ASKARI wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), wameusambaratisha kwa mabomu ya machozi mkutano uliokuwa umeandaliwa na Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chacha Wangwe na kusababisha tafrani kubwa kwa wafanyabiashara na wateja waliokuwa wakifanya shughuli zao sokoni mjini hapa.
Tukio hilo lilitokea jana saa 8:00 mchana katika Uwanja wa Sabasaba mjini Tarime baada ya Wangwe ambaye pia ni Mbunge wa Tarime (Chadema) kutaka kuhutubia wananchi wa jimbo lake licha awali Jeshi la Polisi kuupiga marufuku mkutano huo.
Kutokana na tukio hilo, wafanyabiashara na wateja waliokuwa katika soko la mjini hapa, walikimbia ovyo na kutelekeza bidhaa walizokuwa wakiuza na walizonunua.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, David Saibulu alimwambia mwandishi wa Mwananchi muda mfupi baada ya tukio hilo kuwa walilazimika kuchukua hatua hiyo kwa sababu za kiusalama.
Saibulu alisema hivi sasa nchi jirani ya Kenya inakabiliwa na machafuko, hivyo jeshi hilo haliwezi kuruhusu maandamano wala mikutano ya hadhara ili kuepusha yanayotokea humo kutohamia nchini hapa.
Awali, polisi hao walimzuia Wangwe kuhutubia mjini Musoma, hatua ambayo ililaaniwa vikali na Wangwe huku akidai kuwa lazima wafanye mkutano huo vinginevyo atalishtaki jeshi hilo kwa kuwatia hasara kutokana na gharama zilizotumika kuuandaa na kukiuka Katiba ya nchi inyaowapa wananchi uhuru wa kujieleza, kutoa na kupata habari bila kizuizi.
Hata hivyo, habari za awali zilieleza kuwa Wangwe katika mkutano huo alikusudia kuzungumzia kuhusu Sh25 milioni zilizotolewa na mgodi wa madini ya dhahabu wa North Mara kwa ajili ya kuwasomesha wanafunzi.
Katika fedha hizo ilielezwa kuwa kila kata ilipewa mgao wa Sh7 milioni za awali kwa ajili ya ujenzi wa madarasa kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza pekee, ambazo zimeanza kutumika.
Pia alikusudia kuzungumzia kuhusu vigogo wanane wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugawiwa uwanja wa michezo uliopo Tarime kujenga nyumba badala ya vibanda vya maduka kwa wananchi, kitendo ambacho kimezua mgogoro kwa wakazi wa eneo hilo na mchango wa Sh10,000 kila kaya kwa ajili ya ujenzi wa madarasa.
Kabla ya tukio hilo, Wangwe aliwapongeza wanafunzi wa elimu ya juu kwa kufanikisha maandamano ya amani ya kupinga wizi wa kura na kulaani mauaji ya wananchi wananchi wasio na hatia nchini Kenya.
Akizungumza na umati mkubwa wa wananchi wa mji mdogo wa Sirari ulioko mpakani mwa Tanzania na Kenya waliokwenda kumpokea jana, Wangwe alisema maandamano hayo yanadhihirisha kuwa wapo pamoja na wananchi na vyama vya upinzani katika dhamira ya kukemea maovu yanayopinga demokrasia na haki za binadamu.
Wangwe alilaani hatua ya polisi ya kumzuia kufanya mkutano mjini Musoma akisema kwamba, kitendo hicho ni cha kuwanyima wananchi uhuru wa kuwasikiliza viongozi wao na kupata habari.