Dunia haina usawa

Dunia haina usawa

DUNIA HAINA USAWA

Godwin alikuwa akiendelea kusoma kama kawaida, kichwa chake kilikuwa na mawazo mengi, alikuwa akifikiria namna ambavyo angeweza kuwawekea chuki kubwa wananchi juu ya viongozi wao waliokuwa wakiwaibia fedha wananchi wao na hata kuwakandamiza masikini.
Hakuacha kudukua mawasiliano yao, kila wakati alikuwa akicheza na kompyuta yake, alijua fika kwamba watu hao walikuwa wakiwasiliana, katika kila meseji walizokuwa wakitumiana wabunge wote nchini Tanzania, alizipata kwani alikuwa ameingiakatika namba zao bila kujua.
Ukiachana na hao, pia kulikuwa na watu wa usalama wa taifa ambao aliamini kwamba kama angefanikiwa kuwa na mawasiliano yao na kufuatilia kila kitu basi angefanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Bado aliendelea kukusanya namba za watu mbalimbali, wale waliokuwa na sauti nchini Tanzania. Alifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana na ndiyo maana hata kikao kidogo cha watu sita ambacho kiliitishwa ikulu, naye alipata taarifa kwani kila walipopigiana au kutumiana meseji, alikuwa akipata taarifa hizo.
Alishangaa kuona watu hao walikusanyika kwa kuwa walitakiwa kuandika majina ya watu hamsini. Hakujua katika karatasi hizo waliandikwa wakina nani lakini baada ya mkurugenzi wa usalama wa taifa kupigiwa simu na kuambiwa kwamba walitakiwa kufanya mauaji ya watu waliokuwa nao mule ndani, tena kwa kuwataja majina ndiyo akagundua kwamba tatizo kubwa ni kwa sababu aliweka kila kitu kilichozungumziwa katika kikao kile hasa baada ya kudukua mawasiliano ya simu yaliyofanyika baada ya kikao.
Alijua kwamba kulikuwa na mtu mmoja miongoni mwa watu waliokuwa katika kikao kile alikuwa akienda kuuawa, hakujua ni nani na hivyo macho na masikio yake yalikuwa kwenye simu yake ambayo muda wote kazi kubwa ilikuwa ni kudukua mawasiliano ya viongozi hao.
Hapo ndipo akagundua kwamba mtu aliyekuwa akitakiwa kuuawa alikuwa Mzee Filipo, hakuamini macho yake kwani miongoni mwa watu waliokuwa wakiheshimika katika chama tawala alikuwa mtu huyo.
Hakutaka kuzungumza kitu, alitaka kuona kama mauaji hayo yangefanyika au la. Kile alichokuwa akikitegemea ndicho kilichofanyika kwani mzee huyo alikufa katika ajali ambayo mara baada ya kuifuatilia, akapata maswali kadhaa ambayo aliyaandika kwenye akaunti yake Instagram.
Alishangaa, hakuamini kwamba yeye ndiye alikuwa sababu kubwa iliyomfanya mzee huyo kuuawa, hakutaka kuona mauaji yakiendelea, alichokifanya ni kuposti kuhusu mauaji hayo, Watanzania wajue kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Wakati yeye akitafakari hayo yote upande wa pili Kimwinyi alionekana kuchanganyikiwa, pombe zote alizokuwa amekunywa ziliyeyuka kichwani mwake, ulevi wote ukamuondoka, akaegemea usukani na kuanza kuyafikiria maisha yake.
Alishirikiana na rais kwa kila kitu, walicheza michezo mingi ya mauaji lakini kipindi hicho mambo yalionekana kuwabadilikia, walidili na mtu ambaye hawakujua alikuwa wapi ingawa aliamini kwamba alikuwa na nguvu kubwa.
Mara baada ya kujifikiria kwa muda huku akiwa ndani ya gari, akampigia simu Rais Bokasa na kumwambia kilichokuwa kikiendelea, kwamba alipigiwa simu na mtu asiyemfahamu na kumwambia kwamba alikuwa akijua mchezo mzima na lazima afanye juu chini kuhakikisha majina yao anayaweka katika akaunti ile.
Hilo ndilo lililomchanganya zaidi, pamoja na uovu wake mkubwa lakini hakutaka kugundulika na mtu yeyote yule, kila siku alijifanya mtu mwema, aliwasaidia watu, kitendo cha mtu huyo kusema kwamba angeweka kila kitu hadharani kilimchanganya mno.
“Kwa hiyo tufanye nini Kimwinyi?” aliuliza rais.
“Sijajua! Hii hali inanichanganya sana. Nani anamwambia huyu mtu mambo haya?” aliuliza Kimwinyi.
“Hilo ndilo la msingi kujiuliza. Ila aliponipigia simu, kulikuwa na namba aliyotumia, nadhani tukiitumia hii, tutafanikiwa kumpata,” alisema mwanaume huyo.
“Unayo?”
“Ndiyo!”
“Hebu tuanze kuifuatilia.”
Hilo ndilo lililofanyika, siku iliyofuata Kimwinyi akaondoka kwenda makao makuu ya Mtandao wa Simu wa Tritel ambapo baada ya kufika huko akawapa namba ile iliyotumika kumpigia huku dhumuni lake likiwa ni kujua mahali namba hiyo ilipokuwa mara ya mwisho ilipokuwa ikitumika.
“Hii ndiyo namba yenyewe?” aliuliza dada aliyekaa kwenye meza iliyokuwa na kompyuta.
“Ndiyo!”
Akaanza kuifanyia kazi, akaiangalia kwenye kompyuta yake, muda wote alikuwa kimya, aliikodolea macho kompyuta yake huku Kimwinyi akiwa mbele yake akimwangalia tu.
Msichana yule alihangaika kwa dakika kumi nzima, hakufanikiwa, akaichukua laini ile na kumpatia Kimwinyi ambaye alikuwa na hamu ya kusikia mahali ilipokuwa.
“Hiyo namba bado haijaanza kutumika,” alisema msichana huyo.
“Haijaanza kutumika?”
“Ndiyo! Yaani kwa kifupi bado hatujatengeneza namba ya namna hiyo,” alisema msichana huyo huku akimwangalia Kimwinyi.
“Yaani sijakuelewa. Umesemaje?”
“Tuna namba ambazo tunazitengeneza. Namba zinazoanzia 8 bado hazijaanza kutengenezwa, zipo zinazoanzia na 6 ambazo ndizo tulizofikia,” alisema msichana huyo.
“Kwa hiyo hii namba haipo?”
“Ndiyo!”
“Sasa aliyenipigia mbona ndiyo kaitumia hii?” aliuliza.
“Hebu niione!”
Kimwinyi akampatia simu yake msichana yule ambaye aliiangalia ile namba, kweli ilitumika. Yeye mwenyewe hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, kwa nini namba ile itumike na wakati haikuwa imetengenezwa kwa matumizi.
Kila mtu aliyeulizwa humo, hakujua, vijana wa IT nao walishangaa. Mpaka Kimwinyi akaondoka baada ya kutumia saa mbili makao makuu hapo hakuwa amepata jibu la maswali yake juu ya namba ile.
“Kwa hiyo haipo?”
“Ndiyo mkuu!”
Wakati wao wakijiuliza kuhusu namba, upande wa pili Watanzania walikuwa wakijiuliza kuhusu mauaji ya Mzee Filipo, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mpaka muda huo. Walitaka kusikia taarifa kutoka ikulu juu ya kile kilichokuwa kikiendelea nchini.
“Kumbe Mzee Filipo aliuawa?” aliuliza jamaa mmoja.
“Mmh! Wewe umepata wapi taarifa?”
“Ingia Instagram uone kwenye akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ilivyoadikwa,” alijibu jamaa aliyeulizwa swali.
Jamaa huyo alipoingia, kila alichoambiwa ndicho alichokiona, hakuamini macho yake, si yeye tu bali kila mtu aliyeingia na kusoma katika akaunti ile hakuamini kama Mzee Filipo alikuwa ameuawa.
Kulikuwa na maswali ambayo yaliambatana na picha ile iliyowekwa, maswali hayo ndiyo yaliyozua gumzo kubwa hasa la jamaa ambaye alisema kwamba alikuwa mwanakijiji wa kijiji kilichotokea ajali na wakati hakuwa akijulikana na mtu yeyote hapo.
Jinsi maswali yale yaliyoulizwa yalivyokuwa, kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba Mzee Filipo alikuwa ameuawa na kisha ajali ile kutengenezwa ili ionekane kwamba alipata ajali mbaya na kufa.
Vichwani mwa watu wengi walikuwa na hamu ya kujua ni mtu gani alikuwa amehusika katika mauaji hayo. Waliambiwa kwenye akaunti ile kwamba hatimaye mtu aliyehusika angewekwa hadharani lakini pia waliambiwa kwamba kulikuwa na kikao cha watu sita kilichowekwa, kilikuwa kikao muhimu cha kummaliza mtu aliyekuwa na akaunti hiyo, hawakumfahamu, walikuwa wakicheza mchazo wa kubahatisha tu.
“Mimi ninataka kuwajua hao watu waliokuwa kwenye hicho kikao. Ni nani na nani sasa?” aliuliza msichana mmoja aliyekuwa akisoma posti katika akaunti hiyo.
Hilo ndilo lilikuwa hitaji la watu wengi, kila mmoja alitaka kuona majina ya watu waliokuwa kwenye kikao hicho na pia walitaka kujua watu wawili waliokuwa wamepanga mpango wa kumuua Mzee Filipo, tatizo lilikuwa nini na wakati kila mtu ndani ya chama alikuwa akimpenda mzee huyo?
Wakati watu wakihitaji majibu ya maswali yote waliyokuwa wakijiuliza, Rais Bokasa alikuwa na hofu tele, kwa kile kilichokuwa kikiendelea kilimchanganya kichwa chake.
Alitaka kuwaua watu wanne ambao aliamini kwamba kwa namna moja au nyingine mmoja kati ya ndiye aliyekuwa akihusika katika kumiliki akaunti hiyo lakini kitu cha ajabu kabisa, hata alipokaa na Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Bwana Kimwinyi watu walijua kile kilichokuwa kimezungumziwa, mipango yao mpaka jinsi mauaji hayo yalivyotakiwa kufanyika.
“Sasa huyu atakuwa nani? Au Kimwinyi mwenyewe? Kama tulipanga mipango wawili tu, mimi na yeye halafu kesho huyu mtu wa mtandao anajua, nani kamwambia kama si yeye? Nina wasiwasi naye, atakuwa anahusika huyu,” alijiuliza Rais Kimwinyi huku akionekana kuchanganyikiwa.
Kama walikuwa wawili tu, wakapanga dili na baadaye kubumbulika, akawa na uhakika kwamba Kimwinyi alikuwa akihusika na akaunti ile na kama si yeye basi alikuwa akimpa mtu huyo kila kitu kilichokuwa kikiendelea, ili aendelee kuwa salama ilikuwa ni lazima amuue huyo Kimwinyi kwani tayari alikuwa na wasiwasi naye kupita kawaida.
Katika harakati za kumuua Kimwinyi hakutaka kumshirikisha mtu yeyote yule, alitaka kila kitu kiwe siri kubwa na kusiwe na mtu yeyote ambaye alitakiwa kufahamu kilichokuwa kikiendelea.
“Ni lazima nimtume aende Nigeria, akifika huko niwasiliane na Boko Haram wamuue,” aliwaza Rais Bokasa, mbinu hiyo ndiyo aliyotaka kuitumia, ilikuwa ni lazima amuue mwanaume huyo ambaye aliamini ndiye aliyemsaidia mtu mwenye akaunti ile Instagram kupata taarifa ya kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
***
Rais Bokasa hakutaka kukubali, alihisi kabisa kwamba Kimwinyi ndiye alikuwa adui yake namba moja, hakutaka kuona mwanaume huyo akiendelea kuvuta pumzi ya dunia hii, kile alichokitaka ni kumuua kisiri kwa kuamini kwamba baada ya kufanya mauaji hayo basi angekuwa salama kabisa.
Usiku mzima alikuwa na mawazo tele, aliwasiliana na mkuu wa kundi la Boko Haram lililokuwa Afrika Magharibi hasa nchini Nigeria, akamwambia kwamba alikuwa na kazi ambayo ilitakiwa kufanyika haraka sana, kulikuwa na mtu ambaye alitakiwa kuuawa.
Hilo hakukuwa na tatizo kwa Boko Haram, kwa kuwa kundi hilo lilihitaji sana pesa kwa ajili ya kujiendeleza, kazi ambayo waliambiwa kwamba waifanye haikuwa na tatizo lolote lile, wakapanga tarehe, akawatumia picha na kuwapa ratiba kamili ambayo Kimwinyi alikuwa akiondoka Tanzania na kufika nchini Nigeria.
Rais Bokasa akampigia simu Kimwinyi na kumpa taarifa kwamba alitakiwa kuelekea nchini humo kwa ajili ya kuzungumza na baadhi ya viongozi wa huko kuhusu kuidhibiti akaunti mtandaoni ambayo ilikuwa ikisumbua, alimwambia kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa akimwamini katika serikali yake zaidi ya huyo Kimwinyi maneno ambayo yalimfurahisha pasipo kujua kulikuwa na mpango kabambe wa kummaliza hata kabla hajafika hotelini.
“Nashukuru sana kwa kuniamini!” alisema Kimwinyi.
“Haina shida. Wewe nenda Nigeria kisiri na kila kitu tutazungumza ukifika huko,” alisema rais.
“Sawa.”
Wakati wakizungumza hayo mchana siku ya Ijumaa, kwa nchini Japan tayari ilikuwa ni asubuhi ya Siku ya Jumamosi asubuhi. Godwin alikuwa darasani akijisomea, mara akaona kompyuta yake ikimwambia kwamba kulikuwa na mawasiliano yalikuwa yakifanyika kutoka katika namba ya Rais Bokasa aliyokuwa ameidukua.
Haraka sana akachukua ‘hearphone’ zake, akazichomeka na kuanza kusikiliza mawasiliano yao. Simu ilikuwa imetoka kwa rais huyo na kwenda kwa Mkurugenzi wa Usalama wa taifa, Kimwinyi, aliyasikiliza mazungumzo yote na kitu kilichomjia kwa haraka mno kichwani mwake kilikuwa ni mauaji tu.
