake. Wale maaskari ambao walikuwa nao, walikiwa kimya wakiwasikiliza lakini hawakuelewa kitu, maana walikuwa wakizungumza kwa lugha ya Kiswahili.

Safari nzima walikuwa wakizungumza, Farida akijitahidi kumpa moyo mpenzi wake, lakini Genesis hakuonekana kujali kabisa, alikuwa tayari kwa lolote. Farida alikuwa akilia muda wote.
***
Mama Genesis akionekana kuwa katika bumbuwazi zito, mlango ukafunguliwa tena, uso wake ukakutana na sura nyingine zilizoonesha mlango wa kifo mbele yake.

Walikuwa ni Patrick, kijana anayefanya kazi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam (DIA) na Festo, mtaalam wa mambo ya Mawasiliano na Teknolojia.
“Mungu wangu!” Mama Genesis akatamka bila hiyari yake.
“Vipi tena?” Wambura akauliza.

“NIMEKWISHA!” Akajisemea moyoni mwake.
Tayari mwili mzima ulikuwa umeshalowana na jasho jepesi la woga. Kifo kilikuwa mbele yake na kwa hakika hakuwa na njia za kujinasua.

OFISI nzima ilikuwa kimya kabisa, hakuna aliyefungua kinywa chake kuzungumza chochote. Si mama Genesis, Festo, Patrick wala Dulla waliokuwa wamesimama mbele ya askari wawili waliokuwa mlangoni, wakitazamana uso kwa uso na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Wilaya ya Kinondoni, Yussuf Wambura.

Mama Genesis alikuwa anatetemeka kwa hofu akiwa anaogopa sana, mpaka wakati huo hakujua kama imejulikana aliyemuua Bianca alikuwa ni Genesis, hilo lilikuwa kama giza nene mbele yake.

“Sema bwana, sasa umeshapata picha au bado?” OCID akamwuliza.
Mama Genesis alikuwa kimya, hata hivyo hakuwa na jibu. Kimya kikatawala tena. Alikuwa akijaribu kufikiria kwa kina lakini hakuweza kupata jibu la moja kwa moja.

“Nazungumza na wewe!”
“Afande, sitaweza kuzungumza chochote mpaka wakili wangu awepo.”
“Unataka wakili wako kwanza?”
“Ndiyo!”
“Kwanini?”
“Ni haki yangu.”

“Ni haki sawa, lakini napenda kufahamu kwanini unashindwa kujibu hata maswali madogo madogo, ambayo wakili hatashughulika nayo?”
“Afande mimi sielewi kabisa kinachoendelea, yaani niseme kwamba nimechanganyikiwa sana na hili tukio.”

“Pole sana!” OCID akasema, lakini mama Genesis hakujibu kitu.
“Kwa hiyo huelewi kabisa?”
“Sielewi kitu, nadhani kuna mchezo unataka kufanyika. Wakili wangu angeweza kuniwakilisha vizuri, maana yeye anajua mambo ya sheria.”

“Sawa nimekuelewa na kwa hakika uliyoongea ni ya msingi sana, ila hapa nina swali moja tu kwako, tafadhali naomba ujibu!”
“Sawa.”
“Hawa watu unawatambua?”

“Hawa?” Akauliza mama Genesis akiwaangalia.
“Ndiyo, unawafahamu?”
“Hapana.”
“Kweli?”
“Siwafahamu kabisa.”

“Ok! Subiri kidogo,” akasema OCID kisha akachukua simu yake ya mezani na kubonyeza namba kadhaa halafu akaweka chombo sikioni na kuanza kuzungumza na upande wa pili.

Alipomaliza mazungumzo, akarudisha simu sehemu yake, kisha akaanza kuwaangalia wote, mmoja baada ya mwingine. Wote walikuwa kimya, sura zao zikionekana kuwa na majuto sana. Muda mfupi baadaye mlango ukafunguliwa, wakaingia askari wawili waliokuwa na silaha mikononi mwao,wakiwa wanamwongoza mama Bianca kuingia ndani. Mama Genesis alipomuona akachanganyikiwa.

