New Habari wanajifunza kutoka kwa mmiliki wao maana kwenye nyaraka tata anajiita Rustam, Rostamu, Rastam n.k Hakya nani humfikishi mahakama yoyote wala huwezi kutaifisha mali zake maana Rostam hamiliki kitu lakini ndio "Rais"
Asema wamekodi Al Shabaab kummaliza
*Ahusisha mganga wa kienyeji, Sheikh maarufu
*Amwandikia IGP Mwema barua kurasa saba
*Wasomi, wanasiasa wamshangaa, wambeza
Na Waandishi Wetu
JESHI la Polisi limejipanga kumhoji Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, baada ya ameibua tuhuma nzito dhidi ya Polisi, Usalama wa Taifa, wanasiasa, wafanyabiashara na waganga wa kinyeji, akidai kwamba wamepanga kumuua.
Katika orodha hiyo, pia amewahusisha watu kadhaa anaodai kuwa ni Wasomali kutoka katika kundi la Al Shabaab.
Kuhojiwa kwa mwanasiasa huyo kunatokana na taarifa yake ya maandishi aliyoipeleka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema, Februari 9, mwaka huu.
Mwanasiasa huyo ameeleza mlolongo mrefu wa kishirikina ambao anadai kwamba umefanywa ili kuwapumbaza Watanzania wote baada ya yeye kuuawa ili wasiwe na akili ya kuhoji mauaji hayo.
Uchunguzi wa MTANZANIA umebaini kuwa Februari 8, mwaka huu, Dk. Mwakyembe alizungumza na baadhi ya viongozi waandamizi wa Jeshi la Polisi katika Makao Makuu ya Jeshi hilo jijini Dar es Salaam. Hata hivyo, Polisi walimtaka aweke madai yake kwenye maandishi.
Siku moja baadaye, Dk. Mwakyembe aliwasilisha taarifa yake ya maandishi. MTANZANIA imefanikiwa kuipata taarifa hiyo kutoka kwa baadhi ya wasaidizi wake wizarani ambako iliandaliwa. Ina nembo ya Serikali na anuani ya Wizara ya Ujenzi. Baadhi ya watu wanaotajwa kwenye taarifa hiyo tumehifadhi majina yao kwa sababu za kitaalum kwa kuwa bado MTANZANIA inaendelea kuwasiliana nao ili kupata ukweli.
Dk. Mwakyembe amesema kwenye barua hiyo, Pamoja na kwamba taarifa hii ni mpya yenye matukio ya takriban mwezi moja tu, naamini kwa dhati kuwa msingi wake (kwa maana ya wahusika na maudhui) hautofautiani na ule wa matukio mengine ya awali ambayo baadhi yake yalisharipotiwa Polisi na vyombo vingine vya usalama kwa lengo la kuchunguzwa.
Maelezo ya Barua ya Mwakiembe
Bado nina imani kubwa na Jeshi letu la Polisi kwamba litaifanyia kazi taarifa hii bila kujali nguvu ya ukwasi na ya kisiasa ya watuhumiwa na kwa kuzingatia misingi ya haki na ukweli.
Msingi wa mimi kushtuka na kuamua kulivalia njuga suala hili kwa kuwataarifu watu mbalimbali wenye uelewa na kuvitaarifu vyombo vya dola, ni taarifa nilizozipata kutoka Songea tarehe 22/01/2011 kuhusu kundi la watu saba lililoingia mjini humo usiku wa tarehe 21/01/2011 kwa gari iliyodaiwa kuwa ya Wizara yangu (Ujenzi) aina ya Land Cruiser yenye usajili nambari STK 686 (ambayo kipindi fulani katika safari hiyo ilibadilishwa namba yake kuwa STK 6869). Gari hiyo iliwateremsha abiria hao saba sehemu iitwayo Madaba na baadaye kuchukuliwa na gari nyingine (Hardtop Land Cruiser yenye namba za usajili T76 BDU) hadi Top Inn ya mjini Songea.
Majina ya baadhi ya watu hao saba ni: Wasomali wawili Hafidh na Faraj; kijana wa Kichagga kwa jina Mustafa a.k.a Master, Mkusa, jamaa ambaye wenzake wanaamini kuwa yuko Usalama wa Taifa; na (jina tunalo) kutoka Tanga anayedaiwa kuwa na utaalamu mkubwa wa kukaba watu.
Mwenyeji aliyewapokea Songea watu hao saba ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya akiongozana na mtu aitwaye Manya. Kilichowafanya baadhi ya watu waanze kulidadisi kundi hili, ni dhamira ya safari yao. Tetesi zilisema walikuwa wanaelekea Mbunde, kwa mganga maarufu wa kienyeji kwa jina Majungu. Hivyo, udadisi ukaongezeka kujua nani anakwenda kulogwa safari hii. Tetesi zikarejea na jina langu na msululu wa majina mengine: Dk. Slaa (Wilbrod), Anne Kilango- Malecela, Reginald Mengi, Profesa Mwandosya na Benard Membe.
Akana kuamini ushirikina huku akiuhofia
Pamoja na kwamba sina imani na ushirikina au nguvu za giza, kutajwa kwa jina langu na fursa ya pekee niliyokuwa nayo ya kujua kilichokuwa kinafanyka, kukanipa ari, nguvu na shauku ya aina yake kutaka kulielewa zaidi suala hili ili ikibidi, niwataarifu wenzangu nao waelewe.
Usiku wa Jumamosi tarehe 22/01/11 kundi hilo lilielekea Mbunde, wilayani Namtumbo (kwa gari aina ya Defender STK 265 , likiendeshwa na (jina tunalo) kukutana na mganga Majungu ambaye anaishi ndani ya Selous Game Reserve with impunity. Defender hiyo iligeuza kurejea Songea siku mbili baadaye na kuwaacha wageni hao kwa mganga ambako walikaa siku saba wakitengenezwa. Walirejea Songea tarehe 29/01/11 na kesho yake tarehe 30/01/11 wakaanza safari ya kurejea Dar es Salaam.
Kutoka Songea hadi Mafinga walitumia ile Hard Top iliyowatoa Madaba hadi Top Inn ya Songea (T76 BDU). Walifika Mafinga milango ya saa mbili usiku na kukuta gari mbili zikiwasubiri: Hilux Mayai ya (kampuni moja) na Defender iliyowaongoza hadi Morogoro. Walipokewa Morogoro na askari (jina tunalo). Hapo kundi likagawanyika: watu wanne wakiwemo wale Wasomali wawili wakaingia kwenye Nissan Patrol (T84 ADH) mali ya (kampuni jina tunalo) na wengine wakabaki Morogoro.
Kufuatana na mganga Majungu mwenyewe, ambaye wapelelezi wako wanaweza kuongea naye kama walivyofanya walionipa taarifa hizi, aliwapa masharti ya kutotumia silaha za moto ila njia nyingine kumuua kwanza Mwakyembe, baadaye Slaa, n.k., n.k, n.k. kwa zamu; alitengeneza dawa ya kuwapooza wale wengine (wanaosubiri) kwenye orodha ya kuuawa (Dk. Slaa, Anne Kilango, Mengi, Mwandosya na Membe) wasitaharuki na kupiga kelele za nguvu hata kuamsha hasira za wananchi mauaji yakitokea; aliwazindika vilivyo wasiweze kudhuriwa na tendo la kuua na alitengeneza dawa ya kuwapumbaza waliohukumiwa kifo (wawe mfano wa mbwa mbele ya chatu).
Jijini Dar es Salaam wahitimu hao wa Profesa Majungu walifikia Kiwalani karibu na kiwanda cha Mohamed Enterprises. Jirani na kiwanda hicho kuna jengo la ghorofa: chini ni msikiti wa Waarabu unaoitwa Malkaz na juu ni sehemu ya kuishi. Tarehe 05/02/11, wageni wawili zaidi waliwasili kwa ndege kutoka Uganda; mwanaume mmoja (aliyechanganya rangi) na mwanamke mmoja (mweusi vilivyo). Walipokewa na gari mbili; moja ya Polisi (PT 028 ) na ya pili yenye namba za kibalozi (aina ya RAV 4).
Aelezea ushiriki wa Al Shabaab
Jioni wakawa na mazungumzo ya kina na Wasomali wawili niliowaelezea awali ambao inadaiwa ni wapiganaji wa Harakat al-Shabaab al-Mujahideen (kwa kifupi Al-Shabaab).
Aelezea
Niliweza kupata picha pana zaidi kwa nini wapiganaji wa kikundi hicho (kinachopambana na wanaodhaniwa kuwa maadui wa Uislamu) wameingizwa nchini. Nimeweza kukusanya taarifa zinazodai kuwa awali walifikiriwa kuletwa wapiganaji kutoka Rwanda, lakini wazo hili lilikataliwa na wafadhili wa mpango huu ambao walitaka wanaharakati wa aina hiyo watoke Somalia. Ndipo kikundi hicho kikashawishiwa kwamba Tanzania kuna tatizo la udini, la Uislamu kutishiwa. Mimi na wenzangu hao watano tumejengewa hoja kuwa maadui wa Uislamu tunaotumiwa na makanisa, hivyo hatuna budi kukatishwa maisha yetu.
