SEHEMU YA 15
Haraka anamfuata na kumrukia akimkumbatia kwa furaha sana. Wakati tendo hilo linafanyika, Bianca alikuwa akiwaangalia kwa hasira huku ndani ya nafsi yake kukiendelea kuwa na nia ya kuhakikisha anasambaratisha penzi lao. Hilo linaendelea kuwa siri iliyojificha katikati ya moyo wa Bianca pekee, lakini alijiapiza kuhakikisha kwamba yeye anakuwa mke wa Genesis!
Je, nini kitatokea? Nini mwisho wa mpambano huu wa mapenzi? SONGA NAYO...
“HAKUNA anayekutaka katika familia yao, kwanini unajipendekeza? Kwanini usitafute mafukara wenzako? Watu wengine bwana, sijui wameumbwaje? Unajifanya mzuri, mzuri utakuwa wewe? Hata kama ni kweli mzuri, lakini uwe na pesa sasa, siyo uzuri wa bure, unanuka shida mpaka kwenye nywele,” Bianca aliendelea kumimina maneno makali ya kashfa ndani kwa ndani!
Kama maneno hayo angeyasema kwa sauti kubwa na Farida akasikia, hali ingekuwa mbaya sana, maana yalikuwa maneno ya kashfa na dharau kubwa sana kwa Farida. Aliendelea kuwakazia macho wakiwa wamekumbatiana, moyo wake ukamuuma sana.
“Lakini hata hivyo wameshachelewa, kwa muda uliobaki, ni muujiza tu, utokee ndiyo utamfanya Farida afaulu, lakini nina uhakika huyu lazima afeli, hawezi kwenda Chuo Kikuu huyu! Kikubwa akamsaidie mama yake kuosha vyombo,” kashfa zinazidi kumtoka kichwani mwake Bianca.
Kama angekuwa na uwezo wa kumuua, angefanya hivyo ndani ya sekunde chache sana, kwake Farida alikuwa sawa na kichefuchefu! Alimchukia sana na alimwona kama nuksi katika maisha yake. Yeye ndiye alikuwa kikwazo cha Genesis kukataa kuwa naye!
“Shiiit, lakini bado nina kitu cha kufanya, siwezi kuwaacha muendelee kuwa wapenzi. Mimi ndiye Bianca, mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wakwe zangu ni wahadhiri wakubwa nchini! Si li-Farida lisilo na mbele wala nyuma,” aliendelea kuwaza huku akiwa ameuma meno kwa hasira.
Farida na Genesis wakawa wamejisahau kabisa, hawakukumbuka kama wapo shule, waliendelea kukumbatiana hadi dakika mbili baadaye walipoachiana. Walikuwa wamezama kwenye dimbwi zito la bahari ya mapenzi. Farida alikuwa amelowana uso mzima kwa machozi ya furaha. Kwake Genesis alikuwa kila kitu katika maisha yake.
Alikuwa mwanaume wa maisha yake, hakutamani wala kusikia kuwa na mwanaume mwingine yeyote zaidi yake. Kurudiana naye kwa mara nyingine, alihisi moyo wake kuingiwa na ubaridi mkali, furaha ya ajabu ikabubujika ndani kwa ndani akiwa na amani ya moyo!
“Hongereni mwaya, Farida acha kusikiliza maneno ya watu, Genesis ni wako, acha presha!”
“Ahsante sana Bianca kwa ushauri wako!” Farida akasema.
“Siyo ahsante pekee, ni lazima uniahidi kulifanyia kazi!”
“Nakuahidi Bianca!”
“Nina jambo lingine!”
“Lipi tena Bianca rafiki yangu, niambie tu nakusikiliza, sisi sasa ni marafiki wa kweli!”
“Kwanza batilisha kauli yako, mimi si rafiki yako!”
“Kumbe nani?”
“Mimi ni wifi yako, kumbuka Genesis ni kaka yangu, kwahiyo mimi nabaki kuwa wifi yako na wewe pia.”
