Ukweli Mchungu: Ukitaka Mafanikio Makubwa, Usiwe 'Fair'

Rafiki yangu mpendwa,

Kuna vitu waliofanikiwa sana wanavijua, lakini huwa hawaviweki wazi.

Wanafanya hivyo kwa sababu jamii huwa haielewi vitu vingi kuhusu mafanikio, na hivyo huishia kuwashambulia waliofanikiwa pale wanapojaribu kuwa wakweli.

Mara ngapi umesikia masikini wakiwasema matajiri kwamba ni freemason au wamepata utajiri wao kwa njia za giza?
Umewahi kumwona tajiri akibishana na masikini juu ya hilo?

Jibu ni hapana, tajiri anajua masikini hawezi kuelewa na hata kuamini mengi yaliyomsaidia yeye, hivyo anamuacha aamini anachochagua kuamini.

Leo nakupa siri kubwa, nakupa ukweli mchungu ambao ukiweza kuupokea na kuuishi, utaweza kupata mafanikio makubwa kwenye maisha yako.

Ukweli huo ni kama unataka mafanikio makubwa, basi usiwe ‘fair’. Neno fair yaani usawa limekuwa linatumika sana.
Wengi wamekuwa wanalalamika kwamba maisha hayapo fair, pamoja na juhudi wanazoweka bado hawapati wanachotaka.

Leo nakwenda kukushirikisha maeneo 10 ambayo upaswi kuwa ‘fair’ kama unayataka mafanikio makubwa. Kwenye maeneo hayo, unapaswa kuwa tofauti kabisa na wengine walivyo ili uweze kupata matokeo ya tofauti.

huwezi-kuwaridhisha98.png


Kama unataka mafanikio makubwa, usiwe fair kwenye maeneo haya 10.

1. Usiwe fair kwenye Kazi

Watu wengi wanafanya kazi kwa mazoea na kwa viwango vya chini sana. Wewe nenda kinyume nao, fanya kazi kwa juhudi kubwa na kwa viwango vya juu sana. Anza kwa kufanya kazi muda mrefu kuliko wengine. Kama wanaanza kazi saa mbili asubuhi na kumaliza saa 10 jioni, wewe anza saa moja asubuhi na kumaliza saa 12 jioni. Kila siku weka masaa 2 mpaka 4 ya ziada kwenye kazi unayofanya.
Na unapofanya kazi weka umakini wako wote kwenye kile unachofanya na usiruhusu usumbufu wowote ukuvuruge.

2. Usiwe fair kwenye Muda
Watu wengi huwa wanachezea muda kama vile ni kitu ambacho hakina ukomo. Lakini muda una ukomo, kuna masaa 24 tu kwenye siku, ukishayatumia huwezi kupata tena mengine. Kuwa bahili sana wa muda wako, usikubali upotee hovyo kwa mambo yasiyo na tija. Kila siku unayoianza pangilia muda wako, weka vipaumbele vyako vya siku na vifuate hivyo. Kuwa na orodha ya mambo utakayoyafanya kwenye siku yako na ifuate hiyo. Usiruhusu usumbufu au mahitaji ya wengine yaingilie ratiba yako muhimu ya siku.

3. Usiwe fair kwenye Fedha
Watu wengi wakipata fedha huwa wanakimbilia kuzitumia mpaka ziishe na hata zikiisha hawaishii hapo, badala yake wanakopa ili waendelee kutumia zaidi. Wewe usiwe hivyo, unapopata fedha yoyote ile, tenga kwanza akiba kabla hujatumia. Usitumue kisha inayobaki ndiyo uweke akiba, fedha huwa haibaki. Badala yake weka akiba kwanza kisha inayobaki ndiyo utumie. Na akiba unayoweka, iwekeze mahali inapozalisha na kukua zaidi. Hiyo ndiyo njia ya uhakika ya kuondoka kwenye umasikini na kwenda kwenye utajiri.

4. Usiwe fair kwenye Kusudi

Watu wengi wanaishi maisha ya bendera kufuata upepo, hawalijui kusudi la maisha yao na hivyo ni rahisi kushawishiwa na chochote kinachopita mbele yao. Wewe usiwe na maisha ya aina hii, pambana ulijua kusudi la maisha yako na kuliishi kila siku. Jua kwa nini uko hapa duniani, maisha yako yanapaswa kuacha alama gani na jipe wajibu mkubwa unaokusukuma kuchukua hatua kila siku. Ukiwa na kusudi unakuwa na msimamo.

5. Usiwe fair kwenye Ndoto kubwa
Watu wengi hawana ndoto kubwa, wanaishi maisha ya mazoea, wanafanya shughuli zao, wanapata pesa ya kula na wabaridhika na hayo. Wewe usiwe mtu wa kuridhika na mambo madogo unayopata sasa. Kuwa na ndoto kubwa sana, ndoto ambazo wengine wakizisikia wanaona kama umechanganyikiwa na wanakuambia haiwezekani. Ni ndoto kubwa unazoziamini bila ya shaka zinazokusukuma kufanya makubwa zaidi kwenye maisha yako.

