Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,478
- 39,997
JAMBO lililomkuta Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Jumanne iliyopita, linatosha kabisa kumfukuzisha kazi Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo kwa uzembe na kutokuwajibika. Na kama angekuwa muungwana, yeye mwenyewe angeamua kuvua nembo ya Jeshi letu la Polisi na kuiweka pembeni.
Jaji Bethuel Mmila alijikuta ameibiwa kompyuta ya kubeba (laptop) na zaidi ya yote kujikuta akielekezwa mtutu wa bunduki na jambazi nyumbani kwake ambaye alimtishia kumuua hapo hapo kama angefanya lolote.
Habari hizi zinasikitisha kuwa hazijapata sauti ya kutosha wiki iliyopita kutoka kwa wanasiasa na viongozi wetu kana kwamba tunaishi Baghdad! Inasikitisha uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walikuwa katika ubinafsi wao na mikutano yao na hakuna hata mmoja wao aliyeshtushwa na jambo hilo. Sitashangaa hawakuwa na taarifa hizo kwani wao walikuwa wanawaza; Nape, Nape, Nape!
Jaji huyo anasimulia katika gazeti moja la Kiswahili kuwa hayo yote yalitokea licha ya kuwa anatakiwa kuwa na maafisa wa Polisi kumpatia ulinzi nyumbani kwake.
Jaji huyo amesema kuwa baada ya kuona kuwa kompyuta yake ambayo iko karibu na dirisha imetoweka na dirisha likiwa wazi. Alipotoka kuwatafuta maofisa wa polisi wawili wanaotakiwa kumpa ulinzi, hakukuwa na mtu. Alipokwenda kwenye nyumba ya msaidizi wake wa nyumbani, naye hakuwapo.
Ni hapo ndipo alipojikuta anaambiwa na mtu aliyekuwa na silaha na aliyejificha uso kuwa; ukithubutu kufanya lolote nitakushuti mara moja. Mtu hyo akamuelekeza arudi ndani ya nyumba yake.
Baada ya kujifungia chumbani, Jaji huyo alijaribu kupiga simu polisi Arusha kutoa tahadhari bila kuitikiwa na akajaribu polisi Moshi bila kuitikiwa. Inashangaza kuwa hadi hivi sasa si makamanda wa mikoa hiyo au kutoka makao makuu waliojitokeza kusema lolote na kuwahakikishia majaji wetu kuwa maisha yao yako salama.
Kwa watu wengine kitendo hicho kinaweza kuwa ni ujambazi wa kawaida, lakini kwa mzee wenu hapa naamini kuwa ni mstari wa hatari sana unaoanza kuvukwa. Inapotokea majambazi wanafika hadi kwa majaji na kufanya kweli na wale waliotakiwa kutoa ulinzi wanajiumauma meno hakuna kitu kingine cha kuwaamsha isipokuwa kuwawajibisha.
Kama Lowassa aliweza kuwajibika kwa makosa yake ya kutowajibika kusimamia walio chini yake ipasavyo (si kwa sababu za kisiasa kama Waziri Mkuu alivyojaribu kutuzuga hivi juzi), basi Kamanda huyu wa Arusha pamoja na maofisa waliohusika kutoa ulinzi ni lazima wawajibishwe mara moja.
Tukifumbia macho tukio hili na kulichukulia kama kawaida, tunafungua mlango wa hatari kubwa sana nchini. Hofu yangu si tu tukio hilo la ujambazi, lakini kilicho nyuma yake - ni kitu gani kilisukuma mtu kwenda kumpora Jaji kompyuta?
Je, yawezekana Jaji Mmila alikuwa anasikiliza kesi fulani au kupanga kutoa hukumu juu ya mtu fulani ambaye hajafurahishwa na mwenendo wa kesi? Je, yawezekana Jaji Mmila ametumiwa kutuma ujumbe kwa majaji wengine ambao watakuwa tayari kusikiliza kesi za mafisadi nchini? Hivi kama Jaji huyo angeuawa leo hii tungesema nini; kwa nini kwa vile kanusurika hakuna kelele za kukemea kitendo hiki? Hadi mtu auawe ndio tutaamka na kuona uovu?