Alijua kwamba rais huyo alikuwa akijitahidi kufanya kila kitu kuona akaunti ya Mabadiliko ya Kweli inafutika, na kwa sababu alikuwa amemtuma Kimwinyi kumuua Mzee Filipo, basi alitaka kuificha siri hiyo hivyo kumuua Kimwinyi.
Saa moja baada ya kuyasikia mazungumzo hayo, Godwin akaingia kwenye akaunti yake na kuweka picha ya Tanzania kisha kuandika R.I.P na chini kuweka maneno machache yaliyosomeka ‘Kuna mtu anakwenda kufa, hatokufa Tanzania, atakufa mbali kabisa ila ni mchezo ambao umechezwa na mtu fulani. Unataka kujua ni nani? Endelea kusubiri tu!’.
Alipomaliza, akaiposti. Kila mtu aliyeiona posti hiyo alishtuka, walimwamini mtu aliyekuwa akiitumia akaunti hiyo, waliamini kwamba kulikuwa na mtu alikuwa akienda kufa na watu wengi wakauliza alikuwa nani lakini hakukuwa na aliyekuwa na majibu ya maswali yao.
Kimwinyi hakuwa akijua lolote lile, alipoambiwa hivyo, ndani ya saa moja akapanda ndege na kuanza kuondoka nchini Tanzania huku akiambiwa kwamba hapo uwanja wa ndege angepokelewa na mkurugenzi wa Usalama wa Taifa wa huko, The National Intelligence Agency (NIA), Bwana Andrew Okafor.
Njia nzima alikuwa na mawazo tele, kama alivyokuwa amechanganyikiwa rais naye alichanganyikiwa hivyohivyo. Muda mwingi alikuwa akiongea peke yake, kichwa chake hakikuwa sawa hata kidogo.
Safari hiyo ilichukua saa kadhaa ndipo ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Murtala Muhammed uliokuwa jijini Lagos. Haraka sana baada ya ndege kusimama, abiria wakaanza kuteremka akiwemo yeye mwenyewe.
Mzigo wake ulipochunguzwa na kuuchukua akaanza kutoka ndani ya jengo hilo ambapo nje akakutana na mwanaume mmoja ambaye alikuwa akimwangalia sana, kwa muonekano wake tu ulionyesha ni ofisa wa usalama wa taifa kitu kilichomfanya kumsogelea.
“My name is Jonas Ogwadugu! I was told to come and pick you up,” (naitwa Jonas Ogwadugu! Niliambiwa nije kukuchukua) alisema mwanaume huyo huku akiwa na tabasamu pana.
“Ooh! Thank you! My name is Kimwinyi! How do you find me?” (Ooh! Asante! Naitwa Kimwinyi! Umenipataje?) aliuliza huku naye akitoa tabasamu.
“I got your picture,” (nina picha yako)
Akamchukua na kuelekea naye katika gari moja la kifahari. Kwa jinsi mapokezi yalivyokuwa, muonekano wa gari ulionyesha kabisa mtu huyo alikuwa ni kutoka katika usalama wa taifa wa Nigeria. Gari likawashwa na dereva wa gari hilo na kuondoka mahali hapo.
Njiani walikuwa wakizungumza mambo mengi, Jonas alionekana kuwa mchangamfu kupita kawaida. Kila wakati uso wake ulikuwa kwenye tabasamu pana na alipokuwa akiongea alionekana kama mtu aliyekuwa na akili kubwa mno.
Alimwambia Kimwinyi jinsi walivyokuwa wakifanya kazi, walikuwa na kikosi hatari sana ambacho kilipambana juu chini kuhakikisha nchi inalindwa kwa ngumu kubwa kuliko kitu chochote kile.
Hakumficha, alimwambia jinsi walivyoguswa kwa kuambiwa kwamba kulikuwa na akaunti ambayo ilikuwa ikiwasumbua. Wao, Nigeria walipita huko zamani, kulikuwa na wataalamu wa kompyuta mitaani, wote baadaye wakaajiliwa serikalini, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo mkubwa ambaye alikuwa nje ya serikali ila pamoja na hayo, wangemwambia ni jinsi gani wataweza kuizuia akaunti hiyo.
“Nitafurahi sana! Hakika imetusumbua sana,” alisema Kimwinyi huku akijisikia amani kabisa kana kwamba alipokelewa kupelekwa harusini.
Safari iliendelea, kile alichokitarajia kwamba hotelini alipotakiwa kwenda palikuwa karibuni kilikuwa tofauti na mategemeo yake, gari liliendeshwa kwa mwendo wa kawaida, wakaanza kutoka katika Jiji la Lagos na kuanza kwenda katika Jiji la Ibadan.
Alishangaa, alitamani kuuliza lakini akahisi kama kuingilia jukumu la watu hao hivyo kukaa kimya. Gari lilikwenda mpaka likaacha barabara ya lami na kuanza kuingia kwenye barabara ya vumbi, walikwenda kwa dakika zaidi ya ishirini, gari likasimama nje ya jumba moja kuukuu na kuambiwa kuteremka.
“Tumefika?” aliuliza lakini Okafor hakujibu chochote kile, akateremka kutoka garini.
Hata kabla Kimwinyi hajajua nini kilikuwa kikiendelea mahali hapo, wanaume sita waliokuwa na bunduki aina ya AK47 wakatokea mahali hapo, alishtuka, hakujua kitu chochote kile, akaamliwa kuteremka kutoka garini huku mikono yake ikiwa kichwani, akafanya hivyo huku akitetemeka mno.
“Nimefanya nini jamani?” aliuliza huku akitetemeka.
“Utamuuliza rais wako!”
“Rais wangu? Bokasa ndiye aliyewat...” aliuliza lakini hata kabla hajamalizia swali lake, akapigwa na kitako cha bunduki, akapoteza fahamu, wakamchukua na kuondoka naye.
****
Godwin alikuwa akiandaa ripoti yake ndefu, alitaka kuwaambia Watanzania kila kitu kilichokuwa kikiendelea, tangu mwanzo wa kikao chao mpaka hapo walipofikia, hakutaka kuficha kitu chochote kile, katika ripoti ile aliweka bayana hata ile mipango ambayo ilitakiwa kufanywa baada ya Kimwinyi kuuawa.
Ilikuwa ripoti ndefu na yenye kusisimua sana, aliamini kila Mtanzania ambaye angekwenda kuisoma ilikuwa ni lazima kumchukua rais huyo ambaye alijitahidi kuwaangamiza watu ili mambo yake machafu yasiendelee kutolewa.
Alimini kwamba kwa watu milioni ishirini ambao waliifolo akaunti yake wangeweza kubadilisha kila kitu, aliamini kwamba wengi waliokuwa wamemfolo walikuwa watu wake, waliunga kile alichokuwa akikifanya.
“Ila kweli rais ana mpango wa kumuua Kimwinyi au? Nisije kuonekana muongo!” alijiuliza Godwin, kila wakati macho yake yalikuwa kwenye mitandao mbalimbali nchini Nigeria kuona kama kweli Kimwinyi alikuwa ameuawa kama alivyohisi au la.
Saa ziliendelea kukatika, bado macho na masikio yake yalikuwa yakisikilizia kile kilichokuwa kikiendelea nchini Nigeria. Ilipofika majira ya saa kumi jioni siku ya Jumapili, taarifa aliyokuwa akiisubiri kwa hamu kubwa ikatangazwa.
Mtanzania mmoja alikutwa akiwa ameuawa na mwili wake kutupwa msituni. Japokuwa ilionekana kuwa habari mbaya lakini kwa Godwin ilimfanya kutabasamu sana. Hapohapo akaichukua na kuiweka katika mtandao wake na kuwakumbusha watu kwamba jana yake usiku kwa majira ya Afrika aliandika kwamba kungekuwa na mauaji ambayo yangekwenda kutokea nje ya Tanzania na hatimaye yalikuwa yametokea.
Kila mtu alishangaa, hawakujua ni kwa namna gani mtu huyo aliweza kupata mambo yote hayo. Ni kweli mkurugenzi wa usalama wa taifa alikuwa ameuawa nchini Nigeria ambapo taarifa zilisema kwamba alitekwa na Boko Haram kimakosa kwa kufikiri kwamba alikuwa Mganda, Oseah Mambo waliyekuwa wakimtafuta kwa kipindi kirefu.
“Huu ni mpango na si kwamba walimchanganya! Walijua kwamba walikuwa wakienda kumuua mkurugenzi wa usalama wa taifa, hivyo mnaposikia kwamba walimteka na kumuua kimakosa ni uongo, nitakuwekeeni ripoti kamili ya mambo yote haya” aliandika Godwin katika akaunti yake.
Watanzania wengi wakahisi kama akaunti hiyo ilikuwa ikiendeshwa na malaika kwani mtu huyo alikuwa alikuwa akijua mambo mengi sana, hata kama kulikuwa na mpango mliokuwa mkiufanya chumbani, kesho yake alikuwa akijua kila kitu.
Wengi wakamsifu lakini pia wakatamani kuiona ripoti hiyo ambayo ingezungumzia mambo mengi mno. Mitaani, kila mtu alikuwa akizungumza lake lakini wengi wakabaki na ukweli kwamba Kimwinyi aliyeuawa na Boko Haram ulikuwa ni mpango na si kutekwa kimakosa.
“Nitarudi Tanzania wiki hiihii ndani ya siku tatu! Nikija, nitahakikisha nawapeni mambo mengi zaidi,” aliandika Godwin ambapo watu wengi wakakomenti kwa kumkaribisha kwani hawakuona kama kungekuwa na mtu mwingine wa kuikomboa Tanzania zaidi yake.
“Karibu sana mkombozi wetu,” alikomenti jamaa mmoja. Godwin akajiandaa kurudi nchini Tanzania.
***
Mara baada ya taarifa za kifo cha Kimwinyi kusambazwa katika mitandao mbalimbali, Rais Bokasa akapigiwa simu na rais wa Nigeria na kuambiwa kilichokuwa kimetokea. kwanza akajifanya kushtuka kwa kutokuamini kile kilichokuwa kimetokea. Aliulizwa kama alimruhusu mtu huyo kuelekea nchini Nigeria lakini akakataa katakataka.
Alitaka kujisafisha, alijua fika kwamba kungekuwa na taarifa nyingi ambazo zingeandikwa kuhusu mauaji hayo, alitaka kuyazima mapema hata kabla mitandao ya kijamii haijaweka wazi hisia zao kwa kuhisi kwamba mtu huyo alikuwa ameuawa kimakusudi.
Hakutaka kuchelewa, hapohapo akachukua simu yake na kumpigia mkurugenzi wa televisheni ya taifa ambaye alimwambia kwamba alihitaji waandishi wa habari kwani kulikuwa na mambo aliyotaka kuzungumza.
Hilo halikuwa tatizo, baada ya dakika kadhaa, waandishi hao wakawa ikulu ambapo wakaanza kurusha matangazo moja kwa moja. Hakutaka kujificha, aliwaambia watu hao namna Kimwinyi alivyoondoka, alijifanya kuwasiliana na mawaziri wengine kutaka kujua sababu ya Kimwinyi kuelekea nchini Nigeria lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa na majibu.
“Nilishangaa kupigiwa simu na rais wa Nigeria na kuambiwa kuwa Kimwinyi alitekwa. Alikwenda Nigeria kufanya nini? Nani alimruhusu? Haya ni maswali ambayo nimekosa maj...” alisema lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, akaanza kulia.
Huo ndiyo ulikuwa ujanja wa kwanza kabisa alioufanya. Hakutaka kugundulika, alihisi kitendo cha kutoa machozi mbele ya waandishi wa habari kingemfanya kila mtu kuamini kile alichokisema, hilo ndilo lilivyokuwa kwani baadhi ya wananchi waliokuwa wakimwangalia katika televisheni hiyo waliamini kwamba hakuwa amefanya jambo hilo.
“Mpaka rais analia! Ameguswa sana jamani halafu kuna mpuuzi mmoja kwenye mtandao kajiunga na kibando chake cha wiki anamchafua rais wetu kwamba kahusika na mauaji hayo. Hivi kweli aliyehusika anaweza kulia?” alihoji jamaa mmoja aliyekuwa akiuza duka.
“Kwani kulia tatizo bwana?” aliuliza jamaa mwingine.
“Unadhani chozi la mwanaume linatoka hivihivi!”
“Mbona wengi wanalia bwana! Tena si kulia, wengine wamefiwa na bado wanacheka msibani,” alisema jamaa mwingine.
Ili kuonyesha kwamba alikuwa ameguswa na msiba huo, Rais Bokasa alikuwa bega kwa bega na familia ya Kimwinyi, alikuwa akijitolea kwa kila hali ili isionekane kama yeye ndiye aliyehusika katika mauaji hayo.
Kulikuwa na misiba mingi iliyokuwa imetokea lakini kwa msiba huo, rais huyo alijitoa kwa nguvu zote kiasi kwamba akaanza kuwalaghai Watanzania kwamba hakuwa amehusika katika mauaji hayo. Wakati akiwa msibani, akasikia simu yake ikiita, haraka sana akaichukua kutoka mfukoni na kuipeleka sikioni.
“Kuna nini?” aliuliza.
“Kumbe yule mtu wa ile akaunti hayupo Tanzania! Nimeona posti yake, amesema kwamba atakuja Tanzania ndani ya siku mbili tatu,” alisema mwanaume huyo.
“Hakikisheni mnaweka usalama wa kutosha katika uwanja wa ndege na mipakani, hakikisheni mnampata huyu mtu,” alisema Rais.
“Sawa.”
Akakata simu. Kichwa chake kilichanganyikiwa zaidi, alitamani kuondoka msibani hapo, hakukuwa na kitu alichokitaka kama kumfahamu mtu aliyekuwa nyuma ya akaunti ile iliyokuwa ikimuumiza kichwa chake. Hakutaka kukaa sana msibani, akaondoka na kuelekea ikulu.
Njiani, alikuwa na mawazo tele, aliongea peke yake, hakuonekana kuwa na raha hata mara moja na mpaka anafika ikulu alihisi kabisa kichwa chake kuwa kziito mno, hivyo akajilaza.
