DuaZaMama
JF-Expert Member
- Jun 2, 2025
- 1,882
- 4,129
Soma, Pia: Waziri Mkuu, Majaliwa atangaza kugombea tena Ubunge wa Ruangwa akiaga Bunge
Vyanzo vyetu vya habari kutoka kwa wandani wa Waziri Mkuu Majaliwa vimeieleza Jambo TV kuwa, akiwa jimboni kwake Ruangwa kwa siku kadhaa za mashauriano na wananchi na wazee wa eneo hilo, Majaliwa amefikia uamuzi huo baada ya tafakari ya kina na ushauri wa wadau mbalimbali na amewashukuru Wanaruangwa kwa kipindi chote cha miaka 15 ya kumpa ubunge na kuwawakilisha vyema.
Hatua hiyo imekuja siku chache tu baada ya Majaliwa kutangaza Bungeni, Juni 26, 2025, kuwa anapanga kugombea tena ubunge wa jimbo hilo, akisisitiza kuwa anaendelea kuhitaji ridhaa ya wananchi. Hata hivyo, kauli hiyo sasa imebadilika rasmi.
"Ninatambua wakati mwingi nimekuwa nje ya jimbo nikilitumikia taifa lakini wana Ruangwa wameendelea kuniunga mkono. Nitumie nafasi hii kusema asanteni sana na ninamuomba Mwenyezimungu azidi kuimarisha mshikamano uliopo kati yetu sote. Ninaomba kuwajulisha kuwa ninakuja kuchukua fomu ya kuomba ridhaa yenu tena.", alinukuliwa bungeni.
Uamuzi wa Majaliwa umepokelewa kwa hisia tofauti, huku baadhi ya wachambuzi wa siasa wakiutaja kuwa ni uamuzi wa busara na wa kiungwana, hasa baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka 10 cha Uwaziri Mkuu tangu alipoteuliwa mwaka 2015.
Hatua hii pia inakuja wakati chama chake, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kikiwa katika harakati za ndani za uteuzi wa wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025. Zoezi hilo limeanza Juni 28 na linatarajiwa kukamilika Julai 2, 2025.
=============================
WAZIRI MKUU, na Mbunge wa Jimbo la Ruangwa Kassim Majaliwa leo Julai 2, 2025 ametangaza rasmi kutokugombea tena ubunge wa jimbo la Ruangwa baada ya kulitumikia jimbo hilo kwa miaka 15.
Akizungumza na wajumbe wa kamati ya Siasa ya Mkoa na Wilaya ya Ruangwa Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kuwashukuru wananchi kwa kumuunga mkono wakati wote ambao amekuwa mbunge wa jimbo hilo.
"Imefika wakati kwa mshikamano tulioujenga sasa ni wakati wa kutoa fursa kwa Wana-Ruangwa wengine wapenda maendeleo waweze kuunganisha nguvu hizi ili Kauli mbiu yetu ya Ruangwa kwa maendeleo inawezekana iweze kusonga mbele zaidi."
Aidha, ametoa wito wajumbe wa kamati ya siasa ya Wilaya kuwapa ushirikiano wagombea wote wenye nia ya kugombea ubunge wa jimbo hilo.
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amewasihi Wana-Ruangwa kuendelea kushikamana na itakapofika siku ya uchaguzi waweze kuchagua wagombea wote watakaowakilisha chama cha Mapinduzi kwenye uchaguzi huo.
"viongozi wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mgombea Mwenza Dkt. Nchimbi watakapokuja tujitokeze kwa wingi kwenye mikutano tusikilize sera, lakini siku ya kupiga kura tuwapigie kura nyingi za kutosha."
Aidha, amemshukuru Rais Dkt. Samia Viongozi wakuu wa chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kumuamini na kumpa fursa ya kuwatumikia wana Ruangwa.
Mheshimwa Majaliwa alichaguliwa kuwa mbunge wa jimbo la Ruangwa mwaka 2010 na amehudumu kwa kipindi cha miaka 15.