SEHEMU YA KUMI NA TANO
Alipofika mahali pazuri kabisa
akatoa kitabu chake kidogo
akaibuka na namba za simu
akabofya zikaita.
Hakujitambulisha mapema.
Akatumia uumbaji wa maneno.
Devotha akaingia mtegoni.
Baada ya masaa mawili walikuwa
katika mazungumzo.
Mazungumzo yaliyoanza kwa
furaha tele, lakini baadaye
yakaleta msuguano. Devotha
hayupo tayari kukubaliana na
ukweli wakati mwanaume
anasisitiza kuwa lazima iwe vile.
Devotha anataharuki.
Mwanaume anaposhindwa kuizuia
taharuki ile, anaamua
kuchukua hatua.
Anamkubalia Devotha kwa lile
analolitaka, mwisho wanaagana.
Laiti Devotha angejua, asingefanya
maagano kwa kushikana mikono.
Kwa kutojua hili basi akaibariki
safari yake.
Hatimaye yule dereva taksi
aliyemchukua kumrejesha
nyumbani anatiwa hatiani, kwani
Devotha alikufa akiwa katika
teksi yake.
Taarifa inamfikia Emmy, taarifa
yenye utata.
Mwanamama aliyefahamika kwa
jina la Devotha John amekutwa
amekufa katika taksi. Hilo jina ni
sawa na la mama yake mzazi.
Taarifa ya pili kutoka kwa ndugu
wa karibu ikatoa uhakika,
Devotha aliyetajwa ni yuleyule
mama mzazi na rafiki kipenzi wa
Emmy, mama kitumbo akazimia.
James akamkuta katika hali ile.
Sasa wapo hospitali na Emmy
anasimulia.
UTATA MWINGINE...........
****
Hakuna chozi linaloweza kubadili
msiba kuwa sherehe, na hakuna
kilio kinachoweza kumbadili
aliyekufa aweze kurejea.
Kilio huwa ishara ya uchungu,
kisha maisha yanaendelea katika
hali ya utofauti kwa muda mrefu
kisha huzoeleka.
Emmy hakupata mtu sahihi wa
kumtuliza, kila aliyejaribu
kumtuliza ni sawasawa alikuwa
anampigia Kondoo zeze ili akate
mauno, jambo lisilowezekanika.
Mama yake alikuwa amekufa kwa
kushambuliwa na sumu kali iuayo
mara moja baada ya kupenya
katika ngozi.
Mtu aliyejaribu kwa kiasi fulani
kumtuliza Emmy japokuwa sio
sana alikuwa ni mwanaume
shujaa aliyeyakabidhi maisha yake
kutetea wengine na kuwalinda.
Mwanajeshi kamili Lameck John
Sulube.
Emmy alitulia kwa sababu
hakuwa na taarifa ya marejeo ya
mwanajeshi huyo, na pia ile hatia
ya kuzini nje ya ndoa ikaibuka
upya. Akausahau msiba kwa
sekunde kadhaa. Maneno ya
Lameck yalikuwa yaleyale Ni
mipango ya Mungu!! Usilie sana
utakufuru!!, Bwana ametoa na
bwana ametwaa!!. Maneno
ambayo huwa hayana maana kwa
mfiwa.
Ukaribu wa Emmy na Lameck
Sulube haukumshtua mtu yeyote
ambaye aliijua kwa uchache
familia ile. Waliwatambua hawa
kuwa ni mtu na baba yake
mdogo.
Hata James mumewe hakutilia
mashaka yoyote. Alikuwa anamjua
vyema Lameck, anamfahamu fika
kwani wakati anamrandiarandia
Emmy aliwahi kukunjana mashati
na huyu bwana. Lakini hakuchoka
hadi alipofanikiwa kumuoa na
sasa ni mjamzito.
Ila jicho moja lilikuwa na
mashaka na ukaribu ule.
