Kumekuwa na mjadala mkubwa kuhusu Matumizi ya shilingi 252 bilioni katika Wizara ya Ujenzi. Kamati ya PAC ilikutana na Wizara ya Ujenzi wiki iliyopita na hapo ndipo kashfa hii ilianza kuandikwa kwa uzito wake. Ikumbukwe kuwa suala hili Kambi ya Upinzani Bungeni ilianza kulihoji mwaka 2011 kutokana na Wizara kuomba fedha nyingi sana kama 'KUANZA miradi maalumu ya Barabara nchini' na maelezo ya Mawaziri wote kuonyesha kuwa huu ni mfuko maalumu kwa ajili ya Ujenzi wa barabara na hakuna mahala hata pamoja ambapo Serikali ilisema hizi ni fedha za kulipa Madeni mpaka pale Taarifa ya CAG ilipotoka na kuonyesha kuwa huo mradi ulikuwa mradi hewa.
Kulipa Madeni sio tatizo hata kidogo, suala hapa ni kwanini Serikali iombe fedha Bungeni 'kuanza miradi maalumu ya barabara' wakati inajua inaomba Fedha kwa ajili ya kulipa Madeni? Ingesema inaomba fedha kulipa Madeni Bunge lingekataa? Ndio maana PAC imeamua kuwapeleka kwenye kamati ya Maadili Mawaziri Magufuli, Mwakyembe na Lukuvi kwa kulidanganya Bunge wakati wa kuomba Fedha hizo.
Suala la pili, ni je Fedha hizo zimetumika kulipa madeni yepi wakati kila mradi una kasma yake? Katika hili PAC iliamua kuwa CAG akague matumizi ya Fedha hizo kisha atoe Taarifa kwenye Kamati.
Serikali kwa nini inahaha sana kuhusu suala hili? Katibu Mkuu wa Wizara alipewa muda wa kutosha kabisa katika Kamati kujieleza. PAC huruhusu waandishi wa Habari kuhudhuria vikao vyake na kushuhudia mahojiano kati ya Kamati na Makatibu Wakuu. Ni vema Katibu Mkuu asubiri uhakiki wa Fedha hizo na zilivyotumika. Ni vema pia aache suala la Kamati ya Maadili liende Kamati ya Maadili ambapo Mawaziri hao, Magufuli, Mwakyembe na Lukuvi watajieleza kwa nini walidanganya Bunge wakati wa kuomba Fedha hizo.
Nimesikia CAG kaitwa na Katibu Mkuu Kiongozi na kumtaka awasafishe. Ukweli ni kwamba PAC ilitumia taarifa ya CAG na ni yeye CAG aliyeita matumizi haya kuwa ni matumizi hewa na mradi wenyewe kuwa ni mradi kivuli. Taarifa ya Kambi ya Upinzani Bungeni imenukuu kauli za Mawaziri wakati wa mjadala wa Bajeti za Serikali na Taarifa ya CAG kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni, 2012. Sehemu ya Hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni hii hapa
MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA BARABARA
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya kambi rasmi ya upinzani bungeni kwenye bajeti ya mwaka 2011/2012 tulihoji kuhusiana na fedha zilizokuwa zimetengwa chini ya fungu lililojulikana kama special road construction project , na tulisema ifuatavyo; Nanukuu hansard ya tarehe 01.08.2011 Mheshimiwa Spika, Miradi maalum ya ujenzi wa barabara (kasma 4168).kitabu cha Miradi ya Maendeleo (sehemu-A juzuhu iv) katika fungu 98, kasma 4168 utaona kuwa mradi unaitwa Miradi ya ujenzi wa barabara maalum (special road construction projects) na fungu hili limetengewa kiasi kikubwa kuliko miradi mingine yoyote ya ujenzi wa barabara katika mwaka huu wa fedha kwani zipo jumla ya sh. 348,075,000,000/= na hizi zote ni fedha za ndani. Kwa hakika hizi ni fedha nyingi sana na hasa ikizingatiwa kuwa kitabu hicho kimeonesha miradi yote ya ujenzi wabarabara ambayo itatekelezwa katika mwaka huu wa fedha, ila hii miradi maalum haijaoneshwa ni miradi ya barabara gani na zitajengwa wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kasma hii kwa mwaka wa fedha 2009/2010 na 2010/2011 haikuwa imetengewa kiasi chochote cha fedha na ndio maana imetustua kuona mwaka huu fedha nyingi kiasi hicho zinatengwa kwa miradi isiyojulikana kuwa itajengwa wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata ukiangalia maelezo yaliyotolewa kwenye Kamati ya Bunge ya Miundombinu juu ya mpango na bajeti ya mwaka 2011/2012, kasma 4168 haipo kwenye randama na hakuna maelezo yoyote ambayo yametolewa kuhusiana na fedha hizo ambazo zimetengwa. (Makofi)
Kambi ya Upinzani, tunataka kupata maelezo ya kina ni miradi gani hii ambayo haiwezi kuandikwa na inatengewa fedha nyingi kiasi hicho? Kwani hii italiwezesha Bunge kuweza kupitisha bajeti inayoifahamu na kuisimamia Serikali kwa kuweza kufuatilia utekelezaji wa miradi husika.
