NYEMO CHILONGANI.
KALAMU YENYE SIRI YA DAMU
0718069269
Sehemu ya 17.
Omar hakuamini alichokuwa akikiona mbele yake, ni kama alikuwa akiota, uso wake ulikuwa na tabasamu pana, alikuwa akishangilia kama mtoto mdogo aliyeletewa zawadi ama mchezji wa mpira kufunga bao katika mechi muhimu kabisa.
Televisheni ilikuwa ikionyesha jinsi Marekani ilivyokuwa imeshambuliwa kwa bomu na kulipuka. Kulikuwa na watu waliokuwa wakikimbia huku na kule, chuo kikuu cha Brooklyn kilikuwa kikiteketea kwa moto, watu walilia, kila mtu aliyekuwa mahali hapo alikimbia kuyaokoa maisha yake.
Akamsogelea Miraji mahali alipokuwa na kumpongeza kwa kazi nzuri kwani kati ya vitu alivyokuwa akivitamani sana maishani mwake basi ni kuona akiilipua nchi hiyo kama alivyofanya.
Alijipongeza, akawaita wenzake na kuwaambia kuhusu kile kilichoendelea, huyo Miraji ambaye kwake alikuwa kama Juma Hiza alikuwa mwanaume shujaa, aliyestahili kupongezwa kwa kazi kubwa aliyokuwa ameifanya.
Si Omar tu aliyekuwa na furaha, kila mtu aliyekuwa ameiona taarifa ile kule Uarabuni alikuwa na furaha kupita kawaida, kupigwa kwa Marekani ilikuwa ni furaha kwa mataifa ya Mashariki ya Kati, nchi za Kiarabu hazikulipenda kabisa taifa hilo kubwa.
Siku hiyo walikula na kunywa, walifanya kila kitu walichokuwa wakitaka kufanya. Hawakuwa na habari kwamba kile kilichofanywa kilikuwa ni uongo, walidanganywa kwa kuwa vituo vya televisheni vilidukuliwa na hivyo CIA walifanya kilichoonekana kuwa sahihi kufanywa.
Usiku wa Omari siku hiyo ulikuwa murua kabisa, alilala akiwa na furaha tele. Kwa Miraji kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, alimfikiria Chilo, mwanaume huyo alipanga naye mipango vizuri, alifanya kila kitu alichokifanya lakini hakujua ni kwa namna gani angeweza kuondoka huko Uarabuni kwani kulichosha mno.
Alifanya alichotakiwa kufanya na kuonyesha Marekani ililipuliwa, hilo lilimshangaza mno, lilimfanya kukosa furaha, hakuamini kama yeye ndiye aliyelifanya hilo, moyo wake ulimuuma kujiona kuwa mmoja wa washirika waliofanya mauaji ya kujitoa mhanga.
Alikaa na kumuomba Mungu msamaha, hakuamini kama na yeye alijiingiza kwenye mtego huo. Alikuwa Muislamu aliyependa kuswali kila alipopata nafasi, kwenye kitabu kitakatifu cha Koran kilikataza mambo ya kufanya mauaji kama yale ambayo alijiona kushiriki, alihitaji msamaha thabiti kutoka kwa Mungu.
Wakati yeye akifurahia na kusherehekea, upande wa pili Omar alikuwa chumbani kwake kimya kabisa, alilala huku akionekana kuwa na furaha kupita kawaida, akiwa kwenye hali hiyo mara mlango ukaanza kugongwa kwa nguvu iliyomaanisha alitakiwa kumfungulia mgongaji haraka sana.
Akashtuka na kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuangalia saa yake, ilimuonyesha kwamba tayari ilikuwa ni saa tisa na nusu usiku, hakujua mgongaji alihitaji nini lakini hakuwa na jinsi, akasimama na kuufuata mlango.
“Wewe nani?” aliuliza kabla ya kuufungua, mkononi mwake alikuwa na bastola kwa ajili ya lolote ambalo lingetokea, japokuwa kulikuwa na ulinzi wa kutosha lakini hilo halikumfanya kujiona kuwa salama.
“Abdoulaziz..” aliitikia kijana aliyekuwa nje, hapohapo akafungua mlango.
Macho yake yakatua kwa mwanaume huyo, alionekana kuwa na hofu mno, alimwangalia, kwa jinsi alivyokuwa tu ilionyesha alikuwa na jambo alitaka kumwambia, hapohapo akachukua simu yake na kumpa Omar.
“Kuna nini?” aliuliza Omar.
“Said amekamatwa!” alisema Abdoulaziz huku akimwangalia Omar.
Ni kama hakuamini alichokisikia, alimwangalia mwanaume huyo kwa macho ya kumtaka kurudia kile alichokisema, ilikuwa Said akamatwe na wakati alilipua Chuo Kikuu cha Brooklyn na kufariki dunia kwa kuwa alijitoa mhanga! Kama alikamatwa basi inawezekana alimuwekea bomu mtu na yeye kuondoka, hilo ndilo ambalo lilimjia kichwani mwake.
“Abdoulaziz amekamatwa?” aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Ndiyo!”
“Ilikuwaje?”
“Yaani hata mimi nashangaa!” alisema ijana huyo.
Simu aliyompa ilikuwa ni kwa lengo la kuzungumza na Abdallah ili kumuhakikishia kile alichomwambia. Haraka sana akampigia simu mwanaume huyo na kupokewa, akaanza kuzungumza naye.
“Imekuwaje tena?” aliuliza Omar.
“Mpango umekwenda vibaya!”
“Umekwenda vibaya? Kivipi?”
“Said alikamatwa kabla ya kulipua kile chuo! Nahisi kuna mtu alituchoma,” alijibu.
Omar akashtuka zaidi, hakujua Abdallah alimaanisha nini kwani aliona chuo hicho kikilipuliwa, watu wengi walifariki dunia na kila mmoja alionekana kuchanganyikiwa, si kituo kimoja tu, kila kituo kilionyesha tukio hilo, sasa ilikuwaje aambiwa hapakuwa na mlipuko wowote ule.
Hakukubali, alichokifanya huku akiendelea kuongea na Abdallah, akawasha televisheni yake, bado kulikuwa na habari iliyoonyesha kuhusu ule mlipuko, sasa aliabiwa mtu aliyekwenda kujitoa mhanga, alikamatwa na polisi, ilikuwaje mpaka akamatwe?
‘Yaani bado sijawaelewa!”
“Ni kwamba tulimtuma Said kwenda kulipua chuo!”
“Sawa....”
“Alipofika, kabla ya kulipua akamatwa!”
“Akakamatwa?”
“Ndiyo!”
“Kwa maana hiyo chuo hakijalipuka?”
“Ndiyo mkuu!”
“Kivipi yaani?”
“Kwani wewe una habari gani?”
“Kwamba chuo kimelipuliwa, kuna watu kibao wamekufa, sasa wewe unasemaje?”
“Wewe umeona wapi?”
“Nimeona CNN, Aljazeera, BBC na nyinginezo, kila kona watu wanalia tu!”
“Haiwezekani!”
“Haiwezekani vipi sasa?”
“Hakuna kilicholipuliwa! Kuna mtu atakuwa ametuchoma,” alisema Abdallah.
Omar hakuelewa alichokuwa akiambiwa, ilikuwaje aambiwe Said alikamatwa kabla ya chuo kulipuka na wakati kwenye televisheni aliona chuo kikiwa kimelipuliwa na watu wengi kufariki dunia?
Aliuliza zaidi na zaidi na jibu lilikuwa lile lile kwamba chuo hakikuwa kimelipuliwa na mtu aliyetumwa kwa ajili ya kulipua chuo hicho alikamatwa kabla ya kufanya shambulio hilo.
Hakulala usiku huo, akahisi kulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea, haraka sana akamfuata Miraji kwa lengo la kuzungumza naye, alihitaji kujua ukweli, kama kulikuwa na watu waliowasnichi basi awajue walikuwa akina nani.
Wakati huo Miraji alikuwa amelala chumbani, ghafla akasikia mlango ukigongwa na mtu aliyeonekana tu kuwa na hamu ya kuzungumza naye, huku akiwa na uchovu mwingi, akasimama na kuelekea mahali ulipokuwa mlango na kuufungua.
Macho yake yakatua kwa Omar, mwanaume aliyekuwa na ndevu nyingi kama Osama, alionekana kuwa na jambo moyoni mwake na alitaka kuzungumza naye. Akahisi kulikuwa na tatizo na ndiyo maana usiku mnene kama huo mwanaume huyo alikuwa mahali hapo, akamkaribisha na kuingia ndani.
“Kuna nini tena?” aliuliza Miraji huku akimwangalia mwanaume huyo.
“Chuo hakijalipuliwa,” alijibu Omar kwa sauti ya chini, Miraji akashtuka.
“Hakijalipuka? Kwa sababu gani?” aliuliza.
“Mlipuaji alikamatwa!”
“Ilikuwaje?”
“Hata mimi nashangaa! Ila alikamatwa hata kabla ya bomu kulipuka!” alijibu.
“Mh!”
“Ndiyo hivyo! Hebu niambie ni kitu gani kilitokea,” alimwambia.
“Lakini si kwenye televisheni walionyesha chuo kulipuka?”
“Ndiyo! Yaani hata mimi nashangaa, ndiyo nataka kujua kuna lipi ambalo limetokea!” alimwambia.
Hata Miraji mwenyewe hakujua kilichotokea kwani kwenye maneno yote aliyoambiwa na Chilo, hapakuwa na kitu kama hicho alichoambiwa, sasa kama bomu halikulipuka, tatizo halikuwa lake bali lilikuwa la huyo aliyekwenda kulilipua.
“Inawezekana mlipuaji alikosea!” alisema Miraji.
“Alikosea nini?”
“Alishtukiwa kabla! Hivi kwa jinsi nilivyoandika kitabu hiki kuna mtu angeweza kumgundua? Kuna mtu angeweza kugundua mahali ambapo bomu hilo lingekwenda kulipuliwa? Nadhani huyo jamaa amekosea,” alisema Miraji.
“Inawezekana kweli?”
“Kwenye maisha ya binadamu, kuna kitu kinaitwa kufanya makosa, ndivyo ilivyokuwa kwa huyo uliyemtuma,” alijibu huku akimwangalia Omar, japokuwa mwanaume huyo aliogopeka sana lakini kwake alimuona kuwa wa kawaida tu. Hakumuogopa hata kidogo.
Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumapili...vitabu vitaanza kutoka Ijumaa hii! Kaa tayari. Kaa tayari. Kumbuka hadithi nitasimama kuiposti nikianza likizo ya kuzunguka mikoani.