JanguKamaJangu
JF-Expert Member
- Feb 7, 2022
- 2,309
- 5,464
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene (wapili kushoto) akielekea kukagua moja ya jengo kati ya majengo matatu ya upasuaji, afya ya uzazi na mahabara yanayojengwa na Tasaf katika Kituo cha Afya Budushi wilayani Kwimba. Picha na Saada Amir
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene ametoa muda wa siku 30 kwa uongozi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) kubaini zilipo fedha za wanufaika zilizolipwa bila kuwafikia walengwa.
Pamoja na kubaini zilipo, waziri huyo pia ameagiza kiwango halisi cha fedha zilizopotea kwa mtindo huo kifahamike na ripoti hiyo kuwasilishwa ofisini kwake ndani ya kipindi hicho.
Waziri Simbachawene ametoa maagizo Agosti 3, 2023 alipotembelea Kata ya Sumve Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza kukagua ujenzi wa majengo ya mahabara, upasuaji na afya ya uzazi yanayotekelezwa kupitia mpango wa Tasaf huku akiitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kusaidia uchunguzi wa kiwango na zilipo fedha hizo.
Akizungumza na wakazi wa Kata hiyo mara baada ya kukagua ujenzi wa majengo hayo ya kutolea huduma katika Kituo cha Afya Budushi, Simbachawene amesema hajaridhishwa na maelezo kuwa fedha hizo hazionekani baada ya kutumwa kwa walengwa kupitia namba za simu zilizokosewa.
“Serikali ipo, hela inapoteaje? nataka uchunguzi ufanyike kuanzia Tasaf, kampuni za simu ambazo namba zinazodaiwa kukosewa ziliposajiliwa na walengwa ambao hawajapokea fedha licha taarifa kuonyesha kuwa walishatumiwa," ameagiza Waziri huyo akionya kuwa fedha ya umma haitapotea hata senti tano
Amesema kuna hisia kuwa wapo wajanja wachache wanaotumia kisingizio cha kukosewa namba za simu kujichotea fedha za Tasaf huku akionya kuwa kiama chao kinakaribia.
Akizungumzia utekelezaji wa miradi kupitia Tasaf, Waziri huyo ameagiza kila mradi ufahamike kuanzia ngazi ya mitaa/vijiji, kata, wilaya, mkoa hadi Taifa kutoa fursa ya usimamizi na ufuatiliaji wa karibu kwa kila ngazi.
Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa miundombinu katika Kituo cha Afya Budushi, Ofisa Mtendaji Kata ya Sumve, Emmanuel Lameck amesema zaidi ya Sh291.8 kutoka Tasaf zitatumika kujenga majengo hayo.
Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Ng'wilabuzu Ludigija amesema kukamilika kwa mradi huo kutawezesha wananchi zaidi ya 72, 000 kutoka Kata tano za Wilaya hiyo kupata huduma bora za afya.
Amesema hadi sasa, Serikali imetoa zaidi ya Sh1.5 bilioni kwa ajili ya kuboresha miundombinu ikiwemo ya huduma za afya wilayani Kwimba huku akiwaomba wananchi kuunga mkono juhudi hizo kwa kujitolea kwa hali na mali nguvu zao na ulinzi wa miundombinu.
Mkurugenzi wa Miradi kutoka Tasaf, John Stephen amewaomba viongozi kuhakikisha kamati za ujenzi za vijiji zinahusika moja kwa moja kwenye utekelezaji wa miundombinu huku akitaka kasi ya ujenzi huo iongezeke ili ukamilike kwa wakati na huduma zianze kutolewa.
Diwani wa Kata ya Sumve, Gervas Kitwala ameishukuru Serikali kwa kutekeleza mradi huo huku akiiomba kupeleka gari la kubeba wagonjwa kurahisisha rufaa kwa wanaohitaji huduma zaidi, ombi lilipokelewa na Waziri Simbachawene kwa kuahidi kuzungumza na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu kukipatia gari kituo hicho cha afya kinachohidumia zaidi ya watu 72, 000 kutoka kata tano za Wilaya ya Kwimba.
Chanzo: Mwananchi