Hisia zangu-3
AKAMSOGELEA Edo.
Ilikuwa nafasi ya dhahabu. Edo alimvuta Lilian upande wake na kumkumbatia sawasawa. Alikuwa akitetemeka kwa hisia kali za huba.
Kwa namna hali ilivyokuwa, ilikuwa vigumu sana kukubaliana na ukweli kuwa alitakiwa kulala na mpenzi wake katika hali ile lakini bila kuvunja sharti walilokubaliana.
Sharti la kutokukutana kimwili hadi watakapofunga ndoa.
Nikuambie kitu Lilian? Edo akasema.
Niambie mpenzi.
Ikiwa usiku wa leo hutanipa penzi lako, kesho nitakwenda Malaysia nikiwa sina mchumba niliyemuacha Tanzania. Sitajali muda niliopoteza kwako, ninachotaka ni penzi lako tu! akasema Edo, safari hii machozi yakianza kutiririka machoni mwake.
Lilian hakujibu kitu!
ENDELEA...
ALILIA kama mtoto mdogo. Machozi yalitiririka machoni mwa Edo. Pamoja na mwanga hafifu chumbani mle, Lilian aliweza kuyaona vizuri machozi ya mpenzi wake.
Alikuwa analilia mapenzi. Edo alionekana hakuwa tayari kuondoka Tanzania na kumwacha mpenzi wake wa muda mrefu bila kukutana naye kimwili.
Lilian alichanganyikiwa sana. Hakutaka kumuudhi mpenzi wake, lakini pia hakuwa tayari kuvunja ahadi yake. Bado moyo wake ulimwambia alitakiwa kufanya hivyo baada ya kuingia tu kwenye ndoa yao.
Edo mpenzi wangu, Lilian akaita.
Maneno yako hayatakuwa na maana yoyote kwa sasa.
Nisikilize kwanza mpenzi.
Lilian najua unaweza sana kuongea. Najua ulivyo na maneno ya ushawishi. Ninachokuomba kama kweli una nia na mimi, kama kweli unanipenda, ikiwa kweli mimi ndiye mwanaume wako wa dhati, nakuomba sana, usikatae ninachokitaka.
Utaniacha na mateso makubwa sana ya moyo. Sijui kwa nini moyo wangu una mashaka kiasi hiki. Sina amani hata kidogo. Najua utanisaliti tu Lily, utanisaliti mama, alisema Edo akionesha msisitizo wa hali ya juu katika kile alichokiongea.
Siwezi kufanya hivyo baba, mimi nakupenda wewe tu, sina mwingine na wala sifikirii kuwa na mwanaume mwingine zaidi yako. Kubaliana na maneno yangu nakuomba, alisema Lilian.
Unasema kweli?
Kweli Edo.
Kwa nini hutaki kukutana na mimi sasa?
Si kwa nia mbaya kama nilivyokuambia, nafanya hivyo kwa sababu nzuri. Kwani huwezi kulala na mimi bila kunigusa?
Hebu vuta picha, itakuwa furaha kiasi gani kama siku ambayo utakuwa unafunga ndoa na mimi unikute nikiwa na usichana wangu? Sitaki kumkasirisha mama yangu.
Aliniambia nihakikishe jambo hili nalisimamia. Sipendi kumkosea. Tafadhali kubaliana na mimi mpenzi wangu. Nakupenda Edo, wewe ni wangu wa pekee, alisema Lilian kwa sauti tamu, laini ikionyesha kumaanisha alichosema.
Edo alinyamaza kwa muda. Alitakiwa kutafakari kwanza. Ni kama Lilian alikuwa makini na maneno yake na alijipanga kwa kila neno moja lililotoka kinywani mwake.
Pamoja na yote hayo, Edo alijikuta akiguswa sana na maneno ya mpenzi wake. Ni kweli alivumilia muda mrefu. Kwa nini kipindi hicho kifupi tu?
Alilegeza masharti moyoni mwake, akakubali kumuacha mpenzi wake Tanzania bila kumgusa kabisa. Hilo alilipasisha moja kwa moja moyoni mwake.
Lilian, akaita Edo.
Abee Edo, mpenzi wangu.
Sikiliza maneno yangu.
Nakusikiliza baba.
Tazama macho yangu...
Nayaona baba.
Unaona nini?
Machozi.
Machozi yapo kweli, hakuna kingine unachokiona zaidi ya machozi?
Kwa kweli sioni kitu zaidi ya machozi.
Angalia kwa makini Lilian, akasisitiza Edo.
Lilian akatulia. Hapo sasa akaamua kumwangalia kwa makini zaidi. Alimwangalia tena na tena.
Hola!
Hakuna alichokiona!
Aliishia kuona kilekile...
Aliona machozi ya Edo.
Bado hujaona tu baby?
Tafadhali naomba uniambie.
Sikia, nakupenda sana. Nakupenda kuliko utakavyoweza kufikiria. Nakupenda kwa moyo wangu wote na ninaamini hizi hisia zangu. Sijui kama nawe unanipenda mpenzi.
Nakupenda sana Edo, sina cha kusema au cha kukuonyesha ni kwa kiasi gani nakupenda, lakini fahamu kuwa nakupenda. Kitu pekee kitakachothibitisha kuwa nakupenda ni kukutunzia heshima yako mpaka siku tutakayofunga ndoa.
