Waziri wa Afya wa Kenya, Bi. Beth Mugo, amewakemea waganga wa kienyeji na wale wanaojigamba kwamba wanaponya kwa imani. Amesema kuwa serikali haitawaacha waipotoshe jamii kwamba wanaweza kuponya magonjwa yote.Aliyasema hayo katika sherehe za kuadhimisha siku ya Kifua Kikuu duniani. Aliendelea kusema kwamba waganga wa kienyeji wanahatarisha afya ya Wananchi. Alisema kitendo cha waganga hao wa kienyeji kudai kwamba wanaweza kuponya magonjwa sugu kama vile Ukimwi, kimesababisha magonjwa hayo kuenea zaidi kwa watu wengine. Aliendelea kusema kuwa huo ni uongo unaowafanya watu wachanganyikiwe.
Vile vile Bi Mugo amezitupilia mbali taarifa za vyombo vya habari kuwa mganga wa kienyeji anayejulikana kama babu huko Loliondo Tanzania, anaponya maradhi sugu, kwa kuwapa wagonjwa dawa inayotokana na mti wenye sumu. Bi. Beth Mugo ameiomba serikali ya Tanzania ikifunge kituo hicho cha Loliondo na kuwapiga marufuku watu wanaokwenda kwa babu huyo. Amedai kuwa watu wanaokwenda huko wakirudi wataeneza zaidi Kifua Kikuu na Ukimwi. Tutakapokutana huko Burundi na Mawaziri wengine wa Afya wa nchi za Afrika Mashariki , nitamuomba Waziri wa Afya wa Tanzania, amtie gerezani babu huyo na kuipiga marufuku biashara yake ya uganga alisema Bi. Mugo. Habari hizo ni kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Kenya, KBC.
Wakati huo huo Waziri wa Afya wa Tanzania naye pia amewakaripia vikali waganga wa kienyeji waache kudai kwamba wanaweza kuponya magonjwa sugu kama Kifua Kikuu. Hata hivyo, haijaeleweka wazi iwapo karipio hilo linamhusu pia babu wa Loliondo.
Babu wa Loliondo pamoja na kujiita mchungaji anaingia pia katika kundi la waganga wa kienyeji maana misingi ya tiba yake haitofautiani na ile ya waganga wengine wa kienyeji.
Kwa heshima na taadhima tunaiomba serikali yetu impige marufuku wazi wazi babu huyo ili kudumisha amani na utulivu uliopo kati ya Tanzania na Kenya. Babu asitusababishie chuki, uhasama na mgawanyiko kati yetu na Wakenya. Ni kweli, baadhi ya viongozi wa serikali yetu nao pia wamepata kikombe, kwa sababu hiyo wanaweza kuona aibu kumpiga marufuku babu. Tunaomba wasione aibu, maana wao pia sio malaika, ni wanadamu wanaoweza kukosea kama wengine. Kwa sababu hiyo wasilifumbie macho tamko hilo la Waziri wa Afya wa Kenya. Waziri huyo wa Kenya ametema cheche zinazoweza kutuongezea matatizo makubwa tuliyo nayo ya kiuchumi na kijamii. Wahenga walisema dalili ya mvua ni mawingu, na kinga ni bora kuliko tiba. Wakenya tunawategemea kwa mengi, wasije wakatufungia mpaka tukakosa bidhaa zao. Maduka mengi hapa TZ yamejaa bidhaa za Kenya kuanzia mafuta, sabuni, vinywaji, nguo mpaka pipi. Inaonekana viwanda vyetu vinashindwa kuzalisha bidhaa bora.
Makampuni ya uchapaji, ya TZ, yaliyopo jirani na Kenya yanategemea sana kupata karatasi na vifaa vya uchapaji kutoka Kenya maana huko vinapatikana kwa bei nafuu. Sio hilo tu kuna Watanzania wengi waliopeleka watoto wao Kenya ili wajue vizuri Kiingereza maana shule nyingi za TZ hazina walimu wazuri wa lugha hiyo muhimu kwa mawasiliano kimataifa.
Dawa nzuri za kutibu hata mafua na kikohozi, ukiingia katika maduka ya madawa, utaona zimeandikwa Made in Kenya! Hata wanaotaka kuagiza magari kutoka Japan, wanaona nafuu magari yao yapitie bandari ya Mombasa, Kenya, maana bandari yetu ina ukiritimba mwingi na inachelewesha sana utoaji wa bidhaa.
Tembelea maduka ya vifaa vya ujenzi mjini Arusha, utashangaa kuona vifaa vizuri vya ujenzi, kama vile ceiling board, vimetoka Kenya. Siwapigii debe Wakenya, ila ukweli ndio huo tunawategemea kwa mengi ndio maana hata suala la Jumuia ya Afrika Mashariki bado linasua sua maana tunaogopa Wakenya watazidi kuushusha chini uchumi wetu.
We babu wa Loliondo, usiwafanye Wakenya watuchukie bure kwa sababu yako. Tukakosa hata Panadol(made in Kenya) ya kutibu maumivu ya kichwa. Usisahau Obama asili yake ni Kenya. Na Obama akiamua kuingilia suala lako, na kutuletea manowari na mizaili zake, kama alivyofanya kwa Kadafi, dawa zako haziwezi kumzuia. Kama hukupata mshahara mzuri kabla hujastaafu uchungaji, usitake kuwapora Watanzania walalahoi, pesa ndogo wanayoipata kwa shida, maana mishahara yao haitoshi hata kulipia nauli ya kuja huko Loliondo, mpaka wasafirishwe bure na Wabunge wa Chadema!