Watu wawili wanadhaniwa kufariki na mmoja kujeruhiwa kufuatia ajali iliyohusisha gari dogo aina ya Toyota Harrier lililogongana na lori aina ya Fuso eneo la Melela Mangae wilayani Mvomero mkoani Morogoro.
Ajali hiyo ni ya tatu ndani ya siku tatu mkoani hapo, ambapo juzi basi dogo aina ya Coaster liligongana na lori katika eneo la Iyovi na nyingine iliyohusisha Noah na lori aina ya Fuso iliyotokea kwenye Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.
Jitihada za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Alex Mkama zinaendelea ili kuzungumia ajali hiyo.
Hata ofisa habari wa jeshi hilo alipoombwa na waandishi wa habari kusaidia kupatikana kwa Kamanda huyo amesema kuwa kiongozi huyo yupo kikaoni.
Akizungumza na Mwananchi katika eneo la ajali leo Juni 8, 2023, mmoja wa mashuhuda aliyejitambulisha kwa jina la Adilinia Juma mkazi wa Melela Mangae, amesema ajali hiyo ilitokea usiku na amedai miili ya marehemu na majeruhi walipelekwa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Morogoro.
Juma amesema walisikia kishindo cha kugongana gari hizo na walipotoka waliona ajali hiyo na kuanza kutoa msaada.
"Kwenye hii gari dogo walikuwemo watu watatu ni kama familia hivi na waliokuwa mbele ndiyo wamekufa hapa hapa, aliyekuwa amekaa nyuma amejeruhiwa tu," amesema.
Aidha amesema askari walifika eneo la tukio na kusaidia kuondoa miili na majeruhi, huku akidai kuwa kwenye Fuso hakuna aliyeumia
Naye mkazi wa Mangae, Jabiri Abdallah amesema kipindi hiki cha mvua madereva wanatakiwa kuwa makini barabarani kwani kumekuwa na ajali nyingi zinazosababisha vifo na majeruhi.
CREDIT: MWANANCHI