Waziri wa Ulinzi Na JKT, Dkt Stergomena Tax akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Ulinzi 2022/23 Bungeni

Roving Journalist

JF Roving Journalist
Apr 18, 2017
2,810
11,977
Hotuba ya Waziri wa Ulinzi na JKT, Dkt. Stergomena Tax wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara yake kwa mwaka wa Fedha 2022/2023 Bungeni, Mei 19, 2022.



KAMATI NUU.JPG


HOTUBA YA DKT. STERGOMENA LAWRENCE TAX (MB), WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA KUHUSU
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023

A: UTANGULIZI​


Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo ndani ya Bunge lako Tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupokea na kujadili Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 kwa Fungu 57 - Wizara, Fungu 38 – NGOME, na Fungu 39 - JKT pamoja na kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia uzima na afya njema na kutuwezesha kukutana, wakati nchi yetu ikiwa katika hali ya amani na usalama. Aidha, kwa unyenyekevu namshukuru kwa dhati Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, kwa kuniamini na kuniteua kuiongoza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Pia, namshukuru kwa kuendelea kumuamini Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee, nampongeza Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais na Amiri Jeshi Mkuu kwa jitihada mahususi ambazo zimeliwezesha Taifa letu kuendelea kuwa na amani na mshikamano. Vile vile, napenda kuwashukuru Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, na Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wao makini, na kwa maelekezo na miongozo wanayonipatia katika kutekeleza majukumu ya Wizara yangu.

Mheshimiwa Spika, napenda kukupongeza wewe binafsi Mhe. Dkt Tulia Ackson Mwansasu (Mb.), Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuongoza Mhimili wa Bunge. Vile vile, nampongeza aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Mussa Azzan Zungu (Mb.) kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika. Nampongeza pia kwa uongozi wake thabiti na miongozo aliyotupatia akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya NUU. Miongozo iliwezesha kutekeleza majukumu ya Wizara kwa tija na ufanisi. Mwenyezi Mungu aendelee kuwapa maarifa, hekima, busara na nguvu ili muendelee kuliongoza vyema Bunge letu Tukufu. Aidha, nampongeza Mhe. Vita Rashid Kawawa (Mb.) kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza kwa dhati waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri walioaminiwa na kuteuliwa kuziongoza Wizara mbalimbali katika Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, nawapongeza Mhe. Emmanuel Lekishon Shangai kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, na Mhe. Shamsi Vuai Nahodha kwa kuteuliwa kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kukupongeza wewe binafsi, Mhe. Dkt. Tulia Ackson Mwansasu (Mb.), Spika wa Bunge hili, Mhe. Mussa Azzan Zungu (Mb.), Naibu Spika, pamoja na Waheshimiwa Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge kwa kuendelea kuliongoza Bunge hili kwa mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kumpongeza Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule, kwa kuteuliwa kuwa Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi. Aidha, napenda kuwapongeza Meja Jenerali Anthony Chacha Sibuti, kwa kuteuliwa kuwa Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Meja Jenerali Shaban Barghashi Mani, kuwa Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Anga, Rear Admiral Ramson Godwin Mwaisaka, kuwa Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, na Brigedia Jenerali Idd Said Nkambi kuwa Mkuu wa Kamandi ya Vikosi Chini ya Makao Makuu ya Jeshi.

Mheshimiwa Spika, ninaungana na wenzangu waliotangulia kutoa salamu za pole kwako Mhe. Spika na Bunge lako Tukufu kwa kuondokewa na aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Mbunge wa Jimbo la Ushetu Hayati Elias John Kwandikwa, aliyekuwa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro Hayati William Tate Ole Nasha na aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, Marehemu Irene Alex Ndyamkama. Naomba kutoa pole kwa familia, ndugu na jamaa, na watanzania wote kwa kuondokewa na wapendwa hao. Namuomba Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema, peponi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mhe. Vita Rashid Kawawa (Mb.) akisaidiana na wajumbe wa Kamati kwa maoni na ushauri wanaoendelea kutupatia, na kwa maandalizi ya bajeti hii. Maoni, ushauri na maelekezo ya Kamati wakati wakichambua Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022, na mapendekezo ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023, vimesaidia kuboresha mapendekezo ya makadirio ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023, ninayowasilisha leo hapa bungeni.

B: UTEKELEZAJI WA MAAGIZO YA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA​

Mheshimiwa Spika, katika kikao kilichofanyika tarehe 29 Machi, 2022 Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama ilipitia na kujadili utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022. Kamati ilitoa maoni, ushauri, na maelekezo kwa Wizara yaliyolenga kuboresha utendaji kazi na utekelezaji wa majukumu. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa maoni, ushauri, na maelekezo yaliyotolewa yamefanyiwa kazi na kuzingatiwa wakati wa kuandaa na kukamilisha Mpango na Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2022/2023 ninayowasilisha leo hapa bungeni.

C: UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI YA CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) YA MWAKA 2020 NA DIRA YA TAIFA 2025 KWA MWAKA WA FEDHA 2021/2022​

Mheshimiwa Spika, Katika utekelezaji wa mpango na bajeti katika Mwaka wa
Fedha 2021/2022, Wizara imeendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 kwa masuala yaliyoainishwa katika Sura ya Tano Ibara ya 105 ya Ilani ambayo ni:

“Kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi na mipaka yake ili kudumisha Muungano, kulinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, umoja, mshikamano, amani na usalama wa raia na mali zao;

Kuendeleza jitihada za utatuzi wa changamoto za mipaka ya nchi yetu na nchi jirani;

Kuwezesha ushirikiano wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kufanya utafiti na ubunifu kwa kushirikiana na taasisi za utafiti;

Kuhusisha kikamilifu Majeshi ya Ulinzi na Usalama katika kulinda miradi mikubwa ya kimkakati;

Kuhamasisha na kuelimisha wananchi juu ya masuala ya ulinzi, uzalendo wa kitaifa, usalama na umuhimu wa kushiriki katika ulinzi ikiwa ni pamoja na Jeshi la Akiba na ulinzi shirikishi ili kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi yetu;

Kuimarisha uwezo wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama katika kushiriki shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuanzisha viwanda katika sekta ya ulinzi na maeneo mengine ya kimkakati;

Kuimarisha viwanda vya NYUMBU na Mzinga ili viweze kutimiza azma ya kuanzishwa kwake;

Kuimarisha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU) ili viwe vyombo vya kuwapatia vijana ujuzi wa kujiajiri na kuajiriwa na pia kuwa vyombo mahiri vya huduma na uzalishaji mali hasa katika ujenzi, kilimo, ufugaji na uvuvi;

Kupanua na kuongeza idadi ya kambi za JKT na JKU ili kuwezesha vijana wengi zaidi wakiwemo wahitimu wote wa kidato cha sita kupata fursa ya mafunzo ili kujenga uzalendo na moyo wa kujitolea; na

Kuboresha mazingira ya kazi kwa kuwapatia makazi bora na kuongezea uwezo wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kuvipatia mafunzo ya kitaaluma na kitaalam, vitendea kazi na zana za kisasa zinazoendana na teknolojia ya kisasa;



D: MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA bAJETI YA MWAKA WA FEDHA 2021/2022
Mheshimiwa Spika
, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara ilikadiria kukusanya maduhuli ya jumla ya Shilingi 85,103,000.00 kutoka katika mafungu yake matatu; Fungu 38 – NGOME, Shilingi 22,000,000.00, Fungu 39 – JKT, Shilingi 61,903,000.00 na Fungu 57 - Wizara Shilingi 1,200,000.00.

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Aprili 2022 Wizara imefanikiwa kukusanya maduhuli ya jumla ya Shilingi 120,558,848.50 sawa na asilimia 141.66 ya makadirio. Kwa upande wa Fungu 38 – NGOME, yamekusanywa maduhuli yenye jumla ya Shilingi 43,191,408.00 sawa na asilimia 196.32 ya makadirio, yanayotokana na mauzo ya nyaraka za zabuni, na malipo ya kamisheni zinazotokana na makato ya bima kwa wanajeshi kutoka makampuni mbalimbali ya bima. Fungu 39 – JKT limekusanya Shilingi 61,900,000.00 sawa na asilimia 99.99 ya makadirio, zilizotokana na mauzo ya nyaraka za zabuni, mauzo ya mazao ya bustani (mboga mboga na matunda), bidhaa za mifugo, nafaka na bidhaa zitokanazo na ufugaji wa nyuki. Fungu 57 – Wizara, imekusanya Shilingi 15,467,440.50 sawa na asilimia 1,288.95 ya makadirio, zilizotokana na huduma ya Mtandao wa Mawasiliano Salama na mapato ya Ulinzi Chanel iliyopo kwenye mtandao wa YouTube. Muhtasari wa mchanganuo wa maduhuli kwa kila Fungu umeoneshwa kwenye Jedwali Na. 1.

Jedwali Na. 1: Muhtasari wa Mchanganuo wa Makusanyo ya Maduhuli Kuanzia Julai, 2021 hadi Aprili 2022

Na.FunguMakadirio ya Mapato 2021/2022Makusanyo Julai 2021 hadi Aprili, 2022Makusanyo (%)
138 - NGOME
22,000,000.00​
43,191,408.00​
196.32​
239 – JKT
61,903,000.00​
61,900,000.00​
99.99​
357 – Wizara
1,200,000.00​
15,467,440.50​
1,288.95​
Jumla
85,103,000.00
120,558,848.50
141.66


Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliidhinishiwa jumla ya Shilingi 2,358,694,986,000.00 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika mafungu yake matatu:

Fungu 38 - NGOME, Fungu 39 - JKT na Fungu 57 - Wizara. Kati ya fedha hizo, Shilingi 2,182,116,562,000.00 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, na Shilingi 176,578,424,000.00 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Katika kiasi hiki; Fungu 38 – NGOME limeidhinishiwa fedha za matumizi ya kawaida.

Shilingi
1,779,475,285,000.00, na fedha za maendeleo Shilingi 32,578,424,000.00, Fungu 39 – JKT limeidhinishiwa fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 382,474,955,000.00, na fedha za maendeleo Shilingi 4,000,000,000.00, Fungu 57 – Wizara limeidhinishiwa fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 20,166,322,000.00, na fedha za maendeleo Shilingi 140,000,000,000.00. Muhtasari wa Mchanganuo wa bajeti kwa kila fungu umeainishwa katika Jedwali Na. 2.

Jedwali Na. 2: Muhtasari wa Mchanganuo wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022


Na.FunguMatumizi ya Kawaida Matumizi ya Maendeleo
Jumla
138 - NGOME1,779,475,285,000.0032,578,424,000.001,812,053,709,000.00
239 - JKT382,474,955,000.004,000,000,000.00386,474,955,000.00
357 - Wizara20,166,322,000.00140,000,000,000.00160,166,322,000.00
Jumla2,182,116,562,000.00176,578,424,000.002,358,694,986,000.00


Mheshimiwa Spika,
hadi kufikia Aprili 2022 fedha zilizopokelewa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo ni Shilingi 1,929,384,355,854.61 sawa na asilimia 81.80 ya bajeti iliyoidhinishwa. Kati ya fedha hizo, Shilingi 1,798,774,637,752.05 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, na Shilingi 130,609,718,102.56 ni kwa ajili ya shughuli za maendeleo.

Katika kiasi hiki; Fungu 38 – NGOME limepokea fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 1,477,045,706,363.96, na fedha za maendeleo Shilingi 32,504,052,178.52; Fungu 39 – JKT limepokea fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 307,109,843,712.78, na fedha za maendeleo Shilingi 3,272,048,797.00; na Fungu 57 – Wizara limepokeaa fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 14,619,087,675.31, na fedha za maendeleo Shilingi 94,833,617,127.04. Muhtasari wa mchanganuo wa mapokezi ya fedha kwa mafungu yote umeainishwa katika Jedwali Na. 3
Jedwali Na. 3: Muhtasari wa Mchanganuo wa Fedha Zilizopokelewa Kuanzia Julai, 2021 hadi Aprili, 2022

Na.
Fungu
Matumizi Yaliyoidhinishwa
Bajeti ya Mwaka 2021/2022
Kiasi Kilichopokelewa Hadi Aprili, 2022Asilimia
1​
38 - NGOME​
Malipo na Posho (Pay and Allowance)
1,457,024,047,000.00​
1,211,840,186,673.43​

83.17​
Chakula na Posho ya Chakula
219,284,700,000.00​
182,737,250,000.00​
83.33​
Matumizi Mengineyo
41,086,938,000.00​
33,577,569,690.53​
81.72​
Misamaha ya Kodi
62,079,600,000.00​
48,890,700,000.00​
78.75​
Maendeleo
32,578,424,000.00​
32,504,052,178.52​
99.77​
Jumla ya Fungu
1,812,053,709,000.00
1,509,549,758,542.48
83.31​
2​
39 - JKT​
Malipo na Posho (Pay and Allowance)
253,578,848,000.00​
207,153,323,435.00​