Aliamka majira ya saa tatu usiku, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuchukua simu yake na kumpigia mwanaume aliyempigia kabla na kumpa taarifa kwamba mtu aliyekuwa akitumia akaunti ile angefika nchini Tanzania ndani ya siku mbili tatu, alitaka kujua waliishia wap, alitaka kufahamu kila kitu.
“Mmefikia wapi?”
“Ulinzi umewekwa kila kona mkuu! Kila Mtanzania anayefika ni lazima kuchunguzwa sana!” alijibu mwanaume wa upande wa pili.
“Basi sawa. Ngoja niwaambie kitu kimoja. Mkiwakagua hakikisheni mnawaambia waingie kwenye akaunti zao za Instagram, wasijitoe, hakikisheni mnaangalia akaunti inayotumika ni ipi. Sawa?” alisema na kuuliza.
“Sawa mkuu!”
Hicho ndicho walichokifanya. Polisi na wanausalama wa taifa wakaambiwa kile kilichotakiwa kufanywa. Kila mtu aliyekuwa akiingia nchini Tanzania kupitia mipakani au uwanja wa ndege ilikuwa ni lazima kuchunguzwa yeye kama yeye na pia kuambiwa kufungua akaunti yake ya Instagram kwa ajili ya kuangalia kama wangekuwa watumiaji wa akaunti ya Mabadiliko ya Kweli.
Ilikuwa kazi kubwa lakini ilikuwa ni lazima kufanyika. Kila mtu alikuwa akishangaa, hawakujua sababu ya polisi na wanausalama kufanya kitu kama hicho.
Wakati hali hiyo ikiendelea, Godwin hakuwa akijua lolote lile. Alipanga kurudi nchini Tanzania kwani alisoma na kupata PhD yake katika masuala ya kompyuta. Hakutaka kubaki nchini Japana, akashukuru kwa Mzee Takesh na kurudi nchini Tanzania.
Njiani alikuwa akifikiria kile alichotakiwa kufanya, hakukubali kuona Tanzania ikiendeshwa na rais mmoja kwa miaka mingi, alitaka kubadilisha kila kitu, kama Bokasa aliiongoza Tanzania kwa miaka mingi kwa kuwa tu alibadilisha baadhi ya vipengele kwenye katiba, sasa ulikuwa muda wake kung’oka.
“Habari yako!” alisikia sauti ya msichana mmoja ikimsalimia.
“Salama! Za kwako!”
“Njema tu! Na wewe umetoka Dubai?” aliuliza msichana huyo kwa sauti nyembamba, alionekana kuwa mchangamfu mno.
“Hapana! Nimetoka Uholanzi!”
“Ulikuwa masomoni?”
“Yeah! Jiji Amsterdam!”
“Ooh! Naitwa Manka Msuya!” alisema msichana huo huku akimpa mkono.
“Naitwa Godwin Jr!”
Japokuwa ilikuwa ni mara ya kwanza kukutana lakini kila mmoja alionekana kuwa mchangamfu sana. Walikuwa katika kiti kimoja huku ndege ikiendelea kukata mawingu kuelekea nchini Tanzania. Walizungumza mengi, msichana huyo alionekana kuwa mkweli kwa kila kitu alichokuwa akikizungumza lakini kwa Godwin, hakukuwa hata na kitu kimoja cha kweli alichomwambia Manka.
Baada ya saa kadhaa, ndege ikatua katika Uwanja wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi nchini Kenya. Hawakuteremka, walibaki ndani ya ndege ambapo baada ya muda fulani ikapaa tena na kuelekea nchini Tanzania.
Wote walichoka lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa ladhi kulala kwani kwa jinsi stori zilivyonoga, hakukuwa na yeyote aliyekuwa tayari kumuacha mwenzake na yeye kulala.
Baada ya saa chache wakaingia jijini Dar es Salaam ambapo ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Huku wakiwa pamoja kama mke na mume, wakateremka na kuelekea nje ya ndege ambapo wao na abiria wengine wakaunganisha mpaka katika jengo la uwanja huo.
“Mnatakiwa muende kule,” alisema dada mmoja huku akiwaangalia wawili hao.
“Kufanya nini?”
“Ni maagizo ambayo tumeachiwa! Hatujui kufanya nini!” alijibu dada huyo.
“Ni sisi tu?”
“Hapana! Hata wengine pia!”
“Sasa mbona Wazungu wanasepa zao?”
“Ni kwa ajili ya Watanzania tu,” alijibu msichana.
Si Godwin wala Manka aliyejua kilichokuwa kikiendelea kule, walishangaa lakini hawakuwa na jinsi kwani wenzao ambao walikwenda upande ule hawakuwa wakilalamika kwa lolote lile.
Kule, kulikuwa na watu wa usalama wa taifa waliovalia suti zao, walikuwa na wajibu wa kumchukua mtu yeyote na kumpeleka katika vyumba ambavyo walivitenga kwa ajili ya kufanyia kazi yao.
“Kuna nini?” aliuliza Manka.
“Hata mimi sijui! Hebu twende tukawasikilizie. “
“Ila naogopa mwenzio!”
“Hahaha! Kwani umeua Manka! Twende tukawasikilize,” alisema Godwin.
Walipowafikia usalama wa taifa, wakawachukua na kuwaambia kuingia ndani ya chumba kimoja. Godwin akaambiwa asubiri, Manka akachukuliwa na kuingizwa humo. Alikuwa akitetemeka, hakuwa amefanya kosa lolote lile lakini alijiona kama mhalifu.
Alipoingia, akaanza kuhojiwa baadhi ya maswali na kuambiwa kutoa simu yake. Hakubisha, akaitoa na kuambiwa aingie katika akaunti zake za Facebook na Instagram, hilo halikuwa tatizo, akafanya kama alivyoambiwa.
Ofisa mmoja wa usalama wa taifa akachukua simu ile na kuanza kuangalia alichotaka kuangalia. Alichukua dakika tano, alipomaliza, akamrudishia na kumtaka mtu mwingine aingie.
Godwin akaingia, akaambiwa akae kwenye kiti, akakaa na kuanza kuangalia na wanaume hao walioonekana kuwa makini kwa kila kilichokuwa kikitokea ndani ya chumba hicho.
Wakamuuliza maswali kadhaa, Godwin hakuonekana kutetemeka, alijibu kwa usahihi kila swali aliloulizwa, baada ya kila kitu akaambiwa atoe simu yake na kuwakabidhi.
“Ya kazi gani?” aliuliza Godwin.
“Kuna kitu tunataka kuangalia!”
“Kitu gani?”
“Wewe tupe simu yako,” alisema ofisa usalama.
“Hapana! Siwezi kuwapa kirahisi namna hiyo!” alisema Godwin huku akiachia tabasamu kana kwamba kile alichokuwa akikizungumza kilikuwa na utani.
Huo ndiyo ulikuwa msimamo wake, alikataa katakata kuwapa simu yake. Kila mmoja aliyekuwa ndani ya chumba kile akahisi kwamba inawezekana Godwin alikuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta.
Walimlazimisha, walipoona amekataa, wakaichukua kinguvu. Wala hakubisha. Walipoichukua, kazi kubwa ilikuwa ni kuifungua simu hiyo. Ilikuwa imefungwa, hakukuwa na mtu aliyejua namba za siri zaidi yake.
“Tupe namba zako za siri!”
“Nitawapa vipi na wakati mmeichukua kinguvu! Itumieni basi,” alisema Godwin, hapohapo akakunja nne, kuonyesha kwamba hakuwa na hofu yoyote ile.
Wakaanza kumpa vitisho ndani ya chumba kile ili aogope. Alihisi kabisa kulikuwa na kitu wanausalama hao walitaka kuangalia na kama akili yake ilikuwa imemwambia kwani akaunti ya Mabadiliko ya Kweli iliyokuwa Instagram haikuwa imetolewa hivyo kama watu wale wangeingia katika mtandao huo, wangekutana na akaunti hiyo.
“Toa namba za siri!” alisema mwanaume mmoja.
“Kutoa siwezi! Kama mna uwezo, futeni kila kitu,” alisema Godwin huku akionekana kumaanisha, mwanausalama yule aliyekuwa akimuhoji na mwenzake wakajiangalia viunoni mwao kuona kama kulikuwa na bastola, zilikuwepo, na pingu nazo, zilikuwepo.
“Tunakupa nafasi ya mwisho! Fungua simu yako!”
“Simu ni yangu, nilinunua kwa pesa yangu, hamkunichangia kwa chochote, iweje niwafungulie? Kufungua siwezi! Mkikasirika, vimbeni mpasuke,” alisema Godwin maneno yaliyowafanya maofisa wale kuvimba kwa hasira.

Je, nini kitaendelea?
Godwin umerudi Tanzania kufanya nini....ona sasa yanayotaka kukukuta. Najiuliza ilikuwaje godwin akaja kuwa mpiga debe makumbusho
 
DUNIA HAINA USAWA

Kila mtu aliyekuwa ndani ya chumba kile ikulu akapigwa na mshtuko, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona, rais wao alikuwa chini, alianguka baada ya kupata presha mara tu alipoona pesa zote alizokuwa nazo kwenye akaunti zilikuwa zimehamishwa kwenda katika hospitali moja nchini Marekani.
Wote wakamsogelea na kumbeba, vijana wanne kutoka humohumo ikulu wakafika, wakamnyanyua na kumpeleka katika chumba maalumu ambacho kilikuwa kikitumika kama hospitali ndogo humo ndani.
Presha yake ilipanda kutoka 120/80 mmHg mpaka kufika 230/130 mmHg. Kila mmoja alishtuka, walijua kabisa kwamba kama wasingefanya kazi ya ziada basi huo ingewezekana kuwa mwisho wa rais huyo.
Alitulia kitandani, hakutingishika kiasi kwamba ilikuwa ni rahisi kusema kwamba alikuwa amefariki dunia. Macho yake yaliziba, kwa jinsi alivyoonekana ilionyesha kama tayari system ya mwili wake haikuwa ikifanya kazi kabisa.
Mkewe alichanganyikiwa, akatoka chumbani na kwenda mpaka katika chumba kile cha matibabu, alipomwangalia mume wake kitandani pale, alibaki akilia kwani hali ilionyesha kwamba tayari mume wake huyo alikuwa marehemu.
“Imekuwaje jamani! Imekuwaje mume wangu kupatwa na tatizo hili?” aliuliza Bi Estelita huku akimwangalia mume wake kitandani pale.
“Mumeo alianguka na kuonekana presha kupanda kwa ghafla sana,” alisema daktari wa ikulu ambaye muda wote alikuwa humo kuhakikisha kila kitu kinakwenda salama.
“Ataamka tena?”
“Hatujui! Ndiyo tunaendelea kupambana! Vuta subira na umuombe Mungu! Natumaini kila kitu kitakuwa salama,” alisema daktari huyo ambaye alionekana kuwa bize kupita kawaida.
***
Hali ilikuwa imechafuka katika Benki ya Geneva nchini Uswisi, mkurugenzi wa benki hiyo aliitisha kikao cha haraka sana kwa ajili ya kujadili kitu kilichokuwa kikiendelea katika ‘system’ yao ambayo ilionyesha kulikuwa na muamala ilifanyika pasipo hata mwenye akaunti kuthibitisha muamala huo ufanyike.
Lilikuwa kosa kubwa, kiasi cha dola za Kimarekani milioni mia moja zilikuwa zimehamishwa kwenda katika akaunti nyingine nchini Marekani na mbaya zaidi hata kuzizuia walishindwa kwani pesa hizo zilipelekwa huku zikiwa na ulinzi mkubwa wa kiteknolojia.
Hawakujua mtu aliyefanya jambo hilo, vichwa vyao vilichanganyikiwa na wakati mwingine kuhisi kwamba kulikuwa na wafanyakazi ambao waliihujumu benki hiyo kitu ambacho kila mmoja alikana kufanya tukio hilo.
Lilikuwa tatizo kubwa, walitakiwa kupambana nalo kwa haraka sana hata kabla watu wengine hawakujua kilichokuwa kimetokea. Katika chumba kile kidogo kilichokuwa kikifanyika mkutano, mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Edward Peterson alivimba, kila kitu kilichokuwa kimetokea, kilimtia hasira.
“What the hell wrong?” (kuna tatizo gani?) aliwauliza viongozi wa benki hiyo akiwemo meneja mkuu, Bwana Linderfock.
Hakukuwa na mtu aliyejua kilichokuwa kikiendelea, walichokifanya ni kuwasiliana na watu wa IT hapohapo benki na kuanza kuzungumza nao. Wao wenyewe hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea, kulikuwa na mtu alikuwa ameingia kwenye database yao na kubana kila kitu, mafaili ya wateja wote yalifichwa kwa saa kadhaa na yalipokuja kuachiwa, tayari muamala ulikuwa umefanyika.
“Kweli hamuwezi kumgundua mtu aliyefanya hivyo?” aliuliza Bwana Peterson huku akiwaangalia.
“Tunahisi tutaweza kufanya hivyo! Cha kwanza tuzizuie pesa hizo kutoka kwenye akaunti ya hiyo hospitali,” alishauri jamaa mmoja.
Hilo ndilo lililofanyika, wakafanya mawasiliano na Bank of America na kuwaambia kilichokuwa kimetokea kwamba pesa zilizokuwa zimeingia katika akaunti yenye namba 08637621905 zilitakiwa kuzuiwa haraka iwezekanavyo kwani zilikuwa zimechukuliwa kiwizi kwenye benki kuu nchini Uswisi.
“Hakuna shida! Ila kwa jinsi zilivyo, nadhani hakuna mtu ambaye atakuwa na uwezo wa kuzitoa zaidi ya mhusuka tu, sisi tunazuia, ila hata mkisema tuzirudishe, tutashindwa kwa kuwa hata zilivyoingia tu, hatujui zimeingiaje,” alisema meneja wa Bank of America.
Hawakutaka kukubali, wakawasiliana nna watalaamu wa mambo ya IT na kuwaambia kilichokuwa kimetokea, kila mtu aliamini kwamba kazi hiyo ilikuwa ni rahisi sana kwani kama kulikuwa na virusi vilivyokuwa vimefanya figisu kisha kuhamisha pesa hizo basi vingewezwa kuangamizwa na kila kitu kurudishwa kama kilivyokuwa.
