Kalamu Yenye Siri ya Damu

NYEMO CHILONGANI
KALAMU YENYE SIRI YA DAMU
0718069269

Sehemu ya 09.

Omar huku akisaidiana na Shakoor, wakawatuma vijana kuelekea nchini Nigeria kwa lengo la kumtafuta mwandishi aliyejulikana kwa jina la Juma Hiza, ilikuwa ni lazima wampate na kuzungumza naye zaidi.
Kulikuwa na mambo mengi waliyokuwa wameyafanya, walifanikiwa kwa asilimia mia moja na ghafla tu mipango yao ikaandikwa kwenye kitabu kile, si hicho tu bali hata yale mambo ambayo walihitaji kuyafanya baada ya hapo.
Hilo likawachanganya na ndiyo maana vijana wawili wakatumwa mpaka Nigeria kwa lengo la kumtafuta mwanaume huyo. Walipofika huko wakaambiwa kulikuwa na taarifa mpya kabisa ambayo ilifika mezani kwa Omar dakika chache zilizopita ambayo ilisema huyo Juma Hiza hakuwa nchini Nigeria, alikuwa huko Tanzania.
CIA na Al Qaida zilikuwa taasisi mbili tofauti na kila mmoja alipandikiza watu kwenye kundi la wenzake, walikuwa wakipenyezewa taarifa za siri na kuzifanyia kazi, walikuwa wakifanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Kama ambavyo Marekani walipandikiza watu Uarabuni kwa lengo la kujua kila kitu kilichokuwa kikiendelea basi hata hao Waarabu nao walifanya hivyohivyo, yaani ilikuwa ngoma droo.
Waliambiwa kila kitu kwamba mara baada ya kufika huko walitakiwa kumtafuta mwandishi aliyejulikana kwa jina la Chilo, mwanaume huyo alijua kila kitu kuhusu Juma Hiza na hataka kama walihitaji kuonana naye, lisingekuwa jambo gumu hata kidogo.
Wakaondoka na kuelekea huko, wakajaribu kuwasiliana naye kwenye akaunti ya Facebook, wakaomba kuonana naye huku wakijifanya kuwa watu wema, kitu cha ajabu kabisa Chilo akakubaliana nao na kuonana katika Hoteli ya Giraffe iliyokuwa jijini Dar es Salaam.
Chilo alifahamu kila kitu, alijua kila kitu kingetokea na ingekuwa kazi nyepesi kwake kudili na watu wote hao. Juma Hiza alichukuliwa na kupelekwa nchini Marekani, watu hao walijiona kuwa mabingwa, hivyo alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anavichanganya vichwa vyao.
Alijua kama hao Waarabu wangekuja na kumtafuta, aliyaandika hayo kwenye script yake, na kweli walimfikia na kuzungumza naye. Walichomwambia ni kwamba walihitaji kuonana na mwandishi aliyeitwa kwa jina la Juma Hiza, walihitaji kufanya naye kazi moja kubwa, ila kabla ya yote walitakiwa kwenda naye kuhiji huko Maka.
“No problem! Do you know him?” (Hakuna tatizo! Mnamfahamu?) aliwauliza, watu hao wakaangaliana, alimaanisha kumfahamu kwa sura.
“Yeah!”
Chilo hakutaka kuuliza swali zaidi, alichokifanya ni kuwachukua na kuondoka nao kuelekea maeneo ya Mabibo ambapo huko wakaishia nje ya nyumba moja na kuugonga mlango.
Ni ndani ya sekunde kadhaa ukafunguliwa na msichana mmoja, akawakaribisha na kuingia ndani. Humo wakakutana na vijana wawili, walipowaangalia, huyo mmoja alikuwa yule ambaye walikuwa na picha yake, alikuwa yuleyule, Juma Hiza.
“Nyie mnamtaka nani?” aliuliza Chilo.
“Juma Hiza!”
“Mnamjua ni nani hapo?” aliwauliza.
“Ndiyo! Huyu hapa!”
“Basi mchukueni tukaongee vizuri,” alisema Chilo, jama huyo akasimama na kuanza kuondoka.
Hakuonekana kuogopa, alijua kilichokuwa kikitokea kiliandaliwa, aliambiwa hilo na Chilo kabla, aliondolewa hofu kuwa hakutakiwa kuhofia hata kidogo. Watu hao wakamchukua na kuanza kuongea naye, walimwambia walipenda kusoma simulizi zake ambazo aliziweka kwenye mitandao ya Kijamii, walikubaliana naye na hivyo walitaka kuondoka naye kwenda Dubai ambapo huko maisha yake yangebadilika kabisa.
Akakubaliana nao na siku iliyofuata wakaondoka naye kwa kutumia meli ambayo njiani ilichukua siku kadhaa na kufika nchini Kenya ambapo kwa msaada wa maharamia wa Kisomali, wakawaunganisha na ndege ya Qatar na kuondoka nayo kuelekea nchini Afghanistan.
Ndani ya ndege Juma alikuwa na mawazo tele, hakuwaelewa watu hao, ni kweli aliambiwa na Chilo kila kitu kilichotakiwa kufanywa lakini alishangaa sababu iliyomfanya kuwa rahisi sana kuchukuliwa na kuondoka, alikuwa na maswali mengi lakini kitu cha ajabu kabisa, hakupata majibu yoyote yale.
Baada ya saa kama thelathini na tatu ndege ikaanza kutua katika uwanja wa ndege hapo Afghanistan ambapo kulikuwa na gari lililomchukua mpaka katika Mji wa Kabul ambapo huko akaonana na mwanaume aliyejitambulisha kwa jina la Omar na kuanza kuzungumza naye.
