HISIA ZANGU -8
ILIPOISHIA...
BILA kupoteza muda, Pam akachukua glasi mezani na kummiminia Lilian kisha akamkabidhi.
Karibu ufurahie matunda ya mzabibu! akasema Pam akijilamba midomo, tabasamu aliliachia.
Lilian akapokea akizidi kuonyesha aibu waziwazi. Akapiga funda moja kubwa. Akakunja uso kidogo kutokana na uchungu kiasi aliohisi kutoka katika mvinyo ule.
Maskini, hakujua hatari iliyokuwa mbele yake!
SASA ENDELEA...
Pam alitabasamu! Lilikuwa tabasamu pana ambalo halikujificha kabisa. Alikuwa na haki ya kutabasamu maana alikuwa na uhakika kuwa kazi yake sasa ilikuwa ikielekea kuwa nyepesi kuliko kawaida.
Uso wa Lilian ulikunjika sawasawa. Kwa tabu akameza funda moja kubwa la mvinyo. Ikaingia kooni taratibu kabisa! Akatikisa kichwa kwa nguvu!
Mh! Nitaweza kweli? akasema Lilian.
No! No! No! Utaweza. Sikia... hutakiwi kunywa nusunusu, kwakuwa ni mara yako ya kwanza unatakiwa kumaliza hiyo glasi yote kwanza, halafu kutokea hapo ndiyo utaanza kuzoea.
Paaaam! Lilian akasema akimwangalia Pam machoni.
Yes! Ndiyo ukweli kama unahitaji kuzoea. Siyo chungu sana bwana!
Ngoja nijaribu.
Lilian akanyoosha mkono wake kisha akachukua glasi na kuipeleka kinywani mwake. Aliigika ile mvinyo yote. Aliposhusha glasi ilikuwa tupu kabisa.
Mnawezaje lakini? Lilian akauliza.
Acha hizo bwana, endelea kufurahi, Leila akasema akionekana tayari ameshalemewa na mzigo mzito kichwani.
Haraka Pam akachukua chupa yenye mvinyo kisha akaijaza tena ile glasi ya Lilian. Akamwangalia kwa jicho la kumkaribisha kisha akarudisha macho yake kwa Lucy.
Wakatabasamu!
Kuna nini tena?
Kazi nyepesi kiasi gani?
Karibu mama, endelea kufurahi, akasema Pam.
Sasa Lilian akaichukua tena ile glasi, huku akionekana kuwa na uzoefu kidogo. Alikunywa kidogo, kisha akarudisha glasi mezani.
Kweli sasa umekua mtoto wa mjini, na wewe inaonekana utazoea mapema sana! akasema Lucy.
Kweli wewe una akili sana. Umegundua hilo kama mimi?
Yeah, ndicho ninachokiona kwa Lilian, akasema Latifa.
Kweli Lilian alionekana kuchangamka sana, glasi moja na nusu aliyokunywa tayari ilionekana kumbadilisha kabisa. Uchangamfu wake ukaongezeka ghafla. Hakuna ambaye hakujua kilichotokea.
Ilikuwa tabasamu la pombe!
Palepale Lucy akamwonyesha ishara Pam wasogee pembeni kwa ajili ya mazungumzo. Alianza Lucy kuondoka kisha akafuata Pam, wote wakisema kuwa wanakwenda msalani.
Nipe changu, akasema Lucy akitabasamu.
Usijali, haina shida. Pesa yako utapata.
Lakini si umeniamini sasa?
Sana. Kinachofuata?
Kinachofuata nini tena? Chukua mzigo ondoka nao.
Hapana Lucy, kama nilivyokuambia, nahitaji kumchukua huyu mwanamke kwa ridhaa yake mwenyewe, akasema Pam.
Lucy akabetua midomo yake. Akasema: Sawa. Najua vizuri sana. Kwa hiyo?
Sitaki kumfanya mateka, Pam akasema kwa sauti tulivu sana.