“Huyu unamfahamu?” OCID akamwuliza mama Genesis.
“Ndiyo namfahamu.”
“Ni nani?”
“Ni rafiki yetu, lakini pia marehemu mwanaye aliolewa na mwanangu Genesis.”
“Sawa...Bi. Rwegoshora anayosema Bi. Mshana ni ya kweli?”
“Ndiyo afande,” akasema mama Bianca machozi yakimlenga.

“Unawafahamu hawa vijana?”
“Ndiyo nawafahamu!” Mama Bianca akajibu.
“Ok! Afande warudisheni ndani kwanza hawa watu!” OCID akaamrisha.
“Sawa Mkuu!”
Wote wakachukuliwa na kurudishwa selo.

***
Saa 10:30 za alasiri, Ndege ya Shirika la Ndege la Kenya, waliyokuwa wakisafiria Genesis na Farida, wakisindikizwa na askari wa Interpol, ilikuwa inatua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam (DIA). Walitangulia Farida na Genesis kisha wakafuata askari nyuma yao.

Tayari walikuwa wameshaweka utaratibu wa kuwapokea, kwa hiyo walipotoka tu kwenye mlango mkuu wa kutokea uwanjani, walipokelewa na askari wa Tanzania na kupelekwa moja kwa moja kwenye gari la Polisi. Safari ya kwenda katika Kituo cha Polisi Oysterbay, Kinondoni jijini Dar es Salaam ikaanza.

Farida alikuwa akitetemeka kwa woga, kikubwa alichokuwa akiwaza ni kwamba Genesis alikuwa anakwenda kukabiliana na mashitaka ya mauaji, kesi ambayo kwake yeye aliamini kama si kunyongwa, basi angekuhumiwa kifungo cha maisha jela. Machozi yakaendelea kumiminika machoni mwake.

“Lakini mpenzi wangu nilishakuambia tangu mwanzoni, kwamba huna sababu ya kulia.”
“Najua mpenzi, lakini moyo wangu unauma sana, najua kabisa lazima nitakupoteza.”

“Kila kitu kinapangwa na Mungu Farida, kama alipanga mimi na wewe tufunge ndoa, itakuwa hivyo kama hakupanga basi mapenzi yake yatatimizwa!”
“Unamaanisha nini kusema hivyo?”

“Nina maana kwamba, lolote linaweza kutokea, kama ambavyo Mungu alivyopanga. Hatuwezi kubadilisha uamuzi wa Mungu, ambaye anajua kesho yetu. Kwa nini hutaki tumuache afanye kazi yake anavyotaka?”

“Nimekuelewa lakini naona kama hii kesi itakuwa ngumu sana upande wako. Kwa nini hukuaniacha mimi nikafa Genesis?”
“Kwa nini?”
“Kuna faida gani sasa kama umeniokoa halafu hutanioa?”
“Faida ipo, tena kubwa sana!”
“Gani?”
“Kukutoa kwenye hukumu ambayo haikukustahili pekee inatosha mpenzi wangu.

Tafadhali kuwa na amani na sipendi kabisa kuumiza moyo wangu!”
Farida hakujibu neno tena baada ya hapo. Walikuwa kimya kabisa, gari likiendeshwa kwa kasi hadi dakika ishirini baadaye liliposimama nje ya Kituo cha Polisi cha Oysterbay. Farida na Genesis wakashushwa na kuingizwa kituoni hapo.

Walipelekwa moja kwa moja hadi ofisini kwa OCID. Askari wa Interpol wakasalimiana na OCID kisha kutoa taarifa nzima ya kesi zao. Hapakuwa na jambo geni, kila kitu walikuwa wameshazungumza kupitia simu, kikubwa kilichofanyika ilikuwa ni kutoa ripoti kwa maandishi na maelezo yao waliyoyatoa Saudi Arabia.

Baada ya jambo hilo kukamilika, OCID akasaini fomu maalumu ya kuwapokea Genesis na Farida. Kila kitu kikawa kimekamilika. Kilichofuata ilikuwa ni wale askari kupelekwa hotelini kwa ajili ya mapumziko kabla ya safari ya kurejea kwao Saudi Arabia.

OCID akabaki na Genesis na Farida ofisini kwake. Hakuzungumza nao chochote tangu` walipoingia ofisini kwake. Alichokifanya ilikuwa ni kupiga simu na kuzungumza na upande wa pili, hakuzungumza maneno mengi sana.
“Hebu walete hao wapuuzi ofisini kwangu haraka!” Ndiyo maneno pekee aliyozungumza OCID.

Dakika moja baadaye, mama Bianca na mama Genesis waliingizwa ofisini kwa OCID. Macho ya mama Genesis yakagongana na ya Farida, kisha yakakutana na ya mwanaye
Genesis!
Hakuna aliyeweza kuvumilia, wote mvua ya machozi ikaanza kuwaminika mashavuni mwao.

Je, nini kitatokea? Nini kitampata mama Genesis, mama Bianca na akina Festo na wenzake?
 
SEHEMU YA 32


Akiwa hana hili wala lile, anashangaa Dulla, mjanja wa mjini anayehusika na dawa za kulevya akiingizwa ofisini hapo akifuatiwa na Patrick anayefanyakazi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam, kitengo cha ukaguzi wa mizigo inayoingia na kutoka sanjari na Festo, mtaalam wa teknolojia ya mawasiliano, watu ambao wanahusika na mchezo mzima.

Mama Genesis akiwa amechanganyikiwa kabisa, akaingizwa mama Bianca ambaye alipoulizwa kama anafahamiana na akina Dulla alijibu ndiyo! Hapo mama Genesis akachanganyikiwa kabisa. Tukio lililomchanganya zaidi ni baada ya kupelekwa ofisini kwa OCID na kuwakuta Farida na Genesis! Hapo ndipo alipojua kwamba kila kitu kilikuwa kimeshaharibika na njia ya kujitoa kwenye matatizo hayo ilikuwa ni sawa na giza nene!

Je, nini kitatokea? Mama Genesis na wenzake watafanikiwa kuepuka kitanzi? SONGA NAYO...

WALIENDELEA kuangaliana kwa dakika nzima bila yeyote kati yao kuzungumza chochote. Genesis alikuwa akilia kwa uchungu mwingi huku akiwa haamini kilichokuwa mbele yake. Ni kweli alikuwa akimuona mama yake, ambaye alitakiwa kukabiliana na kesi iliyokuwa mbele yake.

Mama Genesis alishindwa kabisa kujizuia ingawaje alijitahidi sana kuzuia jambo hilo lisitokee bila mafanikio kabisa. Kila alipotazama macho ya mwanaye na baadaye Farida alijikuta akilia.
“Wewe ni mwanangu sasa, sehemu ya familia yangu, una uhuru wa kuja hapa wakati wowote na kufanya chochote. Tayari nimeshabadilisha mawazo na sasa nipo tayari kuona mkioana!” Maneno haya aliyowahi kusema mama Genesis akimwambia Farida yalianza kujirudia kichwani mwake.

Farida akajikuta anazidisha kilio. Zilikuwa ni kumbukumbu za maumivu makali sana ambazo kwa hakika hakupenda kabisa kuzikumbuka mara kwa mara. Chanzo cha yote alikuwa mama Genesis ambaye alijifanya mwema kumbe alitaka kumwangamiza.

Genesis hakuwa na huruma na mama yake, aliamini kitanzi ni haki yake, maana alimdanganya na kumfanya akaingia kwenye matatizo makubwa ambayo hakuyatarajia awali. Ni yeye ndiye aliyesababisha akamuua Bianca, dhambi ambayo inamtesa sana moyo wake.

