Zimesikika habari kuwa chama cha ACT Tanzania au Wazalendo kama kinavyojiita sasa, kimeandika barua kuomba kujiunga na umoja wa vyama vya upinzani ujulikanao kama UKAWA. Mimi naona kukubali kukikaribisha chama hicho ndani ya ukawa ni sawa na kukubali kusambaratishwa au kuchanganywa lugha kama ilivyokuwa kwa wajenzi wa mnara wa Babeli katika Biblia. Hii ni kwasababu kauli na mienendo ya viongozi wake toka awali zimejidhihirisha kuwa wako kinyume na UKAWA na hivyo wanataka kuingia ili kuwasambaratisha.
Kiongozi mkuu wa chama hicho alidai kuwa yeye hakubaliani na UKAWA kwakuwa UKAWA inataka kuvunja muungano kwa kutaka serikali tatu. Huyu pia ndiye aliyekuwa kuwa mmoja wa viongozi wa juu katika chama cha CHADEMA lakini akafukuzwa kutokana na usaliti na kutoa mambo ya chama kwa chama tawala. Kudhihirisha kuwa ni kweli alikuwa msaliti, yeye mwenyewe amekiri kuwa alikuwa akikutana mara kwa mara na JK na kwa muda anaotaka ili kujadili masuala ya nchi. Sasa jiulizeni, kiongozi wa chama cha upinzani anakutana mara kwa mara na rais kujadili masuala ya nchi bila viongozi wenzake katika chama kujua na hakuna taarifa yoyote inayotolewa kwa umma, hayo masuala ya nchi ni yapi mpaka iwe siri kati ya rais na kiongozi wa chama cha upinzani. Sasa mkimwingiza mtu kama huyo kwenye umoja wenu maana yake mikakati yenu yote ya kisisasa atakuwa anakwenda kujadili na chama tawala na rais wake. Mbona huwa tunaona rais anakutana na wapinzani kujadili masuala mbali mbali ya nchi kama ilivyo kuwa wakati wa maandalizi ya kuandika katiba mpya ambapo amekutana nao mara kama 2 na taarifa zake kutolewa hadharani. Sasa hayo ya Kiongozi mkuu wa hicho wakati huo akiwa CDM na rais yalikuwa yepi? Kama ni ya nchi, mbona hakuna tamko walilokuwa wanalitoa baada ya mazungumzo yao ya mara kwa mara?
Ukiacha kiongozi mkuu wa hicho chama, mwenyekiti wake alitangaza hadharani kuwa ni marufuku kwa wanachama wake kushabikia au kuunga mkono UKAWA. Sasa leo wamegundua nini kuwa UKAWA ni muhimu? Mimi nilifikiri cha kwanza kwa wao ni kutengua kauli zao na kuomba radhi kwa UKAWA kisha waombe kufikiriwa kuingizwa katika umoja huo. Lakini hiki chama sio cha kuaminika hata kidogo. Ni vigeu geu. Viongozi wake hawaaminiki na kinaonaonesha wazi kinafadhiliwa na chama tawala hivyo kuwakaribisha katika UKAWA ni kama kutia nazi katika supu! Hawa wakaunde UKAWA yao na CCM
Zaidi ya hayo, hiki chama kina kesi mahakamani ambapo kinaonekana kuporwa na hao ambao leo wanajiita ndio viongozi wake na ambao wanataka kuingia UKAWA. Viongozi wa chama hiki wanadaiwa kupora chama cha wenyewe na kukibadili jina, nembo na kadi na pia kupandikiza watu akiwemo anayejiita kiongozi mkuu. Wenye chama chao na ambao ni waanzilishi wamefungua madai mahakamani.