***
Kwa Joram Kiango ilikuwa kazi rahisi kuliko alivyotarajia. Mara tu alipomwona Inspekta Kombora akishindwa kuchukua hatua dhidi ya Kakakuona, badala yake akianzisha msafara wa kumfuata, yeye pia alifanya hima kuliendea mojawapo ya magari mengi yaliyokuwa yakisubiri abiria nje ya stesheni.
Alichagua gari jipya, aina ya Suzuki, lenye namba za Posta, ambalo ingawa dereva alidai kuwa yuko kazini, lakini Joram hakuchelewa kugundua kuwa alikuwa akisubiri abiria yeyote ambaye angemkodi ili ampatie chochote cha kutia mfukoni.
“Una petroli ya kutosha?” alimuuliza.
“Kwani unakwenda mbali mzee?”
“Itategemea,” Joram alijibu akizunguka upande wa pili ambako alifungua mlango na kuingia ndani. “Ifuate ile. Ifuate taratibu wasijue kuwa wanafuatwa.”
Dereva huyo alionyesha wasiwasi kidogo. “Gari ile, mzee! Kwa nini tuifuate? Unajua…” alisita kidogo. Lakini alipoona kitita cha shilingi elfu tano kikiwekwa juu ya mapaja yake alionekana kubadilika kidogo.
“Wakienda mbali zaidi nitakuongeza,” Joram alisisitiza, huku akimhimiza kuondoa gari.
“Tatizo ni kwamba ile gari naijua brother,” alisema akiondoka shingo upande. “Ile ni gari ya wenyewe ile. Inatumiwa na manjagu, pamoja na kuwa na namba za kiraia. Naogopa wasije wakaniletea matatizo wakijua kuwa wanafuatwa.”
“Usijali, hawatafahamu.”
Akili ya Kakakuona ikiwa juu ya magari ya Kombora ambayo alikwishayakariri namba zake vizuri sana kichwani, hakujishughulisha na gari dogo la Posta ambalo lilionekana kwa mbali sana miongoni mwa magari mengine.
Aidha, Kombora vilevile fikra na hisia zake zote zikiwa katika gari la mbele yake, ambalo lilimchukua muuaji hatari kama Kakakuona, hangeweza kulitazama gari hilo la Posta lililokuwa nyuma yao. Hali kadhalika, ikiwa tabia ya polisi ni kufuata badala ya kufuatwa, kusaka badala ya kusakwa, wazo la kugeuka nyuma mara kwa mara halikumjia akilini kabisa. Tabia hii ilifanya kazi ya Joram na dereva wake iwe nyepesi kama ilivyokuwa.
***
Ulikuwa ni msafara usio na kona nyingi wala mizunguko mingi. Ilielekea kama Kakakuona alikuwa hana haja ya barabara nyingine zaidi ya ile ya Morogoro, Hata hivyo, walipofika Mtaa wa Jamhuri, gari hilo lilionekana likipinda kulia kuufuata mtaa huo. Gari la Kombora likafanya hivyohivyo. Joram pia akamwamuru dereva wake kuwafuata.
Njia hiyo ilikuwa na msongamano mkubwa wa magari hivyo, safari yao ilikuwa ya taratibu, jambo ambalo lilimtia hofu Kombora kuwa Kakakuona angeweza kuitumia fursa hiyo kuchepuka ghafla mahala ambapo asingekuwa mwepesi wa kuona alipoelekea.
Lakini Kakakuona hakuonekana kama mwenye haraka ya kufanya hivyo. Aliendelea na safari yake taratibu kama ambaye alikuwa na nia njema sana ya kumwongoza Kombora na msafara wake hadi alipoufikia uchochoro ambao unachepuka na kuunga mtaa huo hadi Mtaa wa Kisutu ambapo alionekana akisogea kulia na kuliingiza gari katika ukumbi wa jengo moja jipya, ambalo liliacha eneo zuri la kupaki magari chini yake kwa meta kama kumi ndani yake.
Kombora alilitazama gari hilo likipaki kwa utulivu. Alitumia dakika mbili tatu za kuduwaa, akijiuliza afanye lipi, kwa makini. Jengo hilo lenye ghorofa nne lilikuwa moja kati ya majengo mapya yaliyokuwa yakiibuka huko na huko jijini Dar es Salaam.
Vibao vya kampuni na biashara mbalimbali vilionekena katika kuta mbalimbali za jengo hili chini ya kibao kilichoandikwa Sunrise Modern Club. Kibao hiki kilimeza karibu robo ya ghorofa zima ya chini. Maandishi yake yalikuwa juu ya kioo kikubwa, kwa rangi mbalimbali ambazo usiku ziliwaka kwa namna ya kuchezacheza katika hali ya kuvutia macho. Kombora aliwahi kupita hapa mara nyingi usiku na kuvutiwa, kama watu wengine, lakini hakuwahi kuingia ndani. Kumwona Kakakuona akipaki hapo aliyakumbuka mauaji ambayo amekuwa akiyafanya katika hoteli na kumbi za starehe kama yale ya Lang’ata; akajikuta akipatwa na hisia za hatari kuliko awali.
“Liwalo na liwe,’ aliwaza. “Tunamfuata hukohuko ndani,” aliamuru, “Angalieni. La msingi ni kuyaokoa maisha ya Nuru. Hivyo, risasi za kwanza, kama itabidi, ziwe za kumvunja mabega, ili asiweze kuitumia mikono yake. Aliye kulia, alenge mkono wa …”
Kombora alilazimika kuyakatisha maongezi yake alipomwona Kakakuona akishuka huku akifuatiwa na Nuru ambaye alikumbatiwa kiuno kama wapenzi wa damu.
Walishuka harakaharaka na kuingia ndani ya jengo hilo.
Kombora, akiwaongoza askari wake wawili, pia alishuka na kumfuata. Alipolifikia gari lililokuwa likitumiwa na Kakakuona nusura atokwe na ukelele wa mshtuko, mshangao na hasira, alipomtazama dereva.
Alikuwa amelalia usukani wake akitapatapa; tundu kubwa la risasi likiwa limekifumua kichwa chake kisogoni, na kuruhusu damu nzito iliyochanganyika na ubongo iendelee kumwagika kama uji mwekundu unaomwagika toka katika birika.
“Haraka… ndani,” Kombora alinguruma akiitoa bastola yake na kutangulia ndani ya jengo hilo. Mlango uliwaongoza katika korido nyembamba iliyowafikisha katika chumba cha mapokezi, ambacho kilikuwa na makochi manne makubwa yaliyokuwa matupu. Makochi hayo yalikielekea chumba cha kioo ambamo hamkuwa na mtu. Kombora alitazama huku na huko kama anayeomba msaada. Aliiona lifti, na upande wa pili aliiona ngazi iendayo juu.
“Mmoja atumie lifti, mwingine apande kwa ngazi. Upesi. Kama nilivyosema, mkimwona msizungumze naye. Acheni risasi zizungumze. Ok?”
Wakati yule aliyeamriwa kwenda kwa miguu alipoanza kupanda ngazi harakaharaka na yule wa lifi akiita kwa kubonyeza tufe, Kombora aliitoa walkie talkie yake na kuwaamuru makachero wengine kuja mara moja. Kisha, akasogea kaunta bila kujua alihitaji nini. Kama awali alijisikia kupiga kelele, safari hii akijisikia kuzimia kwa kile ambacho alikiona chini ya meza hiyo ya kaunta.
Mzoga wa mtu ulikuwa umelala kifudifudi katika dimbwi la damu nyingi ambayo ilikuwa ikiendelea kujaa sakafuni. Dalili yoyote ya uhai haikuwamo katika umbile hilo ambalo sare alizovaa msichana huyo zilionyesha kuwa alikuwa mhudumu wa mapokezi.
Akili ya Kombora ilidumaa kwa kitambo cha robo dakika. Watu wawili, wasio na hatia, kuuawa huku yeye anashuhudia…! Aliwaza kwa uchungu. Alishindwa kuendelea kuwaza. Badala yake alikurupuka mbio kuiendea ngazi ambayo aliipanda kwa kuruka ngazi tatu tatu, bastola ikiwa imemtangulia.
***
Kwa Nuru ilikuwa kama mtu anayeshuhudia mchezo wa sinema ya kusisimua ambao yeye mwenyewe ndiye mtazamaji, wakati huohuo mwigizaji. Naam, ilikuwa kama ndoto tu; tangu alipojikuta akihama kutoka katika mikono ya yule muuaji Chongo na kuangukia katika milki ya Kakakuona. Kama kondoo, aliafiki kila alichoelekezwa. Aliafiki kuushika mkono wa muuaji huyo huku akitabasamu.
Kadhalika, aliafiki kupita kote huku akijua kabisa kuwa kila hatua anayopiga na muuaji huyo inamsogeza karibu zaidi na mauti yake mwenyewe.
Hata hivyo, ile kiu yake ya kufahamu kwa undani zaidi kiini cha mauaji haya ilikuwa sababu nyingine iliyomfanya aendelee na ukondoo huo. Aidha, ile bastola yake, ambayo aliificha vyema alipokuwa akioga bafuni ilimpa moyo na kumpa matumaini ya kupata fursa nzuri ambayo ingemwezesha kuyaokoa maisha yake mara mambo yatakapovuka kina.
Matumaini hayo yaliongezeka maradufu mara aliposhuka bandarini na kumwona Joram Kiango akimsubiri, bila ya Kakakuona kumtambua. Nuru alizidi kupata moyo.
Ilikuwa mara yake ya kwanza kumtia Joram Kiango machoni. Ile hofu yake kuwa tayari wauaji hawa wamempata ikatokomea. Ingawa hawakuongea wala kupeana ishara yoyote, lakini bado kule kumwona akiwa hai na kuyaona macho yake yaking’ara kama ilivyo kawaida yake kulimwongezea ari na kumpa matumaini makubwa ya ushindi.
Hivyo, hakuwa na hofu kubwa sana pindi walipochukua gari na kuondoka huku domo la bastola ya Kakakuona, iliyofichwa mfukoni, likiendelea kumtekenya ubavuni. Wala hakubabaika Kakakuona alipouandika ule ujumbe wa kejeli kwa Kombora, ambao ulikusudiwa kumwongezea hofu.
Lakini, mara tu baada ya gari kusimama hapa na Kakakuona kufanya kile kitendo ambacho Nuru hakukitarajia, alijikuta akiingiwa na hofu kubwa iliyochanganyika na hasira.
Ndiyo, Nuru ameshuhudia mara nyingi watu wakiuawa. Kamwe hakuwa mgeni kwa hilo. Lakini kuuawa kwa kijana huyu wa Kipemba, asiye na hatia, ambaye aliwaendesha bila hofu wala hisia zozote za hatari, kuliufanya moyo wake ukose baadhi ya mapigo yake, hasa pale alipoona kijana wa watu akianguka ghafla juu ya usukani kama mbuzi.