Vijana kumi na mbili kutoka nchini China wakafika nchin Uswisi kwa ajili ya kuifanya kazi hiyo. Walikuwa wataalamu waliobobea, waliokuwa akifanya kazi chini ya serikali, walipofika hapo, wakafanya kila linalowezekana kuweka mambo sawa lakini hakukuwa na kitu walichofanikiwa.
“Imekuwaje?” aliuliza Bwana Peterson.
“Bado tunapambana! Ila tunaweza kufanikiwa,” alisema kijana mmoja aliyeitwa Shu Yang ambaye alikuwa mtaalamu wa kucheza na system lakini kazi aliyokutana nayo hapo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.
****
Kuanguka kwa Rais Bokasa haikuwa siri tena, watu wengi wakafahamu kile kilichokuwa kimetokea huku sababu kubwa ya jambo hilo likiwa limefichwa kabisa. Watu walishangaa, hawakujua kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka rais huyo kuanguka na kuwa kwenye hali mbaya.
Si kila mtu aliyekuwa akihuzunika, asilimia kubwa ya Watanzania walikuwa wakifurahia, hawakuamini kilichotokea, wakapiga magoti na kumuomba Mungu kwamba kama ingewezekana rais huyo asifumbue macho yake, afe hapohapo kitandani kwani kwa maisha yaliyokuwa yakiendelea, kila mtu alikuwa akiyachukia.
Taarifa tofautitofauti zilikuwa zikiendelea kutolewa kutoka ikulu kwamba rais huyo alikuwa akiendelea vizuri. Taarifa hizo ziliwauma watu wengi kwani kusudio lao kubwa lilikuwa ni kumuona akifa kitandani pale kwani waliamini kwamba kama angekufa basi ingekuwa rahisi sana kwa maisha ya Watanzania wengi kubadilika.
Madaktari hawakutulia, kila daktari bingwa akaitwa kwa ajili ya kumtibu rais huyo, kila mmoja alikuwa akitaka kupewa sifa kwamba yeye ndiye aliyefanikisha mpaka rais huyo kupona ugonjwa huo.
Matibabu yaliendelea lakini hakuna aliyefanikiwa na hatimaye kusafirishwa kuelekea nchini India katika Hospitali ya Ganga kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.
Mpaka muda huo, hakukuwa na aliyekuwa na uhakika kwamba rais huyo angeweza kusimama tena, tangu alipoanguka na kupoteza fahamu hakuwa ameyafumbua macho yake japokuwa mapigo yake ya moyo yalikuwa yakiendelea kudunda kama kawaida.
Mitaani kulikuwa na stori nyingi juu ya tukio hilo. Kuna wengine walisema kwamba alipigwa na mkewe, wengine wakasema kwamba rais huyo alianguka akiwa bafuni, wengine walisema kwamba alitembea na mke wa mtu hivyo mwenye mume kuamua kumroga.
Hakukuwa na mtu aliyejua ukweli ila waliamini kwamba kila kitu kingewekwa wazi katika Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli kwani mtu huyo alionekana kama ofisa wa usalama wa taifa kwa jinsi alivyokuwa akipata taarifa nyingi tena kwa wakati.
Baada ya siku mbili tangu rais aanguke na kupoteza fahamu ndipo Godwin akaandika katika akaunti ile kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba yeye ndiye aliyesababisha rais huyo aanguke na kuumiza vibaya baada ya kuhamisha pesa zake alizowaibia wananchi kuwapelekea wagonjwa waliokuwa katika Hospitali ya St. Lucas nchini Marekani.
“Niliamua kuhamisha pesa zake zote katika akaunti yake iliyokuwa katika Benki ya Geneva, pesa zote hizo niliamua kuzipeleka katika Hospitali ya St. Lucas iliyokuwa nchini Marekani, sababu ya kufanya hivyo ni kwamba pesa si zake, ni pesa zangu, zako, zetu wote, tunalipa kodi, yeye ndiye ambaye aliamua kuzichukua kwa manufaa yake, sasa nimeamua kuziondoa kutoka kwake,” aliandika Godwin.
Hakukuwa na mtu aliyehuzunika, kila mmoja alifurahi kwani kwa kilichokuwa kimetokea, wote waliona kwamba rais huyo alistahili kufanyiwa kile alichofanyiwa.
Wananchi walikuwa wakiumia, kodi zilikuwa juu, ziliwaumiza kupita kawaida kiasi kwamba wengine hawakuona matunda ya kazi waliyokuwa wakiifanya ila kwa kuwa pesa zile walizokuwa wameibiwa kwa miaka mingi ziliondolewa kutoka kwa mbaya wao, walibaki wakimsifu Godwin kwa kile kilichotokea.
Viongozi wengine waliokuwa wameficha pesa zao huko wakashikwa na hofu na kuona kwamba kama wasingefanya kila liwezekanalo kuhamisha pesa hizo basi hata nao pesa zao zingechukuliwa na kupelekwa sehemu nyingine.
Walikuwa mawaziri watano, wakapigiana simu na kujadiliana ni kitu gani walitakiwa kufanya ili kuhakikisha pesa zao zinabaki salama katika mikono yao. Wakakubaliana kwamba ilikuwa ni lazima kuzihamisha pesa hizo kisiri kwenda kwenye benki nyingine nchini Tunisia ambapo zingewekwa kwa mtindo wa kuanzishwa taasisi ndogo ya Kiislamu ambayo iliweka kambi huko kwa ajili ya kusambaza misaada kwa watoto yatima na wanawake wagonjwa.
Wakati wakipanga mipango yao, hawakujua kama simu zao zilikuwa zikidukuliwa na Godwin ambaye alikuwa akifuatilia kila kitu, alipogundua kwamba viongozi hao walikuwa na mpango huo wa kuhamisha pesa zao na kupeleka katika moja ya benki nchini Tunisia, akaanza kucheza nazo kwa ajili ya kuzificha kama alivyomfanyia Rais Bokasa.
“Niwaambie tu kwamba viongozi watano waliokuwa wakiwasiliana jana kwamba watahamisha pesa zao kwenda kwenye moja ya benki nchini Tunisia, mpango wenu umekwamba kwani mpaka inafika asubuhi, hamtoweza kuziona pesa zenu,” aliandika Godwin katika akaunti yake kitu kilichowafanya watu wote kushangaa kwamba jamaa alikuwa akinasa vipi mawasiliano ya viongozi hao kiasi cha kuwatia hofu.
Alichokisema ndicho kilichofanyika, siku hiyohiyo akazizuia pesa za viongozi hao. Walipokuwa wakiingia, waliziona lakini walipotaka kufanya miamala, pesa hazikuwa zikionekana.
Haraka sana wakawasiliana na Mkurugenzi Peterson na kumwambia kilichokuwa kikiendelea. Hakuamini, alichanganyikiwa kwani Wachina aliokuwa amewaita kufanya kazi, walikuwa wakihakikisha Rais Bokasa anarudishiwa pesa zake, sasa kabla kazi hiyo haijafanyika na kukamilika, tayari kulikuwa na kesi nyingine, haikuwa kwa mtu mmoja, kwa wateja wao watano kiasi kwamba yeye mwenyewe hakujua afanye nini.
“Hebu subiri kwanza. Mnanichanganya,” alisema Bwana Peterson.
“Tunajua! Ila kwa nini pesa zetu hazitoki!”
“Kuna mtu amedukua akaunti zenu!”
“Inawezekanaje?”
“Naomba mnipigie baadaye. Sijui hali imekuwaje! Naomba mnipigie baadaye, tunashughulikia tatizo lenu,” alisema Bwana Peterson huku akionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida.
Simu ikakatawa, kila kitu kilikwenda ndivyo sivyo, kilichokuwa kikiwashangaza ni namna ambavyo mtu huyo alivyoweza kupata mawasiliano yao, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
Walisikilizia simu kutoka nchini Uswisi, hawakupigiwa, dakika zilisonga, saa likakatika, saa mbili nazo zikaenda, mpaka saa tano, bado hawakupigiwa hali iliyowapa majibu kwamba watu hao walikuwa wakiendelea kuhangaika kuhakikisha kile kilichokuwa kimetokea kinapatiwa ufumbuzi haraka sana.
“Wakati tunasikilizia huko, waambie usalama wa taifa wamtafute huyo Godwin!” alisema Waziri wa Kilimo, Abraham Ojuku.
“Wanafanya kazi hiyo mkuu. Tatizo picha zake!”
“Hakuna picha zake?”
“Ndiyo! Kwenye mitandao zipo zile za utotoni!”
“Ukubwani hakuwahi kupiga picha?”
“Hapana!”
“Hebu waambie wafuatilie, aliposhuka na ndege alitoka wapi, alikuwa anafanya nini huko. Hakikisha wanafuatilia, na kama alikuwa akisoma chuo, alisoma chuo gani, tukipata yote hayo, tutafanikiwa kwani cha msingi tupate picha yake ya ukubwani, ya utotoni hatutofanikiwa kumpata kwani anaweza akawa na ndevu nyingi kama Osama,” alisema Waziri Ojuku huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Tunafuatilia mkuu!”
***
Usalama wa Taifa hawakutaka kutulia, waliambiwa kwamba walitakiwa kufuatilia kuhusu Godwin na siku hiyohiyo kituo cha kwanza kabisa cha kuanza upelelezi wao kilikuwa ni uwanja wa ndege kulipokuwa na ofisi ya Shirika la Ndege la Orange.
Wakafika katika ofisi hizo na kitu pekee walichokuwa wakikihitaji ni taarifa juu ya msafiri ambaye alisafiri kwa ndege yao siku ya Jumamosi na hivyo kuwapa orodha ya majina ya watu waliosafiri kwa ndege hiyo.
Haraka sana wakaanza kupitia majina ya abiria hao, wala hawakuchukua muda mrefu wakaliona jina la Godwin Mapoto ambaye alikuwa amesafiri huku pembeni yake kukiwa na msichana mwingine aliyeitwa kwa jina la Manka.
Ilionyesha kabisa kwamba Godwin alitokea Dubai katika ndege iliyotokea nchini Japan ambapo huko hawakujua alikwenda kufanya nini kwani kutokana na Waafrika wengi kwenye katika nchini za Mashariki ya Kati, iliwafanya kutokundua kama alikwenda kibiashara au kusoma.
“Ni lazima tusafiri kwenda huko, inawezekana tukapata taarifa zaidi,” alisema Boniphace Ngumije, mmoja wa wanausalama walioambiwa wafuatilie kila kitu kuhusu Godwin na ikiwezekana waweze kupata picha zake.
Wakatoa taarifa kwa mkuu wao na kumwambia kwamba walikamilisha theluthi ya upelelezi wao na kugundua kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa ametokea nchini Japan lakini hawakujua dhumuni hasa la mtu huyo kuwa nchini humo.
“Nendeni mpaka huko, hakikisheni mnafanya kila linalowezekana kupata picha zake,” alisema mkuu wao.
Wakasafiri na kuelekea huko, njiani, walikuwa na mawazo tele, walikuwa wakimtafuta mtu ambaye waliamini kwamba alikuwa nchini Tanzania. Walikuwa wakijadiliana juu ya kitu gani kilitakiwa kufanyika mpaka kuhakikisha wanapata picha za mtu huyo na kurudi nazo nchini Tanzania.
Walichukua saa zaidi ya ishirini mpaka kufika Japan ambapo wakachukua chumba, wakalala na siku iliyofuata ilikuwa ni kufuatilia katika ofisi za Shirika la Ndege la Orange ili kupata kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Kama ilivyokuwa kule Tanzania, napo wakapewa jina la mtu huyo, namba ya tiketi yake lakini kuhusu kila kitu kilichokuwa kikiendelea, kupata picha yake ilikuwa ni lazima kuwasiliana na ubalozi wa Japan nchini Tanzania kuwaambia kuhusu mtu huyo.
“Taarifa hazionyeshi kitu chochote kile, huwa tunazihifadhi katika kompyuta zetu, cha ajabu taarifa za mtu huyo hazipo. Mna uhakika alikuwa Japan?” aliuliza balozi wa Japan nchini Tanzania ambaye alikuwa akitumiwa taarifa zote.
“Ndiyo! Au alizifuta?”
“Haiwezekani! Hakuna mtu anayeweza kuingia kwenye kompyuta zetu,” alisema balozi huyo pasipo kujua kwamba taarifa zote kuhusu Godwin, mwanaume huyo alizifuta.
Hawakutaka kukata tamaa, vijana waliokuwa Japan wakapewa taarifa kuanza kufuatilia katika vyuo nchini humo kuona kama kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo ambaye alimaliza chuo siku chache zilizopita.
Walizunguka kwenye kila chuo, jina walilokuwa wakiliangalia lilikuwa ni Godwin tu. Waliwapata vijana wengi lakini hawakuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa nguvu zote lakini baada ya kwenda katika Chuo Kikuu cha Waseda kilichokuwa Tokyo, wakaambiwa kwamba kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo, aliitwa Godwin Mapoto.
“Ndiye huyohuyo! Hebu tunaomba data zake zote,” alisema Boniphace huku akionyesha tabasamu, walikaa siku tatu nchini humo na hawakupata chochote kile, kitendo cha siku hiyo kupata mwanga, kiliwafurahisha.
“Alikuwa mwanafunzi wa mwisho mweusi kusoma katika chuo hiki. Alichukua PhD yake siku chache zilizopita. Alikuwa raia wa Tanzania. Data zake hizi hapa,” alisema mkuu wa chuo hicho huku akiwaonyeshea mwanaume huyo.
“Safi sana.”
“Ni mtu makini sana. Ana akili nyingi mno, inasadikiwa ndiye mtu mwenye akili kubwa na kucheza na kompyuta, mambo yote kuhusu programming, networking, huyo ndiye alikuwa balaa,” alisema mkuu wa chuo, hakuishia hapo akaanza kuwapa simulizi kuhusu Godwin ambayo iliwasumbua wataalamu wengi, hasa baada ya kuficha mafaili ya chuo.
