MZEE WA ACHECHE, CHUKUA NAMBA MOJA
Na, Robert Heriel
Kila mtu duniani hupenda kazi yake ifurahiwe na watu wengine. Hakuna asiyetaka kazi yake isipendwe. Ndoto ya watu wengi duniani ni kuona kazi wazifanyazo zinapendwa na kufurahiwa na watu. Lakini kufurahiwa peke yake haitoshi bali kufurahiwa pamoja na kuijenga jamii. Sio kufurahiwa lakini hapo hapo inabomoa jamii.
Hata hivyo sio kila mtu anafanikiwa katika hili. Wengi hujikuta wakifanya kazi lakini hazifurahiwi wala kupendwa na watu wengine.
Moja ya vijana waliofanikiwa katika kazi zao ni pamoja na Hamad Abdulrahman Abdallah alimaarufu kama DJ MARK ambaye Taikon napenda kumuita Mzee wa Acheche kutokana na kupenda kutumia neno hilo mara kwa mara.
DJ Mark ananifurahisha sana, ni kijana mwenye kipaji cha kipekee ambacho bila shaka Watanzania wengi wanajivunia kuwa na mtu kama yeye.
DJ MARK ni msanii anayefanya kazi ya kutafsiri filamu zenye lugha ya kigeni kwenda Kiswahili.
Pengine mtu fulani anaweza kuniuliza kwa nini Taikon nampa DJ MARK namba moja katika kutafsiri Filamu hapa Tanzania. Sababu zifuatazo nitazitaja:
1. DJ MARK ANAUTAMBULISHO/ Identity
Katika utambulisho kuna utambulisho wa aina mbili kwenye kazi za utafsiri wa filamu;
i/ Utambulisho wa Sauti
Kazi ya kutafsiri Filamu inatumia sauti. Msanii yeyote katika fani hii ili awe mkubwa lazima ajitofautishe na wasanii wengine na kuwa na sauti yake. Dj Mark amefanikiwa kuwa na Utambulisho.
Akiitafsiri filamu hata ukiwa mbali unajua kabisa huyo ni Dj Mark. Katika hili Dj Mark ameweza kuigwa na baadhi ya vijana chipukizi katika fani hiyo ya utafsiri wa filamu. Kitendo cha kuigwa ni moja ya mafanikio ya wazi kwa DJ Mark.
Wengine waliofanikiwa kwenye Utambulisho wa Sauti ni pamoja na DJ AFRO wa Kenya, Juma khan(Huyu anapenda za wahindi) na DJ Murphy
ii/ Utambulisho wa Maneno/ Msamiati
Katika utafsiri wa filamu mbali na sauti pia kuna Msamiati wanayotumia watafsiri.
Msamiati unaweza kuwa utambulisho wa DJ katika kazi yake ya utafsiri. DJ Mark amefanikiwa katika hili kwa hapa Tanzania. Hakuna Mtafsiri mwingine hapa Tanzania mwenye Identity katika msamiati zaidi ya DJ Mark.
Neno "Acheche" ni utambulisho ambao DJ MARK anatambulika nalo. Popote utakaposikia neno hilo akili yako itakuja kwanza kwa DJ Mark ndio umfikirie anayelitaja.
Mbali na Acheche, Dj mark anamaneno fulani ambayo ni kama punchline, mfano "Mbaruku Toli" "Kudadadadeki" "Dubwana" kisha anamalizia na mlunzi. Hii inaleta ladha kwenye kazi ya usanii ya kutafsiri.
Marehemu Lufufu pia katika hili la msamiati alifanikiwa mno maneno kama "Mdebwedo" yalimbeba.
Huko Kenya DJ AFRO Kalidhibiti vyema soko lake kutokana na Identity yake ya msamiati. Mfano hupenda kutumia msamiati "olololoyae" "Ashalala" "Ooooraiti" "Chunga chana"
Utambulisho ndio kiini cha kwanza cha msanii yeyote katika sanaa. Mtu asiye na utambulisho hawezi kwenda mbali katika kazi yake.
2) Uchaguzi wa Filamu
DJ MARK anajua kupoint filamu za kuzitafsiri lengo ni kuhakikisha sisi Watazamaji wake na wasikilizaji hatujuti kuzitizama filamu anazotafsiri. DJ MARK anajua soko lake kubwa kwa sehemu kubwa ni vijana, na watu wa kipato cha chini na kati. Ambapo kimsingi watu hao hupenda Action Movies na sio zile filamu za kuongea mwanzo mwisho.
Filamu zenye mapigano makali ya kila mara, zenye stori kali ndizo anazipointi jambo ambalo linamfanya mtazamaji na msikilizaji kutaka zaidi na zaidi filamu alizozitafsiri.
Filamu za kutisha kama za mazombie, vampire, Horror movies ndizo anazipenda, na vijana wengi wa tabaka la kati na chini huzipenda.
3) Anajua kushirikisha Hadhira
DJ MARK kama Msanii atahakikisha Mtazamaji au msikilizaji wake ambaye ndiye hadhira kuwa anakuwa makini kufuatilia filamu. Anajua wapi aongee na wapi akuachie utazame mwenyewe. Anajua kukuamsha hisia na mchecheto wakati wa hatari inapotokea kwenye filamu. Hili pia DJ AFRO analimudu kwa sehemu kubwa.
Wasanii wengine wa utafsiri wa filamu hushindwa hapa. Wengine hupoa sana na kuifanya filamu usiipe umakini sana.
Nampongeza kwa kuweza kukitumia kipaji chake vizuri. Hii ni sehemu ya ajira lakini pia ni sehemu ya lugha kwani kazi yake kwa asilimia 50 inategemea lugha mbali na vifaa vya teknolojia.
Je, unafikiri ni Mtafsiri gani anashika nafasi ya pili baada ya DJ MARK? Dondoka hapo chini
Robert Heriel
Taikon wa Fasihi
0693322300
0711345431