Kwanza alimshukuru kufika mahali hapo, alikuwa na mipango mingi ambayo angetaka kuifanya na ilikuwa ni lazima kushirikiana naye. Ni kweli aliandika kitabu kilichogusa maisha ya watu, kama angekubali kushirikiana naye, basi alikuwa na uhakika wa kwenda kutafuta heshima mpya duniani.
“Haina shida. Ila umezungumzia kitabu! Kitabu gani?” aliuliza Juma.
“Hakuna Mungu Kabisa,” alijibu Omar.
Hata kabla Juma hajazungumza kitu kingine mara mwanaume mmoja aliyevalia kanzu akaingia ndani ya nyumba hiyo huku akiwa na simu mkononi, aliingia kwa kasi kama alikuwa akikimbizwa.
Akampa simu na kumtaka kuzungumza na mtu aliyekuwa upande wa pili. Akaichukua na kuanza kuongea naye. Alichoambiwa ni kitu kimoja tu kwamba Wamarekani walifanikiwa kumpata Juma Hiza, kulikuwa na picha kadhaa zilizokuwa zimepigwa wakiwa uwanja wa ndege na mwanaume huyo.
“Wamempata Juma Hiza?” aliuliza Omar huku akionekana kuwa na mshtuko.
“Ndiyo!”
“Hapana si kweli!” aliwaambia, hakutaka kuamini kwani huyo Juma Hiza aliyekuwa akiambiwa alikuwanaye ndani ya nyumba hiyo.
“Bosi! Niamini!”
“Hivi unajua kama Juma Hiza nipo naye hapa?”
“Upo naye?”
“Ndiyo! Nipo naye hapa!”
“Inawezekana vipi?”
“Ndiyo nikuulize wewe, huyo waliyekuwa naye ni nani!”
“Ngoja nikutumie picha mkuu!” alisema mwanaume huyo na kukata simu.
Alikaa kwa dakika kadhaa huku akionekana kutokuelewa kilichokuwa kikiendelea. Alishangaa, ilikuwaje apigiwe simu na kuambiwa watu hao walikuwa na Juma Hiza na wakati mwanaume huyo alikuwa naye?
Baada ya dakika kadhaa mwanaume aliyempelekea simu akatumiwa picha hiyo na kumuonyesha, ni kweli, yule aliyekuwa akimuona akiwa uwanja wa ndege alikuwa Juma Hiza, cha ajabu hata huyu aliyekuwa naye alikuwa Juma Hiza huyohuyo.
“Inawezekana vipi?” aliuliza Omar huku akimwangalia mwanaume huyo.
“Hata mimi nimeshangaa bosi!” alijibu mwanaume aliyempa simu.
“Wewe unaitwa nani?” aliuliza huku akimwangalia Juma.
“Juma Hiza!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo! Ni mimi! Niliandika kitabu cha Hakuna Mungu kabisa. Jamani hebu nielezeni kuna nini!” alimwambia huku akimalizia kama mtu aliyekuwa akilalamika.
Omar akashindwa kujua afanye nini!
***
Picha zilipigwa kwa siri na kusambazwa kwamba yule mwandishi wa Kitabu cha Hakuna Mungu Kabisa alipatikana na hivyo maofisa wa CIA walimchukua kutoka nchini Tanzania. Picha hizo zilianza kusambazwa kila kona, kila aliyeziona alishangaa, alikuwa kijana mdogo ambaye hakuonekana kuwa na uwezo wa kuandika hadithi iliyokuwa na msisimko kama ile, lakini cha ajabu alikiandika kitabu hicho na kukiuza mtandaoni.
Kila mtu alikuwa akishangaa uwezo wake, haukuwa wa kawaida lakini pia kulikuwa na suala la kujua matukio kadhaa, jinsi yalivyofanyika mpaka watu wengi kuuawa, hawakujua kijana huyo aliyajuaje hayo yote, wakati mwingine walihisi inawezekana na yeye alihusika.
Kila mtu kwa kipindi hicho alikuwa na mawazo yake, wapo waliosema aachwe kwa kuwa hakuwa na makosa lakini pia wapo waliosema ashikiliwe na kuhojiwa kwani inawezekana alikuwa na mambo mengi aliyoyajua tofauti na hayo aliyoyaandika kwenye kitabu kile.
Peter alitaka suala hilo liwe siri kubwa lakini kitu cha ajabu alishangaa kuona tayari picha zilisambazwa, waandishi wa habari hawakulala, muda wote walikuwa kazini wakiendelea na majukumu yao kama kawaida.
Juma Hiza alichukuliwa na kupelekwa katika chumba kimoja kwa lengo la kufanyiwa mahojiano maalumu. Kila ofisa aliyekuwa ndani ya jengo hilo la makao makuu lililokuwa Lengley alikuwa akipita na kuchungulia, walitaka kumuona huyo Juma alifananaje.
Walishangaa mno, alikuwa kijana mdogo ambaye kwa muonekano wake tu hakuonekana kama alikuwa na uwezo wa kuandika simulizi iliyokuwa na chembechembe za ukweli kama ile, hawakujua uwezo huo aliutolea wapi kwa kuwa waliamini watu waliokuwa na kipaji cha uandishi kama huo walifariki miaka mingi sana nyuma, sasa huyu wa kizazi kipya alitoka wapi?
Juma alitulia kwenye kiti, kwa mbele ukutani kulikuwa na kioo kikubwa, aliiona taswira yake lakini kutokana na uzoefu wake wa kuangalia muvi mbalimbali alijua nyuma ya kioo kile kulikuwa na watu waliokuwa wakimwangalia.
Uso wake ulikuwa na tabasamu pana, alifurahia sana kuwepo ndani ya jumba hilo kubwa. Ilikuwa ni kama ndoto yake, watu wengi waliokuwa wakiletwa humo walikuwa wale wenye akili ambao waliwasumbua sana CIA.
Baada ya dakika kadhaa, mwanaume mmoja aliyevalia suti akaingia ndani ya chumba hicho, alikuwa Peter, alishika vikombe viwili vilivyokuwa na kahawa ndani yake. Akampa kikombe kimoja na kingine kubaki nacho yeye.
“Hongera sana kwa kitabu chako kizuri!” alisema Peter huku akimwangalia Juma.
“Nashukuru sana!”
“Kwa nini uliandika kitabu kama kile?” aliuliza mwanaume huyo.
“Ni kipaji tu!”
“Kilikuwa kipaji kwenye ishu ya utunzi ama ni kitu cha kweli kilichowahi kutokea?” aliuliza Peter.
“Ni utunzi tu!”
“Ila yote uliyoyaandika yamewahi kutokea!”
“Najua! Ila niliyatunga tu!”
“Utunzi ulioendana na ukweli?”
“Nahisi!”
Peter alikaa kimya, nyuma ya kioo kile kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakisikiliza na kuangalia kile kilichokuwa kikiendelea. Huyo Juma alikuwa maarufu, walitaka kumtumia kwa lengo ya kukamilisha mipango yao, kuwakamata maadui zao na kufanya lolote lile walilolitaka.
“Ukisoma kitabu kwa makini kuna sehemu umeandika Esta alikutana na mwanaume wa Kiarabu sehemu iitwayo Brokline kwa lengo la kuzungumza, ni kweli sehemu ile ipo japo umekosea herufi, ulitakiwa kuandika Brooklyn, haikunichanganya, ila kwa nini ulikosea jina la sehemu maarufu kama hiyo? Hukuona uandishi wako ungeonekana wa ubabaishaji?” aliuliza Peter. Juma akatoa tabasamu pana.
“Nilikosea kimakusudi kwa sababu nilitaka kuwaambia kitu kutokomeza ugaidi,” alijibu Juma na kutabasamu, Peter akashangaa kidogo, si yeye tu, hata watu waliokuwa wakiwaangalia kupitia kile kioo nao walishangaa.
“Sijakuelewa!”
“Ilibidi mjue mengi sana! Kama mtakifuatilia kitabu hicho, nakuhakikishia hakutokuwa na ugaidi katika ardhi ya Marekani,” alisema Juma huku akiwaangalia.
“Ulimaanisha nini?”
“Leo ni tarehe ngapi?”
“Tarehe thelathini na moja mwezi wa saba!”
“Imebaki siku moja, kutakuwa na mlipuko mkubwa hapo Brooklyn. Mtatakiwa mjipange,” alisema Juma.
“Inawezekana vipi?”
“Na ndiyo maana nikawaandikia tarehe na sehemu husika!”
“Ulituandikia tarehe?”
“Ndiyo! Wewe ni ofisa wa usalama wa Marekani nje ya nchi, kweli ulishindwa kubaini hili?”
“Hapana! Yaani ulimaanisha nini?”
“Hebu hesabu moja mpaka kumi!” alisema Juma, hapohapo Peter akaanza kuhesabu.
“Zitaje herufi za mwanzo kwenye kila namba!”
“Kuna OTTFFSSENT” alijibu, akimaanisha One ni O, Two ni T, Three ni T na kuendelea.
“Kwenye mtiririko wako huo, herufi O imekuwa ya ngapi?” aliuliza.
“Ya kwanza!”
“Na E?”
“Ya nane!”
“Hiyo ni tarehe 1/8 saa tisa jioni kutakuwa na mlipuko sehemu iitwayo Brooklyne,” alisema Juma, Peter akanyamaza, alimwangalia kijana huyo, hakummaliza hata kidogo. Alishindwa kuelewa alifikiria nini mpaka kuandika vitu hivyo.
“Kwa hiyo unat....”
“Shambulio litatokea mchana. Ukiziangalia hizo herufi, baada ya herufi E kuna N na T, huo ni wakati na muda,” alisema Juma, hapo alimaanisha Noon Time yaani wakati wa mchana.
“Nani atakwenda kulipua?” aliuliza Peter huku akionekana kuogopa.
“Al Qaida!”
“Al Qaida?”
“Ndiyo!” alijibu Juma.
Huku Peter akiwa amechoka hoi kwa kile alichokuwa amekisikia, mara mlango ukafunguliwa na mwanaume mmoja aliyekuwa na kompyuta ya mapajani, akamfuata mahali alipokuwa na kumuonyesha kitu.
Peter akashtuka, hakuamini alichokuwa amekiona, alishangaa, alimwangalia Juma mara mbilimbili huku uso wake ukionekana kuwa na maswali mengi. Kitu alichokiona kilikuwa ni taarifa kwa njia ya video iliyoonyesha kwamba kundi la Al Qaida la nchini Afghanistan lilifanikiwa kumpata Juma Hiza, tena walimuweka kwenye video kabisa dunia nzima imuone.
Hilo lilimshangaza kwani huyo Juma Hiza aliyekuwa akizungumziwa na Al Qaida walikuwa nae wao, sasa ilikuwaje mwanaume huyo aonekane tena akiwa huko Uarabuni.
“Haiwezekani! Juma Hiza si ndiye huyu hapa?”
“Ndiyo! Sasa yule nani? Tena wanasema wanakusanya data zaidi na kufanya milipuko mingine mingi ikiwemo Brooklyn kwani kitabu kilichoandikwa kiliainisha mambo mengi mno,” alijibu mwanaume huyo.
“Juma! Huyu ni nani?” aliuliza Peter huku akimuonyesha Juma video ile, Juma mwenyewe akapigwa na mshangao.
“Mh!” aliguna.
“Huyu ni nani? Juma Hiza ni nani? Ni wewe ama huyu?” aliuliza mwanaume huyo, Juma alichanganyikiwa, cha ajabu hata yeye mwenyewe alishindwa kufahamu kama Juma Hiza alikuwa yeye ama yule aliyekuwa akimwangalia, ni kama alikuwa akijiangalia kwenye kioo.
Hapo akaanza kuiona akili ya kwanza ya huyo Chilo.
“Chilo.....” alijikuta akijisemea moyoni.

Je, nini kitaendelea?
Kumbuka kitabu cha Dili la Dola Bilioni Nne kinaendelea kupatikana. Wasiliana nami 0718069269.
 
NYEMO CHILONGANI
KALAMU YENYE SIRI YA DAMU
0718069269

SEHEMU YA 10.

St. Monica Hospital, 1995

Zilikuwa zinasikika kelele kutoka kwa mwanamke aliyekuwa ameingizwa ndani ya jengo la Hospitali ya St. Monica iliyokuwa Majengo, Moshi mkoani Kilimanjaro. Kila mtu aliyekuwa mahali hapo alimwangalia mwanamke huyo aliyeingia akiwa na mumewe ndani ya jengo la hospitali hiyo.
Haraka sana manesi waliokuwa pembeni wakachukua machela na kumpelekea mwanamke huyo na kumlaza mwanamke yule na kuanza kuelelekea katika chumba cha kujifungulia.
Alikuwa mjauzito, alisikia maumivu ya tumbo, alihitaji kujifungua kwani tayari hata chini ya kitofu chake kulikuwa na majimaji fulani ambayo yalionyesha mwanamke huyo alikuwa katika hatua za mwisho kabisa kuwa na ujauzito huo.
Wakamuingiza ndani ya chumba hicho na kumlaza kitandani. Daktari aliyekuwa na ndevu nyingi, sura iliyoonyesha kuwa mnywaji mzuri wa pombe, huku akiwa na koti lake akaingia ndani ya chumba hicho na kumwambia manesi wajiandae kwani walitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha mwanamke huyo anajifungua salama.
Kila kitu kiliandaliwa na baada ya hapo hatua ya kwanza ya kujifungua kuanza kufanyika. Mwanamke huyo alikuwa akipiga kelele lakini ghafla tu, akanyamaza.
Huo ulikuwa mtihani mkubwa waliokutana nao, asingeweza kusukuma kwa kuwa alionekana kama kuanza kukosa pumzi na muda wowote ule angeweza kuzimia kitandani hapo.
Haraka sana wakamchomeka dripu iliyokuwa na dawa maalumu iitwayo Bioframidium ambayo hutumika kumuweka mgonjwa kwenye hali nzuri na kuyaweka sawa mapigo yake ya moyo.
“Who have to do caesarean,” (Ni lazima tumfanyie upasuaji wa kumtoa mtoto) alisema daktari.
Hilo ndilo lililotakiwa kufanyika, ilikuwa ni lazima mwanamke huyo afanyiwe upasuaji kwa ajili ya kumtoa mtoto aliyekuwa tumboni mwake. Likafanyika haraka sana, daktari yule ‘chapombe’ akahitaji vifaa vyote na ndani ya dakika kadhaa, tayari kazi ilianza.
“Kumbe ana mapacha,” alisema daktari huyo, tayari uso wake ukawa na tabasamu pana.
“Ni kama Mungu!”
“Hakika ametenda!” alisema daktari huyo.
Kila mtu aliyekuwa ndani ya chumba hicho akakenua kwa furaha, wakaanza kuwatoa watoto waliokuwa tumbo mwa mwanamke huyo, kazi iliyofanyika kwa mafanikio makubwa na kuwaweka pembeni.
“Mnamkumbuka yule mwanamke?” aliuliza daktari.
“Ndiyo! Yule mama mgumba?”
“Huyohuyo! Mpigieni simu,” alisema daktari, nesi akatoka na kupiga simu upande wa pili na kuhitaji mwanamke huyo aende hospitalini hapo haraka sana.
***
Kwa jina aliitwa Amina Mohammedi, alikuwa miongoni mwa wanawake waliokuwa na roho nzuri waliokuwa wakiishi katika Mtaa wa Old Moshi mkoani Kilimanjaro. Mwanamke huyu alifanikiwa kuolewa na mwanaume aitwaye Mrisho ambaye alikuwa mnyenyekevu kwa kila mtu aliyekuwa akiongea naye.
Walikuwa na mafanikio makubwa, pesa, walikuwa wakifanya biashara mbalimbali mkoani Kilimanjaro, walipendwa, biashara zao zilikuwa na mafanikio makubwa kupita kawaida.
Ndoa yao ilikuwa imetimiza miaka kumi na moja lakini bahati mbaya hawakufanikiwa kupata mtoto. Hilo liliwaumiza mno, ndugu waliongea sana, waliwasakama mpaka pale walipoamua kupima hospitalini ili kujua ni nani alikuwa na tatizo.
Mtu wa kwanza kupima alikuwa Amina, alipopima matokeo yakaja na kuambiwa mirija yake ya uzazi haikuwa sawa, isingeweza kutengeneza mtoto yeyote yule. Mume wake alihuzunika lakini pia alihitaji kupata uhakika wa afya yake pia kuhusu masuala ya uzazi.
Alipopima, mbegu zake zikaonekana kukosa nguvu ya kumpa mimba mwanamke kitu ambacho kingedumu katika maisha yake yote. Wote wawili walihuzunika, hawakuamini walichokutana nacho, ingekuwa rahisi kupata mtoto kama tu mmojawapo angekuwa mzima kiafya lakini hilo halikuwezekana kabisa, sasa walitakiwa kupambana.
Walitamani kuwa na mtoto, hata kama asingekuwa wao lakini nyumba hiyo ilihitaji mno kuwa na mtoto kitu kilichowafanya kuwasiliana na daktari wa Hospitali ya St. Monica na kumwambia kuhusu hitaji lao hilo.
Dk. Lyimo alinyamaza, alimwangalia Amina huku akiwa makini kabisa kumsikiliza. Suala alilokuwa akiambiwa lilikuwa kubwa mno, lilimsikitisha, kwa jinsi mwanamke huyo alivyokuwa akielezea, ilionyesha dhahiri alikuwa na shida ya kuwa na mtoto.
“Sasa unataka nikusaidiaje?” aliuliza daktari.
“Ninahitaji uniibie mtoto!”
“Nikuibie mtoto?”
“Ndiyo!”
“Kivipi yaani?” aliuliza daktari, macho yalimtoka, alichokuwa ameambiwa hakika kilimshangaza.
Amina akaanza kumwambia kuhusu mpango wake, hakutaka kufa akiwa hajawahi kulea hata mtoto, alizungumza na mumewe na kumwambia kuhusu suala la kununua mtoto, alikubaliana naye na ndiyo maana alihitaji kuyapanga na daktari huyo.
Kwanza daktari alisema lingekuwa suala gumu kufanyika kwani kila mzazi alikuwa akijua alikuwa akiingia humo kujifungua hivyo kitendo cha kumuiba mtoto lingekuwa suala gumu sana.
Amina hakukubaliana naye, alimwambia kulikuwa na urahisi sana lakini daktari huyo hakutaka kukisumbua kichwa chake, alichomwambia ni kwamba endapo kungetokea mwanamke aliyekuwa na watoto mapacha tumboni basi wafanye juu chini mtoto mmoja anapewa yeye.
“Kwanza una kiasi gani?” aliuliza daktari, aliona maneno yamekuwa mengi sana na wakati kichwa chake kilifikiria pombe.
“Milioni kumi!” alijibu mwanamke huyo.
“Unasemaje?”
“Milioni kumi!” Mwanamke huyo akajibu.
Kwa mwaka 1995 kiasi hicho cha pesa kilikuwa kikubwa, Dk. Lyimo alimwangalia mwanamke huyo mara mbilimbili, hakuamini kama yeye ndiye aliyekuwa ameambiwa kiasi hicho cha pesa.
Alikuwa na nyumba yake ambayo hakuwa ameimaliza, alikuwa na shamba lake la migomba ambalo lilihitaji kama laki mbili kupanda migomba mingine na kubwa zaidi alifikiria sana pombe.
Angepata kiasi hicho cha pesa kilimaanisha angekunywa sana, angelewa na kuyafaidi maisha kana kwamba yaliandaliwa kwa ajili yake tu, baada ya kufikiria hayo yote, akakubaliana naye.
“Ila ni lazima kuna watu tuwashirikishe!” alisema Amina.
“Watu gani sasa?”
“Manesi wenzako! Kwani kwenye chumba cha kujifungulia utakuwa peke yako?”
“Hapana!”
“Watakaokuwepo na wao lazima waambiwe, iwe siri!”
“Sasa milioni kumi itatosha kugawana?”
“Hiyo ni yako, nao watakuwa na malipo yao ila si makubwa kama yako!” alisema Amina.
“Hapo sawa sasa!”
Siku ambayo Farida alipelekwa hospitalini kujifungua madaktari waliona wakiwa watoto wawili, kwa miaka hiyo ya nyuma ilikuwa ni vigumu kugundua kwa kuwaangalia kwenye mashine maalumu kwa kuwa hapakuwa na uwezo huo.
Mtoto mmoja akachukuliwa kutoka ndani ya chumba kile na kupelekwa katika chumba kingine kabisa bila kupitia ule mlango aliokaa mume wa Farida, Athumani Hiza. Akampitisha mtoto mpaka kwenye chumba kingine na kumuhifadhi humo kwa muda na baada ya dakika kadhaa, Amina akafika mahali hapo, akamchukua mtoto huyo na kuondoka naye.
Alipofika kwa mumewe, hakutaka suala hilo ligundulike, haraka sana akamwambia ni lazima waondoke Kilimanjaro na kwenda kuanza maisha jijini Dar es Salaam, na kweli wakaondoka siku iliyofuata na walipofika jijini humo, wakaendeleza biashara zao kwa mafanikio makubwa na kuingiza pesa, mtoto huyo akapewa jina la Miraji Mrisho.
Wakati hao wakiwa wamekwishafanya yao, Amina alikuwa hospitalini, bado hakuwa amerudiwa na fahamu, alilazwa huku mtoto wake mmoja aliyezaliwa akiwa amehifadhiwa katika chumba kingine kabisa.
Mzee Hiza alikuwa akienda huko na kumwangalia mtoto wake, hakuwa akijua kama walizaliwa mapacha na mmoja alichukuliwa na kuuziwa mwanamke aliyekuwa mgumba, kwake, alifurahi kumuona mtoto huyo.
Baada ya siku mbili, hatimaye Farida akarudiwa na fahamu, mwili wake ukawa na nguvu na kuhitaji kumuona mtoto wake, halikuwa tatizo, akaletewa na kuanza kumwangalia. Uso wake ulikuwa na tabasamu pana, kila alipomwangalia alijisikia fahari kubwa ndani yake, alitokea kumpenda mtoto huyo na aliahidi ingekuwa roho yake nyingine duniani.
Mbali na kumkubali mtoto huyo lakini wakati mwingine alikuwa na wasiwasi, alimwambia mume wake kwamba kwa jinsi alivyokuwa akijisikia kipindi alichokuwa mjauzito inawezekana alikuwa na mimba ya watoto mapacha, cha ajabu kabisa alishangaa kuona amejifungua mtoto mmoja tu.
“Kwa nini unasema ulikuwa na mapacha mke wangu?” aliuliza mzee Hiza huku akimwangalia.
“Yaani ni kama walikuwa wakigongagonga kwa pamoja,” alijibu.
“Sasa si kwa sababu alikuwa akikugonga kwa mkono na mguu! Mke wangu umejifungua mtoto mzuri sana,” alisema mzee Hiza huku akimwangalia mtoto huyo, hakutaka stori za kuhisi walizaliwa mapacha ziendelee kuwa kichwani mwa mke wake.
Japokuwa Farida alikubaliana na mume wake lakini moyo wake haukutaka kabisa kukubali, alikuwa na uhakika wa kuwa na mapacha tumboni mwake, kwa jinsi alivyokuwa akijisikia, alijua kabisa tumbo lake lilibeba watoto wawili lakini kitu cha kushangaza kabisa, eti baada ya kujifungua alipelekewa mtoto mmoja.
Furaha yake ni kama haikukamilika hata kidogo, kila alipomwangalia mwanaye, Juma, moyo wake ulimwambia mahali fulani kulikuwa na pacha wake akiendelea na maisha yake mengine kama kawaida.
Kwa miaka hiyo hapakuwa na mambo ya watoto kuibwa na kuuzwa, alitaka kuamini hilo lakini kwa kuwa hakuwahi kusikia kesi ya namna hiyo, akaamua kukubaliana na daktari, mume wake kwamba kweli alijifungua mtoto mmoja.
“Ila kama nilijifungua wawili, kuna siku Mungu atamleta mikononi mwangu,” alisema Farida, moyo wake uliamini kabisa kwamba kuna siku mtoto wake mwingine angekwenda mikononi mwake endapo kulikuwa na ukweli wa kujifungua watoto mapacha.

Je, nini kitaendelea?
 
NYEMO CHILONGANI
KALAMU YENYE SIRI YA DAMU
0718069269

SEHEMU YA 11.

Watoto hao mapacha waliendelea kukua kila siku wakiwa kwenye mikono ya watu tofauti, hapakuwa na yeyote ambaye alijua kama watoto hao walikuwa mapacha zaidi ya madaktari wale waliokuwa hospitalini.
Miaka ilisogea kama kawaida, Miraji akakua na kuanza darasa la kwanza, alisoma na kusoma mpaka alipohitimu kidato cha nne ambapo watu aliojua walikuwa wazazi wake, Amina na mzee Mrisho kufariki dunia baada ya kupata ajali ya gari na hivyo kubaki mwenyewe.
Maisha hayakuwa kama yalivyokuwa, yalibadika, yalikuwa magumu lakini alijitahidi kupambana nayo kama kawaida. Wakati huohuo naye Juma aliendelea kukua mkoani Kilimanjaro na baada ya kumaliza kidato cha nne akaamua kuondoka na kuelekea jijini Dar es salaam kusoma lakini lengo lake lilikuwa ni kuandika vitabu vya simulizi kwa sababu aljua alikuwa na kipaji cha uandishi lakini hakujua angeanzia wapi.
Alipofika huko, mtu wa kwanza kabisa kumtafuta alikuwa huyo Chilo, alisoma simulizi zake katika Mtandao wa Kijamii wa Facebook, alihitaji kujifunza kupitia kwake kwani aliamini kuna siku isiyokuwa na jina angekuwa na pesa nyingi, pesa ambazo zilipatikana baada ya kuandika vitabu kadhaa.
Akampigia simu mwandishi huyo na kuomba kuonana naye, halikuwa tatizo, wakaonana na kuanza kuzungumza. Juma hakujiamini, kila alipokuwa akimwangalia Chilo alihisi alikaa na mtu gani, kwa mbali kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.
“Umesema umeandika simulizi! Zipo wapi?” aliuliza Chilo swali lililomfanya Juma kuchukua begi lake na kulifungua, akatoa daftari na kumuonyesha.
“Kwa hiyo unaandika kwenye daftari?” aliuliza huku akimwangalia.
“Ndiyo bro! Sijapata kompyuta!” alijibu.
“Unahisi kikifanyika kitu gani utaweza kufikisha ndoto zako?” alimuuliza huku akiwa amelichukua daftari hilo na kuanza kuliangalia.
“Kuandika kwenye magazeti!”
“Ili?”
“Nijulikane!”
“Tunahama huko! Tunahamia kwenye mitandao, kila kitu kimebadilika Juma, idadi ya wanunua magazeti imepungua, ni lazima tuwekeze kwenye mitandao,” alisema Chilo huku akimwangalia Juma.
“Sasa mimi nitafanyaje bro! Sina hata kompyuta!” alisema, alitia huruma, kwa jinsi alivyoonekana tu, ni kweli alihitaji msaada.
“Utaitumia yangu nitakapokuwa sipo bize! Unaishi wapi?”
“Temeke!”
“Duuh!”
“Kwani vipi bro?”
“Mbali kichizi!” alijibu Chilo na kuanza kutoa kicheko cha chini.
Waliongea kama marafiki ambao walikutana miaka mingi iliyopita, kila wakati Juma alipokuwa akimwangalia Chilo alitamani kuwa kama yeye, aandike simulizi kama zake, zije kupendwa na wasomaji wengi.
“Na nifanyeje ili nifanikiwe?” aliuliza Juma baada ya mazungumzo marefu.
“Tupo kwenye ulimwengu wa shida sana Juma! Tunapitia nyakati ngumu sana,” alijibu Chilo huku akimwangalia Juma, sasa wakawa wamesimama.
“Sijakuelewa!”
“Unajua kama wasomaji wana akili sana? Tena zaidi yetu?” aliuliza.
“Wasomaji wana akili zaidi yetu?”
“Ndiyo! Tena kubwa sana. Unaweza kuandika kuhusu nyumba kwa muonekano wa nje, wao wanajua mpaka muonekano wa ndani. Sasa ili uweze kwenda nao sawa ni lazima ujifunze, usome sana, ujitahidi kuijua dunia. Siku ukiandika kitabu ukazungumzia madaktari basi daktari fulani akikishika kitabu chako na kusoma aone kweli umeandika kama nawe ni daktari!” alijibu Chilo.
“Aiseee!”
“Hata kama hujawahi kukutana na mwanamke kimwili, ukiandika simulizi za chumbani, andika kama umetoka kucheza filamu za utupu!” alisema Chilo, Juma akaanza kucheka.
“Halafu bro bhana!”
“Najua mifano nikiitolea kwa wanawake lazima uonyeshe hali fulani hivi! Sikulaumu, sisi ngozi nyeusi tupo hivyo, kwanza tunapenda sana ngono! Lishike hilo na kuna siku nitakuuliza nilikwambia nini! Sisi ngozi nyeusi tunapenda sana ngono!” alisema Chilo.
“Utaniuliza siku moja?”
“Kila kitu ninachoongea nawe kuna siku nitakuuliza ama kitakuwa msaada mkubwa kwenye maisha yako! Huwezi kuendelea ukiwa unapenda sana ngono kupita kiasi!” alisema Chilo, kwenye suala hilo akaonekana siriazi.
“Hilo najua!”
“Bado hujajua ipasavyo! Ila nakuahidi kuna siku utajua! Kapande gari, tumeongea sana! Ila endelea kuandika,” alisema Chilo, wakaagana na Juma kuondoka mahali hapo.
Juma alijiona kuwa mwandishi wa kawaida lakini Chilo alipokuwa akimwangalia aliona kabisa kuna siku angekuja kuwa na uwezo mkubwa mno. Aliagana naye lakini kichwa chake hakikuacha kumfikiria hata kidogo.
Aliporudi nyumbani kwake, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuchukua kalamu na karatasi na kuanza kuandika kama kawaida yake. Alikuwa na mipango mingi sana, aliigawa na ilikuwa ni lazima ifanyike, hata kama ingeshindikana lakini siku akikaa chini aseme nilijaribu kufanya kitu fulani lakini kilishindika. Kwenye kidaftari chake aliandika hiviiiiii...

1. Nitaandika filamu Hollywood: Ili kufika huko ni lazima kichwa changu kifkirie zaidi ya watu wengine, nipanue mawazo yangu zaidi ya watu wengine, nisome sana kwenye mitandao kuliko watu wengine.

2. Nitaandika kitabu na kuingiza pesa sana: Na hili nifike hapo ni lazima nifikirie kuhusu kitabu changu kimataifa. Niwe kama akina Ngugi wa Thiongo lakini niwe kidigitali zaidi, kwa hapa ni lazima nitumie mitandao ikiwemo Amazon. Jina nitakaloliweka ni THERE IS NO GOD AT ALL yaani HAKUNA MUNGU KABISA. Nitaliweka jina hili kwa sababu ya kuwafanya watu wasome ili waone kwa nini nimeandika jina hilo.

3. Kwa sababu nitakuwa na mipango mingi, nitamtumia Juma Hiza kukamilisha ndoto zangu! Tutasaidiana, wakati yeye anataka kukamilisha ndoto zake, anitumie kama daraja na mimi nimtumie kama daraja. Ni kama jinsi mwajiri anavyomtumia mfanyakazi wake kuwa daraja la kutimiza ndoto zake.

4. Kitabu nitakachoandika ni lazima niwasumbue akili Wazungu kama jinsi ambavyo Snowden alivyowasumbua Wamarekani. Wanaogopa sana ugaidi, nitaitumia hofu yao kutimiza malengo yangu. Wazungu walipokuja Afrika, walitutisha mno, tukaogopa, kupitia hofu zetu, wakachukua mali zetu na kubaki tulivyo, sasa ili kutimiza ndoto zako, wakati mwingine unatakiwa kuwatisha watu fulani, watakapotishika, unakamilisha ndoto hizo harakaharaka.

Chilo aliandika mambo mengi na baada ya kumaliza, akafunga daftari lake na kuendelea na mambo mengine. Ukaribu wake na Juma uliendelea kama kawaida, waliendelea kuwasiliana na kumsisitiza sana kuhusu uandishi huo wa simulizi ambao aliamini kuna siku ungemfanya kutoka na kuwa sehemu nyingine kabisa.

‘MWANAUME MZURI KULIKO WOTE TANZANIA AONEKANA CHUO KIKUU KWA MARA YA KWANZA!’

Hicho kilikuwa kichwa cha bari kirefu kuandika katika Tovuti ya Michuzi, Chilo aliifungua na kutaka kuona picha ya mwanaume huyo, ilipofunguka, akabaki akiiangalia, alitamani kujua zaidi kuhusu mwanaume huyo, haraka sana akaanza kusoma maelezo yake, akabaini kwa jina, mwanaume huyo aliitwa Richard Mawelle, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
“Nahisi naweza kupata kitu kizuri hapa, acha niende huko chuoni nikajue mengi kuhusu mwanaume huyu,” alijisema Chilo huku akiyasoma maelezo zaidi kuhusu huyo Richard aliyekuwa na sura nzuri kuliko wanaume wote (Sifa zake kemkem zimeandikwa kwenye kitabu cha Dili la Dola Bilioni Nne).
****
Baada ya siku kadhaa, mapema sana Chilo akaelekea katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam huku lengo lake kubwa likiwa ni kumuona kijana huyo, tayari kichwa chake kilikuwa na mambo mengi ambayo alitaka kuyaandika, hasa hadithi ambayo ingemuelezea mwanaume aliyekuwa na sura nzuri kama huyo ambaye alikuwa akienda kumuona.
Ndani ya daladala alikuwa akifikiria namna ya kuisuka simulizi nzuri ambayo ingemuhusisha mwanaume huyo aliyekuwa na uzuri wa sura, alihitaji kuandika simulizi ambayo ingemsisimua kila mtu ambaye angekwenda kuisoma siku moja.
Hakuchukua muda mrefu akafika chuoni na moja kwa moja kuelekea kwenye Ukumbi wa Nkurumah kwa lengo la kutulia kabla ya kuanza kumtafuta Richard, alikuwa na hamu ya kumuona na kadiri alivyokuwa akisubiri ndivyo alivyokuwa na hamu ya kutaka kumtia machoni mwake.
Akiwa humo huku akijifikiria kama alitakiwa kumuulizia mwanaume huyo, ghafla macho yake yakatua kwa kijana mmoja hivi, hakuwa mgeni machoni mwake, alimfahamu, alimuona siku chache zilizopita, kijana huyo alikuwa na wasichana wawili waliokaa katika meza moja wakizungumza.
“Juma Hiza...” aliita Chilo huku sura yake ikionyesha tabasamu pana.
Kijana huyo akayainua macho yake na kumwangalia Chilo, alikuwa akitabasamu, yaani kwa jinsi alivyokuwa akimwangalia ni kama aliwahi kumuona mahali fulani sehemu hivi. Si kijana huyo aliyekuwa akishangaa tu bali hata wale wasichana nao walikuwa wakishangaa.
“Mbona unashangaa sana?” aliuliza Chilo huku naye akivuta kiti na kutulia, jamaa yule akamwangalia Chilo kisha akawaangalia na wasichana wale aliokuwanao.
“Tunafahamiana?” aliuliza kijana huyo.
“Daah! Hiza bwana! Unanikataa mchizi wangu! Ndiyo yaleyale niliyokwambia, ukipenda sana hiyo kitu hutoendelea, sasa unanikataa kisa umekaa na wanawake!” alisema Chilo huku akitoa tabasamu ambalo lilionekana kama kumtaka kijana huyo akubaliane naye.
“Sijakuelewa!”
“Kwani wewe nani? Si Juma Hiza?”
“Hapana! Naitwa Miraji!”
“Miraji? Miraji gani? Acha masihara bwana!” alisema Chilo.
“Siriazi bro! Kwani wewe uliniona wapi?”
“Majuzi ulikuja ofisini kwetu pale Bamaga, ukaomba kuonana nami, wewe si ulisema unaandika hadithi, ama umesahau?” aliuliza Chilo.
“Mimi?”
“Yeah!”
“Hapana! Labda umenifananisha! Mimi na hadithi wapi na wapi!” alisema, wasichana wale wakaanza kucheka.
“Siwezi kufananisha kiasi hiki!”
“Bro! Utakuwa umenifananisha!”
Chilo alikuwa na uhakika hakuwa amemfananisha kijana huyo, alijua dhahiri alikuwa Juma Hiza ila alitaka kumkataa tu kwa sababu alikuwa na wasichana mahali hapo.
Alichotaka ni kuuona uongo wa kijana huyo, si alikuwa na namba yake, alichokifanya ni kuchukua simu yake na kumpigia Juma Hiza huku akiwa mbele ya watu hao, simu ikapokewa na sauti ya Juma kuanza kusikika.
“Niambie bro!” alisikika Juma Hiza kutoka upande wa pili, Chilo akashtuka.
“Upo wapi?”
“Nipo home bro! Kuna ishu?”
“Hapana! Nitakucheki!” alisema Chilo na kukata simu.
Akabaki kimya, akaendelea kumwangalia Miraji, kwa jinsi alivyokuwa akionekana, hakuwa na tofauti yoyote ile na Juma Hiza, yaani walifanana kwa kila kitu, kwa jinsi alivyokuwa akiongea, kutabasamu na hata kucheka.
“Basi poa!” alisema Chilo na kuondoka mahali hapo.
Kilichokuja kichwani mwake ni kwamba kijana aliyekuwa amemuona na Juma Hiza inawezekana kabisa walikuwa mapacha wasiofahamiana kwani hata kama kufanana hakudhani kama kungekuwa na watu waliokuwa wakifanana kiasi kile.
Alihitaji kumfahamu kijana huyo, mbali na jina lake kumwambia lakini alitaka kujua alipokuwa akiishi, inawezekana kwa kufahamu hilo angeweza kufahamu baadhi ya mambo.
Hakutaka kumshirikisha Juma Hiza kwanza, alitaka kuwa siri kwani endapo watu hao walikuwa mapacha basi alitakiwa kwenda kuandika script nyingine nyumbani kwa kile ambacho alitaka kukifanya na kujikuta akiwa bilionea kwa kuuza vitabu tu.
Hakurudi nyumbani, akaenda sehemu na kutulia huku macho yake yakiwa makini kuangalia mlango wa ukumbi ule, alihitaji kumfuatilia Miraji na kufahamu kila kitu.
Baada kama ya masaa mawili hivi, akamuona akitoka na wasichana wale na kuanza kuelekea kwenye kituo cha daladala cha Utawala hapo chuoni, naye akaelekea huko, walipofika, wakaingia, na yeye akaingia.
Gari likaondoka mpaka Mawasiliano ambapo wakateremka na kuelekea kwenye sehemu iliyokuwa na daladala za Mabibo, naye akaenda na kupanda, tayari kigiza kilianza kuchukua nafasi yake na kwa sababu kulikuwa na watu wengi hawakuweza kumgundua.
Gari likawashwa na kuondoka mahali hapo mpaka katika kituo cha External, Miraji akateremka na Chilo naye kufanya hivyo, akaanza kuelekea upande mwingine kabisa kumzuga kijana huyo endapo angemuona, alipofika mbali kidogo, akageuka na kuanza kumfuata Miraji upande mwingine.
Alimfuatilia mpaka alipomuona kijana huyo akiingia ndani ya nyumba moja nzuri, akahisi hapo ndipo alipokuwa akiishi, hivyo akaridhika na kuondoka zake.
Alipofika nyumbani akachukua daftari lake na kuanza kuchora ramani kama ilivyotakiwa kuwa. Alimuweka Juma Hiza lakini uwepo wa mwanaume mwingine mahali hapo ulimaanisha alitakiwa kufanya kitu kingine cha ziada ambacho kingekuwa kikubwa sana.
Aliandika na kuandika, alipomaliza, akalala, asubuhi ilipofika akaendelea na mambo yake mengine huku kila kitu alichokuwa akikifikiria mahali hapo kilionekana tu kingekwenda kuwa na mafanikio makubwa huko mbeleni.

Je, nini kitendelea?
 
Kule insta ipo mbali sana, japo saiv ameacha, ameanza kupost nyingine
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom