HADITHI: KIZUIZI
SEHEMU YA KUMI NA SABA
Alipoanza kupiga mara likatokea jina. Jina katika simu ya
mkewe.
SAM WA PILI.......
James akataharuki, akakata ile simu mara moja.
Wasiwasi ukatanda, Sam wa Pili ndiye Jose B waukweli. Maajabu.
Na ameanza lini kuwasiliana na mkewe, na alimjuaje? Ina maana mkewe anajua juu ya KIZUIZI ambacho kiliondoka na roho za Bibiana na Deo.
James akahisi kijasho chembamba kikipenya katika uti wa mgongo wake.
Kisha akagundua kuwa alikuwa anatetemeka.
Hofu. Hofu kubwa ikatanda.
KIZUNGUMKUTI........
James akabaki katika sintofahamu, alitamani kumwamsha mkewe usiku huohuo aweze kumuuliza Sam wapili ni nani. Akakiendea chumba kwa mwendo mkali wa kisharishari.
James hakuwahi kufikiri kuwa ipo siku anaweza kukumbwa na hasira za kuwaza kumpiga mwanamke lakini siku hiyo alijihisi yupo katika jinamizi la kufanya kitu kama hicho.
Alipofungua mlango alikutanisha macho na kiwiliwili cha mkewe kikiwa hoi kwa usingizi.
Akataka kumuamsha, mara akasita. Akajiuliza swali moja tu.
Kipi kilikuwa bora kwake, mke na mtoto ama ukweli.
Akatumia sekunde kadhaa kuchambua majibu haya. Alifikiria jinsi anavyojisikia amani kuwa na mwanamke kama Emmy, amani inayozidishwa na kitoto kinachorukaruka kwa furaha tumboni. James akakiri kuwa vitu vile vilikuwa vinakamilisha furaha yake na hakuwa tayari kuvipoteza.
Akahamia upande wa pili. Akafikiria namna atakavyoukabili ukweli, ukweli asioufahamu juu ya ni kitu gani Emmy anajua juu ya Jose B.
Vipi kama anajua kuhusu Kizuizi? Huu utakuwa mwanzo wa maelewano kupotea na kisha kuachana. James akaumizwa na fikra hizo za kuachana na Emmy.
Akanywea, akaamua kuachana na ukweli, kizuizi cha kugombana na Emmy kikawa kimemzuia.
Siku iliyofuata asubuhi alimuaga Emmy, wakakumbatiana kisha akatoweka.
Kichwani akiwa amevurugwa kabisa bila kujua ni wapi mahali sahihi anataka kuelekea.
****
Jose B hakuwa mtulivu katika kijiwe chake, kila mara aliwaza juu ya tukio lililotokea baina yake na Emmy, lilikuwa tukio ambalo hakulitegemea hata siku moja lakini sasa lilikuwa limetokea na aliburudika.
Jose B akafumba macho na kumfikiria James. Akaanza kumuonea wivu kwa jinsi anavyofaidi kuchangia kitanda kila siku na msichana mrembo kama Emmy. Jose B akajiona kuwa na yeye alikuwa ana haki ya kufaidi ladha tamu kama ile.
Jose B akajiona kama ni mjinga kwa kutaka kuchangia penzi na mwanaume mwenzake tena ambaye amefunga ndoa kabisa.
Kwanini nisitafute msichana mwingine? Alijiuliza.
Ni hapo alipogundua kuwa licha ya kuwa mwongeaji sana na mjuaji wa mengi hakuwa na uwezo wa kumsimamisha msichana kwa ajili ya kumtaka kimapenzi. Mara yake ya mwisho kuwa katika mahusiano alisaidiwa na rafiki yake ambaye ndiye alikuwa mzungumzaji mkuu.
Sasa yupo jijini Dar na rafiki yule yupo Mwanza.
Jose B akaona hali hiyo inamtia katika kizuizi.
Ni kweli kuna wasichana wengi tu walikuwa wanamchekeachekea na yeye anawachekea, hakuzijua ishara za watoto wa mjini, akangoja msicha amfuate na kumwambia ‘Jose nakupenda....' jambo ambalo aliendelea kulingoja bila mafanikio hadi siku anayokutana kimwili na Emmy bila kutarajia.
Jose B akawa anataka tena mchezo huo ujirudie, lakini uzito wa mdomo wake angeanza vipi kumweleza mama yule mtarajiwa? Kamwe asingeweza.
Siku mbili zikakatika bila hali ile kutoweka katika kichwa chake.
Kila alipokuja msichana kutoa ama kuweka pesa Jose B alijikuta akimtamani. Tatizo hili likawa kero isiyostahimilika.
Hakufanya mawasiliano zaidi na Emmy, alijaribu kufanya hivyo ili aweze kusahau lile tukio lakini kumbe kufanya vile ndio kujitesa zaidi.
Uvumilivu ulipozidi. Akamtumia ujumbe mfupi wa kuhitaji kuonana naye.
