Kusoma Halal Badiri au Albadiri (Ahlul-Badr) Kwa Ajili Ya Kinga Na Kuapiza Ni Shirki Na Dhambi Kuu!
Albadir imetoka katika lugha ya Kiarabu lakini kupotolewa au kuandikwa na kusomwa makosa katika Kiswahili. Wapo wanaosema Alibadirilakini makusudio ni Ahlul-Badr, yenye maana watu wa Badr (wale waliopigana vita vya Badr). Badr ni sehemu iliyo karibu na Madiynah na ndio iliyokuwa sehemu ambayo Waislamu wakiongozwa na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) walipambana na mushirikina wa Makkah katika vita vya kwanza baina ya pande hizo mbili. Waislamu waliohudhuria walikuwa baina ya 313 – 317, lakini pamoja na idadi yao ndogo hiyo waliweza kuwashinda washirikina waliokuwa na idadi kubwa ipatayo mara sita yao.
Kisomo cha Ahlul Badri inakuwa ni kutaja majina ya Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) mmoja baada ya mwingine. Katika kutaja huko ni Imani ya mwenye kusoma hao Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) wanamsaidia kwa njia moja au nyingine. Ima kupata kitu alichopoteza au kilichoibiwa au kulaaniwa aliyefanya. Na hii katika Uislamu ni njia moja ya shirki ambayo Allaah Aliyetukuka na Mtume Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wameikema na kuipiga vita sana. Allaah Aliyetukuka Anasema:
“Hakika Allaah Hasamehe kushirikishwa, na husamehe yaliyo duni ya hilo kwa Amtakaye. Na anayemshirikisha Allaah basi hakika amezua dhambi kubwa” (4: 48). Shirki ni dhuluma kubwa sana.