Hadithi tamu: Hisia zangu

Hadithi tamu: Hisia zangu

Mommadou Keita ni muda mrefu sana mpaka nikaishiwa hisia zote. Twende kazi.
 
Last edited by a moderator:
mkuu mimi naomba bora ukaipost ikaisha yote tu
 
ILIPOISHIA...
Mwanga wa maisha mapya ukafunguka. Alimwamini sana Mai. Alimsogelea na kumvutia kwake. Wakakumbatiana.
Machozi hayakuwa hiyari yake tena, yakamwagika kama maji! Mashavu yake yakawa tepetepe!
SASA ENDELEA...

“USILIE mpenzi, tafadhali usilie. Unatakiwa kujipa moyo…angalia, huu ni mwanzo mzuri kwako. Mwanzo mwema wenye matumaini makubwa,” akasema Mai akiwa bado yu kifuani mwa Lilian.
“Ni kweli usemayo, na ndivyo nifanyavyo sasa. Machozi haya si ya huzuni tena Mai rafiki yangu. Umenifumbua macho. Naona kila kitu kwa upya kabisa mbele yangu. Usijali.”
“Tulia...tena naona, hebu twende nyumbani sasa hivi,” akasema Mai.
“Nyumbani?”
“Ndiyo. Nyumbani kwangu.”
“Ofisi?”
“Nitafunga. Kwanza, nani wa kuniuliza? Ni salon yangu mwenyewe.”
“Najua...lakini wapo wa kukuuliza, wapo mabosi wako.”
“Bosi wa hapa ni mimi.”
“Si kweli. Wateja wako ndiyo mabosi wako. Vipi wakija wakukose? Sioni kama ni busara. Huu ni mwanzo mzuri kwetu, lakini kamwe usiharibu kazi.”
Lilian alizungumza kwa sauti ya taratibu iliyojaa ushawishi. Kwa hakika alionekana kuzungumza mambo ya msingi ambayo yalimwingia Mai kwa kiasi kikubwa sana.
“Ahsante kwa ushauri. Nimekuelewa shoga yangu,” akasema Mai.
“Poa, ngoja nijirudishe nyumbani, baadaye nitakutafuta ukimaliza kazi.”
“Sawa.”
Lilian akaaga.
Akaondoka zake.
***
Lilian alikuwa na mabadiliko makubwa sana katika maisha yake. Ushauri wa Mai ulikuwa na nguvu kama aliyeshauriwa na mtaalamu wa masuala ya ushauri mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka kumi!
Haikuwa hivyo!
Lilian alimwelewa kwa haraka Mai kutokana na mfano halisi na wa wazi kutoka kwake. Kitendo cha kumhakikishia kuwa, hata yeye alikuwa akiishi na virusi hivyo kulimpa faraja kubwa sana moyoni mwake.
Kwake, ukimwi ukawa si tatizo kubwa sana. Kichwani mwake aliwaza jambo moja tu; kuzungumza na shangazi yake Juliana.
“Atanielewa kweli?” akawaza.
“Lakini ndiyo ukweli. Kwa nini nisimwambie wakati huu ambao nina hakika kuwa, sina mashaka tena? Lazima nimshirikishe,” akajijibu mwenyewe.
Hata hivyo, akili yake ilikwenda mbali zaidi, akafikiri mambo mengine makubwa zaidi. Aliamini, pengine kwa kumwambia ukweli, angeweza kumnyanyapaa na kumkatisha tamaa.
Aliwaza pengine asingempa ushirikiano na angewatangazia ndugu zake wote kuwa amepata ugonjwa huo. Alikwenda mbali zaidi, akaamini kuwa, pengine wangefikiri kuwa, amepata ugonjwa huo kutokana na tabia zake mbaya.
“No! Sina sababu ya kumweleza, na si yeye tu, sitamwambia mtu mwingine yeyote,” akawaza mwenyewe kichwani mwake.
Wazo hilo akalipitisha moja kwa moja. Likamwingia kichwani na kulikubali.
Alichokuwa akisubiri kwa hamu ni siku ya kukutana na mshauri aliyemsaidia shoga yake, Mai! Haikuwa mbali sana – ni Jumamosi tu! Siku mbili baadaye!
***
Kilikuwa chumba kidogo, kizuri na kilichopangiliwa vitu vizuri. Rangi ya parachichi iliifanya ofisi ile kuwa yenye kuvutia sana. Samani zake pia zilikuwa nadhifu.
Nyuma ya kiti kikubwa cha kuzunguka, alikaa dada mrembo, aliyekuwa amevaa miwani myeupe yenye fremu nyeusi. Vijishimo mashavuni vinaongeza urembo wa michana huyu.
Nyusi zilizojaa juu ya macho yake, zikiwa hazijawekwa kikorombwezo chochote, zinaongeza idadi ya maksi ya uzuri wa mwanamke huyu wa makamo.