“Oooh! Jamani ahsante sana Bianca, nimefurahi kusikia hivyo wifi yangu! Enhee kuna jambo ulikuwa unataka kuniambia, ni nini hicho?’
“Ni kuhusu masomo, unashuka sana siku hizi, najua sababu ni Genesis, sasa achana na mawazo, nimeshakuhakikishia kwamba sina uhusiano naye, basi unatakiwa kuhamishia akili yako kwenye masomo, sawa wifi yangu?”
“Nimekuelewa vema.”
“Kaka Genesiss, kuwa makini na wanafiki, utakuja kumpoteza mpenzi wako bure!”
“Yaani acha tu Bianca, nachanganyikiwa sana mimi, siwezi kuishi bila Farida wangu. Nipo tayari kupoteza kila kitu lakini si Farida wangu, huyu ni mwanamke wangu, nampenda sana na natamani sana aendelee kuwa wangu milele yote. Naamini nikiishi naye, furaha yangu itakuwa ya kipekee!”
“Ni kweli kabisa.”
“Bianca nakushukuru kwa kila kitu, bila shaka utakuwa mshauri wangu namba moja kuanzia sasa!”
“Bila shaka Farida!”
“Sasa jamani?!” Genesis akasema.
“Nini?”
“Muda, hebu tuondokeni tukajisomee, hatuna muda wa kupoteza tena.
“Poa,” Bianca akaitika.
Wote wakatawanyika wakiwa na furaha ya ajabu mioyoni mwao. Ni Bianca pekee ndiye alikuwa na furaha ya kinafiki, kwa nje alionekana kuwa na furaha lakini ndani ya moyo wake kulikuwa na vitu tofauti kabisa. Alimchukia Farida kuliko kitu kingine chochote duniani.
Bado alikuwa kwenye mapambano. Hakutakiwa kumpa nafasi Farida aongeze juhudi kwenye masomo yake, anamfahamu vizuri sana Farida, anajua kichwa chake kilivyo chepesi kunasa mambo, kwahiyo kama angelegeza uzi kidogo tu, Farida angepanda kimasomo na mwisho wa siku angempoteza Genesis. Jambo hilo hakutarajia litokee akiwa hai, huenda lingetokea, lakini akiwa ndani ya jeneza!
***
Zilibaki siku saba tu, kabla ya kuanza kwa mitihani ya kidato cha sita, bado Genesis alikuwa na wasiwasi sana na Farida, hakuamini kama kweli alikuwa ameshajisomea vya kutosha kuweza kumudu kufanya mitihani.
Jambo hilo lilimuumiza sana, kwani Farida alitumia muda mwingi zaidi kumfikiria yeye kuliko masomo na hivyo kuharibu mustakabali mzima wa masomo yake. Alikuwa ana mawazo sana, akiwa amejilaza chini ya mti jioni hiyo akijiandaa kuanza kufanya mazoezi.
Akiwa katika hali ya mawazo, simu yake ya mkononi ndiyo iliyomnasua! Alipotupa macho kwenye kioo, akakutana na jina ‘Ma Mumy’, alikuwa ni mama yake mzazi anampigia. Mara moja akabonyeza kitufe cha kupokea na kupeleka simu sikioni mwake.
“Shikamoo mama,” ndiyo neno la kwanza kutamka baada ya kupokea simu.
“Mar-haba mwanangu, habari za masomo?”
“Nzuri mama, za hapo nyumbani?”
“Huku ni nzuri kabisa, lakini nilipenda kufahamu maendeleo yako, maana bado wiki moja, uanze mitihani yako!”
“Nipo sawa mama, naamini unanifahamu vizuri, nyie anzeni kunitafutia vyuo vya nje mama, najua nitafanya vizuri mama’ngu!”
“Basi, ni vema kama ndivyo, nilitaka kusahau, vipi kuhusu mwenzako, kuna matumaini?”
“Nani Farida mama?”
“Ndiyo, kwani una mwenzako gani tena zaidi yake?”
