Utata wa barabara ya chalinze
Na Leon Bahati, Dodoma
SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta amesema kuwa vitabu vya bajeti vilivyopo kwenye maktaba ya Bunge mjini Dodoma vinaonyesha kuwa barabara ya Chalinze-Segera-Tanga haikuwa imepangiwa fedha katika bajeti zilizopita, jambo ambalo limemfanya achelewe kutoa majibu kwa serikali dhidi ya mbunge wa Nzega, Lucas Selelii.
Selelii, mmoja wa wabunge wanaoshikia bango ujenzi wa barabara, alitaka ufafanuzi wa serikali kuhusu kuanza kwa ujenzi wa barabara hiyo kabla ya Bunge kupitisha bajeti ya mwaka 2009/10, kitu ambacho kikibainika kuwa ni kweli, serikali itakuwa imevunja katiba.
Wiki iliyopita Sitta alilieleza Bunge kuwa ameshapata maelezo ya serikali kufafanua kuhusu suala hilo, lakini amekuwa hayatangazi kwa madai kuwa, kuna matatizo katika vielelezo vilivyowasilishwa na Selelii na vilivyotumiwa na serikali.
Jana Sitta ataendelea kuliweka kiporo suala hilo kwa kuwa bado hajajiridhisha na utata ulio kwenye vitabu alivyowasilisha Selelii na nakala ya ukurasa wa kitabu cha mwaka huo kilichowasilishwa na serikali.
"Mheshimiwa Mbunge alikwenda katika maktaba ya Bunge akatafuta vitabu vya makadirio vya 2006/07 na 2007/08 na 2008/09. Serikali kwa upande wake nayo ikanipa nakala vivuli vya miaka hiyo hiyo," alisema Sitta.
"Sasa nakala ya serikali inaonyesha kuwa fedha zilitengwa, vitabu vilivyopo maktaba ya Bunge vya makadirio, hususan kitabu cha nne- maendeleo inaonyesha sifuri kwa miaka hiyo. Ndio maana kumekuwa na utata kwamba tunafanyaje.
"Kwa hiyo leo nimeagiza kwamba, baada ya kuonana na mheshimiwa Waziri wa Miundombinu na katibu wa Bunge waangalie mtiririko mzima wa vitabu. Mtaona kwamba mathalan mwaka huu imebidi marekebisho yafanywe. Kwa yule mtu aliyechukua kitabu cha kamati tulipokutana mwezi Mei, Dar es Salaam, hakina usahihi kwa sababu baadhi ya sehemu zilibadilishwa.
"Kwa hiyo limebaki hilo tu, kulinganisha hivyo vitabu na baada ya hapo nitatoa basi ufafanuzi na uamuzi wangu kuhusu kilichotokea. Hii ndio sababu, lakini watu, wengi wetu wauza magazeti wakasema Spika sijui anapambana na serikali na vitu vya kipuuzi vya namna hiyo."
Spika Sitta aliongeza kusema: "Hii ni serikali yetu, mimi siwezi kupambana na serikali. Nipambane na serikali kwa sababu gani. Ni jambo tu la uhakika kwa sababu linalotamkwa hapa, likija kugundulika kuwa Spika naye alilolisema hakulifanyia utafiti, tunaweka msingi mbaya sana wa utawala wa Bunge. Ndio maana limenichukua muda. Kwa hiyo tuwe na subira, hili litakwisha hivi punde."
Ukarabati wa barabara hiyo iliyojengwa miaka 18 iliyopita ulizinduliwa mwezi Mei na Makamu wa Rais, Dk Ali Mohamed Shein. Ukarabati huo unafadhiliwa na serikali ya Denmark kwa kutumia shirika lake la Danida.
Serikali hiyo imetoa Sh44 bilioni, wakati serikali imetenga Sh18 bilioni katika bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya kukamilisha mkataba wa ukarabati huo kwa mujibu wa makubaliano baina ya nchi hizo mbili.