2007-05-17
Na Jackson Joseph
Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), jana waliwekwa tayari kukabiliana na vurugu zozote ambazo zingetokea, kufuatia kuwepo kwa taarifa kwamba, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya Mlimani, walipanga kukutana kujadili hatma ya wenzao 56 ambao bado wamesimamishwa masomo.
Magari aina ya Landrover Pick-up 110 ambayo mara nyingi hutumiwa na kikosi hicho, yalionekana yakiranda randa maeneo ya Chuo na yanayokizunguka.
Magari hayo yalipitapita huku na kule kwa mwendo wa taratibu yakiwa na askari waliokuwa wakionyesha dhahiri wanasubiri tu amri ya kuanza "kuwashughulikia" wanaofanya fujo.
Mbalia na Land Roer hizo, pia kulikuwa na magari makubwa ya maji na jingine ambalo inadhaniwa kuwa ni la kumwaga upupu.
Hata hivyo, askari hao hakuwataka kuongea na waandishi wetu kuzungumzia sababu ya kuyazunguka mara kwa mara maeneo ya chuo kikuu.
Wanafunzi walipanga kukutana jana saa 4:00 asubuhi eneo la Revolution Square, ambalo hutumiwa kwa ajili ya mikutano ya dharura, mara nyingi ikiitishwa na wanafunzi wenyewe, badala ya Serikali yao (DARUSO) ili kutoa madai kwa uongozi wa chuo.
Hata hivyo, uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, uliwasihi viongozi wa DARUSO kuwashawishi wanafunzi hao kuahirisha mkutano huo hadi jana saa 7:00 mchana, jambo ambalo walikubali.
Lakini baadaye, Makamu wa Rais wa DARUSO, Bi. Benedetta Rushahu aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, Uongozi wa Chuo ulishauri mkutano huo wa wanafunzi, uahirishwe hadi leo saa 11.00 jioni.
Alisema Uongozi wa Chuo umeomba muda huo kwa kuwa kamati ya nidhamu inaanza kikao leo saa 2:00 asubuhi kuwajadili wanafunzi hao waliofukuzwa.
Alisema hivyo uliona kuwa ni busara wanafunzi hao kukutana baada ya maamuzi ya kikao cha nidhamu kutolewa leo.
"Ndiyo sasa tunabandika tangazo la kuwajulisha wanafunzi kuwa mkutano wa Revolution Square, utafanyika kesho saa 11:00 jioni na umepewa baraka zote na uongozi wa chuo," alisema.
Wakati tangazo hilo linabandikwa saa 6:50 mchana, baadhi ya wanafunzi walikuwa tayari wamekusanyika katika eneo hilo huku mvua ikionyesha tayari kwa mkutano huo, lakini walitawanyika baada ya kusoma tangazo hilo.
Baadhi ya wanafunzi walisema matangazo ya mkutano wao uliotakiwa kufanyika jana saa 4:00 asubuhi, yaling?olewa na askari waliokuwepo chuoni hapo.
"Tunashangaa matangazo yote tuliyoweka kuwajulisha mkutano wa saa nne yameng?olewa na polisi na kisha Uongozi wa Chuo ukabandika ya kwao ya vitisho," alisema.
Tangazo lililotolewa jana na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma, Ushauri na Utafiti), Profesa Makenya Maboko katika mbao za matangazo, liliwaonya wanafunzi kuepuka mikusanyiko isiyoruhusiwa chuoni hapo kwani ni kinyume na taratibu za sheria ndogo za chuo.
Sambamba na tangazo hilo, pia kulikuwa na minong`ono kuwa kulikuwa na idadi kubwa ya watu wa usalama wa taifa wakifuatilia hali ya usalama chuoni hapo.
Bi. Benedetta alisema hatma ya wenzao 56 ambao wamekwishapewa barua za kutakiwa kufika kesho kujieleza itajulikana leo saa 9.00.
Alisema chochote kitakachojitokeza baada ya kikao hicho, Daruso watafahamishwa na taarifa zitatolewa kwa wanafunzi kupitia mbao za matangazo.
"Baada ya kamati ya nidhamu kukaa na kuwahoji wanafunzi hao 56 mmoja mmoja, ndipo uamuzi utatolewa, na saa 11:00 jioni tutakutana Revolution square wanafunzi wote," alisema.
Hata hivyo, alisema kama wenzao hawatarudishwa chuoni hapo, uongozi mzima wa Daruso na bunge lote litalazimika kujiuzulu.
Alisema watalazimika kufanya hivyo ili kuuachia uongozi wa chuo madaraka yote kwa kuwa hawaoni umuhimu wa wao kuwepo wakati wenzao hawapo.
"Tutakuwa tumewasiliti wenzetu ikiwa tutaendelea na masomo wakati wote tulikuwa pamoja kudai haki zetu," alisema.
Hata hivyo, alisema wana imani kuwa baada ya kikao hicho wenzao watarudishwa na kuendelea na masomo.
Katika barua walioandikiwa wanafunzi waliosimamishwa ambayo Nipashe ina nakala yake, wanatakiwa kujieleza kwa maandishi namna walivyoshiriki kwenye mgomo huo. Barua hizo waliziwasilisha jana.