Ilikuwa sauti iliyoonyesha busara, hekima na uvumilivu. Ndani ya moyo wake hakuwa hivyo, Pam alikuwa mwanaume wa aina ya tofauti kabisa na mwonekano wake.
Utafanyaje?
Nashauri tuwarudishe chuo, nitachukua namba yake ya simu kutokea kwake mwenyewe, halafu sasa nitawasiliana naye mwenyewe. Sitaki ajisikie kuwa amekubali kwa kulazimishwa au kwa kisingizio cha pombe.
Nahitaji ridhaa yake mwenyewe. Nataka yeye akubali bila shinikizo la mtu mwingine. Nimeshasema nina malengo naye!
Lucy akacheka!
Mbona unacheka? Pam akauliza.
Lucy akacheka tena.
Mbona sikuelewi? Kwa nini unanicheka?
Wewe unaweza kuwa na malengo na mwanamke wewe? Haya...umeanza lini mwenzetu?
Fahamu hivyo Lucy, naomba ukubaliane na mikakati yangu maana najua mwisho wake utakuwa mzuri.
Sawa, acha nikubaliane na wewe.
Wakarudi kujumuika na wenzao!
***
Pombe ilikuwa imewakolea sawasawa. Saa 8:30 usiku, waliamua kuondoka klabu na kurudi hosteli. Lilian na Leila walikuwa hawajiwezi kabisa kwa ulevi.
Lucy na Lilian waliingia kwenye gari la Pam, Leila na Latifa, wakaingia kwenye gari la Big, safari ya kuelekea chuoni ikaanza. Mazungumzo njia nzima yalikuwa ya kilevi.
Lilian alikuwa amekaa siti ya mbele ya Pam. Muda wote huo, Pam hakuwa na haraka ya kumweleza hisia zake. Waliposhika Barabara ya Sam Nujoma kwenye mataa ya Mwenge, Pam akaanza kuchombeza...
Lilian, wewe ni mwanamke mrembo sana. Mwanaume yeyote ambaye atapata nafasi ya kukumiliki atakuwa mwenye bahati sana! akasema Pam.
Mh! Kweli?
Kabisa.
Ahsante.
Leila, Pam akaita tena kisha akatulia.
Abee...
Natamani sana uwe mtu wa karibu yangu, hata kama haitakuwa mambo ya mapenzi lakini nitajisikia fahari kukusaidia katika mambo yako. Wewe ni mwanamke mrembo, hutakiwi kuteseka hapa mjini wakati wanaume tunaojitambua wenye fedha zetu tupo, akasema Pam.
Ahsante, haina shida, kama si kwa ubaya ni sawa tu.
Hapakuwa na magari usiku huo, dakika tano baadaye gari lilikuwa limeegesha jirani na jengo la hosteli ambalo wanaishi akina Lilian. Muda mfupi baadaye Big naye alisimamisha gari.
Kwanza alishuka Lucy, kisha akafuata Lilian lakini kabla hajafanya hivyo, Pam alichomoa burungutu na kumkabidhi!
Zilikuwa milioni mbili!
Zitakusaidia hizi! akasema Pam kwa sauti yenye ushawishi wa fedha.
Ahsante, Lilian akaitika akizichukua zile fedha.
Akashuka garini na kumbusu mashavuni Pam. Mwanaume wa watu alisisimka sana. Alihisi kama shoti ya umeme ikimtembelea. Wakaongozana hadi kwenye gari la Big.
Latifa alikuwa tayari ameshashuka, Leila aligoma. Alitaka kuondoka na Big. Wote wakashangaa. Ni muda mfupi tu wamekutana na kuzungumza.
Kutoka Masaki mpaka chuoni tayari walishakuwa wapenzi! Lilikuwa tukio jipya kwa Lilian. Bado aliendelea kuwaza kuhusu burungutu la pesa alizopewa na Pam! Big akaondoa gari Leila akiwa pembeni yake.
Range Rover ya Pam ikaunguruma, akaingiza gia namba moja, akakanyaga mafuta!
Ikapepea!
Itaendelea...