Dk Slaa awaonya CCM kutumia vijana Green Guard
Send to a friend Wednesday, 20 October 2010 09:04 RAIS DK WILBROD SLAA
Dk Willibrod Slaa
Mussa Mkama
MGOMBEA wa urais kwa tiketi ya Chadema, Dk Willibrod Slaa amesema CCM isipoacha kutumia jeshi lake la Green Guard uchaguzi wa mwaka huu hautakuwa huru na haki kwa sababu limekuwa likitumika kuwanyanyasa wanachama wake.
Akizungumza wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika stendi mpya ya mabasi iliyo Kata ya Ikungi, Jimbo la Singida Mashariki, Dk Slaa aliwaomba Green Guard wasiendelee na uchokozi na kuitaka Idara ya Usalama wa Taifa kuacha kumdanganya mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete kwa kuwa baada ya kupiga kura CCM itang'oka madarakani.
"Kwa sasa zimebaki siku 12, damu zimeshamwagika, na zitaendelea kumwagika kwa sababu tayari yeye (Kikwete) ana jeshi linaitwa Green Guard ambalo kazi yake ni kupiga wananchi na wanachama wa Chadema. Huo ni mwanzo wa kukatana mapanga. Sasa kwa hali hiyo kwa nini asiishie mahakama ya kimataifa," alisema.
"Usalama wa taifa acheni kumdanganya mzee huyu kwa kuwa mnaweza kumuua kwa presha... mwaka huu kura hazichakachuliwi, hivyo ajiandae kupumzika kwa amani kama aking'ang'ania madaraka atasababisha matatizo. Ajifunze kwa yaliyotokea Kenya na kwingine kwa sababu ya king'ang'anizi," alisema Dk Slaa.
Awali kabla ya Dk Slaa kuhutubia mkutano wa kampeni Kata ya Ikungi kulikuwa na mwingiliano kati ya Chadema na CCM ambao walidai kuwa walikuwa wakimsubiri katibu mkuu wa chama chao, Yusuf Makamba kwa ajili ya mkutano wa ndani ambao ungefanyika kwenye uwanja ambao Dk Slaa alikuwa na mkutano.
Wakati Dk Slaa akisema hayo, mkoani Arusha gari moja lilivamia mkutano wa kampeni wa mgombea ubunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na kuanza kugawa nguo na kofia zenye nembo ya CCM kabla ya watu hao kukamatwa na kupelekwa polisi.
Waandishi wetu, Moses Mashalla na Musa Juma wanaripoti kuwa gari linalosadikiwa kuwa la serikali lilikamatwa jana jioni na wafuasi wa Chadema kwa madai ya kuvamia mkutano wao wa kampeni kwenye Kata ya Mateves.
Inadaiwa kuwa watu waliokuwa kwenye gari hilo walikuwa wakigawa fedha, kanga, fulana na kofia zenye nembo na rangi ya CCM.
Tukio lilitokea jana majira ya saa 11:00 za jioni wakati mgombea ubunge wa Jimbo la Arusha Mjini kwa tiketi ya Chadema, Godbless Lema alipokuwa akiwandadi wagombea udiwani kwenye kata za Manispaa ya Arusha.
Gari hilo lenye nambari za usajili T 856 ACY aina Toyota Land Cruiser VX halikuwa na nyaraka muhimu zinazohitajika kwa ajili usalama barabarani na utambuzi na pia lilikuwa na namba TZS 4930 katika vioo vyake
Tayari polisi inawashikilia watu wawili akiwemo dereva wa gari hilo na mwanamke mmoja ambao hata hivyo majina yao hayakufahamika mara moja, huku viongozi kadhaa wa CCM wa wilaya ya Arusha walionekana katika harakati za kujaribu kutafuta ufumbuzi wa suala hilo.
Akizungumza na Mwananchi, Lema alieleza kuwa wakati akiendelea kujinadi jukwaani na kuwanadi wagombea wake, ghafla gari hilo liliegeshwa pembeni mwa eneo la mkutano na mwanamke mmoja alishuka na kuanza kugawa kanga na fulana za CCM pamoja na Sh5,000 kwa kila aliyepokea.
Hali iliwafanya watu waliokuwepo kupoteza umakini wa kusikiliza mkutano wetu na ndipo vijana wetu walipowazuia na kuanza kuwahoji sababu za kuvamia mkutano na kugawa fedha kinyume na sheria za uchaguzi, alisema.
"Tuliwabana na kuwahoji lakini dereva alijitetea kuwa yeye ameagizwa tu na wakati huo wengine waliokuwepo walikimbia baada ya kuona kuwa wananchi wameanza kuhamaki na sisi tuliamua kubanana nao hadi tulipowaleta polisi, alisema Lema.
Kamanda wa polisi mkoani hapa, Basilio Matei alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa polisi wanalipekua gari hilo chini ya usimamizi wa mkuu wa upelelezi mkoa, Leonard Paul.
Ni kweli kuna tukio, lakini ni mapema kueleza gari hilo linamilikiwa na nani... mkuu wa upelelezi wa mkoa anasimamia zoezi la kukagua vitu vilivyo ndani ya gari hilo na mbele ya viongozi wa vyama vyote ili kuondoa utata, alisema Matei.
Akihutubia mkutano wa kampeni kwenye stendi ya zamani Singida, Dk Slaa alisema kuwa wananchi wa mkoa huo wamegeuza bendera za CCM kama Mungu wao wakati wamejaa umasikini na kujaa woga waliopandikizwa na serikali ya chama hicho kwa kuwatisha kuwa bila kuweka bendera hizo hawatafanya biashara.
Alisema hakuna kitu kibaya duniani kama umasikini wa fikra, ni nafuu umasikini wa fedha kuliko wa fikra, kwa sababu ni vigumu kumkomboa mwananchi mwenye fikra hizo na akili, labda abadilike.
Akihutubia maelfu ya watu huku akitokwa na machozi, Dk Slaa alisema maisha ya Singida yanafanana kwa kuwa hayana tofauti; yamejaa umasikini wa kupindukia; hawana huduma za afya wala za jamii, lakini ofisi za kata za CCM nzuri.
Alisema miaka zaidi ya 48 bado wananchi wa Singida wanaiabudu CCM, wanashindwa kutambua hali hiyo imesababishwa na nini na serikali gani na kwa sababu gani.
"Chadema tunahitaji wananchi wote waishi maisha ya hadhi ya ubinadamu, ambayo kimsingi ni dira ya taifa. Ili kufanya hivyo tutapunguza bei ya simenti na bati ambavyo vyote hivyo kila kimoja kitauzwa kwa Sh5,000/ ili mwananchi ajenge nyumba nzuri na aishi maisha bora," alisema Dk Slaa.
Naye, mgombea ubunge wa jimbo la Singida Mashariki, Tundu Lisu aliwataadharisha wananchi kuwa makini kwenye uchaguzi na kuwataka wasiichague CCM kwa kuwa haina mchango wa haki kwa wananchi na nchi kwa ujumla.
Lisu alisema kama wananchi wanataka kuendelea na uchafu unaofanywa na CCM, basi waichague na kama wanataka kuepukana nao, basi watumie nafasi hii ya kupiga kura kuutokomeza kwa kuichagua Chadema.