“Aaaaah kuhusu Farida mamaaaa....unajua alikuwa na matatizo kidogo hapa katikati, kwahiyo ninachoweza kusema mama ni kwamba...” Genesis hakuweza kuongea kinachoeleweka, alibaki kujiuma-uma bila kuongea chochote cha maana.
“Naaminisha anaweza kufanya vizuri kwenye mitihani yake?” Mama yake akamkatisha.
“Bila shaka mama,” akajibu haraka, lakini moyoni mwake alikuwa na mawazo sana.
“Sawa, Mungu awatangulie, nilitaka kufahamu hilo tu!”
“Ahsante mama, jioni njema, msalimie sana baba!”
“Namba yake unayo!”
“Lakini nataka hizi salamu uzifikishe wewe mama, kwani ni vibaya?”
“Haya mwanangu usijali nitamwambia unamsalimia na wewe pia msalimie Farida na dada yako Bianca!”
“Zimefika!”
Genesis aliitoa simu sikioni kama vile anashusha mzigo mzito kichwani, alikuwa hana amani kabisa. Simu ya mama yake ilimchanganya sana. Alijua ni kiasi gani alikuwa katika mtihani wake wa mwisho wa kumpata Farida, kama angefeli ni wazi kwamba asingeweza kupata nafasi ya kuwa naye tena katika maisha yake, jambo ambalo hakutaka kabisa kuliruhusu litokee.
Bila kutarajia, machozi yakaanza kumiminika machoni mwake kama maji, alikuwa na uchungu mwingi sana.
***
Ilikuwa Jumatatu saa 2:30 Asubuhi, wanafunzi wote wa kidato cha sita, nchi nzima walikuwa wanaanza kufanya mitihani yao ya mwisho. Miongoni mwao alikuwa Farida, ambaye kwake mtihani huo ulikuwa zaidi ya kipimo cha maarifa yake, alikuwa akifanya mtihani wa mwisho utakaoamua au kupinga kuendelea kuwa katika uhusiano na Genesis.
Aliketi kwenye kiti chake ndani ya chumba cha mtihani akiwa na mawazo tele kichwani, mtihani wa kwanza ukiwa ni Biology - Paper One (Baiolojia - Mtihani wa Kwanza). Kama yalivyo maelekezo katika katatasi yake ya maswali, yaliyomtaka kusoma maswali yote kwanza kwa makini kabla ya kuanza kuyajibu, alifanya hivyo!
Alihisi kutetemeka mwili mzima, maswali mengi yalikuwa ni yale aliyoyafahamu vizuri, lakini alishasahau kabisa jinsi ya kuyajibu! Kabla ya kuanza kufanya ule mtihani, tayari alishajua amepoteza asilimia sabini! Hiyo ilikuwa na maana kwamba, kama angefanya maswali yale aliyoyafahamu vema alikuwa na uhakika wa kupata asimilia thelathini ambayo ingekuwa daraja S, kama angepata chini ya asilimia ishirini na tano, ilikuwa na maana kwamba angepata F, matokeo ambayo kwa hakika yalikuwa mabaya!
Ulikuwa mwanzo mbaya wa kuharibu kwanza maisha yake, lakini pili na muhimu zaidi kwake kwa wakati huo ni MPENZI WAKE GENESIS! Farida akajikuta akianza kulia. Alianza kwa sauti ya chini, lakini baadaye akazidisha kilio, msimamizi wa mtihani akamfuata haraka!
“Una nini binti?” Akamwuliza kwa mshangao.
NDOTO zake zote zilikuwa zinaelekea ukingoni, kila kitu kilikuwa kinakwenda kuharibika. Mtihani ule wa kwanza, ulikuwa kielelezo tosha kwamba, hata mingine iliyokuwa imesalia, angefanya vibaya sana.
