-Miaka saba imepita,
tangu ulipoibuka,
jemedari kujikita,
harakati kuongoza.
-Hatamu ukazishika,
kuongoza tafakari,
imetosha kupigika,
kwa maslahi kiduchu.
-Daktari sio punda,
wa kubebeshwa mizigo,
na mgongo kumpinda,
daima akitumika.
-Wito isiwe ni fimbo,
ya kutodai mafao,
msitupiwe makombo,
wengine wakila kuku!
-Pamoja mkashikana,
kudai haki zaidi,
na sime mkatiana,
mkasimama imara.
-Sumaye akawajia,
kwa makeke na mikwara,
mwishowe akachukia,
kuambiwa iwe noma.
-Uli hukutetereka,
na mwenzio Kigwangwala,
wala hamkutishika,
kucheleweshwa hitimu.
-Hukuwa mbinafsi,
japo walikuandama,
ukazikosa nafasi,
ajira serikalini.
-Wengi walifaidika, kwa majitoleo yako,
ijara kuongezeka,
japo hukuifaidi
-AMO, CO na nesi, wote walichekelea,
nao wakajinafasi,
kupitia jasho lako.
-Maisha yakasogea,
na siku zaendelea, wapo walokusahau,
na wala siwalaumu.
-Mwaka huu ukaanza,
na mambo yake ni mapya,
Njelekela kajiponza,
Interns kuwachokoza.
-Kaka zao wakaguna,
mbona mnawaonea,
wakaamua kwa kina, na utangazwe mgomo.
-Ulimboka hukulemba,
unahodha ukashika,
vuguvugu likatamba,
nchi ikatikisika.
-Pinda katoa vitisho,
watu wakamtazama,
likamtoka na jasho,
hadi kwenye meno yake.
-Mwisho kadai suluhu,
ahadi akazimwaga,
na mrejee kazini,
yote yatatekelezwa
-Kumbe ni danganya toto,
hakuna lililojiri,
mazingira na kipato,
vyote vikatelekezwa!
-Madokta wakagoma,
Rais akawasihi,
na wao wakamsoma,
wakarejea kazini.
-Siku tisini zapita,
madai yajadiliwa,
mwisho tamko lapita,
hakuna pesa hazina.
-Madokta wajadili,
hili haliwezekani,
huu ni udhalili,
fani yetu kutendewa.
-Wakaitisha mgomo,
juni ishirina tatu,
usokuwa na kikomo,
huu ni aina yake!
-Kortini wakaenda,
serikari wasikivu,
kuuzuia mgomo,
wajifiche udhaifu.
-MAT wakaishitaki,
na kujitoa akili,
ya kwamba ni jumuia,
iloitisha mgomo.
-Walipokuja ng'amua,
ya kuwa wamepotoka,
Ulimboka wamsaka, na kumtia nguvuni.
-Walimpiga vigongo,
na taya wakamvunja,
wakamponda ubongo,
ili akome fikiri.
-Na mbavu wakamvunja,
msituni wambwaga,
maskini kajikunja,
wakadhani amekufa
-Ujumbe kwao majuha ,
waliyoyatenda haya,
damu ya Dokta Uli,
haitamwagika bure.
-Amani tunda la haki, hailetwi kwa mtutu,
kwa vile wastahiki,
madokta watashinda.
-Na daima mkumbuke,
mabavu yana mipaka,
mamlaka yenu yote,
yatoka kwa wananchi.
-Daktari Ulimboka, ninakuombea heri,
Mungu akupe fanaka,
na afya njema daima.
MWENYE HAKI DAIMA ATASTAWI KAMA MTENDE, NAAM, KAMA MWEREZI WA LEBANONI!