SoC03 Askari wa Usalama Barabarani (Trafiki) kujigeuza Mahakama wanafanya uonevu mkubwa kwa madereva

Stories of Change - 2023 Competition

sajo

JF-Expert Member
Nov 8, 2010
3,022
5,254

Ukiwauliza madereva, kama wangependa askari wa usalama barabarani wawepo au wasiwepo barabarani, utashangaa pale robo tatu ya idadi ya madereva uliowahoji watakapokujibu kuwa wangependa barabarani kusiwe na askari wa usalama barabarani. Ukiwauliza sababu ya wao kupenda hivyo watakwambia kwa sababu 'trafiki' wamekuwa ni waonezi kwao kwani wanawabambikia makosa na kuwatoza faini isivyo halali na pia kuwacheleweshea safari. Dereva anapomuona Askari wa usalama barabarani, moyo wa dereva unajaa hofu na anapoteza kujiamini kwa kujua kuwa muda wowote atalimwa umeme (atatozwa faini) kwa kosa la usalama barabarani bila kujali amelifanya kweli au la.

Ukiendesha gari siku ya ijumaa kwa safari za mikoa na mikoa, utajikuta mara kwa mara unakanyaga pedeli ya breki kwa hofu inayotengenezwa kila unapoona kwa mbali mtu amevaa vazi jeupe na yupo barabarani, sababu unajua ni askari 'trafiki' na baadae unapata nafuu (relief) baadaya kugundua kuwa kumbe uliyedhania kuwa ni trafiki alikuwa ni muumini wa dini ya kiislamu aliyevaa kanzu ama akienda au akitoka msikitini. Sababu ya kuwa na hofu ni kutokana na ubabe wanaouonesha askari wabarabarani kwenye kushughulikia makosa ya barabarani.

polisi twitter.jpeg

Chanzo: Mtandao wa twitter

Tunafahamu kuwa ni jukumu la kisheria la jeshi la polisi kusimamia usalama barabarani, sipingani na hilo. Lakini je, askari hao wanatakeleza ipasavyo jukumu lao hilo la kisheria?

HAPANA. Jedwali la 1 la The RoadTraffic (Specified Offences) Order ya 1985 linaonesha Fomu ya Polisi Na. 101 ambayo inatoa taarifa (NOTIFICATION) kwa dereva iwapo ametenda kosa la barabarani. Fomu inelekeza kuwa kama dereva atakubali kosa basi atatakiwa kujaza sehemu B na kulipa faini iliyotangazwa na serikali (kwa sasa ni Tshs.30,000/=) au kama hatakubali kosa, atajaza sehemu A na jeshi lapolisi litamfikisha mahakamani kujibu mashtaka kuhusu kosa alilolitenda. Jedwali hilo linasomwa pamoja na Kifungu cha 95 cha Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 198.
 Notification - PF 101.png

Chanzo: Mimi mwenyewe
Msingi wa kumpa dereva uhuru wa kukubali au kukataa kosa ni kwa sababu, chombo pekee kinachoweza kumtia hatiani mtu kwa kosa alilotuhumiwa nalo ni Mahakama, hivyo dereva anaposimamishwa na askari wa usalama barabarabani, anakuwa ni mtuhumiwa wa kufanya kosa na sio mkosaji, askari anakuwa mlalamikaji na sio mwamuzi. Dereva anapokubali kosa basi ndipo sheria ikaona alipishwe kwa askari, faini papo kwa papo au kwa muda uliokubaliwa. ila kama dereva huyo atakana kufanya kosa hilo basi aandikiwe taarifa ya kufika mahakamani kujibu tuhuma zake. Lakini sasa, baada ya Maaskari kupewa mashine za kielektroniki (POS), basi utekelezaji wa sheria umegeuka moja kwa moja, hakuna tena suala la kukataa kosa wala kufikishwa mahakamani , ukidakwa na polisi ni mwendo wa kuandikiwa faini (kubetishwa).

Mashine (POS) walizopewa Trafiki ndio zimekuwa kichinjio chao. Mashine hizo zimefanya polisi wasiheshimu tena sheria wanayoisimamia. Wakikusimamisha na kukuambia umefanya kosa barabarani kuna mambo mawili tu, ama uandikiwe faini ya Tshs. 30,000/= kwa kosa ulilotuhumiwa kufanya au utoe hela kidogo (kati ya elfu 2 mpaka elfu 10) ili askari apotezee na asikuandikie faini. Wengi wa madereva huona njia ya kutoa hela kidogo ni bora kuliko kuandikiwa faini kwani hali ya uchumi ni ngumu, heri nusu shari kuliko shari kamili.