Msimamizi wa mtihani aliyekuwa amesimama mbele yake, ni kama alikuwa hajamuona, alihisi moyo wake kwenda mbio na taswira za kufanya vibaya zikiwa wazi kabisa. Wakati ule hakuwaza sana kuhusu kufeli maisha yake, aliwaza zaidi juu ya Genesis wake, maana tayari alishapewa taarifa kwamba ili wazazi wake wamkubali angalau apate nafasi ya kuendelea na elimu ya chuo kikuu, ambapo angalau angeambulia shahada ya kwanza ambayo kwa familia ya Genesis, wangeona afadhali!
“Binti, una matatizo gani?” yule msimamizi aliendelea kumuuliza, lakini Farida hakujibu kitu.
“Binti si nazungumza na wewe!”
“Enheee...” Farida akashtuka mawazoni baada ya msimamizi yule kumgusa begani.”
“Una nini?”
“Nipo sawa!”
“Mbona unalia?”
“Kichwa kinaniuma sana, nahisi kama kinauma upande mmoja.”
“Pole sana, hebu subiri nifanye mawasiliano na watu wa huduma ya kwanza!”
“Hapana sina hali mbaya sana, nikipata hata maji nikajimwagia kichwani, nitakuwa sawa.”
“Sawa, lakini wanaoweza kukusaidia ni hao watu wa huduma ya kwanza, umesahau kwamba unafanya mtihani wa taifa?”
“Najua!”
“Au kuna ujanja unataka kufanya?”
“Ujanja? Hapana!”
“Basi subiri kwanza, nifanye nao mawasiliano watakuja kukuchukua. Kila kitu utafanya chini ya uangalizi wao, lakini jitahidi kwenda na muda, maana muda wa kumaliza mtihani unazidi kusogea.”
“Nimekuelewa vizuri.”
Mara moja yule msimamizi akafanya mawasiliano na watu wa Huduma ya Kwanza ambao walifika mapema sana na kumchukua Farida.
“Pole sana binti, usijali utakuwa sawa!”
“Ahsante!”
Wakaongozana naye hadi kwenye chumba maalum kilichoandaliwa kwa ajili ya utolewaji wa huduma ya kwanza, akapewa maji ya kunywa, akanywa kisha akapewa na dawa za kutuliza maumivu na kukandwa kwa maji ya baridi kwa ajili ya kupunguza joto ambalo mwenyewe alisema alikuwa akihisi kichwani mwake.
Baada ya dakika kumi na tano, Farida alirudishwa kwenye chumba cha mtihani akiwa ana nafuu kidogo. Muda ulikuwa unazidi kusonga mbele, hivyo aliketi kwenye kiti chake na kuanza kujibu maswali aliyokuwa na uhakika wa kuyapata kwanza.
Baada ya hapo, Farida akaanza kupambana na maswali mengine magumu, ambayo kwa asilimia kubwa hakuwa na uhakika wa kuyapata. Muda wa kumalizika mtihani ulifika, kengele ikalia na wanafunzi wakaanza kutoka nje. Farida alikuwa na uso uliokunjamana maana hakuwa na matumaini ya kufanya ule mtihani vizuri.
***
Jioni, Farida alikutana na Genesis kwenye mgahawa wa shule. Uso wa Genesis ulionekana kuwa na furaha sana, lakini Farida alikuwa na mawazo sana. Hilo Genesis hakuweza kulifahamu mara moja.
“Niambie mpenzi wangu, naamini mtihani wa leo utakuwa umefanya vizuri, umekuja kama vile tumetungiwa na walimu wetu. Ulikuwa mwepesi sana, naamini kama huna A pale basi B safi inapatikana!” Genesis akamwambia Farida akitabasamu.
“Genesis!” Farida akaita kwa huzuni.
“Bee!”
“Ule ni mtihani mwepesi?”
“Hakika, pale najua nina A yangu safi kabisa!”
“Genesis!!!”
“Kwani vipi?”
“Pale nategemea S au F!”
“Usiseme hivyo mpenzi wangu, lazima ujipe moyo, achana na kauli za kujikatisha tamaa!”