Je, yawezekana kuwa mapolisi waliotakiwa kumlinda ndio walikula njama na majambaza/jambazi? Yawezekana kuwa mapolisi wenyewe ndio waliokuwa majambazi?
Katika hili tusikubali kuvumilia uovu na kuuchekea ufisadi. Jaribio hili la kumshambulia jaji na zaidi ya yote kumuondolea ulinzi ni suala la hatari sana kwa utawala wa sheria na kwa hakika lazima likemewe na kupingwa na wapenda utawala wa sheria mahali pote.
Hatutaki majaji wetu, mahakimu na watumishi wa sheria kuanza kuwa wahanga wa mapambano ya ufisadi.
Naomba muungane nami kutaka Kamanda huyo atimuliwe kazi mara moja kama adhabu kali zaidi na fundisho kwa makamanda wengine kuwa kuna maeneo ambayo hayatakiwa kuchezewa hata kuzembewa kwa dakika yoyote.
Zaidi ya yote tunatarajia Inspekta Jenerali wa Polisi atakuwa tayari kuomba radhi kwa jaji huyo na mahakama na kuwahakikishia majaji wetu kuwa uzembe uliotokea kwa Jaji Mmila hautarudiwa tena na ukitokea yeye mwenyewe atakuwa tayari kuwajibika.
Katika mapambano haya tusikubali uovu ati kwa sababu tunaogopa ukweli; Tusikae kuangalia nchi yetu inatawaliwa kwa sheria ya mwituni ambapo mwenye nguvu mpishe. Natoa pole za dhati kwa jaji na ninaomba samahani kwa sisi waandishi na wapenda demokrasia na utawala wa sheria kutopiga kelele za kutosha kuhusu suala hili na kumezwa na mambo ya kitoto ya CCM na Nape!
Nalaani kwa kauli nzito kabisa inayowezekana kitendo cha maofisa wa polisi kuondoka lindoni na kamanda wao kutojua nini kinaendelea. Tunataka wahusika wawajibishwe mara moja kama fundisho wa wengine wote ambao wanachukulia mahakama kama chombo cha kuchezea.
Jaji Bethuel Mmila alijikuta ameibiwa kompyuta ya kubeba (laptop) na zaidi ya yote kujikuta akielekezwa mtutu wa bunduki na jambazi nyumbani kwake ambaye alimtishia kumuua hapo hapo kama angefanya lolote.
Habari hizi zinasikitisha kuwa hazijapata sauti ya kutosha wiki iliyopita kutoka kwa wanasiasa na viongozi wetu kana kwamba tunaishi Baghdad! Inasikitisha uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walikuwa katika ubinafsi wao na mikutano yao na hakuna hata mmoja wao aliyeshtushwa na jambo hilo. Sitashangaa hawakuwa na taarifa hizo kwani wao walikuwa wanawaza; Nape, Nape, Nape!
Jaji huyo anasimulia katika gazeti moja la Kiswahili kuwa hayo yote yalitokea licha ya kuwa anatakiwa kuwa na maafisa wa Polisi kumpatia ulinzi nyumbani kwake.
Jaji huyo amesema kuwa baada ya kuona kuwa kompyuta yake ambayo iko karibu na dirisha imetoweka na dirisha likiwa wazi. Alipotoka kuwatafuta maofisa wa polisi wawili wanaotakiwa kumpa ulinzi, hakukuwa na mtu. Alipokwenda kwenye nyumba ya msaidizi wake wa nyumbani, naye hakuwapo.
Ni hapo ndipo alipojikuta anaambiwa na mtu aliyekuwa na silaha na aliyejificha uso kuwa; ukithubutu kufanya lolote nitakushuti mara moja. Mtu hyo akamuelekeza arudi ndani ya nyumba yake.
Baada ya kujifungia chumbani, Jaji huyo alijaribu kupiga simu polisi Arusha kutoa tahadhari bila kuitikiwa na akajaribu polisi Moshi bila kuitikiwa. Inashangaza kuwa hadi hivi sasa si makamanda wa mikoa hiyo au kutoka makao makuu waliojitokeza kusema lolote na kuwahakikishia majaji wetu kuwa maisha yao yako salama.