Naamini hapo utakubaliana nami kuwa kweli nakupenda. Kwa sasa huwezi kuelewa mpenzi. Usichana wangu ndiyo zawadi ya pekee yenye thamani kuliko zote mpenzi wangu. Niamini baba, nenda salama chuoni, utanikuta. Mimi ni wako, akasema Lilian.
Kweli?
Niamini mpenzi.
Nakuamini mama.
Edo alitulia tena, ni kama alikuwa katika lindi fupi la mawazo. Aliikunja mikono yake kidogo, akanyoosha mguu wake mmoja, akiwa ndani ya blangeti, alijivuta hadi alipokuwa amelala Lilian.
Walitenganishwa na mto uliokuwa katikati yao. Edo aliunyakua haraka na kuurusha mgongoni mwake. Sasa walikutanisha miili yao. Kwa kasi ya ajabu, alimvutia Lilian kwake.
Akaenda mzimamzima!
Lilian hakuwa na nguvu lakini bado alikuwa akitaka kuona kitakachofanywa na Edo. Mwanaume wa maisha yake. Midomo ya Edo ikaanza kucheza.
Alikuwa anazungumza: Mpenzi wangu Lilian, lazima nikueleze kuhusu hili. Siwezi kuacha kusema maana naona inaweza kusababisha matatizo siku za baadaye.
Lilian akashtuka!
Alitaka kujitoa kifuani mwa Edo, akamdhibiti. Haikuwa rahisi kuponyoka mikononi mwa mwanaume yule aliyekuwa mshirika wa kudumu wa mazoezi ya viungo.
Tulia... akasema Edo.
Niambie ni nini baba?
Naheshimu sana hisia zangu za ndani. Sijui kwa nini nafikiria hivyo, lakini nahisi kama nikikuacha huku Tanzania lazima utanisaliti. Kama hisia hizi si za kweli, tafadhali naomba uthibitishe kwa kuwa mwaminifu.
Lilian alihisi moyo wake ukiingiwa na ubaridi kama wa maji ya barafu. Hakutegemea kusikia maneno hayo kutoka kwa mpenzi wake Edo. Yalikuwa maneno mazito sana yaliyomchanganya.
Edo?! Kweli unaweza kunifikiria hivyo baba?
Lazima nikuambie kilichopo moyoni mwangu.
Naomba uwe na amani mpenzi wangu, usinifikirie vibaya hata kidogo. Mimi ni wako na nitaendelea kuwa wako milele. Tafadhali, safiri ukiwa na amani moyoni mwako kuwa nitakuwa salama na nitahifadhi mali zako! akasema Lilian.
Ok! Acha nikuamini. Nakupenda mpenzi. Tulale sasa, umeshakuwa usiku, kesho tutazungumza zaidi.
Sawa mpenzi wangu.
Ilikuwa kama kifaranga cha kuku kikiwa kimekumbatiwa na mama yake, Lilian alilala kifuani mwa Edo. Ahadi yao iliendelea kuwa ileile, kwamba hawatafanya chochote usiku huo.
Ni ahadi ambayo ilitekelezwa!
***
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) ulikuwa bize sana jioni hiyo. Watu walikuwa katika pilikapilika za kusafiri au kupokea wageni wao kutoka ndani na nje ya nchi.
Edo na Lilian walikuwa miongoni mwao; kwao ilikuwa siku yenye maumivu makali ya moyo. Edo alikuwa anaachana na mwanamke wake akiwa na uhakika wa kutoonana naye kwa miaka miwili! Kilikuwa kipindi kirefu sana.
Kilikuwa kipindi ambacho Edo aliamini kingetosha kabisa kubadilisha historia ya uhusiano wao. Aliuona usaliti waziwazi kabisa. Kweli Lilian amvumilie kwa muda wote huo?
Miaka miwili?
Ilikuwa mingi sana. Ni muda ambao ungeweza kubadilisha chochote na akampoteza mpenzi wake. Alikuwa na mizigo yake, tayari kuingia chumba cha ukaguzi na kuendelea na taratibu nyingine za safari.
Walisimama wakiwa wanaangaliana, kila mmoja alionekana kuwa na mawazo yake kichwani. Edo alivumilia yote. Alikubaliana na yote. Alimwacha Lilian aamua mwenyewe. Amsaliti au amtunzie heshima.
Nakuambia kwa mara nyingine nakupenda sana mpenzi wangu. Naondoka nikiwa nimekuacha na usichana wako, tafadhali nikirudi nikukute nao, akasema Edo akimwangalia Lilian kwa hisia kali za mapenzi.
Nakuahidi mpenzi wangu. Nimeshasema mengi, sina ya kuzungumza zaidi. Nakupenda sana, nakutakia safari njema! akasema Lilian.
Haikuwa rahisi, lakini ndivyo ilivyokuwa na ilipaswa kuwa hivyo. Edo aliachiana na Lilian, akasogea kwenye foleni ya kuingia chumba cha ukaguzi.
Edo akageuza kichwa na kumwangalia Lilian, alichokutana nacho, kilimtisha sana. Alipigwa na butwaa!
Itaendelea Ijumaa ijayo...