Waweza kumuita mdada, lakini hata ukimuita mama hutakuwa umekosea sana, maana tayari ni mama wa watoto wawili. Ana umri wa miaka 32 tu, na bado amejitunza vyema na kuendelea kuwababaisha wanaume wakware wa mjini wanaopenda vya mteremko!
Kwa huyu si wa mteremko!
Ni dada mwenye heshima zake. Msomi, aliyeshiba taaluma ya ushauri wa saikolojia ya maisha. Kwa sasa amebobea katika ushauri nasaha, utafiti na upimaji wa magonjwa ya ngono na ukimwi.
Yes! Aliitwa Sista Isabela!
Mbele ya meza yake kubwa, ikiwa na mafaili machache mezani, walikaa wadada wawili – wazuri kama yeye! Ni Mai na Lilian.
Baada ya salamu na utambulisho, Mai alimweleza kila Sista Isabela kuhusu hali ya Lilian na hofu aliyokuwa nayo. Sista Isabela akatabasamu.
“Nashukuru sana Mai kwa kunisaidia kazi. Ninavyokuamini, najua nina kazi ndogo sana kwa Lilian,” akasema akitabasamu zaidi na kuufanya uzuri wake utamalaki maradufu.
“Ni kweli kabisa,” akasema Lilian.
“Utapenda kwenye mazungumzo yetu Mai awepo au akusubiri nje?”
“Mai ndiye aliyenitoa mimi matongotongo. Sina shida akiwepo, labda kama taaluma yako haikuruhusu, lakini kwa upande wangu. Ni sawa akiwepo.”
“Sawa...nimekuelewa vizuri kabisa, lakini naomba Mai umsubiri tu nje, acha nizungumze naye kwa uhuru zaidi.”
Wote wakacheka.
Mai akasimama na kupiga hatua za kivivu kuelekea nje. Ndani ya ofisi wakabaki wawili tu – Sista Isabela na Lilian.
“Naamini sasa utakuwa huru zaidi. Nikuambie tu Lilian, umekuja mahali sahihi kabisa. Tuliza kichwa chako, kuwa huru na ondoa wasiwasi wako kabisa. Kila kitu kitakuwa sawa,” akasema Sista Isabela.
“Najua unafahamu mengi kidogo kwa sasa kuhusu ukimwi. Hatutajifunza wala kuzungumzia sana kuhusu ukimwi. Tayari unao. Nataka kujadili kuhusu maisha. Kuhusu maisha yako mapya baada ya kujua tayari umeambukizwa.
“Hebu tuanze na hili. Ni jambo gani linalokupa hofu zaidi baada ya kujua kuwa umeambukizwa? Namaanisha, ni wapi unahisi kuna giza nene mbele yako? Hapo ndipo ninapotaka kuanza napo,” alisema Sista Isabela kwa sauti tulivu, akiwa ameyatuliza macho yake usoni mwa Lilian.
Lilian akatulia kwa muda. Akajikohoza kidogo, kisha akavuta pumzi ndefu sana, halafu akazishusha taratibu kabisa.
“Kiukweli nina hofu na mengi. Kwanza mimi ni msichana mrembo, naogopa kukonda... kuonekana kama mgonjwa-mgonjwa. Sina mtoto, natamani sana kuwa na wanangu. Nataka kuolewa, ndoto hiyo imefutika, tena tayari nilikuwa na mpenzi wa kweli ambaye alikuwa tayari kunioa, haiwezekani tena.
“Ona maisha yangu yalivyoharibika. Nimehairisha mpaka mwaka wangu wa masomo. Naua nitarudi, nitamaliza na nitapata kazi... halafu fedha nitazopata zitakuwa na faida gani? Naona kama nimekwisha! Ni giza tu mbele yangu!” akamaliza kusema Lilian akihema kwa kasi.
“Tuliza moyo. Yote hayo si matatizo. Labda nikuhakikishie kuwa, huwezi kukonda na kuonekana kama mgonjwa – dhaifu. Utaolewa, utazaa watoto tena wasio na uambukizo na utayafurahia maisha yako mpaka siku Mungu atakapoamua vinginevyo na si kwa sababu ya ukimwi,” akasema Sista Isabela kwa kujiamini.
“Mh! Kuolewa? Kuzaa watoto wasio na uambukizo? Itawezekanaje? Hapo sasa unanidanganya!” akasema Lilian akitoa macho.
“Hakuna udanganyifu mdogo wangu. Sikia...” akasema Sista Isabela, sasa akianza kupekua kitu kwenye kompyuta mpakato iliyokuwa mezani mwake.
Lilian akatulia akisubiri kumsikiliza!

