SIO KWA IDHINI YAKE WALA YA ALIYENITUMIA BUT TUJADILI CONTENT,HASA MAENEO NILIYO YAKOLEZA,MIMI NAAMINI WAPO WENYE NIA NJEMA KWA MAANA WANAAMINI MABADILIKO NDANI YA CCM YENYEWE,SO WANAOAMINI NJE YA HAPO NAO RUKSA...ILA TUSICHOCHEE CHUKI BALI WAJIFUNZE VIJANA KUSHINDANA KWA HOJA,SO MSINGI UWE HOJA SIO PERSONALITIES....TUJADILI...
HOTUBA YA MH. NAPE MOSES NNAUYE, MJUMBE WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA CCM (NEC), MJUMBE WA BARAZA KUU LA UVCCM(T) NA KATIBU MSAIDIZI MWANDAMIZI IDARA YA MAMBO YA SIASA NA UHUSIANO WA KIMATAIFA CCM MAKAO MAKUU, KWA MKUTANO MKUU WA CCM TAWI LA MYSORE-BANGALORE INDIA TAR.06.04.2008.
Ndugu zangu waratibu wa mchakato wa uanzishaji wa tawi la Chama Cha Mapinduzi Mysore Ndugu Antoni Mtavangu na Mohamed Sheini, Waheshimiwa sana wanachama na wapenzi wa CCM wa hapa Mysore.
Hakika, hii ni siku ya furaha kubwa kwangu, kwa Chama chetu na kwetu Watanzania tuishio hapa India wenye mapenzi mema na CCM.
Leo tumefanikiwa kuonyesha mwanga katika kutimia kwa ndoto ya kuanzishwa kwa mashina na matawi ya Chama Cha Mapinduzi India, kutokana na ukweli kwamba India ni moja ya nchi zenye Watanzania wengi, ukilinganisha na nchi zingine Barani Asia.
Hivyo nachukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati kabisa kutokana na kuwa wa kwanza kuonyesha njia ambayo naamini wenzetu katika sehemu zingine za India wataifuata.
Nina hakika kwamba katika historia ya Chama chetu, Mysore itakumbukwa na mchango wenu ndani ya Chama utaenziwa daima.
Chama Cha Mapinduzi, siku zote kinajivunia ninyi kama vijana, wasomi na ambao pia mnapata uzoefu katika moja ya nchi zinazosifika kwa kuwa na uchumi unaokimbia kwa kasi kubwa. Hongereni sana na msisite kutoa uzoefu wenu kwa Chama chenu na nchi yetu.
Vijana ndio nguzo, nguvu na matumaini kwa CCM. Na kwakuwa CCM kwa Tanzania ndio Chama kinachotawala, kilichopewa dhamana ya kuongoza nchi na chenye nguvu kubwa kwa sasa, basi ni wazi kuwa vijana wake ni nguzo, nguvu na tumaini la nchi yetu pia.
Hivyo basi, kutokana na hali hiyo, tunaowajibu wa kuhakikisha sifa na dhamana kubwa tuliyonayo tunaitumia vizuri kwa faida ya chama chetu na nchi yetu.
Wajibu huu unakuwa mkubwa zaidi, hasa kwa wale tuliopata bahati ya kupata elimu, na hasa elimu hii ya juu, na kwa kweli kama ni deni kwa nchi na chama chetu, basi letu linakuwa mara dufu.Mwalimu Nyerere aliwahi kusema, ...dhumuni kubwa la elimu kwa binadamu ni kumpa uwezo wa kuyajua na kuyamudu mazingira yake....hivyo chama kinawategemea ninyi kwa kutumia elimu na uzoefu wenu kuyajua na kuyamudu mazingira yake, hata ikibidi kuyabadilisha yaendane na mahitaji ya sasa.
Inawezekana tu kutimiza wajibu wetu huu kama tutaamua kwa makusudi kutafakari kwa kina tena kwa moyo wa kizalendo, tumetoka wapi, tupo wapi na twataka kwenda wapi kama chama na kama nchi.
Pamoja na mafanikio mengi tuliyoyapata kama chama, zipo changamoto nyingi kwa chama chetu leo, ambazo kama vijana wa CCM tunapaswa kuzijadili na kuzitafutia ufumbuzi na hatimaye kupendekeza kwa chama chetu hatua za kuchukua kwa lengo la kukifanya chama kiende na wakati zaidi.
Tukisaidie chama chetu kiende na mahitaji ya wakati, jamii, uchumi na mazingira ya siasa ya leo. Kwa wasomaji wa Biblia watakumbuka Mtume Paulo katika kitabu cha Matendo ya Mitume alisema.......vijana wenu wataona maono na wazee wenu wataota ndoto.... maono katika tafsiri rahisi hapa ni mipango kwa ajili ya future tunakokwenda.