Hawakuamini kama kungekuwa na Mtanzania ambaye angekuwa na akili kiasi hicho. Walibaki wakiangaliana na kukiri kwamba mtu waliyekuwa wakidili naye hakuwa mtu wa kawaida hata kidogo na ndiyo maana hata ile akaunti yake ilikuwa ni vigumu sana kufutwa na watu wengine.
“Sawa. Tunashukuru sana. Naomba kuuliza swali!” alisema Martin, kijana aliyeongozana na Boniphace.
“Uliza.”
“Mbona kwenye taarifa zake hakuna picha yake?” aliuliza Martin.
“Picha yake? Picha yake ilikuwepo hapa. Sijui imekwenda wapi lakini ilikuwepo hapa,” alisema mkuu wa chuo huku akishangaa, taarifa zote za wanafunzi zilikuwa zikiwekwa na picha ila cha kushangaza kwenye faili la Godwin hakukuwa na picha.
“Una uhakika picha zilikuwepo?”
“Ndiyo! Ni juzi tu zilikuwepo.”
“Tunaweza kuzipata?”
“Haina shida.”
Kuzipata picha za Godwin hakukuwa na tatizo lolote lile kwani kulikuwa na picha nyingi ambazo zilikuwa katika tovuti ya chuo watu walikuwa wamepiga. Mkuu huyo wa chuo alifungua tovuti hiyo na kuangalia picha zote, kitu cha ajabu kabisa ambacho kilimchanganya, kote huko zile picha zote ambazo mwanaume huyo alitokea, hazikuwepo kitu kilichowachanganya.
Boniphace na mwenzake hawakutaka kubaki Japan, walimwambia mkuu wao kwamba kule walipokuwa wamekwenda hawakufanikiwa kupata kile walichokuwa wakikihitaji ila kwa taarifa tu ambazo walizipata kutoka kwa mkuu wa chuo zilieleza kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa hatari sana katika kutumia kompyuta.
Hilo likawafanya kukata tamaa kupata picha zake, walichokifanya ni kuchukua picha zilezile alizokuwa mtoto mdogo na kuzisambaza katika vituo mbalimbali vya polisi ili kama wangemuona mtu aliyekuwa akifanana na mtoto huyo wamchukue na kumpeleka kituoni mara moja.
“Mmh! Hivi tunaweza kufanikiwa kweli? Sidhani ila haina jinsi, ni lazima tutii kile tulichoambiwa!” alisema mkuu wa Kituo cha Polisi cha Mkwajuni.
****
Godwin hakuwa na hofu hata kidogo, kwa kila kitu kilichokuwa kikiendelea kwake kulikuwa na amani tele. Alikuwa akiichanganya serikali, kila siku alikuwa akiwapa taarifa watu kuhusu madudu mengi yaliyokuwa yakitokea nchini Tanzania.
Watu walimshukuru ingawa kwa upande wa pili serikali ilikuwa ikichomwa na mbaya zaidi hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua mahali mwanaume huyo alipokuwa kwani kila walipojaribu kuidukua simu yake kujua alipokuwa, iliwaonyesha kwamba ilikuwa Urusi na wakati mwingine kuwaonyesha ilikuwa Dubai.
Walichanganyikiwa, walituma maofisa wa usalama wa taifa, waliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa katika mtaa mmoja wa kitajiri akila maisha hivyo kuwatuma watu wengi huko. Ni kama Godwin alijua kwani mara baada ya kutoka hotelini, akaondoka na kuanza maisha katika Mtaa wa Tandale kwa Mtogole, akapanga katika chumba kimoja chakavu, akanunua nguo za mtumba Tandale Sokoni na kila siku kazi yake ilikuwa ni kuendeleza harakati zake katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli.
“I want to know who killed my parents and sister,” (nataka kumjua aliyewaua wazazi wangu na dada yangu) aliandika Godwin kwenye akaunti yake kitu kilichozua maneno mengi na wengine kugundua kwamba inawezekana Godwin alikuwa akifanya hayo yote kwa kuwa kulikuwa na watu waliokuwa wameiteketeza familia yake.
Maoni yalikuwa mengi, wengi walikuwa wakiuliza kilichokuwa kikiendelea mpaka kuandika maneno hayo ambayo yaliwasisimua watu wengi. Kila swali alilokuwa akiulizwa, alilijibu pasipo tatizo lolote lile kitu kilichowafanya watu kugundua maovu makubwa yaliyokuwa yakifanywa na serikali iliyokuwa madarakani.
“Nilijua tu! Hii serikali magumashi sana. Inawezeje kuiangamiza familia nzima. Kwanza huyu jamaa ni mtoto wa familia ipi? Baba yake alikwishawahi kuwa kiongozi yeyote yule?” alihoji jamaa mmoja kwenye Mtandao wa Facebook huku akiwa ameipiga picha ile posti aliyoiandika Godwin.
Posti hiyo ikaibua mambo mengi, kila mtu mitaani alikuwa akizungumza lake. Kwa Godwin hakutaka kuzungumzia kitu chochote kwa undani ila alichokifanya ni kutafuta vifaa vyote vya kuchorea tatuu na kujichora tatuu kifuani iliyokuwa na maneno hayo aliyoandika kwenye akaunti yake.
“Hii ni vita ya kisasi na kamwe haitomuacha mtu salama,” aliandika Godwin na kuongezea maneno mengine mengi yaliyosomeka:
“Huu utakuwa mwezi wa viongozi wengi kujiua. Sitowaua mimi, ila ninatarajia viongozi wengi watakwenda kujiua. Kuna data nilikuwa nazikamilisha, zipo poa. Ninawahakikishieni kwamba viongozi wengi watajiua, si kwamba ninapenda kuwaua, hapana, watajiua wao wenyewe kwani kashfa zitakawatafuna, hakika hawatoona thamani ya kuishi.
“Kama mlikuwa hamjui, kuna msichana aliitwa Vanessa Fabian, msichana mrembo ambaye ndiye atasababisha viongozi hao kujiua. Unajua kwa nini? Nitakuandikia Jumatatu kila kitu kilichotokea kwa msichana huyu, wengi mtahuzunika ila mwisho wa siku mtatabasamu, itakuwa historia yenye kumgusa kila mtu. Unataka kuifahamu historia ya msichana huyo, nitawaandikia Jumatatu mahali haphapa,” ilisomeka posti hiyo ndefu.
Kila mtu akawa na hamu, wengi walitaka kumjua huyo Vanessa, alikuwa nani na alibeba historia gani yenye kuhuzunisha ambayo ingewafanya viongozi wengi wa serikali kujiua?
Maoni yakawa mengi mno na kila mmoja alionekana kuguswa kwa kile kilichokuwa kimeandikwa hivyo watu wengi kuwa na hamu ya kutaka kufahamu. Ni mambo gani yalitokea ambayo yangepelekea viongozi wengi kujiua? Kila mmoja alitaka kujua.
***
Godwin hakuwa mtu wa kutoka sana nje, alikuwa mtu wa kukaa ndani kila wakati. Japokuwa akaunti yake ilikuwa maarufu sana lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua kwamba yule mwanaume aliyepanga kwenye nyumba ile mbovumbovu ndiye yuleyule aliyekuwa akiinyima furaha Serikali ya Tanzania.
Kazi yake kubwa ilikuwa ni kudukua mawasiliano yote yaliyokuwa yakifanyika nchini Tanzania hasa kwa viongozi wa nchi hiyo. Alijua siri nyingi, mikataba ya siri iliyokuwa imesaniwa ambayo iliruhusu madini kuondoka, pesa za mitambo ya umeme, kila aina ya uchafu uliokuwa ukifanyika data zake alikuwa nazo.
Alitaka kuandika historia kuhusu msichana Vanessa, hakuwahi kukutana na msichana huyo ila historia yake alikutana nayo katika barua pepe ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Bwana Samson Mwinyimkuu.
Ilikuwa ni historia ya msichana Vanessa, msichana aliyekuwa mrembo mno ambaye aliamua kuiandika historia ya maisha yake na kumtumia waziri huyo ambaye aliiweka katika barua pepe yake na kuifanya siri nzito.
Godwin aliipata barua hiyo, ilikuwa ni ndefu mno lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kuiandika kwa ufasaha na kuiweka katika akaunti ile.
Watu walikuwa wakisubiri kwa hamu kubwa, kuanzia siku ya Jumamosi mpaka Jumatatu ilionekana kuwa kama mwezi mzima. Kila mmoja alitaka kujua kile kilichokuwa kimetokea kwa msichana huyo mrembo, hawakujua alikuwa Vanessa yupi kwani kwa kipindi hicho kulikuwa na wasichana wengi wenye jina hilo waliokuwa maarufu sana.
Mara baada ya Waziri Mwinyimkuu kuona posti hiyo, haraka sana akaingia katika barua pepe yake ili kuangalia kama ilikuwepo, aliiona ila hofu yake kubwa ilikuwa ni juu ya msichana huyo ambaye kwa kipindi hicho alikuwa marehemu, je, alimtumia Godwin barua hiyo hata kabla hajafa?
Wakati akiwaza hayo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, alikuwa na presha kubwa, alikuwa akiheshima na kila alipokuwa akipita watu walimpigia makofi, alikuwa mchapakazi ambaye kila siku viongozi wengi wa serikali waliambiwa waige utendaji kazi wake mkubwa.
Hakujua ni kitu gani kingetokea mara baada ya uovu wake aliomfanyia Vanessa kwa kushirikiana na viongozi wengine kuwekwa wazi. Alitetemeka, mapigo ya moyo wake yalidunda kupita kawaida.
Watanzania wengi waliona Jumatatu kuwa mbali lakini ni yeye tu ndiye aliyeiona siku hiyo kuwa karibu sana. Mishale ya saa yake ilikimbia kwa kasi ya ajabu, alijiona akiwa nje, kwenye umati mkubwa huku watu wakimwangalia, walimcheka na kumdhihaki na watu wengi kutamani kuona mwanaume huyo akifa kutokana na uovu aliokuwa ameufanya.
“Ngriiiii...ngriii...” alishtushwa na mlio wa simu, haraka sana akaichukua na kuipeleka sikioni, kwa jinsi alivyokuwa amechanganyikiwa, hata kuangalia jina la mpigaji hakuangalia.
“Mwinyimkuu! Upo wapi?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili.
“Ny..um..ban..i..” alijibu Mwinyimkuu huku akitetemeka.
“Umeona kilichopostiwa? Ile barua pepe uliifuta kweli au uliihifadhi kama jumba la makumbusho?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili, kama alivyochanganyikiwa waziri huyo hata na yeye alikuwa amechanganyikiwa.
“Sikuifuta!”
“Hukuifuta? Kwa nini? Isije kuwa huyu mtu anataka kuiandika ile historia ya yule binti!” alisema jamaa huyo.
“Sidhani! Hawezi! Atakuwa anatutisha tu!”
“Mh! Ya kweli hayo? Sasa amejuaje kuhusu Vanessa?” aliuliza.
“Sijajua kabisa. Ni bora kama yule msichana angekuwa hai tungemuuliza. Ibra, naomba unipigie baadaye,” alisema Mwinyimkuu na kukata simu.
Hakuishia kupokea simu ya Ibra tu bali alipokea simu za viongozi watatu ambao wote hao walimuuliza kuhusu kile kilichokuwa kimeandikwa, kila mmoja alikuwa na hofu kubwa na kuona kabisa kwamba uovu wote waliokuwa wamemfanyia msichana huyo sasa ulikuwa ukienda kujulikana na kila mtu.
“We are finished,” (tumekwisha) aliandika mwanaume mmoja ambaye naye alishirikiana na Mwinyimkuu katika kila kitu kuhusu msichana Vanessa.
Jumatatu asubuhi tayari watu walikuwa mbele ya kompyuta zao huku wengine wakiwa katika simu zao. Walitaka kushuhudia ni kitu gani kilikuwa njiani kuandikwa. Kazini, kila mfanyakazi alikuwa na simu yake, hakutaka kuiweka chini, walitaka kusoma kuhusu msichana huyo mwenye historia ya kusikitisha mno.
Saa 3:00 asubuhi Godwin akaposti sehemu ya kwanza kuhusu msichana huyo. Alianza kusimulia historia ya maisha yake, jinsi alivyokuwa kwenye maisha ya kimasikini mpaka pale alipoamua kumfuata Mwanyimkuu kwa ajili ya kumsaidia.
Mwanaume huyo alipofuatwa na msichana huyo, aliahidi kumsaidia kwa moyo mmoja lakini badala ya kufanya hivyo, akaanza kwa kumuomba penzi. Kilikuwa ni kitu ambacho Vanessa alimkatalia kwa nguvu zote kwani hakuwahi kufanya mapenzi na mwanaume yeyote, alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni msaada tu kwa kuwa aliamini mwanaume huyo alisaidia watu hivyo hata yeye angemsaidia.
“Bila penzi hakuna msaada.”
“Ila mama anaumwa sana. Naomba unisaidie, umasikini unatutesa, bila pesa, mama yangu atakufa, bila pesa, wadogo zangu watakufa kwa njaa, hatuna kitu, maisha yetu ni masikini, naomba utusaidie,” ilisema sehemu ya posti ile alipokuwa akizungumza msichana Vanessa.
“Bila penzi, mama yako atakufa, na bila penzi wadogo zako watakufa pia,” alisema mzee huyo.
Vanessa hakutaka kuona mama yake akifa, alipenda kuona akiendelea kuishi miaka yote na hivyo kumpa penzi mzee huyo. Alisikia maumivu makali kwa kuwa ilikuwa ni siku yake ya kwanza. Kiasi cha pesa alichokuwa akikihitaji hakukipata kutoka kwa mzee huyo zaidi ya kupewa asilimia ishirini ya kile alichokiomba.
Mzee Mwinyimkuu akatumia pesa na madaraka kumchezea msichana huyo, alimtumikisha kingono na alipoona kwamba ameridhika, akawaambia wengine matatizo ya msichana huyo na hivyo nao kumfanyia mchezo huo msichana huyo mdogo. Wanaume hao wengine watatu walikuwa ni Waziri Mamboleo, Kijuku na Mburu.
Msichana wa miaka kumi na sita akatumikishwa kingono na wanaume wanne, hawakuwa na huruma, waliendelea kumchezea pasipo kumsaidia na wakati alipokuwa akiwatisha kwamba ataenda polisi kushtaki, walimwambia kwamba wangemuua na hivyo kuogopa.