Mheshimiwa Spika, wakati wa mjadala kuhusiana na hotuba ya wizara ya uchukuzi 2011/2012 ilipowasilishwa , Mhe.Mbunge wa Ukerewe Salvatory Machemli alihoji fedha hizi na kusema , naomba kunukuu Hansard ya tarehe 03.08.2011 Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaja mwanzoni kwamba reli inakufa wakati watu wanaiangalia na Serikali haisemi kitu chochote kazi yao kuomba Miongozo tu hapa, pesa zipo nyingi. Wakati mimi nawasilisha hotuba yangu kwa Wizara ya Ujenzi, nilihoji kiasi cha pesa shilingi bilioni 348 ambazo hazikuonyeshwa zinafanya kazi gani kwenye Wizara ile. Mheshimiwa Magufuli jana wakati anafanya majumuisho hakutaja, amemeza tu japokuwa aliona ni chungu lakini akameza kama chloroquine, nataka sasa hizi shilingi bilioni 348 ambazo zimeonyeshwa kwenye vote 4168 ambazo matumizi yake hazikuonyeshwa basi wapelekewe reli ili tuimarishe reli, tuweze kuokoa barabara zetu kuliko kuziacha tu, jamaa wanatia mfukoni, wanachukua wanaweka waa, kama ilivyo kawaida yenu Chama cha Mapinduzi, mnakwenda kujenga masinagogi Ulaya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika mjadala huo aliyekuwa naibu waziri wa Ujenzi Mhe.Dr.Harison Mwakyembe alijibu kuhusiana na hoja hiyo na kusema , nanukuu hansard ya tarehe 03.08.2011 NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Mheshimiwa Mbunge asiendelee kupotosha na kujenga mahekalu hewani, nilitaka kumueleza kwamba hizo pesa zilizopitishwa hapa jana ni za Mfuko Maalum ambao unaisaidia Serikali pale ambapo mfadhili wa nje kwa mfano, anaamua kufadhili ujenzi wa barabara fulani na anasema Serikali ichangie ten bilioni, utaitoa wapi kama wewe huna Mfuko Maalum? Serikali ikaona logic ya kuweka Mfuko Maalum ili isitulazimu tena kuitisha Bunge kupitisha pesa hizo, sasa zianze kuleta maneno, kutufanya wote ni wahuni kama yeye na hii siyo vizuri kusema kwamba tutapeleka hizo pesa wapi? Ahsante. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 04.08.2011 wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Mhe.waziri Mkuu alitoa kauli ya serikali kuhusiana na fedha kuongezwa wizara ya uchukuzi na alisema, nanukuu hansard ya tarehe husika
..Kwa hiyo, baada ya Kamati ya Miundombinu kupitia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kuishauri Serikali kuongeza bajeti hiyo kwa shilingi bilioni 95, jambo ambalo tuliliridhia na kulikubali, lakini hatukuweza kufikia kiwango hicho kama ilivyokuwa imeombwa. Kikao cha jana kimewezesha Serikali kufanikiwa kupata fedha hizo ambazo zitatumika kwenye maeneo matatu yafuatayo: Reli ya Kati, Kampuni ya Ndege Tanzania na Usafiri wa Majini yaani Meli katika Maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa. Kiasi hicho cha shilingi bilioni 95 ni kiasi ambacho Wizara ilikuwa imeji-commit au imejiahidi mbele ya Kamati kwamba, zikipatikana zitawezesha huduma za msingi katika maeneo hayo matatu kuweza kuendelea bila matatizo makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wakati Bunge likiwa limekaa kama kamati ya matumizi wakati wa kupitisha mafungu ya wizara ya uchukuzi Mhe. Tundu lissu aliomba ufafanuzi kama ifuatavyo, nanukuu hansard
..Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nifafanuliwe, kama Bajeti ya Wizara ya Ujenzi ilishapitishwa mafungu yote yalishapitishwa, hii bilioni 95 iliyochotwa kutoka fungu la miradi maalum ya barabara na kuletwa kwenye miradi ya maendeleo ya Wizara ya Uchukuzi ambayo ni Vote tofauti kabisa zimechotwa kwa idhini ya Kanuni ipi, mimi naomba nipewe angalau msingi wa Kikanuni au wa kisheria wa kuchota fedha ambazo tayari zimeshatengwa na Bunge hili bila kupata authorization ya Bunge hili. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, majibu yafuatayo yalitolewa,kwa mujibu wa Hansard WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, URATIBU NA BUNGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu alichokisema Mheshimiwa Tundu Lissu kipo ukurasa 276, Kifungu kidogo cha 4168. Hizi ni fedha ambazo zimewekwa katika Kifungu hiki katika Bajeti hii ya ujenzi lakini ni mfuko maalum, hela hizi hazijawa committed kama unavyoziona. Ukiangalia miradi yote iliyomo katika kfungu hiki ina barabara tayari. Fedha hizi ziliwekwa maalum kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya miundombinu hasa katika maeneo ambayo ipo miradi kadhaa ambayo tuna uzoefu, imekuwa inachangiwa inatolewa na wafadhili, lakini hii tulifikiri sehemu nyingine miradi hii imekwama kwa sababu sisi tulikuwa hatujajitayarisha kuweka counterpart fund. Kwa hiyo, hizi fedha zimewekwa hapa kwa ajili hiyo, miradi yote ambayo Serikali ya Tanzania itafanya kutoka kwenye fedha za wafadhili hizi ni fedha ambazo zimewekwa, ni fungu ambalo haliko committed. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hizi fedha zimechukuliwa hapa zimepelekwa ujenzi kwa maana ya kwamba ni fedha ambazo ziliwekwa kwa ajili ya mfuko wa miundombinu. Zimekuwa voted lakini Mheshimiwa Tundu Lissu atakuja kupata ukweli wa mambo haya yote wakati wa Appropriation Bill. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya fedha hizi kupunguzwa kiasi cha shilingi bilioni 95 na kupelekwa wizara ya uchukuzi zilibakia kiasi cha shilingi bilioni 252.975 katika kifungu hiki, leo tumelazimika kulikumbusha Bunge kuhusiana na suala hili kwani kwa mujibu wa ripoti ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali ya mwaka husika wa fedha kuhusiana na kifungu hiki alisema, naomba kunukuumalipo ya madeni ya mwaka wa nyuma yaliyolipwa kwa fedha za 2011/2012 kwa kutumia jina la mradi usiohalisi shs.252,975,000,000. Miradi katika wizara ilipewa namba 4168 kwa ajili ya kupitisha malipo ya madeni ya miaka ya nyuma kwa miradi inayotekelezwa na TANROADS. Namba hii sio halisi (chanzo: taarifa ya CAG uk.160,fungu 98)
Mheshimiwa Spika, fedha hizi zilizopoteaau kulipwa kifungu hewa ni sawa na fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya barabara zifuatazo kwa mwaka huu wa fedha 2013/2014;
