Joto la mapenzi

Daudi1

JF-Expert Member
Dec 14, 2013
8,799
8,706
JOTO LA MAPENZI-1

Kutokana na maji kuingia kwa kasi katika shimo alilokuwemo kijana ambe yalimzindua kutokana na kuteleza na kudondokea humo wakati wakiwakimbia askari magereza na kupoteza fahamu. Ilikuwa katika jaribio la kutoroka kwa bahati mbaya aliangukia kwenye shimo. Rafiki yake Aloys Mabina hakutaka kumwacha alijitahidi kumwamsha ili amtoe shimoni, lakini aligundua amepoteza fahamu hivyo asingeweza kuendelea kuwepo eneo lile kwa kuhofia askari wanaowatafuta kumkuta eneo lile. Aliona kama angeendelea kuwepo pale lazima askari wanaowakimbiza wangefika eneo lile na kumkamata. Hivyo aliendelea na safari kuwakimbia na kumwacha rafiki yake ndani ya shimo.

Ambe baada ya kuzinduka taratibu alijitoa kwenye shimo huku mvua ikiendelea kupiga kwa kasi, shimo halikuwa refu sana hiyo ilimsaidia kutoka nje kwa urahisi. Alijikuta akiwa njia panda na kushindwa afanye nini arudi gerezani au aendelee kukimbia. Wazo la kurudi lilimtisha kidogo kutokana na kuogopa kuulizwa juu ya mwenzake Mabina aliyekuwa swahiba wake mkubwa gerezani. Walikuwa wamefanya tukio baya la kutoroka na silaha baada ya kumkaba askari magereza na kukimbia na bunduki ambayo ilikuwa inakwenda kutimiza azma ya rafiki yake Mabina ya kuua ili kutimiza kisasi.

Ambe na Mabina walikuwa na matukio ya kufanana yaliyowafanya waingie gerezani na kila mmoja kufungwa miaka saba. Lakini kila mmoja alikuwa na njia yake iliyomwingiza gerezani. Mabina aliapa akitoka lazima alipe kisasi kwa kuwaua wabaya wake na ndiyo sababu ya kutoroka na silaha. Lakini ilikuwa tofauti kwa Ambe, pamoja na kufanyiwa unyama mkubwa lakini aliapa hatalipiza zaidi ya kumuachia Mungu. Mabina hakuwa hivyo hakutaka kabisa kusikia eti mtu anakutendea unyama unamshtakia Mungu wakati una uwezo wa kulipa kisasi.

Baada ya kumweleza rafiki yake sababu iliyomwingiza gerezani ambayo ilikuwa ni uonevu aliapa akitoka lazima aue tena kwa risasi. Ambe pamoja na kumsihi rafiki yake asilipe kisasi hakusikilizwa. Mabina alisema toka alipofanyiwa unyama ule na mwisho wa yote kufungwa bila kosa miaka saba. Asingemsamehe mtu aliapa lazima atalipa kisasi tena cha damu. Ambe akiwa anatoka kwenye shimo huku mvua ikiendelea kumnyeshea, moyoni alijikuta akijilaumu maamuzi ya rafiki yake ya kumpiga askari na kuichukua bunduki ambayo alimwambia ndiyo silaha aliyoitafuta kwa muda mrefu.

Katika muda wote waliokuwa gerezani Mabina aliapa akitoka gerezani lazima aue ili anyongwe na kuamini kile ndicho kitakuwa kifungo cha kweli kwake. Matatizo ya rafiki yake hayakuwa na tofauti na yake ya kutendewa unyama na familia ya rafiki yake wa kike na mwisho wa yote kufungwa gerezani miaka saba bila kosa lolote kisa mapenzi.Tofauti ya kuingia gerezani kwa Ambe na Mabina ilitofautiana, Mabina alitangulia kuingia kwa mwezi mmoja hivyo hata muda wao wa kutoka ungepishana kwa mwezi mmoja.Ambe akiwa bado yupo njia panda aelekee wapi kwa vile pori lile lilikuwa geni kwake japokuwa hakutaka kurudi gerezani.

Alikumbuka kauli za rafiki yake baada ya kumsimulia mkasa uliomwingiza gerezani: "Ambe nakuhakikishia siwezi kuwasamehe wote walionifanyia unyama, hawezi kutudhulumu mali yetu, wamuue baba yangu na mimi kufungwa miaka saba bila kosa kisa tu nilikuwa nikijua mengi juu ya ugomvi wa baba na jirani yake juu ya mpaka wa nyumba.

"Najua sina uwezo wa kipesa, lakini lazima nimuue kwa risasi kama alivyomuua baba yangu."
"Utapata wapi bunduki?" Ambe alimuuliza rafiki yake.
"Hapahapa gerezani." Mabina alijibu kwa kujiamini.
"Hapahapa gerezani! Utaipata vipi?" Ambe alishtuka.
"Utaona tu."

Siku ilipofika walikuwa kwenye kazi za nje kutokana na kubakiza muda mchache wa kuwepo gerezani. Wafungwa wengi walipewa kazi za nje, yeye akiwa amebakiza miezi miwili na Mabina mwezi mmoja wa kutoka gerezani. Wakiwa eneo lililojificha walilopangiwa Ambe na Mabina kukata miti huku askari magereza akiwa mbali kidogo.Mabina alimwambia Ambe amwite askari kwa sauti ya juu, naye alifanya hivyo kwa kupaza sauti kumwita askari.

Askari alifika haraka eneo aliloitiwa alipofika alishangaa kumuona Mabina akigaragara chini kama mtu aliyekuwa akiumwa kitu. alipomuuliza Ambe ambaye hakuwa na jibu. Alipomwinamia ili kutaka kujua anaumwa nini, Mabina alinyanyuka na kumkaba askari huku Ambe akishangaa. Baada ya kumkaba mpaka kupoteza fahamu alichukua bunduki na kumlazimisha Ambe waondoke."Twende wapi?" Ambe aliuliza.

"Ukibaki shauri yako utaulizwa nimekwenda wapi, najua hautakuwa na jibu kwa vile sisi ni marafiki wakubwa watajua nawe unahusika hivyo utaozea gerezani."Ambe alijikuta akimfuata Mabina aliyeanza kukimbia kuingia porini, kwa vile hakuwa amejiandaa baada ya mwendo wa saa tatu bila kupumzika, pumzi ilikata na kujikuta akianza kuona kizunguzungu kwa bahati mbaya pembeni na sehemu aliyokuwa amesimama kulikuwa na shimo aliangukia ndani.

Habari ya siku nyingi wanajamvi, poleni na majukumu ya kujenga taifa, baada ya kupotea muda mrefu nimerudi tena, Kwa hisani ya GLOBAL PUBLISHER kwa wale wapenzi wa mikasa ya mapenzi tupate uhondo huu, kuna mafundisho mengi ndani ya mkasa huu ungana nami muongojazi wako mpaka mwisho wa safari karibuni
 
JOTO LA MAPENZI-2

ILIPOISHIA:

Ambe alijikuta akimfuata Mabina aliyeanza kukimbia kuingia porini, kwa vile hakuwa amejiandaa baada ya mwendo wa masaa matatu bila kupumzika pumzi ilikata na kujikuta akianza kuona kizunguzungu kwa bahati mbaya pembeni na sehemu aliyokuwa amesimama kulikuwa na shimo aliangukia ndani.
SASA ENDELEA…


Mabina alijaribu kumsaidia kumtoa shimoni lakini aligundua amepoteza fahamu hakuwa na jinsi zaidi ya kumwacha ili asije kukamatwa na askari watakaokuwa wakimtafuta. Baada ya saa saba kupita mvua zilianza kunyesha, maji ya mvua yaliyokuwa yakiingia shimoni ndiyo yaliyomzindua Ambe.


Muda aliotoka shimoni ilikuwa usiku kiza kilianza kuimeza nuru ya mchana. Alikumbuka maneno ya Mabina kuwa kama atakamatwa atafia gerezani, aliamua kuendelea na safari yake japo hakujua anaelekea sehemu gani. Wakati huo mvua ilikuwa ikiendelea kunyesha, alijiona ni kiumbe kilichoandamwa na mikosi baada ya kunyang'anywa mchumba wake na kuozwa mtu mwingine bila idhini yake bado ameishia kufungwa gerezani.


Akiamini baada ya miezi miwili atakuwa uraiani na kuuapia moyo wake pamoja na yote aliyotendewa aliusihi moyo wake usilipe kisasi. Lakini mtu aliyemtegemea kuwa rafiki na msiri wake, mwisho wa siku amemwingiza kwenye matatizo makubwa ya kutafutwa na serikali kwa makosa matatu kuua kutoroka gerezani na wizi wa silaha.


Moyo ulimuuma na kutamani kulia, alijiuliza pale alipo atatokea wapi na atawezaje kuikwepa serikali ambayo ina mkono mrefu. Alijua kama rafiki yake Mabina atatimiza azma yake ya kuua na kunyongwa atakuwa ametimiza kile alichokipanga kwa muda mrefu.


Lakini kwa upande wake, baada ya kifungo alipanga kuishi maisha mapya.
Alizidi kutembea kuingia ndani ya msitu ambao kwa upande wake ulikuwa mgeni kwake. Ghafla alijikuta akipata wazo la kijasiri la kurudi gerezani kuwaeleza ukweli kuwa si yeye bali rafiki yake ambaye wamejuana gerezani tu.


Baada ya kutembea kwa hatua kama kumi alishangaa kuona mianga ya tochi zaidi ya nne ikisogea sehemu aliyokuwepo. Wasiwasi ulimjaa na kushindwa kuelewa wale ni kina nani na mbona kama watu wanaotafuta kitu. Mwanga ulipokuwa ukimkaribia aliamua kujificha kwa kupanda juu ya mti uliokuwa karibu.


Alitulia juu ya mti ili watu wale wapite kwa kuhofia huenda ni askari waliokuwa wakiwatafuta. Watu wale walipofika chini ya mti ule aligundua kweli walikuwa askari magereza ambao walionesha walipita kitambo kuwatafuta na kumpita alipokuwa ameangukia kwenye shimo na kupoteza fahamu.
Aliwasikia wakizungumza:


"Tumefanya kazi ya ziada bila hivyo tungekufa wote."
"Lakini katutia hasara kifo cha mtu mmoja hakilingani na askari wetu wawili."
"Lakini rafiki yake ndiye anaonekana amekimbia na silaha lazima tumsake kwa udi na uvumba."


Maneno yale kidogo yamfanye Ambe aanguke juu ya mti aliokuwa amepanda, aliamini kabisa rafiki yake kipenzi Mabina ameuawa na kuwaua askari magereza wawili. Kilichomshangaza ni kauli yao kuhusu kutoonekana kwa bunduki aliyochukua Mabina. Ile ilimshtua kidogo na kujiuliza rafiki yake atakuwa ameificha wapi.


Kauli ya kwanza anatafutwa yeye ambaye ndiye anayesadikiwa ameficha silaha ilimvunja nguvu sana na kuamini kama atarudi gerezani basi atakuwa amejiingiza mwenyewe kwenye kinywa cha mamba.


Alitulia juu ya mti akimuomba Mungu amuepushie mbali balaa lile, askari wale walichelewa chini ya mti ule kutokana na mmoja kujisaidia haja ndogo, baada ya kumaliza waliendelea na safari yao. Ambe hakuteremka mpaka nusu saa na kuona hakuna haja ya kwenda kujisalimisha baada ya kuonekana kuwa ndiye aliyeficha silaha hivyo wasingemuelewa.


Kila lililokuwa mbele yake aliona ni mtihani mzito ambao kwake aliamini haukuwa na jibu la mara moja. Muda ulikuwa umekwenda na kiza kilikuwa kimeingia ambacho hakikuwa kikali sana, mwezi ulikuwa umemezwa kidogo na mawingu. Hali ile ilimfanya aone kidogo sehemu aliyokuwa akienda.


Alitembea kuelekea mbele bila kujua anakwenda wapi kutokana na eneo lote kuwa mbuga yenye miti mingi. Kwa vile hakuwa na saa hakujua muda ule ilikuwa saa ngapi , alipata ujasiri na kuamua kusonga mbele na kuwa tayari kwa lolote kwa kuamini hakufanya jambo lolote baya na Mungu angemsaidia.


Alitembea usiku kucha na kujikuta akichoka sana kutokana na kutembea kwenye baridi kali kutokana na mvua kunyesha sehemu kubwa. Sehemu moja iliyokuwa na bonde alisikia watu wakizungumza:
"Sasa jamani tutakaa mpaka saa ngapi tukitafuta mtu tusiyejua amekimbilia wapi?" Ilikuwa kauli iliyoonesha kumbe askari wengi walikuwa wamesambaa eneo kubwa la pori lile kumtafuta.


"Hivi angalieni tumeshapoteza watu wawili kwa mtu asiye na silaha sasa mwenye silaha si tutakufa wote. Kama mtu ametoroka alitakiwa atafutwe kwa njia nyingine," alimsikia askari mwingine akizungumza.


Ambe alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kugundua anatafutwa kila kona na kama atakamatwa atakufa kwa kipigo kutoka kwa askari wenye hasira hasa baada ya kuuawa askari wawili kutokana na maelezo yao.
 
JOTO LA MAPENZI-3

ILIPOISHIA

Ambe alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kugundua anatafutwa kila kona kama atakamatwa atakufa kwa kipigo kutoka kwa askari wenye hasira hasa baada ya kuuawa askari wawili kutokana na maelezo yao.
ENDELEA NAYO...


Alijiuliza kote alipopita huenda aliwapita wengine ambao walikuwa wamepitiwa na usingizi hivyo kupita bila kumuona.


Kauli za wale askari zilionesha wameshakata tamaa wapo pale kwa kutimiza wajibu lakini waliamini hawawezi kumuona. Aliachana na njia iliyokuwa na sauti ya askari na kuanza kuifuata iliyokuwa ikielekea bondeni ambako kulikuwa kunatisha sana.


Lakini kwa ujasiri mkubwa aliteremka hadi bondeni ambako alikutana na mto uliokuwa ukipitisha maji. Alihofia kuvuka kwa kuingia kwa vile hakujua kina cha maji yale. Aliamua kutembea pembeni ya mto huku akizidi kupigwa na baridi kali la usiku ule, moyoni alijiuliza nini hasa chanzo cha yeye kuingia kwenye matatizo mazito kila kukicha.


Lakini alijipa moyo kwa kuamini si yeye wa kwanza kutokewa na matatizo kama yale. Pia aliamini mwanadamu hasa mwanaume ameumbwa ili kukabiliana na matatizo. Hata kama angelia machozi ya damu hakuna ambaye angemuelewa au angemsaidia.


Aliendelea kutembea huku akiwa makini akisikiliza sauti au kitu chochote kitakachohatarisha maisha yake. Kwa mara ya kwanza alijifananisha na gaidi lililotoroka kwenye gereza la Guantanamo. Alijipa moyo ili kuhakikisha anayalinda maisha yake kwa hali yoyote ile na hakuwa tayari kukamatwa kikondoo.
Aliyakumbuka mafunzo aliyochukua JKT wakati akimaliza kidato cha sita, aliamini kabisa mafunzo yale muda ule ndiyo yatakayomsaidia.


Alivunja kipande cha mti na kukigeuza kama silaha kwa kitu chochote kitakachomtokea mbele.
Kila hatua aliyopiga kwenda mbele ndivyo ujasiri ulivyojaa moyoni mwake. Kutokana na kutembea ambali mrefu kiu kikali kilimshika na kujikuta hana jinsi zaidi ya kunywa maji yale ya mto bila kujua yapo katika usalama gani.


Baada ya mwendo wa saa nzima alijikuta akitokea kwenye njia ya kuvukia upande wa pili iliyokuwa na daraja la mti mmoja. Alivuka na kuendelea na safari yake ya kuwakimbia askari Magereza, kabla hajachanganya miguu baada ya kuvuka daraja alisikia mtu akimuamsha mwenzake.
"Saidi...Saidi."


"Nini Joe? Wewe hebu niache nilale."
"Nimesikia kama sauti ya miguu ya mtu anapita."
"Sasa akipita sisi anatuhusu nini?"


Kauli ile ilimfanya Ambe ajifiche nyuma ya kichaka kidogo huku akishikilia sawasawa kipande chake cha mti na kuwa tayari kupambana na yeyote atakayejitokeza mbele yake. Aliamini kama atalegea naye kifo chake kitakuwa kama cha rafiki yake Mabina.