81.69​
Chakula na Posho ya Chakula
60,150,270,000.00​
47,768,858,500.00​

79.42​
Matumizi Mengineyo
35,376,602,524.00​
27,738,009,701.78​

78.41​
Mafunzo ya Vijana wa Mujibu wa Sheria
21,636,234,476.00​
16,349,652,076.00​

75.57​
Posho ya Msamaha wa kodi
11,733,000,000.00​
8,100,000,000.00​

69.04​
Maendeleo
4,000,000,000.00​
3,272,048,797.00​
81.80​
Jumla ya Fungu
386,474,955,000.00
310,381,892,509.78
80.31
3​
57 - Wizara​
Mishahara (Wizara na Mashirika)
10,221,977,000.00​
7,081,687,000.00​

69.28​
Ruzuku (Mashirika na Majenerali)
6,874,634,814.00​
4,893,672,862.99

71.18​
Matumizi Mengineyo
3,069,710,186.00​
2,643,727,812.32​
86.12​
Maendeleo
140,000,000,000.00​
94,833,617,127.04​
67.74​
Jumla ya Fungu
160,166,322,000.00
109,452,704,802.35
68.34
JUMLA KUU
2,358,694,986,000.00
1,929,384,355,854.61
81.80


Fedha za Matumizi ya Kawaida:
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara imefanikiwa kutekeleza shughuli mbalimbali kwa kutumia fedha zilizotolewa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo. Kwa fedha zilizotolewa kwa matumizi ya kawaida, Wizara imeweza kutekeleza shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na: mafunzo ya kijeshi, mafunzo ya Jeshi la Akiba, huduma za afya na tiba, ushirikiano wa kiulinzi na kijeshi na nchi nyingine, ushirikiano na mamlaka za kiraia katika shughuli mbalimbali za kitaifa, mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa, mapambano dhidi ya magonjwa ambukizi na yasiyoambukiza, utawala bora na utunzaji wa mazingira.

Mafunzo ya Kijeshi
Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) imeendelea kutoa mafunzo mbalimbali ya kozi za kijeshi katika shule na vyuo vya kijeshi ndani na nje ya nchi, kwa ajili ya kuwapatia wanajeshi mafunzo ya awali, na kuwaendeleza katika taaluma mbalimbali za uongozi. Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Wizara imeendelea kuratibu na kuendesha mazoezi na mafunzo. Katika kipindi husika, JWTZ ilifanikiwa kufanya zoezi la pamoja liitwalo ‘Joint Combined Exchange Training’ (JCET) ambalo lilifanyika kuanzia tarehe 28
Julai 2021 hadi tarehe 10 Septemba 2021 kwa ushirikiano na Jeshi la Marekani. Zoezi hili lilifanyika Kunduchi Mkoa wa Dar es Salaam, likiwa na lengo la kuimarisha uwezo wa kukabiliana na matishio ya kigaidi nchini na nchi tunazopakana nazo.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia JWTZ imeendelea kupanga, kuratibu na kusimamia mafunzo ya Maafisa na Askari nje ya nchi. Hadi kufikia tarehe 30 Aprili, 2022, jumla ya Maafisa na Askari 490 wanahudhuria mafunzo nje ya nchi.

Mafunzo ya Jeshi la Akiba
Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia JWTZ imeendelea kutoa mafunzo ya Jeshi la Akiba kwa wananchi katika ngazi ya awali. Mafunzo hayo hufanyika katika mikoa yote ya Tanzania. Katika kipindi cha Julai 2021 hadi Aprili 2022. Jumla ya wananchi walioandikishwa na kuhitimu mafunzo hayo ni 12,510, kati yao wanaume 10,750 na wanawake 1,760. Vile vile, JWTZ kupitia kamati za usalama za Mikoa na Wilaya, imeendelea kuelimisha wananchi juu ya masuala ya Ulinzi na Usalama.

Huduma za Afya na Tiba
Mheshimiwa Spika,
Katika kipindi husika, Wizara kupitia JWTZ imeendelea kutoa huduma za tiba kwa Maafisa, Askari, Watumishi wa Umma, familia za wanajeshi, na wananchi wanaoishi karibu na vituo vya tiba vya Jeshi hapa nchini. Katika kuboresha huduma hizo, juhudi mbalimbali zimefanyika ikiwemo: kuongeza upatikanaji wa madawa na vifaa tiba, huduma ya usafishaji wa Figo katika Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo (GMH), kuboresha huduma katika Hospitali za Kanda na vituo vya tiba vikosini, na utoaji wa huduma za Bima ya Afya Jeshini.

Ushirikiano wa Kiulinzi na Kijeshi na Nchi Nyingine
Mheshimiwa Spika,
JWTZ imeendelea kushirikiana na nchi rafiki katika masuala ya ulinzi na usalama katika maeneo mbalimbali, ikiwemo mafunzo, misaada ya kitaalamu, zana na vifaa. Vile vile, JWTZ inashirikiana na Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) katika mafunzo na ubadilishanaji wa wataalamu. Pia, JWTZ inaendelea kushirikiana na nchi rafiki katika kutoa mafunzo kwa maafisa na askari. Nchi hizo ni pamoja na Algeria, Bangladeshi, Canada, Falme za Kiarabu, Finland, Ghana, Hispania, India, Indonesia, Israeli, Jamhuri ya Watu wa China, Jordani, Marekani, Misri, Morocco, Nigeria, Omani, Pakistani, Sri Lanka, Sweden, Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, Urusi, Uturuki, na Uswisi.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) imeendelea kutoa mafunzo ya Usalama na Stratejia kwa Maafisa wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, pamoja na Viongozi katika Utumishi wa Umma kuanzia ngazi ya Wakurugenzi Wasaidizi. Aidha, katika kipindi husika, Chuo kimetoa mafunzo hayo kwa washiriki kutoka nchi za, Afrika Kusini, Bangladeshi, Botswana, Burundi, China, Kenya, Malawi, Misri, Msumbiji, Namibia, Nigeria, Rwanda, Uganda, Zambia, na Zimbabwe.

Ushiriki wa JWTZ Katika Shughuli za Ulinzi wa Amani
Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia JWTZ imeendelea kushirikiana na Jumuiya za Kikanda na Kimataifa katika operesheni za ulinzi wa amani chini ya Umoja wa Mataifa. Hadi sasa, Kikosi kimoja na Vikundi vidogo vidogo vipo mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, chini ya Misheni ya Umoja wa Mataifa (The United Nations Organization Stabilization Mission in the Democratic Republic of the Congo – MONUSCO).