6. Usiwe fair kwenye Kujifunza

Watu wengi wakishahitimu shule, hawajifunzi tena vitu vipya wala kusoma vitabu. Watu hawasomi kabisa vitabu, wakiamini hakuna kipya wanachoweza kujifunza, tayari wanajua kila kitu. Wewe usiwe hivyo, kuwa mtu wa kujifunza vitu vipya kila siku. Kuwa mtu wa kusoma vitabu kila siku. Hakikisha kila mwezi unasoma angalau kitabu kimoja na kwa kila kitabu unachosoma chukua hatua za kuyabadili maisha yako. Hilo pekee linatosha kukupa fursa nyingi na kukuwezesha kupiga hatua kuliko wengine.

7. Usiwe fair kwenye Mahusiano
Walio wengi wanazungukwa na watu hasi, watu waliokata tamaa na wanaowakatisha tamaa pia. Mahusiano yao mengi yanakuwa kikwazo kwao kupiga hatua. Wewe kuwa makini sana na mahusiano yote uliyonayo, hakikisha yanakuwa mahusiano bora na yanayokusukuma uwe bora zaidi. Waepuke watu hasi na waliokata tamaa kama ukomo, usijenge ukaribu na watu wa aina hiyo, kwani watakuambukiza waliyonayo. Ulivyo ni wastani wa watu watano wanaokuzunguka, chagua watano bora ambao watakusukuma upige hatua zaidi.

8. Usiwe fair kwenye Kujiamini

Watu wengi hawajiamini, wanaweza kuwa na ndoto kubwa ila wanapowaambia wengine na wakawakatisha tamaa, wanawasikiliza na kukubaliana nao. Ndiyo maana kundi kubwa la watu kwenye jamii hawawi na maisha wanayoyataka, maana hawajiamini kiasi cha kuwashinda wale wanaowakatisha tamaa. Wewe jiamini kupitiliza, amini ndoto kubwa ulizonazo utaweza kuzifikia bila ya kujali unaanzia wapi sasa. Hata kama wengine wanakuambia haiwezekani, hata kama wanakuonesha na mifano kabisa, usiwaamini zaidi ya unavyojiamini wewe. Jifunze yote muhimu na endelea kusimama kwenye ndoto zako kubwa.

9. Usiwe fair kwenye Ung’ang’anizi
Ili ufanikiwe lazima uwe king’ang’anizi sana, ujitoe kweli kweli na ukomae mpaka upate kile unachotaka. Utakutana na magumu, vikwazo na kushindwa, lakini usiruhush hayo kuwa mwisho wa safari yako. Jipe kiapo kwamba utapata kile unachotaka au utakufa ukiwa unakipambania, hakuna mbadala wa hilo.

10. Usiwe fair kwenye kutoa Kafara
Ili upate kile ambacho hujawahi kupata, lazima uwe tayari kupoteza kile ambacho tayari unacho sasa. Kuna vitu vizuri unavyo sasa lakini ni kikwazo kwako kupata mafanikio makubwa unayotaka. Wengi wanataka mafanikio lakini hawapo tayari kutoa kafara, kuachana na vile vizuri walivyonavyo sasa ili kupata vilivyo bora zaidi. Ukiweza kuvuka hilo, utaweza kupata makubwa.

Ukiondoa usawa kwenye maeneo haya 10 muhimu, utakuwa na maisha ya tofauti kabisa na utaweza kufanya makubwa sana.
Lakini utakapokua na maisha ya tofauti wengi watakushambulia, hivyo utakuwa kama mpweke katikati ya kundi kubwa la watu.

Nakukaribisha ujiunge kwenye jamii ya tofauti, jamii ambayo utakutana na wanaoishi maisha haya ya tofauti na kukupa nguvu ya kuendelea kuyaishi pia. Jamii hiyo inaitwa KISIMA CHA MAARIFA, kama bado hujawa kwenye jamii hiyo, wasiliana nami sasa kwa wasap namba 0717 396 253 nikupe utaratibu wa kupata nafasi kwenye jamii hii ya kipekee.

Usikubali tena kuendelea kuwa fair kwenye mambo yanayokurudisha nyuma.

Chagua kushika hatamu ya maisha yako ili uweze kufanya makubwa.

Rafiki yako anayekupenda sana,

Kocha Dr Makirita Amani
Hayo ni mafundisho ya SHETANI, MWENYEZIMUNGU humuinua anaemtaka na unaweza usiwe fair na usifanikiwe
 
Unaweza ukafanya yote hayo na bado ukala msoto ,halafu mwengine akala bata tu halafu akatoboa ,life halina formula sana
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom