Afrika kwa ujumla na hususan Tanzania (baada ya Uhuru) Polisi wamekuwa ni watu wa kuogopewa na jamii kama vile nyoka.
Nnakumbuka miaka ya mwanzoni mwa nchi yetu kupata Uhuru Polisi walikuwa ni watu wanaopendwa na jamii, enzi hizo ilikuwa utawakuta polisi wa Kizungu, Kihindi, Kiarabu na Kiafrika.
Kama watoto, kila mmoja wetu alikuwa anatamani siku moja awe askari Polisi. Kilichotupelekea kuwa hivyo ni jinsi enzi hizo polisi walivyokuwa na upole kwa watoto, nnakumbuka wakija mashuleni kutupa mafunzo ya kila aina na kutueleza vipi tuwe raia wema wenye kusaidia wengine. Nnakumbuka pia polisi wakituvusha barabara kwa upole na ingawa magari yalikuwa si mengi.
Nnachokikumbuka zaidi kwa polisi wa siku hizo ni tabasamu zao, awe wa kiume au wa kike (wa kike walikuwa wachache sana), ilikuwa siku zote nikiwaona polisi amma njiani amma wakija mashuleni walikuwa na tabasamu lisilokwisha na wenye nyuso za furaha kiasi cha kukufanya uliye karibu nao uwe na amani.
Hayo yaliisha mara tu baada ya kutangazwa azimio la Arusha.
Baada ya hapo mpaka hii leo, Polisi wamekuwa ni watu wasiocheka na watu, polisi imekuwa ndiyo tishio kwa watoto, mtoto wako akikosa ukimtajia polisi basi anaingiwa na uoga.
Jee, tumejiuliza kwanini? Mimi nna-majibu mengi sana kuhusu hilo lakini nnawaachia wachangia mada nanyi mjinafasi na kutoa dukuduku lenu kwa mtazamo wenu.
Paul Makonda, ameweza kuwasema polisi hadharani, tena kinaga ubaga. Mwiko ambao hata wakubwa zaidi ya Makonda kwenye uongozi wameshindwa kuuvunja kwa hapa kwetu Tanzania na nchi nyingi za Kiafrika kwa ujumla. Jee, kwanini?
Binafsi nnaona kitendo cha Makonda ni cha kishujaa sana. Wewe jee?
Nnaomba tuchangie hii mada huku tukielekeza maoni yetu kwa viongozi wa nchi pamoja na viongozi wa majeshi ya polisi kwa nia ya kuitaka polisi iwe rafiki zaidi wa wananchi na iwe ni kwa ajili ya wananchi na si kwa ajili ya viongozi wa nchi au watawala wa nchi pekee.