Niliweza vile vile kupata picha kuwa wafadhili wa kundi hili, wana mahusiano ya karibu na Sheikh (jina tunalo) ambaye baadhi ya utabiri wake unatokana na agenda za wafadhili hao. Inadaiwa kuwa utabiri wa sheikh mwaka jana ulimlenga Dk. Slaa ambaye alidaiwa kubebwa na makanisa. Utabiri huo haukutimia kwa kuogopa kuiingiza nchi kwenye machafuko makubwa ya kisiasa/kidini ambayo yangewaweka pabaya hata wafadhili wa mpango huo.
Inadaiwa kuwa Sheikh ameombwa tena kutoa utabiri wa mwanasiasa na kiongozi mmoja kupoteza maisha mwezi huu (Fabruari). Inadaiwa kuwa mwanasiasa huyo anayetembea na kifo ni mimi na tayari maandalizi ya hukumu yangu yamefanywa:
(a) Kijana mmoja kwa jina la Hassan alitumwa kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma siku ya Jumamosi tarehe 05/02/11 kwa maandalizi hayo (mahali pa kufikia kikosi hicho cha mauaji, utambuzi wa nyumba ya kuishi niliyopangiwa na kumtafuta mhudumu mmoja wa Bunge ili ile portion ya Mganga Majungu ya kunipumbaza kabla ya hukumu, iweze kunyunyizwa kwenye kiti changu Bungeni);
(b) Kesho yake (Jumapili) tarehe 6 Februari, mnamo saa nne usiku, kikosi hicho cha mauaji kikiwa na watu watano kiliondoka Dar es Salaam kwenda Dodoma kwa gari aina ya Land Cruiser nyeupe ya mkongo (T36 AKU) na kimejichimbia Dodoma mpaka leo (Februari 9).
Waliomo kwenye kikosi hicho ni: Wasomali wale wawili, mgeni moja (wa kiume) kutoka Uganda, Mustafa a.k.a Master na kijana mmoja ambaye tarehe 19/01/11 aliwabeba Wasomali hao kutoka Morogoro hadi Ununio kupitia Kibaha na Baobab kwa gari aina ya VX Land Cruiser (T65 APF). Kijana huyo ana shepu ya Kitutsi na anaongea Kifaransa.
Utabiri atakaoufanya Sheikh (pengine aamue kuachana nao sasa baada ya kubaini kuwa tunaujua) utakuwa na lengo la kuwapumbaza wananchi waelekeze macho na masikio yao zaidi kwenye utabiri wake kuliko kwenye njama za kundi hilo za muda mrefu za mauaji.
Kila siku ya Mungu napata taarifa za ziada kutoka kwa raia wema kuhusu suala hili. Naziingiza kwenye taarifa hii ili ziwasaidie katika upelelezi:
Inadaiwa kuwa Wasomali hao waliingia nchini kutokea Kenya na wakaja kwa barabara hadi Dodoma. Walitumia gari aina ya RAV4 (new model T81 AQS) tarehe 08/01/11 na kusafirishwa hadi Morogoro ambako walipokewa na askari niliyemtaja awali wa Polisi Morogoro.
Mjini Morogoro, walikaa hoteli mbili tofauti: Hilux Hotel Morogoro na Top Life. Aliyewafanyia Wasomali hao booking hapo Top Life ni mmiliki wa hoteli (jina la hoteli na mmiliki tunalo).
Magari waliyotumia wakiwa Morogoro ni RAV4 T81 AQS, VX Land Cruiser STK 128 , Mercedes Benz (Station Wagon) T87 BDT, Toyota Mark II GX100 nyeupe T21 BKR na wakiwa Dar es Salaam wametumia magari VX Land Cruiser T65 APF, Nissan Patrol T84 ADH.
Dk. Mwakyembe anaongeza, Naomba nihitimishe maelezo haya kuwa nimekuwa muwazi kwa asimilia 100 na hata sources zangu ni miongoni mwa watu hao niliowataja katika taarifa hii ambao naamini utachukua hatua ya kuwahoji kulipatia ufumbuzi suala hili.
Suala la msingi hapa, si uhai wangu, kwani ipo siku lazima nitakufa kama ambavyo hao mafisadi wanaodhani wanaweza kufadhili vifo vya wenzao watakavyokufa hata wao hatimaye, watake sasitake, It is simply a question of time. Suala la msingi hapa ni mustakabali wa Taifa letu, Taifa aliloliasisi Mwalimu Nyerere na kulilea kwa misingi ya usawa, haki, umoja, amani na utulivu.
Nimejieleza awali kuwa nina imani kubwa na Jeshi letu la Polisi kwamba litaifanyiakazi taarifa hii bila kujali nguvu ya ukwasi na ya kisiasa ya watuhumiwa na kwa kuzingatia misingi ya haki na ukweli.