Itaendelea...
 
Yaani sijui amekuwaje huyu, hadithi zingine alikuwa anaziweka vizuri tu hapa lakini hii sasa mmmh! Imeshakuwa kero
 

Sehemu ya 26
ILIPOISHIA...

“Mh! Kuolewa? Kuzaa watoto wasio na uambukizo? Itawezekanaje? Hapo sasa unanidanganya!” akasema Lilian akitoa macho.
“Hakuna udanganyifu mdogo wangu. Sikia...” akasema Sista Isabela, sasa akianza kupekua kitu kwenye kompyuta mpakato iliyokuwa mezani mwake.
Lilian akatulia akisubiri kumsikiliza!
SASA ENDELEA...
TATIZO la elimu ya ukimwi kutolewa nusunusu lilionekana kumjaa sana Lilian. Tangu anapata ufahamu na kusikia habari za ukimwi, kitu pekee alichojua ni kwamba ukimwi ni hatari!
Ukimwi unua!
Hivyo tu!
Hakuwahi kusikia kuwa, ukimwi ni ugonjwa ambao kwa sasa una namna ya kupunguza makali yake. Kuishi kwa amani na kuendelea na taratibu zote za maisha hata baada ya kuathirika.
Ubongoni mwake alijua, kupata ukimwi ni tiketi ya kifo, basi! Ukipata ukimwi, ndiyo mwisho wako. Si kweli. Juhudi za wataalamu mbalimbali wa afya duniani, zimesadia kuufanya ugonjwa huu kutokuwa tishio sana katika zama hizi.
Hilo tu ndilo ambalo Lilian hakulijua kabisa. Sister Isabela akaonekana kuangalia kitu kwa makini sana kwenye kompyuta yake. Lilian akionekana kuwa na mawazo sana.
“Sikia...umewahi kusikia kuwa, siku hizi wamama wajawazito ni lazima wapimwe ukimwi?” Sister Isabela akauliza.
“Ndiyo, nimesikia.”
“Unajua ni kwa nini?”
“Ili kujua afya zao.”
“Halafu?!!!”
“Kwa kweli sijui zaidi ya hapo,” akajibu Lilian huku akitingisha kichwa kukataa kuwa na ufahamu na jambo hilo.
“Ngoja nikuambie. Kupima ukimwi ni hiyari, lakini mama mjamzito, kwa kuwa ndani ya tumbo lake ana kiumbe chenye haki ya kuishi, kwa masilahi ya kiumbe hicho, kupima sasa inakuwa si hiyari tena.
“Tunapima ili kujua kama mama ameathirika. Kumbuka kuathirika kwa mama, si sababu ya mtoto kuwa na ukimwi. Iko hivi; kama mama atakutwa ameathirika, mtoto hawezi kuwa na ukimwi. Hapo sasa ni kazi ya madaktari kujitahidi kuhakikisha kuwa, mtoto haambukizwi!” akasema Sister Isabela.
“Habari mpya sana kwangu hizi. Kwahiyo sasa, inakuwaje mtoto anakuwa katika tumbo la mwanamke mwenye virusi halafu asiambukizwe na mama yake?” akauliza Lilian.
“Elimu yake ni pana kidogo lakini kwa sasa unatakiwa kufahamu kuwa, eneo pekee ambalo mtoto anaweza kuambukizwa ni wakati wa kuzaliwa.
“Lakini kwa sababu madaktari watakuwa wameshajua, mama atapatiwa dawa maalumu ya kupunguza kasi ya kusambaa kwa virusi na dawa na kuimarisha zaidi chembe hai zake nyeupe za damu, lakini pia atashauriwa namna kuitunza afya yake.
“Pia atapatiwa dawa za kumkinga mtoto wakati wa kuzaliwa, ambazo zitasaidia mtoto asiambukizwe. Hata hivyo kuna umakini zaidi wa kitaalamu wa kuhakikisha mtoto anakuwa salama angalau kwa asimilia 80.
“Madaktari watakuwa makini sana kuhakikisha wanafuatilia kwa karibu afya ya mama. Wakiona kuna dalili nyingi za mtoto kuambukizwa, mara moja hatua zaidi huchukuliwa ikiwepo kujifungua kwa upasuaji.