i. Barabara ya Usagara-Geita-Kyamyorwa (KM 422)
ii. Barabara ya Kigoma-Kidahwe-Uvinza-Kaliua-Tabora (KM 443)
iii. Barabara ya Nangurukuru-Mbwemkulu (KM 95)
iv. Barabara ya Sumbawanga-Matai-Kasanga Port (KM 112)
v. Barabara ya Manyoni-Itigi-Tabora (KM264)
vi. Barabara ya Tabora-Ipole-Konga-Mpanda (KM 359)
vii. Barabara ya Kidatu-Ifakara-Lupilo-Malinyi-Londo-Lumecha/Songea(KM- 396)
viii. Kuondoa msongamano barabara za Dar (KM- 102.15)
Aidha, ni sawa na kusema kuwa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 316.218 imepotea kwa kutumia mahesabu ya wizara ya ujenzi kuwa kilomita moja ya lami inajengwa kwa kiasi cha shilingi milioni mia nane (800,000,000), hii ni sawa na kusema kuwa barabara ya kutoka Manyoni-Itigi-Tabora (KM 264) Changanya na barabara ya kutoka Chunya Makongorosi (KM 43) na Barabara ya Tangi Bovu Goba (KM 9), zimepotea kutokana na ufisadi huu.
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kupata majibu yafuatayo kuhusiana na suala hili;
i. Fedha hizi zilizokuwa zimetengwa zilitumika kwa ajili ya kufanyia shughuli gani? Kwani majibu yaliyotolewa na wizara na serikali Bungeni sio yaliyotolewa kwa mdhibiti na Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali
ii. Ni madeni gani yalilipwa kama kweli yalikuwepo?au wajanja wachache walijinufaisha ? na wahusika wamechukuliwa hatua gani mpaka sasa.
iii. Nini kauli ya serikali kuhusiana na Ufisadi huu, mbele ya Bunge na watanzania kwa ujumla .
iv. Je, Tunaweza kuendelea kuamini kauli za viongozi wa serikali hii ndani ya Bunge kama hii ndio hali halisi ?
v. Nini kauli ya serikali kuhusiana na Ufisadi huu.
Muhimu
Tusifanye kila jambo ni siasa. Hili ni suala la Uwajibikaji. Hoja hii iliibuliwa na Kambi ya Upinzani Bungeni tangia Fedha hizi hazijaidhinishwa na Bunge. Tumekuwa very consistent katika jambo hili. Tumeendelea kulihoji baada ya Taarifa ya CAG kutoka.
Tumeendelea kuhoji kwenye Kamati ya PAC ambapo Katibu Mkuu wa Wizara alitoa majibu yaliyodhihirisha kuwa Serikali iliomba Fedha Bungeni kwa udanganyifu, haikusema ukweli fedha hizo wanataka kufanyia nini? Hapakuwa na sababu ya Mawaziri kusema uwongo Bungeni ili Bunge liidhinishe Fedha. Wasipowajibishwa kwa haya, wataendelea kuwa wanasema uwongo.
Kama fedha hizo zilitumika vema bila ufisadi wowote uhakiki wa CAG utaonyesha hivyo na tutasema wazi. Kama CAG akiueleza umma kuwa hakuna ufisadi bila ya yeye kufanya uhakiki itakuwa ndio yale mambo ya Jairo ambayo yalimvunjia heshima. Naamini kuwa atafanya ukaguzi huo na kutoa taarifa kwa umma maana hoja ya ukaguzi ni yake na kama pasingekuwa na makosa asingeiweka kwenye taarifa yake ya mwaka aliyoitoa Bungeni mwezi Machi mwaka 2013.
Kamwe tusikubali majibu mepesi mepesi kwenye masuala ya fedha za Umma. Kamwe tusikubali kugeuza kila jambo ni siasa.
Fedha za Umma zinaombwa hadharani kupitia Bunge la Bajeti. Matumizi ya Fedha za Umma lazima yafanyike hadharani kwa kamati za mahesabu kufanya vikao vyao kwa uwazi na kuruhusu vyombo vya habari