Ni maisha yaliyoogepesha na kusisimua mno. Mmoja kati ya wanaume hao alikuwa ameathirika ugonjwa wa Ukimwi, akamuambukiza Vanessa na kuwaambukiza wanaume hao wote.
Ilikuwa ni historia ndefu ambayo Godwin aliiandika kimafungumafungu, hakutaka kuishia hapo, alihakikisha anaweka kila kitu wazi, hawakujua majibu ya vipimo vya Ukimwi alivitoa wapi, aliweka karatasi za majibu ya damu zao baada ya kupima damu hospitalini.
“Mungu wangu! Kumbe wameathirika! Wamemuambukiza na mtoto yule jamani!” alisema jamaa mmoja.
Wanawake waliokuwa wakisoma historia ndefu ya msichana huyo hawakuvumilia, walikuwa wakilia kwa maumivu makali mioyoni mwake, walisisimka, hawakuamini kama kungekuwa na watu waliokuwa na hali ya kinyama kama viongozi hao.
“Hatuwezi kukubali! Tutaandamana kuwataka wajiuzulu,” alisema jamaa mmoja.
Vijana wenye msimamo, walioumizwa hawakutaka kubaki nyumbani kwao. Ilikuwa kashfa kubwa iliyolitetemesha taifa kwa ujumla, viongozi ambao kila siku walikuwa wakiheshimiwa kila walipopitwa kumbe walikuwa na maisha ya kinyama, kwa kutumia pesa na nguvu zao waliamua kumdhalilisha Vanessa kingono.
Msichana huyo alikufa miaka miwili iliyopita kwa ugonjwa huo ambao watu hawakujua aliupata wapi na mbaya zaidi, viongozi hao nao walikwenda kuhudhuria msiba huku wakijifanya kuwa na huzuni mno.
“Siwezi kuishi! Siwezi kuivumilia aibu hii,” alisema mwinyi mkuu, historia ndefu aliyokuwa ameambiwa na Vanessa ndiyo ambayo ilikuwa ikionekana katika akaunti ya Mabadiliko ya Kweli.
Hakujua mahali mtu huyo alipoipata kwani mara baada ya Vanessa kuiandika, akamtumia na alikuwa na uhakika kwamba hakutumiwa mtu mwingine kwa kuogopa kuuawa, sasa ilikuwaje mpaka mtu mwenye akaunti hiyo kuipata?
Aliumia, alijutia kila kitu alichokifanya maishani mwake. Hakujua Tanzania ingemuangaliaje, hakujua familia, ndugu, jamaa na marafiki wangemuangaliaje, uamuzi alioufanya ulikuwa ni mmoja tu, kujiua kwa kujipiga risasi.
“Mwinyimkuu amejiua!” alisema jamaa mmoja.
“Kweli?”
“Ndiyo! Hiyo ni breaking news wameiandika Global. Cheki braza,” alisema jamaa huyo huku akimuonyeshea simu mwenzake.
Huo ulikuwa ni kama mwanzo, ilikuwa ni fedhea, wahusika wote waliumia, hakukuwa na hata aliyebaki, ili kuogopa aibu kubwa mbele yao, wakaamua kujiua kwa vifo tofauti, yule alijipiga risasi, mwingine akajinyonga, mwingine akanywa sumu na mwingine akaamua kujichinja.
“Yapo mengi tu! Nilipowaambia nimekuja Tanzania kufanya kazi namaanisha nimekuja kufanya kazi. Nitaweka wazi mambo mengi sana! Nyie subirini, kuna vitu vingine havielezeki, nitawaelezea mpaka wachungaji ambao wanashirikiana na viongozi serikalini kuwaibia wananchi. Unajua wanawaibia vipi na wachungaji hao ni wakina nani? Nitawaandikia kesho mahali hapa. Lengo ni kuisafisha nchi, hilo tu,” aliandika Godwin, kwa kipindi hicho, kila kitu alichokuwa akikiandika kwenye akaunti ile alikuwa na uthibitisho nacho
Kwa kile kilichokuwa kimetokea, kila kona ikawa gumzo. Akaunti ile iliwasumbua watu wengi, katika nchi nyingine Afrika Mashariki kila mmoja alikuwa akizungumza lake, wengi walilaumu kwa kilichokuwa kimetokea, Tanzania ikaingia doa, kila kona ilizungumziwa vibaya lakini pamoja na hayo yote, watu wote walikuwa wakimsifu mtu aliyekuwa akiweka wazi madudu yote yaliyokuwa yakitokea nchini humo.

Je, nini kitaendelea?
 
Jackal anachelewesha sana hebu muhimize awe anawahisha huenda akakusikiliza..
Hhahahha Tater ebu niache mm nilimwambia aweke mbili kwa siku naona ndio anavyoweka hakuna tatizo jamani
 
DUNIA HAINA USAWA

Vijana wa IT nchini Uswisi walikuwa wakihangaika kuzichukua pesa ambazo zilihamishwa kwenye akaunti moja nchini Marekani katika Benki ya American. Waliweza kuzizuia pesa hizo nyingi zisiweze kutoka lakini kitu cha ajabu kabisa hawakuwa wakiweza kuzichukua na kuzirudisha katika akaunti zilipotolewa.
Walitumia wataalamu wengi lakini kitu kilichokuwa kikiwatatiza kilikuwa ni virusi vilivyokuwa vimeingizwa katika data base yao ambavyo vilizuia pesa kurudishwa katika akaunti ile iliyokuwepo.
Mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Peterson hakulala kwa siku mbili mfululizo, kichwa chake kilichanganyikiwa na hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea. Vijana wa IT aliokuwa amewaita kwa ajili ya kufanya kazi hiyo walionyesha kila dalili za kushindwa kwani walichukua muda mrefu mno na hakukuwa na kitu chochote kile kilichofanyika.
Kwa siku tatu mfululizo watu walikuwa wakihangaika, wakaitwa wataalamu mbalimbali kutoka sehemu tofauti lakini hakukuwa na mtu aliyeweza kuzirudisha pesa hizo zilizokuwa zimetumwa katika akaunti ile ya Hospitali ya St. Lucas.
“Hebu tuwasiliane na mteja kwanza ili tumuombe radhi kwani tunaweza kuchukua muda mrefu kidogo,” alisema Bwana Peterson.
Ilikuwa ni lazima kuwasiliana na Rais Bokasa kumuomba radhi kwa kile kilichokuwa kikiendelea. Mawasiliano kwa njia ya simu yakafanyika na kilichowashtua zaidi ni kwamba mtu huyo alikuwa hoi hospitalini baada ya kuzimia alipopewa taarifa kwamba kiasi hicho kilikuwa kimechukuliwa katika akaunti yake.
Wakati wakiongea na mtu wa pili ndipo mkurugenzi huyo akaambiwa kila kitu kilichokuwa kimetokea. Aliambiwa kuhusu akaunti ya Mabadiliko ya Kweli, akaambiwa kwamba mtu aliyekuwa na akaunti hiyo ndiye ambaye alikuwa ameziiba pesa hizo na kuziweka katika akaunti hiyo, serikali ya Tanzania ilikuwa ikipambana kumtafuta lakini ubaya zaidi ni kwamba walikutana na mtu aliyekuwa akijua sana kutumia kompyuta.
“Kwa hiyo huyo mtu yupo huko?” aliuliza Bwana Peterson.
“Ndiyo! Ila hatufahamu yupo wapi!”
“Na akaunti hiyo anaitumia?”
“Ndiyo!”
“Hebu subiri!”
Alichokifanya Peterson ni kuwasiliana na rais wa nchi hiyo na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea. Kwanza akamuhadithia kuanzia mwanzo mpaka pale ambapo vijana waliitwa kwa ajili ya kurudisha pesa hizo, alipomaliza akamwambia kuhusu ile akaunti na mtu aliyefanya mambo hayo yote alikuwa nchini Tanzania.
“Haiwezekani!”
“Ndiyo hivyo!”
“Kwa hiyo ni Mwafrika?”
“Ndiyo mkuu!”
“Hebu subiri!”
Yaliyokuwa yakifanyika yalikuwa ni mawasiliano kwa njia ya simu. Ilikuwa ni lazima waunganishe nguvu zao kwa ajili ya kumpata mtu huyo ambaye alikuwa akiwasumbua muda wote. Rais hakutaka kukubali kwamba mtu aliyekuwa akiyafanya mambo hayo alikuwa Mwafrika.
Hakuamini kama Waafrika walikuwa na akili kubwa kama Wazungu, kwake, watu hao walionekana kama maboksi fulani ambayo yalikuwa yakifanya kile walichoambiwa wafanye lakini si wao kuwaongoza Wazungu.
Akawasiliana na Mkurugenzi wa usalama wa taifa nchini humo, The Federal Intelligence Service (FIS), Bwana Henrik Kom ambaye akamwambia kila kitu kuhusu mchakato mzima ulivyokuwa na kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima maofisa wawili wa FIS watumwe kuelekea nchini Tanzania kwa ajili ya kumtafuta mtu huyo ambaye aliisumbua Benki ya Geneva kwa kile alichokuwa amekifanya.
“Hilo si tatizo! Wamesema ni Mwafrika?”
“Ndiyo!”
“Mmh! Inawezekana vipi?”
“Ndiyo tunataka muendele mkajue ukweli huko,” alisema rais.
Hilo ndilo walilolifanya, ndani ya siku mbili, vijana wawili, wataalamu kwa masuala ya upelelezi wakatumwa kwenda nchini Tanzania huku wengine wakibaki hapo kwa ajili ya kuifuatilia akaunti hiyo ya Mabadiliko ya Kweli iliyokuwa katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram.
****
Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba yule kijana masikini aliyekuwa amehamia mtaani Tandale ndiye aliyekuwa akihusika katika kuuendesha mtandao huo. Hapo Tandale alipokuwa akiishi alikuwa mtu wa watu, alitaka kuyaficha maisha yake, kusiwe na mtu yeyote kumfahamu au hata kuhisi kwamba alikuwa yeye.
Alichokifanya ni kuanza kwenda katika vilabu vya pombe haramu na kuanza kushinda huko. Kazi yake ilikuwa ni kupiga stori, hakuwa mnywaji ila kila alipokuwa akirudi nyumbani kwake alijifanya kuwa mlevi mkubwa.
Watu walimshangaa, hawakuwahi kumuona mgeni ambaye alifahamiana na watu wengi kwa haraka kama ilivyokuwa Godwin, kila mtu aliyekuwa akiongea naye alijua kabisa kwamba alikuwa akizungumza na mlevi ambaye kila siku asubuhi, mchana mpaka jioni kazi yake ilikuwa ni kushinda klabuni tu.
Akajulikana zaidi kama mlevi, hawakujua kama mtu huyo ndiye aliyewanyima usingizi viongozi mbalimbali, kila siku usiku ilikuwa ni lazima kuangalia kwenye akaunti yake kuona ni jinsi gani watu walikuwa wakitaka aendelee kuwaumbua viongozi wa serikalini kwa maovu waliyokuwa wakiyafanya.
Alijua mambo mengi, watu waliokuwa wakimfuata inbox na kumtumia meseji walimwambia mambo mengi kuhusu viongozi wa serikali ilivyokuwa ikiwatumia wachungaji, maaskofu kwa ajili ya kuwaibia wananchi pesa.
Hakutaka kuliingilia suala hilo kwa pupa, kitendo cha kuwazungumzia wachungaji ilikuwa ni kama kuizungumzia dini fulani au kundi kubwa la watu fulani. Alitaka kufanya uchunguzi wake, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutafuta namba za wachungaji na maaskofu hao, wala hakupata tabu, akazipata na kisha kuzidukua ili aweze kunasa mazungumzo yao, na cha zaidi alichokifanya ni kudukua barua pepe zao.
***
Kwenye barua pepe hizo ndipo Godwin alipopata kila kitu alichokuwa akikihitaji, aliuona uovu mkubwa uliokuwa ukifanyika kwa wachungaji hao. Hakutaka kuvumilia, watu wengi walikuwa wakiangamia pasipo kujua kwamba watumishi hao wa Mungu walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuwachukulia pesa zao.
Alitaka kuweka kila kitu wazi, alitaka Tanzania na dunia nzima ifahamu kile kilichokuwa kikiendelea hivyo kuwaambia Watanzania kwamba alikuwa akitaka kuzitoa taarifa hizo, tena zikiambatana na ushahidi mkubwa mpaka watu ambao walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuhakikisha kwamba baadhi ya viongozi serikalini walikuwa wakitumika kwa ajili ya kuwaibia wananchi.
“Nitaanza na Mchungaji Peter Kibatari,” alianza kuandika Godwin na baadaye kuweka picha ya mchungaji huyo na kuandika mambo mengi kuhusu huduma yake, jinsi alivyokuwa akitumika na viongozi wa serikali.
Kila mtu aliyekuwa na simu yake mkononi, alikuwa akisoma kila kitu kilichokuwa kimeandikwa. Kila mmoja alimfahamu mchungaji huyo, alikuwa ni mtu mwenye nguvu nchini Tanzania, alipokuwa akihubiri kitu chochote kile kila mtu alikuwa makini kumsikiliza.
Wakati mwingine, watu walikuwa wakitoka nyumbani kwao na kwenda kusikiliza mahubiri kanisani kwake. Alijua kucheza na akili za watu, alikuwa na usanii mkubwa ambao hakukuwa na mchungaji mwingine aliyekuwa nao.
Aliwachanganya watu, alipendwa, alikuwa mtu aliyezungumziwa, kitu cha kushangaza kabisa, kila kiongozi serikalini alikuwa akimzungumzia kwa mazuri, kila kitu kilichokuwa kikizungumziwa juu ya mchungaji huyo, kilizungumziwa kwa uzuri tu.
Watu hawakujua kilichokuwa kikiendelea, hawakujua siri iliyokuwa nyuma ya pazia. Televisheni ya Taifa ndiyo ilikuwa ikimtangaza kila siku kwamba alikuwa mchungaji mwenye nguvu ambaye alitakiwa kusikilizwa na kila mtu.
