Historia ya Wahima na eneo la magharibi ya Tanganyika kama ilivyoandikwa ndani ya kitabu Zamani mpaka siku hizi

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Jan 31, 2021
7,224
12,729
zamani_cover_with_bgc.png


Kitabu hiki kilichapwa mara ya kwanza mwaka 1930.

HABARI ZA NCHI ZILIZO MAGHARIBI

Somo 1-Wahima

KATIKA sura ya kwanza tulisoma ya kuwa sisi Wabantu si watu wa asili wa nchi tunazokaa sasa maana tulitoka nchi nyingine tukawasukuma watu waliokuwa wakikaa huku au labda tulichanganyika pamoja nao. Hatuna hakika miaka mingapi imepita tangu tulipoanza kuhama kuja katika nchi hizi, lakini imedhaniwa inapata miaka 2,000 mpaka 3,000. Basi tukaja tuakenea pote tukatawanyika tukafanya makabila mengi na lugha vile vile iligawanyika ikafanya lugha nyingi.

Lakini hatukuachiliwa kukaa peke yetu, na baada ya miaka mingi, watu waliokuwa wakikaa kaskazini walianza kuingia katika nchi hizi kama sisi tulivyoingia zamani sana. Labda walikuwa wale wale waliosukuma babu zetu wakawafanya kuhama kutoka nchi zile walizokaa zamani katika kaskazini. Yaani sisi tulisukuma Watukoko na Wabilikimo tukakaa katika nchi yao, na halafu sisi tulianza kusukumwa na watu wengine. Watu hawa hawakuingia katika nchi hii, lakini wameacha alama za nguvu zao na kwa hiyo imetuhusu tujue habari zao. Hatuna maandiko wala sanamu zinazoweza kutusaidia kueleza habari zao wala kujua walikuja zamani gani, lakini pengine tumehadithiwa watawala wangapi waliotawala katika nchi fulani na hivi tunaweza kukisia tarehe.

Tena tunaweza kujifunza habari zao kidogo kwa habari walizozikusanya Wazungu wa kwanza waliokuja kusafiri katika nchi hizi.

*****

Basi katika sura hii tutasimuliwa habari za sehemu ya nchi iliyo katika magharibi ya kaskazini mwa Tanzania, yaani wilaya za Bukoba, Mwanza, Tabora na Kigoma.

Wenyeji wanaokaa katika sehemu hii ya nchi yetu ni wengi sana, jumla yao ni sehemu ya tatu kwa moja ya wenyeji wote wa Tanzania. Watu hao wote ni Wabantu ila kuna wachache wenye damu ya wageni, lakini watawala walio wengi si Wabantu ila ni wageni. Watawala hao waliojiweka juu ya wenzao ni Wahima, na asili yao wametoka katika taifa la wale watu waitwao Wahamiti waliotoka Kaskazini.

Labda zamani Wahima hao walifanana na Wamasai wanaokaa katika nchi yetu sasa, nao vile vile walitembeatembea wakitafuta malisho kwa makundi ya wanyama wao, lakini baadaye walifuata desturi ya kukaa mahali pamoja kama wanavyokaa Wabantu. Labda walipigana na Wabantu wakawashinda, au labda Wabantu walijiweka chini yao kwa hiari zao, hatuna habari.

Wahamiti hao wanakaa hasa katika nchi ya Ruanda, na hapo wanaitwa Watusi. Hata leo wanajulikana kwa kuwa ni watu warefu tena wembamba, na sura zao ni za kipanga, na rangi yao ni nyekundu kuliko ile ya Wabantu. Watu hao ndio walioleta ng'ombe wale wenye pembe ndefu sana kutoka kwao ambao tunaweza kuwaona Bukoba, na Ankole, na Ruanda na mahali pengine ambapo Watusi walipojiweka kuwa wakubwa wa nchi.

Watu wenye maarifa juu ya mataifa hukubali kuwa Wahima ni Wahamiti, na hudhani ni Wagala au taifa jingine lililo asili ya Wasegeju na Wamasai. Ni ajabu sana ya kuwa karibu kila mahali wanapokaa watu hao katika nchi yetu, lugha yao ya asili imewapotea na sasa hutumia lugha ya watu walioshindwa nao na hata wakitaka kutaja babu zao huwaita kwa majina ya Kibantu. Lakini wengine wanayo lugha ya Kihamiti hata sasa, kama vile Wamasai na wengineo.

Kama tulivyosema, hatuwezi kujua hakika Wahima hao walifika lini katika nchi hii mara ya kwanza, na kwa kuwa habari zao za zamani zimechanganyika sana na hadithi, hatuwezi kupambanua zilizo za kweli na zilizo hadithi tu. Lakini Padre mmoja wa Misioni ya Kikatoliki huko Uganda amezichungua sana, kwa hiyo tutafuata maneno yake katika kusimulia habari zao. (Père Julien Gorju, ndiye aliyetunga kitabu cha Kifaransa chenye habari za Wahima kiitwacho 'Entre le Victoria, l'Albert et l'Edouard'.)

Wahima wote wanajua asili yao walitokea nchi za kaskazini, na ya kuwa ufalme mkubwa ulisimamishwa na babu zao katika nchi ya Bunyoro, tena husema kuwa watawala wote wa Wahamiti walitokea ufalme huo. Bunyoro si katika nchi yetu ila ni katika nchi ya Uganda, lakini inatuhusu tujue habari hizi kwa sababu watawala waliotoka huko walijiweka katika nchi yetu pia. Ufalme huo uliitwa Kitara ukasimamishwa zamani kabla ya kusimamishwa ufalme wa Buganda unaoendelea hata sasa. Hatujui Kitara ulisimamishwa zamani gani, lakini tunajua kuwa ni zamani sana kwa sababu tunayo hakika kuwa wafalme 32 au pengine wanahesabiwa kuwa 36, wametawala katika ufalme wa Buganda, na kama tulivyosema, Kitara ulisimamishwa kabla hajaanza kutawala yule mfalme wa kwanza wa Buganda.

Watu waliosimamisha ufalme huo wa Kitara walikuwa Wahamiti. Lakini ufalme wa Kitara haukudumu miaka mingi sana ukaisha. Labda watu wa jamaa au ukoo mwingine walishindana ili kusudi wapate utawala, au labda waliugawanya ufalme sehemu nyinginezo.

Wakati huo Wahamiti walikuwa wakihama kutoka kaskazini wakitafuta nchi nyingine ili wapate mahali pazuri pa kukaa, au labda walikuwa wakisukumwa na watu wengine waliokuwa wakikaa kaskazini zaidi, hatuna hakika. Lakini huelekea kuwa kweli, maana kama ilivyo katika historia ya nchi za dunia ndivyo baba zetu walivyokuja wakawasukuma Watukoko na Wabilikimo, tena ndivyo Wahamiti walivyotusukuma sisi Wabantu tuliokaa kaskazini.

