Watoto njiti zaidi ya laki mbili Nchini huzaliwa kwa mwaka

JanguKamaJangu

JF-Expert Member
Feb 7, 2022
2,309
5,464
Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amebainisha kuwa takriban watoto laki Mbili mpaka laki Tatu kwa Mwaka huzaliwa kabla ya muda (watoto njiti) Tanzania.

Waziri Ummy amesema hayo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya Jijini Dar es Salaam wakati wa maandalizi ya kuelekea awamu ya pili ya ugawaji wa vifaa tiba kwa ajili ya huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda (watoto njiti) katika Hospitali zaidi ya 80 nchini.

“Watoto takriban laki Mbili mpaka laki Tatu nchini Tanzania wanazaliwa kabla ya wakati lakini pia tunajumuisha na watoto wengine wale wanaozaliwa wakiwa na uzito pungufu chini ya kilogramu 2.5”, ameeleza Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa asilimia 70 ya watoto watoto njiti wanafariki ndani ya masaa 48 kama hawajapata huduma sahihi kwa wakati.

Amebainisha kuwa juhudi zinazofanywa na Serikali chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuwezesha kupatikana kwa vifaa tiba vyote muhimu vya kuwahudumia watoto njiti nchini.

“ Hospitali zilizokuwa zinatoa huduma za uangalizi kwa watoto njiti ni 14 tu lakini kwa sasa zipo Hospitali zenye wodi za watoto Njiti (NICU) zaidi ya 180 nchini, haya ni maendeleo makubwa hapa nchini,” ameongeza Waziri Ummy.

Pia amesema kuwa miaka minne iliyopita, Huduma za uangalizi maalum kwa watoto njiti zilikua zinatolewa Muhimbili, Hospitali za Rufaa za Kanda, lakini kwa sasa huduma hizi zipo katika Hospitali zote za Rufaa za Mikoa mpaka ngazi za Hospitali za Wilaya ambayo ni takriban Hospitali 180 zinazotoa huduma hizo.
 
Back
Top Bottom