Maneno mengi ya kisiasa, kuingilia burudani na kuzungumzia kuhusu viongozi wengine wa siasa kuliwafanya hata Waislamu wengine nao kwenda kanisani kwake kusikiliza mahubiri, si kwamba walitaka kuingia katika dini nyingine bali walichokitaka ni kwenda kusikiliza siku hiyo mchungaji huyo alikuwa na umbeya gani.
Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba mchungaji huyo alikuwa akitumika. Serikali ilimtumia, watu zaidi ya elfu tano walikwenda kanisani kwake kila Jumapili, mapato ya sadaka yaliyokuwa yakipatikana yaligawanywa kwa viongozi mbalimbali ambao wao ndiyo waliokuwa wakihusika kumletea washirika wengi.
Viongozi hao wakawa wakinunua magari ya kifahari na kuyaingiza nchini kupitia kanisa la mchungaji huyo, biashara zote haramu kama madawa ya kulevya yalikuwa yakiingizwa nchini kupitia kivuli cha kanisa hilo, mizigo haikuwa ikikaguliwa, ilipita na kila mtu alipokuwa akiuliza, aliambiwa ni msaada kutoka nchini Marekani kwa ajili ya kanisa la Praise And Worship la Mchungaji Kibatari.
“Whaaaat?” (nini?) aliuliza jamaa mmoja, hakuwa akiamini alichokuwa akikiona, yeye mwenyewe alikuwa mshirika mzuri wa kanisa hilo.
“Kumbe Kibatari naye ni mtumishi wa serikali, na si mtumishi wa Mungu kama tunavyojua! Mungu wangu! Ni nini tena hii?” aliuliza mwanamke mmoja.
Kanisa la Praise And Worship likawa limechafuka, kila mshirika wa kanisa hilo akajitokeza na kuweka maoni yake hadharani. Mchungaji Kibatari ambaye alizoea kupigiwa promo kila siku akajitokeza na kuanza kujitetea lakini kujitetea kwake hakukuwa na nafasi hata kidogo kwa kuwa kila siku ushahidi ulikuwa ukiwekwa katika akaunti ile kwamba alikuwa akitumika.
“Kumbe hata Lucy si mke wake!” alisema jamaa mwingine, wote walijiuliza, kila siku mchungaji huyo alimtambulisha mwanamke aitwaye kwa jina la Lucy kama mkewe, kumbe hakuwa mkewe bali ni mwanamke aliyepewa kwa ajili ya kuwa naye kwa lengo la kuangalia mapato ya kanisa kila yalipokuwa yakiingia.
“Jamani! Kweli Lucy si mkewe?” aliuliza mtu mwingine.
Ili kuwaaminisha kwamba kila kitu kilikuwa ni ukweli, Godwin akaweka picha za mwanamke huyo akiingia katika nyumba nyingine nyakati za usiku kuonyesha kwamba alikuwa akienda kulala, kama kweli alikuwa mke wa Mchungaji Kibatari, kwa nini usiku alikuwa akieka kulala nyumba nyingine?
Kulikuwa na walinzi wanne wa nyumbani kwa Kibatari ambao walikufa katika vifo vya kutatanisha! Hakukuwa na mtu aliyejua kwamba walinzi hao waliuawa kwa kuwa walitaka kutoa siri kwamba Lucy hakuwa mke wa Mchungaji Kibatari? Yaani kila kitu alichokuwa akikiandika Godwin, watu walishangaa mpaka wengine kufikia hatua ya kutotaka kwenda kanisani tena.
“Siwezi kwenda kanisani. Nilidhani nahubiriwa na mchungaji kumbe nahubiriwa na mhuni! Sirudi tena kanisani pale,” alisema mwanamke mmoja huku akionekana kukasirika hasa.
Siri hazikuwa hizo tu, Godwin aliendelea kuzitoa nyingi kuhusu mchungaji huyo, jinsi alivyokuwa akiwatumikia viongozi wa serikali na kuonekana kwamba alikuwa na nguvu kubwa, watu waliokuwa wakianguka mapepo kanisa, walitengenezwa kwa malipo makubwa.
Kwa kuwa kila alipokuwa akifanya mambo mengi makubwa alizungumziwa katika mitandao ya kijamii, hata alipogundulika kwamba alikuwa msanii pia aliandikwa sana katika mitandao hiyohiyo.
Jumapili ya kwanza tangu kashfa kubwa ilipoanza kuzungumziwa kwenye mitandao, hakutaka kwenda kanisani, alijifanya kuumia na hivyo kuomba udhuru kwamba alitaka kusafiri kuelekea nchini Israel kwa ajili ya kumuomba Mungu wake kwani kama kudhiakiwa, alidhiakiwa sana na ulikuwa muda wa Mungu wake wa Mbinguni kumsafisha.
Ilikuwa ni aibu, alipokuwa uwanja wa ndege kwa ajili ya kuondoka kuelekea nchini humo, watu walikuwa wakimwangalia, walimshangaa, hakuonekana kuwa kama mtumishi wa Mungu tena bali alionekana kuwa kama kituko cha mwaka, mtu ambaye alipambana usiku na mchana kuhakikisha anaingiza pesa kwa kutumia migongo ya viongozi wa serikali na kanisa ambalo kila siku alikuwa akiling’ang’ania.
“Nimechafuka sana,” alikuwa akizungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani, Godfrey Kamau ambaye naye alikuwa akimtumia mchungaji huyo kuingiza magari bandarini kwa kutumia kivuli cha kanisa lake.
“Pole sana. Nimeona jinsi yule mtu anavyokuchafua, huu ni wakati ambao hutakiwi kuteteleka,” alisema Kamau.
“Nitapambana na huyu mtu!”
“Utapambana naye? Utaanzia wapi? Hajulikani, halafu inaonekana ni mtu mwenye nguvu sana, kama utaweza kumuomba Mungu na kukuonyeshea mtu huyo, jua tutakuwa nyuma yako,” alisema Kamau wakati alipokuwa akizungumza na Mchungaji Kibatari kwenye simu pasipo kujua kama mazungumzo yao yalikuwa yakidukuliwa na Godwin na kuyarusha moja kwa moja katika akaunti yake kwenye Mtandao wa Instagram.
“Nitamjua tu!” alisema Kibatari na kukata simu.
Kila kitu ambacho walikizungumza kwenye simu, dakika arobaini zilikuwa nyingi sana kuyaona mazungumzo yao kwenye akaunti ile. Kila mmoja alishangaa, wakagundua kwamba simu zao zilikuwa zimedukuliwa na hivyo kuwasiliana na Kampuni ya Simu ya Alcatel na kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea.
Watu wa kampuni hiyo ya simu hawakujua kilichokuwa kikiendelea, hawakujua kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akidukua mawasiliano ya wateja wao. Wakawasiliana na wataalamu kutoka Afrika kusini ambayo nao wakaingia kwenye system kuona kama kulikuwa na mtu alikuwa na uwezo wa kudukua mawasiliano ya wateja wao, hawakubahatika kuona lolote lile.
“Ila Mchungaji Kibatari anasema kwamba mawasiliano yake na mheshimiwa waziri yalidukuliwa. Hebu ingia kwenye akaunti ya Mabadiliko ya Kweli,” alisema mkurugenzi wa kampuni hiyo.
Akaingia na kuangalia, posti alizokutana nazo huko zilihusu mawasiliano baina ya watu hao wawili. Walichanganyikiwa, hawakujua ni kwa namna gani mtu huyo alikuwa ameingia kwenye mitambo yao na kudukua mawasiliano hayo.
Wakati mitandao ya simu ikisumbuka kuziba udukuaji wa mawasiliano ya wateja wao, usalama wa taifa walikuwa mitaani wakimtafuta Godwin. Hawakumfahamu mtu huyo, walikuwa na kazi kubwa mno mbele yao. Kila walipokuwa, waliwaambia watu wawasaidie kumtafuta mtu aliyekuwa akitumia akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ambayo kwao ilionekana kama kuibua vuguvugu la vurugu nchini Tanzania.
“Hakikisheni kwamba mnafanya kila liwezekanalo huyo Godwin anapatikana. Sawa?” alisema mkurugenzi wa usalama wa taifa.
“Sawa.”
Wakati wao wakiendelea kumtafuta Godwin, mwanaume huyo aliendelea kujichimbia, hakutaka kugundulika kwamba yeye ndiye alikuwa mtumiaji wa akaunti hiyo.
Alikuwa mtu wa kushinda Tandale huku kila kitu alichokuwa akikifanya akikifanya chumbani kwake. Baada ya kukaa kwa wiki mbili ndipo alipoamua kuwa mpiga debe katika Kituo cha Daladala cha Makumbusho.
Hakukuwa na mtu aliyemfahamu, alikuwa mgeni kituoni hapo, alionekana kuwa kijana mwenye njaa kali, aliyechoka ambaye mwili wake huku mwili wake ukiwa dhaifu.
Alikuwa mchangamfu, aliyeongea sana, kila siku alipokuwa kituoni hapo alivalia kipensi kichafu, nywele timtim, chini alivaa kandambili zilizokuwa zimechoka huku wakati mwingine vipensi vya jinsi alivyokuwa akivivaa akivifunga kamba badala ya mkanda.
Ilikuwa ni vigumu kujua kwamba huyo ndiye alikuwa kijana aliyewanyima usingizi viongozi wa nchi na viongozi wa dini. Alitafutwa pasipo kujulikana alikuwa vipi. Akaanza kuzoeleka katika kituo hicho, hakuona kama kulikuwa na tatizo lake kujitambulisha kwamba alikuwa akiitwa Godwin, kwa jinsi alivyokuwa, ilikuwa vigumu sana hata kugundua kama mwanaume huyo alikuwa amesoma.
Hayo ndiyo yakawa maisha yake kila siku. Aliendelea kuwatesa viongozi, alionekana kuwa shujaa mkubwa, Watanzania wengi wakataka kumfahamu kwamba alikuwa nani, walitaka kumpongeza, hawakujua kama mtu huyo kila siku walipishana naye katika kituo hicho na hata wakati mwingine kumtukana kila alipowaletea utani wasichana.
Alipokuwa akiendelea kupiga debe katika kituo hicho ndipo alipokutana na msichana aliyeitwa Winfrida, msichana mrembo aliyekuwa akiwatetemesha wanaume wengi chuoni alipokuwa akisoma.
Hakujua lolote kuhusu msichana huyo, hakujua kama alikuwa akimpenda mpaka siku ambayo msichana huyo alimwambia ukweli. Kwanza akacheka sana, ilikuwaje msichana mrembo kama huyo ampende mwanaume kama yeye, mchafu, asiyekuwa na pesa, wakati mwingine akahisi kwamba inawezekana Winfrida alikuwa ofisa wa usalama wa taifa, akakubaliana naye kishingo upande na hivyo kuanza uhusiano wa kimapenzi, ila alikuwa na tahadhari kubwa mno kwani hakutakiwa kumwamini kila mtu.
***
Madaktari katika Hospitali ya Ganga nchini India walikuwa wakibadilishana ndani ya chumba alichokuwa amelazwa Rais Bokasa. Walikuwa wakihangaika kuhakikisha afya ya rais huyo inarudi na kuwa katika hali ya kawaida. Alikuwa kimya, tangu alipofikishwa hospitalini hapo hakuwa akizungumza kitu chochote kile, aliyafumba macho yake na kitu pekee ambacho kiliwaambia kwamba alikuwa hai ni mapigo ya moyo yaliyokuwa yakidunda kwa chini mno.
Mke wake, Bi Consolatha alikata tamaa, hakuona kama mume wake angeweza kufumbua macho yake tena kwani tangu alipokuwa ameanguka na kupoteza fahamu, mpaka siku hiyo alikuwa hivyohivyo, yaani kitandani pale alikuwa kama alivyokuwa ameingia.
Siku ziliendelea kukatika, madaktari walikuwa wakiifuatilia afya yake kwa ukaribu sana. Pale alipokuwa ameanguka, aliumia vibaya kichwani mwake, akatoka damu ambayo iliganda kwa kiasi kidogo katika ubongo wake na hivyo kuwa na hatari ya kupata ugonjwa mmoja kati ya magonjwa matatu.
“Inawezekana atapata kifafa, atapooza mwili wake au kusahau milele kila kitu kilichokuwa kimetokea maishani mwake,” alisema daktari huku akimwangalia Bi Consolatha pamoja na maofisa wa usalama waliokuwa wameongozana naye huko India.
“Jamani mume wangu!” alisema Bi Consolatha huku akilia.
“Tunajitahidi sana, tuna uhakika kwamba hatokufa lakini anaweza kupata tatizo moja kati ya hayo niliyowaambia,” alisema daktari.
“Daktari! Nini kinaendelea?” aliuliza Rais Bokasa mara baada ya kufumbua macho.
Kilichomfahamisha kwamba hapo palikuwa ni hospitali ni mavazi waliyokuwa wamevalia madaktari hao pamoja na kitanda alichokuwa amekilalia. Aliangalia kwa juu aliiona dripu ikiwa inaning’nia.
Hakujua kitu gani kilitokea mpaka kuwa mahali hapo lakini baada ya sekunde kadhaa, akaanza kukumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea. Aliikumbuka meseji aliyokuwa ametumiwa kwamba kiasi cha dola milioni mia moja kilichukuliwa kutoka kwenye akaunti yake iliyokuwa nchini Uswisi, moyo wake ulimuuma mno na hapohapo kitandani alipokuwa akaanza kulia.
Alirudiwa na fahamu lakini mwili wake ukawa na tatizo kubwa la kupooza. Alijaribu kuunyanyua mkono na mguu wake wa kulia lakini vilishindwa kuinuka, alihisi kama kulikuwa na mtu alikuwa amevikandamiza, alishangaa, alijaribu mara kwa mara lakini akashindwa kufanya hivyo.
“Nimepooza! Daktari nimepooza,” alisema Rais Bokasa huku akianza kulia kitandani pale alipokuwa.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli wenyewe, kwenye matatizo aliyosema daktari, tatizo la kupooza lilikuwa mojawapo, alishindwa kufanya kitu chochote kile kwa upande wa kulia. Moyo wake ulimuuma, hali hiyo ilimaanisha kwamba kwa miaka yote mpaka kifo chake maisha yake yangekuwa juu ya kiti cha walemavu.