Kikosi kingine kipo Jamhuri ya Afrika ya Kati, chini ya Misheni ya Umoja wa Mataifa (United Nations Multi dimensional Integrated Stabilization Mission in the Central African Republic - MINUSCA), na Kombania mbili za Polisi Jeshi zipo nchini Lebanon (United Nations Interim Force in Lebanon - UNIFIL).

Aidha, JWTZ linashiriki operesheni ya kupambana na ugaidi nchini Msumbiji (SADC Mission in Mozambique - SAMIM). Vile vile, Jeshi lina Maafisa wanadhimu na Makamanda kwenye operesheni za ulinzi wa amani nchini Sudan, Sudan Kusini, Lebanon, Jamhuri ya Afrika ya Kati na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ushiriki wa JWTZ katika operesheni za Ulinzi wa Amani chini ya Umoja wa Mataifa umeiwezesha nchi yetu kutimiza matakwa ya Umoja wa Mataifa na Jumuiya za Kikanda wa kushiriki katika ulinzi wa amani kimataifa na kikanda.

Vilevile, ushiriki huu unaendeleza Diplomasia ya Kijeshi (Military Diplomacy), na unasaidia JWTZ kupanua uwezo kwa kufanya kazi na Nchi nyingine.

Ushirikiano na Mamlaka za Kiraia katika shughuli mbalimbali za Kitaifa
Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia JWTZ imeendelea kushirikiana na Mamlaka za Kiraia katika shughuli mbalimbali ikiwemo, kutoa misaada wakati wa majanga na maafa, kushiriki katika utekelezaji na ulinzi wa miradi ya kimkakati ikiwa ni pamoja na Reli ya Kiwango cha Kimataifa (Standard Gauge Railway), Bwawa la Kufua Umeme wa Maji la Julius Nyerere (JNHPP), Mgodi wa Tanzanite, Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), na maeneo ya Viwanja vya Ndege.

Mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa
Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia JKT imeendelea kuwapatia vijana wa Kitanzania mafunzo ya ukakamavu, stadi za kazi, kuwajengea uzalendo na umoja wa kitaifa. Katika kipindi husika mafunzo kwa Vijana wa Mujibu wa Sheria na Kujitolea yamefanyika kwenye Kambi mbalimbali za Jeshi la Kujenga Taifa kupitia Operesheni Samia Suluhu ambapo jumla ya
vijana 25,503 wa Mujibu wa Sheria wamepatiwa mafunzo na kati yao 19,544 ni wa kiume na 5,959 ni wa kike. Aidha, vijana 11,739 wa Kujitolea wamepatiwa mafunzo na kati yao 8,165 ni wa
kiume na 3,574 ni wa kike.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuliarifu Bunge lako Tukufu pamoja na umma wa watanzania kwamba, dhumuni la mafunzo yanayotolewa kwa vijana ni kuwapatia stadi za kazi na stadi za maisha ili baada ya kumaliza muda wa mafunzo na kutumikia Jeshi la Kujenga Taifa, waweze kurejea majumbani kwao wakiwa raia wema wenye uwezo wa kujitegemea na kulilinda Taifa. Nitoe rai kwa vijana wote wanaopata fursa za kupata mafunzo hayo kuzitumia stadi za kazi walizozipata kujiajiri na kujitegemea.

Mapambano Dhidi ya Magonjwa Ambukizi na Yasiyoambukiza
Mheshimiwa Spika,
katika kupambana na Virusi vinavyosababisha Upungufu wa Kinga Mwilini, Ugonjwa wa Upungufu wa Kinga Mwilini, na Magonjwa yasiyoambukiza, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Wizara imeendelea kutekeleza mikakati ya kupambana na maambukizi mapya ya Virusi vya UKIMWI, magonjwa yasiyoambukiza pamoja, na UVIKO – 19. Wizara imeunda kamati inayoshughulikia masuala ya VVU, UKIMWI na magonywa yasiyo ya kuambukiza ili kutoa elimu ya kujikinga na magonjwa hayo.

Aidha, Wizara imeunda kamati ya UVIKO – 19, ili kuhamasisha na kutoa elimu kwa watumishi namna ya kujikinga na UVIKO – 19. Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara imeendelea kutoa huduma ya lishe kwa watumishi wenye maambukizi ya VVU. Hatua hizi zinachukuliwa kwa kuzingatia mwongozo wa udhibiti VVU na UKIMWI. Aidha, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Afya imetoa elimu na kuhamasisha upimaji wa hiari, na uchangiaji damu.

Utawala Bora
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Wizara pamoja na Taasisi zake imechukua jitihada mbalimbali ili kuimarisha Utawala Bora. Taasisi hizi zimekuwa zikiandaa taarifa za kila Robo Mwaka ambazo huwasilishwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Vile vile, Semina mbalimbali kwa watumishi, kuhusu jinsi ya kupambana na kuzuia rushwa mahala pa kazi zimeendelea kutolewa. Aidha, Wizara imekuwa ikishirikisha watumishi katika kutoa maoni na ushauri kupitia vikao mbalimbali, hususan Baraza la Wafanyakazi, Kamati ya Maadili, Bodi ya Manunuzi, na Kamati ya Ajira. Juhudi hizi zimelenga kuimarisha dhana ya Utawala Bora kwa Wizara na Taasisi zake.

Utunzaji wa Mazingira
Mheshimiwa Spika,
kwa upande wa shughuli za utunzaji wa mazingira, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara kupitia Taasisi zake imeendelea na utunzaji wa mazingira katika maeneo yake yenye miti ya asili, kuyalinda maeneo hayo yasivamiwe kwa shughuli za kijamii na kuendelea kupanda miti mipya. Vile vile, Wizara imeendelea na utunzaji wa fukwe katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga na Mtwara ili kuzuia mmomonyoko wa ardhi. Aidha, maeneo yote ya Jeshi yana zuio la ukataji miti, kuchoma mkaa, na kulisha mifugo. Napenda nitoe wito kwa wananchi wote kuzingatia zuio hili na kuepusha migogoro isiyo ya lazima.

Mheshimiwa Spika, katika dhana hii ya utunzaji wa mazingira Wizara imefanikiwa kupanda miti 147,724 katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika kambi za JWTZ, JKT na Shirika la Mzinga. Baadhi ya miti hiyo imepandwa pembezoni mwa kingo kuzunguka Bwawa la Mindu, kwa ushirikiano kati ya Shirika la Mzinga na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (Morogoro Water Supply and Sanitation Authority – MORUWASA). Pia, Kikosi cha Mzinga hufanya doria kwenye eneo hilo ambalo ni chanzo kikubwa cha maji katika Mkoa wa Morogoro kuhakikisha mazingira yake yanaendelea kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, mashirika yaliyo chini ya Wizara ambayo ni Tanzania Automotive Technology Centre (TATC), MZINGA na SUMAJKT yameendelea na uzalishaji kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za uhifadhi wa mazingira, ikiwa ni pamoja na njia za kisasa za kutibu maji yenye kemikali yanayotoka viwandani. Vile vile, viwanda vimeendelea na utaratibu wa kuwapa wafanyakazi wake vifaa kinga vyenye mfumo wa kudhibiti sauti ili kuzuia kelele.

