Rutashubanyuma
JF-Expert Member
- Sep 24, 2010
- 219,504
- 911,249
Lowassa anasafishika akichafua kiti
Charles Mulinda
Sambamba na hilo, kwa wasomaji wa safu hii waliokuwa wakinitumia ujumbe mfupi kupitia simu yangu ya kiganjani wakipinga kile nilichokuwa nikieleza kuwa CCM itameguka au itafia mikononi mwa rafiki yangu, Rais Jakaya Kikwete, nadhani sasa wanakubaliana na mimi katika hilo.
Sihitaji tena kutoa maelezo marefu ya kuwasadikisha jambo hili kwa sababu hata kama akili zao zimeganda mithili theluji ya kileleni mwa mlima Kilimanjaro, ninaamini katika mgando ule zitakuwa zina hisi hali ya joto joto la upinzani mkali utakaotolewa na kambi ya wale wanaotakiwa sasa kukaa kando ya uongozi wa chama hicho, kisa! Eti, kwa sababu ya kutuhumiwa kwa ufisadi.
Inashangaza kweli kwa sababu wanaowatuhumu wenzao kwa uchafu huu wanatuhumu kwa macho makavu utadhani wao sio mafisadi. Kwa wenye akili nadhani hapo nimeeleweka. Nirudi kwenye mada yangu ya msingi ya Lowassa na kujisafisha.
Mara zote katika safu nilikuwa nikikwepa sana kuwajadili watu wa aina ya Lowassa kwa sababu ya kutambua umuhimu wao katika uhai wa chama chetu cha maulaji kilichojaa kila aina ya uchafu ambao kwangu mimi kama ingekuwa ni sakafu, hata ikisuguliwa kwa jiwe haiwezi kutakata.
Nilikuwa natambua kuwa ingawa Lowassa anatuhumiwa sana kwa mambo kadha wa kadha, tuhuma hizo ni nyepesi mno kulinganisha na zile kinazotuhumiwa nazo chama cha maulaji na baadhi ya viongozi wake wakuu.
Na ninatambua kuwa Lowassa ana mengi moyoni yanayohusiana na ufisadi wa chama cha maulaji na viongozi wake, hivyo kumwendea kichwa kichwa kungeweza kumfanya akose uvumilivu na kumwanga mchele kwenye kuku wengi.
Naamini wanaCCM wenye akili wanalitambua hili na ndiyo maana hata kama alikuwa na mabaya walikuwa wanayamezea moyoni kwa sababu hata wao wana ya kwao ambayo pengine ni makubwa kuliko ya kwake.
Lowassa naye alikuwa kimya kwa sababu alikuwa bado na kaulaji fulani ndani ya chama cha maulaji hata kama kalikuwa hakalingani na yeye mwenyewe alivyo lakini kalitosha kwa sababu kalikuwa kanampa hadhi fulani ya kujiona na yeye ni miongozi mwao baada ya kudhalilishwa sana, kusingiziwa sana na kufedheheshwa sana.
Na inawezekana pia kama inavyosemwa na baadhi ya wachokonozi kuwa alikuwa kimya kwa sababu alikuwa na malengo ya siku moja kusafishika na kukwea tena katika kilele cha siasa za maji taka ndani ya chama chetu na hata kufikia malengo ya kisiasa aliyojiwekea katika maisha yake.
Hali sasa ni tofauti, mapinduzi ya vigogo wa ndani ya chama chetu ya wiki iliyopita yanamlazimisha na yeye hata kama alikuwa na kaukubwa kidogo kukaachia na kukaa pembeni kabisa! Eti, abaki akiwaangalia wengine wakila tu! Hili ni jambo gumu sana kulikubali hata kama lingetokea kwangu.
Kama mpambanaji naamini atapambana kuhakikisha hafi peke yake, kwa sababu waliomfikisha hapo anapohangaika sasa ndiyo aliokuwa akila na kunywa nao na pengine alitumia nguvu zake kuwafikisha katika maulaji yao ya sasa.
