Tena, walikuwako mainzi wabaya wengi sana waitwao mbung’o. Ilifikiriwa ya kuwa punda na wanadamu hawadhuriki wakiumwa na mbung’o lakini kwakweli punda wetu walidhurika, labda kwa sababu punda walikuwa wamedhoofu au labda kwa sababu mbung’o wa hapa wana sumu kupita kiasi, sijui, lakini punda wetu walikufa.
Kwa bahati hawakufa mpaka ilipopita miezi miwili baada ya kuumwa, na nilipowachuna niliona mistari yenye rangi ya manjano juu ya nyama, ndiyo dalili kuwa walikufa kwa kuumwa na mbung’o.
Tulipotoka mwitu wa Elgumi, tulizidi kuendelea upande wa kaskazini, maana ndiyo njia aliyoitaja Yule msafiri maskini aliyemfikia Bwana Mackenzie aliye kufa kwa namna ile ya kuhuzunisha niliyokwisha eleza.
Hatimaye tulilifikia lile ziwa liitwalo Laga, ambalo urefu wake wapata kadiri ya maili hamsini, na upana wake maili ishirini.
Ndipo tulipoendelea mbele kadiri ya mwezi mzima tulipita katika nchi yenye vilima vilima mfano wa mawimbi makubwa, na vichaka vilitapakaa huko na huko.
Wakati huo wote nchi ilikuwa imeinuka taratibu na kwa kweli ni mwinuko moja kwa moja mpaka kufika chini ya safu ya milima mingi yenye theluji juu ya vilele vyake.
Tulikuwa tukiiendea milima hiyo, maana tumepata habari ya kuwa ndiko liliko lile ziwa la pili ambalo Yule msafiri alisema halina mwisho wa kwenda chini.
Mwisho tulipafikia, na tulipohakikisha ya kuwa ziwa liko juu ya kilele cha mlima, tulipanda tena kadiri ya futi elfu tatu mpaka tulipofika kwenye genge linaloteremka ghafla.
Tukaona chini yetu kadiri ya futi elfu moja na mia tano, liko ziwa lenye umbo la mraba na upana na urefu wake ulipata kadiri ya maili ishirini, ambalo halitoshi ni shimo la volcano ya zamani.
Tuliona miji iko kando ya ziwa, basi tuliteremka kwa shida katika mwitu wa misonobari iliyofunika miteremko ya shimo lile, tukapokewa vizuri na wenyeji wa huko ambao ni watu wa amani. Wasiopata kuwaona watu weupe mpaka wakati huo; wakatutendea kwa heshima na wema, wakatupa chakula na maziwa kadiri tuliyotaka.
Siku tatu za kwanza tulizokaa huko, ilinyesha mvua, na mvua hii ndiyo iliyoanzisha sumu ya mbung’o katika punda wetu waliyobaki, na wote walikufa.
Msiba huu ulituweka katika shida, maana sasa tulikuwa hatuna njia ya kuchukulia mizigo yetu, lakini kwa kweli, hatukuwa na vitu vingi vilivyobaki kuchukuliwa. Tena, risasi na baruti zilikuwa zimepungua sana.
Tulikuwa na risasi kadiri ya mia moja na hamsini, na risasi za marisaa hamsini tu. Hatukujua namna ya kuendelea mbele, ikawa kama tumekwisha fika mwisho wa safari yetu.
Lakini hata kama tungekuwa na nia ya kuliacha kusudi letu la kugundua yale tuliyokuwa tunayatafuta, ingekuwa jambo la upuuzi kufikiri habari za kurudi nyuma mwendo wa maili mia saba mpaka kufika pwani, hali hatuna zana za safari;
Basi, kwa kuwa wenyeji wa hapa ni wema, tulifanya shauri kukaa hapo tulipo na kungojea mambo yatakayotokea, na huku tunatafuta habari za nchi zilizo mbele.
Basi, tulinunua mtumbwi mkubwa mzuri wa kutosha kutuchukua sisi sote pamoja na vitu vyetu vilivyobaki, kwa mkubwa wa kijiji tulimokaa, tukaanza kusafiri ziwani kutafuta mahali pazuri pa kupiga kambi.
Kwa kuwa hatukujua kama tutakirudia tena kile kijiji, tulipakia mizigo yetu yote katika mtumbwi ule tena, tulichukua kipande cha nyama tuliyopika tayari, tukaondoka.
Wenyeji wengine walikuwa wametutangulia ili kuwaarifu wenyeji wa miji mingine kuwa tunakuja.
Tulipokuwa tukipiga kafi kwa taratibu, Bwana Good alisema jinsi maji ya ziwa yalivyo na rangi ya samawati, akasema.
Wenyeji, ambao ni wavuvi stadi wamemwambia kuwa ziwa hilo lina kina kirefu sana, tena lina tundu chini yake na maji yanatoka huku na kwenda kuuzima moto mkubwa sana unaowaka chini ardhini.
Nilisema kuwa habari hizi alizosikia, bila shaka ni mapekeo ya zamani sana, yalioanza wakati volcano za pande hizi zilipokuwa zingali zikitoa moto bado.
Tulipofika ng’ambo ya ziwa, tuliona ya kuwa kingo zake ni genge la mwamba linalopanda juu sana, wala hapana mahali linapoteremka kwa taratibu, basi, tuliliambaa genge hilo tukiuendea mwisho wa ziwa, maana tulijua ya kuwa kuna mji mkubwa huko.
Tulipokuwa tukienda tulianza kupita chungu nyingi za matete na majani na mashina ya miti na takataka nyingi zinazoelea juu ya maji, na Sir Henry alionyesha kundi la mabata weupe wakubwa waliokuwa wametua juu ya chungu nyingine, na sasa wanakula.
Nilikuwa nimekwishaona mabata wanarukaruka juu, nami sijaona namna yake katika nchi ya Afrika, nikataka kumkamata mmoja ili nimtazame vizuri.
Nilikuwa nimewauliza wenyeji habari za mabata hao, wakaniambia kuwa huja kutoka upande wa pili wa mlima majira Fulani ya mwaka, nao huja asubuhi, na kwa kuwa wamechoka, ni kazi nyepesi kuwakamata.
Niliuliza walitoka nchi ipi, lakini waliyatikisa mabega yao tu, wakasema kuwa juu ya genge lile ni nchi ya ukiwa, na kupita huko ni milima yenye theluji, imejaa wanyama wakali, wala hapana watu wanaokaa huko, na kupita milima ile ni mwitu mnene wa maili mia nyingi wa miti yenye miiba, hata tembo hawawezi kuupita, licha ya wanadamu.