Mke wa Dk. Slaa abanwa
Adaiwa kutoa siri za ubadhirifu Hanang
na Ramadhani Siwayombe, Hanang
MKE wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbrod Slaa, Rozi Kamili, ambaye ni diwani wa Kata ya Basotu (CCM), yupo matatani baada ya kuhojiwa na Kamati ya Maadili ya Madiwani wa Halmashauri ya Hanang', akituhumiwa kutoa siri za ubadhirifu wa fedha ndani ya halmashauri hiyo.
Licha ya kamati hiyo ya maadili kuwahoji lakini juzi imeshindwa kutangaza hatua za kinidhamu atakazochukuliwa diwani huyo na wengine watatu wa halmashauri hiyo wanaotuhumiwa kwa kukiuka kanuni za maadili za madiwani.
Madiwani wengine waliohojiwa na kamati hiyo ambao wanasubiri maamuzi ni Anju Mang'ola (CCM), Kata ya Gehandu, Leonard Gepchojiga (CCM), Kata ya Mogitu na Venosa Bura, Viti Maalumu (CHADEMA).
Hata hivyo ajenda ya kutangazwa uamuzi wa kamati hiyo, ilitarajiwa kutangazwa jana, lakini iliondolewa ghafla, kwa sababu ambazo hazikuweza kufahamika mara moja.
Diwani Mang'ola na Gapchojiga wanatuhumiwa kukataa watu waliohamishwa katika Mlima Hanang wapewe ardhi katika mashamba yaliyokuwa yakimilikiwa na Shirika la Taifa la Chakula (NAFCO), ambayo baadhi yaliyorejeshwa kwa wananchi yapo katika vijiji vyao.
Diwani Bura anatuhumiwa kwa kushawishi wafanyabiashara katika Soko la Katesh kutolipa kodi, hadi mikataba yao imalizike, baada ya kujenga wenyewe vibanda vyao.
Akizungumza nje ya ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo mara baada ya kuahirishwa kutangazwa kwa hatua zitakazochukuliwa dhidi yao, mke wa Dk. Slaa, Rozi Kamili, alisema wanashangaa kwa kushindwa kutangazwa hatua hizo, kwani wamehojiwa zaidi ya mwezi mmoja uliopita.
Walituhoji na tumesisitiza tunachokiamini kuwa ni ukweli na kutoa vielelezo vya kuthibitisha hayo, pia nimeiambia kamati kama inaona nimekiuka kanuni wanifikishe mahakamani, alisema diwani huyo.
Diwani Kamili, alisema yeye ameibua tuhuma zilizomo ndani ya halmashauri hiyo, za wizi wa sh milioni 20, ambazo zilitengwa kwa ajili ya kukarabati vituo vya afya na zahanati na mradi huo haujafanyika na mwaka wa fedha uliishapita.
Mangola, Gapchojiga na Bura kwa pamoja wanadai kuwa tuhuma zinazowakabili ni za kupandikizwa ili kuwachafua, hivyo wanasubiri uamuzi wa kamati utolewe ili nao wapate nafasi ya kwenda mahakamani.
Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Ndoliwa, alikataa kuzungumza na waandishi wa habari walipomfuata kutaka kufahamu sababu za kutotangazwa kwa uamuzi wa kamati ya maadili katika kikao hicho.