Lakini pia waswahili wanasema, Kanzu ya Ijumaa hufuliwa Alhamisi. Hali tuliyonayo leo ni matokeo ya jumla ya mambo yote yaliyopita, lakini kama vijana tunao wajibu wa kufanya tuendako kuwe bora zaidi kwa chama chetu na nchi yetu. Tusilazimike kujenga ukuta huko mbele badala ya kuziba ufa mapema kama upo leo.
Kwakuwa karibu wote hapa ni vijana, ninyi ni wadau namba moja wa Umoja wa Vijana wa CCM. Umoja wa Vijana wa CCM unapaswa kuwa chemichemi na chanzo cha fikra mpya za kimapinduzi kwa chama chetu na nchi yetu.
Historia inaonyesha mambo mengi ya manufaa na kujivunia kwa chama chetu na nchi yetu chanzo chake ni umoja wa vijana. Ukifuatilia historia, kwa mfano ni Umoja wa Vijana wa TANU na ule wa ASP ndio walikuwa wakwanza kuunganisha kuwa kitu kimoja na baadae vyama vikaungana kuunda CCM.
Changamoto zipo nyingi, lakini hapa nitatoa mifano michache kuchokoza mawazo. Kuna changamoto kama za upanuzi wa demokrasia ndani ya chama chetu, ili tuendelee kuwa mfano wa kuigwa kwa vyama vingine nchini mwetu na kwingineko duniani.
Ni kweli tumepiga hatua kubwa ya upanuzi wa demokrasia ndani ya chama chetu, lakini je uwakilishi katika vikao vya maamuzi vina uwiano sawa hasa wa kijinsia na idadi kulinganisha na ongezeko la wanachama na makundi mbalimbali katika jamii yetu kama wasomi, vijana nakadhalika? Je, ni lazima leo kuendelea na utaratibu wa kuwa na jina moja tu la kupigiwa kura kwa nafasi kama za Makamu Mwenyekiti CCM kwa mkutano mkuu wa CCM (T) au hata Katibu Mkuu wa chama kwa Halmashauri kuu ya CCM(T)?, badala ya kuwa na majina zaidi ya moja kwa kila nafasi ili kuwezesha wajumbe kuwa na uwanja mpana wa kuchagua.
Je uwepo wa idadi kubwa ya viongozi wengi wa kiserikali wa kuteuliwa hasa na rais ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa chama chetu katika vikao vya juu vya maamuzi vya chama kunaathiri vipi mijadala, uwazi na utendaji wa vikao hivi?
Ni kwa kiasi gani vitendo vya baadhi ya wanachama na baadhi ya viongozi wasiowaaminifu vinaharibu sifa nzuri ya chama chetu?
Tukiangalia mifano ya ufisadi, rushwa, na hata kushindwa kutekeleza majukumu tuliyowakabidhi na hatua muwafaka za kuchukuliwa inapotokea utovu wa nidhamu, kama hatua ya kukiimarisha chama na kujenga imani ya wananchi na wanachama kwa chama chao.
Je, hatua zinazochukuliwa na chama kwasasa kushughulikia maswala kama ya ufisadi, rushwa na uwajibikaji zinatosha?
Ni vema mambo haya tukayaangalia kwa kina, kwani waathirika wakubwa wa vitendo hivi viovu kama vya rushwa na ufisadi ni sisi vijana. Sisi ndiyo tunaoathirika kwa kukosa huduma leo na kesho pia. Hivyo tusimame bila woga kuwanyooshea vidole na kuwakemea mafisadi na wala rushwa, ndani na nje ya chama chetu.Bado naamini sera na mipango ya CCM kwa nchi yetu ni bora kuliko chama chochote kwa sasa. Lakini mara nyingi inaingia doa kwa watekelezaji tunaowapa dhamana, kutokuwa waaminifu na makini katika utekelezaji wao.
Hivyo basi kama vijana wa CCM, tujadili njia bora za kuimarisha ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa sera na maamuzi mbalimbali ya chama chetu ili kuwaletea wanachi maisha bora zaidi.
Na pale inapogundulika tatizo la kiutekelezaji basi hatua zinazostahili zichukuliwe mapema ili chama na sera zake safi zisichafuliwe kwa faida ya wachache na hasara ya wengi.
Nakumbuka zamani kulikuwa na maazimio yaliyokuwa na lengo la kusukuma utekelezaji wa sera na mipango ya CCM. Kwa mfano, Azimio la Musoma, Azimio la Iringa, Azimio la Mlalo na Azimio la Arusha, ambayo kwa kweli yalileta msukumo mkubwa katika utekelezaji wa sera na mipango mbalimbali, ambayo mpaka leo matunda yake yanaonekana.
Nadhani si vibaya tukitafakari uwezekano wa kurejea utaratibu huu katika mazingira ya sasa, tukawa na maazimio mengine katika kusukuma utekelezaji wa sera za msingi.
Mimi ni mmoja ya watu wanaoamini kuwa Azimio kama la Arusha ni muhimu zaidi leo kwa hatua tuliyofikia kama nchi na chama kuliko hata lilipoanzishwa, isipokuwa linaweza kuboreshwa kukidhi mazingira ya sasa.Ni dhahiri kwamba kutokana na hali inavyokwenda, tunayo changamoto kubwa kwa sasa katika siasa za nchi yetu ya kutenganisha siasa na biashara!