Kwa sisi tunaomfafamu Lowassa kwa kusimuliwa ni mtu asiyekata tamaa, ni bingwa wa kupanga mikakati na kiumbe anayefanya kazi bila kuchoka hadi kile anachokipigania kifanikiwe.
Kutokana na masimulizi hayo, ninakuwa wa kwanza kujitokeza kumtia moyo kuwa walichokifanya wenzetu ndani ya chama ndiyo mauti yao kwa sababu funguo za umoja, amani yenye mashaka na mshikamano anayo yeye na wenzake anaotuhumiwa nao. Hivyo ndivyo ninavyooamini.
Anachopaswa kufanya katika kipindi alichonacho cha kuugulia maumivu ya kutoswa ni kusali sala ya toba akimuomba Mungu amuongeze nguvu na ujasiri wa kueleza hata yale machafu ambayo hayapaswi kuelezwa mbele ya watoto na wakubwa, yaliyofanywa na chama chetu bila kujali kama na yeye alishiriki kuyafanya au lah!
Anapofanya hivi awe na lengo moja! La kuchafua kiti cha enzi ya Tanzania ili hata hao wanaomfanyia mtima nyongo sasa asikikalie kama kweli alikuwa akikitaka, nao wakikose. Na wale walioko kileleni wachafuke kuliko yeye.
Baada ya sala ya toba na kama Mungu ataikubali na kumjaza roho mtakatifu kama yule aliyewajaza mitume kumi na wawili kisha wakaanza kunena kwa lugha za mataifa mbalimbali. Na iwe hivyo hata kwake Lowassa, akishajazwa na huyo roho anene, na ili kunena kwake kunoge, aanze hivi;
Aitishe mkutano na waandishi wa habari aeleze alichokuwa amekusudia kukizungumza muda mfupi baada ya kutangaza kujiuzuru na kuanza kufanya mahojiano na televisheni ya Taifa (TBC) kabla hayajakatishwa ghafla kwa sababu ambazo hazijawekwa hadharani hadi sasa.
Kwa ujasiri ule ule kama watume, aeleze Richmond ni mdudu gani? Nani aliuleta! Asema kama baraza la mawaziri chini ya rais Kikwete halikuketi au liliketi kubariki ujio wake, jinsi alivyoshiriki kishinikiza kama ni kweli mdudu huyo kupewa zabuni ya kufua umeme huku akijua au hajui kuwa haina uwezo huo.
Bila kuwaruhusu waandishi wa habari kumuuliza maswali hadi atakapomaliza kutoa maelezo yake, taratibu kama wahubiri, aeleze kilichosababisha hatua ya kuletwa kwa Richmond nchini na kama anajua aeleze ni kwanini rais Kikwete alikuwa akiisifia sana mwanzoni na kujigamba kuwa baada ya kuanza kazi tatizo la umeme litakuwa historia nchini.
Na kama atakuwa anakumbuka, atoboe siri ya kwanini rais Kikwete alifuta sehemu ya hotuba iliyokuwa ikizungumzia Richmond mwezi ule anaoujua yeye, aliyoitoa kwa wananchi na awataje mashahidi wa kushabikia maelezo yake kama ni ya ukweli.
Atakapokuwa akieleza haya atakuwa akikichafua vibaya kiti cha urais, lakini hilo asijali kwa sababu ili afanikiwe kujisafisha ni lazima afanye hivyo. Ni lazima achafue kiti hicho kama alivyochafuliwa yeye ili asafishike.
Akimaliza hapo amgeukie Spika wa Bunge lililopita na kamati teule aliyoiunda na kuibuka na jina lake kama mmoja wa watu waliohusika kwa karibu na kashfa hiyo.
Kwa sababu mtu anapozungumzia jambo lililomuumiza anaruhusiwa kukunja sura kuashiriria anachokizungumza kilimuumiza, akipenda hapa anaweza kukunja sura wakati akieleza ni kwanini Bwana Spika Sitta alifanya vile.
