Hisia Zangu 18
ILIPOISHIA...
Kwa nini usifikiri labda mimi ndiye naonekana nina ukimwi? Tunahitaji kuwa waangalifu mpenzi. Tuna mipango mingi sana mbele yetu kuhusu maisha yetu. Hatuwezi kuwa rahisi kiasi hiki. Kama kweli unanipenda, tutoke sasa hivi, twende tukapime tuwe na uhakika na afya zetu kisha tuendelee na mambo mengine, akasema Edo.
Sawa, akasema Lilian kwa hasira, akainuka kitandani na kukimbilia bafuni ambapo alioga, alipotoka alimkuta Edo ameshavaa anamsubiri yeye.
Haya twende, akasema Lilian.
Ok!
Edo akabamiza mlango, akaingiza ufunguo kwenye kitasa, akafunga. Wakaanza safari ya kwenda kituo cha afya.
SASA ENDELEA...
MOYONI Edo alikuwa na mawazo mengi sana. Alijaribu kumfikiria Lilian wake, si yule mwenye msimamo tena. Nini kimetokea hadi msimamo wake ubadilike? Ni kweli alikuwa na hisia, tena hisia kali sana za kimapenzi, lakini isingekuwa rahisi kuingia kwenye mtego wa namna ile.
Alikuwa na wasiwasi mwingi sana moyoni mwake. Hakujua ilivyokuwa, lakini alijishangaa kwa namna alivyoingiwa na wasiwasi wa ghafla.
Siwezi kuwa mjinga kiasi hiki, lazima kuna kitu, akajisemea moyoni mwake Edo wakati akipiga hatua kutoka kwenye chumba chake na kushika korido kuelekea nje.
Lilian alikuwa akitembea bila wasiwasi kabisa, hakuonekana kufikiria jambo lolote baya kichwani. Alikuwa katika hali ya kawaida kabisa.
Lilian na msimamo wake wote ule? Leo anawezaje kubadilika? Anawezaje kukubali kirahisi namna hii? Lazima atakuwa ameshaanza haya mambo. Angekuwa bado ningejua tu...hapa kuna kitu, akazidi kuwaza Edo.
Edo hakuwa na gari, hivyo walitoka kwa miguu hadi kwenye kituo cha teksi, wakaingia kwenye mojawapo.
Wapi bro? dereva teksi akauliza.
Tabata Health Centre.
Sawa, si pale kwa Dk. Manungu?
Sina hakika, naijua tu hiyo hospitali, sifahamu jina la mmiliki.
Sawa. Kaka, huyo ni daktari maarufu sana, alikuwa Muhimbili, sasa ni mstaafu ndiyo akaamua kufungua senta yake hapa Tabata.
Kikubwa ni kutufikisha hapo kaka, kanyaga mafuta tafadhali, akajibu Edo akionekana kutohitaji maneno mengi kutoka kwa dereva yule.
Gari likapepea!
Hapakuwa mbali sana, dakika kumi tu baadaye, teksi hiyo aina ya Toyota Carina, lenye rangi nyeupe na mstari wa kijani pembeni, iliegeshwa mbele ya hospitali hiyo ambayo iliaminika sana katika Kitongoji cha Tabata.
Kiasi gani?
Elfu tano zinatosha bro.
Sawa.
Edo akaingiza mkono mfukoni, akatoa pochi yake kisha akachomoa noti moja ya elfu kumi kati ya nyingi zilizotunisha pochi hiyo. Akamkabidhi dereva, kisha akamshika mkono Lilian na kuondoka.
Chenji yako kaka... akasema dereva yule akitoa noti moja ya elfu tano kupitia dirishani.
Edo akageuza shingo kumwangalia, akaachia tabasamu changa ambalo alijitengenezea. Akachanganya midomo, akasema: Ni lini utakunywa soda wewe? Kazi njema!
Dereva akachekelea!
Hakuwa amezima gari lake, lilikuwa silence! Alichokifanya ilikuwa ni kuachia mguu aliokanyaga breki taratibu, mikono yake ikiwa kwenye usukani, kisha akahamisha mguu wake wa kulia kwenye kibati cha mafuta, akakanyaga taratibu, teksi ikayoyoma!
Pesa bwana...kweli pesa inaongea, akajisemea dereva yule wakati akiendelea kuongeza spidi kurejea kituoni kwake.
Siku yake ilikuwa inakaribia kuisha vizuri.
***
Karibuni tafadhali, sauti ya dada mrembo, aliyekuwa mapokezi katika hospitali hiyo ilitoka akiwatazama Edo na Lilian.
Ahsante, tunahitaji huduma ya ushauri na kupima.
Oooh! Karibuni sana, bila shaka kabisa. Huduma inapatikana, piteni na hii korido, mtakata kulia pale mbele, room ya kwanza mtaiacha, mtaifuata ya pili ambayo mlangoni imendikwa VCT. Ni hapo mtaingia.
Ahsante sana.
Edo akamshika mkono Lilian kisha wakaongozana kuelekea chumba cha mshauri. Kwa namna walivyoelekezwa, haikuwa vigumu kufika.
Edo akagonga mlango, kisha wakaingia. Wakapokelewa na mshauri mmoja aliyekuwa amekaa kwenye kiti cha kuzunguka. Akawakaribisha na tabasamu mwanana kabisa.
Karibuni na mjisikie huru! akasema mshauri huyo.
Ahsante sana.
Karibuni tena...mimi naitwa Dk. Siwema, ni mwanasaikojia, mtaalamu wa ushauri nasaha kwenye mambo mengi katika jamii lakini kwa sasa nimebobea zaidi kwenye elimu rika na ukimwi. Naomba tufahamiane tafadhali, akasema Dk. Siwema akitabasamu.
Mimi ni Edward lakini nimezoeleka zaidi kama Edo, huyu ni mpenzi wangu, yeye anaitwa Lilian au Lily.
Nimefurahi sana kuwafahamu Edo na Lily, acha nami niwaite hivyo, akasema Dk. Siwema huku akicheka.
Wote wakacheka.
Ndiyo! Sasa naomba niwasikilize.
Sisi tumekuja hapa kwa ajili ya kupima afya zetu.
Kivipi?
Tunataka kupima virusi vya ukimwi.
Vizuri sana, hilo wazo mmeamua pamoja au kuna mmoja amekuwa na shinikizo kwa mwenzake? Dk. Siwema akauliza.
Wote walibaki kimya, ni kama walikuwa wanategeana hivi...
Aaaah! Nataka swali hili anijibu Lily.
Siwezi kusema kama kumekuwa na shinikizo lakini lilikuwa wazo la mwenzangu. Sijaona kama ni vibaya, ni wazo zuri tu, ndiyo maana nimeamua kuja naye hapa.
Je, mmewahi kukutana kimapenzi? akauliza Dk. Siwema.
Hapana, wakajibu wote kwa wakati mmoja.
Kwa nini?
Tulikubaliana kufanya hivyo siku tutakapoona, akajibu Edo.
Je, sasa mpo tayari kuoana?
Tutaona tu, lakini muda bado. Wote bado tunasoma. Mimi nipo Malaysia na mwenzangu anamalizia UD (University of Dar es Salaam), lakini kwa kweli uzalendo umetushinda, tukaamua kuliko kusalitiana ni bora tuanze tu wenyewe.
Sawa. Je, mpo tayari kushauriwa pamoja majibu mpokee pamoja?
Ndiyo, tupo tayari.
Vizuri sana. Najua siku hizi elimu ya ukimwi ipo wazi sana hivyo hakuna mambo mengi sana mapya ya kuwafundisha hapa. Jambo la msingi mnalotakiwa kujua ni kwamba, kwanza mmefanya vizuri sana kuamua kujuana afya zenu kabla hamjaanza kufanya chochote.
Ni wazo zuri, lakini vizuri pia mkiendelea kuwa makini hata baada ya majibu yenu. Mnapaswa kuwa waaminifu katika uhusiano wenu, hapo ndipo mtakapoona raha ya uhusiano. Sasa turudi katika suala lenu. Vipi kama ikitokea mmekutwa wote mmeathirika?
Ikiwa tutakuwa tumeathirika wote, kwa kweli tutaumia sana, lakini itabidi tuendelee na uhusiano wetu huku tukipeana moyo, akajibu Edo.
Niwatoe hofu, ukimwi usiwaogopeshe sana, hata kama mkikutwa nao au mmoja wenu akawa ameathirika, hampaswi kuchanganyikiwa. Mkifuata ushauri vizuri, mtu anaweza kuishi zaidi ya miaka ishirini baada ya kujua kama ana maambukizi.
Ninao marafiki wengi sana ambao wameathirika na maisha yao yanaendelea kama kawaida. Msijali. Kupima ni kujua ukweli wa afya zenu. Hata kama msipojua leo, kuna siku mtajua mkiwa mmeshachelewa.
Ni afadhali mjue mapema, muanze kufuatilia masharti mapema na kwa usahihi ili muweze kuishi maisha marefu. Nasisitiza, msiwe na wasiwasi, sawa jamani?
Sawa dokta.
Sasa mpo tayari nichukue vipimo vyenu?
Ndiyo!
Itaendelea wiki ijayo...