Akiwa amejivika suti nyeusi
iliyomkaa vyema kijana huyu
anayekimbilia miaka ishirini na
mbili, kichwa chake kikiwa na
nywele fupi zilizopakwa mafuta
ya kungara, kiatu cha bei ghali
kikiuvaa mguu wake. Kijana huyu
alikuwa mtulivu sana, leso yake
mkononi akipambana na jasho
ambalo linataka kumharibia
mwonekano wake. Mkono mmoja
alikuwa na funguo zilizofanana na
za gari.nani anajua huenda
nayeye alikuwa ameegesha gari
lake nje ya nyumba.
Kwa kumtazama usingeweza
kudhania yupo katika dunia
nyingine, akijadili mambo yake
tofauti kabisa na msiba
unaoendelea.
Zilipigwa nyimbo za kusihi watu
waandae nyoyo zao kwa sababu
hatujui saa wala dakika ya
mwisho wetu, yeye hakuzisikia
bali alihisi anapigiwa makelele na
wachina wanaoimba nyimbo zao
kwa lugha yao ngumu.
Hatimaye ukafika wakati wa
kutoa heshima za mwisho kwa
marehemu.
Kutokana na uwingi wa watu
katika msiba huu, ilibidi
mwongozaji atoe utaratibu
maalumu kabisa wa kuuaga mwili
wa marehemu Devotha.
Alianza kwa kuiita familia ya
marehemu, hapa akawaita watoto
na baba. Wakaaga.
Dada, mawifi, shangazi, mama
wadogo. Wakaaga.
Baba wadogo, baba wakubwa,
mashemeji, wajomba, kaka. Nao
wakajongea waweze kuaga.
Yule kijana aliyekuwa amejikita
katika kujipangusa jasho
akasitisha zoezi lile, akaiacha
jasho itiririke, akajisahau kuwa
alikuwa amevaa suti, akaanza
kuhaha huku na huko.
Akazidi kujiuliza ile sura kwa nini
inamvutia.
Mwanzoni alidhani kuwa ni mteja
mmojawapo aliyewahi kufika
katika banda lake kwa ajili ya
huduma za kuweka na kutoa
pesa.
Lakini sasa akili ikamruka
hakutaka kuamini kuwa yule ni
kama anavyomdhani.
Samahani kaka mambo vipi. U
mwenyeji wa maeneo haya.
Aliuliza kwa sauti tulivu, akiwa
amelitoa koti la suti na kulitupia
begani.
Jose B waukweli anaingia kazini.
Kiasi fulani kwani vipi?.
Hivi yule jamaa aliyevaa kadeti
ndiye Thomas, mdogo wake na
marehemu? alihoji kiujanja Jose
B.
Mngaro wake na mavazi yake
yakamfanya aheshimike.
Yule bwana hakuwa anajua sana
juu ya ile familia. Lakini alimuita
mwenye ukaribu na familia ile.
Jose B akauliza swali lilelile.
Akapatiwa jibu kuwa yule anaitwa
Lameck, ni shemeji wa
marehemu.
Na yule mwanamke
waliyekuwanaye ni kama mtoto
wake. Alijibu hata ambayo
hajaulizwa.
Na hivyo ndivyo Jose B alikuwa
anapenda. Ili ajue mengi.
Kuna jambo hapa!! Si bure.
Aliwazua Jose, huku akijituliza na
kujiuliza inakuwaje amhisi vibaya
yule bwana.
Baada ya ndugu wa karibu
kumaliza kuaga. Wasindikizaji
wengine nao waliaga.
Jose B hakwenda kuaga, akabaki
kumfuatilia Lameck na nyendo
zake.
Mara Lameck akakutana na
kipande cha mtu, kilikuwa
kinampa pole.
Jose B akashtuka, kile kipande
alikuwa anakifahamu vyema.
Aliwahi kukiona maeneo fulani
jijini Dar es salaam.
Ubungo. Zamzam guest house.
Kipande kile cha mtu kilikuja
kumpokea Emmy, kikamuingiza
ndani kisha kikatoka nje.
Sasa ikajengeka picha ya mwisho
ya kumaliza utata kwa Jose B
waukweli mshakunaku wa
kimataifa. Yule aliyebaki ndani
pamoja na Emmy ndiye huyu
anayeitwa baba mdogo.
Jose B akacheka kisha
akamshukuru Mungu kwa
kumbariki na kipaji hicho cha
kipekee.
Kwa hiyo baba na mwana
wanamahusiano ya
kimapenzi....eeh!! Mungu
ameumba dunia na maajabu yake,
ndo maana nikashangaa kivipi
napewa malipo makubwa hivyo.
Kumbe ni baba na mwana. Jose B
akamaliza kwa kicheko kifupi.
Safari ya kuelekea kuzika
ikafuata.
Jose B alikuwa amekuja na gari
ndogo, ilikuwa ngumu kujua
iwapo ni yake ama amekodi,
aliingia katika gari na kumuamuru
dereva aondoe.
Alifungulia mziki wa taratibu kwa
sauti ya chini.
Wakati mziki ukiendelea, Jose B
akaanza kumfikiria upya Emmy,
akajisahaul,isha kuwa
mwanamama huyu kwa sasa yupo
katika machungu makubwa ya
kumpoteza mama yake mpenzi.
Jose B akamuwaza kama
mwanamke ambaye amejaribu
kumtapeli ama wamefanya
biashara isiyokuwa sahihi.
Mimi nilielewana naye kuwa
anipe milioni saba ama nyumba
nikidhani kuwa alikuwa na mtu
wa kawaida tu wakimsaliti James,
lakini kumbe alikuwa na baba
mdogo? Hii biashara kamwe
nisingeweza kuifanya kwa milioni
saba au kinyumba kile, hii ni
hasara tena hasara kubwa tu.
Yaani mtu na baba yake niiuze
kwa milioni saba? Si bora hata
nisingeiuza kabisa. Mtu na baba
yake unadhani mchezo!! Yaani
hapa sikubali kudhulumiwa
kiwepesi wepesi. Lazima haki
itendeke hapa. Aliwaza Jose B
kwa hisia kali sana kama mtu
aliyewekeza mahali kisha
akadhulumiwa pesa yake halali.
Jose B hakuwekeza chochote!! Cha
ajabu analalamika.
Au huyo baba mdogo amsaidie
huu mzigo, kweli ngoja nimtwike
na yeye mzigo wa kulipia hasara
niliyoingia. Alibadili mawazo yake
Jose B, akaugeuzia upepo kwa
Lameck Sulube.
****
Laiti usingekuwa ukakamavu wa
jeshi, huenda Lameck angeweza
kuanguka wakati wa kutupia
mchanga wa mwisho katika
kaburi la Devotha, mama yake
Emmy.
Ama hakika damu ni nzito
kushinda maji.
Lameck kwa mkono wake alikuwa
ameteketeza maadui wengi
waliothubutu kukatiza mbele
yake katika vita huko Sudani.
Wengine aliwalipua vichwani na
wengine aliwapasua matumbo
kwa bunduki. Hayo yote yalikuwa
ya kawaida kwake, iweje kifo cha
mtu huyu kimguse kwa kiasi
hicho.
Alikuwa nyumbani kwake wakati
akiwaza haya.
Lakini ni ubishi wake..
Lameck aliyakumbuka
mazungumzo yake ya mwisho na
mama yake Emmy katika hoteli
iliyopo pembebi kidogo ya jiji.
Mazungumzo nyororo yaliyoishia
pabaya baada ya mada mpya
kuletwa mezani.
Mtu na shemeji yake wakaanza
kulumbana baada ya Lameck
kumgusia mama Emmy kuwa
anampenda mwanaye sana.
Kumpenda halikuwa tatizo,
Lameck akaleta hoja ya nyongeza
kuwa wamewahi kuwa na
mahusiano ya kimapenzi tangu
wakiwa watoto.
Mnaendelea hadi sasa? Devotha
alimuuliza.
Lameck akapinga. Devotha
akashusha pumzi kali.
Lameck akaendelea kuikaribia
maana aliyoitaka.
Akamgusia Devotha kuwa Emmy
ameolewa akiwa si bikra.
Acha upumbavu wewe...mbona
mumewe alileta shukrani ngombe
mbili nyumbani kwa kumkuta
Emmy akiwa mzima na usichana
wake huko Uganda? Alijibu kwa
kebehi kiasi fulani huku taharuki
ikianza kuchukua mkondo.
Lameck akashtuka, hakutegemea
kusikia hayo kutoka kwa yule
mama. Kumbe James alienda
kujisifu. Kujisifu kwa Bikra feki
iliyotengenezwa na daktari
mashuhuri Lameck John Sulube,
kwa kutumia Shabu, Ndimu na
kisha kuiweka makini zaidi
ikawekewa dondoo za sabuni aina
ya KAISIKI. James akadanganyika
na kutoa ngombe mbili.
Au nimpigie James simu hapa
akuumbue?? aliongezea yule
mama Lameck akiwa bado kimya.
Haina maana shemeji kufanya
hivyo Lameck aliweka nidhamu
mbele.
Kumbe ulichoniitia.
Kuna jambo la ziada....
Lipi? aliuliza kisharishari.
Ni kuhusu Emmy na mimi,
nimeamua nianze kujadili na
wewe kiutu uzima kisha
tutamuita Emmy....... kabla
hajaendelea yule mama mweupe
ambaye uso wake ulikuwa
umeanza kuwa mwekundu
kutokana na hasira alimkatisha,
Shem Lameck naomba
tusivunjiane heshima, yaani mimi
wewe na mwanangu tukae
kuzungumzia bikra mara sijui
mlikuwa na mahusiano utotoni,
unamshutumu mwanangu hana
bikra, hiyo bikra uliitoa wewe
mpuuzi mkubwa, na kwa taarifa
yako ni kwamba Emmy ni mama
mtarajiwa, ana kitoto kinaimba
kwa furaha tumboni, sitaki kabisa
umkere mwanangu, nenda
ukapambane na wanajeshi
wenzako huko si mwanangu....jitu
zima hata aibu huna na nitaenda
kumwambia mume
wake....mshenzi wewe....yaani
umekosa wanawake mtaani huko
unakuja kujishebedua kwa mtoto
wako loooh aibu kweli na
nitakushtaki ukiendelea nasema
nitakushtaki Lameck...ukome,
umkome mwanangu mama
alipaza sauti, ikawa kazi ya
Lameck kumsihi mama huyu
asiongee sauti ya juu.
Mara akasimama aweze
kuondoka. Lameck akamdaka
mkono, akaanza kumlaghai kuwa
alikuwa anatania, lakini yule
mama alikubali kinafiki tu kuwa
hawezi kuyafikisha mahali popote
maneno yale.
Lameck kwa kumsoma macho
yake akaugundua unafiki wake.
Lameck alikuwa amechukizwa
sana na maneno makali kutoka
kwa yule mama, hasahasa maneno
ya mwisho ya kumtishia
kumshtaki. Lameck akaongozwa
na hasira, na kwa kujilinda siri ile
isitoke mapema.
Akatumia msemo wa heri mmoja
afe wengi wapone.
Kitendo cha sekunde kadhaa
kutoka kwa mwanajeshi huyu.
Sumu ikaugusa mwili wa mama
Emmy.
Yeye akanawa upesi upesi.
Akarejea nyumbani, taarifa
aliyoitegemea ndiyo ambayo
aliipata kuwa mama Emmy
alikufa akiwa katika gari
iliyokuwa inamrudisha nyumbani
akitokea hotelini. Bila kujulikana
na nini alikuwa anafanya.
Sasa amezikwa tayari na ni usiku
mwingine Lameck anawaza
yaliyotokea.
Lameck ameua.
***LAMECK amemuua DEVOTHA
ili kujilinda
asichafuliwe...amemuua kabla
hajamwambia ni kipi alichomwitia
wajadili.
***JOSE B anapata kitu kipya
kabisa msibani, kumbe LAMECK
na EMMY ni ndugu wa karibu.
Dili jingine!!
***LAMECK anataka nini kwa
EMMY.....na nini hatma ya JOSE B
kumpa mzigo LAMECK aubebe,
kumbuka JOSE B hajui iwapo
LAMECK ni mwanajeshi.Itaendelea