Emmy aliupokea ujumbe huu majira ya mchana akiwa jikoni anapika. Siku hii hakwenda kazini, ilikuwa siku yake ya mapumziko.
Nyumbani alikuwa peke yake. Mdogo wake Jose na mdogo wake walikuwa wameenda shuleni.
Uvivu wa Emmy kumfuata Jose B alipo, na pia hali ya mumewe kuwa safarini akaamua kumuita Jose B nyumbani.
Jose B hakutegemea majibu yale.
Majibu yale hayakumfurahisha, kikubwa cha kwanza alichowaza ni fumanizi ama kuabishwa mbele ya mume wa Emmy.
Jose akajiuliza mara kadhaa kisha akamuona Emmy kama msichana -------- anayetaka kuiharibu ndoa yake kirahisi namna ile.
"Akiniumbua natibua kila kitu tena nasema kabisa alifanya mapenzi na ndugu yake...hawezi kunifanya mimi mjinga namna hii." Aliapa Jose B.
Baada ya saa zima, kijana mtanashati, ndani ya mavazi ya kisasa alitinga katika nyumba ya Emmy.
Emmy ambaye bado alikuwa katika mapishi, alikuwa amevalia kanga moja pekee, kanga iliyoonyesha vyema maungo yake.
Alikuwa ameumbika haswaa. Jose B akafanya kukohoa kidogo.
"Sam....kuna nini?" Emmy aliuliza huku akionyesha waziwazi kuwa hajaupenda ujio wa Jose.
"Tunaongea huku tukiwa tumesimama ama...."
Emmy akashusha pumzi kwa nguvu kisha akamkaribisha Jose B sebuleni.
Jose akajilazimisha kuizoea ile nyumba akachukua rimoti akabadilisha chaneli katika luninga.
"Sam....." Emmy akaita.
Jose akamtazama kwa makini akiwa amejiandaa kumsikiliza.
"Naomba tusahau yale yaliyotokea na ya siwe chanzo cha wewe kuwa karibu yangu zaidi ya awali. Nakuomba sana Sam, nina ndoa yangu na nimekulipa tayari ulichotaka. Au kuna kipi kingine Sam. Nakuomba Sam kuwa na utu kidogo, nyumba nimetimiza, nimekufungulia lile banda na kodi nimelipia ya mwaka mzima....." Emmy akashindwa kuendelea kuongea midomo ikawa inamtetemeka, na machozi yakaanza kumtoka baada ya kugundua kuwa ndoa yake ipo hatarini.
Akanyanyua upande wa kanga aweze kujifuta machozi, akiwa amesahau kuwa amevaa hiyo kanga pekee.
Jicho la Jose B likakutana na paja lililonona. Midadi ikampanda.
Hakuwa tayari kuikosa ladha aliyoonjeshwa.
"Emmy, kwani nimewahi kuitikisa ndoa yako."
"Hapana, sasa hapa umekuja kufanya nini?"
"Ni wewe umeniita hapa...."
"Baada ya wewe kuhitaji kuonana na mimi." Emmyu alijibu kwa hasira.
Jose B akiwa katika matamanio alijikuta anapata ujasiri. Akazungumza.
"Nina kesi na wewe Emmy. Kubwa kuliko ya awali."
"Kesi?"
"Na malipo yake ni ya kawaida tu, kwa sasa sio nyumba tena. Wala sihitaji banda jingine la kutoa na kuweka pesa. Kwa kifupi sihitaji chochote kitakachokufanya uwaze mara mbili."
"Sam acha kunichanganya tafadhali."
"Ninahitaji ulichonipa siku ile nyumbani kwangu."
"Sam unasemaje? Sam....unasema...sikiliza, naomba usimame na uiache nyumba hii katika utulivu ulioukuta awali."
Jose B akasimama, akaanza kutoka nje, akitembea kwa majivuno.
Emmy alikuwa ameiva kwa hasira, alijisikia msaliti mkubwa kwa jambo alilofanya na Jose B ambaye alimtambua kwa jina la Sam wa pili.
Jose B alipoufikia mlango aligeuka kisha akakiruhusu kinywa chake kuzungumza.
"Nadhani unaikumbuka vizuri biashara yetu ilikuwa inahusiana na wewe kumsaliti Jose kwa mwanaume mwingine huko uswazi Zamzam guest house. Hilo tumelimaliza, lakini kumbe yule mwanaume anaitwa Lameck....na kama hiyo haitoshi ni baba yako mdogo. Emmy una hatari wewe. Yaani na baba mdogo? Ujue hata siamini. Ila sawa ni maamuzi, kama uliweza kumpa baba mdogo Lameck ambaye mnafahamiana na mnachangia damu, sijui kinakushinda nini kunipa mimi mtu usiyenifahamu. Lakini bado unaweza kuamua, aidha niiuze siri hii kwa jamaa mwingine ama utimize nilichokuomba kistaarabu.
Halafu kuna jambo pia nimesahau, umemsaliti James kwa kijana fulani hivi juzi kati...anaitwa Sam wa pili. Biashara nyingine hiyo tunaweza pia kuizungumza ukipenda. Au la nitaiuza mamilioni mengi.
Usiku mwema mama kijacho..." Jose B alimaliza huku akitabasamu.
Emmy alitamani kumzuia asiondoke lakini akagundua kuwa miguu yake ilikuwa haina nguvu tena. Alijaribu kusema neno, mdomo ukawa mzito.
Geti likasikika likibamizwa kwa nguvu, Jose B hakuwa pale tena.
Mshikemshike.
****
Miji miwili katika mikoa tofauti ilikuwa imebeba viumbe wawili wa jinsia tofauti kila mmoja na harakati zake.
Jiji la la Mwanza lilikuwa limemtunza mwanaume jasiri ambaye alikuwa ameamua kuzirudia enzi zake kwa ajili ya kuokoa kile alichokuwa anakipenda kwa dhati.
Huyu alikuwa ni James.
Hakumtaarifu mtu yeyote juu ya uwepo wake katika jiji la Mwanza.
James alikuwa anafanya msako wa kimya kimya. Harufu ya kuua ilinukia katika pua zake.
Aliitamani roho moja baada ya nyingine ili kuuficha ukweli.
James alihitaji kumkabili Jose B ambane ili auseme ukweli wote ambao ameuropoka kwa mkewe kisha amuue ili kuondoa ushahidi.
James aliamini kuwa siri ambayo mke wake anaimiliki haitakamilika bila kuwa na ushahidi. Na kama hapatakuwa na ushahidi atakuwa na uwezo wa kumruka Jose B na kudai kuwa alikuwa anamsingizia.
Na endapo Jose B atatafutwa ili aweze kutoa ushahidi, mwili wake utakuwa ukiendelea kuoza katika aidha ardhi ama utakuwa umeliwa na samaki. Inategemeana kifo atakachokufa.
Uamuzi huu James akauona kuwa ni uamuzi sahihi zaidi.
Sasa yupo katika jiji la Mwanza kumsaka Jose B waukweli aweze kuiondoa roho hii inayoushikilia ukweli.
Jiji la Dar es salaam, lilikuwa limetembelewa na mwanamke wa makamo, akiwa na pete katika kidole chake cha shahada.
Hasira yake ilikuwa imepungua kwa kiasi fulani japo alikuwa hajaridhika.
Hii ilikuwa safari yake kubwa ya mwisho katika mlolongo wa safari zake za siri tangu alipodhaniwa kuwa ni mfu.
Hakuna aliyedhania roho hii ilikuwa inaishi, japo suala la kifo chake lilibakia kuwa katika mabano. Hakuna aliyeweza kukielezea.
Hata baba yake alibaki katika sintofahamu. Akishindwa kumtupia mtu yeyote lawama juu ya kifo hicho.
Akaufuga uchungu wake, uchungu uliokuwa unamtesa.
Hatimaye ule uchungu ukamkondesha kisha ukazalisha magonjwa ya ajabu ajabu katika mwili wake.
Akaiaga dunia huku akiwa haamini kama mwanaye amekufa. Lakini hakuyasema hadharani.
Akazikwa huku ile roho aliyoamini kuwa bado inaishi ikibaki duniani.
Na sasa roho hii ipo katika jiji la Dar es salaam. Roho yenye chuki kali. Chuki ya miaka kadhaa iliyopita, chuki kali, na aliamini kuwa yu hai ili aweze kufanya mambo mawili tu. Kulipa kisasi na kuuweka ukweli wazi kwa kila mwenye mashaka.
Kisasi cha damu ndiyo kisasi pekee alichoamini kuwa ni sahihi kwa majina hayo.
Roho hii ya mwanamke iliyojihifadhi katika mwili dhaifu ilikuwa katika chumba namba kumi na nane katika nyumba ya kulala wageni pembeni kidogo ya jiji.
Majina kadhaa yalipangana katika kichwa chake.
Kindo, Keto na Kakele.
Aliwahitaji kwa hali na mali.
Na aliamini kuwa kwa kumpata mmoja wao lazima atampata na mwingine, kisha huyo mwingine naye lazima atamtaja mwenzake.
Kazi ikapangwa kuanza rasmi siku inayofuata.
Katika jiji hilohilo la Dar es salaam.
****************
**KIZUIZI kimezua balaa..JOSE B ananogewa na penzi, anaongeza kizuizi ili aendelee kuburudika. JAMES yu jijini Mwanza akimsaka Jose B ili aujue ukweli kisha amuondoe duniani....LAMECK na kizuizi cha undugu lakini anamtaka mtoto ambaye anaamini kuwa ni damu yake.
***MWANAMAMA yu katika jiji la Dar anazisaka roho tatu..KETO, KINDO na KAKELE....ni akina nani hawa........
***Kuna siri gani imejificha katika KIZUIZI.......