Mheshimiwa Spika, kama wote tunavyoelewa Jeshi letu linamiliki maeneo ya kimkakati katika mikoa mbalimbali nchini, na maeneo haya yametengwa maalum kwa matumizi ya kijeshi. Hivyo, napenda kutumia fursa hii kutoa rai na kuwaasa wananchi kutovamia maeneo ya Jeshi kwa ajili ya makazi au kuendesha shughuli zao za kila siku, kwani kufanya hivyo ni kuhatarisha usalama na maisha yao kutokana na uhalisia wa shughuli za kijeshi zinazofanyika katika maeneo hayo ikiwemo mafunzo na mazoezi mbalimbali ambayo yanatumia risasi za moto na milipuko. Aidha, kwa kufanya uvamizi katika maeneo hayo, ni kuhatarisha usalama wa Taifa, na kukwamisha baadhi ya shughuli muhimu za kuliweka tayari Jeshi letu kukabiliana na matishio yeyote yanayoweza kujitokeza. Uvamizi huo hupelekea pia migogoro ya ardhi isiyo ya lazima.

Matumizi ya Fedha za Maendeleo
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Wizara imeweza kutumia fedha za maendeleo kutekeleza shughuli zifuatazo :

Ununuzi wa zana, vifaa, risasi na mabomu;

Uhuishaji na uboreshaji wa zana za ulinzi wa anga, matengenezo na matunzo ya zana za kioperesheni za nchi kavu, na majini;

Ujenzi wa mahanga ya kuhifadhia helikopta katika mikoa ya Dodoma na Geita;

Kugharamia mkataba wa matunzo ya helikopta;

Kugharamia ujenzi wa maghala ya kuhifadhi zana na vifaa;

Kuboresha miundombinu ya majengo katika Hospitali ya Jeshi ya Kanda – Mwanza ambapo VIP ward, chumba cha kuhifadhia maiti, na Bweni la Askari Kapera wa kike yamejengwa;

Kugharamia Mradi wa Mawasiliano Salama Jeshini;

Kutatua migogoro ya ardhi kwa kupima na kufanya uthamini pamoja na kulipa fidia kwa wananchi wa maeneo matano (5), eneo la Kaboya - Muleba Mkoa wa Kagera, Nyamisangura Mkoa wa Mara, Mitwero Mkoa wa Lindi, Nyangunguru - Ilemela Mkoa wa Mwanza, na Usule Mkoa wa Tabora;

Ujenzi wa Maabara katika Shule ya Kijeshi ya Ulinzi wa Anga, umaliziaji wa ujenzi wa Karakana katika Shule ya Anga ya Kijeshi – Tanga;

Kugharamia ununuzi wa magari kwa ajili ya Makamanda, Waambata Jeshi na shuguli za utawala;

Kugharamia ununuzi wa zana za kilimo za JKT;

Kulipa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) katika mradi wa ujenzi wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC);

Mafunzo, ufuatiliaji na tathmini ya miradi;

Kununua magari mawili ya usimamizi wa miradi; na vifaa vya upimaji wa ardhi;

Kuendeleza ujenzi wa Makao Makuu ya JKT; na

Kuendeleza ukarabati wa miundombinu na usambazaji wa maji katika vikosi.

Mheshimiwa Spika, naomba pia kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, Wizara kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani kupitia German Armed Forces Technical Advisory Group (GAFTAG) imeanza ujenzi wa Hospitali Kuu ya Jeshi, Msalato – Dodoma. Hospitali hii itakuwa na hadhi ya Daraja la Nne (Level IV Hospital). Aidha, Wizara kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kupitia Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA) imekamilisha ujenzi wa Jengo la Mafunzo na Utawala katika Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC). Jengo hili limeanza kutumika baada ya kuzinduliwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu tarehe 14 Novemba, 2021.

Mheshimiwa Spika,
Wizara kupitia JKT imefanikiwa pia kutekeleza miradi mbalimbali kwa kutumia rasilimali za ndani ifuatavyo:

Ujenzi wa miundombinu ya Mradi wa Skimu ya Umwagiliaji katika Kikosi cha Chita Mkoa wa Morogoro;

Kilimo cha Chikichi (Migazi) katika Kikosi cha Bulombora Mkoa wa Kigoma;

Kilimo cha Mkonge katika vikosi vya Maramba na Mgambo Mkoa wa Tanga;

Kilimo cha kahawa katika vikosi vya Itende Mkoa wa Mbeya na Rwamkoma Mkoa wa Mara;

Kilimo cha Korosho katika vikosi vya Nachingwea, Makutopora, Ruvu na Kibiti katika mikoa ya Lindi, Singida na Pwani mtawalia. Aidha, shamba la Korosho la Kikosi cha Ruvu limepewa hadhi ya kuwa shamba darasa Mkoa wa Pwani;

Ufugaji wa Samaki katika vikosi vya Rwamkoma Mkoa wa Mara, Chita Mkoa wa Morogoro, na Ruvu Mkoa wa Pwani; na

Ufugaji wa nyuki katika vikosi vya Msange Mkoa wa Tabora, Kanembwa na Mtabila Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Spika, shamba la Korosho katika Kikosi cha Kibiti limezinduliwa
tarehe 02 Mei, 2022 na Kiongozi wa mbio za Mwenge kama shamba Darasa litakalotumika kutoa mafunzo kwa wakulima wa Wilaya ya Kibiti na maeneo jirani.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Shirika la TATC, Shirika la MZINGA na SUMAJKT imeendelea kutekeleza majukumu yake ifuatavyo;

Tanzania Automotive Technology Centre (TATC) - NYUMBU
Mheshimiwa Spika,
hadi kufikia Aprili 2022, TATC imepokea kiasi cha fedha
Shilingi 8,974,278,587.25 kati ya Shilingi 9,000,000,000.00 sawa na asilimia 99.71 ikiwa ni sehemu ya Fedha za maendeleo zilizopokelewa na Wizara, na kuweza kutekeleza shughuli za maendeleo zifuatazo:

Ununuzi wa mitambo kwa ajili ya kupima ubora wa chuma katika kitengo cha kukalibu chuma na maabara ya kuhakiki ubora wa bidhaa zinazozalishwa; na

Ujenzi wa jengo la kusimika mitambo ya kuzalisha bidhaa za chuma zisizoshika kutu (metal galvanizing plant).

