ILIPOISHIA...22
Lilian akachanganywa tena na neno mpenzi. Lakini hakuwa na la kufanya, akajibu kichovu: Ndiyo, nipo tayari tangu nusu saa iliyopita.
Sawa njoo basi twende.
Nakuja.
Lilian alipoyatupa macho yake kwenye saa iliyokuwa ukutani, akagungua kuwa tayari ilikuwa saa 1:18 usiku. Akarudisha kitabu. kabatini, akatoka nje.
Edo ana habari gani mpya? akawaza akimfuata.
SASA ENDELEA...
UZURI wa Lilian bado uliendelea kuonekana kwa nje lakini ndani yake hakuwa msichana mrembo tena. Alitembea kivivu, bila mpangilio kama zamani. Alijitoa thamani kabisa.
Mikogo yote ilikaa pembeni, ndani ya moyo wake kulijaa majuto. Hakuchukua muda mrefu tayari alikuwa ameshafika barabarani ambapo Edo alikuwa ameegesha gari lake.
Edo alipotupa macho yake na kumuona Lilian akimfuata, alijawa na huzuni moyoni. Alimuona Lily hana furaha kabisa. Lilian alionyesha wazi kilichokuwa ndani yake.
Alikuwa kwenye majuto makubwa. Lilian alikuwa mpya kabisa. Mpya kwa kila kitu. Taratibu alivuta mlango wa siti za nyuma, ukafunguka. Akaingia.
Habari yako Edo?
Poa.
Mbona huna furaha?
Nipo sawa Edo.
Edo hakuzungumza kitu, aliangalia pembeni, nje kupitia dirisha la upande wa kushoto ambao alikuwa amekaa, aliporudisha macho yake ndani, akakutanisha macho na dereva wa gari lile.
Twende kaka, akasema Edo.
Gari likawashwa, likaanza kuondoka.
Lakini huna sababu ya kuwa na mawazo kiasi hicho mpenzi.
Sifurahishwi na namna ninavyokuona. Natamani kuona tabasamu lako tena. Kwa nini unakuwa hivi? akauliza Edo.
Edo, unajua kila kitu. Unafahamu kuhusu malengo yetu, unajua kuhusu makubaliano yetu. Sasa angalia...kila kitu kimebadilika. Kila kitu kimeharibika. Nawezaje kufanya chochote tena Edo?
Kumbuka mimi sina thamani tena kwako, siyo kwako tu sina thamani kwa mwanaume yeyote kwa sasa. Maisha yangu yamebadilika kabisa, akasema Lilian kwa sauti iliyojaa uchungu moyoni.
Hapana, usiseme hivyo. Ungekuwa huna thamani kwangu, nisingekuwa na wewe muda huu. Ni kwa sababu una thamani ndiyo maana uko na mimi muda huu, akasema Edo kwa sauti tulivu.
Unachokifanya sasa ni kunipa moyo tu. Hilo baasi. Siyo zaidi ya hivyo, akasema Lilian.
Nikuombe kitu? akauliza Edo.
Ndiyo.
Tusizungumze chochote muda huu mpaka tufike tunapokwenda, sawa?
Sawa, akajibu.
Hapakuwa na mazungumzo zaidi. Gari lilishika njia hadi kwenye mzunguko wa Mlimani City, kwenye makutano ya Barabara ya Ardhi na Sam Nujoma. Dereva akakata kushoto kuifuata Barabara ya Sam Nujoma kuelekea Mwenge.
Dakika moja tu baadaye, tayari walikuwa kwenye mataa ya Mwenge, zilipokutana Barabara za Sam Nujoma, Ali Hassan Mwinyi, Bagamoyo na ile ya Coca Cola.
Taa ya kijani ilipowaka, dereva akanyoosha kuifuata Barabara ya Coca Cola. Mbele kidogo kabla ya kukifikia kiwanda cha soda alikata kulia na kupitia jirani kabisa na salon maarufu ya Naznat.
Wote walikuwa kimya kabisa, wakafika kwenye Barabara ya Mwai Kibaki, jirani kabisa na Clouds Media. Wakaishika barabara hiyo, ambapo mbele kidogo, mkono wa kulia, dereva alikata na kuegesha.