Hakuwa tayari kufa kikondoo kwa kujua akikamatwa hata akijitetea vipi hawatamwelewa kwa vile Mabina hakukutwa na silaha, lazima wangemtesa ili atoe silaha asiyoijua ipo wapi, hivyo angeweza kupewa kilema cha maisha au kuuawa kifo cha mateso makali.


Akiwa ameshikilia silaha yake tayari kupambana na atakayekuja mbele yake, aliendelea kusikia mazungumzo ambayo alijua kabisa ni ya askari waliotumwa kumsaka.
"Kwa hapa tunafanya nini?" Mmoja aliuliza.


"Tumekuja kumsaka Ambe baada ya Mabina aliyemkaba John na kutoroka na silaha pamoja na rafiki yake, ambaye ndiye aliyekimbia na silaha."
"Sasa kwa nini tusifuatilie hizo sauti za miguu?"
"Wewe hujipendi, Mabina hakuwa na silaha kaua wawili huyo Ambe mwenye silaha si atatuua wote. Inaonesha wazi jamaa wale ni wazoefu kutumia silaha za moto."


"Lakini kweli, sasa tufanyeje?"
"Kwa vile hatujamsumbua hata kama ni yeye wee tulale ili kesho tuwaeleze tumemkosa. Sisi tunateseka mvua yetu baridi ya usiku mzima yetu, wakubwa wamekumbatia wake zao. Mimi hata nikikutana naye namwambia pita baba sina ubaya na wewe."


Kauli ile japo ilitaka kumchekesha Ambe lakini aliamini kila kiumbe kinapenda kuishi maisha marefu. Hakutaka kukubaliana na kauli yao kwa kujiamini kutembea kifua mbele. Aliamua kutembelea magoti kwenye nyasi zilizokuwa na majimaji kutokana na mvua iliyokuwa imekatika muda si mrefu kuondoka eneo lile ambalo lilionyesha huenda ndipo ulikuwa mpaka wa magereza na sehemu za wananchi wa kawaida.


Alitembea kwa magoti kwa mwendo wa dakika kumi kisha alinyanyuka na kuendelea na safari yake. Sehemu aliyoingia ilionesha wazi ni eneo tofauti na magereza kulikuwa na mashamba ya watu. Kutokana na eneo la mashamba kuwa dogo tofauti na mashamba ya magereza yenye eneo kubwa sana.


Baada ya kutembea mwendo wa dakika ishrini alianza kuona kwa mbali nyumba mojamoja zilizo mbalimbali. Wakati huo mwezi ulianza kumezwa na mawingu kuonesha muda umekwenda sana. Kibaridi cha kukaribisha alfajiri kilimpuliza na kuonesha kumekaribia kupambazuka.


Japokuwa hakujua hatima yake lakini moyo wake ulipata faraja kuona nyumba za watu. Wakati akianza kuyaacha mashamba na kusogelea nyumba moja iliyokuwa karibu naye. Kutokana na kiza kilichokuwa kimetokea kwa ajili ya mwezi kumezwa na mawingu.Hakuweza kuona anapita sehemu gani kwa kukanyaga majani ya pembeni ya shamba.
 
JOTO LA MAPENZI-4

ILIPOISHIA...

Hakuweza kuona anapita sehemu gani kwa kukanyaga majani ya pembeni ya shamba.
ENDELEA...


Bila kujua anapita wapi alijikuta akikanyaga mwiba uliomtoboa vibaya na kumfanya ahisi maumivu makali. Alichechemea kutoka kwenye miba ambayo ilionesha ilipandwa kwenye mpaka wa shamba na kuingia kwenye barabara.


Alikaa chini ili kuutoa mwiba uliokuwa umemuingia sana mguuni kwa ujasiri mkubwa huku akiuma meno aliutoa na kufanya atokwe na damu nyingi. Ilibidi achane shati lake na kujifunga kwenye jeraha ili kupunguza damu isitoke kwa wingi.


Alitumia kipande cha mti alichokitumia kama silaha, kama nyenzo ya kumsaidia kutembelea kutokana na kuwa na maumivu makali ya mguu. Alijikongoja kuelekea kwenye makazi ya watu huku akimuomba Mungu askari wasitokee kwani wangemuokota kwa ulaini kama maiti ndani ya maji. Baada ya mwendo mfupi wa shida alitokea sehemu iliyokuwa na nyumba mbili zilizoezekwa na nyasi.


Kila hatua aliyojitahidi kupiga ili kuingia eneo lile hali ilizidi kuwa mbaya, maumivu ya mguu yalizidi kuwa makali sana na kumfanya ashindwe kutembea. Lakini alijitahidi kuingia eneo la nyumba ile ili hata akizidiwa apate huduma. Kizunguzungu kilikuwa kikali kutokana na njaa, uchovu na maumivu ya mguu alianguka chini na kupoteza fahamu.


***
Ambe aliposhtuka alijikuta amelala kwenye kitanda cha kamba katika chumba chenye mwanga hafifu. Akiwa anajiuliza pale ni wapi alisikia sauti ya watu wakibisha hodi kwenye nyumba ile.
"Karibuni," sauti kutoka mule ndani ilikaribisha.
"Shikamoo babu."


"Marahaba, niwasaidie nini wajukuu zangu?"
"Tunaomba kuuliza, hujamuona mtu mwenye mavazi ya kifungwa akipita eneo hili?"
Kauli ile ilimshtua Ambe aliyekuwa bado amejilaza kwenye kitanda cha kamba na kujua amekwisha baada ya askari kutokata tamaa ya kumtafuta na kuamua kuingia vijiji vya karibu na gereza kumtafuta. Moyo ulimwenda mbio na kujua amekwisha lazima babu atasema ukweli kuwa yumo ndani.
"Mmh! Ametoroka lini?"


"Jana mchana."
"Sasa toka jana mchana leo ndiyo mje kumtafuta huku? Hamuoni ni uzembe, jana yote mlikuwa wapi?"
"Mzee hatukuja kuulizwa maswali tueleze umemuona au la," sauti ya askari magereza ilikuwa kali.
"Si kazi yangu kuangalia watu wanaopita kijijini, sijamuona."


Ambe hakuamini majibu ya mwenyeji wa nyumba ile kukataa hajamuona, alijiuliza kwa nini hakuwaeleza ukweli. Aliendelea kumuomba Mungu amwepushe na balaa lile zito ambalo aliamini kama ataangukia mikononi kwa chombo cha dola basi jina lake litabakia historia midomoni mwa watu.
Baada ya muda mwenyeji wake alirudi ndani na kusogea kwenye kitanda alichokuwa amelala.
"Kijana..kijana."


"Naam babu," Ambe aliitikia bila kujua mwenyeji wake ana umri gani japo alisikia akiitwa babu na askari magereza.
"Umeamka?"
"Ndiyo babu."
"Ni kweli wanakutafuta wewe?"


"Ndiyo babu," Ambe aliogopa kumdanganya.
"Siwezi kukuhukumu lolote zaidi ya kukusaidia kwanza ndipo tuzungumze, pia siwezi kukurudisha gerezani ukitoka hapa maisha yako utayajua mwenyewe."
"Asante babu, ila nahisi nina mikosi mingi sana, kila siku mpya kwangu imeandamwa na mikosi, dhuluma, uonevu ndivyo vilivyotawala maisha yangu. Nina imani nikikamatwa naweza hata kunyongwa bila kosa," Ambe alisema kwa uchungu.


"Inaonesha una mengi moyoni mwako ndiyo yaliyonisukuma kubeba jukumu la kuwaficha askari ili nipate kitu chochote kitakachoweza kunisaidia."
"Mzee ni hadithi ndefu naomba kama kuna chakula unipe kwanza maana nina njaa kama kidonda."
"Uji upo tayari nitakupa sasa hivi, amka ukae."


Ambe aliamka na kuketi kwenye kitanda, kilichomshangaza mguu wake ulikuwa hauna maumivu kabisa. Kukanyaga aliogopa lakini mwenyeji wake alimweleza:
"Kanyaga tu usiogope nimekuwekea dawa umetoa sumu ya mwiba uliokanyaga."
"Nashukuru mzee wangu."


"Kwa vile unatafutwa na askari bado wapo maeneo haya, usitoke nje, kutoka kwako kutakuwa usiku tu."
"Sawa babu."
Mzee alitoka nje na kurudi na bakuli lililokuwa na uji wa ukwaju, kutokana na kuwa na njaa alishambulia uji wote. Mwenyeji wake aliyeonekana mtu mzima wa miaka zaidi ya sabini alimwacha apumzike na yeye kuendelea na kazi zake.
***
Majira ya usiku baada ya Ambe kuamka, mwenyeji wake aliyefahamika kwa jina la Yamungu alitaka kujua nini kilichomsibu kijana yule kutoroka gerezani na kusababisha msako mkubwa kila kona. Ilikuwa baada ya kupata chakula cha usiku.


"Mmh! Mjukuu wangu hebu nipe kisa na mkasa kilichokufanya uwe katika hali hii japo inaonesha jinsi gani ulivyo na maumivu makali moyoni mwako."
"Kwanza kabla ya kuyasema yaliyonisibu sina budi kutanguliza shukrani zangu za dhati kwako mzee wangu kwa kuniokota na kunipa tiba pia kuweza kunificha ili nisichukuliwe na askari. Kama ungenitoa kwa askari ningeuawa kwa kosa lisilokuwa langu.
 
JOTO LA MAPENZI-5

ILIPOISHIA...

Kwanza kabla ya kusema yaliyonisibu sina budi kutanguliza shukrani zangu za dhati kwako mzee wangu kwa kuniokota na kunipa tiba pia kuweza kunificha ili nisichukuliwe na askari. Kama ungenitoa kwa askari ningeuawa kwa kosa lisilokuwa langu.
ENDELEA


"Mpaka leo sijui hii ni laana ya Mwenyezi Mungu na mtume wake pale nilipoweza kuihasi dini yangu na mtume wake. Japo nilirudi katika dini yangu bado mabalaa yameendelea kunipata mpaka leo hii na sijui nini hatma ya mbeleni."


"Hebu nieleze kisa na mkasa, inaonesha nyuma ya moyo wako kuna mengi yamejificha naomba uwe muwazi ili nijue nitakusaidia vipi, hakuna haki ya mtu inayoweza kupotea bure."


"Babu historia inaanzia miaka kumi iliyopita, naikumbuka siku moja nikiwa chumbani kwangu majira ya usiku nilishangaa kumwona mpenzi wangu ambaye nilipoteza mawasiliano naye kwa mwezi mmoja akiingia chumbani kwangu ghafla huku akiniangulia kilio akizungumza maneno ya kukata tamaa.
Ile ilitokana na uhusiano wa muda mrefu kuwa na kikwazo cha dini, mimi ni muislam na mwenzangu alikuwa mkiristo.


Kama ujuavyo siku zote anayetakiwa kumfuata mwenzake katika suala la dini ni mwanamke, japo mpenzi wangu alikuwa tayari kubadili dini lakini familia yake haikuwa tayari. Pakatokea mvutano mkubwa katika familia mbili huku kila moja akitaka ifuatwe upande wake.


Hapo kila upande ukabaki na msimamo wake, hiyo ilitufanya tubakie njia panda tusijue tufanye nini baada ya familia yangu kunipiga marufuku kuwa karibu na mwanamke ambaye hakuwa na faida kwangu. Kwangu lilikuwa pigo zito moyoni mwangu kutenganishwa na mwanamke ambaye niliamini ndiye atakayekuwa mke wangu.


Haikuwa upande wangu tu hata upande wa mwenzangu kila kukicha alikuwa akilia na kuibembeleza familia yake kuwa imruhusu abadili dini ili aolewe na mimi. Lakini walimweleza kama atafanya vile basi atatengwa na familia yake.


Kauli ya mpenzi wangu aliapa pamoja na vikwazo vyote hivyo katu hawezi kunipoteza atapigana kufa na kupona hata kuutoa uhai wake ili tu asinipoteze.Kila dakika iliyokuwa ikija mbele yangu niliiona ni mtihani mzito, wakati mpenzi wangu akijinadi kulipigania penzi lake kwa hali na mali, kwa upande wangu familia yangu ilianza mikakati ya kunitafutia mke wa kuoa.


Siku ambayo bado ipo akilini mwangu ni siku ambayo mpenzi wangu baada ya kupotezana kwa mwezi mmoja alikuja nyumbani kwangu usiku wa saa nne, muda huo tayari nilikuwa nimejilaza kitandani kwangu.
Nilishtushwa na mlango kugongwa ukifuatiwa na sauti ya kilio cha kwikwi.


Kwa vile sauti ya mpenzi wangu Koleta nilikuwa naijua kama pumzi zangu nilinyanyuka haraka kitandani na kwenda kufungua mlango. Nilipofungua mlango aliingia ndani na kujitupa kitandani na kuendeleza kilio ambacho kilihama kwenye kwikwi na kuwa cha sauti ya juu.


"Ambe nimekuja kukuaga mpenzi wangu sina maamuzi mengine zaidi ya haya kwa vile thamani yangu imepotea.""Maamuzi! Maamuzi gani?" nilishtuka.


"Ambe mpenzi wangu kumbuka wewe ndiye mpenzi wangu niliyekufungua moyoni mwangu na ufunguo niliutupa baharini na kuuapia moyo wangu sitamwingiza kiumbe yeyote maishani mwangu labda utakapo tangulia mbele ya haki hapo nitakuwa sina jinsi.


Hata kama nitaolewa na mwanaume mwingine bado sitampenda kama ninavyokupenda wewe, nitakuwa naye kama haki ya kiumbe cha kike kuwa na mwenza lakini si mapenzi toka moyoni mwangu. Tambua nakupenda zaidi ya kupenda," mpenzi wangu alisema kwa hisia kali.
"Natambua hilo."


"Lakini naona kuna viumbe wamekuwa wakiuchokonoa moyo wangu kiasi cha kila kukicha kuitamani ahera ambayo naamini itakuwa suluhu ya mateso yangu. Ambe mtu niliyekuamini kuwa pamoja katika dhoruba ya matatizo yangu umeungana na familia yangu kuniangamiza."
"Mimi nimefanya nini tena mpenzi wangu?" kauli ya mpenzi wangu ilinishitua.
"Uliniahidi nini?"
"Kuhusu nini?"


"Kuhusu penzi langu hasa baada ya kuingia mikono ya watu?"
"Nilikuahidi kuwa na wewe mpaka mwisho wa pumzi zetu."
"Mbona leo umenigeuka?"
"Mimi?"


"Eeh! Wewe Ambe," alisema kwa sauti ya kilio.
"Nimekugeuka kivipi?""Nilikueleza kamwe sitaolewa na mwanaume mwingine zaidi yako, wazazi wangu ili kunitenganisha na wewe wametengeneza mipango ya ndoa na mwanaume mwingine. Nimepinga kuolewa labda mwili wangu ukiwa hauna uhai."


"Una maana unataka kujitoa uhai?"
"Wazo hili lilikuwa gumu kulitoa moyoni mwangu kwa vile naujua upendo wako kwangu, lakini nilichokisia usiku wa kuamkia leo sikuamini nilitamani kujinyonga muda uleule. Lakini sikutaka kuyafanya maamuzi yale kabla sijaja kukueleza mhusika kitendo ulichonifanyia.


"Ninachokuomba kitu kimoja nikifa naomba unizike kwa vile hakuna aliye na haki na moyo wangu zaidi yako japo umenitenda lakini nitaondoka nikiwa bado nakupenda. Siamini mimi mtoto wa kike kuwa na msimamo wa kugoma kuolewa lakini wewe mwanaume niliyekuwa nakutegemea umekubali kulisaliti penzi letu."


"Nani kakueleza uongo huo?" nilijifanya kushtuka.
"Ambe ni uongo?"
 
JOTO LA MAPENZI-6

ILIPOISHIA

"Siamini mimi mtoto wa kike kuwa na msimamo wa kugoma kuolewa lakini wewe mwanaume niliyekuwa nakutegemea umekubali kulisaliti penzi letu."
"Nani kakueleza uongo huo?" Nilijifanya kushtuka.
"Ambe ni uongo?"
ENDELEA.....


"Si kweli."
"Hujatafutiwa mchumba?"
"Nimetafutiwa mchumba lakini sipo tayari kuoa mwanamke mwingine zaidi yako."
"Ambe unaniambia ukweli au unanipaka mafuta kwa mgongo wa chupa?"
" Koleta elewa mtihani ulio mbele yetu ni mkubwa sana hivyo tunahitaji kuwa makini na maneno ya watu wanaotaka kutuvunja moyo."