Basi miaka ikapita na zamani ya mwaka 1,300 hivi, watu wengi zaidi walihama kutoka kaskazini pamoja na mkubwa wao aliyeitwa Ndahura, wa jamaa ya Bachwezi. Ndahura alikuwa na nguvu, maana alisimamisha ufalme mkubwa sana ulioenea kutoka Ziwa Albert mpaka Ziwa Victoria, na ufalme huo uliitwa Kitara vile

****

vile. Ufalme huo ulisitawi sana na hasa wakati aliotawala mfalme mmoja aitwaye Wamala, lakini ndipo habari za jamaa hiyo ya Bachwezi zikakoma kabisa. Wengine husema kuwa jamaa ilitoweka, lakini sasa watu huhadithia kwamba watu wa jamaa hiyo waligeuka miungu! Imedhaniwa ya kuwa wakati huo ulikuwa katika miaka iliyo karibu na 1675.

Basi huku nyuma ufalme mwingine ulisimamishwa katika nchi ya Bunyoro na mtu jina lake Mpugu wa kabila moja la Wahamiti. Mpugu alianzisha jamaa ya Babito akaitwa Mpugu kwa sababu alikuwa mweupe kidogo, au labda alikuwa zeruzeru. Baba yake Mpugu alikuwa wa jamaa ya Bachwezi akaitwa Kyomya. Imehadithiwa kuwa Kyomya alitembeatembea sana mpaka alifika kilima kiitwacho Elgon katika nchi ya Kenya, na hapo alikutana na mwanamke chini ya mti unaoitwa Bito akakaa naye, na halafu yule mwanamke alizaa pacha. Mtoto mmoja aliitwa Mpugu na wa pili aliitwa Kintu.

Basi baadaye Mpugu alisafiri akafika mji mkuu wa Bachwezi akaushika ufalme, lakini wakati huo aliitwa kwa jina jingine, ndilo Wunyi. Mwingereza mmoja Baker alisafiri katika nchi hizi katika mwaka 1871 ili apeleleze habari za mito na milima na maziwa ya nchi, naye ameandika habari kuwa alikutana na mfalme mmoja aliyekuwa wa kumi na tatu kutawala tokea wakati ule aliotawala Wunyi.

Yule mtoto wa pili, Kintu, alisimamisha ufalme mwingine. Watu wengine husema kuwa Kintu alikwenda akashika ufalme wa Ntege aliyekuwa mkubwa wa Buganda wakati ule, lakini alimwacha atawale chini yake. Baadaye Kintu alitoweka na Ndahura aliyekuwa mfalme wa kwanza wa jamaa ya Bachwezi aliyetawala katika Bunyoro, alimwua Ntege, akampa mwanawe Kyomya ufalme wa Buganda kuutawala.

Ufalme mwingine ulisimamishwa Toro na mtu wa jamaa hiyo hiyo, na George David Kumurasi Rukidi III anayeitawala nchi hiyo sasa ni mfalme wa kumi na moja kutawala tokea uliposimamishwa.

Mpaka sasa tumesimulia habari kidogo za nchi zilizo jirani na nchi yetu ili tufahamu vizuri mambo yaliyotokea halafu katika nchi yetu. Basi sasa na tuache tukasimulia habari za Wahima waliokuja wakakaa katika nchi yetu ya Tanganyika.

Katika nchi ya Bukoba kwa upande wa kusini mwa mto uitwao Kagera kuna nchi inayoitwa Kiziba; huko ufalme ulisimamishwa na Kaganda, mtu wa taifa lile lile la Wahamiti. Katika hadithi ya Kibunyoro imesimuliwa kwamba Kaganda ni mwanawe Wunyi yule tuliyemtaja, naye ndiye aliyeusimamisha ufalme wa Babito katika Bunyoro. Lakini hadithi ya Kiganda inasimulia kuwa Kaganda ni mwanawe Kintu aliyekuwa mfalme wa kwanza wa Buganda. Basi Kaganda alitoka kwao Kyagwe akafika Buddu iliyo upande wa kaskazini mwa mto Kagera. Kutoka huko alisafiri mpaka Buyaga kando ya Ziwa Victoria, alipotoka huko alivuka kisiwa Sese. Kutoka Sese alisafiri tena mpaka Bwende katika ghuba iitwayo Sango, na mwisho alisafiri akafika Kyawa.

Tumetaja safari hizo kwa sababu zingali zinakumbukwa na watu wa huko, maana zinaonyeshwa katika desturi zinazoshikwa wakati wa kumweka mtawala mpya. Mtawala mpya huogeshwa kwa heshima kwa maji yanayoletwa kutoka Kibiro iliyo kando ya Ziwa Albert, tena hutiwa chumvi inayoletwa kutoka Kitunga iliyo katika nchi ya Buddu mahali alipokaa Kaganda kwa muda, na hapo ndipo alipowaacha wengine wa wafuasi wake. Mioto yote katika nchi huzimwa, na moto mwingine huletwa kutoka kisiwa cha Sese, kwa sababu yasemwa Kaganda alichukua moto unaoheshimiwa sana na Wanyoro akauacha Sese, na kwa hiyo alirudi huku kutoka Bwende ili aje auchukue.

Basi alipokuwa akitoka kaskazini, Kaganda alifika Kyowa, na hapo alikutana na mwana wa mfalme aliyekuwa amefukuzwa kutoka Kiziba, akafanya shauri naye la kumwua Ntumwa aliyekuwa mfalme wakati huo. Shauri lao likafanyika, na yule mwana wa mfalme aliushika ufalme, na Kaganda akawa waziri wake. Hatimaye yule mwana wa mfalme alikufa, na Kaganda alishika ufalme wa Kiziba akautawala. Basi hii ndiyo namna alivyopata ufalme wake. Lakini tendo hili la kuuliwa mfalme wao liliwachukiza sana wenyeji wa nchi kwa sababu walisadiki kuwa ni ishara mbaya itakayowaletea misiba na taabu. Basi tokea wakati huo walimwita Kaganda kwa jina la 'Kibi' na maana yake ni 'Kiovu' au 'Kibaya'. Imesemwa ya kuwa Kibi aliishi sana mpaka akawa mkongwe, akafa akazikwa mahali kaskazini mwa mto Kagera, yaani kukumbuka mahali alipotokea.

