NYEMO CHILONGANI
KALAMU YENYE SIRI YA DAMU
0718069279
SEHEMU YA 12
Lengo lake kubwa la kwenda katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam lilikuwa ni kuonana na mwanaume aliyeitwa kwa jina la Richard, alihitaji kumuona mtu huyo kwani alikuwa akisifika kwa kila mwanamke aliyekuwa akimfahamu.
Alirudi huko, kama kawaida akakutana na kijana ambaye alionana naye na kuhisi alikuwa Juma Hiza, alipomuona tu kama kawaida yake akamfuata kwa lengo la kuzungumza naye kwani siku hiyo alikuwa peke yake, hakuwa na wale wasichana.
Aliposimama mbele ya kijana huyo, akayainua macho yake na kumwangalia, alikuwa kijana yuleyule wa jana yake ambaye alimuita jina ambalo hakulifahamu, leo alimfuata kwa lengo la kutaka kuzungumza naye.
“Nataka tuongee,” alimwambia huku akimwangalia.
“Kuhusu nini?”
“Utajiri....mapesa mengi tu...utakuwa tayari kunisikiliza?” alijibu Chilo na kukaa pembeni yake.
“Kuna mtu asiyetaka kusikia habari ya mapesa?” aliuliza Miraji na kutoa tabasamu pana.
Chilo akaanza kuongea naye kuhusu lile alilokuwa amemfuatia chuoni hapo, Miraji alikaa kimya huku akimsikiliza mwanaume huyo, kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, mipango alivyokuwa akiipanga ilionyesha kabisa hakuwa mtu wa kawaida, kichwa chake kilikuwa na mambo mengi mno.
Mpaka anamaliza, Miraji alikaa kimya, hakuzungumza kitu chochote kile, alikuwa akimwangalia mwanaume aliyekuwa pembeni yake huku kichwa chake kikiwa na maswali lukuki yasiyokuwa na majibu yoyote yale.
“Ulipata muda gani kuyajua haya yote?” aliuliza Miraji huku akimwangalia.
“Nafikiri umekutana na mtu mwenye akili kubwa tu,” alijibu Chilo na kuanza kucheka.
Kukubali kwa Miraji kulimpa Chilo matumaini makubwa ya kwenda kufanikiwa suala lake lililokuwa mbele yake, muda wote uso wake ulikuwa kwenye tabasamu pana, aliamini kwa namna moja ama nyingine ilikuwa ni lazima kufanikiwa kwa kile alichokuwa amekitaka.
Walizungumza mambo mengi na kubwa zaidi aliloambiwa na Miraji ni kutafuta mastaa ambao wangewezesha kuutangaza ukurasa wake wa hadithi huko Facebook ambapo alipenda sana kuona safari yake ikiwa inaanzia hapo.
Kwenye kumshauri huko akamwambia lingekuwa jambo zuri kama angekutana na msichana aliyejulikana kama Video Vixen na baadaye kujiingiza kwenye muziki, msichana huyo aliitwa Natasha (Umemsoma kwenye Dili la Dola Bilioni Nne).
Kumpata Natasha halikuwa jambo jepesi, muda mwingi msichana huyo hakuwa akionekana chuoni hapo, alikuwa na mambo mengi nje ya masomo yake, Chilo alipata kazi kubwa ya kumtafuta mpaka kuonana naye, ilimchukua mwezi mzima.
Alisimama mbele ya msichana huyo aliyeonekana kuwa na furaha tele, walikuwa canteen na hakujua alikuwa akifurahia jambo gani, pembeni yake alikuwa msichana mmoja mrembo, na kwa mbali alibahatika kumuona yule Richard akiondoka zake, alitoka kwenye meza ile aliyokaa Natasha na rafiki yake.
“Samahanini!” alisema Chilo huku akimwangalia msichana huyo.
“Bila samahani!”
“Nilikuwa nahitaji kuzungumza na wewe kidogo!” alisema Chilo huku akimwangalia Natasha.