Pamoja na viongozi wetu kuliona hili wakiongozwa na rais Jakaya Kikwete mwenyekiti wa taifa wa CCM, bado nadhani mjadala huu tusimwachie peke yake na vikao vya juu vya chama.
Bali tutumie uzoefu tunaoupata huku, kukisaidia chama chetu katika hili ili kukiokoa chama na makucha ya wafanyabiashara wachache wasio na nia njema na chama na kwa kweli na nchi.Tutumie vikao vyetu vya chama kama wasomi kujadili changamoto mbalimbali zinazokikabili chama na nchi kwa jumla.Tutumie pia umoja wetu wa vijana kama sehemu ya mijadala ya hoja nzito za ujenzi wa chama chetu na nchi yetu; tuutumie vizuri ujana wetu wakati tungali na nguvu tusije shituka wakati nguvu hatuna tena, ambayo ni sawa na kukumbuka shuka asubuhi.
Tusipotumia ujana wetu vizuri sasa, tutakuwa hatujakitendea chama chetu haki, chama ambacho kwa sasa ni tegemeo la Watanzania na hivyo tutakuwa hatujaitendea haki nchi yetu pia.
Sisi wanachama wa CCM tuliopo hapa, lazima tuwe mabalozi wazuri wanchi yetu na chama chetu. Mahali chama kinapofanya vyema tusisite kukipongeza, lakini pia kinapokosea tukosoane na kurekebishana kwa faida ya chama na nchi yetu bila unafiki wala woga.
Tukiweza kufanya hivyo, tutaweza kusaidia kujenga viongozi na taifa la watu ambao wako tayari kukosolewa, kukosoana na kujikosoa.
Ni lazima tufute dhana ya kwamba ukishakuwa kiongozi basi unajua yote, hapana. Tukumbuke kuwa kiongozi ni watu. Hivyo kila mwanachama namsihi aone anao wajibu wa kutimiza katika ujenzi wa chama imara, bora na madhubuti ili kiweze kuwatumikia wanachi vyema.
Chama cha siasa ni itikadi, na itikadi ni imani. Sisi vijana na hasa wasomi tuongoze kwa kuonyesha hili kwa vitendo. Vyama vinatofautishwa kwa itikadi zao, tusiwe wepesi wa kuyumbayumba, tuepuke umalaya wa kisiasa, leo CCM kesho CUF, keshokutwa CHADEMA mtondogoo CCM tena.Nadhani vitendo vya namna hii vinachangia kuviza demokrasia yetu.
Ukimuuliza mwanachama wa namna hiyo, nini kilikufanya uamini kule, na kipi kilichokufanya sasa usiamini huku, mtu anakuwa hana jibu la msingi. Si rahisi kwa mtu kuhama kutoka dini moja kwenda nyingine bila sababu ya msingi, vivyo hivyo kwa siasa.
Ukiamini ujamaa simamia na ishi kama mjamaa, sio mara leo mjamaa kesho bepari, keshokutwa aah mjamaa tena, huu ni uhuni wa kisiasa
Sipingi utaratibu wa wanachama wa chama kimoja kuhama kutoka chama kimoja kwenda kingine,lakini tatizo langu hapa ni uhamaji unaoangalia zaidi masilahi binafsi na uroho wa madaraka au ahadi za madaraka au hata pesa.
Ni vizuri vyama vikajikita zaidi katika kupata wanachama wapya kutoka kwa wananchi wasio na vyama hasa vijana badala ya kubaki kunyanganyana wanachama kama vile hakuna wananchi wengine.CCM tufanye hili kwa vitendo kwa kuimarisha utaratibu wa kupata wanachama wetu toka kundi la vijana wasio na vyama.Tunapochagua viongozi wetu leo pamoja na sifa zingine tuangalie changamoto zinazotukabili kama chama chetu. Tuchague viongozi tutakaoshirikiana nao kwa pamoja kukijenga chama na nchi yetu, kwa faida ya kizazi chetu na vizazi vijavyo.
Sisi wanachama wa CCM Mysore tuwe mfano wa kuigwa kwa tabia njema, katika masomo yetu na uhusiano wetu na wenzetu, ili wengine wavutike kukipenda na kujiunga na chama chetu.
Tukumbuke sisi ni wanachama wa chama Tawala, hivyo tuongoze kwa vitendo, uanachama wetu ubebe hadhi ya chama kinachotawala ili kuienzi dhamana ambayo chama chetu kimepewa na Watanzania.
Mwisho nawatakia uchaguzi mwema, wenye mafanikio na amani, huku tukikumbuka kujenga utamaduni kuwa wakati wa uchaguzi CCM huwa tunapangana si kushindana, kwani wote twajenga nyumba moja si vizuri kugombania fito!
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
Mkutano wa CCM tawi la Mysore umefunguliwa!!.