HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-27
ILIPOISHIA:Mzee Andendekisye aliuliza kama vinaweza kupatikana, mganga alimwambia kupatikana vigumu kwa vile vimepelekwa mbali. Pia mwili ule ulitakiwa kuzikwa usiku uleule kwa vile ungelala ungeharibika na kushindwa kuuzika.
Kwa hiyo tutafanyaje?
Mzikeni na mazishi yake yasilale.
SASA ENDELEA...
IlibidI Atuganile azikwe usiku uleule na watu wachache kwa maelezo ya mganga, baada ya mazishi mzee Andendekisye alipanga usiku uleule asafiri na mkewe kurudi Malawi kwa mganga wake ili akamalizia kazi iliyobakia na kuifyeka familia ya Amangise. Ili kupata nafasi ya kuweza kuondoka usiku ule alitangaza hakuna matanga.
Watu walitawanyikia msibani na yeye na mkewe na baadhi ya majirani zake walirudi nyumbani. Lakini baada ya kufika nyumbani waliwaeleza majirani kuwa hawatalala pale, kwa vile walikuwa wamejiandaa walipanda baiskeli na kuwaacha majirani wakirudi majumbani kwao wakiwa wamepigwa na mshangao juu ya mambo ya jirani yao.
Mmoja alisema huenda anakwenda kuyafanya aliyoahidi makaburini kuufuta ukoo wa Amangise. Wapo waliosema kuwa kifo cha Ambakisye kilitokea baada ya kusafiri na kuuacha mwili wa mwanaye ndani na aliporudi majibu yalipatikana kwa kumuangusha kijana mbichi.
Walijiuliza mwisho wao nini katika vita ile ambayo ilionesha imetawaliwa na uchawi. Wazee wa kijiji walipanga baada ya mazishi ya mtoto wa Amangise waitishe kikao ili kuyaweka mambo yale sawa kwani picha iliyokuwa ikijionesha ilikuwa na mwisho mbaya.
Walipotoka kwa Andendekisye walikwenda kwenye msiba wa Ambakisye ambako nako walikuta mtaalamu akifanya mambo yake na kuzidi kuamini kijiji kinapokwenda kina hatari ya kuharibu jamii iliyowazunguka hasa kutokana na heshima ya wazee wale kijijini pale.
Lakini hawakusema kitu waliungana na majirani wengine kwenye msiba.
Wengi walikuwa na wasiwasi huenda na Amangise naye ataondoka usiku ule, lakini haikuwa hivyo baada ya mtaalamu kufanya mambo yake aliondoka na kuacha watu msibani kama kawaida.
Kwa vile usiku ule wazee wote walikuwepo msibani pale, Amangise alitumia nafasi ile kuzungumza nao kuhusu kinachoendelea kijijini na kauli za jirani yake juu yake na vitisho alivyovitoa kwa familia yake. Baada ya kuwapatia pombe, alisimama na kuzungumza na kufanya wote waelekeze masikio kwake.
Wazee wenzangu na majirani, nina imani kipindi kifupi kumetokea mshtuko kijijini kwetu cha vifo vya watu watatu kwa mpigo, bibi yetu Tumwambilile, mkwe wangu Atuganile na mwanangu Ambakisye. Kwa kweli vifo vyote hivyo vimetingisha Ibungu na vijiji vya jirani kutokana na mazingira yake.
Na baada ya vifo hivyo kumetokea vitu vya kushangaza kwenye mazishi ya Atuganile na bibi Tumwambilile. Japo mimi sikuwepo kutokana na msiba wa mwanangu.
Nimesikia maneno mengi ya mzazi mwenzangu Andendekisye juu ya kifo cha mwanaye kuwa mimi ndiye niliyemuua pia ametoa maneno mazito kuwa ndiye mhusika wa kifo cha mwanangu ikiwa kulipa kisasi na pia atahamia kwetu. Nimefikiria mengi kuhusiana na kauli ya kuniua mimi na mke wangu.
Wazee wenzangu naapa tena mbele yenu katika usiku huu kama mimi nilitia mkono kwenye vifo vyote basi Mungu anihukumu nife sasa hivi. Ni kweli tulikuwa na ugomvi wa chinichini kutokana na mimi kumtafutia mke wa kuoa mwanangu wakati tayari walikuwa na uhusiano na mwanaye.