“Siyo kujikatisha tamaa Genesis, mimi ndiyo nimefanya huo mtihani, najua nitakachokipata!”
“Matokeo hayatabiriki!”
“Mbona wewe umejitabiria A?”
“Kwa sababu niliufanya vizuri na ninaamini nitapata alama hiyo kutokana na jinsi mtihani ulivyokuja.”
“Hata kwangu pia ni vivyo hivyo, naona ugumu wake ndiyo maana natabiri matokeo hayo.”
“Lakini umeshasau sharti walilotoa wazazi wangu juu ya penzi letu?”
“Najua ndiyo maana nahuzunika.”
“Sikiliza, acha paniki, mitihani mingine bado inakuja. Jitahidi kutulia, unaweza kufanya vyema na kupata nafasi ya kuendelea na chuo. Isitoshe Farida, kichwa chako nakifahamu vizuri sana, kwa nini ufeli?”
“Kwani napenda Genesis? Ni jinsi mtihani wenyewe ulivyo!”
“Nakuomba kwa sasa utulie, acha kuwa na mawazo ili uweze kufanya vizuri katika mitihani iliyobakia!”
“Nitajitahidi mpenzi wangu.”
Wakaagana.
***
Kila Farida alipokuwa akitoka kwenye chumba cha mtihani alionekana kuwa na mawazo mengi sana, hakuwa na matumaini kabisa ya kufanya vizuri. Mpaka anamaliza mitihani yote, matumaini yake yalikuwa kidogo sana.
Alikuwa na huzuni kubwa sana moyoni mwake, si kwa sababu anakwenda kufeli mitihani yake, lakini kwa sababu anakwenda kumkosa mpenzi wake ambaye alimpenda kwa moyo wake wote. Hilo ndilo lilikuwa tatizo kubwa zaidi kwa Farida.
Baada ya kumaliza mitihani yao, wanafunzi wote wa kidato cha sita walirejea majumbani mwao! Tayari walikuwa wameshamaliza elimu ya kidato cha sita. Shule ya St. Thomas ilisifika kwa ufundishaji mzuri, hivyo asilimia kubwa ya wanafunzi walirudi majumbani mwao, sura zao zikiwa zimejaa tabasamu, maana walikuwa na uhakika wa kufanya vizuri na kusonga mbele katika elimu ya chuo kikuu.
Farida hakuwa na amani kabisa, matumaini yake yalikuwa hafifu sana, alijua kwa vyovyote vile, isingekuwa rahisi kufaulu, kutokana na jinsi alivyojibu maswali yale. Alipokelewa nyumbani kwao Mtoni Kwa Aziz-Ali, jijini Dar es Salaam kama shujaa aliyetoka vitani, matumaini ya wazazi wake yakiwa makubwa sana.
“Tunaamini mwanetu, utakuwa umefanya vizuri mitihani yako. Wewe ndiyo mkombozi wa familia hii, Mungu amekuchagua ili uje utusaidie, ni imani yetu kwamba utafaulu,” alikuwa baba yake mzazi, akimwambia Farida wakati akiingia sebuleni ya nyumba yao chakavu ya kupanga.
“Pole mama, karibu sana, karibu sana mama,” mama yake naye alidakia akichukua begi lake na kuliingiza chumbani.
“Enhee za masomo?” baba yake akauliza.
Farida hakujibu kitu zaidi ya kubaki anamkodolea macho baba yake. Baba yake akashangaa sana, alishindwa kuelewa sababu ya mwanaye kukosa furaha kiasi kile.
“Mbona upo kimya?” baba yake alimwuliza, lakini Farida hakujibu.
“Kuna tatizo?” baba yake akauliza tena lakini pia aliendelea kubaki kimya.
Mama yake akatoka chumbani alipokuwa amekwenda kuhifadhi begi, uso wake ukionekana kupambwa na tabasamu pana, lakini alipowapiga macho mume wake na mwanaye, akaona huzuni zimewatawala.
“Baba Farida, kuna nini?” mama akauliza, lakini hakujibiwa.