Alilia sana, hata alipomuona mke wake, hakuacha kulia, moyo wake uliumia sana, wakati mwingine alibaki akimuomba Mungu kitandani pale kwa kumtaka kubadilisha kila kitu kwamba maisha yake halisi yaliyokuwa yakiendelea basi yawe ndoto moja ya kusisimua ambapo baada ya muda fulani ashtuke kutoka usingizini.
“Mungu! Fanya kitu, nifanyie muujiza, wewe ni mponyaji, naomba uniponye Mungu wangu,” alisema Rais Bokasa pale kitandani. Kwa kipindi cha shida kama hicho ndicho kilikuwa kipindi cha kumkumbuka Mungu wake.
****
Godwin alihisi kwamba msichana aliyeanza kuzoeana naye alikuwa ni miongoni mwa maofisa wa Usalama wa Taifa. Hakutaka kuzungumza naye sana, kila alipokuwa akimfuata, msichana huyo alikuwa akimbugudhi kwa kumwambia maneno mengi ambayo hakutaka kujali kabisa.
Kila siku Winfrida alikuwa akifika hapo Makumbusho na kutaka kuzungumza naye, haikuwa kazi nyepesi kumzoea Godwin kwani alimuona kila mtu mbele yake akiwa adui mkubwa ambaye alikuwa akimtafuta kwa udi na uvumba.
Alihitaji muda mwingi kumzoea msichana huyo aliyekuwa akisomea mambo ya biashara katika chuo kimoja jijini Dar es Salaam. Marafiki zake waliokuwa katika kituo hicho cha Makumbusho walimuona kuwa mmoja wa watu waliokuwa na bahati kubwa, hawakuamini kama kungekuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa Winfrida kutokea kumpenda Godwin ambaye kwa kumwangalia tu, muonekano wake ulionyesha kwamba alikuwa mhuni asiyekuwa na mbele wala nyuma.
“Ninataka kuzungumza na wewe,” alisema Winfrida huku akimwangalia Godwin aliyekuwa kimya akimwangalia.
“Kuhusu nini?”
“Ninahitaji muda wa kukaa na wewe sehemu. Ninahitaji kuzungumza sana na wewe,” alisema msichana huyo huku akimwangalia Godwin aliyekuwa akionekana kushangaa sana.
“Sina muda.”
“Nakuomba.”
“Kweli sina muda. Unaweza kuniacha nikatafute pesa kwanza?” aliuliza Godwin huku akisimama.
Hakuwahi kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na msichana yeyote yule zaidi ya mwanamke mtu mzima Bi Rachel ambaye mpaka kipindi hicho hakujua mwanamke yule alikuwa akiendeleaje, kama alikuwa hai au alikufa pale hospitalini alipokuwa amemuacha.
Wakati Godwin akiondoka, moyo wa Winfrida ulikuwa ukimuuma sana, hakuamini kama mwanaume huyo alikuwa akiondoka pasipo kumsikiliza alichotaka kumwambia wakati huo, akaondoka mpaka kulipokuwa na magari ya kwenda Gongo la Mboto na kuanza kuita abiria.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake ya kila siku, Winfrida hakukoma, kila siku ilikuwa ni lazima kufika mahali hapo na kutaka kuzungumza na Godwin. Mwanaume huyo alikasirika, alimchoka Winfrida kwani kila alipokuwa akija, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutaka kutumia muda mrefu kuwa naye tu.
“Unanikera!” alisema Godwin, hakutaka kumficha msichana huyo.
“Najua! Nisamehe tu ila ninakupenda sana,” alisema Winfrida huku akimwangalia Godwin.
“Unanipenda mimi?”
“Ndiyo!”
“Hivi nilivyo?”
“Mapenzi hayachagui Godwin. Naomba unipende!” alisema Winfrida.
“Siwezi!”
“Nakuomba Godwin. Nakuomba unipende,” alisema msichana huyo, tayari machozi yakaanza kumtoka.
“Nimesema haiwezekani!”
Huo ulikuwa msimamo wake, hakutaka kuwa karibu na msichana huyo hata kidogo. Kila aliporudi nyumbani kwake, alijifungia ndani huku akiwa na rundo la magazeti na kuanza kuyasoma huku akisikiliza mawasiliano ya siri ya namba za simu alizokuwa amezidukua ambazo alikuwa akizirekodi kusikiliza kila kitu kilichokuwa kikiendelea wakati yeye alipokuwa kazini kwake.
“Vijana bado wanaendelea kumtafuta. Halafu nimepata taarifa kwamba vijana wa FIS (The Federal Intelligence Service) walikuwa wameingia nchini Tanzania tayari kwa kuanza kazi yao,” alisikika mkurugenzi wa Usalama wa taifa akimwambia waziri mkuu.
“Safi sana! Sasa hili jambo lisitoke, hutakiwi kumwambia mtu yeyote,” alisikika waziri mkuu.
“Haina shida mkuu!”
Godwin alijua kwamba watu hao walifika nchini Tanzania kumtafuta yeye, si kwa sababu alikuwa akitumia akaunti hiyo bali ni kwa sababu alizihamisha pesa hizo kwenda kwenye akaunti moja nchini Marekani.
Hakutaka kuchelewa, muda huohuo akaingia Instagram na kuwaambia wafuasi wake kwamba kulikuwa na wapelelezi kutoka nchini Uswisi ambao walifika Tanzania kwa ajili ya kumtafuta lakini kamwe wasingeweza kumpata hata kidogo.
Kila mtu alishangaa, mambo hayo yalitakiwa kufanyika kisiri lakini tayari mhusika aliyekuwa akitafutwa tayari alifahamu kila kitu. Watu wengine walishangaa lakini viongozi wengi wakajua kwamba mtu huyo alikuwa amedukua mawasiliano ya waziri mkuu na mkurugenzi wa usalama wa taifa, kumzuia Godwin kupata taarifa lilikuwa jambo gumu sana.
Hakutaka kuishia hapo, ilikuwa ni lazima aendelee kuwaumbua wachungaji wengine, hakuacha, aliwataja wachungaji wengine waliokuwa wakihusika katika kushirikiana na baadhi ya viongozi wakiwemo mawaziri kuwaibia Watanzania pesa zao huku wakati mwingine mtafaruku mkubwa ukitokea baina ya mchungaji na mchungaji mara baada ya kuona wakizidiana katika wingi wa washirika.
****
Kwa kilichokuwa kimetokea, jinsi Godwin alivyokuwa amewachoma wachungaji wengi, washirika wakaanza kupungua makanisani na wengine kuacha kabisa kuelekea huko. Ilikuwa ni sifa mbaya kwa kanisa kwa ujumla, kila mtu alishangaa kwamba ilikuwaje wachungaji waliokuwa wakiwaamini kila siku, kuwatolea mafungu ya kumi na zaka kufanya mambo ya kijinga kama hayo.
Ilikuwa ni vita kubwa, wachungaji wengine wakaamua kuondoka Tanzania na kukimbilia nchi nyingine kujificha, hakukuwa na mchungaji aliyetamani kubaki nchini Tanzania, kila mtu aliondoka kuyaokoa maisha yao kwani tayari kulikuwa na baadhi ya wananchi walikuwa wamepaniki mpaka kufikia hatua ya kutaka kuwamaliza wachungaji hao.
Wakati kila kitu kikionekana kwenda shaghalabaghala hapo ndipo mkurugenzi wa usalama wa taifa akaja na wazo moja kwamba watu wote waliokuwa na jina linaloitwa na Godwin walitakiwa kutekwa kinyemela na kupelekwa sehemu fulani ambapo huko walitakiwa kufanyiwa mahojiano.
Waliamini kwamba kwamba sababu Godwin alikuwa akijiamini kwamba asingeweza kukamatwa ilikuwa ni lazima kutumia jina lake kama kawaida kwa kuwa tu kulikuwa na watu wengi waliokuwa na jina hilo.
Msako huo ukaanza kufanyika kimyakimya. Vijana wengi waliokuwa na jina hilo kwenye mitandao ya kijamii wakaanza kutekwa na kushirikiwa ambapo huko walipolekwa kulikuwa na maswali mengi waliyokuwa wakihojiwa na wakati mwingine wakipigwa ili kusema wao walikuwa wakina nani na kwa nini walikuwa wakiisumbua serikali hiyo.
Rundo la vijana wenye jina hilo walikuwa wakitekwa. Hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua sababu ya vijana hao kupotea ghafla kwani kila kilichokuwa kikiendelea kilifanyika kimyakimya mno. Vyuoni, mitaani na sehemu zingine zote watu waliokuwa na jina la Godwin ilikuwa ni lazima kupotea mazingira ya kutatanisha.
“Kwa Dar es Salaam tuna Godwin mia saba mpaka sasa hivi,” alisema jamaa wa usalama wa taifa.
“Ni wote?”
“Hapana ndiyo tunaendelea kuwatafuta wengine.”
“Basi sawa.”
Godwin hakujua kilichokuwa kikiendelea. Siku moja akiwa katika kituo cha Daladala cha Makumbusho akiendelea na mambo yake akashangaa wanaume wawili waliokuwa na miwani ya jua wakija pale alipokuwa amekaa, hata kabla hajauliza swali lolote lile, mwanaume mmoja akamshika mkono na kumvuta pembeni.
“Jamani kuna nini?” aliuliza Godwin kwa sauti ya kisela tena huku akiwa na kipensi chake na sikioni akiwa na sigara.
“Twende huku!”
“Wapi masela! Mbona mnanishika kibabe washikaji?” aliuliza Godwin huku akiwashangaa watu hao, tayari alihisi kwamba walikuwa usalama wa taifa.
Wakati akiwa anauliza maswali zaidi, akashangaa kuona gari moja aina ya Noah ikija kule alipokuwa, mlango ukafunguliwa, akasukumiwa ndani ya gari na kuondoka mahali hapo huku kila mmoja akishangaa kwamba ilikuwaje mshikaji wao wa nguvu akamatwe kibabe namna ile.
***
Thomas First na Bruno Mendez wakaingia nchini Tanzania kama wapelelezi waliotumwa kutoka nchini Uswis na kwenda Tanzania kwa ajili ya kumtafuta mtu aliyekuwa amehamisha pesa kutoka katika akaunti ya Rais Bokasa na kwenda kwenye akaunti ya hospitali ya St. Lucas nchini Marekani.
Hakukuwa na mtu aliyejua chochote kuhusu watu hao, walionekana kuwa wa kawaida ambapo vibali vyao vyote vilionyesha kwamba waliingia nchini Tanzania kwa ajili ya kutembelea mbuga mbalimbali za wanyama.
Hapo uwanja wa ndege wakachukua teksi ambayo iliwapeleka moja kwa moja mpaka katika Hoteli ya Jumanji iliyokuwa Posta Mpya na kutulia hapo. Vichwa vyao vilikuwa vikifikiria kazi kubwa iliyokuwa mbele yao, hawakujua pa kuanzia lakini waliamini kwamba kama wangekutana na maofisa wa usalama wa taifa basi ingekuwa kazi nyepesi mno kujua ni kit gani walitakiwa kufanya.
Wakakaa katika vyumba tofauti ila kwa kuwa walikuwa na mengi ya kuzungumza, wakatumia chumba kimoja na kuanza kujadili ni kitu gani walitakiwa kufanya. Hawakujua Kiswahili ila kwa kuwa akaunti ya Mabadiliko ya Kweli ilikuwa hewani na ilikuwa ikifanya kazi kama kawaida, wakataka kuitumia kumpata mtu wao.
Ilionyesha kwamba mtumiaji huyo alikuwa nchini Uingereza, walijua kwamba taarifa hizo hazikuwa sahihi hivyo walichokuwa wakikitaka ni kujua kwanza namba iliyokuwa ikitumika ilikuwa eneo gani kwa kipindi hicho.
“Kwenye hii akaunti ameweka namba yake ambayo inatumiwa na kila mtu anayetaka kumtumia taarifa, nadhani tukianza na hii tunaweza kufanikiwa,” alisema Bruno.
Katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli, Godwin aliweka namba ya simu ambayo ilitumika kwa watu waliokuwa mbali naye kumtumia taarifa za ukweli juu ya kitu kilichokuwa kikiendelea wakati wowote ule, kwa kupitia namba hiyo ya Kimarekani, alitumiwa picha na taarifa zingine ambazo hakuwa akizifahamu.
Alichokifanya Bruno ni kupiga picha na kisha kuituma katika namba hiyo, alipohakikisha kwamba picha imetumwa, akapiga simu mpaka Uswisi ambapo akaomba wawasiliane na watu wa mtandao wa WhatsApp na kuwaambia kuhusu namba ile na picha iliyokuwa imetumwa.
Hilo halikuwa tatizo, mawasiliano yakafanyika. Mara ya kwanza WhatsApp walipoambiwa walikataa kwani hawakutaka kabisa kutoa taarifa za mteja wao yeyote yule, waliwaambia hivyo kwa kuwa hata siku chache zilizopita kampuni ya Apple ilikutana na suala hilohilo la kutoa taarifa za mteja wao katika suala zima la kigaidi lakini wakakataa kufanya hivyo.
Waliwabembeleza mno, tena wakati mwingine kumtumia rais wao na kuwaambia ni kwa jinsi gani walikuwa wakimuhitaji mtu huyo ambaye alionekana kuwa hatari kupita kawaida kwa kufanya muhamala wa kifedha pasipo kibali cha mwenye akaunti.
Baada ya kuambiwa hivyo, WhatsApp wakakubaliana nao na kuwafanyia kile walichotaka kukipata. Wakapewa taarifa kwamba mtumiaji wa namba hiyo hakuwa nchini Marekani kama ilivyokuwa ikionyesha bali alikuwa barani Afrika, nchini Tanzania katika Jiji la Dar es Salaam.
“Dar es Salaam kubwa sana. Tutampataje sasa?” aliuliza Thomas.
“Subirini akifungua picha tutajua yupo wapi. Ila taarifa za mwisho zinaonyesha kwamba yupo ndani ya Jiji la Dar es Salaam.
“Sawa. Tunasubiri!”
“Haina shida.”

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumamosi hapahapa.
 
Daah Godwin jamani mwisho wako utakuwaje
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom