Asante mkuu, kwa comment yako. Ni kweli habari hiyo ipo katika kitabu cha 2 Wafalme 2:23–24.
Ngoja nikufafanulie kwa kina, maana umesema tafsiri za Kiswahili zimechakachuliwa! Neno la Kiebrania lililotafsiriwa kama "watoto" (na'ar) halimaanishi watoto wadogo tu. Linaweza kumaanisha pia kijana mdogo hadi kijana mkubwa (kama Daudi alipomwua Goliathi bado aliitwa "na'ar"). Kwa muktadha wa tamaduni za Kiebrania, walikuwa watu wazima kiakili waliostahili kuwajibika kwa maneno yao.
Hii haikuwa dhihaka ya kawaida – ilikuwa dhihaka ya kiroho. Kumbuka, Elisha alikuwa amechukua nafasi ya Eliya, na watu wengi walikuwa wakikataa manabii wa kweli na kumgeukia Baali na ibada potovu. Hawa vijana walimtania kwa makusudi – "Paa wewe!" – kama kejeli kwa Eliya aliyepaa mbinguni. Walikuwa wakidharau kazi ya Mungu hadharani. Huu haukuwa mzaha tu; ulikuwa uasi wa wazi dhidi ya Mungu kupitia mtumishi wake. Hawakuwa watoto hao. Walikuwa vijana wenye ufahamu kuhusu Eliya. Watoto wangejuaje kwamba Eliya alipaa na kujua kuwa Elisha alikuwa successor wa Eliya?
Halafu, haikuwa Elisha aliyeleta dubu – bali Mungu. Elisha aliwalaani tu kwa jina la Bwana kisha Mungu akaamua kushughulikia dhihaka hiyo kwa njia ile. Hii inaonyesha kuwa lilikuwa somo la kiroho – si chuki binafsi ya mtumishi huyo. Mungu ndiye aliyehukumu, si Elisha kama mtu.
Kuhusu Elisha kumchinja mfalme, hakuna sehemu iliyo wazi inayoonyesha kuwa Elisha mwenyewe alimchinja mfalme kwa mkono wake. Mara nyingi alikuwa anatoa maagizo ya kinabii, na hukumu ya Mungu ilikuwa inatekelezwa na wafalme au jeshi. Kama una andiko la moja kwa moja linalosema Elisha alichinja mtu kwa mkono wake, liweke hapa na mimi nijifunze.
Kwa mtazamo wako, unaona ule ulikuwa ukatili wa hali ya juu. Lakini tunapotafsiri matukio ya kihistoria ya Biblia, ni muhimu kuelewa muktadha wa kiroho, kisiasa, na kijamii wa wakati ule. Kulingana na Mungu, dhihaka ya makusudi dhidi ya mamlaka yake ya kiroho ni kosa kubwa sana.
Niseme tu kwamba habari hii inafunua jinsi ambavyo Mungu anachukulia kwa uzito dhihaka, dharau kwa watumishi wake, na uasi wa kizazi dhidi ya mamlaka ya kiroho. Mungu akusaidie kuyajua mapenzi yake hata kupitia habari hii.
Kumbuka Paulo(Sauli) alivyopigwa upofu baada ya kuwatesa wafuasi wa Yesu. Kwa neema tu alipona na kuwa Mtume. Kumbuka Anania na Safira jinsi walivyokufa baada ya kumwambia uongo Mtumishi wa Mungu, Petro. Mungu ni wa upendo lakini pia ni wa haki. Ndio sababu wanaokataa wokovu sasa, watachomwa moto milele na milele.