Kabla ya kufa kwake, Kibi aliusia kwamba mwanawe Samula awe mfalme baada ya kufa kwake, lakini jamaa ya yule Ntumwa mfalme aliyeuawa aliweza kuushika tena ufalme kwa muda, mpaka Samula alipata msaada wa mfalme wa Buganda wakamfukuza yule jamaa ya Ntumwa. Ndipo Samula alipopata jina la Nyakabinga' maana yake, 'Yule aliyefukuza.'

Samula hakupenda watoto wake wala wakubwa wa taifa lake wadhaniwe kuwa wenyeji, yaani Wabantu, hivi aliwaita kwa majina ili asili yao isisahauliwe, akawaita watoto 'Waziba' na wakubwa wa nchi aliwaita 'Wahima.' Tena hakupenda wachanganye damu na ile ya wenyeji, na kwa muda mrefu wana wa mfalme walioa watoto waliozaliwa na wale waliofuatana na Kaganda kutoka kwao. Hata sasa jamaa za watawala wanaheshimu sana miiko ya kabila la Babito, lakini mtawala mwenyewe hufuata desturi ya Kiganda, yaani hushika mwiko wa jamaa za mke wake ili kusudi kuwaheshimu. Desturi hiyo ililetwa na Kimera wa Buganda.

Hatujui tarehe alipoanza kutawala Kibi, lakini tokea wakati wake, wafalme kumi na watano wa jamaa yake wametawala ufalme wa Kiziba mpaka Mutahangarwa alipoanza kutawala. Mutahangarwa alikufa katika mwaka 1916.

Sasa tuchungulie kidogo habari za ufalme wa Wahinda. Kuna nchi nyingine inayoitwa Kiziba ya Kusini, na pengine inaitwa Ihangiro, lakini lazima tukumbuke ya kuwa ni mbali mbali na nchi ya Kiziba tuliyokwisha taja. Tulisimulia kuwa watu walidhani ukoo wa Bachwezi wa Bunyoro walitoweka kabisa wakageuka nchi nyingine wapate kuzishinda. Hadithi zinashuhudia kuwa miungu, lakini kwa kweli haikosi walihama kwenda kutafuta ufalme huu ambao tutasimulia habari zake sasa, ulisimamishwa zamani ya mwaka kama 1675, yaani wakati ule walipotoweka jamaa ya Bachwezi.

Imehadithiwa ya kuwa mtu aitwaye Ruhinda au Luhinda alihama kutoka kwake akaenda Buddu, kisha akaondoka akaenda Koki. Labda Bachwezi walishindwa au labda walihama kutafuta nchi nyingine, yaani walitoweka, na Ruhinda alikuwa mmojawapo waliohama. Basi alipofika Koki alikutana na mhunzi mmoja aliyetoka nchi ya Uzinza, ambayo ni nchi inayojulikana sana kuwa nchi ya wahunzi wa jamaa ya Warongo. Mhunzi huyo alianza kueleza habari za nchi ya Uzinza na Ruhinda aliposikia kuwa mfalme wa nchi hiyo ni mtu dhaifu, aliazimia kwenda huko. Alipofika, alijidai kuwa mganga mkubwa awezaye kuleta mvua, na baada ya kupita muda alipata nguvu akajifanya mtawala wa nchi ya Uzinza na Ihangiro na Karagwe na Urundi. Lakini halafu alipokuwa akisafiri kwenda Kagera kutoka Ihangiro alikufa katika kijiji kiitwacho Lwazi, na ule ufalme aliousimamisha ulivunjika ukagawanywa katika sehemu tatu, yaani Uzinza na Ihangiro, na Urundi na Karagwe.

Nchi ya Ankole iliyo jirani inatawaliwa na Wahima, nao hudai ya kuwa wametokea ukoo wa Ruhinda. Lakini yule Padre tuliyemtaja kuwa amechungua sana katika habari hizi, anadhani kuwa hawakutokea jamaa ya yule Ruhinda aliyetawala Uzinza na Karagwe na Ihangiro, ila labda ya Ruhinda mwingine.

Imesemwa kuwa Ruanda pia ilikuwa katika ufalme huo wa Wahinda, lakini hatuna habari safi juu ya hayo, na kwa kuwa Ruanda si sehemu ya Tanzania, basi habari zake hazituhusu sana. Yatosha kusema kuwa Watusi ambao ni kabila kuu la Ruanda, ni damu moja na Wahinda, yaani wale wanaoitwa pengine Wahima na pengine Wahuma. Tena imehadithiwa asili ya jina hilo Tusi ni jina la milima mirefu iliyo upande wa magharibi inayoitwa Ututsi na Warundi, na labda watu hawa Wahamiti walipewa jina hilo na wenyeji wa nchi hiyo.



Somo 2-Kuendelea na habari za Wahima

Ruhinda alipokufa, ufalme wake uligawanywa katika sehemu tatu, na wafalme wa Karagwe, yaani sehemu moja na ufalme, walitwaa majina ya Ruhinda na Ntare. Wa kwanza aliitwa Ruhinda na wa pili Ntare, na wa tatu Ruhinda na kuendelea hivi kwa vizazi kumi na moja. Wafalme kumi na wanane walitawala katika ufalme huo. Mwingereza mmoja jina lake Speke aliyesafiri katika nchi hizi kutafuta habari nyinginezo, alifika hapa katika mwaka 1861 akamkuta Rumanyika mwanawe Dagara akitawala nchi. Rumanyika alimpokea vizuri sana akamfurahisha kwa ajili ya akili na wema wake. Speke aliandika kitabu chenye habari za safari zake, na tukikisoma tutaona kuwa Rumanyika alikuwa mtu mwenye nguvu nyingi, na watawala wengine wa Kihinda walikubali kuwa yeye ni mkubwa wa jamaa yào, na mfalme wao.

Kwa muda kidogo ufalme huo wa Karagwe uliharibika, maana nchi ya Ihangiro ilitengwa ikawa ufalme wa peke yake ukatawaliwa na mtu aitwaye Sebahinda. Lakini baadaye uliunganishwa tena na Wadachi, na Kahigi aliyekuwa jamaa wa Sebahinda ambaye alipendwa sana na Wadachi, alipewa ufalme kwa sababu walitaka kumfurahisha. Kahigi alikufa katika mwaka 1916. Wahinda wanaotawala kisiwa cha Ukerewe walitoka Ihangiro, na Makaka aliyeanza kutawala katika mwaka 1895 ni mtawala wa kumi na nane tangu walipokiteka kisiwa.

Nchi ya Uzinza, yaani Usui iliyo katika wilaya ya Bukoba, na Uzinza katika wilaya ya Mwanza zilikuwa zikitawaliwa na mtawala mmoja wa Kihinda mpaka katika enzi ya Dagara wa Karagwe, ndipo alipotawala Rwona au Lwoma, na Dagara alimshauri kugawanya nchi na kufanya falme mbili. Basi watoto wa Rwoma, Suwarora na Ruhinda, walipewa kila mmoja sehemu yake. Suwarora alipewa nchi ya Usui na Ruhinda alipewa Uzinza iliyo upande wa Mwanza.