Kwa watu wengine kitendo hicho kinaweza kuwa ni ujambazi wa kawaida, lakini kwa mzee wenu hapa naamini kuwa ni mstari wa hatari sana unaoanza kuvukwa. Inapotokea majambazi wanafika hadi kwa majaji na kufanya kweli na wale waliotakiwa kutoa ulinzi wanajiumauma meno hakuna kitu kingine cha kuwaamsha isipokuwa kuwawajibisha.
Kama Lowassa aliweza kuwajibika kwa makosa yake ya kutowajibika kusimamia walio chini yake ipasavyo (si kwa sababu za kisiasa kama Waziri Mkuu alivyojaribu kutuzuga hivi juzi), basi Kamanda huyu wa Arusha pamoja na maofisa waliohusika kutoa ulinzi ni lazima wawajibishwe mara moja.
Tukifumbia macho tukio hili na kulichukulia kama kawaida, tunafungua mlango wa hatari kubwa sana nchini. Hofu yangu si tu tukio hilo la ujambazi, lakini kilicho nyuma yake - ni kitu gani kilisukuma mtu kwenda kumpora Jaji kompyuta?
Je, yawezekana Jaji Mmila alikuwa anasikiliza kesi fulani au kupanga kutoa hukumu juu ya mtu fulani ambaye hajafurahishwa na mwenendo wa kesi? Je, yawezekana Jaji Mmila ametumiwa kutuma ujumbe kwa majaji wengine ambao watakuwa tayari kusikiliza kesi za mafisadi nchini? Hivi kama Jaji huyo angeuawa leo hii tungesema nini; kwa nini kwa vile kanusurika hakuna kelele za kukemea kitendo hiki? Hadi mtu auawe ndio tutaamka na kuona uovu?
Je, yawezekana kuwa mapolisi waliotakiwa kumlinda ndio walikula njama na majambaza/jambazi? Yawezekana kuwa mapolisi wenyewe ndio waliokuwa majambazi?
Katika hili tusikubali kuvumilia uovu na kuuchekea ufisadi. Jaribio hili la kumshambulia jaji na zaidi ya yote kumuondolea ulinzi ni suala la hatari sana kwa utawala wa sheria na kwa hakika lazima likemewe na kupingwa na wapenda utawala wa sheria mahali pote.
Hatutaki majaji wetu, mahakimu na watumishi wa sheria kuanza kuwa wahanga wa mapambano ya ufisadi.
Naomba muungane nami kutaka Kamanda huyo atimuliwe kazi mara moja kama adhabu kali zaidi na fundisho kwa makamanda wengine kuwa kuna maeneo ambayo hayatakiwa kuchezewa hata kuzembewa kwa dakika yoyote.
Zaidi ya yote tunatarajia Inspekta Jenerali wa Polisi atakuwa tayari kuomba radhi kwa jaji huyo na mahakama na kuwahakikishia majaji wetu kuwa uzembe uliotokea kwa Jaji Mmila hautarudiwa tena na ukitokea yeye mwenyewe atakuwa tayari kuwajibika.
Katika mapambano haya tusikubali uovu ati kwa sababu tunaogopa ukweli; Tusikae kuangalia nchi yetu inatawaliwa kwa sheria ya mwituni ambapo mwenye nguvu mpishe. Natoa pole za dhati kwa jaji na ninaomba samahani kwa sisi waandishi na wapenda demokrasia na utawala wa sheria kutopiga kelele za kutosha kuhusu suala hili na kumezwa na mambo ya kitoto ya CCM na Nape!
Nalaani kwa kauli nzito kabisa inayowezekana kitendo cha maofisa wa polisi kuondoka lindoni na kamanda wao kutojua nini kinaendelea. Tunataka wahusika wawajibishwe mara moja kama fundisho wa wengine wote ambao wanachukulia mahakama kama chombo cha kuchezea.