“Ni elimu pana ambayo inahitaji muda kujifunza taratibu. Nikutoe hofu kuwa, ukimwi siyo kifo. Maisha yanaweza kuendelea kama kawaida baada ya kuwa na virusi hivyo,” akasema Sister Isabela.
Lilian alivuta pumzi ndefu sana, kisha akazishusha taratibu kabisa. Alikuwa amejifunza kitu kipya kabisa katika maisha yake. Hofu iliyokuwa imemjaa, ikaanza kushuka taratibu moyoni mwake.
“Naanza kukuelewa Sister Isabela,” akasema Lilian.
“Najua...najua sana. Lakini Mai alisema eti, inawezekana mwanamke akawa na uambukizo na mwanaume akawa hana, lakini mwanaume asipate. Ni kweli?”
“Kabisa! Ilivyo ni kwamba, mwanamke ana hatari kubwa ya kuambukizwa kuliko mwanaume. Hiyo ni kwa sababu za kibaolojia. Jambo kubwa linaloshauriwa ni mwanamke kuandaliwa vya kutosha kabla ya tendo.
“Jambo hilo likifanyika kikamilifu, mwanaume hawezi kuambukizwa. Hata hivyo watu wanaoruhusiwa kufanya hivi ni wanandoa, ambao mmoja wao kwa bahati mbaya atakuwa ameathirika.
“Hata hivyo, ushauri wa mwisho na mkubwa zaidi kwa wanandoa wa aina hiyo, ni kutumia mpira muda wote, mpaka pale watakapohitaji mtoto ambapo lazima wawe karibu na wataalamu ambao watawaelekeza njia bora na salama zaidi ya kufanya ili mwanamke kupata mimba na kumuacha mwanaume akiwa hana virusi vya ukimwi,” akasema Sister Isabela.
Lilikuwa somo gumu sana, lakini Isabela alijitahidi kuzungumza kwa lugha nyepesi ambayo Lilian alimwelewa kwa urahisi zaidi.
Mpaka anaondoka ofisini kwake, alikuwa Lilian mpya kabisa. Mwenye mtazamo mpya na fikra mpya kabisa. Alimshukuru sana shoga yake Mai.
***
Lilian akiwa ndiyo kwanza anafungua geti la kuingia nyumbani kwa shangazi yake, Juliana, simu yake iliita. Alipoitazama kwenye kioo, akakutana na jina la Edo!
Moyo ukamlipuka!
Mara moja akapokea.
“Edo baba yangu... umenikumbuka leo?” Lilian akazungumza akiwa mnyonge, ushahidi mkubwa ikiwa ni sauti yake.
“Ndiyo mpenzi!”
Lilin akashtuka tena!
Anaitwa mpenzi?
“Lilian...” Edo akaita.
“Yes Edo!” (Ndiyo Edo)
“Usinyongee, wewe ni wangu. Siwezi kukutupa mama. Sasa sikia, nina bonge la surprise!”
“Surprise? Which kind of that?” (Mshtukizo? Ni mshtukizo gani huo?)
“Kesho saa 8:30 mchana kwa saa za huko, nitakuwa airport, naomba usiache kuja kunipokea!”
“Waooo kweli?”
“Sijawahi kukudanganya. Kwa heri kwa sasa Lilian, tafadhali kuwa na utulivu. Nina habari njema sana kwako hiyo kesho nikija.”
“Sawa mpenzi wangu....oooh! No... sawa Edward...” akasita Lilian.
“No! No! No! It’s okay... mimi ni mpenzi wako. Uko sahihi kabisa. Hakuna kilichobadilika,” Edo akasema na kukata simu.
Lilian akabaki anashangaa!
Aliisubiri kwa hamu sana hiyo kesho!
***
Macho ya Lilian yalikuwa yanaangalia kwenye lango kuu la abiria wanaowasili kutoka sehemu mbalimbali katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.
Abiria walikuwa wakitoka huku wakiburuza mizigo yao kwenye vitoroli. Kwa mbali, akamwona Edo akiwa anasukuma kitoroli chenye mizigo yake.
Lilian hakuamini.
Edo alikuwa amejawa na tabasamu. Kwa shauku, Lilian akajikuta akianza kukimbia akimfuata Edo aliyekuwa akitembea kama hataki, kuelekea alipokuwepo!
Ilikuwa siku mpya kwa Lilian.

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia.
 
Yaani sijui amekuwaje huyu, hadithi zingine alikuwa anaziweka vizuri tu hapa lakini hii sasa mmmh! Imeshakuwa kero
Nioneee huruma jamani, niko bize mbaya, ila huwa najitahidi sana kuweka kila wiki, nawapenda ndiyo maana nawawekea, kweli vile niko bize maisha yanabadilika.... nakuomba radhi msomaji wangui na wengine wote ila naahidi kila wiki haitakosekana.
 
hivi ndo nini kutusubirisha muda mrefu kusoma muendelezo wa hii hadithi????kama hujajipanga kuileta kila wiki nakushauri ni bora kuacha kabisa kutuletea hadithi...hebu amka ulipolala njoo utupie vitu.......
Pole ila punguza hasira.
 
Nioneee huruma jamani, niko bize mbaya, ila huwa najitahidi sana kuweka kila wiki, nawapenda ndiyo maana nawawekea, kweli vile niko bize maisha yanabadilika.... nakuomba radhi msomaji wangui na wengine wote ila naahidi kila wiki haitakosekana.

Haya, binafsi nimekuelewa but inapendeza pia kama ni kila wiki basi kama ni jumamosi au jumapili unaipost, sawa momma....
 
Haya, binafsi nimekuelewa but inapendeza pia kama ni kila wiki basi kama ni jumamosi au jumapili unaipost, sawa momma....
Powa tufanye lini Jumamosi au Jumapili, naomba upendekeze.
 
Back
Top Bottom