Mheshimiwa Spika, ununuzi wa mitambo hii ni hatua kubwa itakayoliwezesha Shirika la TATC kukidhi mahitaji ya ndani na kutumia fursa za masoko nje ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi husika, TATC imetekeleza shughuli zifuatazo kwa kutumia rasilimali za ndani:

Kukamilisha ukarabati wa magari ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, na kuendelea na uundaji wa magari mapya ya kuzimia moto ya kiwango cha Manispaa;

Utengenezaji wa vifaa kwa ajili ya matumizi ya JWTZ ikiwemo; vitanda vya chuma na mobile field kitchen;

Utengenezaji wa vipuri mbalimbali (domestic flour milling machine, briquette rollers, brake blocks, hot plate holes na scrap crusher);

Ukarabati wa pampu za maji za Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Mkoa wa Dar es Salaam na Dodoma; na

Ukarabati wa incinerator za Hospitali ya Rufaa ya Tumbi mkoani Pwani na Temeke mkoani Dar es Salaam.


Shirika la MZINGA
Mheshimiwa Spika,
Shirika la Mzinga limepokea kiasi cha Shilingi 5,465,210,622.68 kati ya Shilingi 5,500,000,000.00 sawa na asilimia 99.37 ikiwa ni sehemu ya Fedha za maendeleo zilizopokelewa na Wizara, na kuweza kutekeleza shughuli za maendeleo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na;

ununuzi na ukarabati wa mitambo, uzalishaji wa zao la msingi, vipuri na zana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na shughuli za msingi, Shirika limeendelea na utekelezaji wa shughuli mbalimbali kwa kutumia fedha za ndani ifuatavyo:

Ukarabati wa silaha kutoka katika Vyombo vya Ulinzi na Usalama;

Uzalishaji wa vipuri kwa ajili ya mashine za uzalishaji wa zao la msingi;

Uzalishaji wa mabomu ya kufukuzia wanyama ambayo yanatumiwa na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa, pamoja na Halmashauri zinazopakana na Hifadhi hizo;

Ununuzi na uuzaji wa milipuko na silaha ndogo;

Kusimamia na kutunza zana na silaha zinazomilikiwa na makampuni yanayofanya ulinzi katika meli zinazotia nanga kwenye bandari zilizopo nchini;

Utengenezaji wa samani za aina mbalimbali;

Kupitia Kampuni Tanzu ya Mzinga Holding Company Limited, Shirika linaendelea na ukamilishwaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo Ofisi za Serikali; na

Ujenzi na ukarabati wa majengo ya hospitali ya Mzinga na Kituo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi Mzinga.


Shirika la Uzalishaji Mali la JKT
Mheshimiwa Spika,
SUMAJKT kwa kutumia vyanzo vyake vya ndani imeendelea na shughuli za uzalishaji mali kupitia kampuni tanzu na viwanda vyake, ili kuipunguzia Serikali gharama za malezi ya Vijana wanaojiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa. Shughuli hizo zinatekelezwa kupitia sekta ya ujenzi, viwanda na biashara, kilimo, mifugo, na ulinzi ifuatavyo:

Miradi ya Ujenzi ya Serikali ikiwemo: majengo ya Ofisi za Wizara na Taasisi zilizopo Mji wa Serikali – Mtumba mkoani Dodoma; ujenzi wa Maabara ya Sayansi katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine – Morogoro; ujenzi wa Makao Makuu ya Uhamiaji, na Makao Makuu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa iliyopo mkoani Dodoma; kusawazisha eneo la mradi wa ujenzi wa Hanga la Helikopta uliopo Chato mkoani Geita na ujenzi wa Maabara ya Shule ya Kijeshi ya Ulinzi wa Anga iliyopo mkoani Tanga;

Ujenzi wa miundombinu na usambazaji wa umeme vijijini katika mikoa ya Morogoro na Shinyanga, kufunga (installation) umeme katika Ofisi za Mamlaka ya Mapato Mkoa wa Singida, Shule ya Mfano Mkoa wa Dodoma, na Ofisi ya Rais (Ikulu) Chamwino

Kuimarisha viwanda vyake ikiwemo: Kiwanda cha Samani - Chang’ombe; Kiwanda cha kuzalisha maji ya kunywa ya Uhuru Peak; Kiwanda cha Ushonaji; Kiwanda cha Kuchakata Nafaka – Mlale JKT;

Ulinzi wa Taasisi za Umma na binafsi katika mikoa mbalimbali; na

Shughuli za kilimo katika shamba lililopo Mngeta, Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Spika, pamoja na fedha zilizotolewa kwa Wizara katika kutekeleza Mpango wa Bajeti wa Mwaka wa Fedha 2021/2022, naomba kuchukua fursa hii kuishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kwa kuendelea kutoa uzito katika shughuli za ulinzi, ikiwa ni pamoja na kutoa fedha nje ya Bajeti kiasi cha Shilingi 60,750,781,041.44 kwa ajili ya kugharamia operesheni maalum, ujenzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT – Kikombo), ununuzi wa kitambaa cha vazi la medani (Kombati), na kulipa malimbikizo ya mishahara kwa watumishi wa umma waliopanda vyeo na madaraja.

E: HALI YA ULINZI NA USALAMA WA MIPAKA YA NCHI​

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, hali ya mipaka ya nchi yetu yenye urefu wa jumla ya kilomita 5,461.20, ambayo inahusisha eneo la nchi kavu na eneo la maji, imeendelea kuwa shwari. Mipaka hiyo ni baina ya Tanzania na Msumbiji, Malawi, Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi, Rwanda, Uganda na Kenya. Katika kipindi hicho hapakuwa na matukio ya uhasama yaliyoripotiwa baina yetu na nchi tunazopakana nazo, licha ya kuwepo changamoto kadhaa.

Mheshimiwa Spika, naomba nielezee hali ya ulinzi na usalama wa mipaka ya nchi yetu na nchi tunazopakana nazo ifuatavyo;

Mpaka wa Tanzania na Msumbiji
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 843, ni ya wastani kutokana na mashambulizi yanayofanywa na kundi la kigaidi la Ansar Al Sunna Wal Jamaah (AASWJ) maeneo ya Kaskazini mwa Msumbiji, katika Jimbo la Cabo Delgado linalopakana na Mkoa wa Mtwara. Kundi hilo limekuwa likiathiri usalama kwa kuharibu na kupora mali za wananchi. Katika kupambana na changamoto hii, JWTZ imeendelea kuimarisha ulinzi kwa kufanya operesheni za ndani ya nchi na kukabiliana na kundi hilo.

Aidha, JWTZ inashiriki operesheni chini ya Mwamvuli wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika nchini Msumbiji (SADC Mission in Mozambique - SAMIM) katika jitihada za kudhibiti ugaidi. Operesheni hizi zimeendelea kuimarisha ulinzi katika eneo la Mpaka, kudumisha amani na utulivu.

Mheshimiwa Spika, operesheni zimesaidia kupunguza nguvu ya kundi hilo la kigaidi. Hata hivyo, kundi hilo linatekeleza mashambulizi kwa kuhamahama na kubadili mbinu za kimapigano. Licha ya hali hiyo, vikundi vyetu vinaendelea kupambana kuhakikisha kundi hilo halileti madhara zaidi. Wizara inaishukuru Serikali na hususan Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais na Amiri Jeshi Mkuu, kwa kutoa kipaumbele katika kupambana na suala hili, na kutoa fedha kwa ajili ya mahitaji mbalimbali yanayosaidia vikundi vya ulinzi kupambana na kundi hilo.

Mpaka wa Tanzania na Malawi
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama ya mpaka huu wenye urefu wa kilomita 394, ni shwari. Hakuna tukio la kuhatarisha usalama lililoripotiwa. Ushirikiano uliopo baina ya Jeshi letu na Jeshi la Malawi ni mzuri. Hali hiyo inajidhihirisha kutokana na mahusiano mazuri yaliyopo, ambayo yamepelekea kufanyika michezo ya kirafiki kati ya timu za majeshi ya nchi hizi mbili yaliyofanyika Brigedi ya Kusini mwezi Julai 2021. Changamoto ya mpaka katika Ziwa Nyasa inaendelea kufanyiwa kazi kupitia Tume Maalum ya Usuluhishi (High Level Mediation Team) iliyoundwa na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Aidha, Serikali yetu kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inaendelea kutumia njia za kidiplomasia ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu suala hilo.

Mpaka wa Tanzania na Zambia
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama katika mpaka huu wenye urefu wa kilomita 299, ni shwari. Hakuna tukio la kuhatarisha usalama wa nchi yetu lililoripotiwa hadi sasa.

Mpaka wa Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 554 ni shwari. Hakuna tukio la kuhatarisha usalama kwa nchi yetu. Hata hivyo, ndani ya nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yameripotiwa matukio ya waasi kushambulia miji mbalimbali nchini humo. Wizara kupitia JWTZ imeendelea kuwa macho na kujipanga wakati wote. Aidha, ushiriki wa Tanzania katika Misheni ya Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (United Nations Organisation Stabilization Mission in the Democratic Republic of the Congo - MONUSCO) unaisaidia nchi kujiimarisha kiulinzi ipasavyo.

Mpaka wa Tanzania na Burundi
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 451 ni shwari. Hakuna matukio yoyote yaliyoripotiwa kuhatarisha usalama baina ya nchi hizi, ingawa eneo hili linakabiliwa na uwepo wa wahamiaji haramu, uvamizi wa wakulima na uingizaji wa mifugo kwa ajili ya kupata malisho. JWTZ imeendelea kukabiliana na hali hii.

Mpaka wa Tanzania na Rwanda
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 217 ni shwari, ingawa yapo matukio machache ya kihalifu ya wahamiaji haramu na uingizaji wa mifugo kwa ajili ya malisho. Wizara kupitia JWTZ inaendelea kuchukua hatua za kudhibiti matukio hayo.

Mpaka wa Tanzania na Uganda
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama katika mpaka huu wenye urefu wa kilomita 395 ni shwari. Hakuna tukio la kuhatarisha usalama wa nchi yetu. Hata hivyo, kuna changamoto ya uingizaji haramu wa mifugo kwa ajili ya malisho. Juhudi za kuimarisha mpaka zinaendelea, kwa kuongeza Beacon kati ya marundo ya mawe yaliyowekwa na mkoloni, na kujenga barabara ya usalama kwenye Mpaka.

Mpaka wa Tanzania na Kenya
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 826, ni shwari. Hakuna tukio la kuhatarisha usalama dhidi ya Tanzania lililoripotiwa. Hata hivyo, ipo changamoto ya kuharibiwa kwa alama za mpaka. Kazi ya kuimarisha Mpaka huu inayotekelezwa na timu ya wataalam kutoka Tanzania na Kenya inaendelea vizuri, ambapo awamu ya kwanza imeanzia eneo la Serengeti hadi Ziwa Natron.

Mpaka wa Tanzania Katika Bahari ya Hindi
Mheshimiwa Spika,
hali ya usalama wa mpaka huu wenye urefu wa kilomita 1,424, ni shwari. Katika Mpaka huu tumepakana na nchi za Comoro na Shelisheli. Hakuna tukio lililoripotiwa la kuhatarisha usalama dhidi ya Tanzania. Aidha, JWTZ imeendelea kufanya doria za mara kwa mara katika eneo la Bahari ya Hindi, ili kubaini na kuzuia wahamiaji haramu, usafirishaji haramu wa binadamu, usafirishaji wa madawa ya kulevya na matishio ya kigaidi.


F: MPANGO NA MWELEKEO WA BAJETI kwa MWAKA WA FEDHA 2022/2023 NA MAKADIrIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023 NA MAOMBI YA FEDHA
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imelenga kutekeleza mpango na bajeti kwa kuzingatia mambo yafuatayo; Dira na Dhima ya Wizara, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22 – 2025/26), Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030 (SDGs), Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020, na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu kuwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 ifuatavyo:

Makadirio ya Makusanyo ya Maduhuli

Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Wizara inatarajia kukusanya maduhuli ya jumla ya Shilingi 87,603,000.00 kutoka katika mafungu yake matatu, ambapo Fungu 38 – NGOME linatarajia kukusanya kiasi cha Shilingi 22,000,000.00, Fungu 39 JKT linatarajia kukusanya kiasi cha Shilingi 64,403,000.00 na Fungu 57 – Wizara inatarajia kukusanya kiasi cha Shilingi 1,200,000.00 kama inavyoonekana katika Jedwali Na. 4.