"Ambe, huwezi kuamini wiki ya pili nakunywa maji kuokoa maisha yangu lakini sina hamu ya chakula, baada ya kunilazimisha kuolewa na mwanaume mwingine na kunizuia nisitoke hata simu wameninyang'anya ili tu nisiwasiliane na wewe.


"Lakini usiku wa jana nililetewa taarifa na mtu kuwa nikubali kuolewa baada ya wewe kupata mchumba ambaye utafunga naye ndoa hivi karibuni. Aliyeniletea taarifa alinishangaa mimi kuwa na msimamo wakati wewe hukuwa na mapenzi ya dhati na mimi kiasi cha kutafuta mwanamke mwingine wa kumuoa.
"Kauli ile iliutoboa moyo wangu na kumuona malaika wa kifo mbele yangu, lakini sikutaka kufa bila kusikia kauli yako, Ambe niokoe au nipe ruhusa ya kutangulia mbele ya Mungu ili nihukumiwe kwa kosa la udhaifu wa moyo." mpenzi wangu alizungumza huku akilia.


"Koleta mpenzi wangu naomba usikie kauli toka moyoni mwangu kupitia mdomo wangu wala si katika kinywa cha mtu mwingine. Pamoja na mpango wa familia yangu kunitafutia mwanamke mwingine lakini sipo tayari kukupoteza wala sipo tayari kuona ukiteseka kwa ajili yangu."
"Sasa tutafanya nini, maana zimebaki wiki mbili kabla ya kutoa jibu la mimi kuolewa?" Koleta aliniuliza.
"Mmh! Kwa kweli sina jibu ningekuwa na uwezo ningefanya mpango wa kutoroka, lakini hali ya uwezo wangu unaijua vizuri."


"Basi wacha nifanye maamuzi yangu."
"Yapi?"
"Ya kunywa sumu."
"Aah! Koleta usinywe sumu mpenzi wangu," kauli ile ilizidi kunitisha na kuonesha Koleta hatanii.
"Lazima nifanye hivyo, nimechoka kuteseka, nione nilivyokwisha, kama wao wanaona maamuzi yao ni muhimu kuliko haki ya moyo wangu wacha nife wafurahi."


Mmh! Nilijikuta kwenye wakati mgumu sana wa maamuzi ya kumsaidia mpenzi wangu ili kuokoa maisha yake. Niliamini hakuwa anatania kwani mabadiliko ya afya yake yalionesha jinsi gani alikuwa na mapenzi ya dhati na mimi. Siku zote aliamini mwanamke ndiye mwenye haki ya kumfuata mwanaume hivyo aliamini wazazi wake kumwachia lakini ilikwenda kinyume.


Nilijiuliza nitafanya nini ili kuhakikisha naokoa maisha ya Koleta ambayo niliamini yapo mikononi mwangu. Kila nilivyomuangalia Koleta moyo uliniuma na kuona kama atakufa basi dhambi za kifo chake nitazibeba mimi. Koleta alikuwa amedhoofu macho yake makubwa ambayo nilipenda kuyatazama hasa akijipaka wanja.
Lakini siku ile yalikuwa yamevimba na kuwa mekundu kwa kulia, nilimtazama alikuwa amejikunyata akiendelea kulia kilio cha kwikwi. Nilijiuliza kama alikatazwa asionane na mimi na kunyang'anywa simu amewezaje kutoroka usiku kama ule.


"Koleta umewezaje kutoka usiku kama huu?"
"Hata sielewi, baada ya kuelezwa habari zile moyo uliniuma nililia sana na kupanga usiku wa leo lazima tuonane. Nimetoroka kwa kuruka ukuta, hata siamini niliwezaje kupanda na kurukia upande wa pili na kuweza kuja hapa."


Baada ya kutulia kwa muda nikimwangalia kipenzi changu ambacho kiliteseka kwa ajili yangu, nilijikuta nikipata wazo lenye maamuzi magumu, ambalo niliamini kabisa familia yangu isingekubali. Uamuzi wangu ulikuwa kuyaokoa maisha ya Koleta kuliko kusimamia imani ya kidini.
Niliamini uamuzi wangu wa kukubali kubadili dini usingekubaliwa na familia yangu hata ndugu na marafiki. Lakini kwa upande wangu niliona nipo sahihi hasa nikizingatia bado namuamini Mungu ni mmoja na waliobaki ni mitume wake.


Niliamua toka moyoni mwangu kuwa nipo tayari kwa lolote ili kuokoa maisha ya Koleta. Nilimueleza Koleta nilichofikiria muda ule.


"Koleta kama mimi nitaamua kubadili dini itakuwaje?"
"Ambe unaniuliza swali au umedhamiria kufanya hivyo?" aliniuliza huku ameyatoa macho yake nje kama anataka kuyaona maneno niliyoyasema.


"Nimedhamiria toka moyoni mwangu, nipo tayari kuwa mkiristo ili kuona maisha yako yanaendelea tena kwa furaha niliyoizoea kuiona usoni mwako."
"Kama ni kweli siamini kuna kitu kingine cha kuzuia ndoa yetu," Koleta alisema huku akijitahidi kutengeneza tabasamu.


"Basi nenda kawaeleze familia yako mimi nipo tayari kubadili dini kukufuata wewe."
"Na familia yako?"
"Hiyo niachie mimi."
"Je, wakikataa?"
"Walishakataa, lakini sasa nimeamua mwenyewe sitaki kuingiliwa maamuzi yangu na mtu."
 
JOTO LA MAPENZI-7

ILIPOISHIA:

Niliamua toka moyoni mwangu kuwa nipo tayari kwa lolote ili kuokoa maisha ya Koleta. Nilimueleza Koleta nilichofikiria muda ule."Koleta kama mimi nitaamua kubadili dini itakuwaje?"
"Ambe unaniuliza swali au umedhamiria kufanya hivyo?" aliniuliza huku ameyatoa macho yake nje kama anataka kuyaona maneno niliyoyasema.

"Nimedhamiria toka moyoni mwangu, nipo tayari kuwa mkiristo ili kuona maisha yako yanaendelea tena kwa furaha niliyoizoea kuiona usoni mwako.""Kama ni kweli siamini kuna kitu kingine cha kuzuia ndoa yetu," Koleta alisema huku akijitahidi kutengeneza tabasamu.

"Basi nenda kawaeleze familia yako mimi nipo tayari kubadili dini kukufuata wewe."
"Na familia yako?"
"Hiyo niachie mimi."
"Je, wakikataa?"
"Walishakataa, lakini sasa nimeamua mwenyewe sitaki kuingiliwa maamuzi yangu na mtu."
SASA ENDELEA...


"Ambe sasa harusi yetu haitakuwa na furaha kama tutakosa baraka za upande wa pili?"
"Baraka si muhimu kama maisha yako, siwezi kukupoteza kwa ubinafsi wa roho za watu, nilikuahidi kifo ndicho kitakachotutenganisha na si kiumbe chochote."
"Mmh! Sawa, kwa hiyo?"


"Nenda nyumbani kawaeleze nimekubali kubadili dini."
"Nashukuru mpenzi wangu kwa kuyajali maisha yangu," Koleta alinikumbatia kwa furaha.
"Basi mpenzi nikurudishe kwenu muda umekwenda sana."


Nilimsindikiza hadi kwao na mimi kurudi kulala, usiku ulikuwa mrefu kuliko kawaida baada ya kuwa katika mtihani mzito juu ya uamuzi wangu wa ghafla wa kukubali kubadili dini kitu ambacho wazazi wangu walinieleza kama nataka radhi yao basi nibadili dini.


Kwa upande wangu niliamini kabisa dini ni kama taasisi ambayo ipo kwa ajili ya kumfanya mtu amjue Mungu pia kuyafuata yote mema na kuyaacha yote mabaya aliyoyakataza. Moyoni niliamini hata hiyo radhi yao itakuwa haina nguvu kwa vile nilijitolea kwa ajili ya kuokoa maisha ya mtu aliyenipenda mapenzi ya dhati.


Niliamini kutafuta ushauri kwa marafiki ingenichanganya kwa vile nilikuwa tayari nimeshatoa uamuzi, kilichotakiwa ni utekelezaji na si kupokea ushauri tena. Toka awali nilipata vikwazo toka kwa watu wa karibu pale nilipowaeleza uamuzi wangu wa kutaka kubadili dini ili nisimpoteze Koleta.
***
Siku ya pili nikiwa sebuleni baada ya kumaliza kupata kifungua kinywa, nilishtushwa na sauti ya mtu akibisha hodi. Sauti haikuwa ngeni masikioni mwangu, ilikuwa ya mpenzi wangu Koleta, nilishangaa kubisha hodi siku ile kwani siku zote alikuwa akiingia ndani bila hodi. Nilijua ule ulikuwa wivu wa kimapenzi kwa kuamini akiingia bila hodi anaweza kufumania.


"Karibu," nilikaribisha bila kunyanyuka kwenye kochi kwa kujua mlango upo wazi.
"Hodi tena," sauti ya Koleta ilisema.
"Karibu mpenzi."


Baada ya muda aliingia Koleta akiwa ameongozana na mama yake mzazi nilishtuka na kujikuta nikishindwa kunyanyuka na kubakia nimekaa baada ya kunikuta kifua wazi.
"Karibu mama," nilimkaribisha.


"Asante, mwanangu, samahani kwa kukuvamia."
"Ha..ha..kuna tatizo," niliingiwa mchecheto.
Wakati huo Koleta alipitiliza chumbani na kurudi na fulana na kunipa.
"Ambe hebu vaa fulana uzungumze na mkweo."


Baada ya kuvaa nilimgeukia mama mkwe ambaye hakuwahi kufika kwangu toka nianze uhusiano na Koleta. Kwangu ulikuwa ugeni mzito, baada ya kimya kifupi mama Koleta aliniita.
"Baba."
"Naam mama."


"Najua utaushangaa ugeni huu?"
"Ni kweli mama," nilijibu kwa unyenyekevu.
"Nina imani unajua kuna kitu gani kilichopo kati yetu juu ya uhusiano wenu?"
"Ndiyo."


"Kwa kweli siku zote nilikuwa upande wenu kwa uamuzi wowote ambao mngeamua wewe kumfuata mwenzako au mwenzako kukufuata wewe. Mimi kwangu niliona sawa tu, lakini familia yako na baba yenu walijikuta wakiweka ligi ambayo kwangu sikuona kuna umuhimu wa kutunishiana misuli kwa jambo la maelewano.


"Siamini kati ya mkristo na muislamu nani yupo sawa au aliye na uhakika kuwa ndiye yupo sahihi mbele ya Mungu. Ninaamini sote tunamuabudu Mungu huyohuyo. Kwa kweli ushindani ule ulinikosesha raha hasa baada ya Koleta kuniapia kama atakukosa basi atajiua.


"Mwanangu, nilichanganyikiwa kila siku nilimuomba Mungu huku nikiamini ni yeye peke yake aliyekuwa na uwezo wa kuokoa uhai wa mwanangu. Taarifa nyingine zilizonichanganya zilikuwa kuwa umepata mchumba mwingine tofauti na Koleta. Hapo ndipo nilipokuwa nikihesabu siku za kuishi mwanangu kwa kuamini lazima atafanya alichodhamiria cha kujitoa uhai wake.
 
JOTO LA MAPENZI-8

ILIPOISHIA;

"Taarifa nyingine zilizonichanganya zilisema kuwa umepata mchumba mwingine tofauti na Koleta. Hapo ndipo nilipokuwa nikihesabu siku za kuishi mwanangu kwa kuamini lazima atafanya alichodhamiria cha kujitoa uhai wake."
ENDELEA...


"Huwezi kuamini taarifa zile zilinifanya nikuchukie hata kuuapia moyo wangu kulipa kisasi kama utaoa na mwanangu kuchukua jukumu la kujiua. Lakini jana usiku nikiwa nimelala niligongewa mlango, kwanza moyo ulinilipuka nikijua Koleta ameshafanya ujinga wake.


"Nilipofungua nilikutana naye akiwa katika sura nyingine tofauti na niliyoizoea, siku zote nilizoea kuona sura ya huzuni iliyoambatana na machozi. Lakini jana usiku uso wa mwanangu ulikuwa na tabasamu ambalo ndilo nililozoea kuliona katika uso wake.


"Nilitaka kujua kulikoni kuwa katika hali ile, kitu alichonieleza kilinichanganya sana sikuamini niliamini alikuwa akiota. Lakini alinihakikishia kuwa umetamka mwenyewe kwa mdomo wako kuwa upo tayari kubadili dini na kumuoa Koleta. "Taarifa hizi nilimfikishia baba yenu ambaye kwanza alitaka kudharau lakini nilimuhakikishia kama kweli umekubali kubadili dini ili umuoe mtoto wetu bado anaweka vikwazo vya kijinga. Nilimueleza kama Koleta atapoteza uhai baada ya kupatikana suluhu, maiti ya mwanangu ataila nyama.


"Ulikuwa ugomvi mzito ambao ulihama kwa mwanangu na kuhamia kwangu na kujifunga kibwebwe, nilikuwa tayari kwa lolote hata kuachika lakini kuokoa uhai wa mwanangu. Hajui nilivyoteseka kwa mtoto huyu leo afanye ujinga kwa sababu zisizo na msingi eti ukishamuoa utarudi kwenye dini yako, kwani hata ukirudi kwenye dini yako tutapungukiwa nini?


"Baada ya mshikemshike wa karibia nusu saa chumba kikiwaka moto, alikubaliana na mimi na kunituma nije nipate ukweli wa kauli yako ya kukubali kubadili dini. Je , ni kweli umekubali kubadili dini?" aliniuliza akiwa amenikazia macho.
"Ndiyo mama, nampenda sana Koleta siwezi kumpoteza kwa sababu ya dini," nilimjibu kwa utulivu kuonesha sitanii.


"Asante sana mwanangu kuokoa maisha ya kipenzi mwanangu," majibu yangu yalimfanya mama Koleta kunyanyuka na kuja kunikumbatia.
Baada ya kukaa aliniuliza swali.
"Sasa katika familia yako uamuzi wako wameupokeaje?"
"Mama siku zote kila aliaye ushika kichwa chake, nami nimeshika changu. Uamuzi huu ni wangu wala sitamshirikisha mtu yeyote."
"Je, wakikataa?"


"Maumivu ya moyo wangu hakuna wa kuyabeba kama nitampoteza Koleta kwa kitu cha kuamua mara moja."


"Je, harusi itakuwaje, kama familia yako itasusa."
"Najua itasusa lakini msimamo wangu utabakia palepale, siwezi kumpoteza Koleta kwa habari za kusadikika, nani aliyewaambia Mungu ni wa dini fulani?" nilijijaza ujinga.
"Hilo nimekuelewa, pia baba yako amenituma kwa vile leo kanisani kwetu kuna ibada ya jioni, alitaka leo utambulishwe kwa waumini ili ukaribishwe rasmi katika dini yetu."
"Hilo halina tatizo, nipo tayari."


"Basi mwenzako atakufuata na gari kukuchukua."
"Hakuna tatizo mtanikuta nimejiandaa."
"Ambe nakuhakikishia kuyabadili maisha utakapofunga ndoa na mwanangu," Mama Koleta aliniahidi kwa kinywa chake.


"Tuombe mambo yaende yalivyopangwa."
Waliniaga huku Koleta akionesha furaha ya ajabu kutokana na kauli yangu mbele ya mama yake. Kabla ya kuondoka alinifuata na kuninong'oneza:
"Ambe asante mpenzi, yaani mpaka nafika hapa nilikuwa siamini kama utaweza kuyasema uliyosema jana mbele ya mama yangu. Nilijua ulinitoa kisiasa lakini kauli haikuwa toka moyoni mwako. Lakini ulipokubali mbele ya mama nimeamini kweli unanipenda."


"Koleta ni wewe ndiye uliyenifanya niwe jasiri na kutoa uamuzi huu."
"Asante mpenzi wangu nitakupenda mpaka mwisho wa pumzi zangu."
Koleta alinipiga busu na kumwahi mama yake aliyekuwa ametangulia nje.


***
Baada ya kuondoka nilijiandaa kwenda nyumbani kuwaeleza uamuzi wangu wa kubadili dini, kwanza walishtuka na kuniomba nirudie baada ya kunisikia bila ya kunielewa.
"Unasema?" Mama aliniuliza.