Jacks Pub... Lilian alisoma maandishi kwenye bango dogo barabarani wakati dereva akikata kuelekea kwenye Pub hiyo.
Kumbe tulikuwa tunakuja hapa? Lilian akauliza.
Ndiyo...hujapenda?
Pazuri, haina shida.
Wakashuka garini na kuelekea kwenye meza iliyokuwa na viti viwili tu. Ilionekana wazi meza za namna hiyo zilitengwa maalum kwa ajili ya wapenzi au watu wawili pekee waliokuwa na mazungumzo ya siri.
Yule dereva alikaa sehemu nyingine. Muda mfupi baada ya kukaa, alifika mhudumu na kuwasikiliza.
Juisi ya embe ipo? akauliza Edo.
Ipo ya maembe peke yake, kuna nyingine imechanganywa na maziwa na nanasi. Utapenda ipi?
Embe pekee, glasi mbili tafadhali.
Sawa bosi, akaitikia yule mhudumu.
Sikia Lilian...nimekuita hapa ili kuzungumza na wewe. Najua ni kiasi gani una maumivu, lakini lazima tuzungumze. Nimegundua jambo moja muhimu,alianza kuzungumza Edo akimwangalia Lilian usoni.
Kwa sasa uko kwenye majuto. Najua una maumivu na unahitaji mtu wa kukupa faraja. Nina uhakika, mwanaume uliyetoka naye, hawezi kukupa faraja. Bado mimi ni wako na ninakupenda, akasema Edo.
Lilian akaanza kulia.
Stop crying please! (Acha kulia tafadhali)
Niache nilie Edo.
Hapana. Unakosea. Nini kinachokuliza? Hakuna unachoweza kubadilisha... akasema Edo, kisha akakatisha baada ya kumuona mhudumu akifika mezani kwao.
Tutayarishie makange ya kuku na ugali dona tafadhali, akasema Edo.
Sahani mbili?
Ndiyo.
Edo akaendelea: Mimi ndiye wa kukupa faraja. Nimeshakuambia...nimekusamehe kutoka moyoni. Bado nipo na wewe. Hata kama haitakuwa kimapenzi tena, lakini sitakubali kuona furaha yako inaondoka kwa sababu yangu.
Mimi ni wako, wewe ni wangu. Naomba uwe na amani na uendelee na masomo vizuri. Wiki ijayo narudi Malaysia. Tafadhali nataka nikuache ukiwa na amani. Acha kujifikiria peke yako. Hata mimi nina maumivu makali. Nami pia naumia. Ndiyo maana nataka kuwa sawa na wewe.
Lilian akainuka!
Edo naye akasimama.
Lilian akazunguka upande wa pili aliokuwa amekaa Edo. Akamsogelea, wakakumbatiana.
Ahsante kwa msamaha wako, nimekuelewa. Itakuwa hivyo Edo, akasema Lilian.
Unaniahidi?
Nakuahidi Edo.
Baadaye kidogo chakula kilifika mezani, wakaanza kula huku wakizungumza. Walishasahau kabisa machozi na huzuni walizokuwa nazo muda mfupi uliopita.
***
Edo alirudi Malaysia. Kwa taabu Lilian aliweza kufuatilia masomo yake kwa miezi miwili ya mwazo. Baadaye hakuweza tena. Kila alipokumbuka kuwa anaishi na VVU, alihisi akili yake ikimruka.
Sitaweza kuendelea na masomo kwa staili hii. Nitachekwa nikifeli. Ni afadhali nipumzike kwa muda kwanza, akawaza Lilian.
Uamuzi alioufikia ulikuwa ni kuandika barua ya kuomba kuhairisha mwaka wa masomo hadi mwaka uliofuata. Katika barua yake, alieleza sababu mbalimbali za kutunga, uongozi wa chuo ukakubaliana naye.
Sitakwenda nyumbani, nitakuwa hapahapa Dar, alijisemea Lilian akiwa kitandani, akisoma barua ya majibu aliyopewa na uongozi wa chuo ambao ulikubaliana na maombi yake.
Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia Ijumaa ijayo.