Jedwali Na 4: Makadirio ya Makusanyo ya Maduhuli kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023


Na.
Fungu
Makadirio ya Maduhuli 2022/23
138 – NGOME
22,000,000.00​
239 – JKT
64,403,000.00​
357 – Wizara
1,200,000.00​
Jumla
87,603,000.00


Matumizi ya Kawaida na Maendeleo

Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, Serikali inatarajia kutenga fedha kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Maendeleo ikiwa na jumla ya Shilingi 2,713,787,405,453.00 ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi 2,483,454,234,453.00 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, na Shilingi 230,333,171,000.00 ni kwa ajili ya kugharamia shughuli za maendeleo.

Mchanganuo kwa kila Fungu ni ifuatavyo; Fungu 38 – NGOME linatarajia kutengewa kiasi cha fedha za matumizi ya kawaida Shilingi 2,047,723,503,453.00, na fedha za maendeleo Shilingi 56,367,636,000.00;
Fungu 39 – JKT linatarajia kutengewa kiasi cha fedha za matumizi ya kawaida
Shilingi 411,863,641,000.00, na fedha za maendeleo Shilingi 13,965,535,000.00; na Fungu 57 – Wizara inatarajiwa kutengewa kiasi cha fedha za matumizi ya kawaida
Shilingi 23,867,090,000.00, na fedha za maendeleo Shilingi 160,000,000,000.00 kama ilivyoainishwa katika Jedwali Na. 5.


Jedwali Na. 5: Mchanganuo wa Bajeti kwa Kila Fungu kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

NaFungu
Matumizi ya Kawaida
Matumizi ya Maendeleo
Jumla
138-NGOME
2,047,723,503,453.00​
56,367,636,000.00​
2,104,091,139,453.00​
239-JKT
411,863,641,000.00​
13,965,535,000.00​
425,829,176,000.00​
357-Wizara
23,867,090,000.00​
160,000,000,000.00​
183,867,090,000.00​
Jumla
2,483,454,234,453.00
230,333,171,000.00
2,713,787,405,453.00
Mheshimiwa Spika, shughuli zinazokusudiwa kutekelezwa katika Mwaka wa
Fedha 2022/2023 utazingatia maeneo ya kipaumbele yafuatayo:

Kuendelea kuliimarisha Jeshi kwa zana na vifaa vya kisasa, mawasiliano pamoja na rasilimali watu;

Kuendelea kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi wa Jeshi ikiwemo mafunzo, matunzo ya zana na miundombinu, maslahi, huduma bora za afya, ofisi na makazi;

Kuendeleza jitihada za utatuzi wa changamoto za mipaka ya nchi yetu na nchi jirani;

Kuendeleza tafiti na uhawilishaji wa teknolojia kwa ajili ya kuzalisha bidhaa na huduma kwa matumizi ya kijeshi na kiraia;

Kuendelea kulipa malipo na posho kwa wanajeshi, mishahara na stahili kwa watumishi wa umma;

Kuendelea kujenga uwezo wa Jeshi la Kujenga Taifa kwa kuboresha miundombinu ili liweze kuchukua vijana wengi zaidi na kutoa mafunzo ya uzalendo, ukakamavu, umoja wa kitaifa, na stadi za kazi kwa vijana;

Kuendelea kujenga uwezo wa JKT ili kuiwezesha kujitosheleza kwa chakula kwa vijana wanaojiunga na mafunzo;

Kuendelea kuimarisha na kuratibu mafunzo ya Jeshi la Akiba kwa kuhamasisha na kuelimisha wananchi juu ya masuala ya ulinzi, uzalendo wa kitaifa, usalama, na umuhimu wa kushiriki katika ulinzi wa nchi;

Kuimarisha ushirikiano na Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya za Kikanda, na Nchi mbalimbali katika nyanja za kijeshi na kiulinzi;

Kuendelea kushirikiana na mamlaka za kiraia katika kukabiliana na majanga na dharura itapohitajika; na

Kuendelea kutatua migogoro ya ardhi kwa kupima mipaka ya maeneo ya Jeshi, kufanya uthamini, na kulipa fidia ya ardhi iliyotwaliwa kutoka kwa wananchi kwa matumizi ya Jeshi.

H: SHUKRANI​

Mheshimiwa Spika, kabla sijahitimisha Hotuba yangu, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru Viongozi na watendaji wa Wizara na Taasisi zake kwa michango yao madhubuti katika kutekeleza Mpango na bajeti ya Mwaka wa Fedha 2021/2022, na kutayarisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu ya Mwaka wa Fedha 2022/2023 ifuatavyo:

Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Jenerali Venance Salvatory Mabeyo, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule, Mnadhimu Mkuu wa Jeshi, Meja Jenerali Rajabu Nduku Mabele, Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Wakuu wa Kamandi, Wakuu wa Mashirika, Wakuu wa Idara na Vitengo (Wizara ya Ulinzi na JKT), Wakuu wa Matawi (Makao Makuu ya Jeshi), Wakuu wa Idara (Makao Makuu ya Jeshi la Kujenga Taifa), Maafisa, Askari na Watumishi wa Umma waliopo Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Nawashukuru sana kwa kuendelea kunipa ushirikiano katika kufanikisha majukumu ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii, kwa niaba ya Serikali kutoa shukrani kwa Serikali za nchi mbalimbali na washirika wa maendeleo kwa ushirikiano wanaoendelea kuipatia Wizara yangu, ikiwa ni pamoja na; Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, Jumuiya ya Afrika Mashariki, Canada, India, Jamhuri ya Watu wa China, Marekani, Ufaransa Ujerumani na Uturuki. Aidha, tunazishukuru nchi rafiki kwa ushirikiano wao katika shughuli zetu za Ulinzi. Nchi hizo ni pamoja na Algeria, Bangladeshi, Falme za Kiarabu, Finland, Ghana, Hispania, Indonesia, Israeli, Jordani, Misri, Morocco, Nigeria, Omani, Pakistani, Sri Lanka, Sweden, Uholanzi, Uingereza, Urusi, na Uswisi.

Mheshimiwa Spika, naomba pia kuwashukuru wananchi wote kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika ulinzi wa nchi yetu. Ni matumaini yangu kuwa tutaendelea kushirikiana zaidi kwa manufaa ya Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, napenda kuishukuru familia yangu kwa upendo na uvumilivu wao kwangu unaoniwezesha kutekeleza majukumu yangu.

Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe binafsi, Mawaziri wenzangu na Wabunge wote kwa kunisikiliza. Hotuba hii, inapatikana pia katika tovuti ya Wizara ya Ulinzi na JKT ambayo ni www.modans.go.tz

Mheshimiwa Spika,
naomba kutoa Hoja.


WAKUU WA IDARA NA VITENGO.JPG

 
Back
Top Bottom