Hata hivyo nalazimika kusema nitasikitika sana ikiwa taswira ya ukorofi niliyopewa kwenye kesi moja ya awali (2009) itapewa nafasi kwenye suala hili, hivyo kuninyima fursa ya kusikilizwa vizuri na ulinzi ninaostahili kama raia kikatiba na kisheria. Niko tayari wakati wowote na mahali popote kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi litakaponihitaji.
Maoni ya wanasiasa na wasomi
Baadhi ya wasomi na wanasiasa mbalimbali waliohojiwa na MTANZANIA wameshangazwa na taarifa hii ya Dk. Mwakyembe, hasa kwa msomi kama yeye kuamini masuala ya uchawi.
Ninachoweza kumshauri kaka yangu (Mwakyembe) ni kuchapa kazi zake alizopewa za ubunge na uwaziri, akiingiza masuala ya kuamini ushirikina atakuwa anapoteza sifa yake ya usomi, alisema mmoja wa wahadhiri.
Dk. Mwakyembe anatambulika katika Jeshi la Polisi kama mmoja wa viongozi wanaotoa maelezo yenye utata kuhusu usalama wao.
Ameibua suala hili huku kukiwa bado na kumbukumbu za yeye kupata ajali mkoani Iringa na kudai kwamba lori lililohusika lilikuwa limepangwa kumtoa uhai.
Hata hivyo, Polisi walifanya uchunguzi na kubaini kuwa chanzo cha ajali hiyo kilikuwa ni uzembe na mwendo kasi wa dereva wa Dk. Mwakyembe.
Nimekugongea thenkyu kwa ajili hiii hapo. Mijitu mingine huwa haisomi habari kwa makini then wanaharimu mada. Pse dudes someni vizuri mpate kinachoelezwa si kurukia rukia tu.Insu hapa sio uislamu,hiyo imetumiwa tu km propaganda ya kuwashawishi wale wasomali,.
Tumejenga taifa la watu wazushi. Daktari wa PhD anazusha. Alizusha mambo mengi akiwa mwenyekiti wa kamati teule ya bunge na uzushi wake unatugharimu hadi leo. Akatuaminisha kwamba Richmond na Dowans ni moja na kwamba zote zina mikono ya RA na EL. leo hii haya yote yamethibitika kuwa ni uongo na anafanya hivi ili kujiepusha na kitanzi cha uzushi wake.
Ni bahati tu kwamba watanzania ni wavivu wa kukumbuka, tumeshasahau na bado tunamuona Mwakyembe shujaa. Mtu huyo huyo kwa sababu ya uzushi wake huo aliposikia Tanesco wanataka kuinunua mitambo ya Dowans akafanya press conference na kuliambia taifa ni bora nchi iwe gizani kuliko kuinunua mitambo hiyo, sasa hivi tuko gizani na kazi iliyofanywa na kamati yake imeligharimu taifa karibu shilingi bilioni 100, mitambo ipo haiwashwi kisa ni uchochezi dhidi ya nishati ya umeme uliojengwa na mwakyembe na wahuni wenzake.
Mzushi huyu akaja tena na uongo mwingine alipopata ajali ambayo hakuna shaka ilitokana na uzembe wa dereva wake, akadai kulikuwa na lori lililokuwa likitaka kuwagonga na dereva wake alipokwepa ndipo gari likaacha njia na yeye akapata ajali. Uchunguzi wa polisi ulipofanyika ikabainika kwamba wakati ajali ikitokea alikuwa amelala na wala hakuliona lori alilokuwa akilisema...hakika huyu ana PhD ya uzushi.
Sasa kazusha jipya eti anataka kuuawa na akaandika barua kutoa ushahidi wa kutunga wa kuunga unga mambo na kuwataja watu na namba za magari mengi akijifanya ana mtandao unaompa taarifa za kila kinachotokea. Ana bahati tu kwamba tuna jeshi la polisi la wasanii ambalo linashindwa kumbana atoe ushahidi wa kina wa maelezo yake ambayo hakuna shaka yatathibitisha kuwa ni ya uzushi.
Anafanya hivi lili EL na RA waonekane ni wauaji...ajenda yake ile ile ya kuwazushia na kuwachafua wengine kwa malengo machafu ambayo ufadhili wake unatambulika kuwa ni wa wahuni wachache walio ndani ya idara moja nyeti. Ni aibu kuwa na naibu waziri tena mwenye PhD wa kiwango duni kama Mwakyembe.
Uzushi wake umelifanya taifa kupiga maktaimu na kujadili hoja moja kwa miaka minne sasa, uzushi wake umeliingiza taifa gizani na sasa anatengeneza uzushi mwingine unaoweza kuligharimu jeshi la polisi, idara ya usalama wa taifa, serikali, chama chake na watanzania kwa ujumla. Mwakyembe ni mtu hatari, ni mtu wa kuogopwa kama ukoma. Huyu mtu ana pepo baya, anapaswa kuangaliwa na kuchungwa sana