nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
JUMANNE, OCTOBA 30, 2012 04:52 NA RUTH MNKENI, DAR ES SALAAM
Watuhumiwa waliokamatwa na meno ya tembo yenye thamani ya Sh bilioni 2.1 wakiwa kwenye Kituo cha Kati cha Polisi Dar es Salaam jana. Nyuma yao ni baadhi ya meno hayo. Picha na Deus Mhagale.
*Baadaye yangefunikwa kwa bendera ya taifa, polisi wakataa hongo
JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, linawashikilia raia watatu kutoka nchini Kenya na Mtanzania mmoja, baada ya kuwakamata wakiwa na meno ya tembo 214, yenye thamani ya Sh bilioni 2.1.
Hii ni mara ya kwanza kwa jeshi la polisi nchini, kukamata shehena kubwa ya meno ya tembo, kutoka kwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majangili.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleman Kova, alisema watuhumiwa hao walikamatawa juzi katika eneo la Kimara Stop-Over.
Aliwataja watuhumiwa hao, kuwa ni Polisi Simon (42), ambaye ni dereva wa daladala aina ya Costa, Charles Wainaine (41), mkazi wa Tarakea Wilaya ya Rombo na Peter Kabi, ambao wote ni Wakikuyu kutoka nchini Kenya.
"Uchunguzi wa awali, ulibaini wahalifu hawa, ni wazoefu katika matukio ya mtandao wa ujambazi, usafirishaji na umiliki wa nyara za Serikali.
"Mpango wa siri, walioutumia watuhumiwa ni kutumia gari aina ya Costa, inayoendeshwa na Polisi Simon, kwa kusafirisha... waliweka jeneza lililofunikwa bendera ya Taifa, kama wanasafirisha maiti ya mtu mashuhuri wa Serikalini.
"Lengo ni kutaka kuzubaisha vyombo vya dola au mamlaka zinazohusika...nyara hizi zingevushwa kwenda nje ya nchi, kupitia mpaka wa Tarakea Wilaya ya Rombo mkoa wa Kilimanjaro," alisema Kova.
Alisema katika tukio hilo, mwanamke mmoja Leornad Kabi, alikamatwa kwa kosa la kuwashawishi askari polisi waliokamata mali hizo, ili wapokea rushwa ya Sh milioni 15 na kuahidi kuwapatia fedha nyingine siku inayofuata, kama wangewaachia.
"Tunashirikiana na uongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii, ili kupata uzito wa thamani na uchunguzi wa kina utafanyika, ili kubaini mitandao ya wizi wa nyara za Serikali," alisema.
Alisema polisi walifanya msako, baada ya kupata taarifa kuwa, kuna nyumba inahifadhi mali za wizi, ambazo zinasadikiwa kuwa nyara za Serikali.
Alisema polisi walifika katika nyumba hiyo, ambayo alipanga Peter Kami, anayeishi na Leornad Kabi na kukuta idadi ya meno 214, ambayo yalikuwa yamehifadhiwa katika mifuko ya salpheti 12, ikiwa imefunikwa na bendera ya Taifa, pembe za ndovu 10 na na mifupa ya tembo 500.