Kweli ile ilileta mpasuko mkubwa, nakumbuka majuzi mwanangu alikuja na kunieleza tukae chini kumaliza tofauti zetu na kama nisingemsikiliza angeondoka nyumbani. Japokuwa nilikuwa na hasira kwa kitu alichomfanyia mwanangu za kumuua nguvu za kiume ili asioe.
Nilikubali na kuwa tayari kumrudisha mwanangu Ambakisye kwa mpenzi wake Atuganile, nilikubali kukutana na familia ya Andendekisye ili tumalize tofauti zetu ili wanetu waoane.
Samahani mzee mwenzetu, ulisema ulimtafutia mwanao mke Kilasilo, kwa hiyo angeoa wanawake wawili? mzee mmoja aliuliza baada ya kushindwa kumuelewa.
Nilisahau kuwaeleza habari za mchumba wa mwanangu wa Kilasilo, wakati tunajiandaa kupanga tarehe ya harusi alitoweka katika mazingira ya kutatanisha baada ya kuchukuliwa na mamba wa kimuujiza.
Alipatikana baada ya siku mbili akiwa amekufa, hapo niliona ni muda muafaka wa kumsikiliza mwanangu. Lakini upande wa pili bado walikuwa na hasira na sisi. Baada ya kukubaliana na mwanangu tukae chini tumalize tatizo, siwezi kuelezea jinsi nilivyopata mshtuko baada ya kuelezwa kuwa Atuganile amefariki.
Lakini niliumizwa nilipoelezewa kuwa mimi ndiye niliyemuua Atuganile pamoja na bibi Tumwambilile. Kwa kweli iliniuma sana hasa kutokana na hatua niliyofikia na mwanangu. Siku iliyofuata kulikuwa na mazishi ya mchumba wa mwanangu Kilasilo ambapo ilitubidi twende tukazike ili tuwahi mazishi ya Atuganile na bibi jioni.
Lakini tukiwa njiani mwanangu alianza kulalamika kichwa na kufanya tusimame, baada ya hapo aliendelea kulalamika kichwa huku akikishika na kusema kinataka kupasuka. Ghafla alianguka chini na kuanza kuzungumza kwa shida na kuniambia anakufa.
Ila aliniomba kama atakufa basi nisilipe kisasi, nina imani alijua aliyefanya vile ni Andendekisye kwa vile mwanzo alimuua nguvu za kiume. Ghafla sauti ilipotea na kuanza kutokwa damu puani, mdomoni, masikioni, machoni na kufariki mikononi mwangu, alipofika hapo sauti ilibadilika na kuzungumza kwa huzuni na kufuta machozi ya uchungu na kuondoa kamasi nyembamba.
Wazee wenzangu kwa kweli nimeumizwa sana tena sana na kifo cha mwanangu halafu kuna mtu anajisifu ndiye kamuua, kwa kosa gani au uhakika gani kama mimi nimemuua mwanaye. Nami kusema ukweli wa Mungu nilichokipanga kukifanya kwa Andendekisye wala nisingemvukia boda kutafuta wachawi ningekwenda kumchinja kama kuku nyumbani kwake kwa mkono.
Lakini niliheshimu usia wa marehemu mwanangu, nimeamua kumuachia Mungu najua majibu yake yatapatikana hapahapa duniani. Najua wapo wengi wana maswali juu ya mtaalamu aliyekuja hapa. Lazima niseme ukweli mwenzangu katangaza vita na tayari kanichukulia jicho langu, lazima na mimi nijihami lakini si kwa kulipa kisasi bali kujikinga na mashambulizi ya adui yangu.
Mi nafikiri suala hili tunatakiwa kulizungumza kwa kuwakutanisha ili tumalize uadui kwa vile hali inayokuja mbele ni mbaya sana, alisema mzee John.
Ni kweli, suala hili hatutakiwi kulifumbia macho kwa vile wote watu wetu hatuwezi kuona mnaumizana tunawatazama, mwingine alichangia.
Amangise upo tayari kukutana na mwenzako tuyazungumze?
Nipo tayari hata usiku huu ili kesho tukiamka tuanze upya japo kaniulia mwanangu.
Mzee Mwakyoma unaweza kwenda kwa Andendekisye kuzungumza naye ili tulizungumze?
Nipo tayari, lakini baada ya mazishi Andendekisye na mkewe wameondoka nyumbani kwao na hawakutueleza wanakwenda wapi lakini amesema hakuna matanga na kutufanya wote tuliokuwa msibani kuondoka.
Itaendelea kesho...............