Baada ya kupita muda, Uzinza uligawanywa tena ukafanywa falme nne, ukakaa hivyo mpaka mwaka 1926, ndipo sehemu hizo zilipounganishwa kuwa ufalme mmoja ukatawaliwa na mtu mmoja aliyechaguliwa na wenyeji waliotoka Ukerewe.

Mhinda mmoja alisimamisha ufalme mwingine ulio mdogo, na nchi zilizokuwa katika ufalme huo ni Kiyanja na Kyamtwala na Bugabo, lakini hakuweza kuzishika, na Bankango wa Usui akaja akamnyang'anya nchi za Kyamtwala na Bugabo akamwachia nchi ya Kiyanja tu.

Haya ni majina ya utawala wa Uzinza na Ihangiro: Ruhinda; Ntare (huyu alifia kisiwa kiitwacho Kome); Kabambo Katobaa; Kabula; Nyamulasya (huyu alifanya Kome kuwa mji wake mkuu); Kyeda; Kinwa; Kabambo wa pili; Kabula wa pili; Kakalaza (huyu alifanya Butendwe kuwa mji wake mkuu akafia safarini wakati alipokuwa akienda Uha); Mwiyakabi; Ruhinda wa pili (huyu alipewa jina la Muhangakyaro baada ya kufa kwake).

Kabla hatujaacha kusimulia habari za nchi zilizo karibu na Ziwa Victoria na Ziwa Albert na Ziwa Tanganyika, inafaa tutazame kidogo dalili za utawala wa Wahamiti zinazoonekana pengine katika nchi hizo.

Nchi za Nera na Buhungukira na Usmao ni katika upande wa mashariki wa Uzinza katika wilaya ya Mwanza. Imesemwa kuwa nchi hizo zilikuwa ufalme mmoja ulioanzishwa na mtu mmoja jina lake Wile. Imehadithiwa kuwa huyu Wile alitoka Uzinza akaonana na mwanamke mmoja aitwaye Mhindi, na yeye vile vile alikuwa ametoka Uzinza. Basi walikaa pamoja wakashika nchi wakaitawala na walipokufa, mwana wao Solasi alirithi ufalme. Solasi alipokufa nchi iligawanywa sehemu tatu na nduguze wanawake walizirithi, ndipo zilipoitwa Nera, na Buhungukira na Usmao. Nchi hizi hazikuunganishwa tena mpaka mwaka 1927, ndipo alipoanza tena kutawala mtu mmoja.

Jina la nchi waliyotoka watu hao, yaani Uzinza, na jina la yule mwanamke Mhindi ambalo labda lilikuwa Mhinda yaonyesha dalili ya asili ya watawala hao. Tena mtawala wa Nera asema kuwa jamaa zake ni Watusi, na kwa hakika sura yake inaonyesha dalili ya kabila hilo. Dalili nyingine inayofaa kukumbuka ni ya kuwa tambiko na sadaka hufanyiwa babu zake Solasi, na mzee anayezitoa huitwa Mgabe, na jina hilo linatumika kuita watawala wa Uzinza.

Wasukuma husimulia habari za Mungu wa magharibi anayeitwa Luhinda, lakini labda hadithi zinachanganya jina la Luhinda na Mungu kwa sababu ya nguvu zake na namna alivyoanzisha utawala wa Kihinda. Kwa hakika haiwezekani kukanushwa kuwa ufalme huo wa Usukuma kwa asili yake ni wa Kihinda, tena imesemwa kuwa wenyeji wa Usmao walitoka Uzinza.

Tukizidi kwenda kuelekea upande wa mashariki tutawakuta Wabinza, na watu hawa husimulia habari za mtawala wao wa kwanza aliyeitwa Nkande. Husema kuwa alitokea upande wa magharibi ya kusini mwa Ziwa Victoria, yaani nchi iliyo upande wa mashariki ya Uzinza. Nkande aliwashinda watu wa Mwagala akatawala nchi yote iliyopakana nayo, lakini baada ya kupita miaka kadha wa kadha ufalme ulivunjika wala haukusimamishwa tena na kuwekwa chini ya mtawala mmoja mpaka mwaka 1927.

Basi kwa kadiri tujuavyo, falme hizo zilikuwa za mwisho katika upande huo wa mashariki wa magharibi zilizotawaliwa na Wahinda.

Turudi tena kwenda magharibi tuzidi kutazama dalili zilizopo za utawala wa Wahinda. Usambiro ni nchi iliyo upande wa kusini mwa Uzinza, na sehemu yake imo katika ufalme wa Uzinza wa siku hizi. Imesemwa kuwa wenyeji wa Usambiro walitoka Uzinza na watawala wao hudai kwamba walitoka Bunyoro. Kwa

****

pande zile za kusini kuna nchi ya Usumbwa na huko watawala wengine hudai kuwa ni kabila la Watusi au Warongo, yaani kabila la wahunzi waliofanana na kabila lile la wahunzi linaloitwa El Konono walio katika kabila la Wamasai.

Hatuwezi kusema kwa dhahiri kuwa watu wanaokaa upande wa kusini zaidi wana damu ya Wahamiti, lakini mtu mmoja aliyechungua sana habari hizo, asema kuwa watawala wa asili wa Unyamwezi wengi ni Wahima. Lakini habari hizo haziwezi kuhakikishwa sasa, tunaweza kubahatisha tu. Maana miaka mingi sana imepita na watawala wa Unyamwezi waliotawala katika miaka hiyo ni wengi mno, na hivi ni vigumu kuthibitisha jamaa au ukoo wa wale waliotawala kwa asili.

Kwa upande wa magharibi kuna nchi ya Uha, na watawala wa nchi hiyo kwa hakika ni Wahima, nao wanajua asili yao.