Aseme kama alikuwa na ugomvi naye au kama tatizo lilikuwa uwaziri mkuu au kama walikuwa na ugomvi mwingine ulioeleka huku uswahilini kwa wachokonozi.
Bila kuchoka kuzungumza kwa sauti ile ile, aeleze kile ambacho kamati teule ya bunge ilikificha ili kuilinda serikali yote ya Rais Kikwete isianguke na kumtwisha zigo hilo yeye na waliokuwa chini yake.
Na ili kuwaridhisha waandishi wa habari, awaeleze kuwa amekwishawasiliana na mtuhumiwa mwenzake katika kashfa hiyo, Rostam Aziz, ambaye alifungwa mdomo na Spika Sitta alipotaka kueleza jinsi ripoti iliyowasulubu ilivyokuwa imechakachuliwa na kwamba sasa yuko tayari kuitoa ripoti hiyo hata kama ni kwa kuilipia kama tangazo kwenye vyombo vya habari.
Asiachie hapo, aeleze madudu mengine yoyote yanayomuhusu Spika Sitta kama yapo. Kama anapenda sana ukubwa! Kama alimchukia kwa sababu ya kukataa kumpa walinzi au lolote baya analolijua linalomuhusu ambalo ana uhakika lina ushahidi usiokuwa na shaka.
Maelezo haya yatamsaidia kwa kiwango cha juu kujisafisha na kashfa zinazomuandama sasa hata kama atakiri kushiriki katika madudu hayo.
Atakuwa amezua mjadala mpya wa Richmond ambao kwa jinsi Watanzania walivyo na hasira kwa sasa, hasa kutokana na makali ya mgawo wa umeme na wengi wao kushindia mlo mmoja huku wengine wachache wakila na kusasa, wao na mbwa zao, watailazimisha serikali hii ninayoipenda kuishia kule kule aliko yeye sasa.
Bila Kuwaruhusu waandishi wa habari viherehere kumuuliza lolote, akimaliza tu hilo adakie na ufisadi wa EPA na CCM.
Hapa aanze kwa kueleza historia ya EPA. Jinsi EPA na CCM zilivyojenga ushoga na kuwa kitu kimoja katika uchaguzi wa 2005. Awataje waliosuka dili ya kukwapua mabilioni ya EPA hata kama ni rafiki zake, awataje tu kwa sababu hiyo ndiyo silaha pekee ya kujisafisha. Na hapa azingatie kuwa vita haina macho.
Afumbe macho kama walivyofumba wenzake wakati wanamtosa anapoeleza kama kweli CCM kilitumia mabilioni ya EPA kufanikisha ushindi wa mgombea kiti cha urais wa CCM mwaka 2005 na amalizie kwa kueleza sababu zinazoifanya serikali ya CCM kushindwa kuwakamataka wezi wa mabilioni ya EPA.
Akifanikiwa katika hili, Lowassa atakuwa shujaa wa Tanzania aliyerejea kuwaeleza ukweli wa jinsi wezi wanaotutawala wanavyotuibia.
Atakuwa amejisafisha na kwa kipindi chote kilichobaki kuelekea mwaka 2015 atakuwa akitengeneza vichwa vya habari katika vyombo vya habari vyenye akili kwa sababu atakuwa maarufu kuanzia mijini hadi vijijini.
Na halitakuwa jambo la ajabu hata atakapoamua kurejea katika ulingo wa siasa za CCM hiyo hiyo akakosa mpinzani kwa sababu wote atakuwa amewachafua akiwemo yeye mwenyewe lakini yeye atakuwa na ahueni kwa sababu atakuwa ametubu kwa kueleza ukweli wa kutoa siri za zilizoficha sirini ndani ya chama chetu.
Ikiwa hivi asitokee mtu wa kushangaa kama Lowassa anaweza kurudi kuwa mtu muhimu anayeweza kugombea urais na kushinda au mzee ambaye atakuwa akitegemewa na wengi kumtwaa kati ya vijana wengi ndani ya chama, kijana atakayekuwa mgombea urais 2015 na akampigia kampeni na kushinda.