Malisa Godlisten Leo alikuwa safarini kutoka Marekani ambapo amekuwa kwa zaidi ya miezi tisa (9), tangu alipoenda kuiwakilisha nchi yetu kama mtanzania pekee aliyechaguliwa na Wizara ya Mambo ya nje ya Marekani kwenda kupata mafunzo ya uongozi. Fursa ambayo hujitokeza kwa watanzania wachache sana kama ilivyowahi kutokea kwa aliyekuwa Rais wa awamu ya nne Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.
Alipofika Nairobi- Kenya asubuhi ya leo, alishindwa kuendelea na safari kutokana na kuwepo kwa mgomo wa wafanyakazi unaondelea katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta. Hivyo aliamua kusafiri kwa usafiri binafsi mpaka Namanga ambao ni mpaka kati ya nchi yetu na Kenya ili kuingia nchini kupitia Arusha.
Aliwasili Namanga majira ya saa tisa(9) mchana na kwenda kwa maafisa uhamiaji ili kugongewa hati ya kusafiria (Passport) na hatimaye kuingia nchini kama utaratibu unavyotaka.
Baada ya kufika kwa maafisa uhamiaji hao, walichukua hati yake ya kusafiria na kumwambia kuwa haisomeki kwenye mfumo (system) hivyo wao hawana namna ya kufanya mpaka mkuu wao (in- charge) aje ndio anaweza kuona kwenye mfumo.
Kutokana na kadhia hiyo, na kwa kuwa aliambiwa Mkuu huyo hayupo kwa muda Malisa GJ aliendelea kukaa katika ofisi hizo za uhamiaji akisubiri Mkuu huyo kuja na kuhakikisha tatizo hilo linapatiwa ufumbuzi.
Cha kushangaza ilipofika saa moja jioni, alichukuliwa na gari ambalo si la Polisi jeupe Double Cabin na kupelekwa kituo cha Polisi Longido. Hata hivyo gari hilo halikukaa sana likaondoka kuelekea uelekeo wa Arusha.
Mpaka natoa taarifa hii hakuna taarifa kamili za aliko Malisa GJ na nini ni sababu ya kukamatwa kwake. Aidha simu zake zote zimezimwa tangu alipokuwa anatolewa Namanga.
Nitoe rai kwa Polisi na Uhamiaji kumwachia huru mara moja au kuhakikisha wanatoa taarifa kwa umma za aliko Malisa GJ na sababu ya kukamatwa kwake. Kama haitoshi kuhakikisha anapewa haki zake za kisheria ikiwemo kuonana na mawakili wake na haki ya Mawasiliano.
Dickson Matata (Wakili)
31/8/2026
Arusha-Tanzania.