JE, KUBAMBIKIA NI UTASHI BINAFSI WA ASKARI POLISI ALIYEPO BARABARANI AU KUNA BARAKA ZA JESHI LA POLISI?

Jibu ni kuwa jambo hili la polisi kujigeuza mahakama lina baraka zote za jeshi la polisi kwani licha ya malalamiko chungu nzima kutolewa kwenye mitandao ya kijamii na hata kwenye vituo vya polisi, hakuna hatua zilizochukuliwa na Jeshi la Polisi ama kutamkwa hadharani juu ya hatua walizochukuliwa askari polisi waliobambikia makosa madereva.

Huenda lengo la jeshi la polisi kuweka vimashine vile vya POS ni kuongeza mapato, jambo ambalo kimsingi sio jukumu la msingi la Jeshi, lakini hata lengo hilo halifanikiwi kwa kuwa askari wa usalama barabarani wanatumia mashine hizo kama kujipatia fedha wao binafsi kwa njia ya rushwa. Badala ya mashine kukusanya mapato, zimekuwa ni mwanya wa askari usalama barabarani kuombea rushwa. Akimpiga picha na kamera yake (tochi) hata mahali pasipo na kibao cha ukomo wa mwendokasi wa kiasi fulani, dereva atakapokataa kuwa hujatenda kosa hilo yeye anaomba leseni yake na kuanza kuingiza taarifa kwenye mashine kuwa anamuandikia faini, kwa kuona ataingia hasara ya kifedha basi dereva anajiongeza kwa kutoa rushwa ili aachiwe. Hayati Rais John Pombe Magufuli alisema si vibaya kuwapa askari hela za kubrashia viatu.

MADHARA YA KUTOTUMIA FOMU YA TAARIFA (PF. 101)
  • Kukuza rushwa katika jeshi la Polisi.
Mtu anaweza kusema kuwa lawama za rushwa inabidi ziende kwa madereva maana wao ndio watoaji na ndio wanaowashawishi polisi kutoandika faini, ni kweli, lakini maaskari pia hawawezi kukwepa lawama kwa kuwa wanapokea rushwa hiyo. Ukiangalia kwa kina utagundua kuwa rushwa hii inakuwa imesababishwa na maaskari hao wenyewe (constructive liability), yaani dereva unatengenezewa mazingira ili utoe rushwa, maana unakuwa una njia mbili tu, kutoa rushwa ama kulipa faini kamili ya Tshs. 30,000/=
  • Kutoheshimiwa kwa mahakama na sheria ya usalama barabarani
Askari wamejigeuza mahakama. Wanatuhumu wenyewe, wanakamata wenyewe na kutoa hukumu wao wenyewe, huu ni uvunjaji wa misingi ya haki jinai kwa kuwa mahakama ndio chombo pekee cha kutoa haki na kumtia hatiani mtu na pia mtu hawezi kuwa mwamuzi kwenye kesi yake mwenyewe. Uwepo wa fomu ya polisi namba 101 unasisitiza haki ya dereva kufikishwa mahakamani pale anapokataa kosa alilotuhumiwa, huo ndo utawala wa sheria. Kwa sasa hakuna utekelezaji wa jambo hilo ilhali bado kwenye sheria ya usalama barabarani lipo vilevile. Polisi hawaiheshimu mahakama wala sheria wanayoisimamia.

NINI KIFANYIKE?
  • Fomu ya Polisi Na. 101 irudishwe kwenye matumizi. Dereva awe na uhuru wa kukubali kosa au kulikataa ili afikishwe mahakamani na kusomewa shtaka lake.
  • Kuwe na kamera za kwenye mavazi ya askari usalama barabarani (body camera). Hizi zitakuwa zinarekodi kila jambo analofanya askari barabarani, na zitazuia askari kupokea rushwa kwa kuwa wataogopa kumbukumbu kwenye kamera.
  • Kuwe na kamera za spidi zisizohamishika. Utaratibu wa kumpa askari, kamera ya mkononi, umesababisha wazitumie kubambikia watu makosa kwa kuwapiga picha hata mahali pasipo na vibao vya ukomo wa mwendokasi na kisha kuwaandikia faini.
  • Jeshi la Polisi lijikite kwenye jukumu la msingi la kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara ili kuzuia ufanyikaji wa makosa barabarani na sio kujigeuza wakusanya mapato wa serikali kwa kuwa hapo ndipo panapozalisha upenyo wa rushwa.
Ahsante.
 
Back
Top Bottom