“Kuzungumza na mimi? Kuhusu nini?” aliuliza msichana huyo, alitoka kuongea na Richard, mwanaume aliyekuwa akijulikana kwa sura nzuri, baada ya kuondoka, sasa alikuja mtu kama Chilo, alibaki akishangaa, yaani ilikuwa ni sawa na kumaliza kula pilau lililokuwa na nyama ya kuku, kachumbari na mchuzi mzito halafu ukaletewa sahani ya ugali na mlenda.
“Kuhusu kitu kidogo tu!”
“Kipi? Naomba nitafute muda mwingine!” alisema msichana huyo, alikuwa na nyodo kupita kawaida.
Yeye na rafiki yake wakasimama na kuanza kuondoka mahali hapo, Chilo alikasirika moyoni mwake lakini hakuwa na cha kufanya kwa kuwa kukubali kuongea naye ama kukataa yalikuwa ni maamuzi ya mtu binafsi.
Kwa kuwa hakuwa mwanafunzi wa hapo chuoni, akawasiliana na Miraji na kumwambia kuhusu msichana huyo, kwenye mipango yao mingi ilikuwa ni lazima na huyo apitishwe kwani kupitia jina lake aliamini akaunti yake ingekuwa na wasomaji wengi na hivyo kupata jina zaidi mitandaoni.
Miraji akapewa kazi ya kumtafuta msichana huyo na kuzungumza naye. Kila siku hiyo ndiyo ilikuwa kazi yake, alipokuwa akifika chuoni, mtu wa kwanza kumtafuta baada ya masomo alikuwa huyo Natasha, lilikuwa jambo gumu kumpata kwani si muda wote alikuwa akija chuoni na alipokuwa akienda basi alionekana kuwa bize sana.
Baada ya wiki kama mbili ndipo Miraji akafanikiwa kuonana na msichana huyo, akamsimamisha na kumwambia alihitaji kuzungumza naye kidogo, akamruhusu, alichomwambia ni kwamba kulikuwa na rafiki yake alihitaji sana kuzungumza naye, hivyo alihitaji kuonana naye.
“Ni nani?” aliuliza Natasha.
“Anaitwa Chilo!”
“Ndiye nani na anataka kuongea nami kuhusu nini?” aliuliza maswali mawili mfululizo.
“Ni mwandishi wa vitabu vya simulizi!”
“Sawa! Ila nafasi yangu ni leo tu, akinikosa leo mpaka mwezi ujao,” alisema msichana huyo.
Miraji akampigia simu Chilo na ndani ya dakika chache akafika chuoni hapo na kuanza kuzungumza naye, alimwambia kuhusu suala lake, alihitaji kutangaziwa kurasa zake za mitandaoni, alihitaji kuona akipata wafuatiliaji wengi wa simulizi zake.
“Sawa! Nitakusaidia kwa sababu mwanachuo mwenzangu!” alimwambia, hakujua kama Chilo hakuwa mwanachuo.
“Sawa!”
“Ila mpaka nipate ruhusa!”
“Ya nani tena?”
“My baby! Richard!” alijibu kwa maringo kidogo.
Walibadilishana namba za simu na baada ya hapo wakaagana, kazi ikawa kwenye kutafutana tu. Chilo akawa anapiga simu mara kadhaa lakini haikuwa ikipokewa, hilo lilimkasirisha lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kuendelea kumtafuta msichana huyo kwa kuwa alikuwa msaada mkubwa kwake.
Zilipita wiki mbili nyingine, akampigia simu, ikapokewa na rafiki yake Natasha na kuomba kuongea naye, alichomwambia ni kuwa asingeweza kwa kuwa alikuwa kwenye matatizo makubwa mno kipindi hicho.
“Matatizo gani?” aliuliza.
“Wewe jua makubwa!”
“Ila naweza kumsaidia!”
“Hutoweza!”
“Niamini! Nitaweza,” alisema na msichana huyo kuomba kuonana naye huko Sinza.
Hakuchukua dakika nyingi akakutana na rafiki yake huyo ambaye alimchukua mpaka alipokuwa akiishi Natasha, alipofika na kumwangalia tu akajua msichana huyo alikuwa kwenye matatizo makubwa, akaomba kuzungumza naye, asimfiche na yeye angejua ni kitu gani alitakiwa kufanya.
“Picha zangu za utupu zimevuja,” alisema msichana huyo huku akifutafuta machozi yake.
“Zimevujaje?” aliuliza Chilo.
“Yaani sijui! Nimepigiwa simu na mtu na kuambiwa ana picha zangu za utupu! Mungu wangu nitafanya nini wenyewe wakijua?” aliuliza msichana huyo huku akilia.
“Wenyewe akina nani?”
“Wewe jua wenyewe tu!”
Hakutaka kumwambia kuhusu hao wenyewe ambao mkasa mzima uliandikwa kwenye kitabu cha Dili la Dola Bilioni Nne. Chilo hakutaka kujali sana lakini alihisi kabisa kulikuwa na mtu ambaye alihusika kwenye tukio hilo la kuvujisha picha hizo.
“Lakini simu si ilikuwa yako! Kuna mtu ulimpa?” aliuliza huku akimwangalia.
“Hakuna!”
“Sasa ilikuwaje mtu aidukue iPhone? Hicho ni kitu kisichowezekana kabisa,” alimwambia.
“Sasa amezipataje hizo picha?” aliuliza Natasha, yaani alichanganyikiwa.
“Kwani hukuwahi kumpa mtu simu yako?”
“Hapana!”
“Si kweli! Hebu kumbuka!”
Natasha akakaa kimya na kuanza kukumbuka kama aliwahi kufanya kitu kama hicho, hapo ndipo alimkumbuka Richard, alikuwa mwanaume pekee ambaye alimpa mpaka namba ya siri ya akaunti ya iCloud.
Japokuwa alikumbuka hivyo lakini bado hakuamini kama Richard angeweza kufanya jambo kama hilo, yaani alimpenda mno kiasi kwamba alihisi kumuhisi kwenye ubaya namna hiyo ilikuwa ni sawa na kumuonea.
“Nilimpa mpenzi wangu tu!”
“Basi ndiye aliyefanya hivyo!”
“Haiwezekani!”
“Hebu niambie zaidi kuhusu huyu Richard, nadhani anajua kila kitu!” alimwambia.
Natasha akaanza kumwambia Chilo kuhusu Richard. Hakujua ni kwa sababu gani alimwamini kwani kwa muda huo alihitaji kuufahamu ukweli tu, alichukua dakika kadhaa kusimulia kila kitu, halafu akanyamaza.
“Sasa huo upenzi wenu upo wapi?” aliuliza Chilo baada ya kusikia simulizi yake.
“Kivipi?”
“Siku zote hizo hamkuwahi kufanya mapenzi! Inawezekana vipi?” aliuliza.
“Aliamua tu!”
“Na nikisema Richard alitumwa kuwa na wewe utasemaje?”
“Alitumwa na nani?”
“Sijajua! Ila nahisi alitumwa.”
“Kivipi?”
“Kwa sababu wewe ni staa, hivyo watu wanakuwinda, wanataka kujua mengi kuhusu wewe, hizo picha na mambo mengine! Hebu leo tujifanye kama FBI, tuanze kumfuatilia huyu Richard, kama utashindwa, naiomba kazi hiyo! Kuna mengi nataka kuyafahamu kuhusu huyu mtu,” alisema Chilo huku akimwangalia Natasha ambaye ni kama hakuwa akielewa kilichokuwa kikiendelea.
“Umfuatilie?”
“Yeah! Nisaidie kwa hilo, nadhani nikijua machache kuhusu yeye, basi naweza kuandika moja ya kitabu bora kabisa,” alimwambia.
“Kuandika kitabu tena?” aliuliza msichana huyo huku akionekana kushtuka.
“Ndiyo!”
“Kitabu kuhusu nini?”
“Mambo mengi likiwemo la hii sura ya Richard inayowachanganya wanawake, inayokuchanganya mpaka uhisi hawezi kukufanyia ubaya wowote ule,” alijibu Chilo huku akiachia tabasamu kama kawaida yake.
“Sawa haina shida.”
“Ila utatakiwa kulipia!”
“Kivipi?”
“Kutangaza ukurasa wangu wa Facebook! Unaitwa Simulizi za Chilo!” alimwambia.
“Haina shida, ila nitahitaji unipe matokeo baada ya uchunguzi wako,” alimwambia.
“Haina shida.”
Chilo akaondoka mahali hapo, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, alijiuliza maswali ambayo hayakuwa na majibu yoyote yale, alichohisi ni kwamba Richard alihusika kwenye ishu ya zile picha na hakujua alitaka nini mpaka kuchukua hizo picha.
Kesho yake akaenda chuoni na kuanza kumfuatilia Richard kwa siri sana, mara nyingi aliwaona akiwa na marafiki zake wawili, Robinson na Robert. Akahisi watu hao walikuwa pamoja kwenye kutekeleza yale mambo waliyokuwa wakiyafanya.
Alihitaji kuwajua zaidi watu hao wawili, hasa marafiki zake. Akaulizia kwa watu na kuambiwa kwamba huyo Robinsin alikuwa mtaalamu wa mambo ya kompyuta na huyo Robert kichwa chake kilikuwa hatari kwa kupanga mipango, hasa mambo ya biashara.
Chilo akajiongeza, suala la Natasha likaanza kumrudia kichwani kwa mara nyingine, akahisi inawezekana huyo Robinson ndiye aliyefanya mpango wa kuchukua picha kutoka kwenye simu ya msichana huyo. Yaani baada ya Richard kuchukua namba ya siri ya akaunti ya iCloud, Robinson akafanya mpango wa kuingia kwenye simu hiyo.
“Mh! Kama ni hivi! Hawa watu hatari sana, acha niendelee kuwafuatilia,” alisema.
Aliwafuatilia, baada ya siku kadhaa kwenye ufuatiliaji wake akamuona Richard akiondoka kuelekea Mwenge, hakutaka kubaki, alimfuatilia mpaka pale alipoingia chooni na kutoka huku akiwa na mavazi mengine ambayo yalimfanya kuonekana kama mtu wa mitaani, aliyepigwa na maisha.
Aliendelea kumfuatilia mpaka alipokwenda karibu na kituo cha mafuta cha TSN na kuingia kwenye mtaro mmoja. Chilo alibaki akishangaa, kile alichokuwa akikiona hakuweza kuyaamini macho yake, ilikuwaje Richard aingie humo? Alikuwa na jambo gani?
Hakutaka kuondoka, alibaki mahali hapo huku akiangalia ni kitu gani ambacho kingeendelea. Baada ya dakika chache akamuona Richard akitoka huku akiwa na mfuko ambao hakujua kwa ndani kulikuwa na nini.
“Hapana! Hapa kuna kitu!” alijisemea.
Hakutaka kumfuatilia, alichokifanya ni kuanza kuufuatilia mtaro ule kwa macho tu kwani kama angetaka kwenda kule alihisi kungekuwa na tatizo, aliufuatilia mpaka mahali kulipokuwa na pipa, akatulia kuona ni kitu gani kingetokea.
Baada ya dakika kadhaa akawaona wanaume wawili wakikimbia kuelekea kwenye pipa lile, wakaangalia ndani, kila mmoja alionekana kuchoka, haraka sana wakakimbia huku wakionekana kuwa na hasira, wakaanza kumtafuta mtu ambaye aliwachokoza lakini hawakupata kitu.
Baada ya kuona watu wale wameondoka, Chilo akaelekea kwenye pipa lile, macho yake yakatua kwenye karatasi nyingi kama uchafu, akazitoa ili kuangalia kulikuwa na nini, macho yake yakatua kwenye tundu kubwa lililokwenda mpaka kwenye mtaro, akabaki akishangaa.
Akapata picha kwamba ndani ya pipa lile kulikuwa na mfuko ambao Richard aliuchukua kwa siri, hakuuchukua kwa kulifuata lile pipa, bali alikwenda kule kupitia mtaro, bila shaka aliogopa kuonekana na watu wale waliokuwa wamesimama mbali muda mfupi uliopita.
“Kile ni kitu gani? Alibeba nini? Ni cha hawa watu ama cha nani? Kwa nini alitumia mtaro kwenda kukifuata?” alijiuliza maswali ambayo hayakuwa na majibu yoyote yale.
(Kufuatilia tukio lote hilo lilivyokuwa, limeandikwa kwa undani katika Kitabu cha Dili la Dola Bilioni Nne)
Je nini kitaendelea?