"Nimeamua kubadili dini ili nimuoe Koleta."
"Wee mtoto umelogwa, unataka kubadili dini kwa ajili ya mwanamke sijawahi kuona, naomba ufute wazo hilo," mama alikuja juu.
"Mama nisipofanya hivyo nitampoteza Koleta."
"Huwezi kuzuia kifo chake bali Mungu, hebu acha kutuchefua."


"Mama uamuzi wangu ni huo, nimekuja hapa kukuelezea uamuzi wangu kuwa ninabadili dini na muda wowote nitafunga ndoa na Koleta."
"Hiyo ndoa yako utaifanya peke yako, nakuapia kama kweli utabadili dini basi utafute wazazi na ndugu zako, lakini kwetu utakuwa umejivua."
 
JOTO LA MAPENZI-9

ILIPOISHIA;

“Mama uamuzi wangu ni huo, nimekuja hapa kukuelezea uamuzi wangu kuwa ninabadili dini na muda wowote nitafunga ndoa na Koleta.”
“Hiyo ndoa yako utaifanya peke yako, nakuapia kama kweli utabadili dini basi utafute wazazi na ndugu zako, lakini kwetu utakuwa umejivua.”
ENDELEA...
“Msimamo wangu uko palepale hata nitengwe na dunia nzima lakini siwezi kumpoteza Koleta kama amejitoa kwangu lazima na mimi nijitoe kwake.”
“Wee mtoto kwa nini ututie aibu, kumbuka baba yako kakutafutia mwanamke na mipango inakwenda vizuri.”
“Huyo mnayemtafuta ni wenu lakini wangu ni Koleta,” kwa mara ya kwanza nilikosa heshima kwa kipenzi mama yangu.
“Hebu nenda kajiulize tena nipo chini ya miguu yako usifanye hivyo ni aibu mwanaume kumfuata mwanamke tena ukiwa mtoto wa kiislamu.”
Pamoja na yote aliyozungumza mama sikuwa na chochote cha kukibadilisha kwenye akili yangu. Niliondoka na kurudi kwangu, nakumbuka siku hiyo ndiyo ilikuwa ya kutambulishwa kanisani kwa kumtambua Yesu ndiye Bwana na Mwokozi wa maisha yangu.
***
Majira ya jioni Koleta alinifuata na gari la kwao na kunipeleka kanisani, huko nilipokelewa na shangwe na vigelegele. Baada ya ibada nilitambulishwa mbele ya waumini waliokuwa wamejaa kanisani. Historia yangu iliwavuta wengi kutokana na kuhama dini yangu ya kuzaliwa ya uislamu na kuamua kumfuata Bwana Yesu kwa ajili ya Koleta.
Kwangu ilikuwa historia ambayo haikuwahi kutokea maishani mwangu, baada ya kutambulishwa, waumini walifanya harambee ya kunichangia fedha kwa ajili ya kujiunga na dini yao.
Fedha ya papo kwa papo nilipata milioni sita, baada ya utambulisho nilipewa jina la Godbless. Kwa kifupi jina langu niliitwa God, baada ya ibada nilirudi na familia ya mpenzi wangu hadi kwao kulikokuwa na sherehe ndogo ya kubadili dini.
Mzee Michael Mtoe baba mzazi wa Koleta aliahidi kusimamia kila kitu katika maisha yangu ikiwemo kutupatia nyumba na gari baada ya kufunga ndoa. Kazi yangu ilikuwa ya kuajiriwa, aliniahidi kunibadilisha na kunipeleka kusimamia miradi yake na kunilipa mara sita ya pesa niliyokuwa nikilipwa nilipokuwa nafanya kazi.
Baba mkwe aliniahidi baada ya wiki nitaianza kazi huku wakijipanga kwa ajili ya maandalizi ya ndoa yetu. Nilijiona kiumbe mwenye bahati ya mtende kuoa katika familia yenye uwezo, niliamini muda si mrefu nami nitaishi maisha niliyokuwa nikiyaota ndotoni ya kumiliki nyumba na gari.
Baada ya sherehe nilirudi nyumbani kupumzika kusubiri ahadi za baba mkwe, nikiwa nimejipumzisha nyumbani kwangu, nilipokea ugeni akiwemo baba, mama na baadhi ya ndugu zangu ambao walipata taarifa zangu za kubadili dini siku ile na kutambulishwa rasmi kanisani.
Huwezi kuamini siku ile nilirudi na cd za gospo ambazo nilikuwa nasikiliza huku nikisoma agano jipya kufuatia vipengele nilivyoelezewa na mchungaji nianze kuvisoma.
“Ambe nini kimekusibu mwanangu?” Baba aliniuliza huku akiangalia Biblia niliyokuwa nimeshikilia mkononi.
“Tatizo nini?” Niliwauliza huku nikikaa kwenye kochi na kuweka agano jipya pembeni.
“Ni kweli umebadili dini?” Mama aliniuliza.
“Ndiyo.”
“Mwanangu nini kimekusibu, kwa ajili ya mwanamke?”
“Ni uamuzi tu, kwani kinachompeleka mtu peponi ni dini au matendo yake?”
“Ambe hayo ni maneno gani?” Mama alizidi kuchanganyikiwa.
“Sikilizeni wazazi wangu, uamuzi wangu si kuwavunjia heshima bali ni uamuzi ambao kwa upande wangu una faida kubwa kuliko hasara.”
“Sikiliza wewe mpumbavu kuanzia leo sisi siyo wazazi wako, pia nisikuone kwangu,” baba alisema kwa hasira.
Baba alikuja juu, lakini maneno yake makali hayakulingana na huruma niliyoifanya kuokoa maisha ya mpenzi wangu. Nilikuwa nipo tayari kwa lolote kwa kuamini hata Mungu anajua kiasi gani nilivyoweza kuokoa uhai wa mtu. Sikuona umuhimu wa kung’ang’ania dini wakati nampoteza mtu muhimu maishani mwangu.
Waliamua kuondoka huku mama akinibembeleza kwa kunipigia magoti akitokwa na machozi. Lakini nilimshangaa kama angekuwa tayari Koleta afe kwa ajili ya dini.
Pamoja na kuumizwa na kitendo cha mama yangu mzazi kunipigia magoti bado sikuona sababu ya kuwasikiliza wao wakati uamuzi wangu ulikuwa ukiokoa maisha ya mtu. Baada ya kuondoka niliwapigia simu nyumbani kwao Koleta kuwaeleza familia yangu ilivyopokea. Mama yake Koleta alinipa moyo kwa kunieleza:
“Mwanangu usiwe na wasiwasi waache wakutenge lakini nakuahidi hutajutia uamuzi wako wa kubadili dini pia kuokoa maisha ya mwanangu. Baada ya muda utakuwa na maisha mazuri, wao ndiyo watakuwa wa kwanza kuja kukuomba radhi kurudisha uhusiano.”
Maneno yale yalinitia moyo na kuamini pamoja na familia yangu kuamua kunitenga bado kuna nafasi ya kusameheana kwa kuamini hasira ndizo zilizotawala lakini kama wangekaa chini hasira zingewaisha na kuona jambo la kawaida.
***
Jioni Koleta alinifuata na kunipeleka kwao kutokana na wito wa baba yake, nilipofikishwa mbele ya mzee Michael Mtoe ambaye alinipa habari njema kuwa amenipatia kazi katika mmoja miradi wake ulio mkoani kama msimamizi mkuu na mshahara wangu ulikuwa mzuri pamoja na nyumba ya kukaa pia usafiri wa kutumia.
Kwangu ilikuwa ndoto ya mchana maisha yangu kubadilika ghafla kiasi kile.Katika maisha yangu sikuwaza kuna siku nitakuwa mtu mwenye heshima mbele ya watu kwa kutoa amri na kusikilizwa pia kutembelea gari langu, nyumba yenye kila kitu pia mshahara mara tano ya awali.
Mshahara wangu wa kawaida ulikuwa laki mbili na nusu. Lakini kwa kazi ya kusimamia mradi wa baba mkwe nililipwa milioni moja na nusu.
Nilikubaliana na maneno ya mama Koleta kuwa mafanikio yangu yatawafanya familia yangu kujirudi hata kuniomba msamaha. Niliamini ndani ya mwaka ningekuwa na pesa nyingi hata kumalizia nyumba ya familia iliyokuwa imesimama baada ya baba kustaafishwa kazi.
Huwezi kuamini maisha yetu yalianza kuyumba baada ya baba kustaafishwa kazi kiasi cha kushindwa kumalizia nyumba yetu ambayo ilikuwa ikikata mwaka wa saba ipo vile vile. Niliamini uwezo wangu wa kipesa utaweza kunirudisha kwa wazazi wangu.
Kuamua kubadili dini haikuwa kama siwapendi wazazi wangu la hasha, wazazi wangu nilikuwa nikiwapenda sana lakini baada ya kuzaliwa na kunilea ilifika hatua ya kujua zuri na baya. Wazazi wao walibakia kama walezi na washauri lakini uamuzi wa mwisho nilibaki nao mwenyewe.
Niliamini kabisa suala nimuoe mwanamke wa aina gani lilibaki kwangu, sikuamini kabisa dini ni kigezo cha kumpoteza mpenzi wangu ambaye alikuwa tayari hata nimtoroshe ili asinipoteze. Bado niliendelea kuwaheshimu wazazi wangu japo walinisusa kwa uamuzi wangu wa kubadili dini.
Lakini niliamini ipo siku watakubaliana na uamuzi wangu na kuniona nilichokifanya kilikuwa sahihi.
****
Nilipewa wiki ya kujiandaa kabla ya kuondoka, lakini ajabu muda wote huo sikupata nafasi ya kuwa karibu na mpenzi wangu ili tupange baada ya kuondoka kipi kifanyike. Kingine kilichonishangaza kilikuwa baada ya kuondoka kwenda mkoa wa mbali ambao ni zaidi ya saa kumi na saba kwa basi toka pale.
Swali lilikuwa harusi yetu itakuwaje kama nitakuwa mbali na mwenzangu ambaye sikuruhusiwa kwenda naye kwa vile alikuwa bado mchumba wangu. Lakini niliamini huenda nakwenda kuzoea mazingira ya kazi kisha ndipo mipango ya harusi ifuate.
Sikutaka kuuliza maswali yoyote juu ya harusi yangu kwa kuamini wenyewe ndio wanaojua kila kitu. Niliamini mpaka kunipa kazi nzuri tena yenye mshahara mzuri kulikuwa na mipango mizuri iliyokuwa mbele yangu hivyo sikutaka kula na kipofu nikamshika mkono.
Pamoja na mipango yao mizuri bado nilitakiwa niwe karibu na mwenzangu hasa kipindi kile ambacho nitakuwa naye mbali kwa kipindi kisichojulikana. Sikuwa na jinsi zaidi ya kukubaliana lakini nikiwa katika kipindi kigumu cha kutomuona mpenzi wangu hata kuja kuniaga.
Siku moja kabla ya kuondoka nilipewa pesa za kijikumu ninapokwenda, kwa kweli zilikuwa pesa nyingi sana ambazo kwangu niliona kama ni ndoto kushika pesa nyingi kama zile. Usiku majira ya saa nne baba mke mzee Michael Mtoe alikuja nyumbani kwangu kuja kuniaga. Baada ya kukaa alinieleza:
“Kijana kesho ndiyo siku yako ya kwenda kuanza kazi niliyokutuma pia kutengana na mpenzi wako. Katika hali ya kawaida najua utakuwa na upweke pia majonzi ya kuwa na mwenzako mbali. Lakini nimefanya hivyo kwa maana kubwa moja kukuandaa kimaisha ili uweze kuishi na binti yangu katika mazingira mazuri.
“Kumbuka leo nipo kesho sipo hivyo nakufundisha ili siku moja uweze kuiongoza familia yako bila kutegemea msaada wa mtu. Nakuomba kitu kimoja unapokwenda huko kama mwanaume ondoa mawazo ya nyumbani tafuta maisha kwa nguvu zako zote ili uonekane mwanaume mbele ya wanaume.
“Hata nikikubali muoane leo bado mtakuwa tegemezi kwa vile huwezi kumlea mwanangu kama nimleavyo kwa vile huna fedha za kutosha. Kazi niliyokupa na masilahi mazuri baada ya muda utaweza kusimama wewe kama wewe.
“Hivyo basi nakuomba ukiondoka hakikisha huwasiliani na mwenzako mpaka upate ruhusa yangu. Kama utakwenda kinyume na maagizo yangu utanitafuta ubaya, naomba kipindi ninachowaandalia maisha yenu kaa mbali na mwanangu najua huwezi kuwatumikia mabwana wawili mapenzi na kazi siku zote mapenzi huchukua nafasi na penzi siku zote ni kitovu cha uzembe.
“Hivyo nakuomba kipindi chote msahau Koleta mpaka hapo utakapokuwa tayari kummiliki kama mke ruksa kurudi na kumuoa siwezi kuyaingilia maisha yenu vile ninyi wenyewe mmechaguana.
“Kila tatizo lolote la pesa au ushauri wasiliana na mimi tu hata mama yako hana ruhusa ya kuwasiliana na wewe. Nina imani umenielewa?”
“Nimekuelewa.”
Nilijibu kwa mkato kwa vile sikuwa na kuuliza kutokana na maneno yote kumaliza japo niliamini kabisa kanipa mtihani mkubwa maishani mwangu. Kukaa mbali sawa lakini hata mawasiliano. Mmh! Nilijiuliza hata kutafuta maisha kwa jasho la damu bado nilitakiwa kuwasiliana na mpenzi wangu ambaye angekuwa ni sehemu ya kichocheo changu kutafuta maisha kwa nguvu zote.
Nikikumbuka nimemuacha mpenzi wangu aliyekuwa akinisubiri kwa hamu ili tuishi maisha tuliyo yasubiri kipindi kirefu.
“God...God,”baba Koleta aliniita zaidi ya mara mbili.
“Eeh...Aah! Naam,” nilijikuta nikichanganya majibu kutokana na kuhama kwenye dimbwi la mawazo mazito.
“Najua bado jina hujalizoea lakini utalizoea tu.”
Mzee Michael alisema bila kujua mwenzake sikubabaikia jina bali mtihani mzito, niliamini kubadili dini ni kuwa karibu na mpenzi wangu lakini yalizuka mapya ya kwenda mbali kufanya kazi kisha nisiwasiliane na mpenzi wangu. Upande wa pili niliona sawa kwa vile muda si mrefu nitakuwa nimejipanga kimaisha.
“Ndi..ndi..yo mzee.”
“Nashukuru kwa kunielewa ila ukienda kinyume unaweza kupoteza hata uhai wako.”
He! Makubwa nikienda kinyume naweza kupoteza maisha, kwa kweli kwa kauli ile ilinifanya niulize:
“Mzee mbona kama safari imejaa vitisho?”
“Siyo vitisho, kumbuka sikutaka umuoe mwanangu lakini umetumia hila za kubadili dini ili uihadae familia yangu. Hilo kwangu halikunishtua sana kwa kuamini baada ya kuoa unaweza kubadili dini na kurudia dini yako. Upande wa hila zako naamini umenishinda kwa vile sina uwezo wowote wa kukuzuia.
“Nachotaka ni kuyatengeneza maisha yako na mwenzako ili msimame hata kama sipo.”
“Sasa mbona unanitishia maisha?”
“Si kwanza nakutisha bali sitaki kuona mwanangu akiishi maisha ya kubahati na kama utafanya kwa jeuri yako sitasita kuchukua uamuzi wowote kwako.”
“Basi mzee wangu kama tunaelekea kutishana maisha basi naomba nirudi katika dini yangu nikuache na mwanao.”
“Kijana unataka mke wangu nimwambie nini, kipi kibaya nilicho kifanya kitakacho kurudisha dini yako au unataka Koleta ajiue?”
“Sipo tayari kumuona Koleta akifa, lakini naomba usiniwekee vitisho kwani kila kitu nimekifanya kwa faida yenu ili tu niwe na Koleta.”
“Basi nimekuelewa, nakuomba tuliyozungumza yabakie siri yetu tulikuwa tukizungumza wanaume wawili. Na kuahidi kama utanisikiliza harusi yako na Koleta inakuwa ya kihistoria pia mtaishi maisha ya peponi.”
“Nimekuelewa baba.”
“Basi kesho alfajiri nakutakia safari njema.”
“Nashukuru baba yangu.”
“Jana ulipewa kiasi gani cha kujikimu kimaisha.?”
“Milioni mbili.”
“Sasa hivi nitakuongezea milioni tatu jumla utakuwa na milioni tano.”
“Asante baba.”
“Hujui tu, nina mpango mzito na wewe ya kukufanya siku moja uishi kama mfalme hata kuuvuka mara kumi utajiri wangu.”
“Nitashukuru baba.”
Furaha ya pesa ilinifanya nisahau yote tuliyozungumza na kumuona mzee Michael Mtoe ni binadamu mwenye utu na mwenye kujua thamani ya maisha ya mtu.
“Sasa nikuache upumzike, kesho utapitiwa na gari majira ya saa tisa na kuanza safari yako nina imani mpaka saa kumi na mbili au saa moja jioni bila matatizo utawasiri. Kila kitu nimekwisha kipanga ukifika utapelekwa moja kwa moja nyumbani kwako.
“Kuna mfanyakazi wa kike ambaye atakusaidia kwa kazi ndogo ndogo, nina imani utainjoi maisha. Pesa za matumizi zikiisha nijulishe hazihusiana na mshahara wako. Nina imani umeona kiasi gani ninavyoonesha kukujali kwa vile umejitolea kuyaokoa maisha ya mwanangu.”
“Nashukuru mzee wangu nakuhakikishia kuyafanya yote uliyonieleza.”
“Utaona nitakupa kitu gani katika harusi yako ni zawadi ambayo hutaisahau maishani mwako.”
“Nakuhakikishia kuzingatia yote ili niipate hiyo zawadi.”
Baada ya mazungumzo yaliyoishi saa sita usiku, mzee Michael Mtoe aliniaga na kuondoka. Baada ya kuondoka nilijikuta nikisahau mazungumzo yote zaidi ya kuingia chumbani na kuzimwagia fedha zote kitandani na kuanza kuzihesabu. Niliyaona maisha yangu kama ya hadithi ya mtu kuhadithia kwa muda mfupi kisha hadithi kwisha kwa muda huo mfupi mtu alikuwa maskini na baadaye kuwa tajiri. Niliona hadithi hiyo ilinigeukia mimi, kwa mwezi mmoja nilitengeneza zaidi ya milioni kumi toka mchango wa kanisani na pesa za kijikimu katika maisha yangu mapya pia mama Koleta alinipa milioni mbili za siri mzee asijue.
Nilijikuta nikisahau hata mazungumzo yangu na mzee Michael baba yake Koleta na kuzichukua zile fedha alizonipa na kwenda kuzimwaga kitandani ili nizihesabu. Ile kwangu ilikuwa ndoto ya mchana sikuwahi kuwaza kuna siku nitashika milioni mkononi, lakini siku ile nilikuwa na milioni zaidi ya kumi.
Nikiwa katikati ya kuzihesabu maburungutu ya fedha, mlango uligongwa. Niliacha kuhesabu na kuzirudisha haraka fedha zote kwenye begi na kuziweka kwenye kabati na kutoka hadi sebuleni na kupaza sauti kuuliza:
“Nani?”
“Mimi.”
“Wewe nani?”
“Ambe leo unaniuliza mimi nani, hebu fungua mlango.”
Mmh! Sauti ile ilinishtua baada ya kuishitukia.
“Koleta,” niliita.
“Kuna mwingine tena zaidi yangu anayeingia ndani mwako?”
Sikuhitaji kuongeza neno lolote zaidi ya kufungua mlango, nilishtuka kumuona muda ule, wazo la haraka labda alifuatana na baba yake.
“Karibu mpenzi.”
“Asante.”
“Mbona usiku sana?”
“Nimekuja saa mbili zilizopita.”
“Ulikuja na baba?”
“Hapana peke yangu.”
“Koleta mbona ulitoweka kwenye mboni za macho yangu ghafla?”
“Ambe,” aliniita jina langu la zamani.
“Niite jina langu jipya.”
“Hilo jipya watakuita wao sio mimi, moyo wangu huchanua kulitaja jina lako halisi nilililolizoea hata ndani ya ndoa yetu sitakuita God, nitakuita Ambe mpaka pumzi zangu zitakapogota.”
“Mmh! Hebu nijibu swali langu.”
“Ambe hata sielewi kuna kitu gani kilichopo ndani ya familia yangu.”
“Kwa nini?”
“Kumekuwa na vikwazo vingi eti natakiwa kuwa karibu na wewe baada ya kuoana. Niliwaeleza basi hata univishe pete ya uchumba kabla ya kuondoka ili niweze kuwa karibu na wewe hata mara moja. Lakini hata hicho wakimekikataa kwa kweli hata sielewi wana lengo gani katika penzi letu.”
“Koleta nimezungumza muda mfupi na baba japo nilikuwa vigumu kumuelewa haraka nia na madhumuni yake kwetu, lakini baada ya muda nilielewa lengo lake la kutuweka mbali kwa muda.”
“Ambe mimi siamini kama lengo la baba ni zuri kwetu.”
“Kwa nini?”
“Mmh! Hebu nenda kwanza sijapata uhakika wa kitu nilichokiwaza kama ndicho usishangae kuniona nimekufuata huko huko.”
“Kuna nini tena?” Kauli ya Koleta ilinishtua.
“Nina wasiwasi safari yako ikawa mwisho wa mapenzi yetu.”
“Una maana gani?” Kauli ile ilizidi kunishtua.
“Kuna njama za kulivunja penzi letu kwa nguvu zote.”
“Mbona sikuelewi!”
“Ndio maana nikamkwambia wewe nenda lolote litakalotokea nitakujulisha.”
“Na mbona upo hapa usiku wote huu?”
“Ambe unaondoka lini?”
“Saa tisa usiku wa leo.”
“Ulitaka nikuage lini kama si muda huu?”
“Kwa nini usije mchana?”
“Ambe naomba uende lakini nitakupa jibu la kile ambacho nakiona.”
“Kipi hicho?” Maneno ya Koleta yalionesha ana siri nzito moyoni mwake.
“Kuwa muelewa nikisema leo naweza kusema ikawa sivyo ni mawazo yangu niache nipate ushahidi kamili.”
“Koleta kuna nini mpenzi wangu?” Mbona leo umekuwa na maswali akilini mwangu kuliko majibu.
“Unajua siamini kama kweli baba yangu amekubali kwa moyo wake tuoane.”
“Kwa nini?”
“Mbona ananiwekea mipaka hata simu hataki tuwasiliane hapo unaona kuna nini?”
“Najua utasema hivyo hata mimi nilijua kama unavyowaza wewe, lakini baadaye nilimwelewa. Nia yake ni mimi kusimama ile tuweze kuoana.”
“Sawa anataka usimame, kwa nini tusiwasiliane? Mbona mwanzo sikuwa na mipaka kama sasa?”
“Nakuomba uvumilie muda si mrefu tutaishi yale maisha tuliyokuwa tukiyaota ndotoni. Amini baada ya mwaka mmoja tutakuwa watu wengine.”
“Yaani tuoane baada ya mwaka mmoja?”
“Hapana ila naamini kwa mimi nitakuwa nimesimama vizuri.”
“Ambe nataka kukuambia kitu, kuna siri ipo nyuma ya moyo wa baba ambayo nina wasiwasi nayo sana.”
“Nakuomba niamini nikwenda kutafuta maisha nikirudi tutaishi maisha ya raha.”
“Ambe nilikupenda ulivyo sikukupenda kwa mali, yote haya yametokea wapi?”
Mmh! Lilikuwa swali gumu sana kulijibu.
“Ambe nakueleza ukweli kuwa safari yako ya kuwa mbali na mimi ni njia ya kulipunguza nguvu penzi letu.”
“Koleta nakuahidi mpaka kubadili dini na kukosana na familia yangu hakuna kitu kitakacho kuondoa moyoni mwangu, hata kifo kitauondoa mwili wako lakini si upendo wako moyoni mwangu.”
“Hilo nalijua mpenzi wangu, lakini penzi letu lipo kwenye vita nzito.”
“Hata kama ipo kwa vile sisi wenyewe tumependena pasipo ushawishi wa mtu tutashinda.”
“Ambe kwangu nilikufungia moyoni mwangu kisha ufunguo nikautupa bahari, nakuomba huko unapokwenda ukigeuka basi pembeni yako unione mimi.”
“Hilo nalijua mpenzi wangu, toka nilipojua kupenda jicho langu la kwanza kuona mwanamke mzuri lilitua usoni kwako. Nimekuwa kipofu toka nilipokuona sioni mwingine zaidi yako.”
“Ambe chochote ukisemacho nakikubali kwa vile umenionesha penzi la vitendo, nakuombea uende salama ili tupate tulichokitafuta kwa jasho la mioyo yetu?”
“Amini baada ya mioyo yetu kupata joto la mapenzi tutapumzika kwenye kivuri cha furaha ya mioyo yetu.”
“Naomba nikuage mpenzi wangu kabla hujaondoka ili niwahi nyumbani.”
Kwa kweli sikuwa na kipingamizi nilimkubalia mpenzi wangu, lakini ajabu siku ile hakutaka tutumie mpira wa kinga kama ilivyo kawaida yetu. Nilipomuuliza kwa nini siku ile hataki tutumie mpira wa kinga.
“Sioni umuhimu wa kuutumia kwa vile hiyo ndoa kwangu bado naiona ndoto.”
“Je, ukipata mimba?”
“Mimba si yako?”
“Lakini si tulipanga tuzae mtoto ndani ya ndoa yetu.”
“ Nikimsubiri huenda nisimpate ndoa bora nipate mtoto kuliko kukosa vyote.”
“Kwa nini?”
“Ambe hilo swali usiniulize leo ipo siku utajua leo nazungumza nini.”
Majibu ya Koleta yalionesha kuna siri nzito moyoni mwake, sikutaka kuuliza maswali mengi nilimpa haki yake mpaka tuliposhtuliwa na honi ya gari kunijulisha safari imeiva. Niliamka kujiandaa huku Koleta akioniomba nimuache alale ataamka asubuhi.
Baada ya maandalizi yote nilimuaga Koleta ambaye muda wote alikuwa akibubujikwa na machozi.
“Ambe usinigeuke kumbuka wewe ndiye mabawa yangu ukiniacha sitaruka milele.”
“Nakuahidi kutimiza ahadi yetu ya muda mrefu.”
“Asante mpenzi wangu nenda salama.”
“Na wewe bakia salama.”
Tulikumbatiana kwa muda kisha tuliachiana na mimi kwenda ndani ya gari na safari ya kuniweka mbali na mpenzi wangu ilianza.
Nje nilikuta Toyota Land Cruser Vx V8 likinisubiri, ndani ya gari kulikuwa na dereva tu mzee wa makamo kidogo. Niliingia ndani ya gari na safari ilianza.
“Vipi mzee, za asubuhi?” nilimsalimia dereva.