“Mbona mnanichanganya? Farida nini kinaendelea?” mama akamwuliza mwanaye.
Mara ghafla macho ya Farida yakazungukwa na machozi, ni baada ya taswira ya Genesis wake kuonekana mbele yake huku matumaini ya kumpata yakizidi kufifia! Hapakuwa na mwanaume mwingine duniani ambaye angekuwa na hadhi ya kuishi naye zaidi ya Genesis!
Ni mwanaume huyo pekee ndiye aliyepanga kumpa zawadi ya usichana wake, ambayo aliitunza kwa muda mrefu sana kwa ajili ya mumewe. Mawazo hayo yakasababisha Farida azidishe kilio chake kwa sauti ya juu! Bila kujua kilichokuwa kikimliza mwanaye, mama yake naye akaanza kulia.
NA MALIZIA PART MOJA KWAJILI JANA TULIKOSA
KULIKUWA na kila dalili za tatizo kubwa katika familia yao, kama watu wangepita nje na kusikia sauti zile za kilio, wangejua lazima kulikuwa na msiba au taarifa mbaya katika familia hiyo! Farida alikuwa analia kwa uchungu maana alijua wazi kwamba angefeli mitihani yake, lakini mama yake alijikuta akilia kwa huruma ya mwanaye!
Farida alijua jinsi wazazi wake walivyomtegemea, alifahamu vyema jinsi ambavyo walimchukulia kama kila kitu kwao, tegemeo la familia nzima ya kimasikini. Aliumizwa na mapokezi ya wazazi wake, ni mapokezi ambayo kwake yeye aliona kama hastahili kabisa kupewa!
Tayari alikuwa na uhakika na majibu mabaya ya mitihani yake, kwa nini apewe heshima kubwa kiasi kile? Aheshimiwe kiasi kile? Hakika hakutaka kupongezwa maana alijua kwamba tayari alishaharibu! Pongezi zile zilikuwa ni kumzidishia maumivu zaidi moyoni mwake.
Kufeli mitihani yake kungeweza kuwa jambo la kawaida, kama Genesis angeendelea kuwa wake, lakini tafsiri ya yeye kufanya vibaya ni kwamba, kwanza alipoteza mustakabali wa maisha yake, lakini pia alimpoteza mpenzi wa moyo wake, mwanaume ambaye alimpa hifadhi ndani ya moyo wake; Genesis!
Baba alibaki anawashangaa wote mama na mwana wanavyolia kwa uchungu bila kufahamu sababu.
“Mama Farida, mbona sikuelewi, kuna nini?”
“Huoni mtoto analia,” mama Farida alisema akiendelea kuangua kilio.
“Kwa hiyo mtoto akilia na wewe unalia bila hata kujua sababu.”
“Sababu sio muhimu sana mume wangu, midhali mtoto analia, maana yake ni kwamba ana matatizo, kama unavyojua, matatizo ya mtoto ni yetu wote, ndiyo maana unaona nalia.”
“Acha ujinga, hebu zungumza na mwanao umwulize tatizo ni nini sio kuungana naye kwenye kulia, bila kujua tatizo!” baba akamwambia mkewe.
“Sawa.”
“Tatizo ni nini mwanangu?” mama Farida akamwuliza mwanaye.
“Mitihani mama!”
“Ilikuwaje?”
“Mama karibu yote, sijafanya vizuri.”
“Kwa nini?” baba yake akadakia.
“Nilikuwa sijisikii vizuri, kizunguzungu kilikuwa kinanisumbua karibu siku zote nilizokuwa nafanya mitihani yangu, nashindwa kuelewa baba.”
“Kwa hiyo hakuna mategemeo tena?” baba yake akauliza akionekana kukata tamaa kabisa.
“Yapo, lakini...”
“Lakini nini mwanangu? Inaonekana uliacha kilichokupeleka na kuanza kufanya ujinga. Kwa nini unasema lakini!” baba yake akauliza kwa ukali kidogo.
