UISLAMU HAUNA KITU KINACHOITWA ALBADIRI
Ninapenda kutoa elimu kiasi ninachoelewa kwa wale wote waliopanga kusoma wanachoita Albadir kwamba hakuna kitu kama hicho katika mafundisho ya Uislamu hata kama ni jambo linalotajwa na wengi na limekuwepo kwa muda mrefu na watu kuliamini.
Kwanza kimsingi ilipaswa itamkwe AHLUL BADR yaani maswahaba walioshiriki vita vya badir.
Kwa mujibu wa masheikh waongofu wa 'Ahlul sunna waljamaa' kisomo kinachoitwa Albadir au Alalbadiri kama wengine wanavyotamka hakina asili katika dini tukufu ya Kislamu hivyo ni ibada au kisomo cha kuzua.
Tukisema cha kuzua tunamaanisha hakufundisha kitu hicho Mtume wa Allah.Kila ibada au kisomo katika Uislamu lazima ifanywe/kifanywe kwa masharti mawili:Mosi kwa ajili ya kutaka radhi za Allah na pili kifanywe kama alivyofundisha Mtume (SAW).Hayo mawili yakikosekana hicho kitu ni takataka (uzushi/bidaa)
Ibada zote sahihi zina dalili (ushahidi) ktk sunna (mienendo ya Mtume) na/au Quran.
Inasemekana katika kisomo hicho wanataja majina ya maswahaba walioshiriki vita vya Badr huku wakifanya ushirikina wa madude ya ajabu ajabu kama malimao na sindano.
Hakuna kitu kama hicho katika Uislamu SAHIHI. Hakuna dua ya kuomba kupitia kwa watu. ANAYEOMBWA NI ALLAH MOJA KWA MOJA.
Kama ndivyo, kisomo cha aina hiyo bila shaka wanaotajwa ni mashetani na si vinginevyo na hivyo kinachofanyika ni ushirikina ambao kwa bahati mbaya sana unanasibishwa na Uislamu kimakosa sana.
Kama kuna watu wanataka kumshitakia Mungu ziko dua za kawaida za kisheria na haziitwi albadir na hazina masula ya kuapizana.
Ni vyema niungane na wengine waliojitokeza katika mitandao kuufahamisha umma ujue kwamba hakuna kisomo wala ibada katika uislamu SAHIHI inayoitwa Albadir.
Ni mambo ya hovyo kabisa yanayonasibishwa na Uislamu wakati hayana asili na dini hiyo tukufu.
_Mwandishi wa waraka huu ni Msomi wa Elimu dunia kwa ngazi ya Shahada ya Chuo Kikuu na ni Mbobezi kwenye Elimu Ahera._
_Pia ni Mwandishi wa Habari Mkongwe na amewahi kuwa Mhariri wa magazeti mbalimbali yakiwemo Sunset,The Guardian, Nipashe,Alasiri,Habari Leo n.k._
Nime-copy toka kwa khamis kibari