“Nzuri tu kijana, sijui zako?”
“Namshukuru Mungu, hivi hiyo sehemu ninayokwenda umeshawahi kufika?”
“Mara nyingi tu.”
“Mazingira yake yapoje?”


“Ni pazuri hasa kutokana na cheo chako, vipi umeoa?”
“Aah! Mzee huna habari kuwa mimi ni mchumba wa mtoto wa mzee Mtoe.”
“Unamuoa nani?”
“ Koleta.”


“Mmh! Mbona nasikia Koleta ana mchumba wake mwingine sijui mtoto wa waziri kama sikosei.”
“Hapana utakuwa umesikia vibaya, Koleta ni mchumba wangu mimi ambaye nimebadili dini kwa ajili yake.”


“Ha! Kijana ina maana wewe umebadili dini kwa ajili ya mwanamke?” Dereva aliniuliza.
“Sikuwa na jinsi kwa vile hatua aliyofikia mpenzi wangu haikuwa na njia nyingine zaidi ya kukubali kuikana dini yangu.”


”Kijana unawajua wanawake walivyo vigeugeu, una wazazi?”
“Ndiyo.”
“Wameshiba dini?”
“Ndiyo.”


“Si kweli siamini mzazi wa Kiislamu kumuachia mtoto wake kuingia ukristo.”
“Ni kweli wazazi wangu hawakukubali.”


“Kama hawakukubali nani aliyekupa ruhusa ya kufanya hili.”
“Ni mimi mwenyewe bila hivyo Koleta angejiua.”
“Mmh! Siwezi kukuingilia uamuzi wako kwa vile wewe ndiye uliyebeba mzigo, uzito wake unaujua mwenyewe.”


“Lakini mzee hata ungekuwa wewe ungechukua uamuzi huu, familia zetu zote ziliweka ngumu kuturuhusu kuoana kwa kila mtu na dini yake.”
“Baada ya kubadili dini nini kimefuata?”
“Nimetengwa na familia yangu.”


“Kwa hiyo umeona mapenzi matamu kuliko familia yako?”
“Najua familia yangu ndiyo muhimu lakini umuhimu wa jambo hili ni mkubwa kuliko kutengwa na familia yangu.”


“Sasa unasema ulibadili ili umuoe mbona umeondoka bila kuoa?”
“Amesema kunipeleka kule ni kujijenga kimaisha kabla ya ndoa, lakini ajabu amesema nisiwasiliane na mpenzi wangu.”


“Kijana mbona mnafanya mchezo wa kuigiza itakuwaje uwe mbali na mpenzi wako kisha msiwasiliane?”“Hata mimi nashangaa, mzee Mtoe amenitishia kama nitakwenda kinyume tutaelewana vibaya.”


“Mdogo wangu kuna kitu kina siri nzito, nenda lakini kuna siku utaniambia.

Je, Koleta na Ambe watafanikiwa kufunga ndoa na kutimiza ndoto yao? na Baba yake koleta ana mpango gani juu ya hatima ya ndoa ya mwanae? tuungane jioni mnamo wa kuanzia saa moja ili kujua nini kiliendelea nashukuru kwa uvumilivu wako have a nice time
 
safi mkuu.. jf stori nyingi zote huwa sifuatilii hebu ngoja nijaribu hii labda kuna uhondo huwa nakosa.
 
JOTO LA MAPENZI-10

ILIPOISHIA

"Kijana mbona mnafanya mchezo wa kuigiza itakuwaje uwe mbali na mpenzi wako kisha msiwasiliane?"
"Hata mimi nashangaa, mzee Mtoe amenitishia kama nitakwenda kinyume tutalewana vibaya."
"Mdogo wangu kuna kitu kina siri nzito, nenda lakini kuna siku utaniambia."ENDELEA


Nilijikuta nikiyakumbuka maneno ya mpenzi wangu Koleta kuwa nyuma ya moyo wa baba yake kuna siri kubwa. Sikutaka kuzungumza lolote zaidi ya kusubiri ripoti ya Koleta.Safari yetu ilikuwa nzuri kwani tulizungumza mengi njiani huku bwana Jimmy akinipanua mawazo ya maisha. Kubwa alinilaumu kwa uamuzi wa kubadili dini na kujitoa katika familia yangu kwa ajili ya mwanamke. Nilikiri kosa lakini nilimweleza baada ya muda nitarudi katika dini yangu kwani niliamini Koleta alikuwa tayari kubadili dini kunifuata kutokana na mapenzi mazito kwangu.


Kutokana na mwendo tuliokuwa tunakwenda tulitumia masaa kumi na mbili kufika. Tuliingia mkoani saa kumi na mbili na nusu. Alinipeleka moja kwa moja kwenye jumba langu lililokuwa na hadhi kubwa sehemu ile lilikuwa ndani ya uzio.


Nilimkuta mfanyakazi wa kike akinisubiri na kunipokea, alikuwa binti wa miaka kumi na saba. Niliangalia mandhari ya nyumba yangu iliyokuwa katika hali nzuri na usiku mzee Jimmy alinitembeza kuuona mji ule. Mji haukuwa umechangamka sana kama nilipotoka.


Ilionesha ni wilayani tofauti na mkoani nilipotoka ambako kuna sehemu nyingi za starehe. Baada ya kutembezwa na kuuona mji nilirudishwa nyumbani kupumzika. Siku ya pili nilifuatwa na mzee Jimmy kunipeleka kwenye mradi wa mzee Mtoe.


Ulikuwa mradi mkubwa wa kusimamia mashine za kupasua mbao pia kutengeneza wood bod na siling bod pia kusafirisha mbao kutoka shambani na kuzileta mjini ambako wateja walizifuata na kununua kwa jumla. Ulikuwa mradi mkubwa sana ambao haukuwa sawa na elimu yangu.