Ni mtoto huyo ndiye alikuwa tegemeo lao la kuokoa familia yao, kitendo cha kuanza kusita juu ya matokeo yake, kilimnyima raha kabisa.
“Baba nilikuwa nasoma sana, lakini nashindwa kuelewa, sijui kwa nini mtihani ulikuwa mgumu kiasi kile, lakini hata ile hali ya kizunguzungu ilinichanganya pia baba, lakini mimi naomba tumuombe Mungu, tutulie mpaka matokeo yatakapotoka, unaweza kutokea muujiza.”
“Hakuna muujiza katika kitu ulichokifanya mwenyewe mwanangu, kama ulifanya madudu hayawezi kubadilika na kama ulifanya vizuri itakuwa hivyo,” baba yake akasema.
“Ndiyo maana nasema tusubiri matokeo yakitoka ukweli utajulikana, ingawa mimi naamini lolote linaweza kutokea,” Farida akasema kwa unyonge.
Furaha ya wazazi wake ikayeyuka ghafla, walimwamini sana mtoto wao, lakini majibu aliyokuja nayo, yaliwasononesha sana, matumaini yao yote kuwa angekuwa mkombozi wa familia, yakayeyuka kama barafu!
***
Gari la kifahari aina ya Toyota VX lilikuwa likiingia katika geti jeusi, kwenye nyumba kubwa nzuri ya kuvutia, eneo la Masaki, jijini Dar es Salaam. Alikuwa ni Genesis anarejea nyumbani akitokea Morogoro baada ya kuhitimu elimu ya kidato cha sita akiwa na dereva ambaye alikwenda kumchukua shuleni.
Baada ya gari kuingia, Genesis alishuka na kuanza kutembea taratibu kufuata lango la kuingia sebuleni. Kazi ya kushusha mizigo yake aliiacha kwa dereva ambaye alijua kazi yake ipasavyo. Sebuleni akakutana na sura za wazazi wake zikiwa zimepambwa kwa tabasamu mwanana.
“Karibu nyumbani mwanetu, bila shaka mambo yalikwenda vizuri,” Profesa Mshana, baba wa Genesis alisema akitabasamu.
“Baba...hata salamu?!”
“Karibu nyumbani,” mama yake naye akasema.
“Ahsanteni sana wazee wangu. Shikamooni,” akasalimia Genesis akiachia tabasamu usoni mwake.
“Mar-haba!” Wote wakaitikia kwa pamoja.
“Naamini njia ya kwenda chuoni umeitengeneza,” Profesa Mshana akasema.
“Bila shaka baba.”
“Vizuri sana mwanangu, vipi lakini mitihani yako?” mama naye akaongeza.
“Matarajio ni makubwa sana mama, naamini nitafanya vizuri.”
“Vipi mwenzako?” mama yake akauliza kwa sauti ya utulivu sana.
“Aaah! Chris naye atafanya vizuri, nilizungumza naye. Kwa ujumla matumaini ni makubwa karibu kwa wanafunzi wote, mtihani haukuja vibaya sana.”
“Sizungumzii Chris!”
“Kumbe nani mama?”
“Mwenzako Farida.”
“Naye atafanya vizuri!” akasema Genesis kwa kujiamini.
Ndani ya moyo wake hakuwa na matumaini makubwa ya Farida kufaulu, lakini aliamua kusema hivyo kwa nia ya kujiridhisha yeye mwenyewe! Farida hakuwa na uhakika wa kufaulu, lakini alitaka kuwanyamazisha wazazi wake.
Jibu lake liliubadilisha kabisa uso wa mama yake, ambaye alionekana kuanza kuwa na mawazo kidogo. Ni kama hakupenda kusikia kauli hiyo ya mwanaye.
“Umesema Farida...” baba yake akauliza tena.
“...Atafanya vizuri baba, naye nilizungumza naye baada ya mitihani yake.”
