Mtikila apongeza UV-CCM kuhusu Dowans
Na Grace Michael
Majira
MWENYEKITI wa Democratic Party, Mchungaji Christopher Mtikila amesema kuwa kitendo cha ujasiri kilichofanywa na Umoja wa Vijana wa
Chama Cha Mapinduzi (UV-CCM) cha kupinga kulipwa kwa mabilioni ya fedha kwa Dowans kiwe daraja kwa Watanzania wote katika kuhakikisha fedha hizo hazilipwi.
Mbali na hilo, pia amewataka Watanzania kutoogopa kupinga suala hilo kwa kuwa hakuna sheria yoyote inayoweza kuwabana wakati wa kudai maslahi ya taifa na haki za Watanzania.
Mchungaji Mtikila aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hukumu ya fidia ya sh bilioni 94 za Watanzania kwa Dowans, kitendo ambacho alisema ni 'uporaji wa nchi kwa bastola ya Dowans'.
UVCCM wanapaswa kupongezwa kwa kile walichokifanya kwa kuwa wanawakilisha mawazo ya Watanzania wazalendo, hivyo tukitumie kitendo hicho kama daraja muhimu la kutuunganisha sisi wana wa Tanganyika katika vita ya ukombozi ili kuangamiza magenge ya uporaji wan chi yetu,â alisema Mchungaji Mtikila.
Alhamisi iliyopita, UV-CCM ilitoa msimamo wake kuwa Dowans wasilipwe fedha na serikali, bali waisaidie kuipata kampuni ya Richmond iliyohamishia mkataba wake ili iwalipe fedha hizo.
Vijana hao walipendekeza suala la Dowans lirejeshwe bungeni kwa majadiliano zaidi, ili kuchukua hatua dhidi ya yeyote aliyehusika na madudu hayo.
Alisema kuwa wananchi wanapoamua kulinda maslahi ya taifa lao huwa hawafungwi na sheria kwa kuwa sheria ni chombo kinachoweza kutumiwa kwa ajili ya kudhulumu haki au kutoa haki, hivyo katika mapambano ya haki sheria hukaa pembeni.
Alisema kuwa ibara ya 27(2) inataka wazawa wa nchi kuendesha uchumi wa taifa kwa makini kama watu ambao ndio waamuzi wa hali ya baadaye ya taifa, hivyo akawataka wananchi kujiuliza Dowans inaiuzia bidhaa gani taifa kwa hayo mabilioni ya fedha.
Uzalendo tunaolazimishwa na katiba ni kuipuuza mahakama ya kimataifa na kuwashughulikia waliohusika na uporaji kuanzia wa IPTL, SONGAS, AGGREKO, DCP, EPA, Kagoda Agriculture Ltd, hujuma za mitandao ya simu za mikononi, alisema.
Kutokana na hali hiyo alisema kuwa umefika wakati kwa Watanzania 'kuhamia barabarani kama familia moja' kwa ajili ya kuondoa utawala uliopo kwa kuwa unadidimiza haki za wananchi.
Alisema kuwa Dowans italeta ukombozi katika nchi hii kwa kuwa hata Rais Jakaya Kikwete anahusika kwani alipotuhumiwa na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willibrod Slaa hakuweza kukanusha tuhuma hizo.