Baada ya kufika nilitambulishwa kwa baadhi ya wafanyakazi waliokuwepo pale kazini kwani wengine walikuwa kwenye mashamba ya mbao. Heshima niliyoipata ilinifanya nisikubaliane na Koleta kuwa baba yake alikuwa na mawazo mabaya kwangu.
***
Wiki nzima nilitumia kusoma mazingira ya kazi huku nikitembezwa hadi mashambani na mzee Jimmy. Kwa kweli mradi ule ulikuwa mkubwa sana, baada ya muda nilianza kazi huku nikiabudiwa kama Mungu. Kila nililosema lilisikilizwa. Nilijiona nipo katika sayari nyingine ambayo sikuwahi kuwaza kuifikia.


Ubize wa kazi ambao sikuwahi kuupata siku za nyuma nilijikuta nalala nimechoka hata muda wa kumkumbuka Koleta sikuupata kwani nilielezwa niyatafute maisha ili niishi vizuri. Hali niliyoiona kule niliamini kabisa muda si mrefu ningekuwa na maisha mazuri anayoyataka mzee Mtoe.


Kwa muda mfupi nilikuwa nafahamika kila kona na jina langu maarufu lilikuwa Bosi God, kama kawaida niliendelea kuifuata dini yangu mpya huku kila Jumapili lazima niende kanisani. Mwezi mmoja baada ya kuanza kazi nilitembelewa na mzee Mtoe aliyekuja kutembelea miradi yake na kuangalia utendaji wangu wa kazi. Alinisifia kwa utendaji wangu wa kazi. Kabla ya kuondoka aliniomba nirudi nyumbani mara moja kwa ajili ya kucheza mchezo mmoja wa filamu.


Ni kweli nilikuwa mmoja wa wasanii wa mchezo ya kuigiza runingani. Lakini nilishangaa mzee Mtoe kujua kuwa mimi ni msanii. Lakini nilikumbuka Koleta anafahamu uwezo wangu hivyo pengine alipotafuta msanii wa kucheza sehemu alimshauri anichukue mimi.


Nilimkubalia kucheza filamu hiyo ambayo hata jina lake sikulijua, baada ya kukubali nilishangaa kulipwa fedha nyingi tofauti na malipo niliyokuwa nayajua hata kwa hao mastaa wanaotikisa katika tasnia ya filamu kwa sini niliwazidi mara kumi.


Mzee Michael Mtoe alinilipa kwa kila sini milioni tano, nilijiuliza ni filamu gani yenye malipo makubwa kama yale. Baada ya kufika mjini nilikutanishwa na washiriki wa filamu hiyo ambayo nilifanya nao mazoezi ya siku mbili kabla ya kushooti.


Sehemu niliyocheza mimi ilikuwa ya harusi nikiwa kama bwana harusi aliyemuoa binti wa kiislamu. Kwa hiyo katika mchezo huo nilioa katika dini yangu ya zamani pia niliambiwa na baba mkwe katika filamu hiyo nitumie jina langu la zamani Ambe.


Ndoa yenyewe ilifungwa katika msikiti mkuu wa pale mjini na mfungishaji ndoa yenyewe alikuwa shehe mkuu wa msikiti ule ambaye alikuwa akifahamika. Ndoa ilifungwa mimi na binti mmoja aliyekuwa mzuri sana, niliulizwa maswali yaleyale ya kufungia ndoa ya kiislamu nami niliyajibu kiufasaha.


Baada ya ndoa nilifanya taratibu zote za kwenda kumfichua mke wangu kisha jioni tulikwenda kwenye ukumbi uliokuwa na harusi ya kweli iliyokuwa imejaa watu wengi. Niliamini filamu ile ilikuwa imeandaliwa kitaalamu sana, hata tulivyoingia ukumbini ilikuwa kama harusi ya kweli tulikwenda kukaa kwenye viti kisha baadhi ya watu walipita mbele yetu kutupa pongezi. Baada ya zoezi lile tulitoka ukumbini na kuwaacha harusi ya kweli iendelee.


Tulipotoka pale tulipelekwa kwenye hoteli kubwa pale mjini na kuingizwa chumbani na kupiga picha za maharusi kisha nilimaliza vipande vyangu na kubadili nguo. Kisha nililala palepale na alfajiri nilirudi zangu kwenye kazi yangu.


Ajabu muda wote wa kuwepo pale sikuruhusiwa kuonana na mpenzi wangu Koleta. Hilo halikunisumbua nilifanya lililonipeleka na baada ya kumaliza nilirudi zangu kwenye kazi zangu.


MIEZI SITA BAADAYE
Miezi sita ilikatika huku nikisumbuliwa na vishavishi vya wanawake walionitaka kimapenzi. Lakini nilivishinda kwa kuamini nina kosa kubwa katika familia yangu kwa ajili ya Koleta hivyo sikuwa tayari kufanya kosa lingine la kumsaliti Koleta.


Nilimuomba Mungu siku zote aniepushe na wanawake ambao walidiriki hata kunitamkia kuwa wananitaka hata bila fedha wengine walidiriki kunitamkia nataka kiasi gani ili wawe na mimi. Niliwaeleza nimeoa lakini hawakuwa tayari kuniamini zaidi ya kulazimisha dhamira yao ya matamanio ya mwili.


Muda wote huo ulikatika bila kuwa na mawasiliano na mpenzi wangu Koleta.
Siku zilizidi kukatika huku nikizidi kuwa maarufu niliweza kupata viwanja na kujenga nyumba ambayo niliamini ndiyo nitakayoishi na Koleta kwani mazingira ya sehemu ile nilishayazoea. Nilifanya kazi kama katapila huku kipato changu kikiwa kikubwa ambacho niliona ni wakati wangu mzuri wa kumweleza mzee Mtoe kuwa nipo tayari kumuoa Koleta.


Kwa muda ule nilikuwa na miradi yangu ambayo ilikuwa siri yangu kutokana na watu wangu wa karibu kunipa dili zile ambazo nilizifanyia kazi. Huwezi kuamini mwaka ulikatika bila kumjua mwanamke yeyote nilijilinda kwa ajili ya Koleta mwanamke aliyechaguliwa na moyo wangu.


Ushauri wa mzee Jimmy wa kufanya kazi na kuyaweka mapenzi pembeni ulinifanya nimsahau Koleta kwa kufanya kazi kwa nguvu zangu zote. Kama kawaida mzee Jimmy alikuwa akija na kurudi kupeleka au kuleta taarifa toka kwa mzee Mtoe.


Siku moja nikiwa nimekaa na mzee Jimmy muda mfupi baada ya kuwasili kutoka kwa mzee Mtoe. Mara nyingi alipokuwa akija tulikwenda kwenye klabu moja maarufu pale mjini ambayo huingia watu wenye fedha tu. Mwenzangu alikuwa mnywaji mzuri, kwa vile nilikuwa na fedha ya mchezo kila alipokuwa mjini pale nilimnywesha mpaka alizikataa pombe.
 
JOTO LA MAPENZI-11

ILIPOISHIA

Mara nyingi alipokuwa akija tulikwenda kwenye klabu moja maarufu pale mjini ambayo huingia watu wenye fedha tu. Mwenzangu alikuwa mnywaji mzuri, kwa vile nilikuwa na fedha ya mchezo kila alipokuwa mjini pale nilimnywesha mpaka alizikataa pombe.
ENDELEA..


Lakini mimi mwenyewe nilikuwa situmii kilevi cha aina yoyote. Baada ya kukata bia mbili aliniuliza swali.
"Rafiki yangu pamoja na ukaribu wetu umeoa bila kunitaarifu?"
"Mimi?" Nilishtuka kusikia vile.


"Eeh! Tena umezua tafrani kubwa katika familia ya bosi wako."
"Mimi nimeoa na kusababisha tafrani katika nyumba ya bosi wangu?" niliyarudia maneno aliyonieleza mzee Jimmy kama swali.


"Ndiyo, hivi ninavyosema Koleta ana wiki hayupo nyumbani na ameondoka na ujauzito mkubwa."
"Ujauzito wa nani?" Nilizidi kuchanganyikiwa.
"Inasemekana ni wa kwako."


"Sasa nini kilichomuondoa nyumbani kwao?"
"Inasemekana kuwa mliahidiana kuoana kama ulivyonieleza hapo awali, japo kuna taarifa zingine kuwa kuna mwanaume mwingine aliandaliwa na mzee Mtoe atakayemuoa Koleta na ndiyo sababu ya kukuleta huku na kukatazwa usiwasiliane naye.


"Baada ya kuzungumza na wewe habari zile zilinipa utata kuamini moja kwa moja kuna mchezo mchafu ulichezewa. Wiki mbili nilipata taarifa ambazo zilinifanya niamini yule msichana anakupenda sana, kwanza kabla ya habari za juzi kuna siku nilipata taarifa kuwa mchumba wako amelazimishwa kuolewa kwa nguvu lakini alisema ana ujauzito wako."


"Kabla hujaendelea habari hizi umezipata wapi?" Nilimkata kauli kwanza nijue anayosema kayatoa wapi, si kupandikiza ili kutaka kunikatisha tamaa."Taarifa hizi kila mmoja pale kwenye nyumba ya mzee Mtoe anajua japo wanafanya siri, lakini mambo mengi yamefumuka baada ya Koleta kutoweka."
"Mmh! Sasa mimi nimesababisha vipi?"
"Tatizo kubwa ni wewe kuonekana msaliti."


"Mimi? Nilishtuka tena.
"Wewe si umeoa kwa siri bila kumjulisha mpenzi wako."
"Mimi nimeoa?"
"Ndiyo tena nasikia lilikuwa bonge la harusi ambalo lilivunja rekodi."
"Mimi?" Nilizidi kushangaa.


"God unashangaa nini, ulifanya siri ambayo imezua tafrani kubwa na kusababisha Koleta kunywa sumu baada ya kujua umemsaliti."
"Amekufa?"


"Kweli umechanganyikiwa kama angekufa angetoweka vipi?"
"Hivi mzee Jimmy toka nije huku umesikia nimeoa lini?"
"Mbona nasikia video ya harusi yako imeonekana toka ukienda kuoa katika msikiti kisha ukumbini ambako watu walijaa kufuru.


Kibaya umeonekana umemcheza shele mtoto wa watu kwa kukubali kubadili dini kisha umemgeuka kwa kuoa mwanamke mwingine wa dini yako ya zamani. Lakini huku unajiita God kujifanya mkiristo mzuri kumbe chui katika ngozi ya kondoo."
"Mimi?" Nilizidi kushangaa.


" God mbona unajitia kila neno langu unashangaa, ina maana yaliyosemwa ni uongo?"
"Hakuna jambo lolote la ukweli?"
"Kwani jina lako la zamani si Ambe?"
"Ndiyo jina langu."


"Sasa unabisha nini?"
"Hukufunga ndoa mwezi mmoja baada ya kuja huku, tena imefungishwa na shehe wa mkoa?"
"Aaah," nilijikuta nikicheka mpaka machozi yakanitoka kitu kilichomshangaza mzee Jimmy.
"Nina imani ukweli umeujua?"
"Nimeujua," nilisema huku nikiendelea kucheka.
"Ulifikiri itakuwa siri?"


"Sasa siri ya nini na wakati ule ulikuwa mchezo wa sinema."
"Sinema gani yenye kujaza watu ukumbini kiasi kile?"
"Umeiona?"


"Walioiona wamesema kweli ndoa yako ilikuwa ya kifahari, baada ya kugundua wewe si mkweli kwa mpenzi wako walitumia CD ya harusi kumgeuza mawazo Koleta ambaye hakuwa tayari kukupoteza na kuamua kunywa sumu. Lakini bahati nzuri walimuokoa na kuendelea kumbembeleza aachane na wewe ili aolewe na mchumba waliomchagua wao.


"Koleta alikubali lakini katu alikataa kuitoa mimba na kusema pamoja na wewe kumsaliti hawezi kukiua kiumbe chako kwani kitabakia kama historia katika maisha yake. Ila aliapa hatakusamehe milele, lakini ajabu wiki moja kabla ya harusi Koleta ametoweka ghafla."


"Sasa huyo jamaa alikubali kuoa na mimba yake?"
"Walikubaliana baada ya kujifungua mtoto angelelewa katika kituo cha kulea watoto ili Koleta aweze kuishi katika ndoa yake bila kero ya mtoto, hata kama angezaa mtoto mwingine bado asingepata tatizo lolote."


"Mmh! Unajua naona kama mchezo wa kuigiza unayosema ni kweli au umeamua kunirusha roho?" Bado sikumuamini mzee Jimmy nilikuwa na wasiwasi huenda pombe zinampeleka vibaya.
"God mimi na wewe hatujawahi kutaniana."


"Sasa nini kimemfanya atoroke?"
"Kuna jambo moja nasikia aliwafuma wazazi wake wakiteta, sijajua jambo gani hapo nasikia alimwambia mfanyakazi aliyenipa habari hizi kuwa anaondoka na hataonekana na akionekana basi maiti yake."
"Kwa hiyo unasema yote hayo ni kwa sababu yangu?"


"Hakuna kingine, nasikia mzee Mtoe ana hasira na wewe hata sijui itakuwaje?"
"Sasa mimi nimemfanya nini? Kanileta huku nimekubali kukaa mbali na mpenzi wangu japo nilikubali kubadili dini ili niwe naye karibu."


"Ukaribu gani God wakati umefunga ndoa ya siri?"
"Unajua bado naona kichekesho, sijawahi kuoa wala sitaoa mwanamke mwingine zaidi ya Koleta."
"Tena nimeelezwa kuwa, wakati wa kuiangalia hiyo CD ya harusi familia nzima ilikuwepo pamoja na Koleta."
"Na mzee Mtoe?"
"Wote na mkewe."


"Sasa walikuwa wakiangalia sinema au harusi?"
"Juu ya CD hiyo kuna picha yako na mkeo mmelaliana, ooh, nimekumbuka kuna picha mbili aliniibia yule binti za wewe kuwa na mkeo katika honey moon katika hoteli ya Standard."


"Ooh! Sasa nimeelewa niliyokuwa nikielezwa na Koleta, nina imani huenda kuondoka kwake ukweli kaujua."
"Lakini kwa nini umefanya vile?"
"Sikiliza mzee Jimmy, mzee Mtoe ni muuaji mkubwa."


"Kwa nini unasema hivyo?"
"Unajua yule mzee mwezi mmoja baada ya kuja hapa alinifuata na kuniomba nikacheze filamu yake ambayo hata jina silijui. Sini yangu ilikuwa kwenye ndoa tu, baada ya kucheza nililipwa changu na kurudi kuendelea na kazi yangu zaidi ya hapo sijui kilichoendelea."


"God unajitetea au kweli?"
"Kwa jina la Muumba, kumbe mchezo ule ulikuwa ni janja ya kunitenganisha na Koleta. Naomba uniambie ukweli uliyosema yote ni kweli?"


"Nikudanganye nini?"
"Kesho nakwenda akanielezee ukweli juu ya huo mkanda aliyosema mimi nimeoa," nilijikuta nikipandwa na hasira.
"Punguza hasira."


"Tena nataka wakanielezee mpenzi wangu yupo wapi la sivyo patachimbika. Leo lazima turudi mjini na pia sioni umuhimu wa kuendelea kuwa huku naacha kazi nikamtafute mpenzi wangu."
"Lakini naomba usimwambie mzee Mtoe kuwa mimi ndiye niliyekueleza ukweli, ukiropoka tu ujue sina kazi."
"Siwezi kufanya hivyo, acha nikapumzike nimechanganyikiwa kumbe mzee yule ni mbaya kiasi kile.
 
JOTO LA MAPENZI-12

ILIPOISHIA

"Lakini naomba usimwambie mzee Mtoe kuwa mimi ndiye niliyekueleza ukweli, ukiropoka tu ujue sina kazi."
"Siwezi kufanya hivyo, acha nikapumzike nimechanganyikiwa kumbe mzee yule ni mbaya kiasi kile."
ENDELEA...


Nilinyanyuka na kumwacha mzee Jimmy Hotel na kurudi kwangu kwa miguu hata gari sikulihitaji. Moyo uliniuma kwa hila za mzee Mtoe, niliamini hata nikiacha kazi kwake nilikuwa na uwezo wa kujiendesha mwenyewe kutokana na miradi niliyokuwa nimefungua kwa siri.


Nilipanga usiku uleule niondoke na mzee Jimmy kurudi mjini ili majira ya mchana niwe mjini na kwenda moja kwa moja kwa mzee Mtoe akanieleze ukweli. Kwa mara ya kwanza nilichanganyikiwa mpaka nikapotea kwangu. Mzee Jimmy ndiye aliyenishtua wala sikujua nakwenda wapi.


Majira ya saa nane usiku niliondoka na mzee Jimmy huku mzee Jimmy akiniomba nisimtaje kuwa yeye ndiye aliyenipatia siri ile. Nilifika mjini majira ya saa sita mchana kutokana na mwendo kasi wa gari baada ya kumuomba mzee Jimmy akimbize gari na kuwa tayari kwa lolote kama ajali itatokea.
Aliniteremshia nje ya mji ili niingie peke yangu huku akiniomba nimjulishe kitakachoendelea.
"God kuwa makini pia naomba usinitaje."


"Siwezi kufanya hivyo, wewe ni mtu muhimu sana kwangu najua utanisaidia mengi."
"Basi nakutakia kila la heri."Nilikodi gari hadi mjini na kwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwao na Koleta, nilipokelewa na walinzi kama kawaida huku watumishi wa ndani wakionekana kama kunishangaa. Ile ilinipa picha fulani yenye ukweli na maneno ya mzee Jimmy.


Niliingia hadi sebuleni na kumuulizia Koleta.
"Rose, Koleta yupo wapi?"
"Sijui," alinijibu kwa kubabaika.
"Hujui kivipi?"
"Sijui lolote labda umuulize mama."
"Mama yupo wapi?"


"Amelala na ameomba asiamshwe na mtu."
"Unataka kuniambia Koleta humu ndani hayupo?"
"Ndi..ndi..yo, ha..ha..pana," Rose alizidi kubabaika.
"Mbona sikuelewi yupo au hayupo?"
"Muulize mama."
"Lakini hayupo?"


"Kaka Ambe, ooh kaka God sijui lolote mimi utanionea."
Mara aliingia mzee Mtoe aliponiona alishtuka sana.
"Ambe...Ooh! sorry God umefikaje hapa?"
"Kwa usafiri wa gari," nilimjibu kwa mkato.


"Sina maana hiyo, umekujaje huku bila ruhusa yangu?"
"Koleta yupo wapi?" Nilimuuliza kwa sauti kavu.
"Bado hujanijibu kwa nini umetoka kituo chako cha kazi bila taarifa pia kuja bila ruhusa yangu?"
"Hayo si muhimu kama kumuona mchumba wangu Koleta."


"Koleta ni mwanangu huwezi kuniuliza kama mkeo kumbuka wewe si mume wake wala mchumba huna haki ya kumuulizia hivyo.""Mzee nakuheshimu naomba kumuona mchumba wangu Koleta," nilisema kwa sauti ya juu iliyowatisha wafanyakazi waliokuwepo sebuleni na kumuamsha mama Koleta aliyekuwa amelala.


"Sikiliza kijana unakosa heshima huwezi kuunguruma ndani ya nyumba yangu wewe ni nani?"
"Mimi ni mchumba wa Koleta na mumewe mtarajiwa."
"Nani aliyekueleza wewe ni mchumba wa Koleta?"
"Baba Koleta kuna nini jamani mbona kelele?" Mama Koleta aliuliza akionesha anatoka usingizini.
"Si huyu mpuuzi eti anamtaka Koleta."


"Jamani mwanangu ameonekana?" Mama Koleta alihoji.
"Aonekane wapi si huyu mpuuzi anataka kunichanganya, nilikueleza tuachane na mjinga huyo ona anakosa heshima ni mtu wa kuniulizia mimi Koleta anajua nilimpataje?"


"Wazazi wangu najua kila kitu mlichokifanya juu ya kunitenganisha na mpenzi wangu, Koleta alinieleza muda mfupi kabla ya kwenda kituo changu cha kazi hila mlizoweka ili kututenganisha. Kutokana na maneno matamu ya baba niliamini alikuwa na nia njema kumbe ulikuwa na nia mbaya na mimi.


"Nimebadili dini ili kuokoa uhai wa Koleta aliyekuwa tayari kufa kutokana na vikwazo, nimejitoa muhanga kwa kutengwa na familia yangu ili kuona mwenzangu akiendelea kuishi na kufurahia maisha. Lakini nimekuwa mjinga na mwisho wa siku mnanifanyia mambo hata shetani hawezi kuyatenda.


"Yaani unanifuata nicheze filamu yako kumbe ulikuwa na siri nzito moyoni mwako, kama ulikuwa hutaki niwe na Koleta kwa nini kunizulia uongo ambao hata kama Koleta angekufa angeamini kabisa nimemsaliti. Lakini Mungu alimsaidia kupona sumu aliyokunywa kwa uongo wenu.


" Baada ya hila zenu nilifanikiwa kugeuza mawazo mpenzi wangu aolewe na mume mliyemuandalia japo mlijua ana ujauzito wangu. Japo mlifanya siri ambayo kila mtu humu ndani anajua na kuwakataza wasitoe siri nje na ndiyo maana nilipomuuliza Rose alibabaika.


"Lakini Mungu huwa hamfichi mnafiki Koleta aligundua njama zenu za kututenganisha na kuamua kutoroka kwa hiyo naomba kumuona mpenzi wangu akiwa hai la sivyo tutaelewana vingine," nilikuwa mkali bila kuhofia vitisho vya baba Koleta.


"Wee nani sijui hata jina lako nimelisahau, unaweza kutulazimisha tukuletee Koleta kwa lazima, unajua uchungu wake? Mimi ndiye niliyekaa naye tumboni miezi tisa na kumlea mpaka kumuona. Sasa mimi na wewe nani anayemuhusu Koleta kwanza nani kakueleza Koleta hayupo?" mama Koleta alinihoji.


"Kwanza kuhusu nani anayemuhusu Koleta kati yangu na ninyi, jibu jepesi mimi ndiye anayenihusu kuliko ninyi. Nimeokoa maisha yake kwa kukubali kutengana na familia yangu kwa ajili yake kwa kubadili dini. Pili Koleta hayupo amekimbia baada ya kugundua kuwa mmetengeneza uongo ili anichukie.


"Kwa hiyo Koleta ni halali yangu namtaka sasa hivi mtajua mtamtoa wapi," nilikuwa mkali kuliko maelezo.
"Toka njeee," mzee Mtoe alifoka kwa sauti ya juu."Humu ndani hatoki mtu mpaka nimpate mpenzi wangu bila hivyo hatutaelewana labda mtoe maiti yangu lakini si mimi nikiwa hai."


"Kwanza habari hizi kazijua wapi, huenda anajua wapi alipo Koleta," Mama Koleta alisema huku akionekana presha kumpanda."Na kweli, inawezekana kabisa yeye ndiye aliyemtorosha Koleta, basi leo atamtoa la sivyo atafia gerezani," mzee Mtoe alinitolea vitisho.


"Kuozea gerezani kwa ajili ya Koleta sitaogopa kwa vile alijitoa kwangu kwa hali na mali nami vilevile nilijitoa kwake.""Basi toka humu ndani.""Baba Koleta aende wapi bila kumrudisha Koleta," mama Koleta alimtaka mwanaye.
"Na kweli, hebu ngoja."


Baada ya kusema vile alipiga simu polisi ili kuja kunikamata, sikuogopa baada ya muda walifika polisi na kunitia nguvuni kutokana na kufanya fujo na kutishia uhai wa wazazi wa Koleta. Sikubisha kwa kujua haki itapatikana baada ya kufanyika uchunguzi.


Ajabu nilipofika polisi nilifunguliwa mashitaka ya kutishia kuua, kufanya fujo na kumtorosha Koleta kumficha sehemu isiyojulikana. Makosa yote niliyakana na kueleza ukweli wa yote yaliyofanyika. Baada ya kukosekana ushahidi niliachiwa huru lakini bado sikukaa kimya nilirudi tena kwa mzee Mtoe kumfuata mpenzi wangu ambaye kipindi chote hakujulika yupo wapi.


Nilichukuliwa na polisi na kurudisha kituo changu cha kazi na kuamliwa kutotoka eneo lile mpaka hapo nitakapopata ruhusa ya kipolisi zaidi ya hapo sikutakiwa kutoka nje ya mkoa ule.
 
JOTO LA MAPENZI-13

ILIPOISHIA

Nilichukuliwa na polisi na kurudishwa kituo changu cha kazi na kuamriwa kutotoka eneo lile mpaka hapo nitakapopata ruhusa ya kipolisi zaidi ya hapo sikutakiwa kutoka nje ya mkoa ule.
ENDELEA NAYO


Niliwaeleza kuwa sipo tayari kufanya kazi katika kampuni ya mzee Mtoe wala kuendelea kuishi katika nyumba yake. Pamoja na kuacha kazi bado walinieleza kwa ajili ya usalama nikae kule kwa muda wa miezi mitatu ndipo nirudi. Niliwakatalia kwa vile kule hapakuwa kwetu nilikuwa kule kwa ajili ya mzee Mtoe ambaye aligeuka kuwa adui yangu mkubwa. Niliwaomba waniruhusu nirudi nyumbani, walinikubalia kwa masharti ya kutoifuata familia ya mzee Mtoe kwani ndiyo iliyokuwa na mamlaka ya Koleta na si mimi.


Nilikubali kwa shingo upande kutofuatilia maisha ya Koleta lakini nirudi nyumbani. Baada ya makubaliano nilirudi nyumbani huku roho ikinituma nimfanyie kitu kibaya mzee Mtoe ili kutimiza maumivu ya moyo wangu. Nilipanga kujifanya nimeachana naye lakini moyoni ningepanga kufanya kitu na kuwa tayari kupoteza maisha yangu lakini nilipe machungu ya kutengwa na familia yangu.


Nilirudi nyumbani huku nikikumbuka maneno ya Koleta juu ya siri ya baba yake juu ya kututenganisha kwetu. Nilijikuta nikikonda kwa muda mfupi muda mwingi nilijifungia ndani huku nikilia, kuna kipindi niliona dunia imenitenga na kutamani kujitoa uhai baada ya kudhulumiwa haki yangu pamoja na kuuza utu wangu mbele ya familia yangu.


Wazo la kujitoa uhai niliweka kando mpaka nitakapoifanyia kitu kibaya familia ya mzee Mtoe ili nao wapate maumivu kama yangu. Nikiwa nimekata tamaa ya maisha huku nikiwa kama dume la nyani kwani hata marafiki zangu walinikimbia baada ya kubadili dini kwa ajili ya mwanamke.


Mzee Jimmy baada ya kutoniona kwa muda mrefu alinifuata nyumbani hali aliyonikuta nayo alinionea huruma.
"Ha! God mbona upo hivi?""Naomba kwanza uniite jina langu la zamani sasa hivi nimesharudi katika dini yangu naitwa Ambe."


"Haya Ambe mbona upo hivi?"
"Nimepoteza mwelekeo hata sijui nifanye nini, naona kama sitakiwi duniani wala ahera."
"Ambe wewe ni mwanaume kwa vile umesharudia dini yako unatakiwa kwenda kwa wazazi wako kuomba msamaha."
"Watanikubalia?"


"Kwa nini wasikukubalie wewe ni mtoto wao hivyo hawawezi kukubagua umefanya kosa umejirudi nina imani watakusamehe."
"Nitawezaje nashindwa nianze vipi ili wanielewe."
"Ambe kazi hiyo niachie mimi, twende tukifika huko kazi ya kuomba msamaha niachie mimi."
"Nitashukuru mzee Jimmy."


"Ni wajibu wangu kukusaidia najua upo katika wakati mgumu sana, nilisikia yaliyokukuta lakini sikujua unakaa wapi pia si unajua sikutaka nijulikane kwa mzee Mtoe nipo upande wako. Lakini usingefikia hatua hii."
"Habari za Koleta umeshazisikia?" nilimuuliza mzee Jimmy.


"Kwa kweli waliomuona wanasema mara ya mwisho alionekana ulipokuwa unafanya kazi, lakini baada ya kuelezwa umeondoka aliondoka na hajulikani yupo wapi."
"Inawezekana bado yupo kule."
"Hapana, taarifa zilimfikia mzee Mtoe alituma watu kumtafuta lakini hakuna aliyebahatika kumuona pamoja na kutangaza zawadi kubwa kwa mtu atakayemuona."
"Sasa mpenzi wangu atakuwa wapi?"


"Ambe kwanza tafuta radhi za wazazi wako, mambo mengine yatakuja."
Nilikubaliana na mzee Jimmy kwenda kwa wazazi wangu kuomba msamaha, tulikwenda hadi nyumbani, mama aliponiona aliangua kilio kama nimekufa na kunifanya na mimi niangue kilio. Mzee Jimmy alitubembeleza wote, mama alinitazama mara mbilimbili asiamini kama ni mimi kweli.
"Ni wewe Ambe?"


"Ni mimi mama, mama naombeni msamaha kwa yote niliyowatendea wazazi ndugu na jamaa."
"Mwanangu sina kinyongo na wewe kwa vile nilikwisha kuzaa siwezi kukurudisha tumboni."
"Baba yupo wapi?"
"Baba yako?" Nilishangaa mama kuangua kilio kama mtu aliyepewa taarifa za msiba.
"Mama mbona unalia kuna usalama?"
"Hakuna usalama mwanangu."


"Kwa nini?"
"Baba yako alifariki katika mazingira ya utata."
"Mazingira ya utata?"
"Ndiyo mwanangu, baada ya mzee Mtoe kukubadili dini baba yako alipambana naye mpaka mahakamani, lakini mzee Mtoe aliapa kumpoteza kwa gharama yoyote. Ndipo siku moja wakati anavuka barabara aligongwa na gari ambalo walioona walisema lilimfuata pembeni na kumgonga kisha lilitimua mbio."


"Mama una uhakika ni mzee Mtoe ndiye aliyemuua baba?"
"Kutokana na kauli yake na mazingira ya kifo cha baba yako tunaamini kabisa yeye ndiye aliyepanga kifo cha baba yako."


"Mama, baba anakufa bila kunijulisha nije nimzike," nilimwambia mama huku nikitokwa na machozi ya uchungu.
"Tungekujulisha vipi bila kuwa na mawasiliano yako, ndugu zako walirudisha moyo ili uje umzike baba yako lakini simu yako ya zamani kila ilipopigwa haikuwa hewani."
"Mama kama kweli mzee Mtoe ndiye aliyemuua baba wacha niende na mimi akanimalize," niligeuka ili nielekee kwa mzee Mtoe lakini mzee Jimmy alinishika na kuniweka chini.
"Ambe hebu punguza munkari kwa vile huna ushahidi mshtakie Mungu."
"Haiwezekani lazima alipe uhai wa baba yangu."


Niliangua kilio cha uchungu baada ya kugundua kifo cha baba yangu sababu ni mimi, nilijiona mpumbavu kuokoa maisha ya Koleta na kusababisha kifo cha baba yangu mzazi. Mzee Jimmy alitumia busara zake kunituliza na kukubali kuachana na mzee Mtoe ambaye aliendelea kupanga mipango ya kunimaliza.


Baada ya kumaliza tofauti zangu na ndugu zangu niliendelea na maisha yangu huku nikipata taarifa za kunishtua kuwa Koleta ameonekana sehemu akiwa na mtoto mchanga. Lakini sehemu zote nilizokwenda sikumuona hata nilipoulizia walisema walimuona kitambo lakini muda ule hakuwepo.


Siku moja nilikutana uso kwa uso na mzee Mtoe nilimueleza kwa sauti bila kuhofia watu waliokuwepo.
"Wee muuaji lazima utalipa uhai wa baba yangu."
"Jamani mnamuona huyu kijana anatishia maisha yangu?" mzee Mtoe alisema huku akiwageukiwa watu ambao hawakuwa na habari naye.


"Achana naye kijana maisha yamemchanganya," alisema mpita njia.
"Sijachanganyikiwa huyu mzee ni mbaya sana lakini lazima atalipa uhai wa baba yangu."
"Si mnamsikia nikifa leo wajue wewe ndiye uliyeniua."
 
JOTO LA MAPENZI-14

ILIPOISHIA

"Sijachanganyikiwa huyu mzee ni mbaya sana lakini lazima atalipa uhai wa baba yangu."
"Si mnamsikia nikifa leo wajue wewe ndiye uliyeniua."
"Akuue nani Mungu atanilipia."
"Unageuza eeh! Watu wameshasikia."
ENDELEA NAYO


Nilikuwa na ndugu yangu aliniondoa eneo la tukio na kumwacha mzee Mtoe akizidi kutafuta ushahidi kama nikimuua. Baada ya kuachana ilipita wiki mbili nilishangaa kuvamiwa nyumbani na polisi na kukamatwa. Nilipofika polisi nilielezwa kuwa nimemuua mtu aliyekuwa amepanda gari moja na mzee Mtoe.
"Mimi?" Niliuliza.


"Eeh wewe si ulisema unataka kumuua na jana ulipotaka kumuua mzee Mtoe lakini bahati mbaya risasi uliyomlenga ilimkosa na kumpiga mtu aliyekuwa naye kwenye gari lake."
"Mimi?" Nilizidi kushtuka.
"Usishtuke, ukweli ndiyo huo."


"Jamani hiyo risasi nimempiga saa ngapi wakati sijui hata kutumia bastola."
"Siku zote wauaji hujifanya hawajui kitu."Niliwekwa mahabusu kwa miezi mitano ndipo nilipandishwa kizimbani, pamoja na kujitetea ikionesha kabisa sina kosa nilifungwa miaka saba. Nikiwa gerezani nilikutana na Aloys Mabina ambaye naye alinieleza yaliyompeleka gerezani."


"Na yeye kipi kilichompeleka gerezani?" Mzee Yamungu aliyekuwa akinisikiliza kwa makini alitaka kujua habari za rafiki yake iliyopelekea kuiba silaha na kutoroka gerezani kitu kilichofanya Ambe naye aingie kwenye msafara wa mamba.


Kabla ya kuendelea kumsimulia Ambe alikunywa maji kidogo na kukohoa kisha alianza kumwelezea mkasa uliomkuta Aloys Mabina kufika hatua ya kutafuta silaha ili akalipe kisasi."Basi mzee wangu baada ya kuingia gerezani Aloys Mabina alikuwa mtu wangu wa karibu ambaye alinibembeleza nimueleze sababu za mimi kuingia gerezani. Baada ya kumweleza yangu niliyokusimulia naye alianza kwa kunieleza haya:


Siku moja akiwa anatoka shule wakati huo yupo darasa la sita, alipofika getini alimkuta baba yake akizungumza na mtu kwenye simu kuonesha kuna kitu kadhulumiwa na mtu, alimsikia baba yake akizungumza kwa sauti bila kujua mwanaye alikuwa nyuma yake.


"Bwana Samjo nakuapia kwa fedha zangu utaniua lazima unilipe fedha zangu.... Nimesema hiyo fedha ninaitaka leo hii kama sivyo nitakufa mimi au wewe."Aloys Mabina alishangaa kuona baba yake akipiga ngumi kwenye gari kwa hasira kuonesha alikuwa na hasira sana tofauti na siku zote. Alipogeuka alishtuka kumwona mwanaye nyuma ya gari.


"Wee Aloys njoo hapa," Aloys alikwenda kwa baba yake akiwa na woga mwingi.
"Umekuja saa ngapi?"
"Sasa hivi," alijibu huku akitetemeka.
"Umenisikia nazungumza nini?"
"Sija..ku..kusikia baba."
"Haya ndani haraka."


Aloys Mabina alikimbilia ndani na kumuacha baba yake akitaka kupiga tena simu, Aloys baada ya kuingia ndani nyuma alisikia baba yake akiondoa gari. Usiku wa manane ya siku ile waliamshwa na kuelezwa kuwa baba yao ameuawa kwa kupigwa risasi sita kifuani akiwa kwenye gari lake lililokutwa limeegeshwa pembeni ya barabara.


Kifo cha baba yao kilikuwa pigo kubwa katika familia yao, kutokana na utajiri mdogo waliokuwa nao waliendelea na maisha huku Aloys na ndugu zake wakiendelea na masomo. Kutokana na mawazo ya kitoto hakuweza kufuatilia mazungumzo ya mwisho ya baba yake.


Baada ya kumaliza elimu ya kidato cha sita hali ya kimaisha ilianza kuyumba na kusababisha Chris ashindwe kuendelea na masomo ya chuo kikuu kutokana na uchaguzi wake wa chuo, ada ilikuwa ni kubwa hivyo ilihitaji nguvu ya ziada.


Katika mazungumzo na mama yake alimweleza deni la baba yake alilokuwa akimdai mzee Samjo. Jina lile lilimshtua sana Aloys na kukumbuka kauli ya baba yake muda mfupi kabla ya kifo chake.
"Mama huyo mzee Samjo ni nani?"


"Ni mzee mmoja rafiki ya baba yako waliokuwa wakifanya biashara ya madini pamoja."
"Sasa hiyo fedha aliyokuwa anamdai alimuuzia nini?"
"Alimpa madini akamuuzie lakini malipo yakawa tatizo."
"Kwa hiyo mpaka baba anafariki hajamlipa?"
"Hajamlipa."


"Mama kuna kauli kama sitakosea nilimsikia baba akizungumza na mtu na usiku wa siku ile alifariki."
"Kauli ipi hiyo?""Nilimsikia akisema kama Samjo hatampa fedha zake basi lazima mmoja apoteze uhai wake na pia nakumbuka siku ileile alisema lazima alipwe fedha yake."


"Ha! Kwa nini hukusema siku hiyo ili tuweze kumshtaki Samjo?"
"Kwa kweli sikuwa na mawazo ya kujua kauli ile ndiyo iliyosababisha kifo cha baba yako."
"Sasa mama umeshafuatilia deni hilo?"
"Kila nikimfuata husema hana fedha anayodaiwa na baba yenu."
"Lakini hilo deni unalijua?"


"Si ulisikia na baba yako alisema muda mfupi kabla ya kifo chake, na ungesema siku ile mbona ingetusaidia kumtia hatiani."
"Kwa hiyo umeamua nini?" Aloys alimuuliza mama yake.


"Nimeamua kumuachia kwani asije niua kama alivyomuua baba yenu."
"Basi mama nakuhakikishia fedha yetu anaitoa, ni kiasi gani?"
"Mmh! Ni nyingi sana kama milioni 150 kama sikosei."
"Basi atalipa na riba."


"Utawezaje kumdai mtu katili kama yule?"
"Mama kamuua baba kwa haki yake, mimi nitamuogopa kivipi, wadogo zangu wanatakiwa kwenda shule na mimi kwenda chuoni."
"Mwanangu achana na mtu yule nasikia kuua ni kazi yake hata wakubwa wa polisi wanajua, ndiyo walinishauri niachane naye."


"Mama nikitoka hapa breki ya kwanza kwa mzee Samjo."
"Aloys hebu achana na mtu huyu bado nakuhitaji."
"Mama nikifa muda wangu umefika, lakini si kwa kumuogopa muuaji na mzulumati mkubwa kama yule."
"Hapana baba nipo chini ya miguu yako, " mama Aloys alimbembeleza mwanaye.
"Mama samahani kwa kukataa kukusikiliza, niache na mimi aniue kama baba."


Aloys aliondoka na kuelekea nyumbani kwa mzee Samjo, alipofika alikaribishwa kutokana na kufahamika kama mtoto wa marehemu Madon. Alipofika aliomba kukutana na mzee Samjo alikaribishwa sebuleni. Baada ya muda mzee Samjo alitokea akiwa amejifunga msuli.
"Ooh! Kijana karibu."
"Asante."
"Kweli wewe ndiye nani?"
"Naitwa Aloys."


"Ooh! Aloys umekuwa nakumbuka ulikuwa mdogo, tena unafanana sana na marehemu rafiki yangu baba yako."
"Shikamoo."
"Marahaba, mama yako hajambo?"
"Hajambo."
"Ndiyo kijana, unasemaje?"
"Nilikuwa naulizia fedha baba aliyokuwa anakudai."
"Fedha?" mzee Samjo alijifanya kushtuka.


"Ndiyo, najua mpaka baba anakufa alikuwa anakudai zaidi ya milioni 150 kutokana na kukaa kwako muda wote tunataka fedha hiyo utulipe mara tatu."
"Kijana una kichaa baba yako alikuwa ananidai fedha gani na nilifanya naye biashara gani?"
"Japo najua madai ya haki yake ndiyo yalighalimu uhai wa baba yangu, lakini bado haiondoi deni. Kwa hiyo nipo hapa kwa ajili ya kulipwa fedha zetu."


"Kijana hebu ondoke nitakupoteza sasa hivi," mzee Samjo alimtisha Aloys.
"Mzee najua unavitisho vilivyomfanya mama ashindwe kuendelea kukudai, lakini huu ni moto mwingine kama alivyosema baba, nife mimi au fedha zetu nizipate."


"Kijana sidaiwi senti tano na marehemu baba yako wala kifo chake mimi sihusiki."
"Mzee kabla ya baba kuondoka kuja kumuua nilimsikia mkizozana na akisema usipomlipa afe yeye au wewe lakini ulimuwahi kumuua."
"Ulikuwepo, mbona hamkunishtaki?"
"Sikujua kama muuaji ni wewe, lakini nataka utulipe fedha yetu, mambo ya kulipa uhai wa baba yangu siku nyingine."


"Ina maana unataka kuniua?"
"Unaogopa kufa wakati kuua ni kazi yako, naomba unipe kwa hiyari yako zaidi ya hapo utalipa ukiwa kwenye kitanzi."
"Usinitishe, Jooji," alipaza sauti.
Baada ya kuita alikuja jamaa mmoja mwenye mwili wa mazoezi na kuitikia wito,
"Naam bosi"
 
JOTO LA MAPENZI-15

ILIPOISHIA

"Kweli wewe ndiye nani?"
"Naitwa Aloys."
"Ooh! Aloys umekuwa nakumbuka ulikuwa mdogo, tena unafanana sana na marehemu rafiki yangu baba yako."
"Shikamoo."
"Marahaba, mama yako hajambo?"
"Hajambo."
"Ndiyo kijana, unasemaje?"
ENDELEA...


"Nilikuwa naulizia fedha baba aliyokuwa anakudai."
"Fedha?" mzee Samjo alijifanya kushtuka.
"Ndiyo, najua mpaka baba anakufa alikuwa anakudai zaidi ya milioni 150 kutokana na kukaa kwako muda wote tunataka fedha hiyo utulipe mara tatu."


"Kijana una kichaa baba yako alikuwa ananidai fedha gani na nilifanya naye biashara gani?"
"Japo najua madai ya haki yake ndiyo yalighalimu uhai wa baba yangu, lakini bado haiondoi deni. Kwa hiyo nipo hapa kwa ajili ya kulipwa fedha zetu."


"Kijana hebu ondoke nitakupoteza sasa hivi," mzee Samjo alimtisha Aloys.
"Mzee najua una vitisho vilivyomfanya mama ashindwe kuendelea kukudai, lakini huu ni moto mwingine kama alivyosema baba, nife mimi au fedha zetu nizipate."
"Kijana sidaiwi senti tano na marehemu baba yako wala kifo chake mimi sihusiki."
"Mzee kabla ya baba kuondoka kuja kumuua nilimsikia mkizozana na akisema usipomlipa afe yeye au wewe lakini ulimuwahi kumuua."


"Ulikuwepo, mbona hamkunishtaki?"
"Sikujua kama muuaji ni wewe, lakini nataka utulipe fedha yetu, mambo ya kulipa uhai wa baba yangu siku nyingine."
"Ina maana unataka kuniua?"
"Unaogopa kufa wakati kuua ni kazi yako, naomba unipe kwa hiyari yako zaidi ya hapo utalipa ukiwa kwenye kitanzi."


"Usinitishe, Jooji," alipaza sauti.
Baada ya kuita alikuja jamaa mmoja mwenye mwili wa mazoezi na kuitikia wito,
"Naam bosi"
"Naomba kijana huyu apotee, inaonesha hanijui."
Jamaa walimvaa Aloys na kuanza kumpa kipigo huku akisikia kauli ya mzee Samjo.
"Hakikisheni maiti yake haionekani."


Aloys alijua anakufa anajiona alijitutumua na kufanikiwa kurudisha mashambulizi ya kupambana nao kwa vile alikuwa akijiweza katika mapigano ya mikono aliwazidi nguvu. Mzee Samjo alitoka na bastola kwa ajili ya kummaliza kwa risasi baada ya kuona kijana amejiandaa kukabiliana naye. Risasi yake ilimkosa na kumjeruhi mmoja wa vijana wake, Aloys alifanikiwa kuwatoroka lakini hakufika mbali alipigiwa kelele za mwizi na wananchi wenye hasira kali walimpa kisago cha mbwa mwizi.


Polisi wa doria waliwahi kuokoa maisha yake, lakini alikuwa ameumizwa sana na kulazwa hospitali kwa mwezi mzima chini ya ulinzi akikabiliwa na kosa la jaribio la kuua. Mama yake siku zote alifika hospitali na kumwaga machozi huku akimwambia mwanaye:


"Unaona sasa baba ungekufa bure ona ukitoka lazima utafungwa mzee Samjo ana fedha sana."
"Wala mama usiogope, haki yetu tutaipata hata kwa ncha ya upanga," Aloys hakujutia kilichomkuta.
"Unaweza usitoke gerezani."


"Mama nitakuomba usilie hizi ni dalili za ukombozi hata bwana Yesu aliteseka msalabani kwa ajili ya mataifa. Mateso yake ndiyo ukombozi wetu nami vilevile nimejitoa lakini lazima fedha yetu itapatikana."
"Mwanangu kaa kimya kauli yako inaweza kukupoteza."
"Mama baba yupo wapi, hawezi kutumaliza wote."


"Baada ya kupona Aloys alipandishwa kizimbani na kuhukumiwa miaka saba kama mimi. Baada ya kukutana naye aliapa kulipa kisasi cha kifo cha baba yake kifungo bila hatia pia fedha za marehemu baba yake aliapa kuzirudisha kwa mkono wake.
"Alinieleza akitoka lazima alipe kisasi kwa vile hakuwa na silaha alinieleza lazima ataipata gerezani. Ndiyo siku ilipofika alipomkaba askari na kunilazimisha tutoroke. Lakini mimi niliishiwa nguvu na kuanguka shimoni yeye aliendelea.


"Baada ya mvua kunizindua toka shimoni nilianza safari lakini nilikutana na askari waliokuwa wakitutafuta. Njiani nilisikia Aloys ameuawa lakini silaha haikuonekana ikaonekana ninayo mimi. Msako mpaka sasa unaendelea kunisaka mimi na silaha ambayo sijui imefichwa wapi. Nina imani umenielewa vizuri?" Ambe alimaliza kusimulia mkasa wa Aloys Mabina ambaye alijua ni marehemu kutokana na kauli ya askari magereza.
"Nimekuelewa basi pumzika mengi tutazungumza kesho huenda una hamu ya kujua na mimi sababu ya kuwepo hapa?"
"Ni kweli babu."


"Basi pumzika kuna mgonjwa namuhudumia."
"Babu wewe ni mganga?"
"Utajua kesho."
Ambe alipumzika na kumwacha mzee Yamungu akienda kuhudumia mgonjwa aliyekuwa kibanda cha pili.
***


Siku ya pili baada ya mzee Yamungu kumuhudumia mgonjwa alikaa na Ambe ili amueleze sababu ya kuwa sehemu ile peke yake kama dume la nyani ‘gendaeka'.


"Babu mbona inaonekana kama umetengwa kwa jinsi unavyoishi?" Ambe alimdodosa.
"Ni historia ndefu, miaka kumi na nane iliyopita nilikuwa nikifanya kazi ya tiba asilia katika nchi jirani. Ukweli nilikwenda kule baada ya kuwa nakwenda kufanya huduma ya tiba hivyo mwenyeji wangu alinishauri nihamie kule nami nilikubali.


Kwa muda mfupi jina langu lilikuwa maarufu katika jamii kutokana na kazi yangu ya uhakika, wengi niliwasaidia matatizo yao. Kila kona walifika kupata huduma zangu ambazo nilikuwa sibahatishi. Niliweza kufahamika mpaka kwa viongozi wa nchi, katika kampeni zao za uchaguzi wengi walikuja kwangu. Kila niliyemsimamia alishinda kwa kishindo hata kama alikuwa hakubaliki kwa watu.


Pia wafanyabiashara ambao biashara zao zilikuwa zikisuasua niliwasaidia kuongeza wateja hivyo kupata vipato vikubwa. Wanawake waliopoteza mvuto kwa wanaume na wanaume waliopungukiwa nguvu za kiume ili kustawisha ndoa zao hata ambao hawakubahatika kupata kizazi kwangu walipata tiba ya uhakika.


Siku moja ambayo ilikuwa chanzo cha mkasa huu ninaokuhadithia, alikuja mwanamke mmoja ambaye alionekana mwenye maisha ya kifahari. Ilikuwa tofauti na wateja wengi kuja mchana, yeye alikuja saa moja na nusu usiku.


Baada ya kumkaribisha bila kumjua ni nani alinieleza matatizo ya mume wake.

ITAENDELEA KESHO...............
 
Back
Top Bottom