“Sawa, nadhani unafahamu kwamba huo ndiyo mtihani wake wa mwisho, huo utaamua kwamba atakuwa na wewe au lah!”
“Najua baba, ndiyo maana nilimwambia ajitahidi kusoma kwa nguvu.”
“Sawa basi nenda chumbani ukabadili nguo upumzike; karibu sana nyumbani Genesis,” baba yake akasema akilazimisha tabasamu usoni lakini ndani ya nafsi yake alikuwa amechukia sana.
Genesis akaondoka taratibu akielekea kwenye korido kuingia chumbani mwake. Alipoingia tu kwenye korido, Profesa Mshana akamgeukia mke wake haraka na kumwuliza.
“Kwa hiyo Bianca alikudanganya?” akauliza kwa hadhari na sauti ya taratibu kabisa.
“Sijui...sasa nini cha kufanya?”
“Hakuna cha sasa, kifupi Genesis anatakiwa kumuoa Bianca na si vinginevyo. Huyo Farida afaulu asifaulu, lakini lazima uamuzi wetu uwe huo!” akasema Profesa Mshana kwa sauti yake kali ya kumaanisha.
“Kweli?”
“Ndiyo hivyo!”
“Sasa tutafanyaje?”
“Nitajua cha kufanya, lakini awali ya yote nadhani mpigie Bianca aje nyumbani Jumamosi ijayo, tuzungumze naye kwanza kabla ya kuingia katika hatua ya pili. Sitaki matatizo katika familia yangu, sitaki mikosi ya kimasikini hapa,” akasema Profesa Mshana kwa hasira akisimama na kwenda zake chumbani.
Muda huohuo mama Genesis, akachua simu yake na kumpigia Bianca.
“Vipi mama za shule?” akasema baada ya Bianca kupokea.
“Salama, shikamoo mama.”
“Mar-haba mwanangu, pole na mitihani!”
“Nimeshapoa mama.”
“Vipi kuna matumaini?”
“Makubwa sana mama.”
“Vipi kazi uliyokuwa unaifanya, nayo ina matumaini ya ushindi?”
“Ipi mama?”
“Farida.”
“Unanijua vizuri sana mama, hiyo nimeishughulikia safi sana na imekwenda vizuri kuliko kawaida.”
“Kweli?”
“Niamini mama.”
“Nakuamini mwanangu... sasa Jumamosi tulitaka uje hapa nyumbani, tunahitaji kuzungumza na wewe kidogo.”
“Sawa mama.”
“Haya, siku njema, tutaonana Jumamosi.”
“Usijali mama, nawe pia!”
“Ok! Wasalimie wazee hapo nyumbani.”
“Sawa mama, lakini sijawakuta, wote wamekwenda kazini.”
“Wakirudi!”
“Sawa mama.”
Wakakata simu zao. Sekunde mbili tu baada ya mama Genesis kukata simu, mara Genesis akafungua ghafla mlango wa kioo, unaotokea kwenye korido za kuingia vyumbani. Alipofungua alisimama kama mlingoti mlangoni akimwangalia mama yake kwa jicho la hasira.
Ni wazi kwamba kuna kitu kibaya kilichokuwa kikiendelea ambacho hakukipenda. Ilionekana wazi kuwa alikuwa akifuatilia kwa makini mazungumzo ya mama yake na Bianca kwenye simu.
“Una nini?” mama yake akamwuliza, lakini Genesis hakujibu.
Aliendelea kumwangalia mama yake kwa jicho la hasira, akionekana kuanza kulengwalengwa na machozi.
“Kwa nini mama mnanichagulia maisha yangu? Kwa nini?” Genesis akafungua kinywa na kuuliza kwa hasira sana.
Mama yake hakujibu, alibaki kumwangalia akiwa haamini kama maneno yale yalitoka kinywani mwa mwanaye, kwa mara ya kwanza alishuhudia Genesis akimkaripia! Wakabaki wametoleana macho. Haikuwa rahisi kuamini kwamba walikuwa mama na mwana!
Je, nini kitatokea?