Somo 3-Wafipa

Sasa tutasoma habari kidogo za Wabantu wengine waitwao Wafipa wanaokaa upande wa kusini mwa magharibi, na kumbe, hata huko twaona ya kuwa kabila hilo la ajabu, yaani Wahima, lilienea na kufika mpaka upande wa kusini mwa Ziwa Tanganyika. Kwa miaka mingi kabla hawajafika Wahima hao, yasemwa kuwa Wafipa walitawaliwa na watawala wadogo, na mkubwa wao aliitwa Mwene Milanzi. Basi katika zamani za Mwene Milanzi mmoja aitwaye Ntatakwa, kundi la wageni lilifika nchi yake wakati mwenyewe hakuwako. Wageni hao walikuwa warefu, tena weupe kidogo na sura zao zilikuwa za kipanga, na tena walikuwa kama watu wenye kiburi mno. Katika watu hao walikuwamo wanawake watatu, na mmoja wao jina lake Mwati alikuwa akichukua jiwe. Mwanamke huyo aliomba kiti apate kupumzika. Basi mke wa Ntatakwa alipoona jinsi walivyo na kiburi aliogopa, akatoa kiti cha kifalme akampa akikalie. Imesimuliwa katika hadithi hii ya kuwa asubuhi yake huyo mwanamke Mwati alichukua jiwe lake akapanda nalo mpaka juu ya mlima uitwao Itweleli, na hapo akatangaza habari ya kuwa amekwisha ichukua nchi yote iwe yake. Ntatakwa aliporudi hakufanya matata hata kidogo, bali alikubali kwa unyenyekevu, maana alisema kuwa amekwishaonywa na mzuka ya kuwa wageni watakuja na kushika nchi yake, akaridhika.

Hadithi nyingine husimulia ya kuwa Mwati alimwuliza Ntatakwa nchi yake inafika mpaka wapi, naye alinyosha mkono wake apate kumwonyesha mipaka ya nchi yake, lakini aliona haya kuinua mkono juu Mwati asione chini ya kwapa lake, na hivi alionyesha kipande kidogo cha nchi tu. Kisha, Mwati hakuwa na haya hata kidogo akainua mkono wake juu sana akasema kuwa nchi yake inaenea mpaka mbali sana.

Basi kundi hilo la watu lililotokea Ruanda na imehadithiwa kuwa walikuwa wa jamaa ya Abahinda wa kabila la Watusi. Tumetaja jina hili Hinda mara nyingi katika habari hizi mpaka sasa, tena tutakumbuka kuwa ule ufalme ule wa Karagwe uliosimamishwa na Ruhinda ulienea mpaka Ruanda, yaani nchi waliyotokea Watusi. Hivyo tunaweza kusadiki kwamba watu hao walikuwa Wahima, yaani watu Wahamiti.

Watu wengine katika kundi hilo waliotoka Ruanda walibaki katika nchi ya Kibondo na wazao wao wamekaa huko hata leo, tena wako watawala walio katika nchi hiyo wenye damu ya Watusi. Imesemwa ya kuwa wale waliofika kusini katika nchi ya yule Mwene Milanzi Ntatakwa walisafiri kwa upande wa magharibi wa Ziwa Tanganyika na walipofika mwisho wa ziwa, walizungukia upande wa kusini, ndipo walipotokea wakafikia nchi yake. Wazao wa kundi hilo la watu ni watawala wa nchi ya Ufipa na sehemu nyingine za wilaya ya Kigoma. Zaidi ya haya, mtawala wa kabila la Washamba wanaokaa kusini mwa nchi ya Ufipa hudai kwamba babu yake aliitwa Luhinda.

Yule mwanamke Mwati tuliyemtaja, alizaa mtoto mwanaume akamwita Msili Mkokwe, na alipokua, Ntatakwa alimchukua akamweka awe mtawala. Basi tangu hapo mpaka leo hivi, watawala wa huko huwekwa na mtu anayeitwa Mwene Milanzi ambaye ni mlinzi wa ule mlima aliouwekea Mwati jiwe lake nao unaheshimiwa sana.

Baadaye Msili Mkokwe hakuridhika na nchi yake, akaanza kujaribu kushinda nchi zilizotawaliwa na watawala wadogo apate kutawala nchi yote ya Ufipa mwenyewe. Lakini hakuweza, na alipopigana na Ndasi mtoto wa mjomba wake akashindwa, basi aliona uchungu mwingi akajiua. Basi Ndasi alijiweka kuwa mtawala, lakini hakuwa na siku nyingi, akafa. Ndipo Zumba Mwana Mzia alipoirithi nchi, na katika wakati wa utawala wake nchi iligawanywa sehemu mbili, yaani Nkanzi kwa kaskazini, na Lyangalile kwa kusini. Wakati huo nchi ya Ufipa iliingiliwa na Wanyika walioiharibu sana, lakini mkubwa wao jina lake Chalo alipouawa, ndipo wafuasi wake walishindwa na kuuawa.

Lakini hata baada ya hayo nchi haikustarehe, maana katika wakati walipotawala watawala wanane waliofuata, nchi ilisumbuliwa sana mara kwa mara kwa fitina na vita za kindanindani mpaka alipoanza kutawala Zumba Kalonga, ndipo walipokuja Watuta walioingia nchi na kuwashinda Wafipa. Habari za Watuta zitasimuliwa baadaye. Basi Watuta walikaa katika nchi kitambo, kisha waliondoka wakaenda zao, wala hawakurudi tena. Hivyo, Wafipa walipata nchi yao tena, na katika wakati wa watawala wawili waliofuata hakuna habari kubwa iliyotokea, ndipo Sangu Chapiti Punda alipoanza kutawala, na wakati huo Waarabu walifika katika nchi ya Ufipa mara ya kwanza.

Sangu Chapiti Punda alikuwa mtu mnyonge sana na watu wake walimchukia kabisa kwa sababu ya tabia yake. Basi waliwaomba Wawungu waje wamwondoe katika utawala wake. Wakati ule, Kilanga alikuwa mkubwa wa Wawungu, akaja pamoja na watu wake wakaunguza nyumba ya Sangu Chapiti Punda, wakateka nyara, kisha walikwenda zao. Huku nyuma Sangu Chapiti Punda aliwakimbilia Waarabu wakamwokoa.

Nchi ya Lyangalile vile vile iliathirika, maana watu waliotoka Usangu walikuja pamoja na Kimalunga mkubwa wao, wakaenea katika ponde la Ziwa Rukwa, wakapanda mpaka juu milimani, wakamshinda Ulamasi aliyekuwa mtawala wa Lyangalile. Basi Kimalunga aliishika nchi, na Wadachi walipofika katika nchi hii wapate kuitawala, alikuwa angali akiitawala.



Somo 4-Kuendelea na habari za Wafipa

Sasa turudie nyuma kidogo. Sangu Chapiti Punda alipokufa, Nandi Kapufi aliurithi utawala, na katika wakati wake Wazungu wa kwanza wa mission wanaoitwa 'White Fathers' walifika katika nchi yake. Ntinde Kiteta alifuata Nandi Kapufi lakini alitawala muda wa miezi mitatu tu, ndipo aliporithi Nandi Msulwa. Nandi Msulwa alitawala nchi kwa miaka saba, kisha alijiua, na Mtinde Kapere aliurithi utawala. Lakini kwa kuwa Wadachi hawakufahamu vema desturi za urithi wa Wafipa, walimwondoa wakamweka Kiatu mwanawe Msulwa katika urithi wa Mtinde Kapere. Kiatu alikufa katika mwaka 1915 na dada yake aitwaye Ngalu alirithi utawala, lakini serikali ya Kiingereza ilimweka Mtinde Kapere awe waziri wake.

Mpaka siku hizi za karibu, jamaa za Mtinde Kapere walioana katika ukoo wao, maana katika desturi zao walikatazwa kabisa wasioe wenyeji wa nchi. Na kwa kuwa walitengwa kabisa na watu wa kabila lao, iliwalazimu kuoana katika ukoo wao, na kwa hivi wamepungua sana hata karibu kwisha, maana desturi hiyo huharibu uzazi.

Imedhaniwa kuwa ufalme huu wa Kitusi ulio katika Ufipa ulisimamishwa zamani ya miaka 200 kama hivyo, nao ni ufalme wa mwisho uliosimamishwa na kabila hilo linalotawala mahali pengi katika nchi yetu.

Kabla hatujamaliza kusimulia habari za taifa la Wahima, imetupasa tukumbuke kuwa hata Wataturu au Watatoga wanaokaa pande za Ziwa Victoria husema kwamba walitokea Ruanda. Tutasimulia habari za kabila hilo la Wahamiti baadaye, lakini labda hii ndiyo sababu Watatoga walihama kutoka nchi ya Mbulu wakati waliposhindwa na Wamasai, wakaenda kukaa pande za Ziwa Victoria. Kama ni kweli asili yao walitoka Ruanda, basi yaonyeshwa safari nyingine iliyo kubwa ya watu hao wa Wahamiti.

Sasa tumekwisha onyesha namna watawala wa Kihamiti walivyoenea katika nchi yetu. Kwanza walitoka Ugala, wakafika Bunyoro, kisha walizunguka Ziwa Victoria wakafika pande za mashariki kupita Mwanza. Kutoka Ruanda walisafiri mpaka pande za kusini mwa Ziwa Tanganyika na hapa wakakaa wakajifanya watawala. Ni vigumu sana kusadiki kuwa walifanya mambo waliyoyafanya kwa nguvu ya silaha zao kwa sababu Wabantu walikuwa wengi sana kuliko Wahamiti waliokuja. Hadithi nyingi zinazosimulia jinsi wenyeji, yaani Wabantu, walivyokubali kutawaliwa nao bila ya kukaidi, huelekea kuonyesha kuwa Wahamiti walifaulu kwa sababu ya tabia zao jinsi zilivyokuwa bora kuliko nguvu za silaha.

Labda wenyeji wa nchi walifikiri kuwa wageni hao waliotoka katika nchi za kaskazini wana nguvu za ajabu za uganga. Labda walidhani wanaweza kuleta mvua na maajabu mengine, maana pengine hata sasa wenyeji husadiki kuwa wanazo nguvu hizo. Lakini juu ya hayo yote lazima tukumbuke ya kuwa kwa desturi za tokea asili yao, Wabantu hawana matengenezo ya ufalme wala ya utawala. Walikuwa walimaji tu na kila ukoo ulitawaliwa na babu au mkubwa wa jamaa au ukoo. Basi ni dhahiri ya kuwa namna walivyozoea kukaa, haikosi iliwafanya wakubali kutawaliwa na wageni waliokuja katika nchi yao. Hatuna habari za nchi yo yote iliyotawaliwa na watu wa Afrika kwa muda mrefu kama hivi walivyotawala Wahamiti hao. Tena hatuna habari za nchi kubwa iliyotawaliwa na Wabantu kama hizi zilizotawaliwa na Wahamiti.

Kweli Wabantu wengine walitokea wakatawala wakawa washindaji kwa ushujaa, lakini kwa desturi utawala wao haukudumu sana, wala haukuendelea kwa vizazi vingi.

Haujatokea ufalme mwingine uliofanana na ufalme huo ulioitwa Kitara hata katika nchi yote ya Afrika ya Mashariki.

Utawala wa Wahima ulienea kutoka mstari tokea Mwanza kufika Uzinza, na kupita mstari huo hawakusimamisha ufalme. Labda hawakuweza kwa sababu walikutana na watu wengine wa taifa lao, maana walikutana na Wagala walio kabila lenye asili yake karibu na mto Nile. Wagala walikuja pande za kusini mpaka mto uitwao Mara, wakawashinda watu waliokuwa wakikaa huko. Walipopita mto Mara, walianza kuchanganyika pamoja na Wamasai, na sasa huitwa Waruri. Katikati ya Waruri na Wasukuma, Washashi wanakaa. Washashi ni Wasukuma waliochanganyika pamoja na Wamasai na Watatoga.

Basi, sasa tumekwisha ona kuwa Wahima ndio waliotawala nchi zote zinazozunguka yale maziwa makubwa, Ziwa Victoria, Ziwa Edward, na Ziwa Tanganyika. Wenyeji ni Wabantu wa makabila mengineyo, lakini watawala walio wengi wana asili yao katika taifa lile la Kihamiti, ingawa sasa mahali pengi hata na wao wamechanganyika pamoja na Wabantu mpaka sura na tabia zao za asili zimewapotea kabisa.

Somo 5-Wanyamwezi

Yale mambo tuliyokwisha soma, yaani kuwekwa falme hizo za Kihamiti ndiyo mambo makubwa yaliyotokea katika nchi za magharibi mpaka mwaka 1700 kama hivi. Mambo makubwa mengine yaliyotokea ni mahamio ya Watatoga, na vita za Wamasai waliowafukuza Watatoga huku na huko. Tutazisoma habari hizi halafu. Tena nchi za kando ya Ziwa Victoria zilisumbuliwa sana na watu waliotoka Uganda na wale Wagala au Waruri waliokuwa wakinyang'anya watu mali zao kila mara.

Katika miaka iliyofuata karibu na 1800, wageni wengine walifika nchi hizi, nao ni Waarabu na wengine waliotoka pwani kuja kufanya biashara na hasa biashara yao ya kununua watumwa. Kabla ya wakati huo, watu wa pwani hawakushughulika sana na watu wa bara. Lakini sultani wa Kiarabu alipoanza kutawala Unguja, Waarabu walio pwani walishikwa na tamaa ya kuingia katika nchi za bara ambazo hazikujulikana kwa wakati huo. Hasa walithubutu kusafiri katika nchi hizo kwa sababu walikuwa na bunduki za kujilinda.

Tumekwisha simulia kuwa Waarabu walifika katika nchi ya Ufipa kwa mara ya kwanza wakati alipokuwa akitawala Sangu Chapiti Punda. Hatujui tarehe kwa hakika, lakini tangu walipofika, watawala watano au sita wametawala huko. Waarabu hawakuonekana katika nchi za upande wa Kilimanjaro mpaka katika mwaka 1850 kama hivi.

Husemwa kuwa Waarabu wa kwanza waliofika katika nchi ya Unyanyembe walifika wakati alipotawala Swetu wa kwanza, naye tunajua alitawala katika miaka ya kwanza ya 1800. Imehadithiwa kuwa wawindaji wa ndovu wengine walikuwa wakisafiri kutoka Unyanyembe kwenda pande za mashariki, wakakutana na watu wa pwani wakifanya biashara, wakafuatana nao mpaka pwani, halafu wakarudi tena Unyanyembe.

Waarabu walipofika nchi za bara ilikuwa desturi yao kujenga miji au kambi walizoita bandari. Imesemwa ya kuwa bandari moja ilijengwa Msene katika nchi ya Sumbwa, yaani Kahama, katika mwaka 1830, na moja Ujiji katika mwaka 1845. Lakini mji mkuu wao uliitwa Kazeh na baadaye uliitwa Tabora, nao hudhaniwa haukujengwa mpaka mwaka 1852.

Mtawala wa kwanza ambaye tunazo habari zake ni Swetu wa kwanza, na Fundikira alimfuata katika kutawala. Fundikira na baba yake Swetu walipatana sana na Waarabu, na binti mmoja wa Fundikira aliolewa na yule Mwarabu Hamed Hamadi anayejulikana hasa kwa jina la Tipu Tipu.

Katika mwaka 1858 Waingereza wawili Burton na Speke ambao walikuwa Wazungu wa kwanza waliosafiri katika nchi hizi, walikutana na Fundikira na Waarabu waliokuwa wakikaa Kazeh, wakaandika habari za safari zao. Burton ameandika ya kuwa wakati huo Waarabu walikuwa wamekaa Usukuma kwa miaka kumi, lakini labda alitaka kutaja Sumbwa wala si Usukuma. Akasema kuwa, kwa desturi Waarabu walikaa kwa makundi idadi ya watu ishirini na tano kama hivi, na kwa kuwa walikuwa hodari matata yo yote yalipotokea hawakukubali kutekwa na kuonewa bila kupigana, lakini hawakuwa na nguvu za kutosha kushinda na kutawala nchi kabisa.

Katika mwaka 1858 Mwarabu mmoja aliuawa katika nchi ya Uvinza na mara vita ikavumbuka. Wenziwe walikusanya watumwa wao idadi ya mia mbili au tatu wakawapa bunduki na silaha kwenda kupigana na wenyeji. Lakini kumbe, kila mmoja alitaka wenziwe watoe dhamana juu ya maisha na mali yake kuwa itakuwa salama, kwa hivi walirudi mahali pao bila kufanya neno. Kwa kawaida, ndivyo ilivyokuwa tabia zao: walikuwa na askari wengi wenye silaha na bunduki za kutosha, lakini hawakuwa na majemadari hodari wa kuwaongoza vitani. Lakini hata hivyo waliweza kukaa salama katika nchi za bara, na kwa kawaida walipatana sana na wenyeji, wakaoa wanawake wa wenyeji wakachanganyika na Wabantu. Wasingalipatana nao wasingaliweza kuleta watumwa pwani, maana waliwaleta kutoka mbali sana kupita nchi za wenyeji.

Katika habari alizoandika Burton, asema ya kuwa walikuwako watawala wawili waliokuwa wakubwa katika nchi ya Unyamwezi, ndio Fundikira na Msanga wa Msene, na wote wawili walipatana sana na Waarabu. Wakati huo, Mwarabu mkubwa wa Kazeh alikuwa Snei bin Amiri. Kweli Tipu Tipu alikuwa na nguvu nyingi katika nchi za bara, lakini kazi yake hasa ilikuwa kufanya biashara, na zaidi katika nchi za Kongo, akakaa kwa amani.

Fundikira na Msanga walisaidiwa sana na Waarabu katika matata yaliyotokea mara kwa mara, na kwa msaada wao Fundikira aliteka sehemu ya Uyui, na Msanga alifukuza Watuta waliokuja kumshambulia.

Yule msafiri Speke tuliyemtaja, alisafiri katika nchi hizi mara ya pili katika mwaka 1861 akamkuta Fundikira amekwisha kufa; na Manua Sera, au labda jina lake ni Manasele mwanawe, alikuwa akitawala nchi. Huyu Manasele hakupatana na Waarabu kama baba yake alivyopatana nao, maana alipofika Speke Manasele alikuwa amekwisha gombana nao kwa sababu aliwatoza ushuru juu ya bidhaa zao walizozipitisha katika nchi. Lakini Waarabu walikuwa na nguvu wakamweka mtawala mwingine wasikubali utawala wa Manasele; walimweka Mkisiwa aliyekuwa mwana wa suria wa Fundikira mahali pake. Manasele alikuwa hodari mwenye moyo wa kiburi, akakataa kabisa kutii amri za Waarabu, akajilipiza kisasi kwa kushambulia safari zao zilizopitapita akateka bidhaa na mali zao.

Speke alipofika aliwakuta Waarabu wamekwisha kusanya watu mia nne ili waende wakamkamate Manasele. Basi Manasele alimwendea Speke akaomba msaada, na Waarabu hawakufaulu katika shauri lao, na Manasele aliendelea kuwasumbua sana kwa siku nyingi. Katika mwaka 1873 msafiri Mzungu mwingine jina lake Stanley alifika nchi hizi na Waarabu walimwomba aamue shauri na kuwapatanisha na Manasele. (Stanley alikuwa Mwingereza aliyetumwa kumtafuta Livingstone katika nchi hii, maana kwa muda wa miaka mitatu rafiki zake walikuwa hawajapata habari zake, wakafikiri kuwa amepotea, au amekufa.)

Katika mapatano waliyoyataka Waarabu walikusudia kumpa Manasele nchi nyingine badala ya Unyamwezi, lakini alikataa kabisa kufanya shauri lo lote nao mpaka wamtoe Mkisiwa katika utawala wa Unyamwezi. Basi hapo vita ikaanza tena na mara nyingi Manasele alizingirwa akawa karibu kukamatwa, lakini bahati yake ilikuwa kuokoka kila mara. Basi akaendelea kuwasumbua Waarabu na kuteka bidhaa zao mpaka hatimaye alifia Ugogo.



Somo 6-Habari za Mirambo

Haikosi wasomaji wengi wamesikia jina la mtu huyu Mirambo aliyejulikana sana zamani kwa ajili ya nguvu zake.

Mirambo alikuwa mkubwa wa nchi inayoitwa sasa Urambo. Alikuwa nusu Mha na nusu Mkimbu; alizaliwa kati kati ya miaka 1840 na 1845, yaani aliishi wakati ule ule wa Manasele.

Kabla hajafa Manasele alikuwa amegombana na nduguye jina lake Kiungi, yaani mwana wa mjomba wake, na Kiungi alikimbia akajiweka chini ya ulinzi wa Mirambo. Basi Waarabu walimchagua Kiungi awe mtawala wa Unyanyembe. Labda walimchagua kwa sababu walimweza sana akawa chini yao kabisa, na tena alikuwa akipatana sana na Mirambo ambaye walitaka urafiki wake sana.

Katika mwaka 1870 Mirambo alianza kujitokeza na kupigana vita na kushinda nchi. Majeshi yake yalikuwa makundi ya watu waliotoka kila mahali, na hasa watu wasiotii watawala wao. Akazidi kupata nguvu mpaka akashinda sehemu yote ya magharibi ya kaskazini mwa Unyamwezi. Katika mwaka 1871 aliwashambulia Waarabu waliokaa Tabora akawashinda, lakini hakustarehe huko. Alipigana sana na Watuta akawashinda, lakini alipoona ya kuwa ni watu wakali sana, na tena hodari katika vita, aliona kuwa watamfaa kuwa askari zake, basi akawapa mahali pa kukaa paitwapo Ugala katika nchi ya Kigoma, akawafanya raia zake.

Mirambo alishambulia nchi ya Shinyanga akarudi kwake tena akichukua mateka mengi sana. Watawala wa Shinyanga hawakuthubutu kupigana naye wakampa kila kitu alichotaka kusudi aende zake na kuwaacha kwa amani. Lakini mtawala mmoja jina lake Kajala wa Usule hakukubali kushindwa. Alijenga boma kubwa juu ya mwamba, na humo alipigana na Mirambo na watu wake, nao hawakuweza kumtoa. Mahali walipopigana panajulikana hata leo.

Katika mwaka 1880 Mirambo alianza kujiingiza Ufipa akachoma nyumba ya mtawala wa Wapimbwe. Katika vita hii Waingereza wawili waliuawa. Waingereza hao walikuwa wakirudi pwani baada ya kuchukua ndovu wawili kutoka Bagamoyo mpaka misioni ya Kibeleji iliyo Karema.

Mirambo hakuendelea sana na vita hii ya Ufipa, na alipofika chini ya milima iliyo Ufipa aligeuka akarudi kwake.

Yule Kiungi tuliyemtaja alitawala Unyanyembe kwa muda wa miaka 20, yaani mpaka mwaka 1882. Ndipo Isike alipoanza kutawala akajenga mji wenye boma la nguvu karibu na Tabora. Wakati huo Nungu aliyekuwa mpwa wa Fundikira aliipiga nchi ya Wakimbu iitwayo Kiwere akaishinda, akamwomba Mirambo amsaidie vita wamwondoe Isike, lakini hawakuweza. Katika vita hii Mirambo alizingiwa akakamatwa, lakini aliachiliwa kwenda huru tena.

Labda vita hii ilikuwa vita ya mwisho ya Mirambo, maana katika mwaka 1886 alikufa, na zile nguvu alizokuwa ameziamsha zikafa pia. Mwanawe Siki alijaribu kufuata desturi zake asiweze. Katika mwaka huo huo Wadachi walijitegemeza Tabora wakampiga Isike mwana wa Fundikira wakamshinda kabisa. Isike alipoona ameshindwa alijiharibu mwenyewe pamoja na nyumba yake yote kwa baruti, lakini tutasoma habari zake baadaye.

Isike alipokufa, Nyaso binti Fundikira alirithi utawala, akatawala mpaka mwaka 1889 akafa. Ndipo Karunde binti Gumati alipoanza kutawala. Karunde binti Gumati alizaliwa na mjakazi wa Fundikira, akatawala mpaka mwaka 1917, akafa, na Saidi Fundikira alianza kutawala.

Kabla ya kuacha habari za Unyamwezi, lazima tutaje mtawala mwingine. Katika mwaka 1873 alipofika yule Mzungu Stanley katika nchi, alikuta mtawala mwingine mwenye nguvu, jina lake Mtinginya wa Usongo.

Mtinginya alimsaidia sana Mirambo katika vita zake. Tena alikusanya jeshi la askari kama alivyokusanya Mirambo, lakini hasa walikuwa Wamasai, au labda walikuwa Watatoga, maana Stanley alisema kuwa ni Wamasai lakini labda alikosa, maana ni vigumu sana kuona Wamasai wakitumikia watu wengine, na labda walikuwa Watatoga na yeye aliwadhani kuwa Wamasai kwa sababu walifanana nao.

Lakini Mtinginya hakupata nafasi kufuata desturi za Mirambo kwa sababu Wadachi walikuwa wamekwisha weka imara serikali yao, na tangu wakati huo vita za namna hiyo hazikuwezekana tena.
1.jpg
 
Sijaona Habari za uhusiano wa Wahima na Usukuma Kama ulivyochambua kwa baadhi ya makabila au jamii hapo juu.
Hii ni Chapter ya kwenye kitabu si uchambuzi wangu. Lakini hata kwa kuangalia kijuu juu unaweza kuona. Wasukuma ni kama wabantu pekee pande hizi ambao wamejikita sana kwenye ufugaji, tena ule wa kuhama hama kama Wahima. Pia ng'ombe wa kisukuma. Hao Wenye pembe ndefu sana, wanafanana na ng'ombe wa Kihima.
 
Hii ni Chapter ya kwenye kitabu si uchambuzi wangu. Lakini hata kwa kuangalia kijuu juu unaweza kuona. Wasukuma ni kama wabantu pekee pande hizi ambao wamejikita sana kwenye ufugaji, tena ule wa kuhama hama kama Wahima. Pia ng'ombe wa kisukuma. Hao Wenye pembe ndefu sana, wanafanana na ng'ombe wa Kihima.
Aisee!! Kuna mambo nimekuwa nikiyasikia naona humu yamefafanuliwa zaidi. Na kuna makabila nilikuwa naona yanamuingiliano ila naanza kupata picha.
Niliwahi kuishi sengerema sasahivi ni halmashauri ya buchosa, kuna sehemu inaitwa uzinza.
Hawa wazinza lugha yao inafanana na kihaya,
Pia maeneo ya geita huko kuna watu kama watusi.
Pia hawa walongo duuh,
Alafu wasumbwa pia duuh.
Naomba uendelee na huo uchambuzi ,kuna mengi ya kujifunza.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom