Analogia Malenga
JF-Expert Member
- Feb 24, 2012
- 5,017
- 9,885
Serikali ya China imeipatia Tanzania msaada wa Sh35.37 bilioni zitakazotumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo iliyokubaliwa na kuridhiwa na mataifa hayo mawili.
Hayo yameelezwa leo Jumatano Mei 12, 2021 na Katibu mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Emmanuel Tutuba wakati wa hafla ya kusaini mkataba wa msaada huo kati yake na Balozi wa China nchini, Wang Ke.
Katika maelezo yake, Tutuba amesema mkataba huo ni wa jumla kwa ajili ya kuteleza miradi hiyo, akisema kwa kuanzia wamependekeza fedha hizo zitumike katika upanuzi wa miundombinu ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI).
“Kuboresha miundombinu itakayokipandisha hadhi Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kuwa chuo kikuu. Uhifadhi wa miamba katika eneo la Ngorongoro Geopark na miradi mingine itakayokubalika kati ya Serikali hizi mbili,” amesema Tutuba.
Tutuba amemueleza Ke kuwa Serikali imekuwa ikiisaidia Tanzania katika sekta mbalimbali ikiwemo uboreshaji wa sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu ya Reli, Barabara, Afya, Nishati, Maji, Kilimo na Viwanda pamoja na Mfumo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama).
“Ufadhili wa Serikali ya China kupitia mikopo yenye masharti nafuu kwa miradi iliyokamilika tangu mwaka 2010 ni kiasi cha Sh 4.15 trilioni. Balozi Wang tunaishukuru China kwa ushirikiano huu uliochangia kufikia malengo yetu kwa kuzingatia mipango ya maendeleo,” amesema Tutuba.
Kwa upande wake, Balozi Ke amesema msaada umeridhiwa na kuthibitishwa na Serikali za China na Tanzania. Amesema China inaichukulia Tanzania kama rafiki na mshirika mzuri.
“Tangu kuanzishwa kwa masuala ya diplomasia miaka 57 iliyopita China imekuwa ikiisaidia Tanzania katika sekta mbalimbali ikiwemo kiuchumi na maendeleo ya jamii ikiwemo miradi ya reli ya Tazara na uwanja wa Mkapa,” amesema Balozi Ke.
Mwananchi