“Acha kulia kwa unafki mama, nyamaza maana uliyajua yote haya!” Genesis akasema kwa hasira akifuta machozi yake.
“Genesis!” Mama yake akaita.
“Una nini cha kuniambia?”
“Kumbuka mimi ni mama yako!”

“Ni afadhali usingenizaa, wewe ni mwanamke mbaya na hatari sana katika taifa, unaweza kuangamiza hata nchi nzima. Una roho mbaya sana!”
“Acha Genesis tafadhali!” Akasema Farida aliyekuwa pembeni yake akilia.
“Siwezi Farida...” akasema Genesis akionekana kuwa na hasira sana, lakini OCID alimkatisha.
“Nyamaza bwana mdogo, hapa si mahakamani na sijamruhusu mtu yeyote kuzungumza. Muda ukifika, mtafanya hivyo!” Akasema OCID akiwakazia macho.

“Inaniuma afande.”
“Nyamaza.”
Genesis akanyamaza na kumwangalia OCID ambaye kauli yake ilionekana wazi kuwa ilikuwa ya kuamrisha.
“Farida...” hatimaye OCID akaita.
“Abee!”

“Unamfahamu huyu mama hapa mbele yako?”
“Ndiyo!”
“Unamfahamuje?”
“Ni mama yake na Genesis, huyu niliyenaye naye hapa ambaye ni mpenzi wangu.”
“Huyo ni mpenzi wako?” OCID akauliza.

“Ndiyo!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo afande!”
“Wazazi wa pande zote wanafahamu?”
“Ndiyo...wazazi wangu wanamfahamu Genesis ingawa si rasmi. Wanamjua kwa kumuona kwa kuwa mara nyingi hunipeleka nyumbani, pia wanamfahamu kwa kuwa nilikuwa nasoma naye, lakini mama ndiyo anamfahamu zaidi, maana nilimweleza kuwa ni mpenzi wangu!”

“Alikubali?”
“Ilikuwa ngumu sana kuamini kuwa naweza kuwa naye, kutokana na tofauti zenu za kimaisha na imani ya dini!” Akasema Farida.
“Ikawaje?”
“Baadaye aliamini, baada ya kumweleza kwamba wazazi wake na Genesis wameshanikubali!”
“Kwani waliwahi kukukataa?”

“Ndiyo! Tangu siku ya kwanza kwenda kwao, wazazi wake walichukizwa sana na mimi, hasa baada ya kusikia kwamba naishi Mtoni Kwa Aziz Ally. Walinichukia kutokana na umasikini wangu, lakini Genesis aliendelea kusema kwamba ananipenda na atahakikisha anawaweka sawa wazazi wake ili wanikubali.

“Ilikuwa jambo gumu kidogo kwangu kumuelewa Genesis, lakini nilivumilia hadi siku ambayo niliitwa nyumbani kwao Masaki na kukaribishwa rasmi kama mwari wao, wakinitaka nisahau kila kilichopita!”
“Unaelezeaje uhusiano wenu?”
“Ulikuwa wenye misukosuko mingi, lakini niliivumilia kwa kuwa mwenzangu alinipa moyo!”
“Unafahamu kwamba mwenzako alioa?”

“Ndiyo!”
“Lini?”
“Baada ya mimi kwenda Saudi Arabia na kukutana na matatizo.”
“Matatizo gani?”
“Ni habari ndefu afande, lakini kikubwa ni kwamba kwenye begi langu kulikutwa na madawa ya kulevya nikiwa kwenye ukaguzi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Riyadh, Saudi Arabia!”
“Huwa unauza madawa ya kulevya?”

“Hapana.”
“Sasa ilikuwaje kwenye begi lako kukakutwa hayo madawa?”
“Sijui afande, lakini ukweli halisi anao Genesis!”
“Una maanisha nini kusema hivyo? Au yeye ndiye aliyekutuma?”

“Hapana afande, namaanisha kwamba yeye ndiye aliyekuja Saudi Arabia kuniokoa. Maelezo yake ndiyo yaliyosababisha mimi niwe hapa, maana tayari nilikuwa nimeshafungwa kitambaa cheusi usoni nikiwa mtini tayari kwa kupigwa risasi, ndipo Genesis alipotokea na kunisaidia,” akasema Farida kwa uchungu.

Kufikia hapo alishindwa kabisa kuvumilia, akajikuta akimwaga machozi kama maji akiwa hana amani kabisa moyoni mwake. Muda wote aliokuwa akijibu maswali ya OCID alikuwa akiyaandika kwenye katarasi maalum lililokuwa ndani ya faili.
“Sawa Farida, bado kuna mambo mengi nitayahitaji kutoka kwako!”
“Ahsante sana afande.”

Mama Genesis alichanganyikiwa, tayari alishagundua kwamba kila kitu kilikuwa peupe na hakuwa na njia ya kujinasua katika hatari iliyokuwa mbele yake. OCID akamgeukia mama Genesis na kuanza kuzungumza naye.
“Bi. Mshana umesikia aliyozumgumza Farida?”
“Ndiyo!”

“Ni ya kweli?”
“Sina la kusema afande, kama nilivyosema awali nahitaji mwanasheria wangu afike kwanza hapa, ndipo nitaweza kutoa ufafanuzi!” Akasema mama Genesis.
Afande mrudishe huyu mama selo, niache na hawa vijana, bado nahitaji kuzungumza nao!” OCID akamwambia askari aliyekuwa amesimama mbele yake.
“Sawa mkuu!” Akajibu askari yule akitekeleza agizo alilopewa na mkuu wake wa kazi.

***
Wakati akiwa bado hajapona majeraha ya kufiwa na mwanaye Bianca, huku mtu aliyemuua akiwa bado hajajulikana, Dk. Rwegoshora alishtuka sana alipopokea taarifa za kwamba mke wake amekamatwa na Polisi wa Kituo cha Oysterbay.

Akiwa yupo ofisini kwake akapiga simu katika kituo hicho na kuomba kuzungumza na mkuu wa kituo ambaye alimweleza kila kitu kuhusu sababu za mkewe kukamatwa. Alihisi kuchanganyikiwa baada ya kusikia kwamba aliyemuua mwanaye alikuwa ni Genesis!
“Una uhakika afande?”
“Kwa mdomo wake amekiri hivyo!”

“Mmeshamkamata?”
“Ndiyo!”
“Yupo hapo kituoni?”
“Ndiyo!”
“Nakuja sasa hivi!” Akasema Dk. Rwegoshora na kukata simu bila kuagana na mkuu wa kituo.

HAKUWA na muda wa kuangalia kazi zilizobaki ofisini kwake, alichokifanya ilikuwa ni kuzima kompyuta yake na kutoka moja kwa moja mpaka kwa sekretari wake ambaye alimkuta Mapokezi akisinzia. Kwa Dk. Rwegoshora lilikuwa ni kosa kubwa sana lakini hakutaka kufuatilia.
“Vipi Nice?”

“Samahani bosi!” Nice akasema kwa woga.
“Mimi natoka!”
“Naomba unisamehe bosi,” alisema Nice akiendelea kuomba msahama akiamini kwamba kosa lile lilikuwa limemuudhi sana bosi wake.
“Endelea na kazi!” Akasema Dk. Rwegoshora akionekana kutotilia maanani kabisa maneno ya Nice.

Kichwani mwake kulikuwa na mambo mawili makubwa, mosi,aliwaza kuhusu mwanaye mpendwa Bianca aliyefia hotelini kwa kuchomwa na kisu kifuani akiwa haamini kabisa kama mhusika angeweza kuwa Genesis kama taarifa za kipolisi zilivyokuwa. Kikubwa zaidi kilichomchanganya ni mke wake mpendwa kukamatwa jambo ambalo lilimuumiza hasa akiwa mwanasheria mkuu wa serikali.

Alitoka nje haraka na kuchepuka hadi alipoegesha gari lake, akaingia na kuwasha, haraka akaingiza gia namba moja na kuondoka gari kwa kasi sana. Safari ya kwenda kituo cha Polisi Oysterbay, Kinondoni jijini Dar es Salaam ikaanza.
***
Haikuwa kazi ngumu kwa Dk. Rwegoshora kuonana na mkuu wa kituo cha polisi cha Oysterbay baada ya kujitambulisha kwamba yeye ni mwanasheria mkuu wa serikali. Akapelekwa hadi ofisini kwake na kuanza kuzungumza naye.

“Pole na kazi afande!”
“Nashukuru sana, pole na wewe!”
“Hivi ni nini hasa kimetokea?” Dk. Rwegoshora aliuliza akionekana kuwa na majonzi moyoni mwake.
“Kama tulivyoongea kwenye simu ndivyo ilivyo, lakini hili shauri lipo ofisini na OCID, nadhani uende ukaongee naye!”
“Ok, nashukuru.”

Dk. Rwegoshora akaenda kwa OCID ili kupata ufafanuzi wa kilichotokea. Alipokelewa vizuri sana na OCID, ambaye alimueleza kila kitu juu ya kinachoendelea kuhusu shauri la mwanaye.
“Lakini nashindwa kuelewa ilikuwaje hadi Genesis akamuua mwanangu. Walikuwa wanapendana sana na ni Genesis mwenyewe ndiye aliyeamua kumuoa binti yangu. Unadhani ni rahisi kuamua uamuzi mbaya kama huo, tena siku ya harusi yao?”

“Hata sisi pia tunashangaa, lakini hilo halishangazi sana, Genesis mwenyewe anathibitisha kwamba ndiye aliyemuua Bianca. Hilo haliishii hapo pekee bali anatuhakikishia kwamba alifanya hivyo baada ya kupata taarifa kwamba mpenzi wake wa zamani Farida alibambikiziwa kesi ya madawa ya kulevya.”
“Na nani?”

“Mkeo na mama yake Genesis kwa kushirikiana na vijana ambao tayari tumeshawakamata.”
“Mungu wangu, hivi huwezi kufanya chochote kwa ajili ya mke wangu?”
“Hapana, hapana hili shauri gumu mno, lipo kimataifa na tayari Kamanda Mkuu wa Polisi (IGP), ameagiza suala hili tulihamishie Central kwani linalichafua taifa!”
“Kweli huwezi kufanya chochote?”

“Ni vigumu sana, labda utumie njia nyingine lakini kubwa zaidi nakushauri uende Central ukaongee na wakubwa zangu pengine wanaweza kukusikiliza!”
“Nitafanya hivyo!”

Dk. Rwegoshora akasimama bila kuaga akaondoka zake. Kichwani alikuwa na mawazo mengi sana, lakini kubwa alikuwa akifikiria kuhusu kumtoa mke wake katika aibu iliyokuwa ikimkabili.
***
Rais alikuwa amevimba kwenye kiti chake cha kunesanesa akiwa anafungua kila droo na kufunga bila kujua alikuwa akitafuta nini. Fax iliyokuwa mezani mwake kutoka nchini Saudi Arabia aliyoandikiwa na rais wa nchi hiyo ilimuogopesha.

Hakuwa tayari kupata aibu iliyokuwa mbele yake. Kwa Rais Julius Kambarage Nyerere kubebeshwa lawama ya mwananchi wake kuingiza madawa ya kulevya nchi za nje lilikuwa ni kosa kubwa sana.
Hakuwa na haja ya kumpigia sekretari wake ili amuunganishe na waziri wa mambo ya ndani, akainua mkonga wa simu uliyokuwa mezani kwake kisha akabonyeza namba za ofisi za Waziri wa Mambo ya Ndani, Slivanus Misiga kisha akatulia kwa sekunde kadhaa akisubiri majibu. Kitambo kidogo simu ikapokelewa.

“Naamini unatambua wajibu wako Misiga.”
“Ndiyo Mkuu!”
“Unajua kinachoendelea Saudi Arabia?”
“Ndiyo Mkuu!”
“Umechukua hatua gani?”
“Ahaa! Lipo ofisini kwa OCID wa Kinondoni.”
“Acha utani hamishia hili shauri Central haraka sana na uhakikishe unapata majibu yake mapema. Siwezi kukubaliana na aibu kubwa kama hii.”
“Nimekuelewa Mkuu!”
Wakakata simu zao.

Waziri Misiga alichanganyikiwa, tangu ameanza kuongoza wizara hiyo alikuwa hajawahi kupigiwa simu na rais akilalamika kama siku hiyo. Jambo hilo lilimchanganya kichwa chake na aliamua kulifuatilia kwa karibu zaidi.
***

Profesa Mshana alihisi kurukwa na akili baada ya kusikia mke wake amekamatwa, hilo halikuwa kubwa sana lakini alichanganyikiwa zaidi baada ya kusikia kwamba mwanaye Genesis naye yuko ndani na ndiye aliyetoa ushahidi kwamba Farida alisingiziwa kuhusu kesi ya madawa ya kulevya.

Kilichomchanganya zaidi ni juu ya mwanaye kukiri kwamba ndiye aliyemuua Bianca. Kukiri huko pekee kulitosha kabisa kumfanya Genesis ama anyongwe au kufungwa kifungo cha maisha jambo ambalo hakutamani kabisa litokee.
Kitu pekee kilichoingia kichwani mwake kwa kasi zaidi ilikuwa ni kumpigia simu Dk. Rwegoshora akiamini kwamba kwa kofia yake ya mwanasheria mkuu wa serikali pengine angeweza kulifunika suala hilo.
Hakujishauri zaidi akachukua simu yake kisha akaenda sehemu maalumu ya kuhifadhiwa majina, akabonyeza jina la Dk. Rwegoshora na kupeleka sikioni kusubiria majibu.

“Haloo!” Muda mfupi baadaye alisikia sauti upande wa pili, alikuwa ni Dk. Rwegoshora.
“Ndugu yangu sisi ni marafiki kwa muda mrefu sana, kwa sasa naomba tuachane na yote yaliyotokea tuangalie namna ya kuwaokoa hawa watu katika vyombo vya dola!”
“Watu gani?” Akauliza Dk. Rwegoshora akionekana kukejeli.
“Mke wangu, mkeo na mtoto!”
“Nani Genesis?”
“Ndiyo!”
“Huyo muuaji?”
“Usiseme hivyo!”
“Kumbe nisemeje?”

“Ahaaa.... unajua....” kabla hajamaliza sentensi yake tayari Dk. Rwegoshora alishamkatisha.
“Sikiliza wewe bwege, urafiki wetu hauna thamani kama ya mwanangu Bianca ambaye sasa anaozea mavumbini, hauna thamani kama mke wangu ambaye anateseka polisi.

Kwa taarifa yako kila mtu ahangaikie msalaba wake mwenyewe lakini angalia, kwa hili nitahakikisha sheria inachukua mkondo wake, naamini unanijua jinsi nilivyo makini na ninavyoweza kusimamia ninachokiamini, nitafanya hivyo!” Akasema Dk.

Rwegoshora kwa hasira.
“Haloo.... haloo... haloo...” alisema Profesa Mshana kabla muda mfupi baadaye kugundua kuwa alikuwa akiongea kwenye simu iliyokatwa!
“Mungu wangu!” Akasema Profesa Mshana kwa sauti kubwa huku kijasho chembamba kikianza kumchuruzika.

Hakujua angewezaje kuepukana na hatari iliyokuwa mbele yake.

Je, nini kitatokea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom