ILIPOISHIA
Ester baada ya kurudi ndani kupeleka mikate aliyotumwa, alikuwa na donge zito moyoni juu ya kuficha siri ya kuonekana kwa kipenzi cha tajiri yake. Lakini alijitahidi kuificha siri ile kusubiri siku ambayo Ambe angekuja dukani kuonana na Koleta.
ENDELEA NAYO
Siku-ya pili wakiwa dukani wakifanya biashara Koleta alimwita, baada ya kumsogelea alimweleza kitu:
Ester eti unamuonaje Jose kweli anafaa kumkabidhi moyo wangu?
Mmh! Dada mbona swali gumu, Ester aliruka mtego.
Siyo gumu kwa vile hata wewe unamuona na bado kama siku mbili anivishe pete ya uchumba.
Dada mpaka mnakubaliana uliridhika naye.
Ni kweli, lakini ndoto ya jana ilimtoa kabisa Jose moyoni mwangu.
Ndoto! Umeota nini?
Nimeota nimekwenda shule kumuona Ambe Jr, sikuamini kumkuta yupo na baba yake kwa kweli nilipata mshtuko wa ajabu. Nilimkumbatia kwa furaha kubwa kwa mara ya kwanza kumuona mpenzi wangu aliyepotea muda mrefu.
Kilichoniumiza moyo wangu ni kauli ya ndotoni aliyoisema Ambe senior kuwa ninataka kufanya nini, eti nimemsaliti kwa kukubali kuolewa na mwingine ikiwa matatizo yote sababu ni mimi.
Niliposhtuka usingizini nililia sana na kuamini kabisa sababu ya kufungwa gerezani kwa Ambe kunatokana na mimi. Kwa kweli imeniuma sana, si bora ningejua yupo wapi ili nijue ninayemsubiri yupo wapi, kwa kweli ndoto ile imenipa wakati mgumu sana, Koleta alisema huku akifuta machozi.
Mmh! Pole sana dada.
Ndiyo maana nikakuuliza unamuonaje shemeji yako mpya.
Kabla ya kukujibu ukisikia Ambe yupo utafanya nini?
Sina budi kubadili msimamo wangu, nampenda sana Ambe pamoja na maneno ya baba ya kunikatisha tamaa ili nimchukie, lakini najua sababu yote ni yeye aliyetengeneza mazingira yale ili tu nisioane na mpenzi wangu.
Mmh! Lakini
tuache, Ester alitaka kutoboa siri ya kumuona Ambe na waliyozungumza.
Tuache nini Ester kumbuka kipindi hiki nahitaji msaada wako kuliko kitu kingine, najiuliza huenda ndoto ina ukweli naolewa Ambe anatokea nitauweka wapi uso wangu? Koleta alisema kwa sauti iliyokosa majibu ya maswali ambayo yalitegemea sana uwezo wa Ester.
Ester pamoja na kukatazwa na Ambe aliona ni ujinga kukaa kimya- kwa kuamini huenda akachelewa kutokea na kukuta Koleta kaolewa.
Dada nilikuwa nakuomba umsubiri Ambe.
Sawa nitamsubiri mpaka lini, hajulikani amekufa au yupo hai au amekamatwa tena na kunyongwa.
Ambe ni mzima wa afya.
Mzima! Umemuona wapi?
Tena hukujua, jana usiku kuna mtu aligonga mlango wa gari pale getini ili ufungue lakini hukusimama uliliingiza mpaka ndani na wala hukutoka tena nje.
Eeh! Nimekumbuka kuna mtu aligonga mlango wa gari yangu.
Basi yule alikuwa Ambe.
Muongo! Umejuaje?
Ester aliamua kuifungua siri aliyokatazwa na Ambe, Koleta hakuamini alijilaumu kwa kitendo cha kutomsikiliza.
Ester unayosema ni kweli au uongo ili kunirusha roho.
Mimi nimejuaje hayo, kuna mtu aligonga gari lako hata alipotaka kuingia ndani alizuiwa na mlinzi. Tena kama ungewahi kutoka ndani ya gari ungemsikia akikuita kwa sauti ya juu.
Mungu wangu! Ambe atanielewaje?
Hawezi kukuelewa vibaya kwa vile hamkuwa na miadi ya kuonana.
Kwa nini hukunifuata kuja kumuona.
Alikataa.
Alimuulizia mwanaye.
Alimuulizia.
Ulimjibu nini?
Nilimwambia yupo katika hali nzuri.
Afya yake ipo vipi, amekonda sana?
Wala tena ana afya nzuri huwezi kuamini utadhania kama hakuwa gerezani.
Kwa nini alikataa kuonana na mimi, au amenichukia kwa ajili ya baba kusababisha kufungwa.
Bado Ambe anakupenda tena anakupenda sana, tena kanihakikishia kuna siku atarudi mjini na kufunga ndoa na wewe.
Eti? kauli ile ilimshtua Koleta.
Amesema atarudi mjini na kufunga ndoa na wewe.
Ester unayosema ni kunifurahisha au kweli?
Sijawahi kukutania pia siwezi kuleta utani katika jambo zito kama hili.
Amesema anakaa wapi?
Hakusema, lakini inaonesha yupo nje ya mji, hata mavazi yao kama watu wa machimbo, pia wamefuga nywele na ndevu nyingi.
Alikuwa na nani?
Na rafiki yake mmoja.
Mmh! Sasa huu mtihani mwingine.
Mtihani gani tena?
Si kuhusu mchumba na Ambe.
Mwenye mali karudi hapo kuna mtihani gani?
Na kweli, sasa sijui atakuja lini?
Kwa vile nimemuelekeza huenda anataka kukufanyia suprise.
Yaani siamini, nitaamini baada ya kumuona, kwa nini hakutaka kuniona au alijua simpendi tena, nisipompenda yeye nimpende nani.
Wakati huo mwanaye Ambe Jr alikuwa akiingia na bibi yake, alimuangalia kwa muda na kukumbuka taarifa za kuonekana kwa baba yake. Aliomba kimoyomoyo mwanaye amuone baba yake hata mara moja kwani alishakata tamaa ya mwanaye kumuona baba yake.
******
Usiku wa siku ile kama kawaida- Ambe na Mabina walifika mji aliokuwa akiishi mzee Samjo mtu aliyesababisha kifo cha baba yake Mabina na kufungwa kwake ili kujua nini kinaendelea baada ya muda mrefu kupita bila taarifa ya nini kinaendelea.
Baada ya kufika nje ya geti la nyumba ya mzee Samjo lililokuwa linalindwa na walinzi wa kampuni za ulinzi.
Sasa tutafanyaje? Ambe alimuuliza Mabina aliyekuwa ametulia akijaribu cha kufanya.
Cha muhimu kujua kama bado yupo na anapatikanaje?
Hilo wazo zuri.
Hapa ni kumfuata mlinzi atatusaidia tu.
Walisogea hadi getini na kugonga geti, baada ya muda alitoka mlinzi.
Niwasaidie nini?
Mzee Samjo yupo?
Ninyi kina nani?
Kaka badala ya kutujibu unatuuliza swali.
Lazima niwajue kabla ya kuwajibu.
Mpaka tunafika hapa tuna shida naye tumevuka nyumba ngapi?
Yupo, mnasemaje?
Tulitaka kujua hilo, mengine tutazungumza naye kwenye simu, asante kwa msaada wako.
Waliagana na yule mlinzi na kurudi pembeni kupanga jinsi ya kuingia ndani ya nyumba ya mzee Samjo.
Sasa tufanye nini? Ambe aliuliza.
Nilikuwa na wazo moja la kuja kufanya mauaji akiwa mlangoni kwake.
Sasa si utakuwa umefanya kazi bure.
Kivipi?
Ukimuua bila kupata vyako utapoteza vitu vyako vingi.
Ambe, nikimuua kila kitu kitarudi kimoja baada ya kingine.
Kivipi?
Nitaua mmoja baada ya mwingine mpaka mali zangu zipatikane.
Sasa utamuua nani?
Ukoo mzima.
Huoni utakuwa unaingia katika vita nyingine na serikali?
-
Ambe kwanza nikifanikiwa kumuua mzee Samjo moyo wangu utakuwa kwatu hata nikikosa vitu vyangu.
Unajua unachotaka kufanya ni kitu cha kubahatisha unaweza kumkosa mzee Samjo na wewe kufa kibudu.
Una maana gani?
Kwa nini tusifanye jambo kisomi zaidi.
Tufanyeje?
Inatakiwa tukiweza kupenya tuingie mpaka ndani kwa mzee Samjo kisha akuone upo hai na kumweleza akulipe haki yako kwa hiyali yake, kama atakataa tutaanza kuiteka familia yake na kumuomba atulipe haki yako na akikaidi basi tutarudisha mwili bila uhai.
Mmh! Mbona hayo mawazo hukuwa nayo siku tulipokwenda ukweni?
Hiyo ndiyo faida ya kuwa wawili mawazo yangu mwenyewe ningeweza kupotea.
Lakini huoni mpango wako ni njia ndefu inayohitaji mtaji mkubwa pia tuwe na vyombo vya kufanyia kazi japo ni mzuri sana.
Kama huo ni wa njia ndefu tena wa gharama basi tunangalie mwingine ambao utafanikiwa kulipa kisasi- pia kupata haki yako, unajua nini?
Nitajuaje bila kuniambia.
Mpaka sasa hivi kila mtu anajua wewe ni marehemu.
Kama wanajua- mimi marehemu inasaidia nini?
Ni wewe kuvaa vizuri na kwenda nyumbani kwa mzee Samjo nina imani akikuona atachanginyikiwa na hapo kumweleza ukweli kuwa amefufuka kudai haki yako na kumweleza huta kufa mara mbili tena kwa kujiamini mweleza unaitaka siku gani akikupa kinafuata kifo chake.
Na asipokubali kutoa?
Tunamuua popote.
Unaweza kufanya mauaji wewe?
Hilo jibu, hivi nimepanga kumuulia mbali mzee Mtoe.
Unajua sikuelewi unasema bado unamtaka mpenzi wako, atakukubali ukimuua baba yake?
Kuua kuko pale pale hata kwa siri lakini lazima nimtie adabu.
Mfano mpenzi wako akiwa tayari kuwa na wewe na kukuomba usimuue baba yake utafanya nini?
Hebu kwanza kujadili hili la kwako tulipatie ufumbuzi tulichanganya mada mbili kwa mara moja.
Najua jibu lake ni gumu, haya tuendelee na mipango yetu.
Tuliishia wapi vile unajue ulivuruga mipango yangu.
Kama atakataa kutoa mali tumuue popote, nimekuuliza ukasema kuua kwako si tatizo.
Nataka tufanye mambo kitaalamu, tumeona kwenye sinema watu wanavyodai fedha zao na polisi hawawakamati na mwisho wa siku wanapata vitu vyao.
Ambe kuigiza kuna tofauti na tukio la kweli.
Mabina kuna matukio mangapi ya kweli- yametokea na watu kusikia wakisema tukio lilikuwa kama muvi.
Sisi tumejiandaa kufanya hayo?
Kwani hao wana miguu na mikono- mingapi?
Unajua kutumia siraha?
Mimi ni mtaalamu wa mapigano ya mikono nikichanganya na uwezo wako wa siraha litakuwa jeshi kamili.
Unaweza kuwa na uwezo wa mapigano ya mikono lakini huna moyo wa ujasiri.
Maisha niliyoishi porini nina roho kama shetani.
Kama una roho kama shetani mbona mapenzi yanakuendesha.
Kaka mapenzi kitu kingine, huyo Samson kwenye mapenzi alitepeta kwa Delilah, huyu simba mkali lakini kwenye mapenzi huwa mpole. Samson si kitu kwa Delilah lakini katika suala la kujitetea Samson aliua simba kwa mkono.
Nimekuelewa, kwani ulivyokuwa gerezani na ulivyotoka ilikuwa tofauti kabisa nimekukuta unafanya kazi kama katapira.
Nimeamini mwanadamu huweza kuishi maisha ya aina yoyote sikuwaza kuna siku nitaishi kama mnyama na kuyazoea maisha na kuyaona ya kawaida.
Kwa hiyo?
Nataka tujipanga wiki ijayo baada ya kuonana na Koleta tunavamia kwa mzee Samjo.
Unajua tuna bunduki na kazi yetu inataka inataka siraha ndogo.
Mmh! Nimepata wazo acha nionane na Koleta nitakupa jibu la uhakika.
Hiyo siraha ataitoa Koleta?
Nimekwambia ngoja nionane naye nijue kwanza msimamo wake kwangu kisha tutamalizia na la kwako.
Hakuna tatizo.
Walitafuta usafiri na kurudi kijijini kwao kujipanga kwa ajili ya siku ya pili ya kwenda kuonana na Koleta.